Monday, October 31, 2016

Black African Voices: Tungo za Afrika

Pamoja na kwamba fasihi ya Afrika, kama ilivyo ulimwenguni kote, inastawi kwa kasi kadiri miaka inavyopita, na waandishi wapya hujijokeza na kujipambanua, ni lazima pia kukumbuka na kusoma uandishi wa zamani. Kwa yeyote anayependa fasihi, awe ni mwanafunzi, mwalimu au msomaji wa kawaida, usomaji wa aina hii ni jambo lisilohitaji mjadala. Fasihi inahitaji usomaji usio na kikomo, sio tu kwa kuwa ina historia ndefu, bali pia kwa kuwa inastawi ulimwenguni kote na daima inaendelea kuchanua kama maua.

Mimi, mwalimu wa fasihi, ninazingatia umuhimu wa kufundisha kazi za tangu zamani hadi leo. Fasihi ya kila taifa au sehemu yoyote ya dunia ina historia, na fasihi inayoandikwa leo ni mwendelezo wa mkondo ulioanza zamani.

Katika siku hizi chache, nimekuwa ninasoma Black African Voices, kitabu kilichohaririwa na James E. Miller na wenzake. Sikumbuki ni lini nilikinunua kitabu hiki, lakini mara kwa mara katika kuangalia vitabu vyangu, nilikuwa ninakichungulia kitabu hiki, nikawa ninakumbuka kwa furaha enzi za ujana wangu, kuanzia miaka ya sitini na kitu, nilipokuwa ninasoma badhi ya tungo zilizomo. Kuna hadithi kadhaa na nyimbo za fasihi simulizi, mashairi, hadithi fupi na maandishi mengine ya waandishi mbali mbali.

Baadhi ya waandishi ambao tungo zao zimo katika kitabu hiki ni Ezekiel Mphahlele, Raphael Armatoe, Peter Abrahams, Birago Diop, David Diop, Cyprian Ekwensi, Richard Rive, Wole Soyinka, John Pepper Clark, James D. Rubadiri, na Grace Ogot. Ni furaha isiyoelezeka kuzisoma tena hadithi zilizonisisimua tangu miaka ile ya sitini na kitu, nilipokuwa mwanafunzi katika seminari ya Likonde, 1967-70 na Mkwawa High School, 1971-72.

Baadhi ya hadithi hizo ni "No Room at Solitaire," ya Richard Rive; "The Dignity of Begging," ya Bloke Modisane, "The Rain Came," ya Grace Ogot. Baadhi ya mashairi yaliyonisisimua miaka ile ni "Stanley Meets Mutesa" (James D. Rubadiri), "Africa" na "Listen Comrades" (David Diop), na "Prayer to Masks" (Leopold Sedar Senghor). Kuna pia tamthilia ya Edufa ya Efua Sutherland.

Katika Black African Voices kuna pia tungo za waandishi ambao sikuwafahamu miaka ile ya ujana wangu, kama vile J, Benibengor Blay (Ghana), Tshakatumba (Congo), Rui Nogar (Mozambique). Siwezi kuwataja waandishi wote ambao kazi zao zimo katika kitabu hiki, bali ninapenda tu kusisitiza kuwa ninaguswa sana na uandishi huu wa kuanzia miaka ya kabla ya kuzaliwa kwangu hadi ujana wangu. Wahariri walifanya kazi nzuri kuzikusanya tungo hizi katika kitabu kimoja.

Wednesday, October 26, 2016

Miaka 80 ya "The Snows of Kilimanjaro"

Kwa mara nyingine tena, ninaandika ujumbe kuhusu kutimia kwa miaka 80 tangu hadithi ya Ernest Hemingway, 'The Snows of Kilimanjaro" ilipochapishwa kwa mara ya kwanza. Niliandika ujumbe wa aina hiyo katika blogu hii. Leo nimesoma tena ujumbe wangu, nikajiridhisha kwamba niliyosema ndiyo ninayoamini hadi sasa.

Jambo moja kubwa kabisa ni kuwa wa-Tanzania tunajipotezea fursa za wazi za kutumia hazina kama hii hadithi ya Hemingway kuitangaza nchi yetu. Niliandika katika ujumbe wangu baadhi ya mambo ambayo tungeyafanya mwaka huu wa kumbukumbu. Lakini mwaka unaelekea ukingoni, na hakuna tulichofanya. Hii ni hasara ya kukosa utamaduni wa kusoma vitabu. Tunashindwa hata kutumia fursa zilizo wazi.

Nimeona niandike ujumbe huu leo kwa sababu wiki hii, hapa katika Chuo cha St. Olaf ninapofundisha, litatokea jambo la pekee linalohusiana na Ernest Hemingway. Keshokutwa, tarehe 28, pataonyeshwa kwa mara ya kwanza filamu ya "Papa's Shadow," ambayo niliwahi kuielezea katika blogu hii.

Hiyo ni filamu iliyotokana na kozi niliyofundisha Tanzania mwaka 2013 iitwayo Hemingway in East Africa. Nilisafiri na wanafunzi 29 wa Chuo cha St. Olaf, tukazunguka maeneo kadhaa ya Tanzania kaskazini, ambamo alipita Ernest Hemingway mwaka 1933-34. Katika safari hiyo, tulikuwa tunasoma maandishi ya Hemingway kuhusu maeneo hayo na maeneo mengine ambayo alipitia mwaka 1953-54.

Maandishi hayo ni pamoja na Green Hills of Africa na Under Kilimanjaro, ambavyo ni vitabu, kadhalika hadithi fupi mbili: "The Short Happy Life of Francis Macomber" na "The Snows of Kilimanjaro." Pia aliandika makala katika magazeti na barua nyingi akielezea aliyoyaona na kufanya katika safari zake. Kwa ujumla wake, maandishi haya ya Ernest Hemingway yanaitangaza nchi yetu na Afrika Mashariki kwa ujumla kwa namna ambayo sisi wenyewe hatujaweza kujitangaza.

Hiyo filamu ya "Papa's Shadow" inawasilisha vizuri mambo muhimu ya uhusiano wa Ernest Hemingway na Afrika Mashariki. Sehemu kubwa ya filamu hii ni mazungumzo baina yangu na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee aliyebaki wa Ernest Hemingway. Tunajadili kwa kina na mapana fikra za Ernest Hemingway kuhusu Afrika, uandishi, na maisha kwa ujumla.

Kwa kuwa hiyo filamu inaonyesha sehemu mbali mbali za Tanzania na maelezo kuhusu mambo yanayoifanya Tanzania kivutio kwa watalii, kama vile Mlima Kilimanjaro, na kwa kuwa filamu hii imejengeka katika maandishi ya Ernest Hemingway, mwandishi maarufu sana ulimwenguni, ni wazi kuwa filamu hii itakuwa chachu ya kuitangaza Tanzania kwa namna ya pekee. Taarifa zaidi Kuhusu "Papa's Shadow," zinapatikana kwenye tovuti ya Ramble Pictures.

Monday, October 24, 2016

Ninarekebisha Kitabu Nilichochapisha Mtandaoni

Mara kwa mara, ninaongelea suala la kuchapisha vitabu mtandaoni, kutokana na uzoefu wangu. Ninatarajia kuwapa wengine uzoefu wangu wa kutumia tekinolojia za uchapishaji mtandaoni, ambazo zinatoa fursa tele kwa yeyote kujikomboa na taabu na vikwazo vya uchapishaji wa jadi.

Faida mojawapo ya uchapishaji wa aina ninayotumia kuchapishia vitabu vyangu ni fursa isiyo na mipaka ya kurekebisha kitabu chako wakati wowote uonapo dosari ndani yake au fursa ya kukiboresha. Hilo linawezekana kwa kuwa mswada wako unakuwa umehifadhiwa kama faili la kielektroniki mtandaoni, hata kama hukuuhifadhi katika kompyuta, disketi, au kifaa kingine.

Mimi ninatumia mtandao wa lulu.com. Hapo, ukishachapisha kitabu, nakala ya mswada inahifadhiwa hapo hapo mtandaoni. Unapotaka kurekebisha kitabu chako, unachofanya ni kuuingiza "(down-loading") mswada katika "flash drive" na kuufanyia marekebisho. Kisha unaurudisha ("up-loading") sehemu ya kuchapishia. Yeyote atakayekinunua baada ya hapo atakuwa ananunua kitabu kilichoboreshwa.

Hatua zote hizi zinafanyika bila mtu yeyote kutambua kinachotokea, bali wewe mhusika tu. Na wakati wote, unaporekebisha mswada, kitabu hakitoweki hapo mtandaoni. Kinakuwa kama kilivyokuwa mwanzo, na yeyote anaweza kukinunua, wakati wewe unaendelea na marekebisho. Unapomaliza marekebisho na kukiingiza tena mtandaoni ("up-loading"), ndipo kitabu kilichoboreshwa kinachukua nafasi ya kile cha awali.

Sasa hivi, niko katika kurekebisha kitabu changu, Notes on Okot p'Bitek's Song of Lawino. Hakuna anayetambua kuwa kinafanyiwa marekebisho, kwani kinaonekana hapo mtandaoni kama kawaida. Nitakapomaliza marekebisho na kukichapisha tena, itakuwa kama vile hakuna lililotokea.

Urahisi huu wa kurekebisha kitabu hauko katika uchapishaji wa jadi, ambapo inabidi kungoja hadi wakati wa kutoa toleo jipya la kitabu. Aghalabu, wachapishaji huwa hawana uwezo wa kifedha wa kutoa toleo jipya. Nakala zikiisha, huwa ndio mwisho wa kuchapishwa kitabu.

Lakini tatizo hili haliko katika uchapishaji wa mtandaoni kama huu ninaotumia. Kitabu hakiwezi kutoweka, yaani kuwa "out of print," labda mtu uamue kukiondoa wewe mwenyewe hapo mtandaoni. Ukibadili mawazo ukataka kukirudisha tena ulimwenguni, ni hiari yako kufanya hivyo, wakati wowote. 

Sunday, October 23, 2016

Siku ya Mashujaa wa Kenya, Rochester, Minnesota

Jana nilikwenda mjini Rochester, Minnesota, kuhudhuria sherehe ya siku ya Mashujaa wa Kenya. Hii ni sikukuu ambayo wa-Kenya huifanya kila mwaka tarehe 20 Oktoba, kuwakumbuka mashujaa wa tangu enzi za kupigania uhuru hadi leo. Sherehe ya jana iliandaliwa na jumuia ya wa-Kenya waishio Rochester.

Nilipata taarifa ya sikukuu hii kutoka kwa Olivia Njogu, m-Kenya aishiye Rochester, na mwanabodi wa Rochester International Association. Anaonekana pichani hapa kushoto, wa pili kutoka kulia. Chama hiki huandaa tamasha la kimataifa kila mwaka, na Olivia tulifahamiana niliposhiriki tamasha hilo mwaka huu, kama nilivyoelezea katika blogu hii. Baada ya tamasha, Olivia alisoma kitabu changu Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, na kisha akaniandikia kunielezea alivyokipenda. Taarifa hiyo niliiandika katika blogu hii.

 .


Hii haikuwa mara yangu ya kwanza kuhudhuria sherehe za wa-Kenya hapa Marekani. Daima nimependezwa kujumuika nao, kama nilivyowahi kuandika katika blogu yangu ya ki-Ingereza. Hali ilikuwa hivyo hivyo jana. Nilivyokuwa ninapaki gari kwenye eneo la sherehe, walikuja wa-Kenya kadhaa kunipokea, ingawa hatukuwa tunafahamiana. Tulitambulishana na hima tukazama katika maongezi ya dhati na michapo.













Hii ilikuwa ni sherehe iliyojumuisha watoto vijana na watu wazima. Pamoja na maongezi yasiyo kikomo, vicheko na chereko, kulikuwa na vyakula tele na muziki. Nilivutiwa kwa namna ya pekee na muziki wa Kenya, nikakumbuka safari zangu za Kenya kuanzia mwaka 1989, za utafiti juu ya tungo za zamani na utamaduni wa wa-Swahili.














Picha hapa kushoto ni ushahidi wa hali ya furaha iliyotawala.






























Wengi waliohudhurua sherehe ya jana sikuwa nimefahamiana nao kabla, ingawa wachache walinikumbuka kwa kuwa waliniona katika tamasha la kimataifa la Rochester la mwaka huu.

Sherehe hii haikuwa ya wa-Kenya pekee. Ingawa sikuweza kuongea na kila mtu, nilipata fursa ya kuongea na watu wawili wa mataifa mengine: mmoja kutoka Nigeria na mwingine kutoka Uganda.




Katika kuishi kwangu hapa Minnesota, nimeweza kufahamiana na wa-Afrika wengi waishio Minneapolis, St. Paul, na maeneo ya jirani. Sasa ninafurahi kuweza kujenga mtandao wa aina hiyo maeneo ya Rochester.

Wanadiaspora wa Afrika tuna wajibu wa kujenga mshikamano miongoni mwetu, kama msingi wa ushirikiano katika bara letu. Waliotutangulia huku ughaibuni, kama akina Peter Abrahams, Jomo Kenyatta, na Kwame Nkrumah walifanya hivyo. Kwangu kama mwandishi na mwalimu, hizi zote ni fursa za kielimu. Darasa ni popote, kama nilivyowahi kuandika katika blogu hii.


Wednesday, October 19, 2016

Nimepata Vitabu Vipya vya Uislam

Leo nimepata vitabu kadhaa vya u-Islam kutoka kwa profesa Nadia Mohamed wa Minneapolis Community and Technical College. Huyu profesa, mzaliwa wa Misri, tulifahamiana mwaka jana. Muhula uliopita nilimwalika kutoa mhadhara katika darasa langu, Muslim Women Writers. Nilimwalika tena, na amekuja leo.


Katika vitabu alivyonipa leo, kuna nakala za Quran, yaani tafsiri tofauti. Kabla, nilikuwa na tafsiri mbili: moja ya Abdallah Yusuf Ali, yenye maelezo ya kina, ambayo nimekuwa nayo kwa miaka mingi, na ya pili aliyonipa Profesa Nadia Mohamed alipotembelea darasa langu muhula uliopita, kama nilivyoripoti katika blogu hii.

Lakini leo, amenipa The Message of the Quran, iliyotafsiriwa na kufafanuliwa na Muhammad Asad. Humo kuna Quran kwa hati ya ki-Arabu, na hicho ki-Arabu kipo pia kwa hati ya ki-Rumi. Na kuna tafsiri ya ki-Ingereza, pamoja na maelezo ya kina. Nakala ya Abdallah Yusuf Ali ina sura mbili: hati ya ki-Arabu na tafsiri ya ki-Ingereza.

Profesa Nadia Mohammed amenipa nakala zingine mbili za Quran, tafsiri ya Abdallah Yusuf Ali, ila ni tofauti na ile niliyokuwa nayo tangu zamani, kwa kuwa hii ni tafsiri tu bila yale maelezo. Hizi nakala ni vitabu vidogo kwa ukubwa, na kwa hivi ni rahisi kubebwa popote. Zinaonekana pichani hapa kushoto, zikiwa na majalada tofauti.

Kuna uzuri wa kuwa na tafsiri mbali mbali za Quran. Tunaambiwa kwamba ki-Arabu cha Quran ni cha pekee, sio rahisi kukitafsiri kwa lugha yoyote. Maneno yake mengi yana utajiri wa maana na ladha ambao ni mtihani mkavu kwa yeyote anayejaribu kutafsiri. Kutokana na ukweli huo, ambao unahusika pia katika tafsiri ya lugha yoyote, ni bora kusoma tafsiri mbali mbali. Nilimwambia hivyo Profesa Nadia Mohamed, ambaye ni mtaalamu, akaafiki.

















Vitabu vingine alivyonipa ni viwili vidogo vidogo. Kimoja kinaitwa A Brief Illustrated Guide to Understanding Islam na mtunzi ni I.A. Ibrahim. Cha pili ni Wisdom for Life & The Afterlife: A Selection of Prophet Muhammad's Sayings, ambacho ni mkusanyiko wa mafundisho ya Mtume Muhammad, yaliyotafsiriwa na Samir Saikali kwa ki-Ingereza, kutoka ki-Arabu, na kuchapishwa na Islamic Literacy Project.




Friday, October 14, 2016

Mwalimu Nyerere Aliiogopa CCM

Ingawa alikuwa mwanzilishi wa CCM, kwa nia njema ya kuendeleza mapinduzi katika nchi yetu, miaka ilivyozidi kwenda Mwalimu Nyerere alishuhudia jinsi CCM ilivyobadilika na kuwa mzigo kwake na pia tishio kwa usalama wa Taifa.


Mwaka 1993 Mwalimu alichapisha kitabu kiitwacho Uongozi Wetu na Hatima ya Tanzania (Harare: Zimbabwe Publishing House, 1993). Pamoja na mambo mengine katika kitabu hiki, Mwalimu alisema kuwa kuna kansa katika uongozi wa CCM. Nanukuu baadhi ya maneno yake:

Chama cha Mapinduzi, kwa sababu ya uzito wa historia yake, hadhi ya jina lake, mfumo wa wavu wake, mazoea ya watu, na ubovu wa Vyama vya Upinzani, kinaweza kuchaguliwa na Watanzania, pamoja na kansa ya uongozi wake. Au watu wanaweza wakachoka, wakasema, "potelea mbali:" wakachagua Chama cho chote, ilimradi tu watokane na kansa ya uongozi wa CCM. Hainifurahishi kuyasema haya, lakini uhai wa Nchi yetu unataka yasemwe
. (Ukurasa 61)

Mwalimu hakuishia hapo, bali aliongezea namna hii:

Nilisema awali kwamba kansa ya uongozi ndani ya Chama cha Mapinduzi isingekuwa ni jambo la kutisha sana kama tungekuwa tumeanza kuona Chama kizuri cha upinzani kinachoweza kuiongoza Nchi yetu badala ya CCM. Ubovu wa uongozi ndani ya CCM ndio uliofanya nikapendekeza tuanzishe mfumo wa Vyama Vingi. Nilitumaini kuwa tunaweza kupata Chama kingine kizuri ambacho kingeweza kuiongoza Nchi yetu badala ya CCM; au ambacho kingekilazimisha Chama cha Mapinduzi kusafisha uongozi wake, kwa kuhofia kuwa bila kufanya hivyo kitashindwa katika uchaguzi ujao. Lakini bado sijakiona Chama makini cha upinzani; na wala dalili zo zote za kuondoa kansa ya uongozi ndani ya CCM. Bila upinzani mzuri wa nje, na bila demokrasia halisi ndani ya Chama cha Mapinduzi, Chama hiki kitazidi kudidimia chini ya uzito wa uongozi mbovu. Kwa hali yetu ya kisiasa ilivyo nchini hili si jambo la kutarajia bila hofu na wasi wasi
! (Ukurasa 66)

Ni wa-Tanzania wangapi wenye utamaduni wa kusoma vitabu? Ni wangapi wanaosoma vitabu vya Mwalimu Nyerere? Ni wazi kuwa umbumbumbu miongoni mwa wa-Tanzania ni neema kwa CCM.

(CHANZO: Blogu ya Hapakwetu)

Monday, October 10, 2016

Ki-Ingereza Kama Lugha ya Ulimwengu

Jana, katika blogu hii, nilikiongelea kitabu cha Charles Derber, People Before Profit, ambacho kinahusu utandawazi. Katika kukisoma kitabu hiki, nilivutiwa na maelezo yake, na nikapata hamasa ya kufuatilia mada ya utandawazi kwa namna nyingine.

Nilikumbuka kwamba nina kitabu cha David Crystal, English as a Global Language, ambacho nilikinunua miaks michache iliyopita, ila nilikuwa nimekipitia juu juu tu. Leo nimeamua kukisoma, na ninaona jinsi maelezo yake kuhusu lugha ya ki-Ingereza yanavyofungamana na suala la utandawazi. Kwa mfano, katika utangulizi wake, mwandishi anasema,

"We have as yet no adequate typology of the remarkable range of language contact situations which have emerged as a consequence of globalization, either physically (e.g. through population movement and economic development or virtually (e.g. through Internet communication and satellite broadcasting)." (xi)

Kitu kimoja kilichonifanya nikumbuke kitabu cha David Crystal ni kuwa huyu ni mtaalam maarufu ulimwenguni wa masuala ya lugha. Nilipokuwa mwanafunzi katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kuanzia mwaka 1973, nikisomea "Literature" na "English," ndipo niliposoma maandishi ya Crystal, sambamba na mabingwa wengine, kama vile Frank R. Palmer, John Lyons, Noam Chomsky, Sydney Greenbaum, na Randolph Quirk. Kumbukumbu hiyo ndiyo ilinifanya ninunue kitabu cha Crystal, English as a Global Language miaka michache iliyopita. Sasa, kwa kuwa ninafuatilia suala la utandawazi, ninaona nilifanya vizuri kununua kitabu hiki.

Pamoja na kuelezea jinsi ki-Ingereza kilivyofanikiwa kuenea duniani na kinavyoendelea kuiteka dunia kama lugha ya mawasiliano ulimwenguni iliyo muhimu kuliko zote, Crystal anabainisha pia kuwa hatuwezi kuwa na uhakika kama hali hii itaendelea hivi siku za usoni. Kama nilivyoeleza katika ujumbe wa jana, nikinukuu kitabu cha People Before Profit, utandawazi hausambai bila upinzani kutoka katika jamii na tamaduni mbali mbali zinazotaka kulinda jadi na misingi yao.

Ni hivi hivi katika kuenea kwa ki-Ingereza. Crystal anatuelekeza kwenye kitabu cha Tom McArthur, The English Language, na anatumabia kuwa McArthur

"adopted a more synchronic perspective, moving away from a monolithic concept of English. His primary focus was on the kinds of variation encountered in the language as a consequence of its global spread. He suggested that English was undergoing a process of radical change which would eventually lead to fragmentation into a 'family of languages.'" (x)

Hilo wazo la ki-Ingereza kugawanyika katika vilugha mbali mbali linasisimua akili. Lakini, hata kama ki-Ingereza kitaishia kuwa vilugha vingi, ninategemea kuwa bado kutakuwa na misingi itakayodumu katika vi-Ingereza hivyo na kuendelea kuwawezesha watumiaji kuwasiliana na kuelewana. Hata wakati huu, tayari ki-Ingereza kina lahaja nyingi, sawa na ki-Arabu, ki-China, ki-Swahili, na lugha zingine.

Jambo la muhimu la kuzingatia, kwa nchi kama Tanzania, ni hoja ya msingi ya English as a Global Language, kwamba hakuna namna ya kukizuia ki-Ingereza kutawala dunia kama lugha ya mawasiliano. Tupende tusipende, lazima tutafute namna ya kuhakikisha kuwa tunaijua lugha hiyo. Tusipumbazwe na siasa reja reja zilizovaa gwanda la utaifa, tukasahau kwamba ki-Ingereza ndiyo nyenzo na silaha itakiwayo katika mapambano ya ulimwengu wa utandawazi wa leo na kesho.

Saturday, October 8, 2016

People Before Profit: Kitabu Kuhusu Utandawazi

Leo nimejipatia kitabu kiitwacho People Before Profit kilichoandikwa na Charles Derber. Nimeanza kukisoma leo hii hii.

Kwanza, niseme kuwa kitabu hiki kina utangulizi ulioandikwa na Noam Chomsky. Hilo pekee ni ishara ya thamani ya kitabu hiki, kwani Chomsky ni mchambuzi maarufu wa masuala ya ulimwengu kwa mtazamo wa kimaendeleo. Ninamheshimu sana, kama ninavyowaheshimu wachambuzi kama Seymour Hersh na Amy Goodman.

People Before Profit ni hazina ya elimu. Kinafafanua dhana ya utandawazi. Kwanza kinaelezea ukale wa utandawazi, na kwamba utandawazi una historia ndefu. Haukuanza zama zetu hizi, bali umekuwepo kwa miaka maelfu na maelfu, ukibadilika katika kila zama.

Pili kitabu kinaelezea uhusiano wa utandawazi na tekinolojia, kama vile mapinduzi ya miundombinu na viwanda. Tatu, kitabu kinaelezea mahusiano ya utandawazi na utamaduni, na hasa katika mazingira ya leo, kuna suala la mahusiano ya utandawazi na itikadi, kama vile demokrasia.

Kuna dhana kadhaa juu ya utandawazi ambazo tunapaswa kuzihoji, kwa mfando dhana ya kwamba utandawazi unaondoa tofauti miongoni mwa nchi na jamii mbali mbali, na kuifanya dunia iwe na sura moja. Dhana hii imekuwa ikijadiliwa sana.

Inahojiwa, kwa mfano na watu wanaosema kwamba pamoja na juhudi za utandawazi kuufunika ulimwengu, kuna pia nguvu za jamii na tamaduni mbali mbali zinazopambana ili kujilinda, kujihami, na kuendelea kuwepo kwa misingi tofauti na ile ya utandawazi. Nami, katika warsha zangu, kama zile nilizowahi kuendesha Arusha na Dar es Salaam, nilijaribu kuibua masuala haya.

Kifupi ni kwamba kitabu hiki kinaibua masuala muhimu ya kuelimisha kuhusu hiki kinachoitwa utandawazi. Ninakipendekeza kwa yeyote anayethamini elimu.

Wednesday, October 5, 2016

Tafsiri ya "Ye Tradefull Merchants," Shairi la Edmund Spencer

Siku kadhaa zilizopita nilichapisha mashairi mawili ya Edmund Spencer katika blogu hii. Nilivutiwa na wazo la kuyatafsiri mashairi haya, ingawa magumu, ili kuchangamsha akili yangu na kujipima ufahamu wangu wa lugha.

Siku ile ile, nilijaribu kutafsiri "Ye Tradefull Merchant," tangu mwanzo hadi mwisho, halafu nikaamua kuiweka kando tafsiri yangu, kwa kuwa sikuridhika na namna nilivyotafsiri vipengele viwili vitatu. Leo, bila kutegemea wala kupangia, nimepata hamu ya kurekebisha vipengele hivyo.

Ninafahamu kwamba, kwa mujibu wa nadharia za tafsiri, tafsiri ni dhana tata. Kutafsiri ni sawa na kujaribu kukikamata kitu kinachoteleza sana. Kwa ujumla, tunajidanganya au tunadanganyana tunaposema tumetafsiri utungo wowote wa fasihi. Hata hivyo, kwa kuzingatia jadi yetu ya kujidanganya na kudanganyana, ninaleta tafsiri yangu ya "Ye Tradefull Merchants."

---------------------------------------------------------------------------------------------

YE TRADEFULL MERCHANTS (Edmund Spencer)

Ye tradefull merchants, that with weary toyle,
Do seeke most pretious things to make your gain,
And both the Indias of their treasures spoile,
What needeth you to seeke so farre in vaine?
For loe! my love doth in her selfe containe
All this worlds riches that may farre be found:
If saphyres, loe! her eies be saphyres plaine;
If rubies, loe! hir lips be rubies sound;
If pearles, hir teeth be pearls, both pure and round;
If yvorie, her forhead yvorie weene;
If gold, her locks are finest gold on ground;
If silver, her faire hands are silver sheene:
     But that which fairest is but few behold,
     Her mind, adornd with vertues manifold.

ENYI WAFANYA BIASHARA MAKINI

Enyi wafanya biashara makini, mnaomenyeka na kazi,
Mkitafuta vitu ghali kujipatia faida,
Na India zote mbili mwazipora utajiri wao,
Nini mnajisumbua kutafuta mbali kote huko?
Kwani, hakika, mpenzi wangu anao nafsini mwake,
Utajiri wote wa dunia upatikanao mbali huko:
Kama ni yakuti, lo! macho yake ni yakuti bayana;
Kama ni akiki, lo! midomo yake ni akiki murua;
Kama ni lulu, meno yake ni lulu, safi za mviringo;
Kama ni nakshi ya pembe ndovu, panda la uso wake linayo;
Kama ni dhahabu, nywele zake ni dhahabu bora ya ardhini;
Kama ni uzuri wa fedha, mikono yake ni mizuri hivyo:
     Lakini kilicho kizuri kabisa na wachache wanakiona,
     Ni akili yake, iliyojaa mema maridhawa.

Tuesday, October 4, 2016

Wadau wa Vitabu Vyangu Kwenye Mkutano wa Africa Network

Jana jioni nilirudi kutoka Ohio, katika Chuo cha Denison, ambako nilikwenda kushiriki mkutano wa Africa Network kama nilivyoripoti katika blogu hii. Nina mengi ya kusema kuhusu mkutano ule, na hapa napenda kusema neno juu ya maprofesa wanaoonekana nami pichani hapa kushoto, ambao wote walinigusa kwa namna walivyoongelea vitabu vyangu.

Huyu aliyeko kushoto ni Stephen Volz, profesa wa Chuo cha Kenyon. Tumefahamiana miaka kadhaa katika mikutano ya Africa Network. Aliwahi kuishi Botswana akijitolea chini ya mpango wa Peace Corps. Juzi, nilipowasili kwenye ukumbi wa mkutano, ulikuwa wakati wa chakula cha jioni. Nilienda kukaa kwenye meza ambayo ilikuwa na kiti cha ziada. Mmoja wa watu waliokuwa wameketi hapo ni Profesa Volz.

Baada ya kusalimiana, profesa Volz alianza hima kutuambia kuwa alikuwa anajiandaa kwenda Botswana na wanafunzi wa Associated Colleges of the Midwest (ACM), na kwamba atatumia kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences katika programu hiyo. Nilifurahi kusikia hivyo, ingawa sikushangaa, kwa sababu msukumo mojawapo wa mimi kuandika kitabu hiki ulianzia kwenye mikutano ya bodi ya ACM nilipoombwa kuandika chochote cha kusaidia ufahamu wa tamaduni. Niliwahi kuelezea msukumo huo katika blogu hii.

Kulia hapo pichani ni Profesa Kristofer Olsen wa Chuo Kikuu cha Montana. Huyu naye tumefahamiana kwa miaka kadhaa. Nilimfahamu wakati wa mkutano mojawapo wa Africa Network uliofanyika katika Chuo cha Denison, alipokuwa moja wa watumbuizaji katika kikundi cha ngoma za kiafrika. Baada ya hapo tulikuwa marafiki katika Facebook.

Siku moja aliniandikia ujumbe kuwa alikuwa anafundisha kozi ya "Mythologies," na kati ya vitabu walivyokuwa wanasoma ni kitabu changu cha Matengo Folktales. Aliniulizia kama ningekuwa tayari kuongea na wanafunzi wake kutumia Skype, nami nilikubali, tukapanga siku na tukafanikisha darasa hilo kama nilivyoandika hapa.


Katika mhadhara wake kwenye mkutano wa juzi, kama anavyoonekana hapa kushoto, Profesa Olsen aliongelea kozi yake, akasema kuwa mwanzoni, watu waliposikia anapangia kutunga na kufundisha kozi ya "Mythologies," walidhani alikuwa anamaanisha jadi za Wagriki na Warumi wa kale. Hawakutegemea kuwa alikuwa anataka kufundisha jadi za mataifa mbali mbali hata wa leo. Ndipo akaamua kutumia kitabu cha Matengo Folktales, ambacho alikifahamu tangu alipokuwa mwanafunzi katika Chuo cha St. Olaf.

Profesa Olsen alituelezea kwamba wanafunzi wake walivutiwa kuonana na kuongea nami tulipojumuika kwa Skype. Walivutiwa kuniona mimi mwandishi wa kitabu cha Matengo Folktales walichokuwa wanasoma na pia kunisikia nikiimba nyimbo zilizomo katika hadithi hizo.

Maelezo ya Profesa Olsen yaliwagusa wasikilizaji. Hatimaye, mkutano ulipoisha, wanabodi wenzangu wa Africa Network waliniomba niandae video kutokana na Matengo Folktales ili iwekwe kwenye tovuti ya Africa Network. Nilikubali wazo hilo.

Monday, October 3, 2016

Mkutano wa Africa Network


Wikiendi hii nilikuwa chuoni Denison, katika jimbo la Ohio, kuhudhuria mkutano wa Africa Network, mtandao wa vyuo vinavyoshughulikia masomo juu ya Afrika. Nimekuwa mwanabodi wa Africa Network tangu mwanzo, na nimeshuhudia historia yake hadi leo. Mtandao wa wanachama na washiriki wetu unaendelea kupanuka.

Picha zote zinazoonekana hapa nilipiga mimi, ambaye naonekana hapa kushoto.




Mikutano ya Africa Network ni fursa ya waalimu na watafiti kubadilishana mawazo na uzoefu katika taaluma na nyanja mbali mbali zinazohusu Afrika. Wikiendi hii, tulipata fursa ya kusikia na kujadili mada juu ya masuala kama uhifadhi na usambazaji wa kumbukumbu kidigitali, historia ya kale ya Afrika na umuhimu wake katika masomo juu ya Afrika, kuboresha viwango na ubora katika elimu ya juu, program za kupeleka wanafunzi Afrika.
Mkutano wetu huo ulijumlisha washiriki kutoka Marekani na nchi kadhaa za Afrika. Kwa ujumla wetu, tuna uzoefu wa utafiti katika nchi nyingi za Afrika, kama vile Ghana, Kenya, Msumbiji, Senegal, Tanzania, Uganda, Zambia, na Zimbabwe. Taaluma tunazowakilisha ni kama anthropolojia, uchumi, fasihi, historia, na lugha.




Nitaendelea kuandika kuhusu mkutano wa wikiendi hii, kwani ninazo kumbukumbu nyingi.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...