Saturday, March 31, 2012

Changamoto za Kuendesha Blogu

Kuenesha blogu sio kazi rahisi. Kuna changamoto nyingi. Kwa mfano, wakati mwingine unashindwa kujua uandike nini. Huna wazo kichwani. Wakati mwingine unaandika ukijiuliza kama kweli uchapishe hicho unachoandika. Unajua fika kuwa chochote unachochapisha, kinasambaa duniani dakika hiyo hiyo.

Kuna pia upande wa wasomaji, yaani hao tunaowaita wadau wa blogu. Binafsi, nawakaribisha wadau wanaotembelea blogu yangu. Unapoandika makala kwenye blogu yako, huwezi kujua watu wataipokea vipi. Kila mtu ni tofauti na mwingine. Kinachomridhisha au kumpendeza huyu kinaweza kumuudhi mwingine. Ufanyeje hapo?

Huwezi kumridhisha kila mtu, na kwa upande wangu siandiki kwa lengo la kumridhisha yeyote. Najaribu tu kuelezea kilichomo akilini au moyoni mwangu wakati ninapondika.

Kuna pia wadau wanaoandika maoni. Hapo pana changamoto. Kuna watoa maoni ambao wanamshambulia au kumbeza mwendesha blogu. Je, ni sahihi kwa mwendesha blogu kuyafuta maneno yao yasionekane kwenye blogu? Binafsi, naona ni bora watu wawe na fursa kamili ya kujieleza. Tatizo tu ni jinsi wengi wao wanavyojificha chini ya kivuli cha anonymous. Mimi mwenye blogu najitambulisha wazi, na hata ninapoancika maoni kwenye blogu za wengine ninajitambulisha wazi, hata pale ninapoandika jambo linalowaudhi watu. Sielewi kwa nini wengine wasifanye hivyo hivyo.

Lakini je, mdau akiandika matusi dhidi ya mtu mwingine, au akimdhalilisha mtu mwingine, ni sahihi kuruhusu hayo kwenye blogu yako? Suali hili lilijitokeza katika kikao changu na Mwenyekiti Mjengwa siku chache zilizopita.

Nilijifunza mawili matatu kutoka kwake. Ninajua kuwa endapo blogu yangu itaendelea na kuwa maarufu kama ya Mjengwa, changamoto za aina hii zitanipata.

Nakaribisha uzoefu na maoni ya wanablogu wengine, na ya wadau.

Thursday, March 29, 2012

Profesa Anapotinga Baa

Kwa siku hizi ambazo nimekuwepo hapa Dar, nimekuwa nikitinga kwenye baa hii au ile, ingawa sinywi ulabu. Watu wengi hapa nchini wananifahamu kutokana na kuona taarifa zangu mtandaoni. Huko kwenye baa, wengine huambiwa na wenzao mimi ni nani.

Wadau wakishagundua kuwa mimi ni profesa, hupenda kuanzisha mijadala nami. Wanadadisi mambo mengi, yakiwemo yale ya Marekani. Nimejikuta nikilumbana na wadau wa aina aina, wakiwemo wale ambao wamelewa chakari. Ni burudani ya aina yake kuwashuhudia hao waliolewa chakari wakijibidisha kutema umombo ili ijulikane kuwa nao wamo.

Sasa, katika hizi siku zijazo, nataka kuanza kuwaambia hao marafiki zangu kuwa kwa kweli, mahali ambapo profesa anapaswa kuwepo ni maktabani, darasani, au sehemu ya utafiti wake. Anapaswa kuwa anatumia muda wake mwingi katika kusoma na kuandika makala na vitabu, si kukaa kaunta akitema cheche kwa wadau wa konyagi, Tusker, na Kilimanjaro za baridi.

Wadau kwenye baa hawatambui hilo. Hatari mojawapo ni kuwa watu wanadhani mtu kwa vile alishasoma sana na kumaliza shahada za vyuo, basi ameelimika kabisa na hahitaji wala kuwajibika zaidi ya pale. Wanaamini kuwa mtu aliyefikia cheo cha uprofesa amemaliza. Kwa hivyo hawaoni tatizo kuwa naye baa kila siku na kulumbana.

Kwa mtindo huu, Tanzania hatutafika. Tutashindwa kutoa mchango wa maana katika taaluma hapa ulimwenguni. Kiwango cha maprofesa kitaporomoka, kama hakijaporomoka tayari. Mimi mwenyewe, kwa siku chache hizi ambazo nimekuwa nikitinga baa badala ya kusoma vitabu na makala, najisikia kabisa kuwa nimedidimia kitaaluma kiasi fulani, kwa maana kwamba sijaandika lolote la maana kwa siku hizi kadhaa, wala sijasoma kitabu na makala katika taaluma yangu. Mihandara na malumbano yangu yote yamehamia baa. Nikiendelea namna hii kwa miezi au miaka, nitadidimia zaidi, ingawa bado wadau mitaani na kwenye baa wataendelea kuniona ni profesa maarufu. Hili ndilo tatizo la Tanzania. Kwa mtindo huu hatutafika kabisa.

Sio vibaya kwa profesa kuingia baa mara moja moja na kupata moja baridi. Lakini kukaa masaa humo baa, mara kwa mara, au kila siku, ni balaa tupu, wala tusidanganyane. Vile vile, kwa sisi tunaotafiti masuala ya jamii, baa panaweza kuwa sehemu moja muhimu ya kutafiti na kujifunza mengi. Ila, nadhani ili kufanikisha hilo, na kwa vile sisi ni waelimishaji, tunaopaswa kuwa mfano, tusiwe tunakata ulabu kama wadau wengine. Bia moja mbili sio mbaya.

Tuesday, March 27, 2012

Kunywa Maji Badala ya Ulabu

Kwa siku kadhaa sasa, nikiwa katika kutumia dawa nilizoandikiwa na daktari, ni marufuku kukata ulabu. Badala yake, kinywaji changu ni maji tu. Nikikaa mahali, hata baa, kinywaji changu ni maji tu.








Mwanzoni, nilidhani itakuwa adhabu kali kuziangalia chupa za bia baridi katika joto hili la Dar es Salaam bila kunywa hata glasi moja. Lakini nimegundua kuwa kunywa maji kuna raha yake. Ningejiona shujaa iwapo ningeweza kuendelea hivyo hivyo maisha yote.

Sunday, March 25, 2012

Nimetua Safari Resort Dar es Salaam

Jana, Jumamosi, nilitua Safari Resort, eneo la Kimara, Dar es Salaam. Ilikuwa mchana, nami nilitamani kwenda tena mahali hapa, ambapo nilipapenda kuanzia miaka ya 1976, nilipoanza kufundisha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Hapo kushoto unaiona Safari Resort, ukiwa kwenye barabara iendayo Morogoro.






Hapo ndipo getini, palivyo siku hizi. Miaka ile, Safari Resort ilikuwa inavuma sana. Gwiji wa Muziki King Kikii alikuwa akiimba hapa na bendi yake,na kukonga nyoyo za wa-Tanzania kupita maelezo.








Sikwenda Safari Resort kuchapa ulabu. Wiki hii natumia dawa kutibu tatizo la afya lililonipata. Kwa hivi, sinywi bia kabisa. Nanywa maji tu. Hata hivyo, nimegundua kuwa kwenda sehemu za starehe kama hizo na kuishia kunywa maji haimaanishi kuwa unakaa hapa ukiwa na majonzi. Sio lazima ukienda mahali kama hapa upige ulabu hadi upotee njia, au uanzishe varangati ya kufa mtu, kama tufanyavyo wa-Tanzania. Maji yanatosha, na bado unafaidi kuangalia mazingira, kukutna na watu, kujikumbusha mambo kadha wa kadha ya zamani na kupiga picha.

Banda hili hapa kushoto linanikumbusha mbali. Mwaka juzi nilipata fursa ya kukaa kwenye banda hilo na Mheshimiwa Balozi Mstaafu Andrew Daraja, tukaongea kwa masaa manne, kuhusu masuala mbali mbali. Yeye tulifahamiana alipokuwa Balozi wetu Washington D.C. Wakati akiwa kule, alisoma kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, kisha akanipigia simu ofisini kwangu, akionnyesha kufurahishwa na niliyoandika. Ni mtu makini, mwenye kuhamasisha wa-Tanzania wanaofanya mambo ya maana. Kwa mfano, msikilize Youtube, hapa. Balozi Daraja alinivutia kwa ufahamu wake wa mambo ya nchi hii na dunia, akaniacha hoi aliponukuu vifungu kutoka kwa Shakespeare. Kwangu mimi mwanafasihi, hii niliiona ni kali kabisa. Basi hizo ndizo kumbukumbu zilizonijia jana nilipokuwa naliangalia banda hili.

Watu wanaokaa Tanzania wanaweza wasielewe umuhimu wa blogu kuweka picha kama hizi ninazoweka hapa. Lakini wale wanaoishi ughaibuni, wanaguswa, kwani wako mbali. Mimi mwenyewe sikosi kungalia blogu kama ya Mjengwa, kwa jinsi inavyoleta picha kutoka sehemu mbali mbali hasa za Uswanzi za vijijini, pamoja na kule kunakovunjika jembe ukabaki mpini.

Saturday, March 24, 2012

Mkulima wa Msoga, Msoma Vitabu

Jana nimekutana tena na Gilbert Mahenge, mkulima wa Msoga, Bagamoyo, ambaye tumeshakuwa marafiki. Nilishaandika habari zake hapa, nikimnadi kuwa ni msomaji makini wa vitabu.

Alikuja tukakutana Dar es Salaam, katika hoteli ya Deluxe, Sinza. Lengo kubwa la kukutana lilikuwa kuongelea shughuli za kampuni yangu ya Africonexion, tukazama katika kutafakari changamoto zinazotokana na utandawazi wa leo, na fursa zake.

Mahenge alishasoma kitabu changu cha CHANGAMOTO, kama nilivyoelezea kabla. Anapenda kuyanukuu niliyoandika. Basi, hiyo jana, nilimletea vitabu vyangu vingine viwili avione, yaani Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, Matengo Folktales, na Notes on Achebe's Things Fall Apart. Ili kuzuia malalamiko na maulizo miongoni mwa wasomaji wa blogu hii, niseme tu kuwa vitabu hivi vinapatikana Dar es Salaam, simu namba 0754 888 647 na 0717 413 073.

Tulipokuwa tunaongelea masuala ya changamoto za malengo na maendeleo ya mtu binafsi, nilitaja suala la mtu kuwa ngangari katika kufuatilia malengo, bila kukata tamaa. Hapo Mahenge akakumbushia mvumbuzi aliyehangaika kuunda balbu ya umeme, akashindwa mara elfu. Nami nikamtaja mvumbuzi huyo, kuwa ni Thomas Eddison. Tukaongelea zaidi habari za mvumbuzi huyo, ambaye alikuwa mtundu sana katika shule ya msingi, akijaribu hiki na kile na kuvunja vitu, hadi mwalimu akamfukuza shule. Hakumaliza shule ya msingi, lakini alikuja kuwa mvumbuzi wa vitu vingi sana katika uwanja wa tekinolojia, mvumbuzi maarufu labda kuliko wanadamu wote.

Mwaka jana, wakati niko Marekani, tuliongea kwa simu na Mahenge. Aliniambia kuwa ana hamu ya kusoma kitabu cha Parched Earth cha Elieshi Lema. Kwa bahati nzuri, nilikuwa nimeacha nakala hapa Dar, na nikafanya mpango akaja kukichukua. Hiyo jana, tayari aliniambia aliyosoma katika kitabu hicho.

Sasa basi, unapokutana na mkulima ambaye yuko katika upeo wa kuongelea masuala mengi namna hiyo, ni faraja tupu.

Thursday, March 22, 2012

Nimeugua Dar es Salaam; Natibiwa Hapa Hapa, Sio India

Nimeugua Dar kuanzia siku chache zilizopita. Nimejikuta nikiwashwa hasa mikononi, miguuni, na mgongoni. Kwa siku mbili sikuweza kulala usiku. Katika kuulizia watu, nikaambiwa ni "allergy." Na mhudumu mmoja kwenye duka la madawa maeneo ya Sinza aliniambia niende Magomeni, kwenye hospitali ya Dr. Ole.

Nilienda hapo. Wakati wa kuchukuliwa damu ili ipimwe, mpimaji alinipiga mchapo kuwa isije ikawa nimewekewa sumu ya unga. Akazidi kutonya, huku akijifanya ananyunyizia unga mezani, kuwa kaunga kidogo tu kanatosha. Nami nilijibu kuwa mtu huwezi kujua, kwani Bongo haina dogo. Tukawa tunacheka.

Ni kweli daktari alipochunguza ripoti ya upimaji amegundua nina "allergy," na akanielezea sababu zake. Pia alisema kuna bakteria katika damu. Aliniandikia sindano na vidonge vya aina mbali mbali. Alisema kuwa hiyo dozi itafuta kabisa hili tatizo. Nimedundwa sindano jana na vidonge nikaanza. Tayari nimeshaanza kujisikia nafuu. Naendelea vizuri kabisa.

Nimeleta habari hii binafsi kwa sababu maalum. Kwanza, mimi kama m-Tanzania nina imani na madaktari wetu. Ninafundisha Marekani, na ninapougua kule natibiwa kule. Ninapougua Tanzania natibiwa hapa. Tena, miaka yote ya maisha yangu, kabla sijaenda Marekani nilikuwa natibiwa hapa Tanzania, bila matatizo.

Sioni kama kuna tofauti kati ya madaktari wa Marekani na wa kwetu. Kilichopo tu ni kuwa madaktari wa kwetu wapewe mahitaji yanayopasika katika kumshughulikia mgonjwa. Na hilo ni jukumu la serikali, wala isijaribu kukwepa, kwani Tanzania si nchi maskini. Nakerwa ninapowasikia viongozi wa nchi hii wakidai kuwa sisi ni nchi maskini. Juzi hapo nimemsikia waziri kwenye kipindi cha televisheni akitoa huo upupu kwamba Tanzania ni nchi maskini.

Nawashangaa wa-Tanzania waoendelea kuwapigia kura mbumbumbu wa aina hiyo, wasio na upeo kiuongozi, hawana fikra za kuijengea jamii ari ya maendeleo, badala yake wana upeo wa kudumaza na kukatisha tamaa. Nawashauri wajifunze kutoka kwa Rais Obama, ambaye katika mazingira yoyote yale, hawakatishi tamaa raia wake, bali anawahakikishia kuwa Taifa litapambana na litashinda, litafanikiwa. Lakini viongozi wa kwetu, kila kukicha ni vilio kuwa sisi ni nchi maskini!

Uwezo wa kuimarisha hali ya mahospitali yetu tunao, tukizingatia rasilimali nyingi tulizo nazo katika nchi hii. Pia, magonjwa mengi tunayopata hayahitaji daktari bingwa. Yanatibiwa vizuri, iwe ni Marekani au Tanzania. Tena yako magonjwa ambayo ni ya nchi kama zetu, ambayo wataalam wake ni hao madaktari wentu. Mifano ni malaria. Usidhani kuwa ukipata malaria, ukimbilie Marekani. Unaweza ukafia kule, kwa sababu sio madaktari wengi wanaijua malaria na namna ya kupambana nayo kama wanavyojua madaktari wa nchi kama Bongo. Hao madaktari wetu wanasomea magonjwa ya hapa kwetu. Ninavyofahamu, wanapoenda kusomea Ulaya, utakuwa wanasomea "tropical medicine" ambayo ndio uwanja wa mapambano katika nchi kama yetu.

Madaktari wetu wana ujuzi wa hali ya juu, utawakuta wako katika nchi mbali mbali. Ninawafahmu baadhi ambao wako Marekani, katika hospitali mbali mbali, kama vile Mayo Clinic, ambayo ni maarufu sana duniani. Yaani inashangaza kuwa ukienda hizo hospitali, unawakuta madaktari wengi wa kutoka Afrika, yaani madaktari kama hao wanaonyanyasika Tanzania kwa sababu ya viongozi wetu kutokuwa na upeo upasao.

Kwa hiyo, serikali yetu inachopaswa kufanya ni kuwekeza katika huduma za mahospitali yetu hapa hapa nchini. Iweke vifaa na miundombinu, ili madaktari wetu waweze kutumia ujuzi wao ipasavyo. Wakipata vifaa na miundombinu, na wakilipwa ipasavyo, watafanya yale yale ambayo baadhi ya watu nchini wanayatafuta India au ughaibuni. Tunapowapeleka watu nje eti kuchekiwa afya, wakati hizi ni taaluma za madaktari wetu pia, au tunawapeleka watu kutibiwa ugonjwa kama niliopata mimi wiki hii, ambao madaktari wetu wanajua namna ya kuutibu, ni kuwadhalilisha madaktari wetu, na mimi sitalilazia damu suala hilo.

Miezi michache iliyopita, nilipata fursa ya kumsikiliza Daktari m-Marekani, Mark Jakobson, ambaye ni mwendeshaji wa hospitali ya Selian, Arusha. Alikuwa akitoa mhadhara Minnesota, kuhusu shughuli za hospitali hiyo. Siku moja, Insh'Allah, nitaelezea hotuba yake katika hii blogu yangu. Jambo mmoja ninalokumbuka ni jinsi alivyowapigia debe madaktari wa ki-Tanzania wanaofanya naye kazi. Anatamani tu angekuwa na uwezo wa kuwalipa vizuri zaidi, ili wasipate vishawishi vya kwenda sehemu zingine.

Makala hii nimeiandika pia kwa sababu juzi hapo niliandika makala kuhusu mgomo wa madaktari nikaishutumu serikali kwa kudiriki kugombana na madaktari. Kwa hivi, nimejichukulia fursa hii kuelezea zaidi hisia zangu. Kati ya mambo niliyosema ni kuwa kisaikolojia, daktari anapaswa awe kazini akiwa amefurahi na moyo mkunjufu.

Huyu jamaa aliyenipima damu alitoa mchapo na tukacheka. Muuguzi au daktari anapokuwa na moyo mkunjufu na ucheshi, anapokuwa hana msongo wa mawazo, ni baraka kwa wagonjwa. Watafiti wa masuala ya saikolojia ya wagonjwa na matibabu wanathibitisha hilo. Ndio maana niliishutumu serikali kwa kutotambua umuhimu wa kuwaridhisha madaktari.

Thursday, March 15, 2012

Nimetua Kunduchi Beach Hotel

Jana mchana nilichukua dala dala nikaenda zangu Kunduchi Beach Hotel. Kuanzia maeneo ya Lugalo na kwenda mbele, kuna shughuli kubwa ya ujenzi wa barabara.

Napenda kupunga upepo sehemu za ufukweni. Napenda pia kuandika taarifa za sehemu hizo, kama nilivyofanya kuhusu Matema Beach na Mbamba Bay.

Tuesday, March 13, 2012

Nimetua Bongo, Na "Laptop" Yangu Imetoweka

Nimetua Bongo kutokea ughaibuni tarehe 3 Machi. Wiki moja baadaye, "laptop" yangu imeibiwa hapa Dar es Salaam, eneo la Sinza. Ilikuwa ni Apple mpya. Nilikuwa nimeipakia maandishi yangu mengi, miswada na ripoti za utafiti wa kuanzia 1993.

Ninachohitaji ni haya maandishi. Huu ni mchango wa taaluma ambao natoa kwa wa-Tanzania na walimwengu. Miswada ya vitabu viwili nilitaka kuchapisha hapa Tanzania wakati huu, kwa manufaa ya wanafunzi, walimu, na jamii.

Hii "laptop" ukiifungua inakupa jina la Joseph Mbele, na unahitaji "password" ili kuweza kuitumia.

Habari ndio hiyo. Hivi sasa najiona kama mkulima mwenye ari ya kulima, lakini jembe hana. Nakala za miswada ziko ofisini Marekani. Lakini mimi nilipania kufanya kazi kubwa kwa wiki hizi nitakapokuwa hapa Tanzania. Nimekwama.

Thursday, March 8, 2012

Mgomo wa Madaktari: Tusidharau Wakunga na Uzazi Ungalipo

Niko Dar es Salaam, kuanzia Machi 3, na kuanzia siku mbili zilizopita, kumekuwa na mgomo wa madaktari, kufuatia madai yao kuwa serikali haijatekeleza makubaliano yaliiyofikiwa wiki chache zilizopita. Nimesikiliza kauli za Waziri Mkuu Pinda pia.

Ninachoweza kusema, kwa ufupi kabisa ni kuwa serikali ya Tanzania imeamua kukiuka busara ya wahenga kwamba tusidharau wakunga na uzazi ungalipo. Ni jambo la ajabu na la kutisha kwa serikali au nchi kugombana na madaktari. Kwamba Tanzania imefikia hapo ni dalili tosha za kutowepo busara za kiuongozi.

Madai ya madaktari, tangu mwanzo nayaafiki. Madai hayo ni pamoja na kuboreshwa kwa mazingira ya kazi mahospitalini, uwepo wa vifaa, madawa, na kadhalika. Vipato vya madaktari navyo ni duni sana. Tafsiri yangu ni kuwa madai ya madaktari hayahusu maslahi yao binafsi tu, bali maslahi ya wagonjwa. Tanzania, nchi yenye rasilimali nyingi, yenye serikali ambayo inafuja mali kwa namna mbali mbali, inaweza kabisa kutekeleza madai ya madaktari.

Nitoe mfano moja tu wa ufujaji unaofanywa na serikali. Wakati serikali hii ilipoanza kazi, Waziri Mkuu Pinda aliliambia Taifa kuwa alikuwa amenunuliwa gari la bei kubwa sana, na kwamba kutokana hilo, hakuwa tayari kulitumia. Binafsi najiuliza: je, waliofanya uamuzi wa kununua hilo gari waliwajibishwa? Na je, gari la fahari lililonunuliwa ni hilo moja tu? Na je, kwa nini serikali ya Tanzania isipige marufuku magari ya fahari? Nasikia Rwanda walishapiga marufuku magari hayo. Kwa nini serikali ya Tanzania isifanye hivyo hivyo. Huo ni mfano moja tu, lakini ningeweza kuandika zaidi.

Sote tunakubaliana na kuwa kazi ya udaktari ni nyeti kabisa, kwa maana kwamba inahusu uhai wa binadamu moja kwa moja. Hilo suala la unyeti wa shughuli za madaktari lilisisitizwa na Waziri Mkuu Pinda katika hotuba yake wiki hii. Hakuna ubishi hapo. Sasa basi inabidi tukubaliane kuwa ni muhimu maslahi ya madaktari ni lazima yawekwe mbele kuliko ilivyo sasa. Ni hatari kwa maisha yetu iwapo madaktari wako kazini huku wakihofia kodi ya umeme watalipaje au watoto wao watakula nini. Tufanye kila liwezekanalo ili daktari akiwa kazini, awe pale kwa roho moja, akitoa tiba.

Madaktari wamesema hawana imani na viongozi wawili wa wizara ya afya. Inashangaza kuona serikali ikipuuzia jambo hilo na kuliendesha kiubabe. Busara za kiuongozi zinaeleza kuwa morali ya watu ni jambo muhimu sana. Morali ya madaktari ingekuwa juu iwapo wangetekelezewa dai lao kuhusu kuondolewa kwa viongozi hao wa wizara.

Lakini serikali imeamua kuwakingia kifua watu wawili na hivi kudidimiza morali ya jumuia kubwa ya madaktari. Halafu, serikali inajaribu kujenga hoja kuwa madaktari hawathamini uhai wa wananchi. Hoja hii imenishangaza.

Kama kuna ambaye hathamini uhai wa wa-Tanzania ni serikali tuliyo nayo. Serikali hii imeacha wazi mianya ya rasilimali ya Taifa kuporwa, wakati rasilimali hii ingeweza kutumiwa kuokoa maisha ya watu mahospitalini kwa kununulia madawa na vifaa mbali mbali. Serikali inayofumbia macho ufisadi ndio mhujumu wa maisha ya wa-Tanzania. Hainiingii akilini kuwa serikali hii inajaribu kujifanya ndiyo ina uchungu na maisha ya wa-Tanzania.

Mambo mengine ya serikali hii yanachekesha. Pakitokea maandamano, kuanzia chuo kikuu hadi Songea, tunashuhudia jinsi polisi wanavyorusha mabomu na hata risasi. Hakuna siku tukasikia kuwa kuna upungufu wa mabomu na risasi. Serikali imewekeza katika mabomu ya kuwalipulia wananchi, wakati huduma za hospitali zina walakini. Ni ajabu na kweli.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...