Tuesday, May 30, 2017

Likizo Inaanza: Ni Kujisomea Vitabu na Kuandika

Tumemaliza muhula wa mwisho wa mwaka wa masomo hapa chuoni St. Olaf. Tunamalizia kusahihisha mitihani na matokeo yatakuwa yamekamilika tarehe 5 Juni. Kuanzia pale tutakuwa na miezi mitatu ya likizo. Lakini kwetu waalimu, likizo si likizo, bali fursa ya kujisomea, kufanya utafiti, na kuandika, bila kuhusika na ufundishaji darasani.

Mpango wangu kwa likizo hii ni kutumia wiki sita za mwanzo katika kujisomea vitabu na kuandika, halafu wiki sita zitakazofuata nitafundisha kozi ya fasihi ya Afrika. Kufundisha kipindi hiki cha likizo ni jambo la hiari. Mwalimu anatangaza kozi anayotaka kufundisha na wanafunzi wanaohitaji wanajisajili. Wanafunzi huwa wachache. Ni fursa nzuri kwa mwalimu kujaribisha mambo mapya.

Wakati huu ninavyoandika ujumbe huu, ninafadhaika katika kuamua nisome vitabu vipi. Maktaba yangu ina vitabu vingi ambavyo sijavisoma. Kwa likizo hii, nimewazia nisome tamthilia za William Shakespeare, au George Bernard Shaw, au Sean O'Casey, au Anton Chekhov, au riwaya za Orhan Pamuk ili niweze kupata mwanga juu ya huyu mwandishi maarufu aliyejipatia tuzo ya Nobel mwaka 2006 na ambaye nimekuwa nikimtaja katika blogu hii. Nimewazia pia kusoma hadithi fupi na riwaya za Ernest Hemingway, zile ambazo sijazisoma.

Ningependa kuonja uandishi wa Svetlana Alexievich, ambaye nimemgundua wiki iliyopita. Nilijipatia kitabu chake, Secondhand Time: The Last of the Soviets, cha bure, hapa chuoni. Sikuwa ninamfahamu mwandishi huyu mwanamke m-Rusi, ambaye alipata tuzo ya Nobel mwaka 2015, "for her polyphonic writings, a monument to suffering and courage in our time," kwa mujibu wa kamati ya tuzo.

Wafuatiliaji wa nadharia ya fasihi wanafahamu kuwa dhana ya "polyphony" katika fasihi ilifafanuliwa vizuri na mwanafalsafa na mhakiki m-Rusi Mikhail Bakhtin akimaanisha sauti na mitazamo mbali mbali inayounda kazi ya fasihi. Nimefurahi kumfahamu mwandishi huyu mwanamke kutoka u-Rusi. Amenifanya nimkumbuke mwandishi mwanamke m-Rusi, Anna Akhmatova, mshairi maarufu. Nina dukuduku ya kujua kama waandishi hao wawili wanaweza kulinganishwa.

Hakuna kazi ya fasihi inayozuka katika ombwe. Inatokana na jadi fulani na mfumo mpana wa kazi za fasihi, na kazi yoyote mpya inachangia jadi na mfumo wa fasihi. Dhana hiyo ilielezwa vizuri na T.S. Eliot, mshairi na mwanafasihi maarufu, katika insha yake, "Tradition and the Individual Talent."

Ninapowazia waandishi wa fasihi wanawake waliopata tuzo ya Nobel, majina yanayonijia akilini hima ni Sigrid Undset wa Norway, Nadine Gordimer wa Afrika Kusini, Toni Morrison wa Marekani, Alice Munro wa Canada, na Doris Lessing wa Zimbabwe na Uingereza. Ninashawishika na wazo la kutunga na kufundisha kozi juu ya maandishi ya wanawake waliopata tuzo ya Nobel katika fasihi.

Papo hapo, katika likizo hii ninataka kuendelea kuandika makala ambayo nilianza kuiandika miezi kadhaa iliyopita, "Folkloric Discourse in Ama Ata Aidoo's The Dilemma of a Ghost." Azma ya kuendelea kuandika makala hii ni kubwa, kwani ninaamini kuwa hii itakuwa makala bora kabisa.

Hizi ndizo ndoto zangu. Ni ajenda kubwa, kielelezo cha namna akili yangu inavyohangaika kutokana na kutambua kuwa vitu vy kusoma na kuandika ni vingi kuliko muda unavyoruhusu. Sitaweza kufanya yote ninayowazia kwa likizo hii, lakini si neno. Nitatumia muda wangu vizuri na kufanya nitakachoweza.

Saturday, May 27, 2017

"Witchcraft by a Picture" (John Donne)

Juzi, nilinunua kitabu cha mashairi kiitwacho The Works of John Donne, kama nilivyosema katika blogu hii. John Donne aliishi Uingereza, hasa London, miaka ya 1572-1631.

Katika kuyasoma mashairi yake, nimeona kuwa yanahitaji utulivu wa pekee, na tafakari, kwani matumizi yake ya lugha yanaonyesha uangalifu mkubwa. Ki-Ingereza chake ni cha miaka ile, ambayo ni miaka ya William Shakespeare, si cha leo. Hapa naleta shairi mojawapo, "Witchcraft by a Picture." Labda siku moja nitapata ujasiri wa kujaribu kulitafsiri kwa ki-Swahili.



         Witchcraft by a Picture

I fixe mine eye on thine, and there
     Pitty my picture burning in thine eye,
My picture drown'd in a transparent teare,
     When I looke lower I espie;
          Hadst thou the wicked skill
By pictures made and mard, to kill,
How many wayes mightst thou performe thy will?

But now I have drunke thy sweet salt teares,
     And though thou poure more I'll depart;
My picture vanish'd, vanish feares,
     That I can be endamag'd by that art;
          Though thou retaine of mee
One picture more, yet that will bee,
Being in thine owne heart, from all malice free.

Thursday, May 25, 2017

Vitabu Nilivyonunua Leo

Leo nikitokea Minneapolis, nilipita Apple Valley, katika duka la vitabu la Half Price Books. Nilikuwa nimepania kununua kitabu juu ya Hemingway, Hemingway's Boat: Everything He Loved in Life, And Lost, kilichotungwa na Paul Hendrickson, ambacho nilikifahamu kwa miezi, na hivi karibuni nilikiona katika duka hilo, kama nilivyoripoti katika blogu hii.

Kwa hivi, leo niliombea nikikute hiki kitabu, na kwa bahati nzuri nilikikuta. Baada ya kukichukua mahali kilipokuwepo, nilienda sehemu panapouzwa vitabu kwa bei ndogo zaidi. Bila kuhangaika sana, niliona kitabu kiitwacho F. Scott Fitzgerald, kilichotungwa na Arthur Mizener.  Nilifungua kurasa mbili tatu, nikakichukua.

Nilifahamu kwa muda mrefu kuwa Fitzgerald alizaliwa St. Paul, Minnesota, mji ninaoutembelea mara kwa mara. Nilishasoma riwaya yake maarufu, The Great Gatsby. Halafu, miaka hii ambapo nimekuwa nikisoma sana maandishi na habari za Ernest Hemingway, nimeelewa kuwa haiwezekani kumtenganisha Hemingway na Fitzgerald.

Hemingway alipokuwa kijana, akiishi Paris kama ripota wa gazeti la Toronto Star na pia kama mwandishi wa hadithi fupi na riwaya, alikuwa na mahusiano ya karibu na waandishi wengine waliokuwepo Paris, kama vile Gertrude Stein, Ezra Pound, na huyu F. Scott Fitzgerald. Fitzgerald alifanya bidii kumwezesha Hemingway kuanza kuandika riwaya, akafanya juhudi zilizomfanya Marx Perkins, mhariri maarufu wa kampuni ya Scribners Sons, akachapisha riwaya ya Hemingway, The Sun Also Rises. Hayo ndiyo mawazo yaliyonifanya nikanunua kitabu hiki.

Hapo hapo, nilivutiwa na kitabu kiitwacho The Works of John Donne, kilichoandaliwa na The Wordsworth Poetry Library. Sikuwa ninakifahamu kitabu hiki. Jina la mshairi John Donne nimelifahamu tangu zamani, labda nilipokuwa mwanafunzi katika shule ya sekondari. Nadhani nilishasoma mashairi yake mawili matatu, lakini sio zaidi.

Ila kwa kusoma maandishi ya wahakiki na wanataaluma, nilifahamu kuwa Donne anahesabiwa kama mshairi anayeandika mashairi magumu kuyaelewa. Habari hii ilichangia kunifanya nisiwe mwepesi wa kusoma mashairi yake. Nadhani si jambo zuri kwa mwandishi kuvumishiwa sifa kwamba tungo zake ni ngumu kueleweka. Inaweza kuwakatisha wasomaji hamu ya kujisomea maandishi ya mwandishi huyo.

Kwa Afrika, mashairi ya Christopher Okigbo yamepewa sifa hiyo. Pia mashairi ya Wole Soyinka. Lakini kwa umri nilio nao, na uzoefu wangu wa kusoma na kufundisha fasihi, naona ni vema kuwahimiza watu wajisomee wenyewe tungo zozote, kwani kwa kufanya hivyo, na kama wanafanya juhudi ya dhati, ni lazima wataambulia chochote. Nazingatia nadharia inayosema kwamba utungo wa fasihi una uwezo wa kuzalisha maana na tafsiri nyingi bila kikomo. Nadharia hii imefafanuliwa na wataalam kama Roland Barthes.

Sunday, May 21, 2017

"Contagious Success," Kitabu Muhimu

Nina furaha wakati huu kwa kuwa ninasoma kitabu kiitwacho Contagious Success: Spreading High Performance Throughout Your Organization. Nilinunua kitabu hiki siku chache zilizopita, kama nilivyoripoti katika blogu hii. Sikupoteza fedha zangu.

Mwandishi wa kitabu hiki, mwenyekiti wa Hudson Highland Center for High Performance, ni mwenye ujuzi na uzoefu mkubwa. Kitabu chake hiki ni matokeo ya utafiti ulioshirikisha watu wa sehemu mbali mbali ulimwenguni, ambao ni wafanyakazi katika sekta zinazotegemea na kuendeshwa na ujuzi na maarifa. Kwa ki-Ingereza, watu hao huitwa "knowledge workers." Hii ni dhana muhimu katika dunia ya leo na kesho, ambayo inaendelea kuwa dunia ya "knowledge economy."

Tangu mwanzo, kitabu hiki kina mafundisho muhimu kwa viongozi, mameneja, wamiliki wa biashara, watoa huduma na kadhalika. Ujumbe mahsusi ni namna ya kuyaeneza mafanikio katika shirika, kampuni, taasisi, au jamii. Mwandishi anasema: "Every company has high-performing workgroups that both make money for the business and develop new products, services, or markets. These work groups create environments in which results are achieved and people flourish."

Jambo muhimu kabisa ni kujenga mazingira ya kuwezesha ufanisi. Hata kama mtu ni hodari namna gani, hawezi kufanikiwa ipasavyo katika mazingira yasiyo muafaka. Mazingira ni msingi wa mafanikio, na ufanisi wa kikundikazi au vikundikazi unapata fursa ya kuenea katika kampuni au shirika zima.

Mwandishi ananukuu kauli za wataalam waliofafanua mawazo hayo: "According to Daniel Gilbert, Professor of psychology at Harvard University, 'Four decades of scientific research have shown that situations are powerful determinants of human behavior--and much more powerful determinants than most of us realize.'"

Baada ya maelezo, mwandishi analeta nukuu nyingine: "'Changing the situation and shaping the environment--that's what leadership is all about,' noted Linda Ginzel, clinical professor of managerial psychology at the University of Chicago Graduate School of Business."

Mwandishi anaelezea zaidi wazo hilo, na halafu analeta mawazo ya ziada. Kwanza, nyakati zimebadilika. Dunia ya leo si ile ya wakati mapinduzi ya viwanda ("Industrial Age") ambapo wafanyakazi walisimama katika mstari na uzalishaji wa bidhaa ulikuwa unatiririka kama mnyororo ("assembly line"). Wakati ule maamuzi ya namna kuendesha kiwanda yalikuwa mepesi na wazi kuliko sasa. Ushindani haukuwa mkubwa kama leo. Amri zilikuwa zinatoka juu kwa viongozi na kwenda chini, bila matatizo. Wafanya kazi waliwajibika kutii walichoambiwa. Hawakuhitaji kuwa wabunifu.

Leo mambo yamebadilika. Wafanyakazi hawatakiwi wawe watu wa kufuata tu maelekezo. Lazima watumie akili na ubunifu, kukabiliana na mazingira ya leo. Mazingira haya yanahitaji pia mabadiliko ya mtindo wa uongozi: "The strategies that worked in the Industrial Age are no longer effective. Leaders need to be honest about their own strengths and weaknesses. They must recognize that they can't be or do everything and, therefore, should make sure the people around them have complementary strengths."

Anaendelea kufafanua, kwa kunukuu kauli ya Carol Hymowitz katika Wall Street Journal:  "Arrogance is out of fashion in the executive suite. So are autocratic executives who rule by intimidation, think they have all the answers and don't believe they need to be accountable to anyone."

Kuhitimisha suala hili la uongozi mpya, mwandishi anasema kuwa uongozi ni lazima uwe unawathamini watu, unathamini ubunifu na uthubutu, na uwe mwepesi kuzitambua na kuzikamata fursa zinazojitokeza.

Nilivyokuwa ninasoma haya mawazo, nimejikuta nikiwazia Tanzania na malengo ya serikali ya kujenga nchi ya viwanda. Nimeona wazi kuwa ili tufanikiwe, lazima tujiweke sawa kwa mambo mengi, kama haya ya kuwathamini watu, kuweka mazingira muafaka na kuzingatia rasilimali watu, ambayo inakwenda sambamba na kuwapa watu uhuru wa kufikiri, kuwa wabunifu na watundu, hata kama kwa utundu wao wanaishia kufanya makosa. Watu wakiwa na uoga wa kufanya makosa, mafanikio yanaweza kuwa shida kupatikana.

Kitabu hiki cha Contagious Success nimekifurahia sio tu kwa sababu kinaelimisha sana, bali pia, kwa kiasi kikubwa, kwa sababu kimenikumbusha kitabu kingine, Leading Beyond the Walls, ambacho ninacho na nilikiongelea katika blogu hii.

Thursday, May 18, 2017

Vitabu Nilivyonunua Jana

Jana nilinunua vitabu vitatu katika duka la vitabu la chuoni St. Olaf. Viwili, Two Years Eight Months and Twenty-Eight Nights cha Salman Rushdie na A Strangeness in my Mind cha Orhan Pamuk, niliviona juzi. Cha tatu, Why Homer Matters, kilichotungwa na Adam Nicolson, nilikiona hiyo hiyo jana.

Nilipoingia dukani, nilikumbuka makala niliyoisoma juzi usiku, kuhusu vitabu halisi na vitabu pepe. Makala hii, sawa na nyingine nyingi, inatafakari iwapo vitabu vya jadi vitasalimika katika himaya hii ya vitabu pepe. Lakini inahitimisha kuwa hakuna ushahidi kuwa vitabu vya jadi vitapoteza mvuto au kufifia.

Mimi ni mmoja wa wale ambao hatujabadilika. Bado tumezoea vitabu halisi, yaani vitabu vya jadi, na ndio maana sisiti kuvinunua, wala sisiti kuelezea tabia yangu hiyo. Hapa nitaelezea kifupi kwa nini nimenunua vitabu hivi vitatu.

Kitabu cha Salman Rushdie kilinivutia kwa sababu ya umaarufu wa mwandishi huyu. Bila shaka wengi watakumbuka kitabu chake, Satanic Verses, ambacho kilipigwa marufuku katika nchi nyingi kwa madai kuwa kinaukashifu u-Islam. Ayatollah Khomeini wa Iran alitangaza fatwa kuwa Salman Rushdie anapaswa kuuawa.

Duniani kote, na hata miongoni mwa wa-Islam wenyewe hukumu hii ilizua mjadala. Baadhi walisema kuwa fatwa haikupaswa kutolewa kabla ya Salman Rushdie kupewa fursa ya kujieleza na kukiri kosa lake. Watu wengine walisema kuwa zogo hili lilimpa Salman Rushdie umaarufu ambao hakustahili kwa kigezo cha ubora wa uandishi wake.

Ninavyo baadhi vitabu vya Salman Rushdie, kikiwemo hiki cha Satanic Verses. Nimemewahi kufundisha riwaya yake maarufu, Midnight's Children. Ninavutiwa na ubunifu wake katika kuelezea mambo, na uhodari wake wa kutumia lugha. Uandishi wake unasisimua na kufikirisha.

Orhan Pamuk ni mwandishi ambaye nimewahi kumtaja katika blogu hii. Nina vitabu vyake kadhaa, na nimekuwa na hamu ya kuvisoma, ila bado sijapata wasaa. Huyu amenivutia si tu kwa kuwa alipata tuzo ya Nobel, bali pia kwa sababu ninafahamu kiasi fulani kuhusu fasihi simulizi ya Uturuki, kama vile hadithi za Nasreddin Hodja na Dede Korkut.

Why Homer Matters nimekipenda kwa kuwa taaluma ya tendi nimeipenda na kuishughulikia kwa miaka mingi. Homer, ingawa taarifa zake hazijulikani vizuri, ndiye anayehusishwa na tendi maarufu za u-Griki ya kale, The Iliad na The Odyssey. Kwa kuangalia juu juu, niliona kuwa mwandishi wa Why Homer Matters ana uwezo mkubwa wa kuelezea masuala ya Homer na hizi tendi.

Sunday, May 14, 2017

Vitabu Nilivyonunua Leo

Leo nilikwenda tena Apple Valley, kwa muda mfupi, nikaingia katika duka la Half Price Books. Niliangalia kwanza sehemu vinapowekwa vitabu vya Hemingway au juu ya Hemingway. Kitabu cha pekee nilichokiona, ambacho nimekifahamu kwa miezi kadhaa ila sijakinunua, ni Hemingway's Boat: Everything He Loved in Life, And Lost, kilichotungwa na Paul Hendrickson.

Nilielekea sehemu ambapo huwekwa vitabu vya bei rahisi kabisa. Kwa kuwa sikuwa na muda mwingi, niliangalia haraka haraka, nikaona kitabu cha Matigari cha Ngugi wa Thiong'o, kilichotafsiriwa kwa ki-Ingereza na Wangui wa Goro. Ngugi alikuwa amekiandika kwa Kikuyu. Nilivutiwa kuona kuwa ni nakala ya jalada gumu, iliyochapishwa na Africa World Press. Nilichukua. Wasomaji wa Ngugi wanakumbuka kuwa tafsiri hii ilichapishwa kwanza na Heinemann.

Kisha, sehemu hiyo hiyo, katika kuchungulia chungulia, niliona kitabu Contagious Success: Spreading High Performance Throughout Your Organization, kilichoandikwa na Susan Lucia Annunzio. Nilivyoona kuwa kinahusu mbinu za kusambaza ufanisi katika makampuni na mashirika nilikichukua hima. Dhana ya maambukizi ya mafanikio ilinivutia.

Ninapenda kusoma vitabu vinavyohusu ujasiriamali na biashara, kwa sababu mimi mwenyewe ninajiona kama mjasiriamali jamii ("social enterpreneur"). Vile vile, ninavipenda vitabu hivi vinahusu masuala yenye uhusiano na taaluma ambazo nimezizoea, hasa saikolojia.

Saturday, May 13, 2017

Msikilize Raia wa Marekani Anavyomrarua Kiongozi

Jambo moja linalonivutia kuhusu Marekani ni uhuru wa kujieleza. Katiba ya Marekani inalinda uhuru huo kikamilifu. Kwa mfano, kulikuwa na kesi dhidi ya mtu aliyechoma moto bendera ya Taifa, lakini mahakama kuu iliamua na imeendelea kusisitiza kuwa kuchoma moto bendera ya Taifa ni sehemu ya uhuru wa kujieleza, ambao unalindwa na katiba. Mahakama kuu inasisitiza kuwa kauli tata, za kukera, au za kuwakosoa watawala ndizo hasa katiba ilikusudiwa kuzilinda.

Serikali ya Marekani inafahamu kuwa raia ana uhuru na haki kamili ya kuikosoa. Viongozi wa Marekani wanajua hilo. Ninaleta video hapa, inayomwonyesha mwananchi akimfokea kiongozi bila kumung'unya maneno. Mwone kiongozi huyu kutoka chama tawala cha Rais Donald Trump alivyonywea, wakati kipigo kinaendelea.

Thursday, May 11, 2017

Shukrani kwa Msomaji

Msomaji mwingine wa kitabu cha Africans and Americans; Embracing Cultural Differences amejitokeza na kuandika maoni yake kuhusu kitabu hiki. Ameandika maneno matatu tu, "Short and sweet," katika mtandao wa Goodreads, ambao ni maarufu miongoni mwa wasoma vitabu. Humo wanaweka maoni yao kuhusu vitabu walivyosoma au vitabu wanavyopangia kusoma.

Kama ilivyo kawaida yangu katika blogu hii, ninamshukuru kwa kujipatia kitabu hiki, kukisoma, na kuwajuza walimwengu maoni yake. Amefanya hivyo kwa hiari yake, akijua kwamba kauli yake itasomwa na watu wengi. Namshukuru kwa hisani yake; amenifanyia kazi bila malipo wala kutegemea shukrani.

Maoni ya wasomaji yana manufaa makubwa. Kwanza yananiwezesha kufahamu kama ninafikisha ujumbe wangu na unaeleweka vipi. Kila msomaji anapotoa maoni, hutaja jambo fulani au mambo fulani yaliyomgusa kwa namna ya pekee. Wasomaji wanaweza kuwa wamekipenda kitabu hicho hicho, lakini kwa misingi au namna mbali mbali.

Pili, kuwepo kwa maoni ya wasomaji kunaniondolea jukumu la kukiongelea kitabu changu, kwa watu wanaokiulizia. Badala ya mimi kuwaelezea, ninawaelekeza watu wakasome maoni hayo, ambayo wasomaji wameyatoa kwa hiari yao, bila msukumo wa aina nyingine.

Siku nne zilizopita, kwa mfano, m-Tanzania moja aishiye Marekani, aliniandikia ujumbe binafsi katika Facebook akinielezea kuwa anatakiwa kuongea na waalimu kutoka Marekani katika kuwaandaa kwa safari ya Tanzania. Hiyo ni programu baina yao na walimu wa Tanzania kuhusu tamaduni na ufundishaji. Alihitaji pendekezo la kitabu kuhusu tamaduni.

Nilimtajia kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, na baadaye nimemshauri kuwa ili ajiridhishe, aangalie maoni ya wasomaji kwenye mtandao wa Amazon na pia mtandao wa Goodreads. Kuna sehemu zingine pia ambapo maoni yamechapishwa, kama vile blogu, tovuti, na majarida.

Friday, May 5, 2017

Mwanahabari Amy Goodman Amehutubia Hapa Kwetu

Leo, mwanahabari na mwanaharakati maarufu Amy Goodman amehutubia chuoni Carleton hapa Northfield. Mada yake ilihusu "threats to freedom of the press and the importance of independent media," yaani mambo yanayotishia uhuru wa vyombo vya habari na umuhimu wa media zisizo chini ya mamlaka yoyote. Ninaamini tafsiri yangu inaweza kuboreshwa.

Amy Goodman ni maarufu kama mwendesha kipindi kiitwacho Democracy Now!, ambacho kinachambua masuala kwa mtazamo tofauti na ule wa watawala wakandamizi na propaganda zao za kurubuni watu na kuhalalisha hali iliyopo. Mtazamo wa Amy Goodman ni wa kichochezi kwa maslahi ya walalahoi, wavuja jasho, na wale wanaoonewa na kudhulumiwa. Ni mwana harakati ambaye hasiti kujitosa sehemu ambapo watu wanadhulumiwa ili kuwaunga mkono na kuwezesha sauti zao kusikika ulimwenguni.

Katika mhadhara wake wa leo, ameongelea zaidi hali ya Marekani, akiainisha madhaifu ya vyombo vya habari na media kwa ujumla. Alianza hotuba yake kwa kauli ya kusisimua na kufikirisha ya Thomas Jefferson, "were it left to me to decide whether we should have a government without newspapers or newspapers without a government, I should not hesitate a moment to prefer the latter," yaani "ingekuwa ni mamlaka yangu kuamua kama tuwe na serikali bila magazeti au magazeti bila serikali, nisingesita hata dakika moja kuchagua hilo la pili."

Baada ya hotuba yake, Amy alisaini nakala za kitabu chake, Democracy Now: Twenty Years of Covering the Movements Changing America. Wakati ananisainia, aliniuliza ninatoka wapi. Nilipomtajia Tanzania, alitabasamu, akasema "Julius Nyerere." Niliguswa, ingawa sikushangaa, kuwa Amy ni mmoja wa watu wa ughaibuni wanaomwenzi Mwalimu Nyerere. 

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...