Ninaamini, tangu zamani, ingawa sijafanya utafiti, kwamba maktaba ndizo zinazohitaji sana vitabu hivi vyenye jalada gumu, kwani vinaweza kuhimili vizuri zaidi misukosuko ya kuazimwa azimwa na wasomaji. Lakini kuna pia watu binafsi wanaopenda vitabu vya aina hiyo, hata kama nakala zenye jalada jepesi ziko pia.
Mimi mwenyewe nina vitabu vingi vyenye jalada gumu. Kila mtu ana sababu zake za kuvinunua vitabu vya aina hiyo. Kwa upande wangu, kisaikolojia, ninaviona vina hadhi ya pekee, mbali na kwamba vina nafasi ya kudumu zaidi katika hali nzuri.
Nimefurahi kuipata nakala hii ya kitabu changu wakati hali ya Krismasi bado iko hewani. Naona kama nimejipatia zawadi nyingine ya sikukuu. Kuanzia sasa, nitakuwa nachukua nakala hii popote nitakapokwenda kutoa mihadhara inayohusu au inayotokana na yale niliyoandika humo. Ni uamuzi wangu, hata kama hauna mantiki maalum. Ni binadamu gani anatafakari kwa makini kila kitu ambacho moyo wake unapenda?
Yeyote atakayehitaji nakala ya kitabu hiki anaweza kukipata kwenye stoo yangu ya mtandaoni. Nakala ya "kindle" inapatikana Amazon.com. Anayesita au asiyeweza kununua vitu mtandaoni awasiliane nami kwa barua pepe, africonexion@gmail.com au kwa simu, namba (507) 403-9756.
No comments:
Post a Comment