Friday, September 30, 2016

M-Kenya Kaniandikia Kuhusu Kitabu Changu

Nimefurahi sana, tangu usiku wa kuamkia leo, kupata maoni ya msomaji wa kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Msomaji huyu ni mama m-Kenya ambaye anaishi hapa Minnesota, Marekani. Aliniandikia katika Facebook ujumbe huu:

I did not tell you how precious your book is. My friend and I were reading it to our kids during a sleep over and it is amazing how your culture is similar to ours. You did well and it was very easy to understand and flow with. You are gifted Mwalimu. God bless you more. Thank you again for the great gift.

Huyu mama tulikutana tarehe 30 Aprili, mwaka huu, kwenye tamasha mjini Rochester. Alikuja kwenye meza yangu, tukasalimiana na kuongea. Alivutiwa na kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, akaulizia namna ya kukipata siku nyingine, kwa kuwa hakuja na hela. Hapo hapo nilimpa nakala ya bure. Alishangaa, akashukuru sana.

Nimefurahi kuwa ameniandikia maoni yake kuhusu kitabu hicho. Ninamfananisha na wa-Tanzania kadhaa ambao, baada ya kuniomba, nimewapa nakala za bure za kitabu hiki. Nilitegemea na ningefurahi iwapo wangeniletea neno kuhusu kitabu, lakini sikuwasikia tena. Nawajibika kusema kuwa sioni kama huu ni uungwana.

Ninapowazia jambo hilo, ninapata hisia kuwa huenda hao watu hawakusoma kitabu hicho. Wazo hilo linanifikia kwa kuzingatia ukweli kwamba utamaduni wa kusoma vitabu hauonekani katika jamii ya wa-Tanzania. Hili ni jambo ambalo limelalamikiwa na linaendelea kulalamikiwa na wadau wa vitabu kama vile waandishi na wachapishaji.

Kwa upande wa wa-Kenya, nimejionea kuwa wanao utamaduni wa kupenda vitabu, kama nilivyowahi kuandika katika blogu hii. Hali hiyo ninaishuhudia sio tu huku nje ya Afrika, bali pia  nchini mwao. Ushahidi moja wa wazi ni kuwa makala kuhusu vitabu si jambo geni katika magazeti ya Kenya. Kwa upade wa Tanznia, sijui ni lini niliwahi kuona gazeti la aina hiyo.

Hainifurahishi kusema mambo hayo kuhusu wa-Tanzania, lakini ninachosema ni ukweli nilivyouona. Ukweli unapaswa kusemwa, hata kama unauma. Hainishangazi kwamba hata katika soko la ajira, iwe ni Afrika Mashariki au kwingineko, wanajiamini kuliko wa-Tanzania.

Thursday, September 29, 2016

Darasa ni Popote

Tangu nilipokuwa mdogo, nilikuwa nataka kuwa mwalimu. Mungu si Athmani, ndoto yangu ilitimia. Ninafurahia kazi yangu na ninaifanya kwa dhati na kwa uadilifu. Ninaona raha kuwa na wanafunzi katika kutafakari masuala.

Zaidi ya kufundisha darasani katika jengo, ninapenda kushiriki matamasha. Matamasha hayo ni kama shule, fursa ya kuongea na watu juu ya shughuli zangu, kama vile utafiti na uandishi.

Uandishi ninauchukulia kama aina ya ufundishaji. Ni ufundishaji usio na mipaka, kwani maandishi yanakwenda popote, iwe ni vitabu halisi au vitabu pepe, iwe ni makala katika majarida au mtandaoni,  zote hizo ni njia za kuniwezesha kufundisha bila mipaka.

Ninafurahi kuwa nimejiingiza katika uwanja wa blogu. Blogu ni kumbi zinazonipa fursa ya kueneza mawazo yangu, ingawa kwa ufupi. Mara kwa mara ninaongelea vitabu na kutoa dondoo za kiuchambuzi zinazoweza kumpa mtu fununu ya mambo muhimu yaliyomo katika vitabu hivyo. Blogu zangu zinatoa fursa kwa watu kuchangia mawazo na mitazamo. Ninaendesha blogu kwa mtindo huo kwa kuwa ninaheshimu uhuru wa fikra ambao ndiyo injini inayoendesha elimu.

Ni wazi kwamba tafsiri yangu ya shule au darasa ni tofauti na ilivyozoeleka. Tekinolojia za mawasiliano zimeleta mazingira na fursa mpya. Fikra zetu kuhusu darasa au shule sherti zibadilike. Katika mazingira ya leo, darasa au shule ni dhana isiyofungwa au kufungamana na kigezo cha jengo, madawati, au mwalimu na wanafunzi kuonana ana kwa ana.

Leo kwa kutumia tekinolojia za mawasiliano, mwalimu anaweza kuendesha darasa kwa njia ya Skype, kama nilivyowahi kufanya kwa wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Montana, au anaweza kuendesha darasa mtandaoni na wanafunzi wakiwa wametapakaa sehemu mbali mbali za dunia. Ninategemea kuwa wa-Tanzania, wakiwemo wanaotaka nirudi Tanzania nikafundishe, watasoma na kutafakari hayo niliyoandika hapa.

Thursday, September 22, 2016

David Robinson Ahutubia Chuo Kikuu cha Minnesota

Leo mchana nilikwenda Chuo Kikuu cha Minnesota, Minneapolis, kumsikiliza David Robinson, m-Marekani Mweusi anayeishi Mbeya, Tanzania, ambako ni mkulima wa kahawa. Huyu ni mtoto wa mwisho wa mwanariadha maarufu sana wa Marekani, Jackie Robinson, ambaye alikuwa pia mpinzani shujaa wa ubaguzi na mtetezi wa haki za wa-Marekani Weusi.

David Robinson aliamua kwenda kuishi Tanzania, kwenye kijiji cha Bara wilaya ya Mbozi. Alijitambulisha kwa wanakijiji akajieleza kuwa ni mtoto wa Afrika aliyepotezewa ughaibuni kwa karne kadhaa, katika utumwa, na sasa ameamua kurudi nyumbani. Wanakijiji walimpa shamba akaanza kulima kahawa. Aliungana na wanakijiji wengine, wakaanzisha chama cha ushirika kiitwacho Sweet Unity Farms

Aliongelea shughuli za chama chao cha ushirika, wanavyoshughulikia matatizo na changamoto na kujifunza. Alielezea mahusiano yao na wateja wa nchi mbali mbali, ikiwemo Marekani. Ingawa wao wako kijijini, wanashiriki katika uchumi wa ulimwengu, na ndio hali halisi ya utandawazi. Daima wanatafuta namna ya kujiweka kibiashara, pamoja na uwezo wao mdogo, katika ulimwengu ambao umetawaliwa na makampuni makubwa ya kimataifa.

Pichani hapa kushoto anaonekana David Robinson, Limi Simbakalia, mwanafunzi m-Tanzania wa Chuo cha St. Olaf ambapo ninafundisha, na mimi.

Kuna taarifa nyingi mtandaoni juu ya David Robinson na Sweet Unity Farms, yakiwemo mahojiano naye. Taarifa moja nzuri kabisa ni hii hapa. Aidha, kuna taarifa nyingi juu ya baba yake, mwanariadha Jackie Robinson. Mfano mmoja ni filamu hii hapa chini, inayoonyesha magumu aliyopitia na alivyopambana kishujaa katika mazingira ambayo yalikuwa mabaya sana kwa wa-Marekani Weusi.

Tuesday, September 20, 2016

"The Dilemma of a Ghost:" Tamthilia ya Ama Ata Aidoo

The Dilemma of a Ghost ni tamthilia ya kwanza ya Ama Ata Aidoo wa Ghana. Aliitunga alipokuwa mwanafunzi katika chuo kikuu cha Ghana, Legon, ikaonyeshwa mara ya kwanza mwaka 1964, na kuchapishwa mwaka 1965. Ama Ata Aidoo aliendelea kuandika na bado anaandika, na kazi zake ni pamoja na tamthilia nyingine iitwayo Anowa, ambayo ilichapishwa mwaka 1970, hadithi fupi, na riwaya kadhaa.

The Dilemma of a Ghost inaongelea juu ya kijana wa Ghana aitwaye Ato aliyekwenda masomoni Marekani na huko akakutana na Eulalie, binti Mwamerika Mweusi. Huyu ni kati ya wale wa-Marekani Weusi wanaoiwazia Afrika kwa hamu kama mtu aliyeko ugenini anavyowazia nyumbani kwake.

Ato na Eulalie wanaoana na kurejea Ghana, ambako wanakumbana na mambo magumu. Kwanza ndugu zake Ato wanashtuka kusikia kuwa Ato ameoa bila kuwashirikisha. Halafu binti mwenyewe hana kabila wanalolitambua, na hata jina lake wanashindwa kulitamka, na kibaya zaidi, kwa mtazamo wao, ni kuwa binti huyo ni kizalia cha watumwa. Wanaukoo wanaona Ato amewasaliti.

Halafu, Eulalie naye anashindwa kuelewa na kufuata mila na desturi za hao ndugu. Wao wanamwona kama kizuka, kwa tabia zake, ikiwemo kukataa kunywesha dawa za kienyeji za kumwezesha kupata mimba. Mama mkwe wake, Esi Kom, anapofanya ukarimu wa kumletea konokono, ambao ni chakula cha heshima, Eulalie anashtuka, na haamini macho yake, na hatimaye anawatupilia mbali hao konokono. Jambo jingine linalowashangaza ndugu hao ni jinsi Eulalie anavyovuta sigara. Basi, inakuwa shida juu ya shida, na hatimaye binti anajikuta katika upweke na msongo wa mawazo.

Lakini, hatimaye, mama yake Ato anaridhia kumpokea huyu mkwe wake na anachukua hatua za kuwashawishi ndugu wote wampokee, kwa hoja kwamba mgeni hastahili kulaumiwa, bali mwenye lawama ni mwenyeji, yaani Ato. Ato anajikuta akiwa mpweke, aliyesongwa na mawazo, karibu kuchanganyikiwa. Ndivyo tamthilia inavyokwisha.

The Dilemma of a Ghost imejengeka katika mfumo wa hadithi za jadi ambazo huitwa "dilemma tales" ambao ni muundo unaowaacha wasikilizaji wakiwa na masuali yasiyojibika kirahisi. Katika tamthilia hii, suali moja muhimu ni nani wa kulaumiwa kwa matatizo yanayoibuka. Tamthilia hii inatumia pia aina nyingine za fasihi simulizi, kama vile nyimbo na methali. Vile vile kuna imani za jadi, kama vile juu ya mizimu na matambiko.

Ama Ata Aidoo ni mmoja wa waandishi wa ki-Afrika ambao ni hodari wa kutumia miundo na dhamira za masimulizi ya jadi. Hilo suala la kijana kujifanyia mwenyewe uamuzi wa kuoa au kuolewa bila kuwahusisha wazazi ni dhamira maarufu katika fasihi simulizi za Afrika, na matokeo ya kiburi hiki huwa si mema. Katika tamthilia ya Anowa, Ama Ata Aidoo ameiweka pia dhamira hiyo. Msichana Anowa anaamua kuolewa na kijana aliyemkuta bila wazazi kuhusika.

Tangu mwanzo, nilivutiwa na mtindo huu katika uandishi wa Ama Ata Aidoo, ambaye miaka ile alikuwa anajulikana kwa jina la Christina Ama Ata Aidoo. Ninakumbuka vizuri, kwa mfano, hadithi yake moja ya mwanzo kabisa iitwayo "In the Cutting of a Drink" ambayo niliisoma kwa mara ya kwanza miaka ya sitini na kitu, nilipokuwa mwanafunzi katika shule ya sekondari.

Nilivutiwa sana na hadithi hiyo kwa mtiririko wake sawa na wa mtambaji hadithi. Miaka ya baadaye, nilipojifunza somo la fasihi simulizi, nilianza kuelewa vizuri jinsi waandishi kama Ama Ata Aidoo wanavyotumia jadi hiyo.

Jambo muhimu sana jingine kuhusu Ama Ata Aidoo ni kuwa ni mwandishi mwenye kuchambua masuala ya jamii. Alivyokuwa anatunga The Dilemma of a Ghost, masuala kama ya mshikamano na mahusiano ya watu weusi ulimwenguni yaani "Pan-Africanism," yalikuwa yakivuma na kuwashughulisha viongozi maarufu kama George Padmore, W.B. Dubois, Kwame Nkrumah, Ahmed Sekou Toure, Jomo Kenyatta, na Julius Nyerere. Miaka iliyofuatia, Ama Ata Aidoo amekuwa akienda na wakati kama mwanaharakati katika masuala ya ukoloni mambo leo, haki za wanawake, na hata ujamaa. Sawa na ilivyokuwa kwa Mwalimu Julius Nyerere, Ama Ata Aidoo ni muumini wa fikra za kijamaa.

Saturday, September 17, 2016

Jionee Ukakamavu wa UVCCM

CCM ina kila sababu ya kujivunia vijana wake, yaani UVCCM. Sio tu ni vijana wanaozingatia wajibu wao wa kutetea na kutekeleza ajenda za serikali ya CCM, kama wanavyotamka katika tovuti yao, bali ni wakakamavu, ambao wako tayari kwa lolote.

Hapa naleta picha kadhaa kuthibitisha jambo hilo, nikizingatia usemi wa ki-Ingereza kwamba "a picture is worth a thousand words," yaani picha ina thamani sawa na maneno elfu. Jionee mwenyewe uwajibikaji na utendaji wa hao vijana.


Kwenye masuala ya itikadi, vijana hao wako mstari wa mbele pia. Angalia hilo bango walilobeba katika maandamano yao huko Visiwani.


















Kama hizi picha hazitoshi kukushawishi, basi angalia video hii hapa chini. Kwa kweli, CCM ina kila sababu ya kujivunia vijana wake.

Thursday, September 15, 2016

Ujumbe kwa Ndugu na Marafiki

Napenda kuwajulisha ndugu na marafiki kuwa leo tumemaliza wiki ya kwanza ya muhula mpya wa masomo hapa chuoni St. Olaf. Nimeanza vizuri, kama nilivyogusia katika blogu hii, kwa ari kubwa. Wanafunzi wanaonekana wenye ari ya kujifunza. Sitawaangusha.

Tarehe 17 mwezi uliopita ilikuwa ni kumbukumbu ya kuzaliwa kwangu. Nilitimiza miaka 65 ya maisha yangu. Ninavyoingia mwaka wa 66, ninamshukuru Mungu kwa kuniweka hai na mwenye uwezo wa kutekeleza majukumu yangu kama nilivyozoea.

Uhai na afya ni baraka kutoka kwa Mungu. Nitaendelea kutumia fursa hii, ambayo ni dhamana, kwa kufanya kazi zangu za kufundisha kwa juhudi yote na uadilifu, kusoma kwa bidii, na kuandika ili kuuneemesha ulimwengu kwa elimu.

Nawaombeni ndugu na marafiki mniombee ili nizingatie mwelekeo huo, nami nawaombea baraka na mafanikio.

Tuesday, September 13, 2016

Utangazaji wa Vitabu

Mara kwa mara, katika blogu hii, ninaandika kuhusu vitabu. Ninaongelea masuala kama uandishi wa vitabu, uchapishaji, na uuzaji. Mara kwa mara ninaviongelea vitabu kwa namna ya kuvitambulisha kwa wasomaji wa blogu hii, na pia kujiwekea kumbukumbu. Ninafurahi ninapopata taarifa kutoka kwa wasomaji wa blogu hii kuwa wamefuatilia taarifa zangu na kuvisoma vitabu nilivyoviongelea.

Ujumbe wa leo ninauelekeza kwa waandishi wa vitabu. Kama ilivyo desturi yangu, maelezo yangu yanatokana na uzoefu wangu kama mwandishi. Ujumbe wa leo ni mwendelezo wa yale ambayo nimewahi kuandika katika blogu hii.

Katika kutafiti suala hili la utangazaji wa vitabu, nimejifunza kuwa, kwa mwandishi, kuandika na kuchapisha kitabu si mwisho wa safari. Nimejifunza kutoka kwa waandishi na wachapishaji kwamba kwa namna moja au nyingine, mwandishi analo jukumu la kukitangaza kitabu chake.

Inaweza kutokea kwamba mchapishaji ana uwezo mkubwa wa kutangaza kitabu. Ana bajeti kubwa au mfumo wa kusambazia matangazo. Lakini, wachapishaji wengi hawana uwezo huo, au uwezo wao ni hafifu, na hivyo kumlazimu mwandishi abebe jukumu la kutangaza kitabu chake.

Hata kama mchapishaji ana uwezo mkubwa, mwandishi anayo pia nafasi ya kuchangia katika kukitangaza kitabu. Kwa hapa Marekani, jadi iliyojengeka ni kwa mwandishi kwenda sehemu mbali mbali kukitambulisha kitabu chake. Sehemu hizo zinaweza kuwa vyuo, maktaba, au maduka ya vitabu.

Ziara hizo, ambazo kwa ki-Ingereza huitwa "book tours," ni muhimu sana. Ratiba ya ziara hutangazwa kwenye vyombo vya habari mapema. Sehemu ambapo mwandishi ametegemewa kuja kuzungumzia kitabu, kama vile maktaba au duka la vitabu, panakuwa na matangazo pia. Wateja wanaofika hapo wanayaona matangazo hayo.

Kwa kuwa usomaji wa vitabu umejengeka katika utamaduni wa Marekani, ziara ya mwandishi huwavutia watu. Wakati mwandishi anapokuja, zinakuwepo nakala za kutosha za kitabu chake, ili watu wanaohudhuria waweze kununua nakala na kusainiwa na mwandishi.

Watu hapa Marekani wanapenda kusainiwa vitabu, kama nilivyowahi kuandika katika blogu hii. Mimi mwenyewe nimealikwa sehemu mbali mbali hapa Marekani kwenda kuongelea vitabu vyangu, hasa Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Njia nyingine muhimu kwa mwandishi kutangaza vitabu vyake ni kushiriki maonesho ya vitabu. Hapa Marekani kuna maonesho ya vitabu mara kwa mara, kwenye maeneo mbali mbali ya nchi. Mengine huwa ni ya sehemu fulani ya nchi, na mengine huwa ni ya kitaifa. Nimeshiriki maonesho haya mara kwa mara, na nimekuwa nikiandika taarifa katika blogu hii na pia blogu ya ki-Ingereza.

Mwandishi anaweza kulipia matangazo katika vyombo vya habari. Lakini kutokana na uzoefu wangu, ninasita kupendekeza utangazaji wa aina hii. Ni bora mwandishi atumie njia zisizo na gharama. Kwa mfano, mwandishi anaweza kupeleka nakala za kitabu chake kwa wahakiki, ili wasome na kuandika uchambuzi katika magazeti.

Vile vile, tuzingatie kuwa tunaishi katika dunia ya mitandao, ambayo imeleta fursa nyingi. Kwa mwandishi mwenye blogu au tovuti, ni rahisi kutangaza kitabu chake. Mimi mwenyewe ninafanya hivyo katika blogu zangu na katika tovuti ya Africonexion. Vile vile tekinolojia za uchapishaji zinatuwezesha kuchapisha moja kwa moja mtandaoni, na vitabu vikapatikana huko, kama ilivyo kwa vitabu vyangu.

Hata hivyo kuna aina ya utangazaji ambayo huenda ni muhimu kuliko zote. Hii ni aina ya utangazaji unaofanywa na wasomaji. Kama ilivyo katika biashara yoyote, wateja ni watangazaji wakuu. Mteja akiridhika au kufurahi, anakuwa mpiga debe mkuu wa bidhaa au huduma.

Sisi wote tunafanya utangazaji wa bidhaa na huduma. Tukiona filamu nzuri, tunawaambia wenzetu. Tukinunua simu bora, tunawaambia wenzetu. Tukiwa katika mji mgeni, tukataka kujua nyumba bora ya kufikia wageni, au hoteli nzuri, wenyeji au madreva wa teksi watatuelekeza. Tunafanya kibarua cha kutangaza bidhaa za watu bila malipo.

Na vitabu ni hivi hivi. Msomaji akishasoma kitabu akakipenda, hakosi kuwaambia wengine. Hivi ndivyo kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences kilivyoenea kwa kasi hapa Marekani. Baadhi ya wasomaji wangu ambao wamekuwa wapiga debe wangu nimekuwa nikiandika habari zao katika blogu hii.

Utangazaji huu unaofanywa na wateja walioridhika au kufurahi unaaminika sana. Sisi sote tukiambiwa na marafiki au ndugu zetu kuhusu ubora wa bidhaa fulani au huduma fulani tunaamini bila kusita. Tunaweza kuwa na wasi wasi na matangazo yanayowekwa na watu tusiowajua katika vyombo vya habari. Huenda tunahisi kwamba wafanya biashara hawaangalii maslahi yetu bali yao wenyewe, na wako tayari hata kutuuzia bidhaa mbovu. Lakini tunajua kuwa marafiki au ndugu zetu wanazingatia maslahi yetu. Hii ndio sababu utangazaji unaofanywa na wateja una umuhimu sana.

Pamoja na yote niliyosema hapa juu, uamuzi wa kukitangaza kitabu unaweza kuwa na utata. Kwa upande moja, kitabu kikishachapishwa, kuna umuhimu wa kukijulisha kwa jamii. Kwa upande mwingine, kuna busara ya wahenga kuwa chema chajiuza; kibaya chajitembeza. Je, mwandishi afanyeje? Kwa mtazamo wangu, ni juu ya kila mwandishi kutafakari suala hili na kufanya uamuzi.

Sunday, September 11, 2016

Umuhimu wa Kusoma Vitabu

Kusoma vitabu kuna manufaa mengi kwa mtu binafsi na kwa jamii. Tunaweza kuitafakari kauli hii kwa namna nyingi. Binafsi, daima ninakumbuka usemi wa Ernest Hemingway, "There is no friend more loyal than a book," yaani hakuna rafiki wa kweli kuzidi kitabu. Ni kauli fupi na rahisi kukumbukwa, lakini ninaiona kuwa yenye ukweli kabisa.

Kitabu ni rafiki ambaye yuko kwa ajili yako muda wowote unapomhitaji. Kitabu kinaweza kuwa mshauri wako, kiongozi wako, nguzo ya kuitegemea.

Akili ya binadamu inahitaji matunzo, sawa na bustani. Bustani inahitaji kurutubishwa na kupaliliwa. Ikiachwa ivamiwe na magugu, inageuka kichaka. Kusoma vitabu ni kurutubisha akili na kuipalilia. Kama mtu anaweza, ni muhimu kusoma vitabu vya aina mbali mbali: vya siasa, saikolojia, fasihi, sayansi, maisha ya watu maarufu, falsafa, historia, uchumi, na kadhalika.

Ni makosa kudhani kuwa kusoma vitabu kunawahusu wanafunzi na waalimu pekee. Kila mtu anapaswa kusoma vitabu. Tutafakari manufaa yake kwa afya ya akili ya binadamu kama yalivyoelezwa kwa ufupi katika makala hii. 

Saturday, September 10, 2016

Mashairi Mawili ya Edmund Spencer

Edmund Spencer ni mmoja kati ya washairi maarufu kabisa katika ki-Ingereza. Alizaliwa London mwaka 1552, akafariki 1599. Ni sahihi kusema kwamba shairi maarufu kabisa la Edmund Spencer ni utenzi uitwao "The Faerie Queene." Lakini Edmund Spencer ni maarufu pia kwa utunzi wa mashairi ya muundo wa "sonnet." Mwanatamthilia Shakespeare, ambaye alizaliwa mwaka 1564 na kufariki mwaka 1616, naye alikuwa mtunzi maarufu wa "sonnet."

Hapa naleta "sonnet" mbili za Edmund Spencer ambazo zinabainisha sanaa ya mshairi huyu. Ki-Ingereza cha mashairi haya ni cha zama zile, lakini ukikisoma kwa utulivu na umakini, utakielewa.

Katika "Ye Tradefull Merchants," mshairi anawasuta wafanya biashara wanaosafiri mbali kutafuta utajiri. Anawaambia kuwa mpenzi wake ana utajiri wa uzuri kuliko hata vito wanavyovihangaikia hao wafanya biashara. Utajiri wa mpenzi huyo si tu wa kimaumbile, bali pia akili.

Katika "Trust Not the Treason," mshairi anatahadharisha kuhusu ghilba na udanganyifu wa mwanamke, tusije tukanaswa katika mitego ya  mwenye ghilba na udanganyifu, kwani mitego hiyo huwa kama ndoana ya dhahabu ambayo imebeba chambo cha kuwanasia samaki wajinga, na mwisho wake ni balaa. Sherti niseme kuwa, kwa mtazamo wa leo, wengi tunakerwa na dhana hii ya kwamba mwanamke ni chanzo cha matatizo.

Sio jambo jema kuuwasilisha utungo wa fasihi kwa muhtasari. Ni kosa lililojadiliwa kinaganaga katika insha maarufu ya Cleanth Brooks, "The Heresy of Paraphrase," ambayo imo katika kitabu chake kiitwacho The Well Wrought Urn. Utungo wa fasihi unajieleza wenyewe kikamilifu. Ni lazima kuusoma wote kikamilifu na kwa umakini. Muhtasari ni hujuma dhidi ya utungo.

Nimalizie kwa kusema kuwa ninavutiwa na wazo la kuyatafsiri mashairi haya kwa ki-Swahili, kama chemsha bongo. Si kazi rahisi, lakini inavutia.
--------------------------------------------------------------------------------------------------

(1) YE TRADEFULL MERCHANTS

Ye tradefull merchants, that with weary toyle,
Do seeke most pretious things to make your gain,
And both the Indias of their treasures spoile,
What needeth you to seeke so farre in vaine?
For loe! my love doth in her selfe containe
All this worlds riches that may farre be found:
If saphyres, loe! her eies be saphyres plaine;
If rubies, loe! hir lips be rubies sound;
If pearles, hir teeth be pearls, both pure and round;
If yvorie, her forhead yvorie weene;
If gold, her locks are finest gold on ground;
If silver, her faire hands are silver sheene:
     But that which fairest is but few behold,
     Her mind, adornd with vertues manifold.


(2) TRUST NOT THE TREASON

Trust not the treason of those smyling lookes,
Until ye have theyr guylefull traynes well tryde:
For they are lyke but unto golden hookes
That from the foolish fish theyr bayts do hyde:
So she with flattring smyles weake harts doth guyde
Unto her love, and tempte to theyr decay;
Whome, being caught, she kills with cruell pryde,
And feeds at pleasure on the wretched pray.
Yet even whylst her bloody hands them slay,
Her eyes looke lovely, and upon them smyle,
That they take pleasure in her cruell play,
And, dying, doe themselves of payne beguyle.
     O mighty charm! which makes men love theyr bane,
     And thinck they dy with pleasure, live with payne.

Friday, September 9, 2016

Nimeanza Kufundisha Leo

Jana tumeanza muhula mpya wa masomo hapa chuoni St. Olaf, nami nimeanza kufundisha leo. Masomo yangu kwa muhula huu ni matatu: First Year Writing, African Literature, na Muslim Women Writers.

Tumeanza vizuri. Nimepata fursa ya kuwaeleza wanafunzi mambo ya msingi kuhusu falsafa yangu ya ufundishaji, na kuhusu masomo. Nimesisitiza wajibu wa kufikiri na kuchambua masuala, wajibu wa kujenga hoja. Nimesisitiza msimamo wangu wa kulinda na kutetea uhuru wa fikra na kujieleza. Nimewahahakishia wanafunzi kuwa wawe tayari kukabiliana na fikra na hoja mbali mbali.

Siku ya kwanza ya muhula ni kama kitendawili. Hatujui safari itakuwaje, siku hadi siku, lakini tunategemea matokeo mema. Ingawa uzoefu wangu wa kufundisha unaendelea kuongezeka muda wote, haiwezekani kupanga na kuwa na uhakika nini kitatokea. Jambo pekee lisilobadilika ni kwamba kila muhula ni tofauti na mwingine.

Thursday, September 8, 2016

Wasomaji Wangu Wa Nebraska Waendao Tanzania

Nina jadi ya kuwaongelea wasomaji wangu katika blogu hii, kama njia ya kuwaenzi. Ni jambo jema kwa mwandishi kufanya hivyo. Leo ninapenda kuwakumbuka wasomaji wangu wa sinodi ya Nebraska ya Kanisa la Kiluteri la Marekani, ambao tangu zamani wamekuwa na programu ya kupeleka watu Tanzania kuendeleza uhusiano baina yao na wa-Luteri wa Tanzania.

Hao wasafiri, sawa na wenzao wa sinodi zingine za Marekani, wamekuwa wakitumia kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences katika kujiandaa kwa safari, ili kuzielewa tofauti za tamaduni za Marekani na Afrika. Ni elimu muhimu katika ulimwengu wa utandawazi wa leo, ambayo nje ya ufundishaji wa darasani, ninashughulika nayo.


Wakati huu ninapoandika, waumini wa Nebraska wanajiandaa kwa safari ya Tanzania, ambayo itafanyika mwezi Februari mwaka 2017. Wameitangaza safari hii mtandaoni, na mratibu mojawapo wa safari, Martin Malley, ameniandikia ujumbe leo akisema, "We still recommend your book." Katika ukurasa wa 16 wa chapisho la maelezo na maandalizi ya safari, kitabu hicho kimetajwa.

Ninapowakumbuka wasomaji wangu wa Nebraska, ninakumbuka nilivyokutana katika uwanja wa ndege wa Amsterdam na kikundi cha watu wa Nebraska waliokuwa wanakwenda Tanzania, tukasafiri pamoja. Mimi sikuwajua, ila wao walinitambua, kama nilivyoelezea katika blogu yangu ya ki-Ingereza.


Tuesday, September 6, 2016

Tamko la ACT-Wazalendo Kuhusu Hali ya Nchi

Tamko Rasmi la Kamati Kuu ya Chama cha ACT-Wazalendo kuhusu HALI YA NCHI
Dar Es Salaam, Jumanne, 06 Septemba 2016
Utangulizi
Jana Jumatatu, 5 Septemba 2016, Kamati Kuu ya Chama cha ACT-Wazalendo ilikutana katika kikao chake cha kawaida. Pamoja na mambo mengine, Kamati Kuu ilipokea, kujadili na kuidhinisha Taarifa kuhusu HALI YA NCHI. Taarifa hii sasa inatolewa rasmi kwa umma. Taarifa ipo katika maeneo makubwa manne: Hali ya kisiasa, hali ya kiuchumi, umoja wa kitaifa na hitimisho.
Hali ya Kisiasa
Kamati Kuu imezingatia kuwa Kikatiba, nchi yetu inafuata mfumo wa demokrasia ya vyama vingi. Katiba na Sheria mbalimbali zimeanisha utaratibu wa kazi na shughuli za vyama vya siasa. Ili kuhakikisha kwamba kazi na shughuli za vyama vya siasa zinakuwa endelevu, vyama vyenye kukidhi vigezo hupewa ruzuku kupitia Bajeti ya Serikali inayopitishwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano Tanzania.
Hata hivyo, katika awamu hii ya tano, Serikali ya Chama cha Mapinduzi imeamua kuzuia shughuli za siasa kwa kutumia nguvu ya Jeshi la Polisi na hata Jeshi la Wananchi. Kwa mujibu wa serikali ya CCM, shughuli za kiuenezi za vyama vya siasa kama vile mikutano ya hadhara, maandamano, makongamano, mijadala na hata mikutano ya ndani inapaswa kukoma mapema baada ya uchaguzi. Kisheria, huu ni uvunjifu wa Katiba na Sheria za nchi.
Kisiasa, tunatambua kwamba Viongozi wa CCM wamepoteza mvuto kwa wananchi na sasa wanamsukuma Mwenyekiti wao Rais Magufuli kutumia jeshi katika kuokoa taswira ya Chama cha Mapinduzi mbele ya umma.
Kwa kuzingatia hali ya kisiasa nchini kwa sasa, Kamati Kuu ya chama chetu:
i) Tunalaani na kupinga kwa nguvu zetu zote hatua za Serikali ya Chama cha Mapinduzi za kuvunja Katiba na kujaribu kuweka pembeni utawala wa sheria.
ii) Tunapinga vitendo vinavyozidi kushamiri katika serikali hii ya CCM ya kujaribu kuendesha nchi kwa ubabe na matamko ya viongozi badala ya utawala wa sharia.
iii) Tutasimama imara, na tutaungana na vyama vingine vya siasa pamoja na taasisi zingine za kiraia katika kulinda mfumo wa demokrasia ya vyama vingi, uhuru wa maoni, na utawala wa sheria katika nchi yetu
Hali ya Kiuchumi
Katika miaka 10-15 iliyopita, nchi yetu imejenga uchumi ambao umekuwa ukikua kwa kiwango cha asilimia 6-7 kwa mwaka katika kipindi chote hiki. Ukuaji huu wa uchumi ulitokana na juhudi za nchi katika kuvutia wawekezaji na kuchochea shughuli za uzalishaji mali kwa wananchi wenye kipata cha chini. Awamu ya tano ya Serikali ya Chama cha Mapinduzi imerithi changamoto ya uchumi unaokua bila kuwafaidisha wananchi wa kawaida. Hili ndilo tulitegemea Serikali mpya ishughulike nalo.
Kamati Kuu imeshtushwa na hali ya kuanza kudorora kwa shughuli za uchumi katika kipindi cha miezi kumi ya utawala wa awamu ya tano. Kwa mfano:
a) Taarifa za Benki Kuu zilizopo kwenye tovuti yake (Quarterly Economic Review na Monthly Economic Review) kwa robo ya mwisho ya mwaka 2015 (Oktoba – Desemba 2015 ) zinaonesha kuwa kasi ya ukuaji wa Pato la Taifa ilikuwa 9%. Katika robo ya kwanza ya mwaka 2016 (Januari – Machi 2016) kasi ya ukuaji wa Pato la Taifa ilishuka hadi kufikia 5.5%. Kiuchumi, hii inamaanisha kuwa ukuaji wa shughuli za kiuchumi katika kipindi cha miezi 6 ya mwanzo ya utawala wa awamu ya tano chini ya Rais Magufuli umepungua kwa 4%.
b) Shughuli za uchumi zinazohusu wananchi masikini zimeshuka kutoka kasi ya ukuaji ya 10.20% robo ya mwisho ya mwaka 2015 mpaka 2.7% katika robo ya kwanza ya mwaka 2016, ikiwa ni punguzo la 8% ndani ya kipindi kisichozidi miezi sita. Hii ina maanisha kwamba Wananchi wetu wanazidi kudumbukia kwenye ufukara kwa kasi tangu awamu ya tano ya Serikali ya Chama Mapinduzi iingie madarakani
c) Ukuaji wa sekta ya ujenzi katika robo ya mwisho ya mwaka 2015 ilikuwa 13.8% lakini ukuaji wa sekta hii katika robo ya kwanza ya mwaka 2016 ilikuwa ni 4.30%, ikiwa ni tofauti ya takribani -10%. Hii ni kwa sababu uwekezaji katika sekta hii umeanza kushuka.
d) Kasi ya ukuaji wa sekta ya usafirishaji imeporomoka kutoka kukua kwa 14.50% robo ya mwisho ya 2015 mpaka kukua kwa 7.9% robo ya kwanza ya 2016, ikiwa ni kuporoka kwa 7% katika kipindi cha miezi 6 tu ya kwanza ya utawala wa Rais Magufuli. Kuporomoka kwa sekta ya usafirishaji itaathiri watu wengi, wakiwemo madereva, matingo, pamoja na mama Ntilie wanaowauzia chakula. .
Kwa kuzingatia mwenendo wa hali ya uchumi katika nchi, Kamati Kuu:
a) Tunaitaka serikali izingatie sayansi ya uchumi katika kuendesha uchumi wa nchi. Uamuzi wa CCM wa kuitelekeza serikali yake kwa mwanasiasa mmoja anayedhani ndiye anayejua kila kitu na yeye kugeuka kuwa mshauri wa washauri wa uchumi itasambaratisha uwekezaji nchini na kuua kabisa juhudi za miaka 20 za kuvutia wawekezaji na kujenga uchumi shirikishi.
b) Inahimiza wananchi kuzingatia kuwa msingi wa uchumi wetu ni uwekezaji kutoka ndani na nje ya nchi. Msingi wa kuvutia wawekezaji ni utawala wa sheria. Juhudi za serikali ya CCM za kuua utawala wa sheria zitaua uwekezaji na kuangamiza uchumi wa nchi. Tusirihusu CCM iue uchumi wa nchi kwa maslahi yake ya kisiasa na viongozi wake.
Umoja wa Kitaifa
Nchi yetu imefanya juhudi kubwa katika miaka 50 iliyopita katika kujenga umoja na mshikamano wa kitaifa kwa kuhakikisha kuwa makabila, dini na baadaye vyama vya siasa tunaishi bila kukamiana. Juhudi za dhati za kupambana na ubaguzi ndiyo umekuwa msingi imara wa kujenga Umoja wa Kitaifa na amani tunayojivunia.
Hata hivyo, Kamati Kuu imezingatia kuwa utawala mpya wa Serikali ya CCM, kupitia Mwenyekiti wake mpya na Rais wa Jamhuri wa Muungo, umeanza kwa juhudi na kasi kubwa kuchokonoa na kumomonyoa misingi ya utaifa na umoja wetu. Sasa tunaye Rais asiyechagua maneno na asiyejua aongee nini na wapi. Vijana waliosoma kwa bidii katika mazingira ya shule zilizotelekezwa na serikali ya CCM anawaita VILAZA.
Katikati ya uhasama mkubwa wa kisiasa na kijamii huko Zanzibar Rais wetu amefunga safari, sio kujaribu kutibu majeraha yaliyosababishwa na kuchezewa kwa sanduku la kura, bali kuchochea uhasama chini ya ulinzi wa vyombo vyetu vya dola vyenye jukumu la kulinda na kudumisha amani. Sasa Rais wetu, kupitia kauli zake, ameanza kuubomoa muungano wetu uliojengwa kwa unyenyekevu na katika mazingira magumu.
Kila asimamapo kuhutubia, jambo moja la kutarajiwa kutoka katika kinywa cha Rais wetu ni matamshi yanayodhoofisha nguzo fulani ya umoja, mshikamano na undugu wetu kama taifa. Yote haya yakitokea chama chake cha CCM ama kimekaa kimya au kinachekelea. Inasikitikitisha kwamba Chama kilichoasisiwa na Mwalimu Nyerere kinamruhusu kiongozi wake kubomoa misingi ya umoja wa kitaifa na kuchochea chuki katika jamii ya watanzania.
Kwa kuzingatia mtikisiko mkubwa katika umoja na mshikamano wa kitaifa unaoendelea nchini, Kamati Kuu:
a) Tunalaani juhudi zinazofanywa na Serikali ya CCM kupitia Mwenyekiti wao za kuchochea chuki katika jamii ya watanzania na kubomoa misingi ya umoja wa kitaifa na amani ya nchi
b) Tunatoa wito kwa watanzania wote waipendayo nchi yao kusimama kidete katika kulinda misingi ya nchi yetu na kukataa chuki inayoanza kujengwa na utawala wa CCM
c) Tunatoa wito wa kipekee kwa viongozi wetu wa dini na wakuu wa nchi waliopita, hususani Mzee Ali Hassan Mwinyi, Mzee Benjamin Mkapa na Mzee Jakaya Mrisho Kikwete, pamoja na wazee wengine wanaoheshimika katika nchi yetu wavae ujasiri wa kumuonya Mwenyekiti wa CCM kuwa juhudi zake za kuchochea chuki katika jamii yetu ya watanzania zitasambaratisha Taifa letu.
Hitimisho
i) Sisi kama chama cha siasa, tunaendelea kusisitiza kuwa tutaunga mkono juhudi za serikali ya awamu ya tano katika kupambana na ufisadi na kujenga uwajibikaji nchini.
ii) Tunaamini kwa dhati kabisa kuwa kuheshimu na kulinda demokrasia na kuzingatia utawala wa sheria nidyo msingi wa mapambano dhidi ya ufisadi. Tunasisitiza kuwa mtu yeyote, wa kawaida au kiongozi, anayesema kwamba anaweza akapambana na ufisadi kwa kukanyaga misingi ya demokrasia na utawala wa sheria mtu huyo ni mwomgo na kwa kweli ni fisadi na anataka kujenga himaya mpya ya ufisadi. Mtu huyo, pamoja na mambo yake yote, yafaa akataliwe na kudharauliwa haraka!
iii) Tunasisitiza kuwa msingi wa uchumi wetu ni kuvutia uwekezaji wa ndani nan je ya nchi. Kuzingatia utawala wa sheria ndiyo msingi wa kuvutia uwekezaji. Juhuzi za hivi karibuni za serikali ya CCM za kujaribu kuua utawala wa sharia ni juhudi ovu za kuua uchumi wa nchi yetu. TUZIKATAE juhudi za kuua utawala wa sheria kwa kuwa zitaangamiza taifa letu kiuchumi, kisiasa na kijamii.
Kabwe Zuberi Ruyagwa Zitto, Mb
Kiongozi wa Chama
Dar es Salaam, Jumanne 6 Septemba 2016.

Sunday, September 4, 2016

Naomba Kitabu Changu Kipigwe Marufuku

Naiomba serikali ikipige marufuku kitabu changu, CHANGAMOTO: Insha za Jamii. Kitabu hiki kina mawazo ambayo ni kinyume na yale yanayotakiwa na serikali. Kama vile hii haitoshi, kitabu hiki ni cha uchochezi. Tusikubali kurudia makosa kama yale ya kale ambapo Socrates alikuwa anawachochea watu, hasa vijana, wahoji mambo yanayokubalika katika jamii.

Imenibidi nitoe ombi hili la kupigwa marufuku kitabu changu kwa sababu za msingi. Kwanza kama mtu mwingine yeyote mtiifu kwa serikali, ninatambua wajibu wangu wa kuripoti jambo lolote linalokwenda kinyume na maelekezo au matakwa ya serikali. Pili, mimi sina mamlaka kisheria ya kukipiga marufuku kitabu chochote. Kwa hivi, ninaiangukia serikali.

Mawazo yaliyomo katika kitabu hiki yasipodhibitiwa, yakiachwa yaenee, yatajenga ukaidi miongoni mwa raia na tabia ya kutowaheshimu viongozi. Ninaelewa kuwa ni juu ya serikali kufikiri na kufanya maamuzi. Wajibu wa raia ni kutii. Raia wakiachwa huru kufikiri na kujiamulia mambo, kuna hatari kwamba misingi imara ya amani na utulivu nchini itaharibika na itakuwa vigumu kwa nchi kutawalika.

Saturday, September 3, 2016

Shakespeare Ametawala Mawazo Yangu Leo

Leo Shakespeare ametawala mawazo yangu, nami ninapenda kuelezea ilivyotokea. Ni maelezo yanayoweza kubainisha namna akili yangu inavyofanya kazi ninapohangaika kuandika makala ya kitaaluma.

Kwa miezi kadhaa, nimekuwa nikiwazia kuandika makala juu ya utangulizi wa The Dilemma of a Ghost, tamthilia ya Ama Ata Aidoo wa Ghana. Utangulizi huu umeitwa "Prelude" katika tamthilia hiyo, ambayo Ama Ata Aidoo aliitunga alipokuwa mwanafunzi wa chuo kikuu Ghana, Legon, ambapo alihitimu mwaka 1963. Tamthilia yake iliigizwa kwa mara ya kwanza mwaka 1964 na kuchapishwa mwaka 1965.

Nimefundisha tamthilia hii mara kadhaa, na kwa miezi kadhaa nimepata hamu ya kuchambua utangulizi wake, yaani "Prelude." Nimeona kwamba hakuna mhakiki yeyote ambaye ameichambua sehemu hii ya tamthilia hii kwa kiwango kinachoniridhisha. Hii "Prelude" si rahisi kuifafanua. Ninahisi hii ndio sababu ya wachambuzi kuiacha kando.

Katika kuitafakari hii "Prelude," nimeona kuwa ujuzi wangu wa taaluma ya "Folklore" utakuwa nyenzo muhimu. Vile vile, nimeona kuwa italazimu kugusia jadi ya tamthilia ya nchi za Magharibi kuanzia Ugriki ya zamani.

Ni katika kuwazia jadi hii ndio nikajikuta ninamkumbuka Shakespeare. Katika "Prelude" yake, Ama Ata Aidoo ametumia dondoo za lugha ambazo zinatupeleka kwa Shakespeare. Sishangai, nikizingatia kuwa Ama Ata Aidoo alisomea ki-Ingereza na fasihi katika mfumo wa elimu wa ukoloni wa ki-Ingereza. Kwa maana hiyo, Ama Ata Aidoo alilelewa katika mfumo ambao walilelewa waandishi wa enzi zake, na waliofuatia, kama vile Efua Sutherland, Wole Soyinka, na James Ngugi, ambaye baadaye alibadili jina na kujiita Ngugi wa Thion'go.

Baada ya kujiridhisha kwamba kuna athari za Shakespeare katika "Prelude" ya The Dilemma of a Ghost, ndipo nikawa nawazia kutafuta ushahidi katika tamthilia za Shakespeare. Kwa miezi yote hii, nilikuwa na uhakika kwamba baadhi ya athari zimetoka katika tamthilia kadhaa na pia mashairi ya Shakespeare, na baadhi ya athari nilihisi zilitokana na au tamthilia ya The Merchant of Venice au Hamlet.

Kwa hivi, leo nimeteremsha kabatini buku langu kubwa liitwalo The Yale Shakespeare, ambalo lina tamthilia zote za Shakespeare na mashairi yake yote. Kila tamthilia imetanguliwa na insha iliyoandikwa na mchambuzi mahiri na imeambatana na maelezo ya dhana, misemo na maneno ambayo watumiaji wa leo wa ki-Ingereza inaweza kuwawia vigumu kuelewa.

Kwa miezi kadhaa, kabla ya kuanza kufukuafukua maandishi ya Shakespeare leo, nimekuwa nikitafakari vipengele vya "Folklore" ambavyo ninavyoviona katika "Prelude." Pia nimekuwa nikitafiti zaidi vipengele hivyo, kwa kufuatilia maandishi ya wataalam kama William Bascom. Sina shaka kwamba tafakari hiyo na utafiti vitaniwezesha kuifafanua "Prelude" na matumizi ya "Folklore" katika tamthilia nzima ya The Dilemma of a Ghost.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...