Wednesday, June 15, 2016

Vitabu Nilivyochukua Safarini

Ninaposafiri kwa basi au ndege, ninapenda kuchukua kitabu au vitabu. Kwa kuwa si mimi ninayeendesha hilo basi au ndege, ninakuwa na muda mwingi wa kujisomea. Siku tatu zilizopita, tarehe 12 Juni, nilisafiri kwenda Boston, nikiwa na kitabu cha A Moveable Feast cha Ernest Hemingway, na Kusadikika cha Shaaban Robert.

Nilichukua A Moveable Feast kwa sababu safari yangu ilikuwa ya kwenda kufanya utafiti juu ya Hemingway na pia kwa kuwa kitabu hiki, ambacho nilifahamu habari zake, nilikuwa nimeanza kukisoma miaka michache iliyopita, hata nikanukuu sehemu yake moja katika blogu hii. Niliona kuwa ingekuwa jambo jema kuendelea kukisoma katika safari yangu ya Boston.
Nilichukua kitabu cha Kusadikika, kwa kujiweka tayari endapo ningependa kusoma pia kitabu tofauti. Sioni kama ni lazima nimalize kusoma kitabu nikiwa safarini. Inatosha kusoma kiasi fulani.

Jana, nikiwa bado mjini Boston, nilitembelea sehemu iitwayo Harvard Square, ambayo niliifahamu zamani kuwa ni sehemu yenye maduka ya vitabu. Niliingia katika duka moja la vitabu. Niliangalia vitabu vingi, nikanunua kimoja kiitwacho Rethinking Architecture: A Reader in Cultural Theory, kilichohaririwa na Neil Leach.

Nilivutiwa nilipoona kuwa ni mkusanyo wa makala za wataalam wengi, wakiwemo Theodor Adorno, Gaston Bachelard, Roland Barthes, Georges Bataille, Jean Baudrillard, Walter Benjamin, Ernst Bloch, Helene Cixous, Gilles Deleuze, Jacques Derrida, Umberto Eco, Michel Foucault, Jurgen Habermas, Martin Heidegger, Hans-Georg Gadamer, na Fredrick Jameson,



Majina ya wataalam hao niliowataja tulikuwa tunayasikia na maandishi yao tukiyasoma, nilipokuwa masomoni Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison, miaka ya 1980-86. Nilivutiwa kuona maandishi kama ya Walter Benjamin, "On Some Motifs in Baudelaire;" Gaston Bachelard, "Poetics of Space;" Martin Heidegger, "Building, Dwelling, Thinking;" Roland Barthes, "Semiology and the Urban;" Umberto Eco, "Function and Sign: The Semiotics of Architecture;" Fredrick Jameson, "Is Space Political?" Michel Foucault, "Space, Knowledge and Power (interview conducted with Paul Rabinow).

Kama nilivyogusia, nimevutiwa na juhudi ya mhariri wa Rethinking Architecture: A Reader in Cultural Theory kuzitafuta makala zinazohusu mada moja lakini kwa mitazamo mbali mbali kutoka uwanja mpana wa falsafa. Kwa jinsi ninavyowaheshimu wataalam ambao maandishi yao yamo katika kitabu hiki, nina imani kuwa hiki ni kitabu bora sana.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...