Friday, May 30, 2014

Tembo wa Hifadhi ya Tarangire, Tanzania

Tarangire ni moja ya hifadhi maarufu Tanzania, yenye wanyama mbali mbali.

Nimefika katika hifadhi hii mara nne, kwa miaka tofauti. Mwezi Januari, mwaka juzi, 2013, nilipiga picha mbali mbali. Baadhi ni picha za tembo zinazoonekana hapa. Nilikuwa naongoza darasa la wanafunzi 29 wa chuo cha St. Olaf, katika kozi ambayo nilikuwa nimeitunga, kumhusu Ernest Hemingway.





Mwandishi Ernest Hemingway aliitembelea hifadhi hii mwaka 1933. Aliandika hayo katika kitabu chake cha Green Hills of Africa ambamo amezitaja na kuzielezea sehemu nyingi za Tanganyika alimopita.

Green Hills of Africa, kwa mtazamo wangu, ni kitabu bora sana, ambacho kiliitangaza nchi yetu vizuri kabisa, kuliko ambavyo sisi wenyewe tumefanya, kuliko tunavyoweza. tunaendekeza uzembe katika lugha na katika nidhamu ya uandishi kama ille ya Hemingway.. 



Kila ninapofika sehemu kama Tarangire, ninamkumbuka Hemingway na maandishi yake, hasa hiki kitabu chake cha Green Hills of Africa. Haiwezekani kujizuia.

Thursday, May 29, 2014

Duka Dogo Langoni pa Hifadhi ya Tarangire

Mwezi Januari, mwaka 2013, nilikuwa nazunguka maeneo ya kaskazini mwa Tanzania na wanafunzi 29 wa chuo cha St. Olaf. Tulikuwa katika kozi kuhusu safari za mwandishi Ernest Hemingway, tukisoma maandishi aliyoandika kuhusu sehemu hizo. Kati ya sehemu tulizotembelea ni hifadhi za Ngorongoro, Serengeti, Manyara, na Tarangire.

Kwenye sehemu ya kuingilia Tarangire, niliona duka dogo ambalo lilinivutia. Niliamua kupiga picha.



 


Kwa wale ambao wamefika Tarangire, hapa mahali ni karibu kabisa na Tarangire Safari Lodge. Ingawa nilishafika Tarangire mara mbili tatu miaka iliyotangulia, sikumbuki kama nililiona duka hili. Nilivutiwa na rangi mbali mbali za vitu vilivyokuwa vinauzwa humo. Nilijisikia kama vile naangalia kazi ya sanaa.

















Kwa wale ambao hawajafika, nimeona ni jambo jema kuwapa fununu kidogo kuhusu vitu ambavyo vinanivutia nchini mwetu.










Tuesday, May 27, 2014

How to Win Friends & Influence People

Kwa miezi kadhaa, labda  miaka, nimekikumbuka kitabu maarufu kiitwacho How to Win Friends & Influence People (New York: Pocket Books, 1982) kilichoandikwa na Dale Carnegie, na kuchapishwa mara ya kwanza mwaka 1936.

Imetokea tu kuwa hiki ni kimoja ya vitabu ambavyo vimetawala akili yangu kwa miezi kadhaa. Nimekumbuka jinsi katika ujana wetu tulivyokipenda kitabu hiki. Hapa Marekani, nimekuwa na kitabu hiki kwa miaka kadhaa. Kimekuwa kikinikumbusha ujana wangu.

Nilikuwa mwanafunzi Mkwawa High School, Iringa, miaka ya 1971-72, na hapo ndipo nilipokisoma kitabu hiki kwa mara ya kwanza. Wanafunzi wa wakati ule tulikuwa tunapenda sana kusoma vitabu. Wengi walisoma vitabu vya waandishi kama James Hadley Chase na Ian Fleming. Kitabu cha How to Win Friends & Influence People kilikuwa kimojawapo.

Nina hakika, kwa vile mimi sasa ni mwalimu wa ki-Ingereza, tabia hii ya kusoma sana vitabu vya ki-Ingereza ilichangia sana katika kutufanya tuifahamu na kuimudu vizuri lugha hiyo.

Kitabu cha How to Win Friends & Influence People kina mawaidha mengi ya kusisimua kuhusu namna ya kuhusiana na watu katika hali na mazingira mbali mbali. Kwa mfano, kama wewe ni kiongozi, unapaswa ufanyeje katika mahusiano yako na wale unaowaongoza ili wahamasike kufanya yale unayotaka wafanye, ili wakukubali na kukupenda.

Dale Carnegie ananukuu matokeo ya tafiti mbali mbali, kuthibitisha hoja zake. Moja ulionigusa ni utafiti uliofanywa na Carnegie Institute of Technology, utafiti uliothibitisha kuwa "even in such technical lines as engineering, about 15 of one's financial success is due to one's technical knowledge and about 85 percent is due to skill in human engineering--to personality and the ability to lead people." (uk. xiv)

Hapo utaona jinsi wa-Tanzania walivyopotoka wanapong'ang'ania kuwa vijana wao wasome masomo ya sayansi, bila kuzingatia umuhimu masomo ya elimu jamii kama vile fasihi na saikolojia. Jamii yetu imegubikwa na ujinga, na hapo ndipo ninapowajibika kusema kuwa utaratibu ule ambao nimeuona hapa Marekani, kwenye vyuo kama hiki chuo ninapofundisha, utaratibu wa kumfanya kila mwanafunzi asome masomo ya sayansi na ya elimu jamii, ni utaratibu wa kufaa sana. Hii huitwa "liberal arts education." Ni elimu inayomkuza mwanafunzi kiakili kwa namna mbali mbali, asiwe na ufinyu wa fikra na mtazamo.

Viongozi wengi hawajui hayo, na badala yake wanawakandamiza wale wanaowaongoza au wanamwaga mbwembwe ili waonekane wao ni mabosi na waogopwe. Kitabu hiki kinaelezea mbinu za kuwafanya watu waupokee msimamo wako katika masuala mbali mbali, sio kwa shinikizo bali kwa staili yako ya kuongea nao na kujieleza.

Ingawa hasemi hivyo wazi wazi, mwandishi ametumia vizuri sana taaluma ya saikolojia. Kukisoma tena kitabu hiki wakati huu, nimeona wazi kabisa kuwa matatizo mengi ya uongozi na mahusiano katika jamii yetu yangetoweka iwapo tungezingatia mawaidha yake.

Dale Carnegie aliandika vitabu vingine kadhaa. Leo nimeamua kukitaja hicho kimoja tu, ambacho kinavuma sana ulimwenguni, na kimeshauzwa nakala zaidi ya milioni 15. Cha zaidi ni kuwa kimeandikwa kwa lugha ya kuvutia. Ni mfano mzuri wa uandishi bora.

Sunday, May 25, 2014

Nyumbani mwa Mzee Patrick Hemingway Mjini Craig, Montana.

Hapa ni katika nyumba ya Mzee Patrick Hemingway katika mji mdogo wa Craig, Montana.

Picha hii nilipiga Tarehe 28 mwezi Aprili. Hapo mbele ya Mzee Hemingway kuna vitabu vyangu vilivyoandikwa na Ernest Hemingway, au vilivyoandika juu yake. Nilimpa Mzee Patrick Hemingway avisaini, naye alifanya hivyo bila kusita.

Nina vitabu vingi vya Hemingway au vile vilivyoandikwa juu yake. Siku tulipomtembelea Mzee Patrick Hemingway nilichukua hivi vichache tu, ambavyo vimechapishwa miaka ya karibuni.

Pembani mwa vitabu vyangu hivi vikubwa, kuna pia nakala nne za kitabu cha True at First Light. Mzee Patrick Hemingway alihariri mswada mkubwa wa Ernest Hemingway kuhusu safari na kukaa kwake Kenya, tangu 1953-54. Mzee Hemingway alituzawadia nakala za kitabu hiki. Siku nyingine, panapo majaliwa, nitaandika zaidi kuhusu zawadi hiyo.

Vile vile, hapo hapo mezani, kinaonekana kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Nilimchukulia nakala Mzee Hemingway, kutokana na ombi lake. Mzee Hemingway anakipenda kitabu hiki, na ameshaniambia, kwa nyakati tofauti, kuwa ni kitabu kilichoandikwa vizuri.

Kauli yake hii, tangu aliponiambia mara ya kwanza, ilinipa furaha kubwa. Siku hiyo nilipopiga picha hii, Mzee Hemingway alifungua kitabu hiki, akatusomea sehemu mojawapo, ukurasa 89, ambapo nimemnukuu Ronald Ngala akiongelea desturi za Wagiriama. Nilijisikia vizuri sana Mzee Hemingway alipendezwa na tafsiri yangu ya maneno hayo ya Ronald Ngala.

Huyu mama anayeonekana pichani ni Mama Carol, mke wa Mzee Hemingway. Aliwahi kuwa profesa, na pia ni mwandishi wa tamthilia.

Hizo ni baadhi ya kumbukumbu zangu za safari yetu ya Montana, kuonana na Mzee Patrick Hemingway. Naziandika kumbukumbu hizi kwa ajili yangu mwenyewe. Sina deni na mtu, wala siwajibiki kwa yeyote.

Friday, May 23, 2014

Tunawazia Kwenda Tena Montana Kuonana na Mzee Patrick Hemingway

Mwishoni mwa mwezi Aprili, mwaka jana nilienda Montana kuonana na Mzee Patrick Hemingway. Huyu ni mzee wa miaka 86 sasa, na ndiye mtoto pekee aliyebaki wa mwandishi maarufu, Ernest Hemingway. Niliandika kifupi kuhusu safari hii katika blogu hii.

Tulisafiri watu watano. Wanafunzi wangu ambao wanaonekana kushoto kabisa pichani, baba ya huyu mwanafunzi aliyevaa kaptura, na rubani wa ndege ya huyu baba mzazi. Mzazi wa mwanafunzi na rubani wake hawamo pichani. Mzee anayeonekana pichani ndiye Mzee Patrick Hemingway. Hapa tuko nje ya nyumba yake iliyoko katika mji mdogo wa Craig. Maskani yake hasa hasa, kwa miaka mingi, ni katika mji wa Bozeman, Montana.

Wanafunzi hao wawili ni kati ya wanafunzi 29 wa chuo cha St. Olaf, ambao nilienda nao Tanzania mwezi Januari, 2013, kuwasomesha kuhusu maandishi na safari za Hemingway katika Afrika Mashariki, miaka ya 1933-34 na 1953-54.

Wakati tukiwa Tanzania, wanafunzi hao walinisikia nikiongelea habari za Mzee Patrick Hemingway, kwamba ni mtoto pekee aliyebaki wa Ernest Hemingway, na kwamba nina mawasiliano naye kwa simu, na kwamba ninapangia kwenda Montana kuonana naye.

Huyu mwanafunzi aliyevaa kaptura alisema bila kusita kuwa baba yake angewezeza kutupeleka Montana kwa ndege yake. Hatimaye, siku tuliyopanga, alikuja na ndege yake hapa Minnesota, akitokea nyumbani kwake Ohio. Tulipokutana, nilikuja kufahamu kuwa baba huyu sio tu shabiki wa maandishi ya Hemingway, lakini pia ni msomaji hodari wa vitabu, vya fasihi ya ki-Ingereza, ingawa shughuli zake kimaisha ni biashara.

Kama nilivyogusia kabla, Mzee Patrick Hemingway aliwahi kuishi Tanzania kwa miaka yapata 25 akifanya shughuli kadhaa, ikiwemo ya utalii na kufundisha chuo cha Mweka. Alitukaribisha vizuri sana, tukaongea naye kwa masaa mengi. Huyu mwanafunzi mwingine ni mpiga picha na video, na alirekodi mazungumzo hayo, ambayo ni hazina kubwa. Yana mengi kuhusu maisha, maandishi na mitazamo ya Hemingway, na pia habari nyingi kuhusu waandishi wengine wa nyakati za Hemingway, hasa wale waliokuwa na mawasiliano au uhusiano na Hemingway.

Tuliwazia kwenda tena Montana huu mwezi Mei, kama mwaka jana, lakini kutokana na mimi kuumwa tangu mwanzo wa mwaka, hatujaweza kufanya hiyo safari. Tuna matumaini ya kwenda baada ya miezi michache kuanzia sasa, nitakapokuwa nimepona kabisa, Mungu akipenda.

Kuna mengi bado ya kuongea na Mzee Patrick Hemingway. Jambo moja muhimu ni maisha yake Tanzania. Hilo ni suala ambalo napenda kulifuatilia sana, hasa nikizingatia kuwa mwaka 1954, Hemingway mwenyewe alikwenda hadi Iringa kumtembelea mwanao Patrick akakaa yapat5a wiki tatu. Hiyo ni habari ambayo nataka kuifuatilia kwa undani. Hatujui, huenda Hemingway aliandika hiki au kile kuhusu Iringa, kwani hakuwa mtu aliyekaa mahali asiandike mambo ya mahali hapo. Suala hili linahitaji kufanyiwa utafiti wa kina katika hifadhi ya maandishi ya Hemingway yaliyoiko Cuba na pia maktaba ya John F. Kennedy kule Boston. Mungu akinijalia uzima, nategeme4a kwenda huko miaka ya usoni.

Thursday, May 22, 2014

Ninablogu kwa Faida Yangu Mwenyewe

Ninablogu ili kuhifadhi kumbukumbu, fikra, na hisia zangu. Ninafurahi kufanya hivyo. Hadi sasa, nimehifadhi mengi sana ambayo bila shaka ningekuwa nimeyasahau.

Kila mtu ana mawazo, fikra na hisia. Ni mambo binafsi. Hapa ni tofauti na darasani kwangu au katika  majarida na vitabu vya taaluma. Sina mpango wa kuifanya blogu hii iwe sawa na darasa langu la chuo kikuu, au jarida la kitaaluma.

Ikitokea nimeandika humu ujumbe wenye kugusia taaluma, hiyo ni sawa, lakini, kama ninavyosema blogu hii inanisaidia mimi kuhifadhi mambo yangu, mengine yakiwa ni mambo binafsi.

Mara kwa mara naonglea vitabu. Ninapofanya hivyo najitunzia kumbukumbu kuhusu vitabu hivyo. Sijui kama kuna yeyote anayepata dukuduku na hamasa ya kuvitafuta na kuvisoma. Huo ni uamuzi wa mtu. Wako watu ambao hawana hamu na kitu kinachoitwa kitabu. Lakini mimi sitachoka kuandika kuhusu vitabu, kwani navienzi na kuvipenda sana. Ninafurahi kujitunzia habari za vitabu hivyo, ingawaje kwa ufupi.

Wednesday, May 21, 2014

Biashara, Ujasiriamali, na Vitabu

L
Nina vitabu kadhaa kuhusu biashara na ujasiriamali. Mara moja moja huvipitia. Ninajielimisha katika uwanja wa ujasiriamali kwa mategemeo kuwa nami nitakuwa mjasiriamali. Ninavutiwa na ujasiriamali jamii, ambayo ni tafsiri yangu ya "social entrepreneur." Mjasiriamali jamii hawanii kujitajirisha yeye binafsi kwa fedha, bali hutafuta hizo fedha ili zimwezeshe kutoka mchango wa manufaa kwa jamii.

Kitabu kimojawapo ambacho nakipenda sana na nakipendekeza kwako msomaji wa blogu hii ni  Leaving Microsoft to Change the World: An Enterpreneurs Odyssey to Educate the World's Children (New York: HarperBusiness, 2007) kilichoandikwa na John Wood.

Wakati huu, nasoma kitabu kiitwacho Reengineering the Corporation: A Manifesto for Business Revolution (New York: Harper Collins Publishers, 1993) kilichoandikwa na Michael Hammer na James Champy.

Reengineering the Corporation ni kitabu maarufu sana. Nilikinunua miaka michache iliyopita baada ya kusoma kauli za wataalam zilizoonesha ubora wake. Siku chache zilizopita, niliamua kukisoma. Ninaamini kama vile ingekuwa dini, umuhimu wa kusoma vitabu, hasa kuhusu nyanja ambazo mtu huna ujuzi nazo. Inakupanua akili na kadiri unavyosoma vitabu unakuwa tajiri wa fikra, mawazo, na mitazamo kuliko yule asiyesoma. Ni lazima tukubali hilo.

Reengineering the Corporation ni kitabu kinachofundisha jinsi makampuni na mashirika yanavyopaswa kujibadilisha daima ili kujipatia ufanisi zaidi na kuweza kukabiliana na hali halisi ya utandawazi na ushindani. Hakuna namna nyingine bali kujibadilisha kwa hali zote na muda wote, vinginevyo shirika au kampuni inajichimbia kaburi.

Mambo yanayohitaaji mabadiliko ni pamoja na muundo wa shirika au kampuni, mtindo wa utoaji huduma, mahusiano miongoni mwa wafanyakazi, na baina ya wafanyakazi na wateja, pia matumizi ya tekinolojia mbali mbali, kama vile "information technology." Ni muhimu kutong'ang'ania jadi na mazoea. Lazima kufanya mabadiliko mapema kwani hali halisi ya dunia, wateja, na ushindani hubadilika daima na haitabiriki.

Ningekuwa mfanyabiashara ningefanya kila juhudi kujielimisha kwa kusoma vitabu vya aina hii, kwani elimu ni mtaji muhimu.


Friday, May 16, 2014

Vitabu Vya Kutuendeleza Kimaisha

Katika ujumbe wangu wa jana, kuhusu nia yangu ya kuandika kitabu kingine kufuatia kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, nilisisitiza umuhimu wa kujiamini. Hilo ni fundisho linalotolewa katika vitabu vingi, labda niseme vyote, vinavyojadili suala la maendeleo ya mtu binafsi, kumweka katika hali ya kufanikiwa.

Pamoja na kujiamini, mtu unapaswa kuangalia uwezo wako na kuutumia, badala ya kukaa na kulalamika kuwa huna hiki au kile, au kuwasikiliza watu wanaojaribu kukukwamisha au kukukatisha tamaa. Hakuna sababu ya kuwa na watu kama hao, bali ambatana na watu wanaosonga mbele na wana mtazamo wa kusonga mmbele.

Jana hiyo, nilitaja kitabu kimojawapo ambacho ni maarufu, kiitwacho The Power of Positive Thinking. Sijui ni wa-Tanzania wangapi wanakifahamu kitabu hiki, wamekisoma, au wanakisoma. Kama wapo, watakuwa ni wachache sana, kama vile kijana Meshack Maganga wa Iringa, ambaye habari zake naziona kwenye mitandao kama Facebook.

 Kwanza, kuna suala la lugha. Wa-Tanzania wamepuuzia ki-Ingereza, kwa visingizio mbalimbali. Kwa hivi, ni lazima elimu iliyomo katika vitabu hivi inawapitia mbali; wanabaki gizani, wakiwa na fikra na mitazamo ya kuwakwamisha. Pili, kwa ujumla, wa-Tanzania hawana utamaduni wa kununua na kusoma vitabu. Hilo ni janga la Taifa.

Kwa miaka kadhaa nilikuwa nimekisikia kitabu cha The Power of Positive Thinking. Nimesoma baadhi ya vitabu vya aina hiyo, lakini sio hicho. Hivi karibuni, nilipolazwa kwa wiki sita katika hospitali ya Abbott Northwestern ya mjini Minneapolis, nilikwenda na nakala yangu ya kitabu hiki, nikawa najikongoja kukisoma kidogo kidogo, kutokana na hali ya kuumwa na kuwa kitandani siku zote.

Baada ya kuja kupumzika nyumbani, ingawa naendelea na matibabu, nimemaliza kukisoma kitabu hiki. Kina mafundisho mengi na ushauri wa thamani. Jambo moja ambalo limenikaa sawa sawa akilini ni kuwa fikra na mtazamo ulio nao, ndio msingi wa kufanikiwa au kutofanikiwa. Ukiwa na fikra za kutojiamini, au fikra kwamba hiki au kile huwezi, basi hutaweza. Utabaki hivi hivi ulivyo.

Fikra na mtazamo ndizo zinakuongoza au kukukwamisha maishani. Kama huna mafanikio, ni wewe mwenyewe unasababisha hali hiyo. Tukirudi Tanzania, tunaona matatizo makubwa. Wengi hawajiamini; hawaelewi kuwa kufanikiwa au kutofanikiwa ni juu yao, badala yake wanakuja na visingizio au wanatafuta wachawi.. Utawaona wanaenda kwa waganga wa kienyeji, kwa mfano. Au utawasikia wakitafuta wa kumlaumu, kama vile wa-Islamu wengi wa Tanzania wanavyoaminishwa kwamba tatizo ni "Mfumo Kristo."

Basi, napenda kusisitiza kuwa ni muhimu tujibidishe kusoma vitabu mbali mbali vinavyotufungua macho na akili ili tuwe watu wa kujiamini, kutambua uwezo wetu na neema tulizojaliwa; tuzitumie juhudi yote ili tufanikiwe. Ndio maana katika ujumbe wangu wa jana, nilielezea kwa kujiamini azma yangu ya kuandika kitabu kingine kufuatia kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Nilitamka bila kusita kuwa hiki kitakuwa kitabu bora kabisa, kuliko hiki kingine, ingawa ni maarufu miongoni mwa wasomaji.

Thursday, May 15, 2014

Kitabu Kingine Kufuatia "Africans and Americans: Embracing Cultural Differences"

Ni yapata miaka tisa sasa tangu nichapishe kijitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences
Kadiri siku zinavyopita, wazo la kuandika kitabu kingine cha aina ile linazidi kuimarika akilini mwangu.

Tangu pale nilipochapisha Africans and Americans, nilifahamu kuwa sijaongelea masuala yote ambayo ningependa au ningeweza kuongelea. Sikupenda kuandika kitabu kikubwa; ilinibidi nifanye uchaguzi wa mada na kuandika kitabu kidogo.

Wazo la kuandika kitabu hiki cha pili nimekuwa nalo kwa miaka mingi. Kuna wasomaji wa Africans and Americans ambao, tangu mwanzo, walinishauri niandike kingine, ili kuongelea masuala ambayo sikuwa nimeyaongelea. Nami niliafiki wazo hilo.

Vile vile, kwa miaka yapata saba hivi nimeandika sura ambazo zitakuwemo katika hiki kitabu kipya. Ingawa Africans and Americans kimejipatia sifa tele miongoni mwa wasomaji, nilipania kuwa kitabu hiki kinachofuata kiwe bora  zaidi.

Uwezo wa kuandika kitabu bora zaidi ninao.Mungu akinijalia uzima, nitakamilisha kazi hiyo. Sio kazi ya wiki chache, au miezi michache. Nahisi itachukua miaka, ingawa, kama nilivyosema, sura kadhaa nilishaandika. Nataka kutumia uwezo wangu wa lugha kwa ufanisi kuliko ambavyo nimefanya kabla. Kitabu hiki kitakuwa kimeandikwa kwa ki-Ingereza kizuri sana, mfano wa kuigwa. Uwezo wa kuandika hivyo ninao, bora tu niwe na muda wa kutosha. Kama Ernest Hemingway alivyotufundisha, uandishi bora ni kazi ngumu inayohitaji muda sana.

Halafu, sina haraka, tofauti na mazingira ambamo niliandika Africans and Americans. Niliandika kitabu kile kwa kusukumwa na maprofesa tuliokuwa katika bodi ya uongozi wa Associated Colleges of the Midwest, ambao ni jumuia ya vyuo kumi na nne maeneo haya ya katikatika ya Marekani (USA. Kwa kutambua changamoto za kuwaelimisha wanafunzi wanaoenda kusoma Afrika kuhusu tofauti za utamaduni, na kwa kutambua kuwa hapakuwa na kitabu cha mwongozo cha kufaa kwa shughuli hiyo, waliniomba na kunishinikiza niandike. Nami nilifanya hivyo, ili kuhitimisha andiko hilo kwa muda mfupi, lianze kutumika.

Ninaongea hivi kwa sababu nataka kuwashauri wengine umuhimu wa kujiamini. Vitabu mbali mbali ambavyo nimekuwa nikisoma kuhusu maendeleo na mafanikio binafsi vinasisisitza umuhimu wa kujiamini, sio kuangalia zaidi vipingamizi, na matatizo, bali uwezo na fursa. Kitabu kimojawapo ambacho ningeshauri kila mtu asome ni The Power of Positive Thinking, kilichoandikwa na Norman Vincent Peale (New York: Simon and Schuster, 2011) kikachapishwa  mara ya kwanza mwaka 1952.

Wednesday, May 14, 2014

Nimejifunza Katika Kuwapiga Picha Ndege

Nimejifunza mambo kadhaa katika kuwapiga picha ndege  kiasi cha yadi chache tu kutoka hapa nyumbani.

Kwanza sio ndege wa aina zote wanaruka zao  ukijaribu kuwasogea. Kuna aina ya ndege ambao  wana subira. Hao ni rahisi kuwapiga picha.

Katika ujumbe wangu wa juzi, sikufafanua suala hilo. Kwa hivi, leo narekebisha kauli yangu.


Jambo jingine ambalo nimejifunza ni kuhusu matumizi ya "zoom" kwenye kamera. "Zoom" ikielekezwa kwa ndege peke yake, halafu akakuzwa sana bila kitu kingine pembeni,  inapotosha ukubwa au udogo halisi wa ndege huyu. Ndege mdogo kabisa anaweza kuonekana mkubwa kama kuku.

Kwa hiyo leo nimejaribu kuwaonesha ndege wakiwa katika mazingira yao ili ukubwa au udogo wao ufananishwe na nyasi zinazowazunguka, au majani, au vijiti.

Monday, May 12, 2014

Ndege Mhandisi

Leo, katika matembezi huko nje, nilimwona ndege huyu akiwa ardhini, sio mtini. Alikuwa ng'ambo ya barabara, name nikiwa ng'ambo ya pili.

Kwa macho, alionekana ndege mdogo. Lakini nilipompiga picha, nikiwa nimefungua "zoom" ya kamera, nimegundua kuwa alikuwa amebeba nyasi mdomoni. Bila shaka ni nyasi za kujengea kiota.

Nilivutiwa na jinsi ndege huyo alivyo na nidhamu. Alifanya kazi hiyo bila usimamizi au amri ya yeyote. Na aliifanya kwa uaminifu ina kujiamini. Laiti wanadamu wote tungekuwa na moyo wa aina hii.

Sunday, May 11, 2014

Najaribu Kuwapiga Picha Ndege

Yapata wiki mbili zilizopita, nilinunua kamera mpya kule Amazon.com. Kwa vile bado afya yangu haijatengemaa, siendi mbali, bali hatua kadhaa tu kutoka hapa nyumbani. Kwa vile kipindi cha baridi kali kinaonakana kwisha, mazingira huko nje ni mazuri. Nyasi zimeota kwa vingi; hali ya hewa imeanza kuvutia,  na wanyama wadogo wadogo na ndege wa kila aina wanaonekana huko na huko.

Nimekuwa na hamu sana ya kupiga picha za ndege, lakini nimegundua ugumu wake. Ndege ni wajanja sana, wepesi kurukia tawi jingine unapotaka kuwapiga picha, au kuruka na kwenda zao. Lakini jana niliwaona ndege wawili wakubwa wakitembea pamoja. Sikuwa nimechukua kamera. Leo nilitoka tena, na ndege wale walikuwa sehemu ile ile ya jana wakitembea. Hao ingawa wanatembea, sio vigumu kuwapiga picha, nami nimepiga picha kadhaa. Kamera yangu ina "zoom" nzuri; kwa hivi sio lazima kuwasogea sana. Sina uzoefu na kamera hii; bado ninajifunza namna ya kuitumia katika vipengele vyake vyote.


Nmeamua kuwatafuta ndege na kuwapiga picha kutokana na kuvutiwa na picha anazopiga rafiki yangu, Profesa Bill Clemente wa Peru State College, Nebraska. Navutiwa sana na picha zake, na huwa nashangaa hao ndege anawawezaje. Picha zake nyingi huziweka katika Facebook. Hapo ndipo ninapoziona na kuzifurahia. Labda siku za usoni nami nitakuwa na uwezo kama wake.

Friday, May 9, 2014

Kitabu Kinawasaidia Wasafiri waMarekani

Ni furaha kwangu ninapoona malengo niliyokuwa nayo katika kuandika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences yanaendelea kutimia. Lengo kubwa lilikuwa kuwasaidia Wamarekani kuufahamu utamaduni wa MwAfrika, kadhalika kuwasaidia waAfrika kuufahamu utamaduni wa waMarekani.

WaMarekani wana tabia ya kusoma kuhusu nchi waendako. Nimeshaona tena na tena jinsi wale waendao Afrika wanavyosoma kitabu changu hicho Kama sehemu ya maandalizi ya safari.

Jana, wakati navinjari mtandaoni, niliona taarifa kutoka kwa wasasfiri kutoka Wisconsin ambao walienda Tanzania hivi karibuni. Kwa vile walishasoma kijitabu changu kabla ya kusfiri, ilikuwa rahisi kwao kuelewa mambo walioyoyaona kule Tanzania. Katika taarifa yao wameandika hivi:

In the United States we are accustomed to running from place to place, chasing time and cramming all we can into a day. In Tanzania we found a slower pace--we experienced "African Time." The day is not driven by the clock but rather shaped by people's relationships. It is accepted practice to be "late" as a result of lending a helping hand, catching up with an old friend, or extending hospitality to a stranger. This is something we learned prior to landing at the Julius Nyerere International Airport, having read "Africans and Americans: Embracing Cultural Differences" by Joseph L. Mbele as part of our seminar pre-work.

Kifungu hiki nimekinukuu kutoka katika taarifa nzima, ambayo ni hii hapa:www.leadershipwisconsin.org/2014/04/24/safari-of-a-lifetime-part-I/.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...