Sunday, November 30, 2014

Kuhusu "Macbeth"

Makala hii nilianza kuiandika mara tu baada ya kuanza kusoma Macbeth, tamthilia ya Shakespeare, ambayo niliitaja hapa na hapa. Jana usiku nimefika mwisho wake. Inafurahisha kujisomea namna hii, bila msukumo kutoka popote.

Hapa na pale katika Macbeth nimejikuta nikiyakumbuka maandishi mengine ya Shakespeare ambayo niliyasoma zamani, kama vile The Merchant of Venice, Othello, The Tempest, na Twelfth Night. Hii ni kwa sababu kuna mawazo ambayo yanajitokeza tena na tena katika maandishi ya Shakespeare. Wazo mojawapo ni kwamba dunia ni jukwaa ambapo sisi wanadamu ni waigizaji. Kuna misemo pia ambayo inajitokeza tena na tena.

Kwa mfano, nilivyosoma katika Macbeth kauli ya mchawi kuhusu meli kukumbwa na dhoruba (I, III, 25-26) nimekumbuka The Tempest. Nilivyokutana na usemi huu wa mfalme kwa kapteni shujaa: "So well thy words become thee as thy wounds; They smack of honor both," (I, II, 47-48) nimekumbuka hotuba ya Portia katika The Merchant of Venice, ambamo anaelezea thamani ya huruma.

Kati ya mambo anayosema kuhusu thamani ya huruma ni kwamba "It becomes the throned monarch better than his crown." Kwa tahadhari, niseme kuwa neno "becomes" anavyolitumia Shakespeare, lina maana tofauti kabisa na ile tunayoijua. Jambo hilo nilishaligundua katika kusoma tamthilia za Shakespeare.

Unaposoma Macbeth, sawa na kazi nyingi maarufu za fasihi, mahusiano ya namna hii hujitokeza, sio tu baina ya maandishi ya mwandishi mmoja, bali pia baina ya maandishi ya waandishi mbali mbali. Katika nadharia ya fasihi, mahusiano hayo huitwa "intertextuality" kwa ki-Ingereza.

Kufafanua zaidi wazo hili, napenda kusema kuwa jambo moja lililonistua katika Macbeth ni pale Fleance anaposema, "The moon is down; I have not heard the clock" (II, I, 2). Hapo nilikumbuka riwaya ya John Steinbeck, The Moon is Down, nikapata shauku ya kufuatilia kama kuna uhusiano. Lo, nimegundua kuwa Steinbeck alipata jina la riwaya yake hapo kwenye tamthilia ya Macbeth.

Ni wazi kuwa kusoma vitabu kunasisimua akili. Unaposoma masimulizi ya aina hii, ubongo unafanya kazi muda wote, kukumbuka hiki au kile, kuelewa kile unachosoma, na pia kubashiri kinachofuata katika mtiririko wa matukio.Kuelewa huko na kukumbuka vimefungamana. Akili hailali; inapata mazoezi, sawa na mazoezi ya viungo vyovyote vya mwili. Manufaa yake ni makubwa.

Ninavyosoma Macbeth, nakumbuka vizuri taarifa niliyosoma miaka kadhaa iliyopita kuhusu onesho la Macbeth lililofanywa Uingereza na kikundi cha waigizaji cha wa-Zulu. Niliisosoma makala hiyo, "The Zulu Macbeth," katika jarida la The New African, kama sikosei. Kuna ripoti kadhaa mtandaoni kuhusu onesho hilo la tamthilia ya Macbeth ya ki-Zulu, ambayo ilitungwa na Welcome Msomi na kupewa jina la "Umabatha." Kwa mfano, soma makala hii.

Ningeweza kuandika makala ndefu kuhusu Macbeth, nikijadili masuala kama dhamira, wahusika, mawaidha, falsafa, na umahiri wa Shakespeare katika kutumia lugha. Pamoja na mengine yote, Shakespeare ni mwanafalsafa anayefikirisha. Kwa mfano, tafakari kauli hii maarufu ya Macbeth mwenyewe, mhusika mkuu wa tamthilia hii, anapoambiwa kuwa mke wake amefariki:

She should have died hereafter;
There would have been a time for such a word.
Tomorrow, and tomorrow, and tomorrow
Creeps in this petty pace from day to day
To the last syllable of recorded time;
And all our yesterdays have lighted fools
The way to dusty death. Out, out, brief candle!
Life's but a walking shadow, a poor player,
That struts and frets his hour upon the stage
And then is heard no more. It is a tale
Told by an idiot, full of sound and fury,
Signifying nothing (V, V, 19-30).

Kwa kuhitimisha, napenda kusema kuwa nimefurahi sana kuisoma Macbeth hadi mwisho. Najisikia raha kuwa nimeongeza kitu cha thamani katika akili yangu. Ndivyo inavyokuwa katika kusoma vitabu vyenye thamani.

Thursday, November 27, 2014

Kitabu Changu cha Ki-Swahili

Kitu kimoja ninachojivunia kama mwandishi ni juhudi niliyofanya kwa miaka mingi katika kuandika kwa ki-Swahili. Aliyenihamasisha na kunisukumia katika uandishi wa ki-Swahili ni rafiki yangu Mugyabuso Mulokozi, ambaye sasa ni profesa mstaafu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Tangu tulipokuwa tunasoma wote "Mkwawa High School," aliona jinsi nilivyokuwa nimezama katika ki-Ingereza bila kujibidisha upande wa ki-Swahili.

Hatimaye, hasa tulipokuwa chuo kikuu, ambapo yeye nami tulikuwa tunafundisha, nilijitosa katika ulimwengu wa ki-Swahili. Kwanza nilisoma maandishi ya ki-Swahili, kisha nikaanza kufanya utafiti na kuandika makala magazetini. Kati ya maandishi niliyochapisha ni mapitio ya tamthilia ya Kijiji Chetu, iliyotungwa na Ngalimecha Ngahyoma.

Baadaye, nilianza utafiti kuhusu tungo za zamani za ki-Swahili, kama vile Utenzi wa Fumo Liongo, Al-Inkishafi na Utenzi wa Ras il Ghuli. Utafiti huu niliuendeleza nilipokuwa nasomea shahada ya uzamifu katika Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison, huku Marekani, miaka ya 1980-86.

Hatimaye, kwa kuombwa na Ndugu Maggid Mjengwa, mmiliki na mwendeshaji wa Mjengwablog, niliandika makala katika gazeti aliloanzisha, Kwanza Jamii. Baadaye, makala hizi nilizikusanya na kuzichapisha kama kitabu kiitwacho CHANGAMOTO: Insha za Jamii. Nilipochapisha kitabu hiki, niliandika taarifa katika blogu yangu ya ki-Ingereza.

Kuandika kwa ki-Swahili ni namna ya kuienzi lugha hii. Lugha ni utambulisho wa utaifa na ni kielelezo cha jinsi mtu unavyoheshimu utaifa wako na unavyojitambua na kujiheshimu wewe mwenyewe, kama alivyobainisha Frantz Fanon hasa katika vitabu vyake viwili: The Wretched of the Earth na Black Skin, White Masks.

Ninajivunia kitabu hiki kwa vile kimenipa fursa ya kupima uwezo wangu wa kuandika ki-Swahili sanifu. Ingawa bado naandika zaidi kwa ki-Ingereza, sijarudi nyuma katika uandishi wa ki-Swahili. Mbali na hili suala la kujitambua na kujitambulisha kwa kuienzi lugha yetu kwa vitendo, kitabu hiki kilitokana pia na msukumo wa watu waliokuwa wananiuliza kwa nini naandika kwa ki-Ingereza tu. Watu hao waliniambia kuwa ingekuwa bora niandike pia kwa ki-Swahili, ili wa-Tanzania walio wengi waweze kuyaelewa mawazo yangu. Nami niliona hii ni hoja nzuri.

Hata hivi, kitabu hiki hakijapata wasomaji wengi. Labda hii ni kwa sababu nilikichapisha huku Marekani, mtandaoni. Kama hili ndilo tatizo, napenda kusema kuwa kitabu hiki, sawa na vitabu vyangu vingine, kinapatikana kutoka kwangu, kwa anwani hii: africonexion@gmail.com au simu namba (507) 403 9756.

Lakini pia kuna suala la kukosekana kwa utamaduni wa kununua na kusoma vitabu miongoni mwa wa-Tanzania, jambo ambalo limekuwa likisemwa na wahusika mbali mbali katika sekta ya vitabu. Tungekuwa na utamaduni huu, tungeona tahakiki na mijadala kuhusu vitabu, sio tu miongoni mwa wanafunzi na wasomi, bali katika jamii, kupitia vyombo vya habari, magazeti, na mitandao ya mawasiliano.

Tuesday, November 25, 2014

Tuna Likizo Fupi ya "Thanksgiving"

Leo hapa chuoni tunaanza likizo fupi itakayokwisha mwisho wa wiki. Ni wakati wa sikukuu maarufu hapa Marekani iitwayyo "Thanksgiving." Kwa mwaka huu, "Thanksgiving" ni keshokutwa, tarehe 27.

Kwa upande wangu, nilianza hayo mapumziko jana mchana, baada ya kufanyisha mtihani katika somo langu la "South Asian Literature." Kwa hivi, kipindi hiki ambacho ni cha mapumziko sitapumzika, bali nitakuwa nasahihisha huo mtihani.

Vile vile, wakati huu ambapo hatufundishi, ninaendelea kujisomea maandishi mbali mbali, hasa tamthilia ya Macbeth. Ninangojea kwa hamu kuandika ripoti yake wiki hii hii katika blogu hii. Pamoja na jukumu la kusahihisha mtihani, naona akili yangu imetulia vizuri, kiasi cha kuniwezesha kuitafakari tamthilia ya Macbeth na kuifaidi vilivyo.

Nikirudi kwenye hii sikukuu ya "Thanksgiving," ningeweza kusema mengi kuhusu historia yake, pia malumbano na migogoro ya kiitikadi ambayo imeigubika sikukuu hii hasa miaka ya hivi karibuni.

Kifupi ni kuwa hii ni sikukuu ambayo ni kumbukumbu ya ujio wa wazungu katika nchi hii ya Marekani. Historia wanayoisimulia ni kuwa wale wazungu wa mwanzo waliwakuta wenyeji, tunaowaita Wahindi Wekundu, na hao wenyeji waliwakaribisha wageni hao, na ndio waliowawezesha hao wahamiaji kustawi katika mazingira ya nchi hii.

Kwa mujibu wa masimulizi hayo, hiyo "Thanksgiving" ni kumbukumbu na fursa ya kutoa shukrani. Batamzinga ndio chakula rasmi kwa siku hiyo, kiasi kwamba wa-Marekani wanapowazia sikukuu hii, wanaiunganisha moja kwa moja na mlo huo. Historia yake nayo ni ndefu.

Lakini, hasa miaka ya karibuni, wanaharakati wa hilo taifa la Wahindi Wekundu na wengine, wanaikosoa historia inayosimuliwa kuanzia katika vitabu vya watoto hadi katika media zingine, kwa msingi kuwa inapotosha ukweli kwamba wale wazungu waliingia nchi hii kwa mabavu, wakafanya maovu mengi dhidi ya wenyeji, yakiwemo mauaji na kupora ardhi. Wanaharakati wanaona hii sikukuu ya "Thanksgiving" kama ni tusi kwao. Wanaiona kama siku ya maombolezo.

Ni vema kwetu ambao hatukukulia nchi hii kujielimisha ili angalau tuelewe huu mgogoro wa kiitikadi. Tuelewe hisia za wenyeji wa asili wa nchi hii. Tusiwe watu wa kusherehekea tu, na kula batamzinga, kama wanavyosherehekea wengine hapa Marekani, bali angalau tufahamu utata wa suala zima la hii sikukuu.

Kwa upande mwingine, kila kabila au taifa hapa duniani lina wakati ambapo wanasherehekea na kutoa shukrani, hasa wakati wa mavuno. Dhana ya kutoa shukrani sio dhana ya Marekani pekee. Ingawa mimi si m-Marekani na hii si nchi yangu, ninaamini kuwa kinachotakiwa ni wao kutafuta njia za kutatua huu mgogoro wa kiitikadi niliouelezea.

Monday, November 24, 2014

Mwaliko wa Profesa Barbara Zust

Asubuhi hii, nimefika ofisini na kukuta ujumbe kutoka kwa Profesa Barbara Zust wa Chuo cha Gustavus Adolphus, Minnesota. Ananiulizia iwapo naweza kwenda kuongea na wanafunzi wake tarehe 4 au 5 Januari, katika matayarisho yao ya kwenda Tanzania kimasomo. Nimempigia simu, tukakubaliana niende tarehe 5.

Profesa Zust amenialika mara kwa mara anapoandaa wanafunzi wake kwa safari ya Tanzania. Nimewahi kuandika taarifa hizo, kwa mfano hapa, hapa, na hapa. Wanafunzi hao huwa wamesoma kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Mihadhara yangu huhusu masuala ninayoongelea kitabuni, nami hupenda sana kujibu au kujadili masuali wanayokuwa nayo.

Nimefurahi kwa jinsi Profesa Zust alivyonieleza umuhimu wa mikutano yangu na wanafunzi hao. Nimefurahi pia kuwa yeye na wanafunzi wanaona ninachofanya kina faida kubwa kwao. Ni wazi kuwa, ingekuwa hawafaidiki, hawangekuwa wananialika tena na tena.

Kwa hivi, siku yangu ya leo imeanza vizuri, nami nimeona niweke kumbukumbu hii hapa.

Nimekumbuka pia jinsi Profesa Zust na mwenzake Profesa Paula Swiggum, walivyoanza kunialika kuongelea kitabu changu kwa wanafunzi ambao wanasomea uuguzi ("nursinng"). Nilijiuliza inakuwaje mimi, ambaye sina utaalam wowote katika uwanja huu, niwe na lolote la kuwagawia wanafunzi wa somo hilo.

Katika kutafakari suala hilo, nilianza kusoma maandishi mbali mbali, nikagundua kuwa kwenye huu uwanja wa uuguzi wameingiza kipengele kiitwacho "transcultural nursing." Maana yake ni kwamba wanawafundisha wanafunzi kuhusu athari za tofauti za tamaduni katika kuwashughulikia wagonjwa.

Watu wa tamaduni tofauti wanauchukulia au wanauelewa ugonjwa, au uponaji, au wadhifa wa muuguzi, kwa misingi tofauti, kufuatana na utamaduni wao. Muuguzi akijua jambo hilo, anakuwa amejiandaa kuepuka kutoelewana na mgonjwa, na ana nafasi nzuri ya kutoa huduma muafaka kwa mgonjwa.

Katika kujisomea kuhusu mambo hayo ya "transcultural nursing," nimejifunza na ninaendelea kujifunza mengi, na papo hapo naelewa kwa nini watu kama Profesa Zust wanapenda niongee na wanafunzi wao. Nimeelewa vizuri kuwa kuna dhana nyingine ambayo inamwangalia mgonjwa katika mkabala mpana kuliko tu kile kinachomsumbua. Kuna uwezekano wa kuwepo masuala ya kisaikolojia na ya mahusiano katika jamii, ambayo ni muhimu katika kumwelewa na kumshughulikia mgonjwa. Kwa ki-Ingereza hii huitwa "holistic approach." Kwa kuzingatia hiyo dhana, nimeelewa zaidi kwa nini mambo kama yale niliyoandika kitabuni yanathaminiwa hata katika fani hii ya uuguzi.

Jana katika blogu hii, mdau Malifa Michael alniuliza kama nina mpango wa kutoa mwendelezo wa kitabu changu, nami katika kumjibu, niliongelea mambo kadhaa, likiwemo hilo la kutoa mihadhara itokanayo na kitabu, kwamba ni sehemu ya mwendelezo.

Namshukuru Mungu kwa kunipa fursa hizi za kuwaandaa vijana wanapoenda nchini kwetu, kutembelea sehemu mbali mbali, kujionea taasisi zinazohusika na masuala ya afya na matibabu, na kujumuika na wa-Tanzania katika utamaduni wetu.

Friday, November 21, 2014

Nilivyohojiwa na Radio Butiama Kuhusu Kitabu Changu

Nimewahi kuandika kuwa kama mwandishi, najikuta nikialikwa kuongelea maandishi yangu, na pengine kuongelea kitabu maalum. Hayo niliandika katika blogu hii

Wakati mwingine, mwandishi unaalikwa kwenye mahojiano katika vyombo vya habari. Nami nimewahi kuhojiwa katika redio, blogu, na magazeti.

Hapa naleta mahojiano niliyofanyiwa mwaka 2006 na m-Tanzania Deus Gunza, ambaye alikuwa anamiliki na kuendesha Radio Butiama, kule Columbus, Ohio. Mahojiano hayo ya papo kwa papo yalihusu kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Yasikilize mahojiano haya hapa:

http://butiama.podomatic.com/entry/2006-09-02T06_26_37-07_00

Thursday, November 20, 2014

Ninasoma Vitabu Kiholela

Jana, baada ya kufundisha darasa langu la South Asian Literature, nilikuwa ofisini kwa muda, nikawa napekuapekua bila lengo maalum katika makabati ya vitabu vyangu. Niliamua, kiholela tu, kuchukua tamthilia ya Macbeth ya Shakespeare, nikarudi nayo nyumbani na kuanza kuisoma.

Nilikuwa na hamu ya kujikumbusha enzi za ujana wangu, nilipokuwa nasoma sekondari hadi chuo kikuu. Nilipenda kusoma vitabu vya waandishi mbali mbali, kama vile Shakespeare na Charles Dickens.

Leo asubuhi, nilipoamka, niliendelea kusoma Macbeth, lakini nikakumbuka kuwa kuna vitabu kadhaa ambavyo nilianza kuvisoma au nilikuwa navisoma siku kadhaa zilizopita, au wiki kadhaa zilizopita, au miezi kadhaa iliyopita, ambavyo sikuvimaliza. Mifano ni A Moveable Feast na Islands in the Stream, vilivyoandikwa na Ernest Hemingway; Lost For Words, kilichoandikwa na J.W. Patrick Creber, na Nomad, kitabu cha Ayaan Hirsi, yule dada m-Somali anayetishiwa maisha yake kwa vile anaukosoa u-Islam. Hiyo ni mifano tu ya viporo.

Wakati kuna viporo, inatokea mara kwa mara kuwa naanza kusoma kitabu kingine kabisa na kukimaliza. Hivi ndivyo ilivyokuwa niliposoma The Pearl, kitabu cha John Steinbeck. Nilikiongelea kitabu hiki katika blogu hii, hapa na hapa. Nilikianza nikakimaliza, huku viporo kadhaa ninavyo.

Pamoja na yote hayo, jana nimekurupuka na kuanza kusoma Macbeth. Kwa hakika, nimepania kumaliza kuisoma tamthilia hii, ingawa nimeichagua kiholela tu. Hakuna uhakika kuwa kesho na keshokutwa sitaanza kusoma kitabu kingine tofauti kabisa. Kusema kweli, jana hiyo hiyo nilianza pia kusoma kitabu cha Postcolonial Criticism, kilichohaririwa na Bart Moore-Gilbert na wengine ambacho nilikinunua miaka kadhaa iliyopita, nikawa nimechunguliachungulia tu kurasa zake, bila kukisoma.

Leo nimejikuta nikitafakari tabia yangu hii kama msomaji. Siongelei vitabu ninavyofundisha darasani. Hivyo huwa navisoma kwa nidhamu, tangu ukurasa wa kwanza hadi wa mwisho, kama impasavyo mwalimu, na ninawaongoza wanafunzi katika kuvijadili. Hii tabia ya kusoma vitabu kiholela inahusu vitabu ambavyo ninajisomea mwenyewe, bila msukumo kutoka kokote. Najiuliza kama ni jambo jema kusoma vitabu kiholela.

Lakini, papo hapo, sioni ubaya wake. Wakati huja ambapo napata hamu ya kuendelea kusoma kitabu ambacho nilikiweka kando siku zilizopita. Ajabu ni kuwa, ninapoamua kuendelea kusoma kitabu ambacho nilikianza siku zilizopita nikakiweka kando, kumbukumbu hunijia kuhusu yale niliyosoma kabla.

Naamini kila msomaji wa vitabu ana tabia yake katika usomaji. Nimeona nitafakari tabia yangu na kuieleza kama nilivyofanya. Labda hii itawapa wasomaji wengine fursa ya kujitafakari pia.

Tuesday, November 18, 2014

Naulizwa Malipo ya Mihadhara Yangu

Hapa Marekani, mtu unapoalikwa kwenda kutoa mhadhara, nawe ukakubali, huwa unaulizwa malipo yako ni kiasi gani. Hapo unawatajia kiwango cha malipo unayotegemea. Unazingatia umaarufu wako, na wale wanaokualika wanategemea uwatajie kiwango chako bila maneno zaidi. Hata siku chache zilizopita, nilipoletewa mwaliko wa kwenda kutoa mhadhara mjini Zumbrota, niliulizwa malipo yangu ni kiasi gani.

Miaka yapata mitano iliyopita, kwa nyakati tofauti, nilipata wasaa wa kuongea na wa-Marekani wawili wenye wadhifa katika jamii kuhusu suala hili. Tulikuwa katika mazungumzo kuhusu shughuli zangu za uandishi na utoaji mihadhara katika jumuia na taasisi mbali mbali. Ndipo wakaja na hili wazo la malipo. Ingawa waliongea nami kwa nyakati tofauti, wote walisema kuwa kufuatana na umaarufu niliokuwa nao wakati ule, nilikuwa na haki ya kutegemea kiasi cha dola 2,500 au 3,000 kwa mhadhara.

Kwangu, huu umekuwa ni mtihani miaka yote. Sijaweza kutaja hata siku moja nilipwe kiasi gani. Ukiniuliza sababu zangu, unaweza kushangaa au kunionea huruma. Imekuwa ni kawaida yangu, ninapoulizwa malipo yangu ni kiasi gani, kusema kuwa suala hili nawaachia wanaonialika. Waamue wenyewe wana uwezo gani, nami sitakuwa na tatizo.

Imekuwa hivyo miaka yote. Sibagui wenye pesa na wasio na pesa, au wenye pesa nyingi na wenye pesa kidogo. Nikialikwa kutoa mhadhara, ninakwenda, ili mradi mhadhara hauingiliani na ratiba yangu ya masomo.

Kuna vikundi ambavyo vina hela kidogo tu, au havina. Kwangu hiki si kipingamizi. Ninazingatia kuwa uwezo nilio nao umetoka kwa Mungu, na nina wajibu wa kuutumia kwa faida ya wanadamu. Wako ambao wana uwezo wa kunilipa, tena vizuri kabisa, lakini sijawa tayari kuwaweka kando wale ambao hawana hela za kunilipa. au wale wenye uwezo mdogo. Ninapokea chochote ambacho wameamua kipo katika uwezo wao. Na kama hawana uwezo, nawaambia kabisa kuwa hiki kwangu sio kizuizi.

Wa-Marekani wananishangaa kwa msimamo huo, kwani hauendani na utamaduni waliouzoea. Lakini mimi nafuata  dhamiri yangu. Kama watu wengine wengi, nina mahitaji makubwa ya fedha. Wale wanaoishi Marekani wanajua kuwa hii ni nchi ya madeni kila upande, na hayamaliziki. Hasa wakati huu, ambao nimekuwa katika matibabu kwa miezi mingi, pesa hazishikiki, na pamoja na kuwa na bima nzuri, madeni ni mpaka shingoni.

Lakini hayo yote hayajanifanya nibadili msimamo wangu kuhusu malipo ya mihadhara yangu. Ningekuwa nataja angalau hizo dola 2,500 au 3,000 kwa kila mhadhara, ningekuwa sina madeni, na labda ningeanza kuwa tajiri.

Roho yangu haiko huko.Nawashangaa mafisadi waroho wanaokwapua mabilioni ya hela za nchi yetu, wakati wananchi wana dhiki zisizosemeka, kama vile hospitali zisizo na vifaa na madawa, na madaktari na wahudumu wanateseka kwa kutolipwa wanavyostahili. Nawashangaa mafisadi hao kwa jinsi walivyo waroho wa pesa, na wasivyo na huruma, wakati watoto wengi mashuleni hawana viti wala madawati, wala vitabu, na mazingira ya walimu yanasikitisha.

Hapo juu nimeongelea malipo halali, ambayo naambiwa ningeweza kuyataja kwa wale wanaonialika. Lakini bado roho yangu inasita. Lazima niwashangae mafisadi, ambao hawachukui malipo halali, bali wanaliibia Taifa bila huruma.

Nimewazia kwa miezi mingi kuandika ujumbe huu, lakini sikujua niuandikeje. Leo nimeamua kuandika. Labda kuna wadau wenye ushauri wa kunipa.

Sunday, November 16, 2014

Mwandishi Unapoitwa Kuongelea Kitabu Chako

Siku hizi, mara kwa mara, nawazia jukumu linaloningoja, la kwenda mjini Zumbrota, Minnesota, kutoa mhadhara. Mada ni "Incorporating Immigrants into our Culture and Worship," kama nilivyoeleza katika blogu hii. Mwaliko wa kutoa mhadhara huu umetokana na kitabu nilichoandika, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Sikualikwa nikaongelee kitabu hiki, lakini kwa hali yoyote, baadhi ya yaliyomo kitabuni yatajitokeza katika mhadhara na katika kipindi cha majibu na masuali. Napenda kusema machache kuhusu jukumu la kutoa mhadhara kuhusu kitabu ulichoandika.

Mara nyingi, hutokea kwamba watu utakaozungumza nao wanakuwa wameshakisoma kitabu. Ni lazima utafakari kabla kwamba utaongelea nini, na jambo hilo hutegemea aina ya kitabu.

Kama ni riwaya, watu hutegemea utawaeleza mambo kama vile nini kilikuwa chanzo cha wewe kuandika, yaani nini kilichokufanya uandike, njia uliyopitia katika kuandika, maandishi au waandishi waliokuathiri, matatizo uliyokumbana nayo, na mambo uliyojifunza.

Lakini, watu hutegemea pia, au labda zaidi, kuwa utasoma angalau kurasa kadhaa za riwaya yako, ili wasikie sauti yako na sauti ya wahusika katika hadithi yako kwa mujibu wako wewe kama mtunzi.

Hapa kushoto tunamwona mwandishi Nuruddin Farah wa Somalia, alipokuwa anaongelea riwaya yake mpya ya Crossbones, chuoni Carleton. Anaonekana akisoma kurasa kadhaa.

Wasikilizaji huvutiwa kumsikia mwandishi namna hiyo, kwani usomaji wake ni aina ya tafsiri sio tu ya kile alichoandika, bali kilichokuwa mawazoni mwake wakati anaandika. Watu huamini kuwa usomaji wa mwandishi una ukweli na uhalisi ambao msomaji mwingine hawezi kuufikia.


Hiyo ndiyo halisi inavyokuwa, iwapo kitabu ni riwaya au mashairi. Sauti na usomaji wa mwandishi vina mvuto huo niliouelezea, ingawaje kwa kifupi.

Lakini kuna pia vitabu vya aina tofauti, kama hiki changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Unapokuwa umealikwa kuongelea kitabu cha aina hiyo, ni lazima utafakari vizuri suala zima.

Iwapo watu hao wameshakisoma, nadhani jukumu lako sio kuwasomea kurasa za kitabu, bali ni kuongelea mambo yatokanayo na yale uliyoandika. Jukumu lako ni kufafanua baadhi ya yale uliyoandika, ambayo unaamini yanakidhi mahitaji ya watu watu wale, kufuatana na mwaliko wao.

Pengine, inawezekana uzungumze bila kufungua kitabu, ingawa unacho mbele yako. Kwa mfano, kwenye hii mada ya mhadhara wangu wa Zumbrota, siamini kama nitahitaji kuwasomea kurasa zozote kutoka kitabuni. Badala yake, ikibidi, nitajumlisha mafundisho yatokanayo, yenye kukidhi mategemeo ya mada.

Aina hii ya mhadhara nimeshatoa mara nyingi. Kwa mfano, hapa kushoto ninaonekana nikiongea na wanachuo waliokuwa wanajiandaa kwenda Afrika Kusini kwenye ziara ya kimasomo. Walishasoma kitabu changu, na profesa wao aliniita kuja kuongelea masuala ya aina niliyozungumzia kitabuni, kama sehemu ya maandilizi ya safari ya wanafunzi wale. Kwa vile wanafunzi walikuwa wameshasoma kitabu, mhadhara huu ulitawaliwa zaidi na masuali na majibu. Profesa wao aliandika kuhusu mhadhara wangu katika blogu yake.

Kwa ujumla, fursa hizi hunifurahisha, sio tu kwa sababu nakutana na wasomaji na wadau wengine ana kwa ana, bali pia napata wasaa wa kujipima ni kiasi gani naifahamu mada husika na vipengele vyake.

Friday, November 14, 2014

Kuhusu Kunyanyaswa kwa Jaji Warioba

Kati ya mambo yaliyonishtua sana mwaka huu ni kunyanyaswa kwa Jaji Warioba. Kadhia hii imetokana na kazi murua aliyofanya Jaji Warioba na tume yake ya kukusanya mawazo ya wananchi kuhusu Katiba Mpya.

Kumekuwa na mlolongo wa matukio kadhaa ya unyanyasaji huo, ambao, kwa kadiri ninavyofahamu, mwanzilishi wake ni Ikulu. Tukio la kupigwa Jaji Warioba mkutanoni, ambalo limeripotiwa sana, ni kilele cha utovu huu. Wengi tunaamini kuwa Jaji Warioba ananyanyaswa kwa sababu ya uwazi na uwakilishi wa mawazo ya wananchi, jambo ambalo ni mwiba kwa mafisadi.

Nimeshtushwa vile vile na kauli ya Rais Kikwete kuhusu tukio hili la vurugu na kupigwa Jaji Warioba. Kwa mujibu wa taarifa za vyombo vya habari, Rais Kikwete aliishia tu kusema kuwa anaomba yasimkute yaliyomkuta Jaji Warioba. Sikuona popote kama aliongelea suala hili kwa undani na mapana kama linavyostahili.

Yeye kama Rais, nilitegemea kwanza atambue kuwa vurugu zile ni aibu kwa nchi anayoiongoza. Nilitegemea awakemee walioleta vurugu zile zilizohusisha pia kunyanyaswa kwa Jaji Warioba.

Nilitegemea Rais Kikwete atumie fursa ile kuwakumbusha wa-Tanzania, wajibu wao wa kuheshimiana na kulumbana kwa hoja, sio kwa mabavu. Angefanya hivyo, nigesema Rais ameonyesha busara za kiuongozi. Nilitegemea angekemea utovu wa ustaarabu uliojitokeza. Angewakumbusha wa-Tanzania njia ya usataarabu. badala ya yeye kujiwazia yeye binafsi, kwamba anaomba yasimpate. Je, kauli yake hii si sawa na kumezea uovu? Kauli yake haikuonyesha busara za kiuongozi.

Halafu, kuna pia kauli ya Samuel Sitta, ambayo nayo imenikera. Sitta aliripotiwa akisema kuwa Jaji Warioba alijitakia yaliyomkuta. Niliposoma taarifa hii, sikuamini kama mzee Sitta, anayetegemewa ana busara, angeweza kuwa na msimamo kama huo.

Nasikia Sitta ni msomi. Nami najiuliza: ni msomi gani ambaye hatambui wala kutetea mijadala au malumbano ya hoja. Kusema kuwa Jaji Warioba alijitakia yaliyompata ni sawa na kumezea suala la mjadala kuingiliwa na vurugu ambazo hazikubaliki katika mijadala. Kauli ya Sitta ni kama inahalalisha ukosefu wa ustaarabu unaotegemewa hasa kwa wasomi.

Sijui Sitta alikulia wapi na katika maadili gani. Sisi wengine tulilelewa katika maadili ya kuwaheshimu wazee. Kitendo cha kumpiga mzee, kwa mujibu wa maadili yale, ni mwiko kabisa. Kama hukubaliani na mzee, unapaswa kutafuta namna ya kujieleza, ambayo ni ya heshima kabisa. Nilitegemea Sitta atambue na kuzingatia hilo. Atoe mfano kwa watoto na vijana.

Tena na tena, katika jamii yetu, tumezoea kukemea tabia tunazoziiita haziendani na maadili au utamaduni wetu. Nimeshangaa kuona kuwa Sitta, ambaye ni mzee, anayetegemewa kuwa mlinzi na mtetezi wa maadili bora, haonekani kutambua kuwa Jaji Warioba kama mzee, hawezi kuletewa vurugu kama alizoletewa. Nimekerwa kabisa na kauli ya Sitta na kauli ya Rais..



Sunday, November 9, 2014

Nimealikwa Kutoa Mhadhara

Siku chache zilizopita, nilipigiwa simu kutoka Faribault, kwenye Kanisa la First English Lutheran Church. Wananiuliza iwapo nitaweza kwenda kutoa mhadhara katika Cannon River Conferenc utakaofanyika mwezi Aprili mjini Zumbrota, Minnesota.

Mada ya mkutano itakuwa "Incorporating Immigrants Into our Culture and Worship," na mhadhara wangu unatarajiwa kuwa dira ya mkutano.

Miaka kama sita hivi iliyopita, nilialikwa First English Lutheran Church, Faribault, kutoa mihadhara kuhusu yale niliyoandika katika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Nimefurahi kuwa mihadhara yangu ile inakumbukwa, tena mama aliyenipigia simu alinikumbusha kuwa anaikumbuka baadhi ya michapo yangu na pia kitabu changu. Hata hivi, kwenye mkutano kama huu wa Zumbrota, mada sio niliyoandika katika kitabu changu, ingawaje nitakitumia kama msingi mojawapo wa kuijadili mada niliyopewa. Patakuwepo pia na muda wa masuali na majibu. 

Huu mkutano wa Zumbrota utawaleta pamoja wanajumuia kutoka makanisa ya eneo hili la Minnesota ya Mashariki Kusini. Hapa Marekani, makanisa yako mstari wa mbele katika kuwapokea na kuwahudumia wakimbizi kutoka nchi mbali mbali.

Kwenye mji wa Faribault wenyewe, kwa mfano, makanisa ya kiLuteri na Katoliki yamekuwa yakifanya shughuli hiyo tangu pale wakimbizi na wahamiaji walipoanza kuja, kutoka sehemu kama Amerika ya Kati, Somalia, na Sudan. Hawana ubaguzi, iwe ni kwa msingi wa taifa, dini, au jinsia.

Nami, moja ya shughuli zangu katika mfumo huo imekuwa kuwasaidia wenyeji na wakimbizi na wahamiaji kuzitambua na kuzitafakari tofauti za tamaduni zao. Kuna ugumu kwa wageni kuelewa mambo ya Marekani, na kwa wa-Marekani kuna ugumu kuelewa mambo ya hao wageni. Msimamo wangu, kwenye mikutano ya aina hii, daima umekuwa kwamba sote tunawajibika kufanya juhudi kujielimisha. Hatuwezi kuuachia upande moja tu uwajibike. Wengi hawajazoea kusikia wazo kama hili.

Ninawaenzi hao waumini wa-Marekani  wanavyojitahidi kutatua tatizo hilo kwa namna yoyote iwezekananyo. Mikutano kama huu wa Aprili ni mfano mojawapo, kutoa changamoto ya kuwawezesha kuzitambua na kuzitafakari tofauti za tamaduni, kwa lengo la kuleta maelewano bali pia kuwezesha masuala kama hili suala la ibada za pamoja.

Nililazwa Tena Hospitalini

Kwa siku kadhaa, sikuandika chochote katika blogu zangu: hii na ile ya ki-Ingereza. Inapokuwa hali ni hiyo, wasomaji hujiuliza kuna nini.

Nilikuwa nimelazwa tena, kwa wiki moja, katika hospitali ya Allina Abbott Northwestern, kule Minneapolis.

Baada ya kuachiwa, nimekuwa nikipumzika. Kesho nategemea kuanza tena kufundisha. Chuo ambacho ni mwajiri wangu, kwa maelekezo ya daktari, kimenipunguzia sana majukumu, kuliko hata nilipoachiwa kutoka hospitalini miezi kadhaa iliyopita.

Nitakuwa nafundisha kozi moja tu, "South Asian Literature."

Mungu ni mkubwa na madaktari wanajua wanachofanya. Wananiambia kuwa hatimaye, hata kama ni baada ya miezi kadhaa, wana imani watayatatua matatizo ya afya yangu. Baada ya kurekebisha  matatizo mengine, sasa wanashughulikia figo. Wamenihimiza niendelee kufundisha, wakati wao wanashughulikia matatizo hayo.

Kama kawaida, nawashukuru wote wanaonikumbuka katika maombi na salaam. Nimeona nilete taarifa hii, kuelezea hali yangu, na kwa kuzingatia ukimya uliokuwepo kwa mwezi na siku kadhaa katika blogu zangu.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...