Wednesday, January 28, 2015

Katika Blogu, Sijui Ninamwandikia Nani Zaidi Yangu Mwenyewe

Je, mwandishi wa blogu anamwandikia nani? Kwa mtazamo wangu, hili ni suali gumu. Naliona gumu kulitafakari, achilia mbali kulijibu.

Baada ya kuona ugumu wa suali hili, nimeamua kukiri kuwa ninajiandikia mwenyewe. Ndio maana makala ninazoandika aghalabu zinanihusu mimi mwenyewe, shughuli zangu, matatizo na mafanikio yangu, mategemeo yangu na kumbukumbu zangu.

Sipendi sana kuwaongelea watu wengine, wala sipendi sana kuongelea mambo kinadharia, bila kujihusisha mwenyewe. Naweza kusema kuwa ndivyo nilivyoandika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Sijajificha nyuma ya pazia la nadharia au taaluma. Nimejiweka wazi kwa namna nilivyoweza.

Mwandishi Ernest Hemingway aliongelea suala hili vizuri alipofafanua dhana ya ukweli katika uandishi. Nilivyomwelewa, anasema kuwa ukweli katika uandishi ni kwa mwandishi kuifungua na kuiweka bayana nafsi yake.

Ningependa sana niweze kuandika namna hii aliyoongelea Hemingway. Ni ndoto inayovutia, sawa na nyota inayong'aa mbali, ambayo mtu unaifuata kwa hamu ingawa haifikiki. Lakini, naona huku ndiko kujiandikia mwenyewe.

Kusema kuwa kuna hadhira ninayoiandikia katika blogu yangu ni kama kuota ndoto. Ni kujidanganya. Nasema hivi sio tu kutokana na tafakari yangu mwenyewe, bali ninakumbuka makala ya kufikirisha ya Walter J. Ong, "The Writer's Audience is Always a Fiction."

(Picha hapo juu nilijipiga mwenyewe jana, kwa ajili ya matangazo ya mihadhara yangu Mankato)

Sunday, January 25, 2015

Mipango ya Ziara Yangu Mankato Inaendelea

Kama nilivyoandika katika blogu hii, nitakwenda kuongea na wanafunzi wa chuo cha South Central mjini Mankato. Mipango ya ziara hii, ambayo itafanyika tarehe 24 Februari, inaendelea vizuri.

Mwenyeji wangu, mwalimu Rebecca Fjelland Davis, amenieleza kuwa shughuli ya kwanza nitakayofanya siku hiyo ni kuongea na wanafunzi katika darasa lake, kuanzia saa nne hadi saa tano na dakika hamsini asubuhi. Hao ni wanafunzi wanaojiandaa kwa safari ya kimasomo Afrika Kusini. Kama sehemu ya maandalizi hayo, wanasoma kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, na maongezi yangu nao yatahusu yale niliyoandika kitabuni.

Baada ya darasa hilo, kuanzia yapata saa sita, nitatoa mhadhara kwa wanachuo na wana jamii. Mwalimu Fjelland Davis ameniarifu kuwa duka la vitabu la hapo chuoni litakuwa limeandaa nakala za kitabu changu, kwa ajili ya kuuza. Kama ilivyo desturi hapa Marekani, nategemea kuwa baada ya mazungumzo nitasaini nakala za vitabu.

Hii sio mara yangu ya kwanza kufanya shughuli mjini Mankato. Nimewahi kwenda kutoa mhadhara katika Chuo Kikuu cha Mankato kwa wanachuo waliokuwa wanajiandaa kwenda Afrika Kusini. Nilialikwa na Profesa Scott Fee, ambaye ni muasisi na mratibu wa mpango wa ushirikiano baina ya chuo kikuu cha Mankato na chuo kiitwacho Eden Campus cha Afrika Kusini. Nakumbuka ukumbi ulivyojaa watu siku hiyo, nami kwa kutekeleza ombi la Profesa Fee, niliwasilisha nakala yapata 40 za Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Nimewahi pia kushiriki maonesho ya Deep Valley Book Festival, na mengine yaliyofanyika katika uwanja wa maonesho ya magari, ambao jina lake nimesahau. Ningekuwa na blogu miaka ile, ningekuwa nimeandika taarifa. Siku nyingine nilialikwa Mankato na taasisi inayoshughulika na huduma kwa jamii, nikaongea na wahamiaji na wakimbizi kutoka nchi mbali mbali, kama vile Somalia, Ethiopia, na Sudani. Mazungumzo hayo yaliripotiwa katika gazeti la Mankato Free Press.

Nikirudi kwenye mwaliko wa tarehe 24 Februari, napenda kusema kuwa Mwalimu Fjelland Davis na Profesa Scott Fee wanashirikiana katika mpango wa kupeleka wanafunzi Afrika Kusini. Wote wawili walihusika katika mhadhara niliotoa kwa wanafunzi wao ambao taarifa yake iliandikwa hapa na hapa.

Saturday, January 24, 2015

Wanachuo wa Gustavus Adolphus Wako Tanzania

Wanachuo wa chuo cha Gustavus Adolphus, ambao niliongea nao kabla ya safari yao, walifika salama Tanzania. Wako Tanzania kwa ziara ya kimasomo kwa mwezi moja. Wamekuwa wakiandika kuhusu ziara yao katika tovuti ya chuo chao.

Walitua uwanja wa ndege wa kimataifa wa Kilimanjaro wakatembelea sehemu kama hospitali ya KCMC na shule ya wasichana ya Maasae. Kisha walienda Iringa, ambako wameshatembelea sehemu kama vile Chuo Kikuu cha Iringa, soko kuu, na hospitali ya Ilula. Wamesafiri hadi Tungamalenga, pembeni mwa hifadhi ya Ruaha, ambapo wamepata fursa ya kutembelea hospitali na kuangalia utendaji kazi wake.

Kwa ujumla, wanachuo hao, kama ilivyo kwa wa-Marekani wengine wanaotembelea Tanzania, wanaifurahia nchi yetu na watu wake. Wanawasiliana na familia zao na marafiki huku Marekani, na kwa namna hii jina la Tanzania linasambaa kwa namna nzuri. Kwa kawaida, ziara za wanafunzi nazienzi kuliko zile za watalii. Kwa vile wanafunzi wanajumuika na wananchi katika mazingira mbali mbali, wanaondoka wakiwa na ufahamu fulani wa jamii yetu kuliko watalii, ambao wanakaa nchini mwetu siku chache tu, wakikimbizwa kutoka kivutio kimoja hadi kingine, hasa Mlima Kilimanjaro, mbuga za wanyama, na fukwe za bahari.

Kwangu ni heshima na furaha kuweza kuchangia maandalizi ya vijana hao, kama ninavyofanya mwaka hadi mwaka, kupunguza matatizo yanayoweza kutokea sababu ya tofauti za tamaduni. Haiwezekani mgeni aelewe kila anachoshudia katika utamaduni usio wake. Hata mimi ilinichukua miaka mingi hadi kuanza kuelewa misingi muhimu ya utamaduni wa Marekani, kama nilivyoelezea katika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, na bado ninajifunza. Ndio maana, wanafunzi wanaporejea tena nchini kwao Marekani, tunajitahidi kuongea nao kuhusu yale waliyoyashuhudia kwenye nchi waliyoitembelea, ili wawe na ufahamu zaidi.

Friday, January 23, 2015

Kwa Anayewazia Kuchapisha Kitabu

Wazo la kuchapisha kitabu linawavutia watu wengi. Ni wazo lenye ndoto za mafanikio.Wako wanaoamini kuwa kuchapisha kitabu kutawapa umaarufu. Kuna wanaoamini kuwa kuchapisha kitabu kutawaletea fedha nyingi. Wengi, labda wote, wanaamini kuwa wakisha chapisha kitabu, kazi yao inakuwa imemalizika; kinachobaki ni kungojea matokeo, kama vile umaarufu na fedha.

Ni bora mtu anayewazia kuchapisha kitabu ajielimishe zaidi kuhusu jambo hili, nami hupenda kuchangia yale ninayoyafahamu, kwa kadiri ya uwezo wangu. Vipengele ni vingi, lakini hapa nitaongelea vichache tu.

Mtu uandike kitabu kutokana na kujua kuwa una jambo la kusema kimaandishi. Uwe una jambo ambalo linakuelemea akilini mwako na kukusukuma uandike. Msukumo utoke ndani ya nafsi yako. Ukishaandika kitabu kwa msingi huo, utajisikia una raha sawa na mtu aliyetua mzigo. Kuridhika kwako ndilo jambo mihimu. Mengine yanafuata baadaye.

Huenda kitabu chako kitawavutia watu wakakinunua na kukisoma, au huenda kisiwavutie. Lakini sidhani kama hili ni tatizo lako, maadam umeshakidhi haja ya kutua mzigo uliokuwemo akilini mwako, na sasa uko huru kuwazia mambo mengine. Uhuru huu ni jambo muhimu.

Katika miaka yangu ya kuandika, na hata kuchapisha vitabu, nimekuwa nikisoma kuhusu uandishi, uchapishaji na uuzaji wa vitabu. Kitu kimoja mihimu nilichojifunza ni kuwa kuandika na kuchapisha kitabu sio mwisho wa kazi yako kama mwandishi. Kuna kazi kubwa mbele yako, kazi ya kuutangazia ulimwengu kuhusu kuwepo kwa kitabu chako, na kazi ya kukiuza kitabu chako.

Watafiti na waandishi wa masuala hayo wanasisitiza kuwa wajibu wa kuuza kitabu ni yako wewe mwandishi. Kabla ya kuanza kusoma mawazo haya, niliamini, kama wengi wanavyoamini, kwamba kazi ya kutangaza na kuuza kitabu ni ya mchapishaji. Kumbe, hata kama mchapishaji anaweza kuchangia katika jukumu hilo, mwandishi unawajibika sana, na pengine zaidi kuliko mchapishaji.

Kwa upande wa Tanzania, kwa hali ilivyo, tatizo kubwa ni kwamba utamaduni wa kununua na kusoma vitabu ni hafifu sana. Watu wengi wanadhani kusoma vitabu ni shughuli ya wanafunzi, na hivi vitabu viwe vimo katika mitaala ya shule.

Kujisomea vitabu bila shinikizo la shule au mitihani ni utamaduni ambao unakosekana. Hii ni sababu moja inayonifanya nitoe angalizo kuwa mtu unaweza kuchapisha kitabu na kisiwe na wasomaji.

Masuala haya ya uandishi na uuzaji wa vitabu nimeyaelezea katika kitabu changu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii, na katika makala mbali mbali katika blogu hii. Ninaendelea kujielimisha kuhusu masuala hayo, na nitaendelea kuandika.

Tuesday, January 20, 2015

Mihadhara Nisiyolipwa

Nimewahi kuongelea suala la kulipwa ninapotoa mihadhara. Nilisema kuwa wa-Marekani wanapokualika kutoa mhadhara huuliza malipo yako ni kiasi gani. Nilitamka kuwa huwa sitaji kiasi ninachotaka kulipwa, bali nawaachia wanaonialika waamue kufuatana na uwezo wao. Hata kama hawana uwezo, niko tayari kuwatimizia ombi lao.

Napenda kufafanua kidogo kuhusu utoaji wa mihadhara bila kulipwa. Labda wako watu ambao watashangaa kwa nini ninaridhika kutoa mihadhara ya aina hiyo. Labda wako watakaosema ninapoteza muda wangu. Huenda wengine wataniona nimechanganyikiwa. Ni jambo la kawaida kwetu wanadamu kuwa na fikra na mitazamo inayotofautiana.

Nina sababu zangu kwa kuwa na huu msimamo wangu. Kwanza ninatanguliza ubinadamu na utu, sio hela. Kuwasaidia wengine ni jambo jema sana, ambalo lina maana kuliko hela. Unaweza kuwa na hela nyingi ukazifuja, zisikuletee faida yoyote maishani, lakini, kama walivyosema wahenga, wema hauozi.

Kuna usemi mwingine, "Tenda wema nenda zako; usingoje shukrani." Ni usemi unaoniongoza na kunipa faraja maishani. Nazingatia kuwa kuna Mungu, ambae ndiye anayenipa uzima siku hadi siku, na akili timamu ya kuweza kuelewa mambo na kuwafundisha wengine. Siwezi kujivunia au kuringia vipaji alivyonipa Mungu, kwani ni dhamana kwa manufaa ya walimwengu. Falsafa hii inanitosha kikamilifu.

Ninapotoa mhadhara popote, kwa watu wenye kunilipa, wasio na uwezo wa kunilipa, au wenye uwezo kidogo sana, ninajua kuwa ni fursa ya mimi kujiongezea uzoefu na elimu, hasa wakati ninapojiandaa na wakati wa masuali na majibu. Uzoefu na elimu ni bora kuliko hela. Ni mtaji  unaoweza kutumiwa kuzalisha hela nyingi. Huenda ni mtaji imara kuliko yote.

Nilipwe nisilipwe, ninapotoa mhadhara ninalichukulia jukumu langu kwa dhati na umakini wa hali ya juu. Ninajua kuwa ni fursa ya kujinadi, bila mimi kulipia, kama tunavyolipia matangazo. Kwa ufafanuzi zaidi, napenda niseme kuwa mihadhara ninayoongelea hapa aghalabu huhusu masuala ya elimu na tofauti za tamaduni na athari zake katika dunia ya utandawazi wa leo. Wanaonialika hufanya hivyo kutokana na kusoma maandishi yangu, kama vile kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Kwenye mhadhara, nakala zinakuwepo na zinauzwa.

Kutoa mihadhara bila kulipwa si kupoteza muda wala si hasara. Ni aina ya uwekezaji. Huwezi kujua hao wanaokusikiliza ni watu wa aina gani. Huenda wako ambao wana uwezo wa kukuunganisha na jumuia, taasisi au kampuni zitakazopenda kukualika na zenye uwezo wa kukulipa. Mungu husawazisha yote, tena kwa namna tusiyotegemea. Narudi kwenye usemi kuwa wema hauozi. Kukataa kuwahudumia watu kwa vile tu hawana uwezo wa kukulipa ni kukosa upeo wa kuona mbali.

Nimeona niseme hayo machache, kujiwekea kumbukumbu za mtazamo wangu kwa wakati huu. Akili yangu haijasimama, bado natafakari masuala ya aina hii, na hakuna ubaya iwapo nitarejea tena siku za usoni na kufafanua zaidi mtazamo wangu, kuongeza na kuboresha, au kurekebisha baadhi ya vipengele vyake. Ni matumaini yangu kuwa wako ambao watajifunza kitu kutokana na mawazo yangu.

Wednesday, January 14, 2015

"Leading Beyond the Walls:" Kitabu Murua

Kwa siku kadhaa sasa, nimekuwa nikisoma Leading Beyond the Walls: How High-Performing Organizations Collaborate for Shared Success, kitabu kilichohaririwa na Frances Hesselbein, Marshall Goldsmith, na Iain Somerville. Ni mkusanyo wa makala 23 zilizoandikwa na wataalam mbali mbali katika tasnia ya uongozi, wakizingatia hali halisi ya utandawazi wa leo, na umuhimu wa kwenda na wakati.

Kwenda na wakati kunahitaji wepesi wa kubadilika kifikra, kimwenendo, kimfumo na hali zingine, ili kumudu mahitaji na hali halisi ya mabadiliko yanayotokea ulimwenguni, ambayo hayakwepeki. Mafanikio ya shirika, taasisi, au kampuni
yanategemea utayari wa kujibadili. Mazoea ni kipingamizi kikubwa cha mafanikio; ni kama kuta ambazo tumejizungushia. Jukumu letu, ambalo halikwepeki, ni kuvunja hizo kuta, tuwe na uwanja na upeo usio na mipaka.

Wengi wa watunzi wa makala zilizomo kitabuni humu nilikuwa sijawahi hata kuwasikia, isipokuwa Joseph S. Nye, Jr., Stephen R. Covey, na Peter F. Drucker, ambaye niliwahi kusoma andiko lake mojawapo. Kati ya makala ambazo nilivutiwa nazo hata kabla ya kuzisoma ni "And the Walls Came Tumbling Down" (Jim Collins), "Dissolving Boundaries in the Era of Knowledge and Custom Work" (Sally Helgesen), "Culture is the Key" (Regina Herzlinger, "New Competencies for Tomorrow's Global Leader" (Marshall Goldsmith, Cathy Walt), na "Creating Success for Others" (Jim Belasco).

Kila makala ambayo nimesoma katika kitabu hiki imenipanua mawazo. Nimegundua mambo ya maana ambayo yataboresha mihadhara ninayotoa kwa jumuia, taasisi na makampuni. Nawazia, kwa mfano, mihadhara niliyotoa kwenye kampuni ya RBC Wealth Management.

Ninashukuru kuwa nilinunua kitabu hiki, ingawa sikumbuki ilikuwa lini. Nina ari kubwa ya kumaliza kusoma insha zote zilizomo, na nina hakika kuwa, Mungu akinijalia uzima, nitazisoma tena na tena.

Tuesday, January 13, 2015

Maazimio ya Mwaka Mpya, 2015

Kila unapoanza mwaka mpya, ni kawaida kwa watu kujipangia au kuweka bayana mambo ya kufanya katika mwaka unaoanza. Nami nina yangu, lakini kwanza namshukuru Mungu kwa kuniwezesha kuuvuka mwaka uliopita na kuingia katika mwaka huu mpya.

Jambo la msingi ninalopangia ni kuendelea kufanya bidii katika kazi ambayo naamini Mungu mwenyewe alinipangia, kazi ya ualimu. Kazi hii inajumlisha mambo kadhaa hasa kujielimisha na kuwa tayari muda wote kuwapa wengine yale ninayoyajua. Elimu yangu si yangu pekee, bali ni dhamana kwa manufaa ya wanadamu.

Nitaendelea kusoma vitabu na makala za kitaaluma kwa bidii. Hii ni njia muhimu ya kujielimisha, ili niweze kufundisha kwa ufanisi zaidi.

Nitaendelea kutoa ushauri kwa jumuia na taasisi yoyote au kwa watu binafsi. Hii sio tu kwa faida yao, bali kwa faida yangu, kwani kwa kufanya hivyo ninapata fursa ya kupima ni kiasi gani ninafahamu jambo fulani.

Nitaendelea kufanya utafiti na kuandika. Kuandika ni aina ya ufundishaji. Mwalimu wa kiwango cha chuo kikuu ana wajibu wa kufanya utafiti na kuandika, ili kuchangia taaluma. Nitafanya bidii zaidi katika nyanja hizi.

Jambo moja la msingi ni kuwa nitachapisha vitabu vyangu Tanzania, kwa gharama yangu, ili kuchangia elimu, ingawa ninajua kuwa utamaduni wa kununua na kusoma vitabu kwa ujumla ni hafifu sana.

Nashukuru kuwa mwaka jana nimeweza kusoma vitabu vilivyoelezea vizuri masuala muhimu ya maisha na mafanikio. Jambo moja ambalo limesisitizwa katika vitabu hivyo ni kuwa kama mtu huna mafanikio maishani, kosa ni lako mwenyewe. Usitafute mchawi wala visingizio. Jirekebishe wewe mwenyewe.

Jambo jingine ni kuwa usipoteze muda wako na watu ambao kazi yao ni kujaribu kukusema vibaya au kukukatisha tamaa. Hao ni watu wasio na maana katika maendeleo yako. Usiyumbishwe na watu wa aina hiyo, wala usiwatilie maanani. Zingatia malengo yako. Shirikiana na watu wenye mwelekeo wa maendeleo na mafanikio.

Msingi wa yote hayo ni kumweka mbele Mwenyezi Mungu, mwezeshaji wa yote. Pia kuendelea kuwa sambamba na familia, ndugu na jamaa, na mtandao wa marafiki na wengine wote wenye mapenzi mema.

Saturday, January 10, 2015

Tumefanya Kikao cha Bodi ya "Africa Network"

Leo tulikuwa na kikao cha bodi ya Africa Network. Hii jumuia ya vyuo vya Marekani ambavyo vinataka kushirikiana katika ufundishaji na utafiti kuhusu Afrika. Mwanzilishi wake ni Profesa Tom Benson.

Kikao chetu cha leo kilikuwa cha kutumia simu ("teleconferencing"). Hii ni tekinolojia ambayo haihitaji watu kusafiri na kukutana uso kwa uso. Nimeshiriki mikutano ya aina hii mara nyingi katika nyadhifa zangu kama mwanabodi wa Africa Network na Afrifest.

Leo tumeongelea zaidi masuala ya kutafuta fedha, kuboresha tovuti yetu, na kupata wanachama wengine. Mbali na suala la tovuti yetu, tumeongelea pia suala pana zaidi la kujiingiza katika mitandao ya kijamii kama Facebook na Twitter.

Jambo jingine muhimu ambalo tumekubaliana ni kuwa badala ya kuwa na mkutano wa jumuia yote mwaka huu, tufanye kikao cha wanabodi pekee, ili kujinoa katika masuala mbali ya uendeshaji wa Africa Network na kujipanga kwa miaka ijayo. Tutafanya kikao hiki mwezi Aprili, mjini Chicago.

Thursday, January 8, 2015

""Till I End My Song:" Tungo za Mwisho za Washairi Maarufu

Kila siku ninapokuwa chuoni St. Olaf, ambapo nafundisha, sikosi kupita katika duka la vitabu. Mbali ya vitabu vilivyomo dukani, wanaweka pia vitabu vingi kwenye meza na makabati nje ya duka. Hapo nje unaweza kuvipata vitabu kwa bei nafuu kuliko kuviagiza wewe mwenyewe sehemu nyingine.

Basi, siku moja, katika kuangalia angalia vitabu hapo nje, nilikiona kitabu ambacho rangi za jaladaa lake zilinivutia. Nilivutiwa zaidi nilipoona kimehaririwa na Harold Bloom, na kinauzwa kwa  dola 4.98, ambalo ni punguzo kubwa, kwani bei yake ya halisi ni dola 24.99. Hapo hapo niliamua kukinunua, ingawa nilikuwa na hela kidogo tu, kwani ilikuwa ni mara tu baada ya Krismasi, huku tungiingojea siku kuu ya Mwaka Mpya.

Harold Bloom ni bingwa mojawapo duniani katika masomo ya ki-Ingereza na fasihi yake, sio tu kwa upande wa uchambuzi wa maandishi bali pia upande wa nadharia ya fasihi. Ameandika au kuhariri vitabu vingi. Nilipokuwa nasomea shahada ya uzamifu katika Chuo Kikuu Cha Wisconsin-Madison, 1980-86, tulisoma baadhi ya maandishi ya Harold Bloom, sambamba na maandishi ya watalaam wengine, kama vile M.H. Abrams, Jacques Derrida, Edward Said, Wayne Booth, Michael Raffartere, Terry Eagleton, na Fredrick Jameson. Ninavyo baadhi ya vitabu vya wataalam hao, na nimehudhuria mihadhara ya Edward Said, Wayne Booth, na M.H. Abrams.

Nilivyoona hiki kitabu kipya, Till I End My Song, chenye jina la Harold Bloom, sikuweza kujizuia kukinunua. Nilivyoona kitabu kimeelezwa kama "A Gathering of Last Poems" nilipata shauku ya kukiangalia zaidi, hata kabla ya kukinunua. Nilihisi kuwa ni mkusanyiko wa mashairi ya waandishi maarufu, ambayo yalikuwa ni mashairi yao ya mwisho au ya mwisho mwisho kabla hawajafariki. Hapo dukuduku na shauku vikanielemea. Nilivutiwa, kwani sikuwahi kusikia kuhusu kitabu kilichojaribu kufanya hivyo katika lugha yoyote.

Dukuduku yangu ilikuwa kubwa: je, tungo za mwisho kabisa za washairi maarufu kama Shakespeare, Christopher Marlowe, Milton, Geradd Manley Hopkins, Wallace Stevens, na Robert Lowell, zilikuwaje? Walisema nini? Walituachia usia gani? Nilikuwa nimesoma mashairi mengi ya watunzi hao, lakini sikuwahi kuwazia dhana hii ya mkusanyiko wa mashairi yao ya "lala salama," kama wasemavyo wa-Swahili.

Harold Bloom anafafanua, katika sentensi za mwanzo kabisa za utangulizi wake, maana ya "last poems," dhana iliyomwongoza katika kuandaa kitabu hiki. Nanukuu:

There are three kinds of "last poems" in this anthology. Some literally are the final poems these women and men composed. Others were intended to mark the end, though the poet survived a while longer and continued to work. A third group consists of poems that seem to me an imaginative conclusion to a poetic career. With all three kinds I have made an aesthetic judgement: everything in this volume is here because of its artistic excellence.

Kwa jinsi kitabu hiki kilivyokusanya tungo za washairi mashuhuri sana, wa tangu zamani hadi leo, ni hazina kubwa kwa yeyote anayependa kuuelewa urithi wa uandishi katika lugha ya ki-Ingereza.

Tuesday, January 6, 2015

Mazungumzo ya Jana na Wanachuo wa Gustavus Adolphus Yalifana

Jana niliandika taarifa fupi kuhusu mazungumzo yangu na wanachuo wa chuo cha Gustavus Adolphus. Ningeweza kuandika kirefu na kuelezea, kwa mfano, masuali niliyulizwa kuhusu yaliyomo na yasiyokuwemo katika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Ningeweza kuelezea jinsi wanachuo na wakufunzi wao walivyoyapenda mazungumzo yale, kama walivyoniambia wao wenyewe.

Lakini niliona ni bora ningoje watakavyoandika kuhusu mazungumzo yale, wakiwa peke yao bila mimi. Nimeona leo kuwa tayari mmoja wa wanachuo ameshaandika kwenye tovuti ya chuo chao.

Sishangai kusikia kauli kama ya mwanafunzi huyu, kwani ninapoalikwa popote kutoa mhadhara, ninalichukulia jukumu langu kwa umakini. Ni namna yangu ya kuwaheshimu wanaonialika na wale watakaohudhuria. Ni kudhihirisha jinsi ninavyoiheshimu taaluma na jinsi ninavyojiheshimu mwenyewe kama mwanataaluma.

Kwa jinsi ninavyowafahamu wanafunzi wa Marekani, kuna uwezekano mkubwa kuwa wengine wataandika pia, na nikiona taarifa zao, nitaziweka katika hii blogu yangu.

Monday, January 5, 2015

Mkutano na Wanachuo wa Gustavus Adolphus

Leo asubuhi nilikwenda Mount Olivet Conference & Retreat Center, eneo la Farmington, hapa Minnesota, kuongea na wanachuo wa chuo cha Gustavus Adolphus ambao wanaelekea Tanzania kimasomo. Kwa siku hizi mbili tatu kabla ya safari yao, wamekuwa katika maandalizi, nami niliitwa na profesa wao Barbara Zust, kuongea nao kuhusu masuala ya utamaduni ambayo yamo katika kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Nimeshaalikwa mara kadhaa miaka iliyopita, kuongea na wanachuo wa Gustavus Adolphus, katika maandalizi ya kwenda Tanzania, kama nilivyoelezea katika blogu hii.

Nilikuwa nimeamua kuwa leo, baada kutoa utangulizi mfupi, nitumie muda karibu wote katika kujibu masuali ya hao wanachuo, kwani nilishafahamishwa kuwa watakuwa wamekisoma kitabu changu. Ilidhihirika wazi, kutokana na masuali yao, kuwa walikuwa wamekisoma kwa makini. Wote tuliyafurahia mazungumzo yetu, ambayo yalidumu kuanzia saa nne hadi saa sita. Baada ya hapo, tulikula chakula cha mchana, ambapo niliendelea na maongezi na Profesa Zust na mshiriki wake Mchungaji Todd Mattson, na wanachuo ambao tulikaa meza moja.

Tulipokuwa tayari kwenda kula, na mara baada ya chakula, wanafunzi kadhaa waliniletea nakala zao za kitabu changu ili nisaini,shughuli ambayo ninaamini inamgusa kila mwandishi na yule anayesainiwa kitabu. Baada ya shughuli hii tuliagana, tukiwa tunapeana shukrani tele, nami nikaanza safari ya kurejea Northfield, ambapo ninaishi.

Katika picha ya mwanzo hapa juu, ninaonekana hapo mbele. Kule nyuma kabisa, upande wa kulia mwishoni, anaonekana Mchungaji Mattson, mwenye ndevu nyeupe, na mbele yake ni Profesa Zust. Pichani hapa kushoto, naonekana nikisaini kitabu cha mwanafunzi mojawapo.

Thursday, January 1, 2015

Kwa Kina na Prof. Joseph Mbele

Niliwahi kuhojiwa na Jeff Msangi, mwanzilishi na mmiliki wa blogu ya Bongo Celebrity. Yeye, pamoja na Freddy Macha, ambaye ni mwandishi, mwanamuziki, na mwanzilishi wa blogu ya Kitoto, ndio walionihamasisha kuanzisha blogu. Daima ninawashukuru hao ndugu wawili, ambao ni wafuatiliaji makini wa maandishi yangu.

Mahojiano yangu na Jeff Msangi yalifanyika mwaka 2008, lakini naona yanastahili kujadiliwa hata leo na siku zijazo. Wadau wengi walichangia maoni yao ambayo unaweza kuyasoma hapa.

Mahojiano haya yamechapishwa pia katika kitabu changu cha Changamoto: Insha za Jamii.
.
-------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------
KWA KINA NA PROF.JOSEPH MBELE
Mbali na kuwa na utajiri wa asili wa aina yake,Tanzania ni nchi ambayo inajivunia kuwa na wasomi maarufu ambao wametapakaa kote ulimwenguni wakifundisha katika mashule na vyuo mbalimbali au kuongoza vitengo nyeti katika idara za kimataifa na zenye uzito wa ki-dunia nzima.

Mmojawapo miongoni mwa wasomi hao ni Prof.Joseph Mbele(pichani),mtanzania anayefundisha katika Chuo cha St.Olaf kilichopo Northfield jimboni Minnesotta nchini Marekani.Miongoni mwa wasomi na wafuatiliaji wa mambo mbalimbali ya kitaaluma jina la Prof.Mbele sio geni hata kidogo.Prof.Mbele ni mtunzi wa kitabu maarufu sana kiitwacho Africans and Americans:Embracing The Cultural Differences.Kitabu hicho ndicho kinachotumika zaidi hivi leo mashuleni na katika taasisi mbalimbali(zikiwemo balozi mbalimbali) wanapokuwa wanawaandaa watu wao kuja kusoma, kutembea tu,kufanya kazi au tafiti mbalimbali barani Afrika.

Kutokana na kwamba kumekuwepo na mijadala mingi sana kuhusiana na masuala yote yahusuyo mila,tamaduni,desturi,maisha ya ughaibuni nk,BC tuliamua kumtafuta Prof.Mbele ambaye ni msomi anayetambulika kimataifa na mwenye mamlaka ya kutosha kuhusiana na maeneo yaliyotajwa hapo juu ili kupata maoni na mitizamo yake.Katika mahojiano haya,Prof.Mbele anafafanua mambo mengi sana kama vile’je kuna kitu kama mila,tamaduni na desturi za kitanzania?Kwanini watu wengi hivi leo hususani vijana wanazidi kubobea kwenye tamaduni za kimarekani?Kwanini aliandika kitabu hicho kilichotajwa hapo juu? Kama wanajamii tunakubaliana kwamba tumepoteza dira na muelekeo katika tamaduni,mila na desturi zetu,nini kifanyike?Kwa majibu ya maswali hayo na mengineyo mengi,fuatana nasi katika mahojiano yafuatayo;


BC: Kumekuwepo na mijadala mbalimbali kuhusiana na suala la mila,tamaduni na desturi za mtanzania.Kuna ambao wanasema hakuna kitu kama mila,utamaduni na desturi za kitanzania ingawa wanakubali kwamba inawezekana kukawa na mila,tamaduni na desturi za makabila fulani fulani. Nini maoni yako kuhusu dhana kama hizi? Unadhani kuna mila,tamaduni na desturi zinazoweza kuitwa “za kitanzania”?


PROF.MBELE: Pamoja na tofauti zote baina ya makabila,kuna pia mambo ya msingi ambayo yamo miongoni mwetu sote. Mifano ni kama kuheshimu wazee, kupenda kuwa na watoto, kushirikiana kwenye shughuli kama mazishi na sherehe. Mambo hayo yamo miongoni mwa Waafrika kwa ujumla. Kuna mengine ambayo tunaweza kusema ni ya kiTanzania. Kwa mfano, Mtanzania ana utamaduni wa kutotilia maanani ukabila katika mahusiano na Watanzania wengine. Anazingatia utaifa kwanza. Huu ni utamaduni wa Mtanzania. Lugha ni nguzo muhimu ya utamaduni, na Mtanzania anathibitisha kuwepo kwa huu utamaduni wa kiTanzania kwa kuongea kiSwahili anapokuwa na Watanzania wa makabila mengine. Kwa kiasi kikubwa, hayo ni matokeo ya juhudi ya Mwalimu Nyerere.


BC: Vijana wengi wa hivi leo wanapenda(pengine hata kuabudu) tamaduni za kimarekani.Hii sio kwa vijana wa kitanzania peke yao bali dunia nzima.Unadhani hii inatokana na nini? Nini faida au madhara ya mapokeo haya ya tamaduni za kigeni au kimarekani?


PROF.MBELE: Hao watu wanaoiga namna hiyo wana matatizo.Tatizo moja ni kuwa wanayoiga ni yale yenye mushkeli hata huko Marekani kwenyewe. Marekani, kama sehemu yoyote duniani, ina watu wanaokiuka maadili ya jamii. Vijana wetu wanaiga mambo hayo yenye walakini, iwe ni katika mitindo, lugha, na kadhalika.

Kwa mfano,badala ya kujifunza kiIngereza sanifu, ambacho kingewawezesha kusonga mbele kielimu na kimaisha, vijana wetu wanaiga kiingereza kibovu na cha matusi ambacho wanakisikia kutoka kwa baadhi ya wanamuziki wa kiMarekani.Vijana wetu wanaiga mitindo ambayo hata huku Marekani inawabughudhi wengi. Kuna miji hapa Marekani imeshaanza kupiga marufuku aina ya mavazi wanayoiga hao vijana wetu.

Filamu nyingi za Hollywood zinawapotosha watu.Wanadhani mambo ya Hollywood ndio hali halisi ya Marekani. Hollywood kwa ujumla inapotosha ukweli wa Marekani, kama vile inavyopotosha ukweli kuhusu Arabuni, Afrika, Asia, na kwingineko.Hollywood au inatia chumvi au inadhalilisha. Hollywood inatafuta biashara, sio kuelimisha watu, na hata kama kinachouzwa ni pofotu, wao wanauza tu. Ukweli ni kuwa Wamarekani kwa
ujumla ni watu wenye heshima zao, kwa mujibu wa utamaduni wao, kama ilivyo katika nchi nyingine yoyote, na wanavaa na kutumia lugha ya kawaida na ya heshima kama vile wanavyofanya Watanzania walio wengi.


BC: Utamaduni wa “kimarekani” ambao kila kukicha unazidi kuenea dunia nzima sio jambo linalotokea kama ajali.Ni mipango madhubuti ya kiserikali ya Marekani katika kuhakikisha inaendelea kuwa “super power’ wa dunia. Je unakubaliana na dhana hii? Kama ndio,unadhani serikali za nchi kama yetu ya Tanzania ina wajibu gani katika sio tu kujaribu kukabiliana na hali hii bali pia kuhakikisha mila,tamaduni na desturi za kitanzania zinalindwa,kutunzwa na kuheshimiwa?


PROF.MBELE: Kinachoenea duniani kutoka Marekani ni utamaduni wa kibepari, ambao unageuza kila kitu kuwa bidhaa, kama alivyotueleza Karl Marx kwenye kitabu chake cha Communist Manifesto. Mabepari wanasambaza mitindo na vishawishi, ili kuwafanya watu wapende kununua bidhaa au huduma mbali mbali hata kama hazina maana katika maisha. Wao wanatafuta pesa. Wamarekani wa kawaida hawana uwezo wa kufanya hayo yote, wala hawahusiki.

Serikali ya Marekani ni mshiriki na pia wakala wa hao mabepari, na inachofanya ni kuweka mazingira ya kuuwezesha ubepari kustawi duniani kote.Serikali ya Marekani inazishinikiza nchi kama yetu ziweke mazingira muafaka ya kuuwezesha ubepari kufaidika, pamoja na kwamba wananchi walio wengi wanaathirika. Serikali ya nchi kama Tanzania ingepaswa kuwa mstari wa mbele kuwaelimisha wananchi kuhusu masuala hayo, kama alivyokuwa anafanya Mwalimu Nyerere.

Lakini, leo tumekwama;viongozi wenyewe sidhani kama wana upeo unaohitajika,wala dhamira inayohitajika.Hakuna juhudi inayofanywa na serikali kuhimiza elimu kuhusu ubepari, badala yake kinachofanyika ni kuupigia debe ubepari na utamaduni wake. Hatutafika mbali, bali tutaanza kuona matatizo makubwa katika jamii yetu. Kujenga utamaduni wa kujifahamu,kujiamini, kujithamini, kujitegemea, na kujiheshimu kutatusaidia kuepuka kuwa jalala la kila kinachotoka kwa hao mabepari.
Cover la mbele la kitabu cha Prof.Mbele.


BC: Katika kitabu chako cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences( Tunashauri kila mtu akisome kitabu hiki) umeelezea kwa umakini kabisa tofauti za kimila,tamaduni na desturi kati ya waafrika na wamarekani.Nini hasa kiini cha wewe kuamua kuandika kitabu hiki? Kuna uzoefu wako binafsi wowote ule nyuma ya kitabu hiki?


PROF.MBELE: Katika kuishi na Wamarekani kwa miaka mingi, nilitambua umuhimu wa kitabu cha aina hii, ambacho kingetoa mwanga kuhusu utamaduni wao na namna unavyotofautiana na utamaduni wetu Waafrika. Lengo lilikuwa kuzuia au kupunguza mikwaruzano na kutoelewana baina ya Waafrika na Wamarekani, ambayo haikwepeki endapo hawachukui hatua za kuzifahamu tofauti zao. Mikwaruzano hii haiko baina ya Wamarekani na Waafrika tu, bali inaweza kutokea popote wanapokutana watu wa tamaduni tofauti, iwe ni katika ndoa, shuleni, kwenye biashara, diplomasia, utalii, na kadhalika.

Msukumo mkubwa wa kuandika hiki kitabu ulitoka kwa Wamarekani waliokuwa wanaenda Afrika, iwe ni kwa masomo, utafiti, kazi za kujitolea, au kwa safari tu,ambao
walikuwa wananiulizia masuali kuhusu maisha na utamaduni wa Waafrika.Lengo lao lilikuwa ni kujiandaa ili wakiwa Afrika wasipate taabu, na ili wasifanye makosa katika masuala ya mila na desturi. Pamoja na kuwaeleza ana kwa ana au kwa njia ya mawasiliano mengine, niliona niandike hiki kitabu.Nilijua kuwa Wamarekani kwa ujumla wanapenda kusoma vitabu, na hii ikawa ni njia bora ya kuwasiliana nao.

Kwa upande mwingine, nilikuwa nawawazia pia Waafrika.Wengi wanaoishi Marekani au wanashughulika na Wamarekani sehemu mbali mbali kule Afrika. Hao nao niliona watahijaji kujifunza mambo ya Wamarekani, ili iwe rahisi kuelewana nao.

Vinginevyo,nilijua kuwa watapata ugumu fulani, na hata migongano.Tatizo ni kuwa
Watanzania hawathamini vitabu kama Wamarekani wanavyothamini.Hilo limethibitishwa tena na tena.Kwa hivi, sina hakika kama lengo langu litafanikiwa kwa upande wa Watanzania.
Prof.Mbele(mwisho wa meza upande wa kulia) akiwaandaa wanafunzi wa Colorado College kwa ajili ya safari ya kimasomo Tanzania.


BC: Una mpango wowote wa kukitafsiri kitabu hiki katika lugha ya Kiswahili ili watu wengi zaidi waweze kukisoma? Kwa anayetaka kukisoma kitabu hiki hivi sasa,kinapatikana wapi au anaweza kukipata vipi?


PROF.MBELE: Itakuwa vizuri kukitafsiri kitabu hiki kwa kiSwahili na hata lugha zingine, kama vile kiSomali, kiArabu, na kiFaransa. Hapa Marekani, kuna maelfu ya waAfrika wanaotumia lugha zote hizi, na ninafahamu kuwa wanahitaji kuelewa mambo niliyoandka. Kitabu hiki kinapatikana kwenye tovuti hii http://www.lulu.com/content/105001. Ninataka kitabu hiki kipatikane Tanzania kiurahisi, kiwasaidie Watanzania wanaoshughulika na Wamarekani kwa namna yoyote. Kwa sasa, kinapatikana Dar es Salaam,simu namba 717 413 073.


BC: Ubaguzi wa rangi ni jambo ambalo hukatisha watu wengi tamaa. Kwa maoni yako nini hasa chanzo cha ubaguzi wa rangi duniani? Je wewe katika kazi zako za kila siku za ufundishaji nchini Marekani unakumbana na matatizo unayohisi ni matokeo ya moja kwa moja ya ubaguzi wa rangi? Unakabiliana nayo vipi na unatoa ushauri gani kwa watu wengine wanaokabiliwa na tatizo kama hilo?Je unadhani ubaguzi wa rangi’ ni sehemu ya utamaduni au ni tabia tu za watu?


PROF.MBELE: Sio vizuri kukata tamaa, na huenda hata wale wanaolalamikia ubaguzi nao ni wabaguzi. Kuna aina nyingi za ubaguzi, kama vile ubaguzi wa dini, jinsia,taifa, lugha, kabila, rangi, umri, uwezo wa kiuchumi, na kadhalika. Hata mahali penye watu wa rangi moja tu, ubaguzi unaweza kuwepo na kuleta matatizo makubwa, kama yale ya Rwanda mwaka 1994. Ubaguzi ni ubaguzi. Pamoja na kwamba ni muhimu kutambua ubaya uliopo katika jamii za wengine,ni muhimu pia kuona ubaya uliomo katika jamii zetu au katika nafsi zetu.

Jamii ya Tanzania, kwa mfano, ina maovu mengi. Wakati mamilioni ya watu wanaishi kwa dhiki kubwa, kuna Watanzania ambao wanafuja mali ya nchi kwa starehe na mambo yao binafsi. Na wanaiba hata hela za umma na kuzifuja. Kuna maelfu ya watoto yatima katika nchi yetu ambao wana dhiki kubwa, wakati mamilioni ya shilingi yanafujwa kila siku.

Nikirudi kwenye suala la ubaguzi wa rangi, napenda kusema kuwa,badala ya mtu kukaa na imani kuwa hutaendelea sababu ya ubaguzi wa rangi, ni bora kutambua kuwa ukiwa na elimu, maarifa na ujuzi, utahitajika, na hakuna atakayeweza kukupuuzia eti kwa sababu ya rangi yako. Dunia ya leo ni dunia ya aina yake, inategemea elimu, maarifa, na ujuzi. Makampuni na mashirika yanashindana, na yanalazimika kutafuta watu wenye ujuzi, elimu, na maarifa. Kama wewe ndio bingwa, utatafutwa wewe.Yule tajiri maarufu duniani, Bill Gates, amewekeza India, kwa sababu Wahindi wanawika kwenye fani ya kompyuta. Anawajali Wahindi kwa hilo, na wala rangi yao sio kipingamizi. Watanzania tutambue hilo. Tujifunze kutoka kwa Wahindi; tujibidishe katika elimu.

Mimi nimekuwa na msimamo huo tangu zamani. Nimelenga katika kujielimisha muda wote. Mfano mmoja wa matokeo yake ni kuwa kutokana na ujuzi wangu katika fani yangu, nilifuatwa na chuo cha St. Olaf cha Marekani nije kuwafundishia masomo fulani. Sikuomba kazi hapa. Shughuli zimeenda vizuri kwa miaka yote niliyofundisha hapa, wala sijaona usumbufu wala ubaguzi wowote. Kama ni usumbufu au kukosewa haki sehemu ya kazi, hayo yalinisibu kule Tanzania. Nimejibidisha sana pia katika utafiti wa tamaduni mbali mbali, na matokeo yake ni kuwa ninatafutwa na hao Wamarekani wanapohitaji ushauri kwenye masuala hayo.

Jambo jingine ambalo naona ni muhimu kusema ni kuwa kama kweli kuna kipingamizi kama hiki cha ubaguzi, basi tukumbuke kuwa sio lazima tuwe watu wa kuajiriwa na wengine. Kama tunao ujuzi na maarifa, tutafakari namna ya kujiajiri. Hilo wazo limenijia miaka hii ya karibuni, na niko katika kulifanyia kazi. Ujuzi na maarifa ndio msingi na ndio silaha thabiti katika mapambano ya ulimwengu wa leo.


BC: Nadhani tunakubaliana kwamba suala la udumishaji wa mila,tamaduni na desturi lina misingi yake katika malezi. Mtoto umleavyo ndivyo akuavyo.Mporomoko wa maadili uliozikumba jamii zetu hivi leo inasemekana unatokana na malezi mabovu.Unasemaje kuhusu suala hili na unatoa ushauri gani kwa wazazi kuhusiana na suala zima la malezi?


PROF.MBELE: Ni kweli kuna mporomoko mkubwa wa maadili. Wazazi na watu wazima kwa ujumla wana wajibu wa kuwa mfano wa maadili bora. Lakini hali iliyopo katika nchi yetu, kwa mfano, hairidhishi. Mwalimu Nyerere alijitahidi sana kuongelea maadili, kuanzia kufanya kazi kwa bidii, kuwatetea wanyonge, kufuata haki, kujielimisha, kuheshimiana.

Leo hii watu wanatafuta pesa kwa namna yoyote, na maadili yamewekwa kando. Kiu ya pesa imeleta madhara ya kila aina, kama walivyoelezea akina Karl Marx. Imevuruga maadili ya dini, serikali, elimu, na kadhalika. Utapeli umeingia sehemu nyingi za maisha ya jamii.Naamini kuwa tunaweza kujirekebisha. Kwa upande wetu Tanzania, kitu kimoja tunachoweza kufanya ni kuanza kujielimisha kuhusu yale aliyokuwa anatufundisha Mwalimu Nyerere, kwani yanaendana na mazingira ya kihistoria na utamaduni wetu.

Elimu ni jambo la msingi. Kwa mfano, tungejielimisha kuhusu masuala ya afya, tungepunguza utumiaji wa pombe. Lakini Tanzania tunaona sifa kunywa pombe sana, badala ya kutambua kuwa tunahujumu akili, afya, na maisha yetu. Watoto wanakua katika mazingira ambayo hayawafundishi maadili mema. Hata kama shuleni watafundishwa, huko mitaani wanaona na kusikia mengine. Kwa mila za mababu na mabibi, watu wazima wanawajibika kuwaongoza na kuwanyoosha wadogo, lakini kwetu mambo ni kinyume. Watu wazima wanawakwaza na kuwapotosha wadogo.

Niliwahi kuhudhuria tamasha la vitabu pale Dar es Salaam. Watoto walikuwa hapo lakini watu wazima wachache sana walioonekana hapo. Watoto waliimba nyimbo, wakiwaomba wazazi wawanunulie vitabu na wawe na utaratibu wa kusoma majumbani. Lakini wazazi wenyewe hawakuwepo hapo kwenye tamasha. Ilikuwa hali ya kusikitisha. Jioni, nilipokuwa napita mitaa mbali mbali, nikirudi nyumbani, nilikuwa nawaona watu wazima kwenye baa, mtaa hadi mtaa, kama kawaida. Badala ya kujumuika na watoto kwenye tamasha la vitabu, wao walikuwa kwenye baa. Na hata viongozi hawakuwepo kwenye tamasha: wajumbe wa nyumba kumi, makatibu kata, makatibu tarafa, wabunge, na kadhalika. Hawakuwepo.Huwezi kuamini kuwa hii ndio nchi ya Mwalimu Nyerere.

Mimi kama mwalimu lazima niwaambie Watanzania kuwa hapo Wamarekani wametuzidi: wanahudhuria sana matamasha ya vitabu, na kwenye maduka ya vitabu utawakuta wakinunua vitabu. Kama nilivyosema, dunia ya leo inatawaliwa na elimu, maarifa na ujuzi, na malezi bora ya watoto lazima yazingatie hilo.
Prof.Mbele(kulia) akiongea na walimu na watoto jijini Dar-es-salaam.


BC: Hivi leo kila mtu anaongelea kuporomoka kwa maadili ya kijamii hususani miongoni mwa vijana. Kwa uzoefu na utaalamu wako, ni mila,tamaduni na desturi zipi ambazo hivi leo tumeachana nazo ambazo sio tu hatukutakiwa kamwe kuachana nazo bali tulitakiwa kuzienzi kwa udi na uvumba? Nini kinaweza fanyika hivi sasa ili kurejesha suala zima la maadilli.


PROF.MBELE: Kama nilivyogusia, ingebidi tuanze kufuata nyayo za Mwalimu Nyerere, ambaye alithamini utu. Leo hii mtu anayeheshimiwa ni yule mwenye pesa. Hili ni tatizo kubwa,na dalili ya kuporomoka maadili. Jamii kwa ujumla imeingia katika hali hiyo, na vijana wanalelewa namna hiyo. Ndoto zao ni za kupata pesa nyingi, kwa njia yoyote. Lakini watu wazima ndio wameanzisha mkondo huu, na hao vijana wanafuata nyayo.

Alichojaribu kujenga Mwalimu Nyerere katika jamii yetu ni ule moyo wa kila mtu kumjali mwingine na kuangalia maslahi ya jamii, si maslahi binafsi. Na Mwalimu Nyerere alikuwa anajenga fikra zake kwenye msingi wa mila na desturi za mababu na mabibi zetu. Leo tumeachana na mwelekeo huo. Na hili ni tatizo kubwa. Naamini kuwa tukijizatiti upya na kuanza kuangalia yale aliyokuwa anafundisha Mwalimu Nyerere, tuyaingize mashuleni, sehemu za kazi, mitaani, na kila mahali, tutaweza kuanzisha mkondo ule alioutaka Mwalimu Nyerere.


BC: Dunia yetu hivi leo inakabiliwa na suala gumu la vita dhidi ya ugaidi. Unaweza kuhusisha vipi ugaidi na mila,tamaduni na desturi za binadamu au mataifa mbalimbali?


PROF.MBELE: Kitu kigumu ni kuelewa dhana ya ugaidi na kukubaliana kama wote tunaelewa hivyo hivyo. Kwa bahati mbaya, dhana hii inatafsiriwa namna mbali mbali na watu au jamii mbali mbali. Matokeo yake ni kuwa wako ambao wanasema wanapiga vita ugaidi hali kwa mtazamo wangu wao wenyewe ni magaidi. Mara nyingi nashangaa, na sijui kama kinachopigwa vita ni ugaidi au ni kitu kingine. Halafu serikali nyingi sasa zimepata fursa ya kufanya dhuluma kwa kisingizio cha kupambana na ugaidi. Kwa maneno mengine hii inayoitwa vita dhidi ya ugaidi ina mikanganyiko ya kila aina.


BC: Mwisho una ujumbe gani kwa vijana,wanajamii,viongozi wa kiserikali,dini nk kuhusu mila,tamaduni na desturi?


PROF.MBELE: Ujumbe wangu ni kuwa Watanzania tujifunze na kuzingatia aliyotufundisha Mwalimu Nyerere: kujenga jamii yenye haki, yenye kuzingatia usawa wa binadamu, isiyo na unyonyaji na ukandamizaji, yenye kushirikiana na kuhemishimiana. Huu ndio utamaduni unaotufaa. Tuzingatie aliyotufundisha Mwalimu Nyerere kuhusu elimu. Alisema elimu haina mwisho, na aliongelea elimu kwa mapana na undani, kuanzia kisomo chenye manufaa, elimu ya watu wazima, na elimu mashuleni hadi vyuo vikuu.

Elimu ndio msingi wa mafanikio katika ulimwengu huu wa ushindani mkubwa. Msisimko wa elimu aliouwazia Mwalimu Nyerere umedidimia. Asilimia ya watu wasiojua kusoma na kuandika inazidi kuongezeka. Mashuleni watu wanatafuta vyeti, badala ya elimu. Watu wanatumia muda mwingi vijiweni, badala ya kujitafutia maarifa na elimu.

Tulipopata uhuru, Nyerere alieneza ujumbe maarufu: Uhuru na Kazi! Leo utamaduni wa kufanya kazi kwa bidii umetetereka. Hata hao Wamarekani tunaowasema, wengi wako katika nchi yetu, kuanzia vijijini hadi mijini, wakifanya kazi za kujitolea, wakati sisi wenyewe tuko vijiweni tunapiga soga, tuko kwenye sherehe au tuko kwenye maandalizi ya sherehe.Hata hivyo, bado fursa tunayo ya kujirudi.


BC: Shukrani sana Prof.Mbele kwa mahojiano haya.Tunakutakia kila la kheri
katika kazi zako.

PROF.MBELE: Nashukuru sana kwa fursa hii ya kujieleza kwa wadau wa ukumbi huu. Nawe nakutakia kila la heri.
Prof.Mbele pia ni Mwanzilishi na Mkurugenzi wa shirika lijulikanalo kama AFRICONEXION. Unaweza kutembelea tovuti ya shirika hilo kwa kubonyeza hapa.
Je unakubaliana au unapingana na chochote alichokisema Prof Mbele?Usisite kuweka maoni yako na pia kumpelekea link ndugu,jamaa au rafiki yako ili naye apate soma ulichokisoma.Asante.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...