Wikiendi hii iliyopita, nilipokuwa Madison kwenye
mkutano wa Peace Corps, nilitembelea sehemu kadhaa nilizozifahamu tangu wakati nasoma
Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison, 1980-86. Nilivutiwa kwa namna ya pekee na wazo la kutembelea maskani yangu miaka ile.
Niliingia Madison nikitokea Tanzania mwezi Agosti mwaka 1980. Sikumbuki tarehe. Lakini nilifikia mahali palipoitwa Union South, katika eneo la
Chuo. Hapo nilikaa siku chache, nikingojea fedha kutoka Ofisi ya
Fulbright, ambao ndio walinilipia gharama zote za masomo.

Baada ya siku chache za kukaa Union South, nilihamia Saxony Apartments, sehemu inayoonekana hapa kushoto. Jengo nilimoishi liko nyuma ya hili linaloonekana.
Saxony Apartments ilikuwa maarufu, kwa vile walikuwepo wa-Afrika wengi. Tulijisikia nyumbani.

Nadhani nilikaa hapo Saxony Apartments kwa mwaka moja na zaidi, nikahamia Mtaa wa West Wilson, namba 420, jengo linaloonekana hapa kushoto. Ni karibu na Ziwa Monona. Wa-Tanzania tulikuwa na mshikamano sana, tukitembeleana na kushirikiana katika raha na shida. Nakumbuka mikusanyiko tuliyofanyia hapa kwangu.

Miaka yangu ya mwisho mjini Madison, niliishi mahala paitwapo Eagle Heights, eneo lenye nyumba nyingi sana za wanafunzi wenye familia. Nilikuwa naishi katika nyumba hii, orofa ya juu. Ukianzia kushoto, ni dirisha la tatu na la nne.
Wikiendi hii nilipokuwa nazungukia maeneo hayo nilijiwa na kumbukumbu nyingi za miaka ile. Niliwakumbuka wa-Tanzania na wa-Afrika wengine tuliosoma wote, na mengine mengi. Yawezekana baadhi yao wataziona picha hizi na kukumbuka mambo ya miaka ile.