Monday, January 5, 2015

Mkutano na Wanachuo wa Gustavus Adolphus

Leo asubuhi nilikwenda Mount Olivet Conference & Retreat Center, eneo la Farmington, hapa Minnesota, kuongea na wanachuo wa chuo cha Gustavus Adolphus ambao wanaelekea Tanzania kimasomo. Kwa siku hizi mbili tatu kabla ya safari yao, wamekuwa katika maandalizi, nami niliitwa na profesa wao Barbara Zust, kuongea nao kuhusu masuala ya utamaduni ambayo yamo katika kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Nimeshaalikwa mara kadhaa miaka iliyopita, kuongea na wanachuo wa Gustavus Adolphus, katika maandalizi ya kwenda Tanzania, kama nilivyoelezea katika blogu hii.

Nilikuwa nimeamua kuwa leo, baada kutoa utangulizi mfupi, nitumie muda karibu wote katika kujibu masuali ya hao wanachuo, kwani nilishafahamishwa kuwa watakuwa wamekisoma kitabu changu. Ilidhihirika wazi, kutokana na masuali yao, kuwa walikuwa wamekisoma kwa makini. Wote tuliyafurahia mazungumzo yetu, ambayo yalidumu kuanzia saa nne hadi saa sita. Baada ya hapo, tulikula chakula cha mchana, ambapo niliendelea na maongezi na Profesa Zust na mshiriki wake Mchungaji Todd Mattson, na wanachuo ambao tulikaa meza moja.

Tulipokuwa tayari kwenda kula, na mara baada ya chakula, wanafunzi kadhaa waliniletea nakala zao za kitabu changu ili nisaini,shughuli ambayo ninaamini inamgusa kila mwandishi na yule anayesainiwa kitabu. Baada ya shughuli hii tuliagana, tukiwa tunapeana shukrani tele, nami nikaanza safari ya kurejea Northfield, ambapo ninaishi.

Katika picha ya mwanzo hapa juu, ninaonekana hapo mbele. Kule nyuma kabisa, upande wa kulia mwishoni, anaonekana Mchungaji Mattson, mwenye ndevu nyeupe, na mbele yake ni Profesa Zust. Pichani hapa kushoto, naonekana nikisaini kitabu cha mwanafunzi mojawapo.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...