Saturday, February 20, 2010

Maandalizi ya "Afrifest 2010"

Leo nilienda Minneapolis kwenye mkutano wa maandalizi ya Afrifest, tamasha la utamaduni linalofanyika hapa Minnesota kila mwaka, kama kielelezo cha historia na mchango wa wa-Afrika katika ulimwengu.
Tulikutana katika mgahawa uitwao 1st Cup Cafe. Ni sehemu ambapo wa-Afrika hupenda kukutana na shughuli nyingi hufanyika hapo, kama vile mihadhara, uzinduzi wa vitabu, na burudani.

Mwanzilishi wa Afrifest ni Nathan White, ambaye anaonekana katika picha hapa juu, wa pili kutoka kulia. Mimi ninayeonekana kulia kabisa nimekuwa mwanachama wa kamati hii tangu mwanzo. Mchango wangu umekuwa zaidi katika kuelezea historia ya watu wenye asili ya Afrika, tangu chimbuko la binadamu katika Afrika hadi kuenea kwa wa-Afrika hao sehemu mbali mbali za dunia. Hilo ndilo somo ninalotoa siku ya tamasha, nikiwa na vielelezo kadha wa kadha vya kimaandishi.
Shughuli zote tunazofanya kama wanakamati ni za kujitolea, lakini tunazifanya kwa moyo mmoja kwa vile tunaamini umuhimu wa kuwakutanisha watu wenye asili ya Afrika kwa kufuata nyayo za wale waliotutangulia, kama vile Marcus Garvey, Kwame Nkrumah, W.B. Dubois, Gamal Abdel Nasser, Jomo Kenyatta, Julius Nyerere, Malcolm X, Bob Marley na Walter Rodney. Ni fursa ya kujielimisha sisi wenyewe, kujikumbusha tulikotoka katika historia yetu na harakati tulizopitia, mafanikio na matatizo, na pia ni fursa ya kuwaelimisha wa-Marekani na wengine.
Kwenye mkutano wetu huu tulishughulikia zaidi masuala ya kuandaa katiba ya "Afrifest Foundation." Tulianza shughuli za Afrifest tukiwa na mfumo tofauti, ila sasa tunataka kujiimarisha zaidi kwa muundo wa "Foundation."

Kwa mwaka huu, tumepangia kufanya tamasha la Afrifest tarehe 7 Agosti. Wanakamati tutakuwa na mikutano mingi hadi kufikia siku ya tamasha. Wajumbe wawili watatu hawaonekani kwenye taarifa hii, kwa vile walikuwa na udhuru siku hiyo.

2 comments:

Sisulu said...

ni suala la kutia shime ni suala la kutia afya kuyajadili yahusuyo afrika kuyanyumbua na kuyahamasisha. udumu umoja wa kiafrika.DAIMA MBELE

Mbele said...

Tuzidi kujibidisha na masuala haya. Tutafika.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...