Thursday, April 2, 2015

Nimewasili Bemidji, Minnesota

Alasiri hii, nimewasili mjini Bemidji, nikiwa njiani na wenzangu watatu, ambao tumesafiri pamoja kutoka Minneapolis. Tutalala hapa, na kesho asubuhi tunakwenda Leech Lake Tribal College kwenye mkutano  kuhusu "Narratives of Identity." Mimi ni mmoja wa watoa mada wanne. Mada yangu itakuwa "Being African in America."

Tulipokuwa tunakuja, tulisimama kidogo katika mji uitwao Akeley, ili kuona sanamu ya Paul Bunyan, mhusika maarufu katika masimulizi ya jadi ya sehemu hii ya Minnesota, ambaye anajulikana sana pia Marekani na ulimwenguni. Sanamu hii inamwonyesha akiwa ameshika shoka lake. Ili kujionea jinsi sanamu hii ilivyo kubwa, ifananishe na sisi watatu ambao tumesimama hapo Mbele yake.


Tulipoingia Bemidji, tulikwenda moja kwa moja kwenye sanamu nyingine ya Paul Bunyan, ambayo inamwonyesha akiwa na fahali wake wa buluu ambaye ni sehemu muhimu ya masimulizi kuhusu mhusika huyu. Sanamu hiyo, sawa na ile ya Akeley, ni kubwa sana.

Kwa mujibu ya masimulizi, Paul Bunyan alikuwa jitu kubwa la ajabu, nadhani kumzidi hata Liongo Fumo, shujaa katika masimulizi ya jadi ya wa-Swahili, wa-Pokomo, na wengine katika mwambao wa Kenya.

Bemidji ni mahali ambapo niliwahi kufika miaka mitatu hivi iliyopita, lakini tangu muda mrefu kabla ya hapo nimetamani kuja kwa shughuli za utafiti wangu juu ya mwandishi Ernest Hemingway.

Mary Welsh, mke wa nne na wa mwisho wa Ernest Hemingway alizaliwa na kukulia eneo hili la Bemidji, kabla hajaenda kusoma katika Chuo Kikuu cha Northwestern, karibu na Chicago. Katika safari zake Kenya, Tanganyika, na Uganda, mwaka 1953-54, Hemingway alitanguzana na mke wake huyu.

Panapo majaliwa, nitakuja Bemidji kufanya utafiti huo. Kwa leo nimefurahi kuziona hizi sanamu, na kujionea jinsi Paul Bunyan alivyo maarufu eneo hili. Jina lake liko kila mahali. Nimeona mtaa wenye jina hilo, biashara mbali mbali, hata kampuni ya mawasiliano ya intanenti.

Hata katika hoteli tunamolala usiku huu, Hampton Inn, nimeona picha kubwa ya Paul Bunyan katika ukuta wa mgahawa. Kwangu mimi kama mtafiti wa masimulizi na mambo mingine ya jadi ("folklore"), nimeguswa sana na kupata hamasa ya kufanya utafiti juu ya Paul Bunyan.


No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...