Pamoja na kuwa kazi yangu ya msingi huku Marekani ni kufundisha, ninajishughulisha pia na mipango ya uhusiano baina ya vyuo vya Marekani na Tanzania na nchi zingine za Afrika. Mipango hii ni ile ya kupeleka wanafunzi Afrika. Kwa upande wa Tanzania, napata pia fursa ya kufanya mahojiano (intavyuu) na wasomi wanaotafuta nafasi ya kuja Marekani kwa masomo zaidi au utafiti. Hizi ni kazi za kujitolea, lakini nazifanya kwa moyo moja, nikizingatia umuhimu wake kwa upande wa Marekani na nchi zetu, kwani, pamoja na kutoa fursa mbali mbali kwa wahusika, zinakuza maelewano duniani. Mtu unapokuwa na fursa au wadhifa kama wangu, wa-Tanzania wanasema umeula. Wanaamini unalipwa hela nyingi sana, tena dola, si madafu. Pili, wanategemea kuwa unatumia fursa hizi kujitajirisha sana kifedha kwa msingi wa "akili mkichwa." Zaidi ya yote, wa-Tanzania wanataka wakuone unaishi maisha ya hali ya juu, si uwe unakula pilau au chapati kwenye vihoteli vya Ubungo au Kinondoni. Siku moja, miaka ya tisin