Wednesday, December 31, 2014

Vitabu vya Kukumbukwa Nilivyosoma Mwaka 2014

Leo, siku ya mwisho ya mwaka 2014, napenda kujikumbusha vitabu nilivyosoma mwaka huu ambavyo nitavikumbuka kwa namna ya pekee. Sitavitaja vitabu tulivyovisoma darasani.

Kwanza, napenda kumshukuru Mungu kwa kuniwezesha kushuhudia mwaka 2014 ukiisha, huku zikiwa zimebaki saa nne tu hadi kuanza kwa mwaka 2015. Ingawa huu umekuwa mwaka mgumu kwangu kuliko miaka yote ya maisha yangu kwa sababu ya kuugua, nashukuru nimefikia hapa nilipo, kwa rehema ya Mwenyezi Mungu, huduma za madaktari, wauguzi na familia yangu, na maombi ya ndugu na marafiki.

Kutokana na hali yangu hiyo, sikuweza kusoma kama ilivyo mazoea yangu. Hata hivi, kila nilipojisikia nafuu, nilishika kitabu na kusoma, hata nilipokuwa nimelazwa hospitalini. Vitabu ni moja ya vitulizo vyangu, na madaktari na wauguzi walitambua jambo hilo.

Nilipokuwa nimelazwa katika hospitali ya Abbott Northwestern, mjini Minneapolis, nilikwenda na kitabu cha mashairi ya Robert Frost kiitwacho Robert Frost: Selected Poems, ambacho binti yangu Zawadi alikuwa amenipa, kama nilivyoelezea hapa. Nilijitahidi kusoma mashairi mengi yaliyomo. Kabla ya kitabu hiki, nilikuwa nimesoma mashairi machache ya Frost wakati wa ujana wangu, na kati ya mashairi hayo, moja ambalo nimelikumbuka daima ni "The Road Not Taken."

Ninafurahi kuwa nimepata fursa ya kusoma mashairi mengi ya Frost mwaka huu 2014, ingawaje, kwa ujumla, yanahitaji tafakari sana, na kama mtu ni mvivu, hatafika mbali katika kuyasoma. Hata hilo shairi la "The Road Not Taken" linatuacha njia panda.

Kwa sababu kama hizi nilizotoa hapa juu, nitamkumbuka Robert Frost kwa namna ya pekee kama mmojawapo wa waandishi niliowasoma mwaka 2014. Nimeweza kupanua upeo wangu wa kumfahamu mshairi huyu maarufu.

Kitabu kilichonigusa kwa namna ya pekee ni The Pearl, riwaya ya John Steinbeck, ambayo niliielezea hapa. Ni riwaya inayosomeka kirahisi na inavutia kama sumaku kwa mtiririko wa matukio yake na jinsi inavyoelezea  tabia za binadamu, kama vile upendo na wivu, wema na ubaya. Ni riwaya ambayo sitaweza kuisahau.

Nimepata fursa ya kujiongezea ufahamu wa Shakespeare kwa kusoma Macbeth, tamthilia yake mojawapo ambayo sikuwa nimeisoma. Niliiongelea tamthilia hii katika blogu hii. Sina matumaini ya kusoma tamthilia zote 37 za Shakespeare. Ni nani amezisoma zote? Hii ndio hali halisi katika ulimwengu wa fasihi. Hata usome saa nyingi kila siku na kwa miaka yote ya maisha yako, utakachokuwa umefanya ni kama kuchota maji ndoo moja katika bahari inayoendelea kujaa maji. Kuna waandishi wengi maarufu, wa zamani, wa siku hizi, na wanaochipuka muda wote.

Lakini, hii isiwe sababu ya kukata tamaa, bali changamoto ya kukufanya ujitahidi kuvuna kila uwezacho katika hazina hii isiyo na mwisho. Nami, tunapoingia katika mwaka mpya, nina viporo vya vitabu ambavyo nilianza kuvisoma na napangia kuendelea navyo katika huu mwaka mpya, na papo hapo, nina shauku kubwa ya kusoma vitabu vingi zaidi, kwa kuwa afya yangu inaendelea kuimarika.

Tuesday, December 30, 2014

Benki ya Mkombozi na Mabilioni Kubebwa Katika Viroba, Magunia, na Mifuko ya Rambo

CHANZO: MKOMBOZI COMMERCIAL BANK

Taarifa Kwa Umma Kuhusu Akaunti Ya VIP Engineering And Marketing Iliyopo Katika Benki Ya Biashara Ya Mkombozi

Taarifa hii inatolewa kwa umma kutokana na ripoti mbalimbali zilizotolewa na baadhi ya vyombo vya habari mitandao ya kijamii na taarifa iliyotolewa kwenye mjadala katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

  • Ufunguzi wa akaunti ya VIP engineering and Marketing (VIP)
Kampuni ya VIP engineering and Marketing ni kampuni ambayo imesajiliwa kwa mujibu wa sheria za Tanzania. Kampuni hii ilifungua akaunti katika benki ya biashara ya Mkombozi na hivyo kuwa moja kati ya wateja wa benki. Benki ilijiridhisha na ilizingatia taratibu zote za ufunguzi wa akaunti husika kwa kuzingatia sheria za nchi na kanuni zinazozitaka benki kupata nyaraka muhimu kutoka kwa mteja wakati wa ufunguzi wa akaunti hiyo. Nyaraka hizo ni pamoja na kuwepo kwa cheti cha usajili wa kampuni, kanuni za kampuni, idhinisho la kampuni kumruhusu moja kati ya wanahisa wake kuendesha akaunti pamoja na picha na hati ya kusafiria ya mhusika wa kuendesha akaunti hiyo.
2.0     Mauzo ya hisa za VIP
Kampuni ya VIP ilileta mkataba kwenye benki ya Mkombozi wa mauziano ya hisa za asilimia 30 baina ya VIP na kampuni ya Pan Africa Power Solutions (PAP) ambazo inamiliki katika kampuni ya IPTL. Mkataba huo ulisainiwa tarehe 19 Ogasti, 2013. Bei ya asilimia 30 ya hisa hizo ilikuwa ni dola za Marekani milioni 75. Katika kifungu namba 2.4 cha mkataba wao kinaelekeza fedha za mauzo ya hisa zilipwe kwenye akaunti ya VIP iliyopo benki ya Mkombozi. Mkataba huo wa mauziano ya hisa baina ya kampuni hizi mbili ulitambuliwa na hukumu ya Mahakama Kuu ya Tanzania iliyotolewa na Jaji J.H.K Utamwa tarehe 5 Septemba, 2013.


  • Mchakato wa kulipa kodi ya serikali
Benki ilitambua kwamba katika mauziano hayo ya hisa ni lazima kodi ya Serikali ilipwe na hivyo iliizishauri pande zote mbili kupeleka mkataba husika katika ofisi za Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ili kufanyiwa makadirio ya kodi husika. Tarehe 20 Januari, 2014 TRA iliiandikia barua kampuni ya VIP na nakala ya barua hiyo kuletwa kwenye benki ya Mkombozi. Katika barua hiyo TRA iliitaarifu kampuni ya VIP kuwa makadirio ya kodi yatokanayo na mauzo ya hisa ni shilingi 38,186,584,322.00 ikiwa ni kodi ya mauzo ya hisa ya asilimia 30 za mauzo ya hisa kutoka VIP kwenda kwa PAP.(Capital gains and stamp duty). TRA pia iliiagiza benki ya Mkombozi kuhakikisha kuwa inalipa kodi hiyo kwa niaba ya VIP mara tu fedha zitakapoingia kwenye akaunti yake.

Malipo ya kodi ya shilingi 38,186,584,322.00 yalilipwa TRA kwenye akaunti 11120100 iliyopo katika Benki Kuu ya Tanzania na TRA ilikiri kupokea kodi hiyo kwa barua yake yenye kumbukumbu namba 3-4/100/100/223/4 ya tarehe 24 Januari, 2014.

  • Ufafanuzi wa mambo mbalimbali
4.1      Benki ya mkombozi kuhusika katika kusafisha fedha chafu
Fedha zote zilizoingizwa kwenye akaunti ya VIP iliyopo kwenye benki ya Mkombozi zilitokana na mauziano ya hisa kati ya VIP na PAP kwa mkataba uliotambuliwa na Mahakama Kuu ya Tanzania. Chanzo cha malipo hayo ni kuhamisha fedha kutoka kwenye akaunti ya PAP iliyopo katika benki ya Stanbic na kuingizwa kwenye akaunti ya VIP iliyopo katika benki ya Mkombozi. Fedha hizo zilihamishwa katika mafungu mawili. Fungu la kwanza ilikuwa ni shilingi 73,573,500,000.00 zilihamishwa kwa njia ya TISS kwa kumbukumbu namba 000000050720 ya tarehe 23 Januari, 2014 na fungu la pili ni dola za Kimarekani 22,000,000.00 zilihamishwa kwa TISS kwa kumbukumbu namba 000000050812 ya tarehe 23 Januari, 2014. Malipo mengine ya asilimia kumi ya mauzo ya hisa yalilipwa kwenye akaunti ya Mkombozi iliyopo Benki Kuu ya Tanzania. Kutokana na mchakato huo benki ya Mkombozi ilijiridhisha kuwa fedha hizo ni malipo halali na siyo fedha chafu. Benki ya Mkombozi haijihusishi na utakasishaji wa fedha chafu na haramu katika uchumi wa Tanzania.



4.2      Malipo yatokanayo na akaunti ya VIP
Malipo toka kwenye akaunti ya mteja hufanywa kutokana na maelekezo ya mteja. Benki ikishajiridhisha kuwa fedha ya mteja ni halali na ipo kwa mujibu wa sheria na hamna zuio lolote toka katika mahakama hapa nchini hutekeleza malipo kwenye akaunti ya mteja kutokana na maelekezo yake. Benki ilijiridhisha kuwa malipo yote yaliyofanywa kutoka kwenye akaunti ya VIP ni halali kwa kuwa chanzo cha pesa hizo ilikuwa ni halali kutokana na mauzo ya hisa na ulipwaji wa kodi ya Serikali kama ilinyoelezwa hapo juu. Kutokana na sababu hiyo benki haikuwa na shaka juu ya malipo hayo.

4.3      Malipo taslimu kwa wateja na kubeba fedha kwenye viroba, mifuko ya rambo na magunia
Benki inatoa tamko kuwa malipo yote yaliyofanywa katika akaunti ya VIP yalilipwa kupitia akaunti za walipwaji. Hakuna fedha zilizolipwa taslimu kwa wateja na kubebwa kwenye viroba au magunia kama ilivyoripotiwa Bungeni. Pesa iliyotoka kwenye akaunti ya VIP tarehe 6 Februari, 2014 kiasi cha shilingi 3,314,850,000.00 ililipwa kwenye akaunti nane za wateja tofauti na siyo kubebwa kwenye viroba au magunia. Na zile zilizotoka toka benki ya Stanbic zilizotajwa hapo juu zilitumwa kwa njia ya TISS na siyo kubeba kwenye magunia au viroba.
4.4      Malipo kwa mfanyakazi wa benki ya Mkombozi
Gazeti la Mawio la tarehe 20-26, Novemba, 2014 tolea namba 0122 liliandika kuwa mwanasheria wa benki ya Mkombozi ajulikanaye kwa jina la Rweyengeza Alfred alipokea malipo toka akaunti ya VIP ya shilingi milioni 40.2. Benki inatoa tamko kuwa haina mfanyakazi anayetambuliwa kwa jina hilo na wala hakuna mfanyakazi yeyote wa benki aliyelipwa fedha toka kwenye akaunti ya VIP.
  • Wito kwa umma
Benki ya Mkombozi inachukua fursa hii kuwatarifu wateja wake na umma kutopotoshwa na taarifa au tuhumma zilizofafanuliwa hapo juu na kuwataka wateja wake wote kutokuwa na hofu yeyote kwani benki ipo imara na inafanya kazi kwa kufuata misingi ya sheria, taratibu na kanuni zilizowekwa na Benki Kuu ya Tanzania. Benki inawataarifu wateja wake na Watanzania kwa ujumla kutoyumbishwa na tuhumma hizo ambazo hazina ukweli ndani yake na badala yake waitumie benki yao kwa shughuli za maendeleo ya nchi yetu. Pamoja tunajenga nchi na uchumi wa nchi yetu.

  • Hitimisho
Benki ya biashara ya Mkombozi haijihusishi na haitajihusisha na utakasishaji wa fedha chafu.


Imetolewa na:

MKURUGENZI MTENDAJI BENKI YA BIASHARA YA MKOMBOZI

Sunday, December 28, 2014

"As You Like It:" Kitabu cha Kumalizia Mwaka

Nimeanza kusoma As You Like It, moja ya tamthilia za Shakespeare. Ni wazi kuwa, nikizingatia kwamba leo ni tarehe 28 Desemba, hiki kitakuwa kitabu cha kumalizia mwaka.

Kama zilivyo tamthilia zingine za Shakespeare, As You Like It ni hazina kubwa ya mafundisho kuhusu mahusiano baina ya wanadamu na kuhusu maisha kwa ujumla. Tamthilia yoyote ya gwiji huyu, sawa na mashairi yake, ni hazina ya lugha ya ki-Ingereza.

Ningefurahi kama ningekuwa nimesoma angalau kitabu kimoja kwa kila wiki. Padre Lambert Doerr, OSB, mwalimu wetu wa ki-ingereza tulipokuwa tunasoma seminari ya Likonde, ambaye sasa ni abate askofu mstaafu, alitushinikiza kusoma angalau kitabu kimoja kwa wiki. Kila mmoja wetu alipewa daftari ambamo alitakiwa kuorodhesha vitabu alivyosoma, na alitegemewa kuweza kutoa maelezo mafupi kuhusu kila kitabu. Ningefurahi kama ningeweza kuendeleza jadi hii miaka yote.

Nirudi tena kwenye As You Like It. Simulizi inapoanza, tunamsikia Orlando akilalamika kuwa amedhulumiwa na kaka yake mkubwa, Oliver, kuhusu urithi. Anasema kuwa baba yao aliacha wosia kwamba Oliver amgawie yeye Orlando fungu fulani la mali yake na pia amsomeshe, lakini Oliver hakufanya hvyo. Dhuluma hii inamsononesha Orlando.

Mtindo huu wa kuanzia simulizi na mhusika akielezea masononeko tunauona pia katika tamthilia ya Shakespeare iitwayo The Merchant of Venice. Halafu katika sehemu hii ya mwanzo ya As You Like It kuna pia dhamira ya kiongozi kuporwa madaraka na ndugu yake, dhamira ambayo inajitokeza pia katika The Tempest, tamthilia nyingine ya Shakespeare. Hili suala la Shakespeare kurejea tena na tena kwenye dhamira au kipengele fulani cha sanaa yake nimeligusia kabla katika blogu hii.

Tangu mwanzoni mwa As You Like It, Shakespeare anatuweka katika hamaki ya kujua nini kitakachofuata katika mtiririko wa matukio. Vile vile, kama ilivyo kawaida yake, anatupeleka mbali katika ulimwengu wa fasihi na masimulizi na imani za zamani, kuanzia enzi za wa-Griki hadi wa-Ingereza wenyewe. Mifano ya wahusika wa masimulizi hayo ni Fortune na Robin Hood.

Sijui kama nitaweza kumaliza kusoma tamthilia hii kabla ya mwaka mpya kuanza, lakini nitajitahidi. Jambo moja linalonifanya nisome pole pole ni kuvutiwa na umahiri wa Shakespeare katika kutumia lugha kwa namna ambayo aghalabu haionekani katika ki-Ingereza cha leo. Ni aina ya chemsha bongo.

Friday, December 26, 2014

Kitabu Changu Katika Jalada Gumu

Leo nimepata nakala ya kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences kikiwa katika jalada gumu ("hard cover"). Wiki iliyopita, kwa kutumia tekinolojia ya uchapishaji vitabu mtandaoni, niliuchapisha upya mswada wa kitabu changu, ili kitabu kipatikane pia katika jalada gumu. Nilipomaliza tu kuchapisha, niliagiza nakala, ambayo nimepata leo. Ni nakala ya kwanza kabisa, nami nimeridhika nayo.

Ni jambo la kawaida, huku ughaibuni, kwa kitabu kupatikana katika jalada jepesi ("paperback") na pia katika jalada gumu. Kuna vitabu vingine ambavyo hupatikana katika jalada jepesi tu, au katika jalada gumu tu.

Ninaamini, tangu zamani, ingawa sijafanya utafiti, kwamba maktaba ndizo zinazohitaji sana vitabu hivi vyenye jalada gumu, kwani vinaweza kuhimili vizuri zaidi misukosuko ya kuazimwa azimwa na wasomaji. Lakini kuna pia watu binafsi wanaopenda vitabu vya aina hiyo, hata kama nakala zenye jalada jepesi ziko pia.

Mimi mwenyewe nina vitabu vingi vyenye jalada gumu. Kila mtu ana sababu zake za kuvinunua vitabu vya aina hiyo. Kwa upande wangu, kisaikolojia, ninaviona vina hadhi ya pekee, mbali na kwamba vina nafasi ya kudumu zaidi katika hali nzuri.

Nimefurahi kuipata nakala hii ya kitabu changu wakati hali ya Krismasi bado iko hewani. Naona kama nimejipatia zawadi nyingine ya sikukuu. Kuanzia sasa, nitakuwa nachukua nakala hii popote nitakapokwenda kutoa mihadhara inayohusu au inayotokana na yale niliyoandika humo. Ni uamuzi wangu, hata kama hauna mantiki maalum. Ni binadamu gani anatafakari kwa makini kila kitu ambacho moyo wake unapenda?

Yeyote atakayehitaji nakala ya kitabu hiki anaweza kukipata kwenye stoo yangu ya mtandaoni. Nakala ya "kindle" inapatikana Amazon.com. Anayesita au asiyeweza kununua vitu mtandaoni awasiliane nami kwa barua pepe, africonexion@gmail.com au kwa simu, namba (507) 403-9756.

Wednesday, December 24, 2014

Maana ya Krismasi Inavyopotoshwa

Kimsingi, Krismasi ni siku ambayo sisi wa-Kristu tunakumbuka kwa namna ya pekee kuzaliwa kwa Yesu. Au labda niseme, ni siku ambayo wa-Kristu tunategemewa kukumbuka kwa namna ya pekee kuzaliwa kwa Yesu. Ni siku muhimu katika dini yetu, nasi tunategemewa kuwa tumejiandaa kiroho kwa kumpokea Yesu. Ni siku ambapo tunakumbushwa kuhusu utukufu wa Mungu, uokovu wetu, na amani duniani.

Wanataaluma tuna mazoea ya kutafiti mambo, na tunajua kuwa Krismasi ina historia ndefu, na sio vipengele vyake vyote vinatokana au kuhusiana na dini ya u-Kristu. Lakini ninachozingatia hapa ni kuwa, pamoja na hiyo historia ndefu, Krismasi kama tunavyoijua leo, ni siku takatifu, ya kukumbuka kuzaliwa kwa Yesu, siku ambayo wa-Kristu tunapaswa kuizingatia kwa misingi hiyo.

Lakini, kwa hali ilivyo, mtazamo huu wa kuiona Krismasi kama siku takatifu unazidi kupungua, na wengi wameshasau jambo hilo. Badala yake, maana ya Krismasi inapotoshwa. Badala ya kuzingatia kuwa maandalizi ya Krismasi ni ya kiroho, watu tunajiandaa kwa mambo ya kidunia.

Tunawazia kununua vitu kama vile nguo, viatu, na zawadi mbali mbali. Wafanyabiashara wanangojea kwa hamu kuuza bidhaa zao. Tunaingojea Krismasi kwa hamu ili tukasherehekee, na tunasherehekea hata kwa namna ambazo zinakiuka mafundisho ya dini.

Kila Krismasi, nalikumbuka shairi la Lawrence Ferlinghetti, liitwalo "Christ Climbed Down," ambalo nimelifahamu tangu mwaka 1991. Ni shairi ambalo linatufanya tuutafakari upotoshaji wa Krismasi:


Christ Climbed Down

Christ climbed down
from His bare Tree
this year
and ran away to where
there were no rootless
Christmas trees
hung with candycanes and
breakable stars

Christ climbed down
from His bare Tree
this year
and ran away to where
there were no gilded Christmas
trees
and no tinsel Christmas trees
and no tinfoil Christmas trees
and no pink plastic Christmas
trees
and no gold Christmas trees
and no black Christmas trees
and no powderblue Christmas trees
hung with electric candles
and encircled by tin electric
trains
and clever cornball relatives

Christ climbed down
from His bare Tree
this year
and ran away to where
no intrepid Bible salesmen
covered the territory
in two-tone cadillacs
and where no Sears Roebuck
creches
complete with plastic babe in
manger arrived by parcel post
the babe by special delivery
and where no televised Wise
Men
praised the Lord Calvert
Whiskey

Christ climbed down
from His bare Tree
this year and ran away to where
no fat handshaking stranger
in a red flannel suit
and a fake white beard
went around passing himself
off as some sort of North Pole
saint
crossing the desert to
Bethlehem
Pennsylvania
in a Volkswagen sled
drawn by rollicking Adirondack
reindeer
and German names
and bearing sacks of Humble
Gifts from Saks Fifth Avenue
for everybody’s imagined Christ
child

Christ climbed down
from His bare Tree
this year
and ran away to where
no Bing Crosby carollers
groaned of a tight Christmas
and where no Radio City
angels
iceskated wingless
thru a winter wonderland
into a jinglebell heaven
daily at 8:30
with Midnight Mass matinees

Christ climbed down
from His bare Tree
this year
and softly stole away into
some anonymous Mary’s womb
again
where in the darkest night
of everybody’s anonymous soul
He awaits again
an unimaginable
and impossibly
Immaculate Reconception
the very craziest of
Second Comings

Copyright 1958 by Lawrence Ferlinghetti

Monday, December 22, 2014

Mkutano na Wanachuo wa Gustavus Adolphus Unakaribia

Siku zinakwenda haraka. Tarehe 5 Januari, ambayo imekaribia, ndio siku nitakayokutana na wanachuo wa chuo cha Gustavus Adolphus, kama nilivyoandika hapa. Hao ni wanafunzi wanaojiandaa kwa safari ya Tanzania, kujiongezea elimu kuhusu masuala ya afya na matibabu katika mazingira tofauti na ya Marekani, hasa kwa upande wa utamaduni.

Profesa wao aliniomba nikaongee nao kuhusu masuala ya aina hiyo kwa mapana kufuatia yale niliyoandika katika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ambacho watakuwa wamekisoma kabla ya mimi kukutana nao.

Kutokana na kusoma hiki kitabu, wanachuo hao watakuwa wameandaa masuali. Kama ilivyotokea siku zilizopita, masuali mengine yatazuka hapo hapo.

Jukumu hili linanifanya nikipitie tena kitabu changu, angalau kijuujuu, kwani sina mazoea ya kusoma sana yale ambayo nimeshayaandika na kuyachapisha. Napendelea kutumia muda wangu na akili yangu katika kutafiti, kutafakari na kuandika mambo mapya. Ingawa yale yaliyomo kitabuni sijayabadili, na sijaona sababu ya kuyabadili, ninafahamu mengi zaidi na naendelea kujifunza, kwani elimu haina mwisho.

Kutokana na ukweli huu, mazungumzo yangu na hao wanachuo wa safari hii hayawezi kuwa sawa na yale ya miaka iliyopita. Hata kama kutakuwa na masuali yanayofanana na yale ambayo nimeshaulizwa kabla, majibu yangu yatajengeka katika upeo mpana zaidi. Fursa za aina hii zinachangia kupanua upeo huo.

Tutakutana, kama siku zilizopita, Mount Olivet Conference & Retreat Center, pembeni mwa mji wa Lakeville, Minnesota. Nangojea kwa hamu kuonana tena na Profesa Zust, na kuonana na hao wanachuo wapya. Panapo majaliwa, nitaweka ripoti katika blogu hii, kama nilivyozoea.

Sunday, December 21, 2014

Kitabu Kingine: "A Goal is a Dream With a Deadline"

Usiku wa kuamkia leo, nimemaliza kusoma kitabu kiitwacho A Goal is a Dream With a Deadline, ambacho nilikinunua siku za karibuni. Mwandishi wake, Leo B. Helzel, amekusanya kauli za watu mbali mbali wenye ujuzi na uzoefu, ili kuwaelimisha wajasiriamali, mameneja, na watu werevu kwa ujumla, wenye mitazamo ya kimaendeleo.

Kitabu hiki ni tofauti na vingine kwani ni mkusanyo wa misemo ya busara kuhusu mambo kama kujiwekea malengo, kustahimili matatizo, kutafuta masoko au wateja, kujiwekea maamuzi na kuyatekeleza kwa dhati na bila kuchelewa, kuwasikiliza wateja kwa makini na kuwahudumia vizuri, kuzingatia ubunifu, kupunguza urasimu, na kujiamini. Hayo ni baadhi ya yaliyomo katika kitabu hiki.

Sura zote za kitabu hiki zina mambo muhimu. Kwa vile mimi ninashughulika na kutoa ushauri kwa jumuia, taasisi, makampuni, na watu binafsi kuhusu tofauti za tamaduni na athari zake, nimevutiwa sana na sura ya kitabu hiki iitwayo "Going Global." Baadhi ya mawaidha yaliyomo katika sura hii ni haya: "Never assume that business is conducted in a foreign country just as it is at home" (uk. 146), "Learn about your host's people by reading about their history and culture" (uk. 147), " "Always assume that time will be handled differently in a foreign country" (uk. 147), "Latin Americans may refuse to do business with you if you are too serious. So lighten up and slow down" (uk. 151), "In Asia, learn when "maybe" really means "no" (uk. 151).

Mawaidha haya yanafanana na yale ninayotoa na kuyafafanua katika mihadhara na warsha zangu. Yamo katika kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, na pia mara moja moja katika blogu hii.

Nimejifunza mambo kadhaa muhimu katika kusoma A Goal is a Dream With a Deadline, na nakipendekeza kwa yeyote anayetaka mabadiliko yenye manufaa katika fikra, shughuli, maisha yake na ya jamii.

Thursday, December 18, 2014

Kitabu Sasa Kinapatikana Katika "Kindle"

Baada ya kujaribu jaribu, jana nimefanikiwa kukichapisha kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differeces katika "Kindle." Yeyote, sehemu mbali mbali za dunia, mwenye kifaa cha kuingizia na kusomea vitabu pepe anaweza kukipata mtandaoni, kwenye duka la Amazon Kindle.

Kwa miezi mingi nilikuwa nawazia kukiweka kitabu hicho katika Kindle, lakini sikujituma vya kutosha na kufanya kazi hiyo. Wiki hii, nilipania kuitekeleza, na nimefanikiwa. Katika kuhangaika kwangu, nimejifunza mambo ya ziada kuhusu tekinolojia hii, ambayo nilianza kujifunza kwa vitendo wakati nilipochapisha kitabu hiki hiki katika lulu.com.

Kuna sababu zilizonifanya niingie huko Kindle. Kwanza, ninafahamu kuwa kadiri tekinolojia inavyosonga mbele na kuenea, shughuli nyingi zinahamia mtandaoni, kuanzia elimu, biashara na mawasiliano ya aina mbali mbali. Nami najaribu kwenda na wakati.

Vile vile, ninalikumbuka tukio lililonitokea siku moja katika tamasha la vitabu la Twin Cities, mjini St. Paul, Minnesota. Kati ya watu waliofika kwenye meza yangu, alikuwepo bwana mmoja ambaye aliniuliza kama hiki kitabu cha Africans and Americans; Embracing Cultural Differences kinapatikana katika "Kindle." Nilipomwambia hakipatikani, alijibu kuwa yeye ni mtu anayesafiri mara kwa mara kwa ndege, na hataki udhia wa kubeba mzigo wa vitabu safarini. Anatumia vitabu pepe.

Kauli yake hii ilinigusa na kunifanya nijisikie vibaya. Tangu siku ile, kauli ile imekuwa changamoto kwangu, ikinikumbusha umuhimu wa kuwatimizia mahitaji wateja wa aina yake. Sasa, kwa kukichapisha kitabu katika Kindle, ninajisikia kama nimetua mzigo uliokuwa unanielemea moyoni.

Hata hivyo, Kindle sio mahali pekee mtandaoni ambapo huchapishwa vitabu pepe. Kwa mfano, kama nilivyogusia hapa juu, kitabu hiki hiki cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences nilikichapisha kwanza kule lulu.com. Kuna sehemu zingine pia, ambako mwandishi anaweza kuchapisha kitabu chake na wateja wakakipata huko. Kadiri siku zinavyopita, fursa zinaendelea kuongezeka.

Kwa kumalizia, napenda kusema kuwa mara kadhaa nimewahi kuelezea suala hili la kuchapisha vitabu mtandaoni. Mfano ni makala hii hapa na hii hapa. Vile vile, katika kitabu changu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii, nimeelezea suala hilo (kurasa 27-29), ili kuwagawia wengine yale ninayoyajua na ninayoendelea kujifunza. Ni jambo la kutia moyo kuwa kuna wa-Tanzania wenzangu ambao wanayasikiliza mawazo yangu, kama inavyodhihirika katika makala ya Ibrahim Yamola hii hapa.

Wednesday, December 17, 2014

Mwaliko Mwingine

Leo nimepata mwaliko mwingine wa kwenda kuzungumza na wanachuo wa chuo cha South Central ambao wanajiandaa kwa safari ya masomo Afrika Kusini. Mwaliko umetoka kwa mwalimu wao, Becky Djelland Davis. Hii ni mara pili yeye kunialika. Mara ya kwanza ilikuwa ni mwaka jana, naye baadaye aliandika kuhusu mazungumzo yale katika blogu yake.

Nami nimeguswa kwa namna alivyoniandikia leo:

I will be taking students to South Africa again in May. This coming semester, we will again be reading your book Africans and Americans. I hope that perhaps you can talk with my students again? They loved you last time!

Huu ni mwaliko wa tatu kwa siku za hivi karibuni, na yote inangojea utekelezaji katika miezi michache ijayo. Wa kwanza niliuelezea hapa, na wa pili hapa. Mialiko hii ninayopata sio jambo jepesi au la mteremko. Inahitaji tafakari katika kujiandaa ili nitoe mawazo na mitazamo ya kiwango kinachokidhi mahitaji ya hao wanaonialika, na bora zaidi ni kufanya vizuri kuliko wanavyotegemea.

Hiyo inawezekana kutokana na juhudi ya kutafiti na kutafakari mambo kwa kina na upeo mpana zaidi ya yale yaliyomo katika kitabu changu, ambacho ndicho kinachochea hii mialiko. Sijioni kama ni mtaalam, bali mtafutaji wa elimu.

Kwa kuhitimisha, sherti nikiri kuwa ninafurahi kuona kuwa watu walionialika kabla wanaendelea kufanya hivyo, nami siwezi kuwaangusha. Hii ndio habari moja muhimu ya leo, ambayo nimeona niiwekee kumbukumbu katika blogu yangu hii.

Saturday, December 13, 2014

Zawadi ya Vitabu

Nimeona picha hii hapa kushoto katika Mjengwablog. Maggid Mjengwa (kulia) anaonekana akikabidhi vitabu kwa mzee wa kijiji cha Mahango, Madibira, kwa ajili ya maktaba ya kijiji.

Nimeguswa na taarifa hii, kwani vitabu ni sehemu muhimu ya maisha yangu. Hii sio tu kwa kuwa mimi ni mwandishi na mwalimu, bali pia kwa kuwa nathamini sana kitendo cha kupeleka vitabu popote vinapohitajika.

Kwa mtazamo wangu, kitabu cha maana kina thamani isiyopimika. Nikipata fursa ya kuchagua kati ya kitabu cha aina hiyo na kreti ya bia, nitachagua kitabu, kwa furaha kabisa.

Mimi mwenyewe hupeleka vitabu Tanzania. Nimeshapeleka kwenye maktaba mbali mbali, zikiwemo za Mbinga, vyuo vikuu vya Dar es Salaam, Makumira, na Tumaini,  na pia kwa watu binafsi. Kuna wakati niliwahamasisha wanadiaspora wanachama wa jumuia ya mtandaoni ya Tanzanet wakachangia dola 500 kuendeleza jukumu hilo. Mbali na hilo, kila ninapokwenda Tanzania, kwa kadiri ya uwezo wangu, nabeba vitabu kwa madhumuni hayo.

Siandiki makala hii kwa kuwa tu nimeona hii taarifa katika Mjengwablog. Wazo la vitabu kama zawadi nimekuwa nalo kwa muda mrefu. Niliwahi kuongelea jambo hili katika blogu hii. Mimi mwenyewe hufurahi nikipewa kitabu, kama nilivyoandika hapa, na hapa.

Kama ambavyo ninasema mara kwa mara katika blogu hii, ninapenda kununua vitabu. Sio kwamba nina pesa sana, bali ni kutokana na kuviona vitabu kuwa ni muhimu zaidi ya mambo mengi ambayo wengine wanayathamini zaidi. Kwa mfano, kama wewe ni mnywaji wa bia, ukiachana na bia, utagundua kuwa kumbe hela unazo. Ninasema hivyo kutokana na uzoefu wangu.

Nikirudi tena kwenye hii taarifa ya Mjengwablog, napenda kusema kuwa ni jambo jema sana kuanzisha na kuboresha maktaba vijijini. Ingetakiwa katika nchi yetu tuwe na mwamko wa namna hiyo. Kuna wageni ambao wanajitahidi kupeleka huduma ya vitabu vijijini. Mifano ni shirika la TETEA na Friends of African Village Libraries. Ingetakiwa sisi wenye nchi yetu tuwe mstari wa mbele katika kutimiza majukumu hayo, badala ya kuwaachia au kuwaangalia tu wageni wakifanya hivyo.

Kwa miaka mingi kidogo, nimewazia kuanzisha maktaba kijijini kwangu, lakini bado sijafanya hivyo. Kitu kimoja kinachonisukuma ni kuona jinsi wanakijiji wanavyotumia muda wao mwingi kwenye kilabu cha pombe. Papo hapo, kuna shule kadhaa jirani na kijiji, zikiwemo shule za sekondari, ambazo zingefaidika na kuwepo kwa maktaba kijijini. Wazo hili sio lazima alitekeleze mtu mmoja. Ni wajibu kwetu wote tunaotambua umuhimu wa vitabu.

Thursday, December 11, 2014

Sitafundisha Mwezi Januari, 2015

Awali, kwa ratiba iliyopangwa, nilitarajiwa kufundisha mwezi Januari, kozi iitwayo "The Hero and the Trickster." Hiyo ni kozi ambayo nimefundisha karibu kila mwaka, mwezi Januari. Tuna utaratibu, katika chuo hiki cha St. Olaf kuwa na kozi za mwezi Januari ambazo zinaitwa "interim." Kozi yangu ya "Hemingway in East Africa" ambayo nilifundishia Tanzania, ilikuwa ya aina hiyo.

Pamoja na kwamba ilipangwa kwamba Januari ijayo nifundishe, hivi karibuni, viongozi wa chuo wameonelea nisifundishe bali nipumzike, ili niendelee kupona vizuri. Kwa hali yangu ilivyo, nina hakika ningeweza kufundisha, lakini uongozi wa chuo umeamua kunipa hii likizo ambayo sikuitegemea.

Ninashukuru sana. Ninaona ni mipango ya Mungu, kwani kwa miezi niliyokuwa na hali mbaya kiafya, hadi nikashidwa kufanya kazi nilizozizoea, nilikuwa katika majaribu makubwa. Kutoweza kufundisha, kufanya utafiti, kuandika au kurekebisha makala za kitaaluma ulikuwa ni mtihani mkubwa kisaikolojia.

Kwa bahati nzuri, imani ya dini, kwamba yote anayajua Mungu, na kwamba yeye ndiye mwenye uwezo wote, ilinifanya nisikate tamaa. Hata muuguzi mmoja katika hospitali ya Abbott Northwestern, kule Minneapolis, aliponiuliza inakuwaje kwamba ingawa nilikuwa nimelazwa siku nyingi, sikuonyesha dalili ya kulalamika, kusononeka au kukata tamaa, kama wagonjwa wengine wafanyavyo. Nilimjibu kwamba ninamtegemea Mungu, na sina sababu ya kulalamika, kusononeka wala kukata tamaa. Alivyokuwa ananiangalia usoni, aliona kuwa naongea kwa dhati.

Sasa, huu uamuzi wa viongozi wa chuo kwamba nisifundishe mwezi mzima ninauona kama ni neema ambayo Mungu ananishushia, baada ya kipindi kirefu cha majaribu. Nataka kumia muda ule kwa kujisomea vitabu na kuandika, mambo ambayo, sambamba na ufundishaji, yananiletea raha maishani.

Nimeona niandike ujumbe huu sio tu kwa lengo la kujiwekea kumbukumbu ya yale yanayojiri maishani mwangu, bali kujaribu kuwatia moyo wengine wanaopitia katika kipindi kigumu na majaribu maishani mwao.

Tuesday, December 9, 2014

Uhuru wa Tanganyika na Ukoloni Mamboleo

Siku hii ya leo, ambayo ni ya kumbukumbu ya siku ambapo Tanganyika ilijipatia Uhuru, nilitaka kuandika makala, "Uhuru wa Tanganyika na Ukoloni Mamboleo." Nilianzza kuandika, lakini nilijikuta naandika insha ndefu, sio makala fupi ambayo nadhani inatakiwa katika blogu. Kutokana na jambo hilo, nimeifuta ile makala na badala yake nimeandika kwa ufupi mambo yafuatavyo.

Uhuru tulipata tarehe 9 Desemba, 1961. Nilikuwa mwanafunzi wa darasa la tatu, na ninakumbuka msisimko, hata kule kijijini kwangu. Waalimu wetu, Charles Kinunda, John Pantaleon Mbonde, na Alois Turuka, walikuwa chanzo kikubwa cha ufahamu wetu wa mambo yaliyokuwa yanatokea.

Kati ya kumbukumbu ambazo haziwezi kutoweka akilini mwangu ni picha ya askari Alexander Nyirenda akiweka mwenge wa Uhuru juu ya Mlima Kilimanjaro. Sambamba na tukio hili la kihistoria ni hotuba ya Mwalimu Julius Nyerere, ambamo alisema:

Sisi tunataka kuwasha mwenge, na kuuweka juu ya Mlima Kilimanjaro, ili umulike hata nje ya mipaka yetu, ulete tumaini pale ambapo hakuna matumaini, upendo mahali palipo na chuki, na heshima palipojaa dharau.

Mwalimu Nyerere, alifanya kila juhudi kuliongoza na kulielimisha hili Taifa huru, akisema kuwa tunaingia katika mapambano na maadui watatu: ujinga, umaskini na maradhi. Miaka ilivyopita, alifafanua vizuri malengo mengine ya Taifa hili: kujenga jamii ya usawa kwa wote, isiyo na matabaka; jamii yenye kutoa fursa sawa kwa wote, katika nyanja mbali mbali, kama vile uchumi, elimu, na afya; kuhakikisha kila mtu anatimiza wajibu wa kufanya kazi, chini ya kauli mbiu ya "Uhuru na Kazi," kujenga Taifa linalojitambua, kujiheshimu, na kujitegemea, Taifa huru lisilofungamana na upande wowote katika mazingira yale ya "Cold War," Taifa lenye kukaribisha urafiki na nchi yoyote kwa msingi wa kuheshimiana, Taifa ambalo halitamruhusu rafiki kutuchanguia marafiki au maadui, na tuwe mstari wa mbele kuunga mkono harakati za ukombozi Afrika na sehemu zingine duniani.

Hayo ndio yalikuwa malengo muhimu, ambayo Mwalimu Nyerere aliyaelezea katika hotuba zake, makala na vitabu mbali mbali. Alikuwa akienda na wakati, akizingatia mahitaji ya Taifa yalivyokuwa yanajitokeza. Kwa msingi huu, baada ya "Azimio la Arusha," aliendelea kuandika maandishi mengine, kama vile "Mwongozo," "Siasa ni Kilimo," "Elimu ya Kujitegemea," na "Binadamu na Maendeleo."

Hayo yote, tangu enzi za harakati za Uhuru hadi miaka ya mwisho mwisho ya sabini na kitu, yalifanyika chini ya uongozi wa chama cha TANU. Mtazamo na mwelekeo wa TANU ulikuwa wa kuongoza mapinduzi, kufuatana na mazingira ya kihistoria: kwanza ilikuwa kuwaunganisha wa-Tanganyika na kuwaongoza katika kupigania Uhuru, halafu, kuongoza harakati za kujenga ujamaa na kujitegemea.

Mwalimu Nyerere alifahamu fika kwamba Uhuru haukuwa mwisho wa safari. Kulikuwa na haja ya kupambana na urithi wa ukoloni, yaani ukoloni mamboleo na kuleta uhuru wa kweli, unaodhihirishwa na hali ya kujitegemea chini ya uongozi bora.

Miaka ilivyopita, baada ya chama kipya cha CCM kushika hatamu, hali ilikuwa hiyo kwa kipindi cha mwanzo. Lakini, pole pole, mwelekeo huu wa kuwa daima katika harakati za mapinduzi, ulianza kubadilika. Chini ya sera za CCM, kama vile "Azimio la Zanzibar," nchi imeendelea kuzama zaidi na zaidi katika mfumo wa matabaka na ukoloni mamboleo. Kwa lugha rahisi, CCM ni mhujumu wa Mapinduzi.

Ndoto na mategemeo ya Uhuru yametekwa nyara. Pamoja na kwamba tunasherehekea Uhuru tuliojipatia mwaka 1961, tutambue, kama TANU ilivyotambua, kuwa ule haukuwa mwisho wa safari. Enzi za TANU, tulitegemea kuwa tutajenga nchi ambayo iko chini ya mamlaka ya wakulima na wafanyakazi. Lakini, kama nilivyosema hapa juu, tunazidi kuzama katika ukoloni mamboleo. Wakulima na wafanyakazi, pamoja na washiriki wao, bado wana jukumu la kuendeleza harakati za kutafuta Uhuru wa kweli.

Monday, December 8, 2014

Vitabu Nilivyonunua Juzi

Juzi, Jumamosi,  nilienda Minneapolis, kuhudhuria mkutano wa bodi ya Afrifest Foundation, ambayo mimi ni mwenyekiti wake. Wakati wa kurudi, nilipitia Apple Valley, nikaingia katika duka la Half Price Books, ambalo nimeliongelea mara kadhaa katika blogu hii.

Ingawa ilikuwa jioni sana,  watu walikuwa wengi humo dukani: watu wazima, vijana, na watoto. Nami nilijichanganya nao, nikaangalia angalia sehemu zenye vitabu vya fasihi. Nilinunua vitabu vinne, ambavyo nitavielezea leo.

Lakini kabla ya kuelezea vitabu hivi, napenda kujikumbusha kitu kimoja kilichonigusa, wakati nimesimama katika foleni ya kulipia vitabu. Mbele yangu walikuwepo baba na mama na watoto wadogo wawili wasichana. Walikuwa wameshaweka vitabu vyao kwenye kaunta ya kulipia, huku wakiwaelezea wale watoto jinsi watakavyowasomea vitabu. Kati ya vile vitabu kwenye kaunta, niliviona viwili vikubwa vikubwa vya Harry Potter. Muda wote wale watoto walikuwa na furaha na msisimko. Kwa mara nyingine tena, nilishuhudia jinsi wenzetu wanavyowalea watoto wao katika utamaduni wa kupenda kusoma vitabu.

Kitabu kimojawapo nilichonunua ni Much Ado About Nothing, ambayo ni tamthilia ya Shakespeare iliyohaririwa na Barbara A. Mowat na Paul Werstine. Wasomaaji wa Shakespeare wanajua kuwa tamthilia zake zimehaririwa na wahariri mbali mbali katika hii miaka 500 tangu kufariki kwake.

Tamthilia za Shakespeare, ambazo ni 37, hupatikana pia zikiwa zimekusanywa katika kitabu kimoja kikubwa sana. Ingawa ninazo nakala za kitabu hiki--nakala mbili hapa Marekani na nyingine Tanzania--huwa napenda, mara moja moja kununua hivi vitabu vya tamthilia moja moja, kwa vile ni rahisi kubeba katika mkoba na kwenda navyo popote.

Kitabu kingine nilichonunua ni The Pickwick Papers, kilichotungwa na Charles Dickens. Wengi wetu tuliosoma sekondari miaka ya sitini na kitu na sabini na kitu tunamkumbuka Dickens na riwaya zake, kama vile Oliver Twist na A Tale of Two Cities. Binafsi, nilimpenda sana Dickens, na nilisoma vitabu vyake kadhaa. Nimewahi kumwongelea Dickens katika blogu hii.

Kitabu cha tatu nilichonunua ni Hemingway on Hunting. Nimenunua toleo lililochapishwa na The Lyons Press, mwaka 2001. Kitabu hiki ni mkusanyo wa maandishi ya Ernest Hemingway yanayohusu uwindaji. Mhariri wake ni Sean Hemingway, mjukuu wa mwandishi mwenyewe. Pia kuna utangulizi mfupi ulioandikwa na Patrick Hemingway, mtoto pekee wa Ernest Hemingway aliyebaki. Sean amekusanya maandishi kutoka katika vitabu  kama vile Green Hills of Africa, For Whom the Bell Tolls, Across the River and into the Trees, na pia makala na barua mbali mbali alizochapisha Ernest Hemingway katika magazeti.

Ingawa mengi ya maandishi hayo ninayo, niliona ni vema kuwa na kitabu hiki ambacho kinahusu hili suala la uwindaji. Ningependa kusema pia kuna kitabu cha aina hiyo hiyo, ambacho ni mkusanyo wa maandishi ya Hemingway kuhusu uvuvi, na kingine kuhusu uandishi. Hemingway, katika falsafa na nadharia zake, aliongelea uhusiano baina ya  uandishi na uwindaji.

Kitabu cha nne nilichonunua ni Minaret, riwaya iliyotungwa na Leila Aboulela, ambaye alikulia Khartoum na anaishi Dubai na Aberdeen. Ni mwandishi maarufu, ambaye ameshajitwalia tuzo kadhaa kwa uandishi wake. Ingawa nimesikia habari zake kwa miaka kadhaa, sikuwahi kusoma kitabu chake hata kimoja. Leila Aboulela anajulikana kwa umahiri wake kisanaa, pia kwa jinsi anayowaelezea suala la wanawake katika u-Islam kwa mtazamo tofauti na ilivyozoeleka. Nina dukuduku ya kusoma Minaret, kwa kuanzia, na nitapenda pia kusoma riwaya zake zingine.

Saturday, December 6, 2014

Mapitio ya Kitabu

Kama mwandishi, huwa nina hamu ya kujua maoni ya wasomaji kuhusu vitabu vyangu. Nawashukuru kwa lolote wanalosema baada ya kusoma na kutafakari yaliyomo kitabuni. Kama kitabu kimewaridhisha au kuwafurahisha, nami nafurahi. Wakiona dosari wakazibainisha, nitawashukuru kwa kunielimisha.

Leo nimeona mtandaoni kuwa kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, kimefanyiwa mapitio katika "The Zumbro Current," jarida la kanisa la ki-Luteri la Zumbro, lililopo kusini mashariki mwa Minnesota, Marekani:

Book Review Africans and Americans: Embracing Cultural Differences

The Abner Haugen Library at Zumbro Lutheran Church has a copy of this extremely helpful book on cultural differences between Americans and Africans. It is written by Joseph L. Mbele, a Tanzanian scholar who currently is a professor of English at St. Olaf College. Anyone traveling to another country or continent would find this short book well worth reading. A few of the topics covered are: eye contact, personal space, gender issues, gifts, how “time flies, but not in Africa.” Both my wife Ann and I recommend this 98-page book.

-Duane Charles Hoven. "The Zumbro Current," Oktoba 2014, uk. 7.

Friday, December 5, 2014

Kitabu cha "Siasa Hapo Kale"

Ninasoma Siasa Hapo Kale, kitabu ambacho nilikifahamu na kukipenda tangu nilipokuwa nasoma shule ya msingi kule nyumbani kwangu Litembo, katika mkoa wa Ruvuma. Mtunzi wa kitabu hiki ni Lucius Mabasha Thonya. Kama sikosei, nilikuwa na nakala ya kitabu hiki miaka ile kijijini kwangu. Ingawa sijui kilienda wapi, mara moja moja nimekikumbuka, hasa kwa vile mimi ni mtafiti katika fasihi simulizi. Hilo ni jambo moja katika utangulizi wa makala ya leo.

Jambo jingine ni kuwa kwa miaka kadhaa, nimevutiwa na juhudi za Dada Yasinta katika kudumisha lugha ya ki-Ngoni kwa kuanzisha na kuendesha blogu ya Vangoni. Ingawa ki-Ngoni sio lugha yangu, ninaielewa kiasi fulani nikiisikia au kuisoma, kwa vile inakaribiana na lugha yangu ya ki-Matengo.

Katika kusoma blogu ya Vangoni, nilipata wazo la kumwambia Dada Yasinta kuhusu kitabu hiki cha Siasa Hapo Kale. Hatimaye, nilimpelekea ujumbe, nikijua kuwa atapenda kusikia habari zake, na ndivyo ilivyokuwa. Kupitia maktaba ya hapa chuoni ninapofundisha, nilikipata kwa kutumia utaratibu unaotumiwa na maktaba wa kuazimishana vitabu na machapisho mengine, utaratibu uitwao "interlibrary loan."

Nilifurahi kukipata. Nilitengeneza nakala nikampelekea Dada Yasinta, naye aliandika habari hiyo katika blogu yake.

Siasa Hapo Kale ni mkusanyiko wa methali za ki-Ngoni, ambazo mtunzi amezitungia hadithi za kuzielezea. Katika maelezo yake, amefanikiwa vizuri kutupa maana na matumizi ya methali hizi, kwa kutumia maisha na mahusiano ya wahusika katika hadithi hizo. Anahitimisha kila hadithi kwa kusisitiza ujumbe muhimu uliomo katika methali. Kwa maneno yake mtunzi mwenyewe:

Hadithi zilizomo kitabuni humu zimesimuliwa kwa njia ya kubuniwa tu kupatana na mambo yalivyoweza kutokea katika maisha ya watu wa zamani zile. Hadithi hizo zimebuniwa ili kuwaangalisha wasomaji katika matukio ya namna mbalimbali yalivyopata kutokea katika kabila la Wangoni wa wilaya ya Songea iliyopo kusini mwa Tanganyika iliyo karibu na ziwa Nyasa.

Methali hizi zinathibitisha busara za wahenga, yenye falsafa, maadili, na mafundisho muhimu ya maisha. Napenda kunukuu baadhi ya methali, na tafsiri zilizomo kitabuni: "Njala likoko, yikoma na mhavi" (Njaa ni adui, hata mchawi inaua). "Mbanga kufwata manji kwegihamba" (Fuata maji yanakokwenda). "Katumbi ka ngolyongo ikwela mwe ngolyongo" (Utando wa buibui akwea yeye mwenyewe tu). "Mheka pangende kumwoyo lwitimba lungi" (Yu mcheshi machoni moyoni kuna mengine). "Imekela kandumba ka ngemelelu" (Ajivunia dawa ya bahati).

Mwandishi alifanya kazi kubwa ya kufikiri katika kuzitunga hadithi zilizomo kitabuni. Vile vile, ameandika kwa ki-Swahili sanifu, kinachovutia. Kitabu hiki kilichapishwa mwaka 1960, nami nakumbuka kuwa waandishi maarufu kama Shaaban Robert walikuwa bado hai. Miaka ile ya zamani, shirika la uchapishaji la East African Literature Bureau lilikuwa makini katika kuangalia matumizi ya lugha, kabla ya kuchapisha kitabu.

Wednesday, December 3, 2014

Wazo la Kutafsiri Kitabu

Kwa wiki kadhaa, nimekuwa nikiwazia kutafsiri kitabu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii. Siku chache zilizopita, niliandika kuhusu kitabu hiki katika blogu hii.

Nawazia kuzirekebisha insha zilizomo, na kuchapisha kitabu cha ki-Ingereza. Kufanya hivyo kutakipa kitabu hadhira kubwa zaidi kuliko ile ya wajuao ki-Swahili. Nina hakika, kwa mfano, kuwa wa-Marekani watakitafuta na kukisoma. Kwa ujumla wasomaji wa vitabu vyangu ni wa-Marekani.

Ninaposhiriki matamasha hapa Marekani, watu kadha wa kadha huja kwenye meza yangu na kuangalia vitabu, kuvinunua, au tu kuongea nami. Wako wanaoniuliza kama nimechapisha kitabu kingine, kwani vile vilivyopo mezani, vya ki-Ingereza, wanavyo au wamevisoma. Kauli hizi hata binti zangu, ambao hushirikiana nami, wamezisikia tena na tena.

Kwa miaka kadhaa, sijachapisha kitabu kipya. Sababu kubwa ni kuwa kuandika kitabu huchukua muda. Yaweza kuwa miezi au miaka. Kwa mfano, ilichukua miaka 23 hivi kuandaa kitabu cha Matengo Folktales. Vile vile, muda mwingi natumia katika kufanya utafiti na kuandika makala. Kutafsiri kitabu cha CHANGAMOTO, ni njia moja ya wazi ya kupatikana hicho kitabu kingine.

Kutafsiri CHANGAMOTO sio jambo la haraka. Kuna kitabu kingine katika lugha ya ki-Ingereza ambacho nataka kumaliza kukiandika kabla ya kuanza kutafsiri CHANGAMOTO. Hata hivi, siwezi kusema kuwa ni lazima ningoje. Muda wote ninakuwa na kazi kadhaa ninazoandika, na huwa sio rahisi kujua ni ipi itamalizika kabla ya ipi. Wanadamu tumejaliwa uwezo wa kufanya shughuli nyingi kwa pamoja, "multitasking" kwa ki-Ingereza. Ninachoombea ni uzima na akili timamu.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...