Wednesday, March 30, 2011

Maskani Yangu Madison, 1980-86

Wikiendi hii iliyopita, nilipokuwa Madison kwenye mkutano wa Peace Corps, nilitembelea sehemu kadhaa nilizozifahamu tangu wakati nasoma Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison, 1980-86. Nilivutiwa kwa namna ya pekee na wazo la kutembelea maskani yangu miaka ile.

Niliingia Madison nikitokea Tanzania mwezi Agosti mwaka 1980. Sikumbuki tarehe. Lakini nilifikia mahali palipoitwa Union South, katika eneo la Chuo. Hapo nilikaa siku chache, nikingojea fedha kutoka Ofisi ya Fulbright, ambao ndio walinilipia gharama zote za masomo.

Baada ya siku chache za kukaa Union South, nilihamia Saxony Apartments, sehemu inayoonekana hapa kushoto. Jengo nilimoishi liko nyuma ya hili linaloonekana.

Saxony Apartments ilikuwa maarufu, kwa vile walikuwepo wa-Afrika wengi. Tulijisikia nyumbani.

Nadhani nilikaa hapo Saxony Apartments kwa mwaka moja na zaidi, nikahamia Mtaa wa West Wilson, namba 420, jengo linaloonekana hapa kushoto. Ni karibu na Ziwa Monona. Wa-Tanzania tulikuwa na mshikamano sana, tukitembeleana na kushirikiana katika raha na shida. Nakumbuka mikusanyiko tuliyofanyia hapa kwangu.

Miaka yangu ya mwisho mjini Madison, niliishi mahala paitwapo Eagle Heights, eneo lenye nyumba nyingi sana za wanafunzi wenye familia. Nilikuwa naishi katika nyumba hii, orofa ya juu. Ukianzia kushoto, ni dirisha la tatu na la nne.

Wikiendi hii nilipokuwa nazungukia maeneo hayo nilijiwa na kumbukumbu nyingi za miaka ile. Niliwakumbuka wa-Tanzania na wa-Afrika wengine tuliosoma wote, na mengine mengi. Yawezekana baadhi yao wataziona picha hizi na kukumbuka mambo ya miaka ile.

Tuesday, March 29, 2011

Mkutano wa Peace Corps, Madison, Ulifana

Machi 24-27 nilikuwa Madison, Wisconsin, kuhudhuria mkutano wa Peace Corps, uliojumuisha waMarekani walioenda kujitolea Afrika chini ya mpango wa shirika la Peace Corps. Mwaka huu ni mwaka wa maadhimisho ya miaka 50 tangu kuanzishwa kwa Peace Corps, na maadhimisho hayo yanafanyika sehemu mbali mbali hapa Marekani.

Mkutano huu wa Madison ulikuwa na mengi ya kuelimisha na kusisimua kuanzia historia ya kuanzishwa kwa Peace Corps hadi masimulizi na kumbukumbu za watu walioenda katika nchi mbali mbali za Afrika kujitolea katika nyanja mbali mbali.

Kulikuwa na masumulizi kuhusu Rais Kennedy ambaye alichangia kuotesha mbegu ya Peace Corps kwa mtazamo wake wa kuwahamasisha raia wake wawe na moyo wa kujitolea, si kwa nchi yao tu, bali kwa ulimwengu. Rais Kennedy aliweka sahihi ya kuzindua Peace Corps tarehe 1 Machi, 1961.

Kulikuwa na masimulizi kuhusu Sargent Shriver, ambaye ndiye alikuwa mwanzilishi wa Peace Corps, akiwa na moyo na ari isiyomithilika iliyowasha moto mioyoni mwa wana Peace Corps, moto ambao bado unaendelea kuwaka, ukiwahamasisha kwenda kujitolea sehemu mbali mbali za dunia, na kuishi katika mazingira yoyote.

Kulikuwa na masimulizi kuhusu Kwame Nkrumah alivyojenga shule sehemu mbali mbali za nchi yake, akakuta hana walimu. Ndipo alipomwambia Scriver kuwa wanahitajika walimu. Na Peace Corps ikafanya hima kuandaa watu wakaenda Ghana mwaka 1961. Jina la Julius Nyerere pia lilitajwa, kwani naye aliwakaribisha Peace Corps mapema hivyo hivyo.

Watu mbali mbali, kama vile mabalozi, wasomi, walimu, wajasiriamali na waandishi walikuwepo kuelezea kumbukumbu zao za Peace Corps na mtazamo wao kuhusu umuhimu wa Peace Corps katika maisha yao na ya wanadamu kwa ujumla.

Nilipata fursa ya kukutana na watu waliojitolea Tanzania, kama vile Mzee Ernie Zaremba, ambaye tulipiga hii picha. Tulipiga stori siku zote tatu kuhusu Tanzania. Yeye alijitolea miaka ya 1964-66 Mwanza, Misungwi. Mzee huyu sasa anajishughulisha na kurekodi habari za wana Peace Corps, na kuwaunganisha. Huwa anatembelea Tanzania kukutana na watu waliofahamiana na wana Peace Corps au waliofaidika kutokana na Peace Corps kwa namna moja au nyingine.

Nilipiga stori na Mark Green, ambaye alikuwa balozi wa Marekani Tanzania, 2007-2009. Nilianza kufuatilia habari za Mark Green alipokuwa balozi. Niligundua kuwa maskani yake ni Wisconsin, na kuwa aliwahi kufundisha katika kijiji fulani Kenya. Nilivutiwa na shughuli zake nchini mwetu, nikagundua kuwa tulisoma wote katika chuo kikuu cha Wisconsin-Madison, ingawa hatukufahamiana. Mimi nilimaliza shahada ya uzamifu mwaka 1986 na yeye 1987. Sote tulifurahi kufahamiana.

Kitu kimoja kilichonifurahisha zaidi katika mkutano huu ni kukutana na rafiki yangu Mwalimu Wade DallaGranna, ambaye tulifahamiana mwaka 1980, nilipofika Madison kusoma. Yeye alikuwa amerejea kutoka Lesotho, ambako alikuwa mwana Peace Corps.

Tangu nilipomaliza masomo Madison na kurudi Tanzania katikati ya mwaka 1986, hatukuwahi kukutana tena, hadi hiyo juzi. Tulifurahi sana, tukawaambia wengine pia.

Nina mengi ya kuelezea kuhusu mkutano huu, na natengemea kuendelea kuandika. Inatia moyo na hamasa kubwa kuwemo katika jumuia kubwa namna ile ya watu ambao fikra na mazungumzo yao ni juu ya kujitolea na kuwasaidia binadamu wengine, kujenga mahusiano mema duniani, na kuwaletea wengine maisha bora na mafanikio.

Monday, March 28, 2011

Dhana Duni ya Mfumo Kristo

Kila kukicha, unajitokeza ushahidi kwamba kiwango cha kufikiri miongoni mwa wa-Tanzania wengi ni duni. Siku hizi, kwa mfano, imeibuka hii dhana ya mfumo Kristo.

Walioibuni dhana hii na ambao wanaieneza wana ajenda ya kujenga hoja kuwa mfumo wa utawala na uchumi Tanzania unaendeshwa kwa misingi ya kiKristu, na kwa lengo la kuwanufaisha wa-Kristu na kuwakandamiza na kuwanyima wa-Islam fursa na haki wanazostahili, katika nyanja mbali mbali, kama vile elimu na uongozi.

Hii ndio dhana ya msingi ya hiki kinachoitwa mfumo Kristo. Wanaojenga hoja hii wanadai kuwa serikali ya Tanzania yenyewe inaendeshwa na maaskofu kama sehemu ya uendelezaji wa huu wanaouita mfumo Kristo.

Kwanza napenda kusema, kama ninavyosema daima, kuwa kila mtu ana uhuru wa kutoa mawazo yake. Uhuru huu ni pamoja na uhuru wa kuyahoji au kuyapinga mawazo ya wengine, kufuatana na mchakato wa kujielimisha na kutafakari masuala. Ni pamoja na uhuru wa kuyapinga mawazo yako mwenyewe.

Nashangaa kwa nini mfumo mbovu uhusishwe na jina la Yesu Kristu. Dini zote mbili, u-Islam na u-Kristu, zinamtambua na kumheshimu Yesu. Yesu anatambuliwa kama Mungu katika u-Kristu. Na katika u-Islam, anatambuliwa kama mtume maarufu. Dini zote zinamheshimu sana Yesu.

Kama mfumo wa Tanzania umeoza kama inavyosemwa, hauwezi kuwa mfumo Kristo. Kuuita mfumo Kristo ni dhihaka isiyo kifani. Huwezi kuuhusisha uchafu wowote na Mungu au mtume. Kama kweli maaskofu wanaendekeza na kuulinda mfumo wa dhuluma, wanakiuka mafundisho na maadili ya Kristo. Huu si mfumo Kristo. Mfumo Kristo ni mfumo wa haki na maadili aliyotufundisha Kristo.

Sidhani kama inahitaji akili ya pekee sana kuitambua hoja hii. Lakini ni wazi kuwa watu wengi Tanzania wana kiwango duni cha kufikiri au kuelewa mambo. Kwa dhana yao ya mfumo Kristo, wanaudhihaki u-Kristo, na pia wanaudhihaki u-Islam. Ila, kutokana na akili zao duni, hawatambui hilo. Kilichopo ni kuwaombea dua njema, waweze kujitambua na kujirekebisha.

Wednesday, March 23, 2011

Eti Wahadhiri Waeneza Siasa za Chuki Vyuoni

Niomeona taarifa hii hapa chini nikaona lazima niseme moja mawili, nikitumia wadhifa wangu kama mwanataaluma na mzoefu wa kufundisha au kutoa mihadhara vyuo vikuu sehemu mbali mbali za dunia.

Sio kazi ya serikali kuingia darasani chuo kikuu ili kuchunguza mwalimu anafundisha nini au anafundishaje. Hii ni kazi ya wanataaluma na wahadhiri, kufuatana na taratibu zinazotambulika katika jumuia ya wanataaluma. Taratibu hizi ni za kulinda, kutathmini, kuratibu na kuboresha viwango vya utafiti, ufundishaji na taaluma kwa ujumla.

Serikali inapaswa kutambua kuwa dhana ya chuo kikuu, duniani pote, inaendana na haitengeki na uhuru wa kitaaluma. Walimu wa vyuo vikuu sio tu wana wajibu, bali uhuru wa kufukuzia taaluma bila vipingamizi, kwa mujibu wa vigezo vya taaluma hizo vinavyotambulika miongoni mwa wanataaluma kimataifa.

Kama kuna walakini katika utendaji kazi wa mwalimu wa chuo kikuu, kama vile kutofundisha somo inavyotegemewa, wanaowajibika kuchunguza ni wanataaluma wenzake, si serikali. Serikali haitegemewi wala kuruhusiwa kuingilia uhuru wa walimu na watafiti chuo kikuu katika kufanya utafiti, ufundishaji, uandishi na kadhalika kwa misingi na viwango vinavyotambuliwa kitaaluma.

Jambo jingine la msingi kabisa kuhusu chuo kikuu ni kuwa hapa ni mahala pa tafakari na malumbano kuhusu masuala mbali mbali, kwa kiwango cha juu kabisa. Ni mahala ambapo fikra za kila aina na hoja za kila aina zinapaswa kusikika na kuchambuliwa.

Chuo kikuu cha kweli, chenye hadhi ya chuo kikuu, ni maskani ya wachochezi wa fikra na hoja, katika taaluma mbali mbali, ikiwemo siasa. Huwezi kumwambia mtafiti au mhadhiri asiiponde serikali iliyoko madarakani iwapo utafiti na tafakari yake inampeleka huko.

Dhana ya kwamba kuna wanaoeneza siasa za chuki miongoni mwa wanafunzi wa chuo kikuu ni dhana ya kusikitisha. Inamaanisha kuwa hao wanafunzi ni wajinga sana, au ni wavivu sana, ambao hawana uwezo au dhamira ya kujibidisha katika kusoma na kutafakari mambo ili waweze kugundua mapungufu ya hoja wanazosikia, na kupambana kwa hoja. Inamaanisha hao ni wanafunzi mbumbumbu, wasio na akili au wasiotumia akili. Kitendawili ni je, walifikaje hapo chuoni, kama si kwa njia za panya?

Wanafunzi wa chuo kikuu wanawajibika kuwa tayari na makini katika kupambana kwa hoja na wanafunzi wenzao na pia na walimu wao. Ni fedheha iwapo wanafunzi hao kiwango chao ni duni kiasi cha kuweza kupotoshwa na walimu wao. Hawastahili kuitwa wanafunzi wa chuo kikuu, na hicho chuo chenyewe hakistahili kuitwa chuo kikuu. Na ni fedheha kama tumefikia mahali ambapo serikali inaona ije darasani kuwanusuru hao wanafunzi feki.


------------------------------------------------------------------------------------
WAHADHIRI WAENEZA SIASA ZA CHUKI VYUONI


Chanzo:Habari Leo

Wahadhiri waeneza siasa za chuki vyuoni
Imeandikwa na Theopista Nsanzugwanko; Tarehe: 23rd March 2011


SERIKALI inawachunguza wahadhiri wa vyuo vikuu nchini wanaotumia muda mrefu madarasani kuzungumzia siasa badala ya kufanya kazi zinazohusu taaluma.

Kwa mujibu wa Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philipo Mulugo, Serikali ina taarifa kuwa, baadhi ya wahadhiri wanatumia muda wa kutoa mihadhara ya masomo kwa kuzungumzia siasa hasa kupiga vita Serikali iliyopo madarakani.

“Tunaendelea na uchunguzi wa kuwabaini baadhi ya wahadhiri wanaojihusisha na siasa kwa kuingia madarasani na kuzungumzia siasa kwa dakika kumi kabla ya kuanza kufundisha,” amesema Mulugo.

Kwa mujibu wa Naibu Waziri huyo, lengo la wahadhiri hao ni kuwafanya wanafunzi kuchochea migomo na maandamano na kupandikiza chuki baina ya Serikali na wanafunzi.

Naibu Waziri ameyasema hayo katika mkutano kati ya Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa na wahadhiri wa Chuo Kikuu cha Sayansi ya Tiba Muhimbili (Muhas), Dar es Salaam.

Mulugo amesema, ingawa si katika chuo hicho, lakini kuna taarifa katika baadhi ya vyuo vikuu, wahadhiri wanafanya hivyo na kuwaonya kuwa kazi yao ni kuelimisha na si kuwavuruga wanafunzi akili kwa kuchanganya yale wanaojifunza na siasa na akawataka kujiepusha na siasa kwa kuwa wao ni wataalamu.

“Tena siasa zenyewe ni za kupiga vita Serikali iliyopo madarakani, tutawachukulia hatua,” alisisitiza.

Kauli hiyo iliungwa mkono na Waziri Kawambwa ambaye aliongeza kuwa wahadhiri wasipojihusisha katika siasa, watasaidia kuweka utulivu katika vyuo na kuepusha migogoro.

Awali, kabla ya onyo hilo, Dk. Kawambwa alisema Baraza la Mawaziri limeazimia kuanzia Machi mwaka huu wahadhiri wastaafu walipwe pensheni sawa na wastaafu wengine serikalini.

Alifafanua kwamba uamuzi huo unatokana na malalamiko ya wahadhiri wastaafu kwamba wanapata mafao finyu kutoka Mfuko wa Pensheni wa PPF tofauti na wanaostaafu kutoka Serikali Kuu ambao hupata mafao yenye neema kutoka Mfuko wa Pensheni ya Wafanyakazi wa Serikali Kuu (GSPF).

Mbali na Dk. Kawambwa, pia Rais Jakaya Kikwete katika shughuli tofauti ya kuzindua Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Udhibiti na Usimamizi wa Hifadhi ya Jamii (SSRA) jana, aligusia malalamiko ya wafanyakazi wote kuhusu tofauti kubwa ya sana katika utoaji wa mafao ya mkupuo na pensheni ya uzeeni.

“Utakuta wafanyakazi wenye viwango sawa vya mshahara, muda sawa wa utumishi wanapostaafu, mmoja anapata hadi mara tatu zaidi ya mwenzake aliye mfuko mwingine,” alisema Rais Kikwete.

Kutokana na tofauti hiyo aliyosema imelalamikiwa na vyama vingi vya wafanyakazi, Rais Kikwete aliagiza SSRA iangalie tofauti hiyo kwa makini na kuhakikisha kunakuwa na uwiano sawa wa mafao kati ya mfuko na mfuko, lakini akawataka pia wazingatie ustawi wa mfuko huo.

Lakini kuhusu maombi ya wahadhiri wa Muhas, kutaka kulipwa mafao kwa mkupuo kwa asilimia 50 ya mafao yao na kulipwa kwa miaka 15 baada ya kupokea mafao ya mkupuo, Dk. Kawambwa alisema bado yanafanyiwa kazi.

Kati hilo, Dk. Kawambwa alibainisha wataalamu wanaangalia suala la malipo hayo kwa kuwa limeonekana na utata unaoweza kusababisha baadhi ya mifuko kufa iwapo itapata wastaafu wengi hivyo unaangaliwa mfumo utakaotumiwa na mifuko yote.

Akizungumzia madai ya wahadhiri wa chuo hicho kuhusu posho ya nyumba ambazo hawajalipwa kuanzia mwaka jana, alisema hali hiyo ilitokana na ufinyu wa bajeti, lakini tayari wamepeleka malalamiko yao kwa Wizara ya Fedha ili walipwe katika bajeti ijayo.

Kabla ya kauli hizo za mawaziri, Makamu Mkuu wa Chuo hicho Profesa Kisali Pallangyo alielezea changamoto anazopata ikiwemo ya miundombinu michache ya chuo hicho.

Kutokana na uhaba huo wa miundombinu, kati ya wanafunzi wanne wanaostahili kujiunga na chuo hicho, ni mmoja tu anayepata nafasi wakati Taifa linakabiliwa na uhaba mkubwa wa wataalamu wa afya.

Dk. Kawambwa akijibu hoja hiyo, alisema, katika kuongeza wataalamu hasa katika masomo ya sayansi, Serikali imejipanga katika mpango wa maendeleo ya elimu ya juu kuboresha miundombinu ya vyuo hivyo ili wanafunzi wote wenye sifa wajiunge na vyuo stahili.

Sunday, March 20, 2011

Kazi ya Kunywa

Ukiondoa kazi ya kukaa vijiweni, kazi muhimu ya wa-Tanzania wengi ni kunywa. Huyu jamaa kwenye katuni ni m-Tanzania halisi. Yuko kazini, wala hafanyi mchezo. Ameshaamrisha kuwa kaunta ihamie hapa alipo, tena haraka sana.



Wako wa-Tanzania ambao wanajifunza kunywa tangu utotoni. Wanapofikia ujana wanakuwa wameshahitimu.

Kazi ya kunywa ni muhimu kwa wa-Tanzania wengi kiasi kuwa wamehamia baa, na wanaishi huko, kama nilivyoandika hapa.

Shughuli nyingi za jamii Tanzania zinawezekana tu iwapo zinaendana na kunywa. Yaani ili watu waje kwenye hizi shughuli, ni muhimu ulabu uwepo. Hata kwenye uzinduzi wa kitu kama kitabu, ni muhimu pawe na ulabu, kama nilivyoelezea hapa.

Nilisoma kwenye jarida la Tanzania Schools Collection, 1, (2009), kuwa mtoto mmoja wa miaka kumi alionekana kwenye maonesho ya vitabu Dar es Salaam akiwa mwenyewe. Mratibu mojawapo wa maonesho alipomwuliza kwa nini hakuja na baba yake, mtoto alijibu kuwa baba angefika kama kungekuwa na bia (uk. 12).

Kwa mwendo huu, naweza kusema kuwa miaka ijayo, itabidi tuwe na bia kila mahali, kuanzia shuleni hadi Bungeni.

(Katuni nimeipata katika kitabu cha Kula...Mtoto wa Bosi, kilichoandikwa na Simon Regis na kuchapishwa na Regis Art Production, Dar es Salaam. Sikumbuki ni wapi nilipata hii picha nyingine. Ningependa kuweka taarifa ipasavyo)

Friday, March 18, 2011

JK: Maprofesa Wananisikitisha

JK: Maprofesa wananisikitisha

Chanzo: Uhuru

NA JANE MIHANJI

RAIS Jakaya Kikwete amewataka maprofesa na wasomi nchini kutunga vitabu ili kukabiliana na tatizo la kushuka kiwango cha elimu, kunakochangiwa na upungufu wa vitabu vya kiada na ziada.

Amesema anasikitishwa na kitendo cha maprofesa na wasomi chini kulalamikia upungufu wa vitabu katika fani mbalimbali, huku wakikwepa kutoa mchango wa kutatua tatizo hilo.

Rais Kikwete amewata kila mmoja kwa nafasi yake, kuhakikisha anafanya jitihada za kuboresha elimu ili kuwa na kizazi kilichowiva kitaaluma.

Alisema hayo jana, mjini Dar es Salaam, alipotembelea Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi. Taarifa ya wizara iliyosomwa na waziri, Dk. Shukuru Kawambwa, ilieleza uhaba wa vitabu ni moja ya matatizo yanayokwamisha sekta ya elimu.

Dk. Kawambwa alisema shule nyingi zinakabiliwa na upungufu wa vitabu na katika baadhi, wanafunzi hutumia vya tofauti, tatizo linaloweza kupatiwa ufumbuzi kwa wasomi kujikita katika uandishi wa vitabu.

"Hili ni tatizo, wakati tunasoma Msoga kitabu cha Bulicheka, mwanafunzi aliyekuwa akisoma Lindi alikisoma, lakini siku hizi mambo yamebadilika," alisema rais Kikwete na kuiagiza wizara kutoa kipaumbele katika uchapishaji vitabu vya kiada na ziada.

"Lazima tupange kila mwaka bajeti ya kuchapisha vitabu vya watoto wetu, hatuwezi kuacha waendelee kuchangia vitabu kwa kuwa hili ni la kwetu, na hatuwezi kusubiri wafadhili," alisema.

Alionya fedha za vitabu, maabara na ujenzi wa nyumba za walimu zisipelekwe katika matumizi mengine.

Kwa upande wake, Dk. Kawambwa alisema wizara inakabiliwa na upungufu wa walimu wa shule za msingi na sekondari, hususan katika mikoa ya pembezoni.

Alisema pia kuna tatizo la kiwango kidogo cha ufaulu kwa wanafunzi katika mitihani ya kuhitimu elimu ya msingi, sekondari na ualimu, hususan masomo ya sayansi, hisabati na kiingereza.

Waziri Dk. Kawambwa alisema ufinyu wa bajeti katika utekelezaji programu za elimu na mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu pia ni tatizo kubwa.

Akizungumzia kiwango cha ufaulu, rais Kikwete aliwataka walimu wanaotunga mitihani ya shule za msingi, sekondari na vyuo, kuacha kutunga migumu kupita kiasi, kwa kuwa yawezekana kuwa ndicho chanzo cha matatizo.

"Changamoto ya ufaulu mdogo kama mnavyodai katika masomo ya sayansi, hisabati na kiingereza pengine inatokana na ugumu wa mitihani... lakini msitunge rahisi sana," alisema na kuongeza ni lazima wahitimu wawe na viwango vinavyostahili.

Wednesday, March 16, 2011

Eti Wananchi Msiwasikilize Wapinzani

Kuna mambo mengi katika siasa Tanzania siku hizi. Katika hali ya ushindani wa kisiasa uliopo, mara kwa mara tunawasikia hao wanaoitwa viongozi wetu wakisema, pengine kwa jazba, kuwa wananchi msimsikilize fulani au msiwasikilize watu fulani. Wanaotajwa hasa ni wapinzani. Wananchi wanaambiwa wasiwasikilize wapinzani.

Kiongozi wa kweli, mwenye busara na ufahamu, hawezi kutoa kauli za namna hiyo. Kila mtu ana haki ya kusikiliza mawazo mbali mbali, yawe vitabuni, magazetini, au kwenye mikutano ya hadhara. Haki hii inapaswa kutambuliwa, kutetewa na kuheshimiwa. Yeyote anayesemekana kuwa ni kiongozi anapaswa kufahamu hilo.

Pamoja na kwamba ni haki ya kila mtu, vile vile ni sehemu ya uhuru alio nao binadamu. Kila mtu ana uhuru wa kutafuta maoni, mawazo na mitazamo ya wengine katika masuala mbali mbali. Ana uhuru wa kusoma vitabu na magazeti, au kusikiliza redio na televisheni, au kusikiliza hotuba kwenye mikutano ya hadhara.

Zaidi ya suala la haki na uhuru, kuna suala la wajibu. Wananchi wana wajibu wa kufahamu yanayoendelea nchini mwao. Ni lazima wajibidishe kutafuta taarifa, mitazamo na uchambuzi mbali mbali kuhusu masuala ya nchi yao na dunia kwa ujumla. Bila hivyo, wananchi hao watakuwa ni wajinga na maamuzi yao yatakuwa ni ya kijinga na pengine ya hatari kwa nchi yao. Kuweka vizuizi au mipaka, kwamba tuwasikilize watu fulani tu au mitazamo ya aina fulani tu ni kukiuka wajibu. Kutafuta elimu ni wajibu wa kila binadamu mwenye akili timamu.

Kwa kuzingatia hayo, kila ninapowasikia hao wanaoitwa viongozi wakiwaasa wananchi eti wasiwasikilize watu fulani, najiuliza kama tuna viongozi au la. Na kama kuna wananchi wanaoafiki maelekezo hayo yasiyo na mantiki wala tija, ni wazi kuwa bado tuna njia ndefu, na labda niseme tunaelekea kubaya, kwa kuendekeza ujinga.

Kilipopigwa marufuku kitabu cha Hamza Njozi kuhusu mauaji ya Mwembechai, nilifanya juhudi kutetea haki ya mwandishi na nilipinga kitendo cha kupiga marufuku kitabu kile. Hamza Njozi mwenyewe, kwenye utangulize wa kitabu chake kilichofuata alinishukuru kwa msimamo wangu.

Msingi huu huu wa kutetea uhuru na haki ndio nautumia katika kuwashutumu hao wanaoitwa viongozi, ambao wanawaasa watu wasiwasikilize watu fulani. Kitu muhimu ni kila mtu mwenye fikra au wazo apewe fursa kamili ya kujieleza, na wenye kupinga nao wapewe fursa kamili ya kutoa hoja zao. Kuhusu kitabu cha Njozi, msimamo wangu ulikuwa kwamba wasiokubaliana naye, waandike vitabu vyao. Kwa njia hiyo tutaelimika sana.

Tuesday, March 15, 2011

Kichekesho: Eti Dr. Slaa Kama Savimbi!

KONA YA KARUGENDO

Chanzo: Raia Mwema

KICHEKESHO: ETI DR. SLAA KAMA SAVIMBI!

Watwambie ni kwa lipi wanafanana?
KAWAIDA ya mfa maji haishi kutapatapata, na katika hali hiyo ya kutapatapa anafanya mambo mengi na yasiyokuwa ya kawaida. Lengo zima likiwa ni kuyaokoa maisha yake.

Mtu anayetapatapa anaweza kuropoka na wakati mwingine kuupotosha umma. CCM ni kama mfa maji; wanatapatapa, wameanza kuropoka na kupotosha. Eti Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Wilbroad Slaa ni kama Savimbi wa Angola. Kwa lipi?

Mbali na kwamba Savimbi alikuwa binadamu, na Dk.Slaa ni binadamu, Savimbi alikuwa Mwafrika na Dk. Slaa ni Mwafrika; hawana kingine cha kufanana! Savimbi alikuwa mwanajeshi, alipigana msituni zaidi ya miaka 20!

Aliendesha mapigano ya wenyewe kwa wenyewe; watu wengi walikufa. Wengine walipata ulemavu wa kudumu kutokana na vita alivyoviendesha Savimbi, na wengine waliikimbia nchi yao.

Savimbi alipora raslimali za nchi yake ili kuendesha vita hiyo iliyokuwa ndefu kiasi chake. Hadi leo hii wanahistoria wana kazi kubwa ya kutafiti na kuandika juu ya nia ya Savimbi ya kuendesha vita miaka 20 bila kuchoka wala kukata tamaa. Ni lazima alikuwa na lengo; nachelea kusema ni “uchu wa madaraka”; maana hata wale wasioingia msituni wana “uchu wa madaraka” kwa kutumia njia nyingine ambazo pia ni mbaya.

Kuvuruga uchaguzi kama ilivyotokea Kenya na Ivory Coast, ni mbaya zaidi ya kuingia msituni. Kutangaza matokeo ya uchaguzi kwa kutumia nguvu za dola kama ilivyotokea kule Karagwe, ni mbaya; maana watu wanapoteza imani na zoezi zima la uchaguzi na labda ndo maana idadi ya wapiga kura katika nchi za Afrika inapungua kila mwaka.

Uchaguzi unakuwa hauna maana yoyote kama Tume ya Uchaguzi inaweza kutangaza jinsi inavyojisikia bila kufuata ukweli wa kura zilizopigwa. Watu wengi wanaamini Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2010 Rais Kikwete angemshinda Dk. Slaa kwa kura chache za kuchakachua kiasi cha CCM kushindwa kuunda serikali bila kushirikiana na CHADEMA.

Hivyo kuna watu wenye uchu wa madaraka; hawaingii msituni – wanapambana kwa kuvuruga taratibu na kwenda kinyume na sheria; huku wakitumia vyombo vya dola kuwalinda.

CCM ilivuruga Uchaguzi Mkuu. Leo hii CCM inapiga kelele kwamba CHADEMA wanataka kuleta vurugu! Huwezi kuvuruga uchaguzi wa kidemokrasia ukategemea utulivu. Wale wote walioshiriki kuchakachua uchaguzi na kuhakikisha CCM inapata ushindi mkubwa, baadhi si waaminifu kwa chama chao. Walifanya hivyo kupata fedha, na baadaye walivujisha habari za kuchakachua upande wa pili.

Watu makini ni lazima watahoji, ni lazima watafuatilia na kuhakikisha haki inatendeka. Harakati za kutafuta haki zisichanganywe na vurugu. CHADEMA wanajua CCM ilichakachua uchaguzi, wanajua ufisadi wote unaoendelea kwenye Serikali ya CCM – hayo ndo mapambano yao, na wala si vurugu wala vita.

Ikitokea watu wakahoji masuala hayo, utakuwa si uchochezi; bali ni ukweli wa wazi; maana yanayotendeka Watanzania wanaona na kushuhudia. Kila kitu kina wakati wake. Wananchi wakifikishwa mahali pa kuchoka na kukata tamaa, hakuna risasi wala mzinga utakaowanyamazisha. Natuombe Mungu nchi isifikishwe huko.

Kumlinganisha Savimbi na Dk. Slaa kama alivyofanya kiongozi mmoja mwandamizi wa CCM katika mkutano wake na waandishi wa habari, ni kuropoka. Ni kupotosha na kumkosea haki mwanaharakati huyu shupavu anayepambana kwa nguvu ya hoja.

Wanasiasa wana maneno mengi; kuna kutambiana, kuna majivuno, kuna kutukanana, kuna kupotosha ukweli kwa lengo la kutaka watu wasahau yale yaliyo uwanjani – lakini maneno ya wanasiasa yanapovuka mpaka kiasi cha kumdhalilisha mtu ni lazima kuingilia kati.

Wachambuzi wa masuala ya kijamii, viongozi wa dini, wanaharakati, mashirika yasiyokuwa ya kiserikali na wasomi, ni lazima kuingilia kati na kuweka mambo sawa. Mwalimu Nyerere alitufundisha kwamba mtu anaweza kumvumilia kichaa; lakini kichaa huyo akizidi mipaka, ni lazima afungwe kamba.

Kumfananisha Dk. Slaa na Savimbi ni kuropoka kunakoelekea kwenye ukichaa cha kufungwa kamba! Savimbi alipambana msituni na kusababisha uhai wa watu wengi kupotea. Dk. Slaa yeye alipambana Bungeni, na sasa anapambana majukwaani!

Wakati Savimbi alitumia mtutu wa bunduki, Dk. Slaa anatumia nguvu ya hoja. Yeye anasema hata mende hajafa katika harakati za CHADEMA! Hakika huwezi kuwafananisha watu hawa wawili.

Savimbi aliwalazimisha vijana kuingia msituni – waliokataa waliuawa. Hatujamsikia Dk. Slaa akiwalazimisha vijana kujiunga na chama chake na wanaokataa kupoteza maisha yao. Vijana wanajiunga na CHADEMA kwa kuvutiwa na sera za chama hicho, na hasa harakati za kupambana na ufisadi. Hivyo kumlinganisha Dk. Slaa na Savimbi ni kuropoka.

Savimbi alitumia mtutu wa bunduki kuyalinda machimbo ya madini; si kwa faida na ustawi wa watu wa Angola; bali kutumia madini hayo kununulia silaha za kupambana na kulinda himaya yake. Madini ya Savimbi yaliwanufaisha watu wa nje; wawekezaje wa nje kuliko yalivyowanufaisha watu wa Angola.

Hatujasikia Dk. Slaa na CHADEMA yake kuwa wanamiliki mgodi wowote, hatujasikia kuwa wana silaha za moto zaidi ya hoja na maandamano. Katiba yetu inaruhusu maandamano na haki ya mtu kujieleza na kusikilizwa. Tunachokisikia ni mwanga wanaoutoa kwa wananchi juu ya ufisadi unaoendelea kwenye taifa letu - ufisadi ambao umeendekezwa na chama tawala CCM.

Dk. Slaa amekuwa mstari wa mbele kupigia kelele kashfa zote kubwa za EPA, Richmond na nyingine zote hadi ufisadi ndani ya halmashauri za wilaya.

Wanataka tufikiri kwamba Dk. Slaa anapenda vita kama Savimbi? Ni vita ipi ameianzisha Dk.Slaa? Labda vita dhidi ya ufisadi ambayo anaipigana kwa hoja na ukweli na si kwa mtutu wa bunduki.

Yaliyotokea Arusha ni kazi ya CCM. Kama taratibu za kumchagua meya wa Arusha, zingefuatwa – hakuna damu ingemwagika Arusha. CCM wanataka wakikosea taratibu na kwenda kinyume na sheria, watu wakae kimya kwa vile wao ni chama tawala? Enzi hizo zimepita!

Kuna ushahidi wa kutosha kwamba kama Tanzania tungekuwa na Tume Huru ya Uchaguzi, CHADEMA ingeweza kujizolea wabunge wa kutosha kiasi cha kuizua CCM kuunda Serikali kwenye uchaguzi wa 2010.

Tulishuhudia wenyewe jinsi bunduki na mabomu ya machozi yalivyotumika kutangaza ushindi bandia wa mbunge wa Karagwe. Na kule Shinyanga jinsi mbunge wa CCM alivyoshinda kwa kura moja. Mkurugenzi wa Halmashauri alijificha baada ya kutangaza uongo.

Tuliambiwa walijiandikisha watu milioni 20 kupiga kura, lakini waliojitokeza kupiga kura ni milioni 8 tu! Kuna tetesi kwamba shahada nyingi ziliuzwa ili watu wasijitokeze kwa wingi kuvipigia kura vyama ya upinzani.

Mheshimiwa Rais Jakaya Kikwete ametutangazia hali ya hatari kwamba CHADEMA wanataka kuipindua serikali yake. Mwenye akili za kutosha alielewa alichokuwa akilenga. Na sasa wapambe wake wanaingiza mpya ya kwamba Dk. Slaa ni kama Savimbi! Maana yake nini?

Maana yake akamatwe na kuwekwa ndani kwa kulinda usalama wa taifa? Maana yake ni nini? Kwamba huyu ni mtu wa hatari kama alivyokuwa Savimbi? Maana yake ni nini? Kwamba hata jumuiya ya kimataifa imuweke kwenye orodha ya watu hatari duniani?

Tumesikia msajili wa vyama vya siasa, John Tendwa akitishia kukifuta CHADEMA. Ukichunguza utaona kuwa kinachoiponza CHADEMA ni kupambana na ufisadi; hivyo kama hakitaki kufutwa, basi, kiiache vita hiyo.

Kwa nini CHADEMA washinikizwe kuiacha vita hiyo?? Kwani sisi tunaupenda ufisadi? Kwa nini sisi tunamwona anayepora raslimali za nchi na kujiwekea vijisenti nchi za nje ndo mwanaume wa shoka? Mtu anayenunua shahada zetu wakati wa uchaguzi ndiye mwanasiasa bora? Kwani sisi tumezoea mikataba mibovu? Hatutaki umeme? Hatutaki barabara nzuri? Hatutaki maji?

Kwa taarifa ya wale wanaojifanya kutouona ukweli, ni kwamba hata CHADEMA ikifutwa na Dk. Slaa kuwekwa ndani, miti na mawe yatasimama na kuandamana! Kama Rais wa nchi anasimama na kusema sukari iuzwe si juu ya Shilingi 1,700 na leo hii sukari inauzwa Shilingi 2,000 hadi 2,300, unategemea nini? Wananchi wanaona kabisa kwamba Rais wao hana nia ya kweli kupunguza bei ya sukari. Je ni kweli Rais wa nchi hana uwezo wa kupunguza bei ya sukari? Rais ana vyombo vyote vya dola, ashindweje kupunguza bei ya sukari?

Rais anasema anapambana na ufisadi wakati mafisadi papa bado tunawaona mitaani wakitanua na kutembea vifua mbele. Inakuwaje Rais mwenye nguvu zote za dola na katiba yetu bado inampatia Rais nguvu kubwa, ashindwe kupambana na mafisadi hawa? Ni kweli anashindwa kupambana nao?

Je usalama wa taifa hawana habari za kutosha juu ya mafisadi hao? Ni kushindwa kupambana nao au ni kucheza siasa na kutaka kuwalinda maswahiba wao?

Sasa hivi mafuta yanapanda, umeme umepanda na kila kitu kitapanda – unga utapanda; maana mashine za kusaga zinatumia ama umeme au mafuta. Unga ukipanda, hakuna haja ya kumtafuta mchawi. Watu watajitokeza na kulalamika na pengine kuandamana kwa amani.

Kama Raisi Kikwete angekuwa na washauri wazuri wangemwambia kwamba badala ya kuiogopa CHADEMA, awaogope wananchi; maana hao ndiyo wenye uwezo wa kumwondoa madarakani kikatiba.

Watu wanaojitokeza kwa wingi kwenye maandamano ya CHADEMA si wanachama wa CHADEMA. Maandamano na migomo inayoendelea vyuoni si wanachama wa CHADEMA. Maandamano na migomo inayoendelea kazini si wanachama wa CHADEMA.
Inawezekana CHADEMA ina wanachama na washabiki wake, lakini si wengi kiasi cha wale tunaowaona kwenye maandamano. Tunachokishuhudia kwenye maandamano haya ni wananchi waliochoshwa na ugumu wa maisha. Wananchi wamechoshwa na ubabaishaji wa serikali. Wamechoshwa na ahadi hewa.

Tuliambiwa tatizo la umeme itakuwa historia, sasa tunaingia gizani. Tuliambiwa maisha bora kwa kila Mtanzania, sasa kila kitu kinapanda. Nauli inapanda, karo inapanda, sukari inapanda, mafuta yanapanda, bei za matibabu zinapanda na maisha yanaendelea kuwa magumu.

Maisha yakiwa magumu, utulivu na amani ni ndoto. Ni kweli Tanzania ni nchi ya mani na utulivu, na hali hii haiwezi kuondolewa na CHADEMA. Si kweli kwamba CHADEMA wanacheza mchezo mchafu ambao ni mauti kwetu. Amani na utulivu vitatoweka kwa sababu ya maisha kuendelea kuwa magumu na Serikali ya CCM kuendeleza ubabaishaji.

Amani na utulivu vitaondoka kwa sababu ya wale wenye “uchu wa madaraka”. Nani hao? Si wengine bali CCM. Wamekuwa madarakani zaidi ya miaka 40, wanataka kutawala Bunge zima, wanataka kuongoza halmashauri zote, wanataka kushika nafasi nyeti zote katika taifa letu. Uchu wa madaraka wa CCM ni mauti kwetu!

Mwenye macho haambiwi tazama. Tishio kubwa la usalama wa taifa letu si CHADEMA wala Dk. Slaa, bali ni CCM chenyewe na serikali yake.

Friday, March 11, 2011

Mteja Nimefurahi

Juzi niliandika makala fupi, "Mteja ni Mfalme". Leo napenda kuendelea na mada hiyo, kutokana na jambo lililonitokea.

Nilipeleka kigari changu kwenye kampuni ya CarTime, kubadilisha "oil." Kama kawaida, wakati fundi anaendelea na shughuli, nilikuwa kwenye sehemu ya mapumziko ambako wateja hungojea magari yao. Baada ya muda, niliitwa na kuambiwa kuwa gari yangu tayari, nikalipia na kuchukua ufunguo. Kama kawaida, mhudumu wa hapo mapokezi alinishukuru.

Nilienda nje fundi alikopaki gari nikafungua mlango. Kwenye kiti cha mbele alikuwa ameweka karatasi ambayo picha yake nimeiweka hapa juu. Fundi makenika alikuwa ameiweka hapo. Ujumbe wake ni huu: Asante kwa kuchagua CarTime. Tumefurahi kuhudumia gari lako. Kama vile hii haitoshi, fundi ameshukuru tena na kuandika jina lake, Eric.

Katika makala yangu ya juzi niliongelea umuhimu wa kumridhisha mteja. Sasa leo hapa nimeweka mfano hai. Mimi kama mteja nimefurahi kwa huduma niliyopata. Lakini kwa hapa Marekani, hili si jambo la ajabu, kwani wenye biashara wanazingatia suala la huduma kwa mteja. Niliwahi kusema hivyo hata kwenye mahojiano niliyofanyiwa na Radio Mbao.

Kwa vile wanablogu tunafahamu kuwa blogu ni kama shule, na kwa kuzingatia kuwa watu wengi nchini wanasoma hizi blogu, nimeona niweke taarifa hii na mawazo mawili matatu yanayotakiwa kuzingatiwa na wafanyabiashara na watoa huduma wa Tanzania, ambao mara nyingi tunawalalamikia.

Niliwahi kuhudhuria semina ya biashara hapa Minnesota ambapo baadhi ya mambo yaliyosisitizwa ni kuwa unapokuwa na mteja, uwe makini sana. Ujue kuwa mteja huyu akiridhika na kufurahi, atakwenda kukutangazia biashara au huduma yako kwa marafiki na watu wengine.

Sisi wenyewe tunafanya hivyo kila siku. Tukiwa tumevaa nguo nzuri, halafu marafiki wakatuuliza tumenunua wapi, tunawatajia duka. Au watu wakituuliza hoteli nzuri iko wapi, tunawatajia. Waulize watu Dar es Salaam kitimoto safi kinapatikana wapi, watakutajia. Tukiona filamu nzuri, tunawaambia watu wengine na kuwahamasisha nao wakaione. Kwa maana hiyo, tunawapelekea wafanyabishara wateja bila wao kuingia gharama ya matangazo.

Katika semina hiyo hiyo tulionywa kwamba mteja akiudhika, atakwenda kutangaza habari mbaya kuhusu yaliyompata. Habari hiyo itaenea. Wale watakaosikia watawaambia wenzao, na inakuwa kama sumu ambayo itahujumu biashara au huduma yako.

Mimi mwenyewe mwaka jana nilikumbana na wahudumu wa ovyo katika hoteli moja mjini Arusha. Ni hoteli nzuri, na niliiipenda. Nililipia nikapelekwa chumbani. Baada ya muda kidogo nilihitaji msaada wa kurekebishiwa taa. Hapo ndipo nilipokumbana na uzembe usio kifani. Wahudumu walichelewa sana, na huenda hata walisahau. Nikawakumbusha. Bado hawakuja, nimi nikaendelea kuwangoja. Hatimaye nilienda chini walikokuweko nikaanza kuwafokea. Bosi wao naye akaja, nami nikamjumlisha katika mhadhara wangu wa jazba, nikaendelea kutema cheche na kuwapa vidonge wote. Hawakuwa na sababu kabisa ya kushindwa kutekeleza nilichokuwa nimewaambia.

Basi, kutokana na usumbufu walionipa, hata wakati huu ninapoandika sipendi hata kuiwazia hoteli ile. Inakuwa kama vile natonoshwa kidonda. Sina hamu ya kufikia tena katika hoteli ile. Bahati yao ni kuwa hapa sitataja jina lao. Wangenikoma.

Haya ndio mambo ambayo wenye biashara wanapaswa kuyaelewa na kuyazingatia. Inashangaza kwamba wengi nchini mwetu wanaamini kuwa jambo la kufanya ni kwenda kwa waganga wakapate dawa ya kuwavutia wateja. Inakuwaje sisi tuzingatie imani hizo wakati wenzetu kama hao CarTime hawatumii dawa?

Wednesday, March 9, 2011

Mteja ni Mfalme

Kwamba mteja ni mfalme ni dhana inayojulikana, hata kama wengi wenye biashara hawaifuati. Mantiki ya usemi kuwa mteja ni mfalme iko wazi, kwamba mteja akiridhika anakuwa ndio mpiga debe wako, bila wewe kumlipa chochote. Kwa hivi, kama wewe ni mfanyabiashara, ukiwa na tabia ya kumridhisha kila mteja, utafanikiwa.

Kwa kawaida nadharia ni rahisi, ila utekelezaji unaweza kuwa mtihani mgumu. Hayo ninayaona wakati huu ninapoandika makala hii. Kuna mtu ameanza mawasiliano nami, kunialika nikazungumze kwenye kampuni anapofanyia kazi, kuhusu masuala ninayoongelea katika kitabu changu cha Africans and Americans.

Ingawa nimethibitisha kuwa shughuli hii itafanyika, nimeona kuwa huyu mhusika hana uzoefu mzuri katika kupanga mipango ya aina hii. Nimeanza kupata usumbufu fulni, kwani wakati fulani anasema kitu nami nikadhani nimemwelewa, kumbe baadaye inaonekana hatukuelewana. Hata tarehe aliyopangia tufanya hiyo shughuli ameniambia kuwa imebidi waibadili.

Ninajua kabisa kuwa hatimaye nitaenda kutoa huo mhadhara, lakini usumbufu unanikera. Sasa hapo ndipo suala la mteja ni mfalme linapoingia. Mimi ninatoa huduma ya ushauri katika masuala kama haya niliyoongelea katika kitabu changu. Nimesajili kijikampuni kiitwacho Africonexion hapa Minnesota na huduma nazitoa chini ya kivuli cha kampuni hiyo. Huduma hizo ni pamoja na ushauri, warsha, na vitabu.

Sasa basi, kwa mujibu wa dhana ya kwamba mteja ni mfalme, ni wazi kuwa nawajibika kuwa sambamba na huyu jamaa anayenisumbua, nimsikilize vizuri muda wote na kuongea naye kwa uchangamfu, kama vile hakuna kinachonikera. Kero zake nizione kuwa ni fursa ya mimi kujiongezea uzoefu katika kuwashughulikia wateja na kuimarisha sifa ya kikampuni changu.

Najua kuwa pamoja na yote, kikampuni changu kitafaidika. Kwanza, malipo tumeshapatana, na maandalizi yake yameanza. Siku itakapofika, nitaenda kutoa mhadhara wa kusisimua na kuelimisha. Wao watafaidika, nami nitajipatia wapiga debe wengi.
(Katuni ni ya Nathan Mpangala)

Monday, March 7, 2011

Uandishi Bora wa ki-Ingereza

Suala la uandishi bora kwa ki-Ingereza limenifikirisha kwa miaka mingi na bado ninalifikiria. Nilipokuwa kijana, nilidhani kuwa uandishi bora wa ki-Ingereza ulihitaji matumizi ya maneno magumu na mbwembwe katika miundo ya sentensi. Kwa vile nilipata bahati ya kujifunza ki-Latini, nikiwa shule ya seminari, nilikuwa na uwezo wa kuyafahamu maneno mengi magumu ya ki-Ingereza, kwani asili yake ni ki-Latini.

Imani yangu hii ilikuja kugonga mwamba nilipokuwa nasomea shahada ya uzamifu katika Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison. Hapo nilikumbana na profesa Harold Scheub, ambaye alikuwa mkali kama mbogo katika suala la uandishi kwa maana kuwa alikuwa anataka uandishi unaotumia lugha nyepesi, kama ilivyoelezwa katika kitabu cha Elements of Style kilichotungwa na William Strunk na E.B. White. Huu ni uandishi usio na mbwembwe. Kila neno ni lazima lichunguzwe ili kuona kama ni lazima liwepo kwenye sentensi au la. Kama si lazima, sherti liondolewe.

Nilipata taabu sana kujifunza kuandika namna hiyo ya kutumia maneno yanayohitajika tu, tena yawe ya kawaida, bila mbwembwe. Sio mimi tu, bali kwetu wanafunzi wote ilikuwa ni kilio na kusaga meno.

Nilipopata jukumu la kufundisha uandishi bora wa ki-Ingereza hapa chuoni St. Olaf, nami nilianza tangu mwanzo kusisitiza hayo niliyojifunza kwa Profesa Scheub. Wakati huo huo, katika kuendelea kujibidisha katika kujifunza, nilitambua kuwa ni kweli huo ndio uandishi unaohesabiwa kuwa uandishi bora. Kwa mfano, ninajifunza mengi kutoka kwa mwandishi Ernest Hemingway, kama nilivyoelezea hapa.

Sasa basi, katika darasa langu la uandishi bora wa ki-Ingereza, huwa nawapa wanafunzi baadhi ya maandishi yangu ambayo yamechapishwa, ili wayachunguze na kuona ni vipi wanaweza kuyarekebisha ili yawe bora zaidi. Kwa mfano, nawapa insha yangu iitwayo "Do You Have an Accent?"

Insha hii imeandikwa vizuri. Hata walimu wengine wa ki-Ingereza wameipenda. Kwa mfano soma hapa. Lakini najua kuwa mtu makini akiichunguza zaidi, ataona vipengele ambavyo vingeweza kuboreshwa. Ndio maana nawapa wanafunzi wangu insha hii ili wajaribu kuvigundua vipengele hivi na kuvirekebisha. Ni zoezi ambalo linafaa kwa yeyote anayedhani anaifahamu lugha ya ki-Ingereza. Mimi mwenyewe nimegundua vitu yapata nane ambavyo vinahitaji kurekebishwa ili insha iwe bora zaidi. Hebu nawe iangalie insha hiyo kwa makini: "Do You Have an Accent?".

Saturday, March 5, 2011

Tafakari: Mwalimu Nyerere Aliiogopa CCM

Makala hii, "Mwalimu Nyerere Aliiogopa CCM," niliichapisha kwanza mwaka jana. Soma hapa. Kwa kuzingatia umuhimu wa ujumbe, nimeona niichapishe tena.
----------------------------

Mwalimu Nyerere Aliiogopa CCM

Ingawa alikuwa mwanzilishi wa CCM, kwa nia njema ya kuendeleza mapinduzi katika nchi yetu, miaka ilivyozidi kwenda Mwalimu Nyerere alishuhudia jinsi CCM ilivyobadilika na kuwa mzigo kwake na pia tishio kwa usalama wa Taifa.

Mwaka 1993 Mwalimu alichapisha kitabu kiitwacho Uongozi Wetu na Hatima ya Tanzania (Harare: Zimbabwe Publishing House, 1993). Pamoja na mambo mengine katika kitabu hiki, Mwalimu alisema kuwa kuna kansa katika uongozi wa CCM. Nanukuu baadhi ya maneno yake:

Chama cha Mapinduzi, kwa sababu ya uzito wa historia yake, hadhi ya jina lake, mfumo wa wavu wake, mazoea ya watu, na ubovu wa Vyama vya Upinzani, kinaweza kuchaguliwa na Watanzania, pamoja na kansa ya uongozi wake. Au watu wanaweza wakachoka, wakasema, "potelea mbali:" wakachagua Chama cho chote, ilimradi tu watokane na kansa ya uongozi wa CCM. Hainifurahishi kuyasema haya, lakini uhai wa Nchi yetu unataka yasemwe. (Ukurasa 61)

Mwalimu hakuishia hapo, bali aliongezea namna hii:

Nilisema awali kwamba kansa ya uongozi ndani ya Chama cha Mapinduzi isingekuwa ni jambo la kutisha sana kama tungekuwa tumeanza kuona Chama kizuri cha upinzani kinachoweza kuiongoza Nchi yetu badala ya CCM. Ubovu wa uongozi ndani ya CCM ndio uliofanya nikapendekeza tuanzishe mfumo wa Vyama Vingi. Nilitumaini kuwa tunaweza kupata Chama kingine kizuri ambacho kingeweza kuiongoza Nchi yetu badala ya CCM; au ambacho kingekilazimisha Chama cha Mapinduzi kusafisha uongozi wake, kwa kuhofia kuwa bila kufanya hivyo kitashindwa katika uchaguzi ujao. Lakini bado sijakiona Chama makini cha upinzani; na wala dalili zo zote za kuondoa kansa ya uongozi ndani ya CCM. Bila upinzani mzuri wa nje, na bila demokrasia halisi ndani ya Chama cha Mapinduzi, Chama hiki kitazidi kudidimia chini ya uzito wa uongozi mbovu. Kwa hali yetu ya kisiasa ilivyo nchini hili si jambo la kutarajia bila hofu na wasi wasi! (Ukurasa 66)

Ni wa-Tanzania wangapi wenye utamaduni wa kusoma vitabu? Ni wangapi wanaosoma vitabu vya Mwalimu Nyerere? Ni wazi kuwa umbumbumbu miongoni mwa wa-Tanzania ni neema kwa CCM.

Friday, March 4, 2011

Makala Yangu Imepita

Blogu yangu ni sehemu ninapoweka chochote nipendacho, hata mambo binafsi, kama kumbukumbu au hata kujifurahisha. Niliwahi kusema hivyo. Leo nina taarifa ambayo imeniletea furaha moyoni.

Niliandika siku chache zilizopita kwamba mhariri wa jarida la Monday Development alikuwa ameiomba makala yangu, "What is Development?" Baada ya kuikarabati kidogo, niliipeleka.

Ni siku chache tu zimepita, nami nimefurahi kupata ujumbe kutoka kwa msahihisha makala (copy editor) wa jarida hilo. Hakuona kitu cha kusahihisha. Badala yake ameandika: "Thank you for the thoughtful, honest and well-written article."

Kwa huku Marekani, uamuzi wa msahihisha makala ni wa mwisho kabla ya makala kuchapishwa. Taarifa kama hii inaniongezea ari ya kuendelea na jitihada ya kuandika vizuri. Ninajua kuwa ninaweza kuandika vizuri kwa ki-Ingereza. Kama andiko langu likawa si zuri, sababu itakuwa ni uvivu au kukosa muda, sio kutojua ki-Ingereza bora kinakuwaje.

Wakati moja, mwandishi Jim Heynen, ambaye tulikuwa tunafundisha wote katika idara ya ki-Ingereza hapa chuoni St. Olaf, aliiona insha yangu moja fupi, "If You Came Where I was Born," akaomba aitumie katika darasa lake la uandishi kama mfano wa uandishi bora. Aliitumia hivyo hadi alipostaafu. Kutokana na umaarufu wa huyu mwandishi, niliguswa sana na jambo hilo.

Kwa hali hiyo, sikushangaa kupata ujumbe wa msahihisha makala wa Monday Development kuhusu makala yangu. Ila nina furaha sana kutokana na ukweli kwamba mzunguko wa jarida hili ulivyo mpana, makala yangu hii italisambaza jina langu kuliko chochote kingine ambacho nimeandika hadi sasa. Ninahisi hivyo, na ninahisi makala hii fupi itanifungulia milango na fursa mbali mbali, nami sitasita kuweka taarifa hapa katika blogu yangu.

Lakini hayo hayaji kwa muujiza au kwa bahati nasibu. Ni matokeo ya kujituma na kujishughulisha kwa dhati. Pamoja na kuandika, nimejikita katika shughuli ya kufundisha uandishi bora wa ki-Ingereza. Kuangalia na kutathmini uandishi wa wanafunzi na kuona makosa wanayofanya katika kutumia ki-Ingereza na kuyasahihisha imekuwa ni namna ya kujinoa mimi mwenyewe.

Hitimisho langu ni kuwa kama mimi nimefikia hatua hiyo, kutokana na juhudi, kila mtu anaweza pia, katika uwanja wake, kwa kutumia juhudi. Hakuna sababu ya kukata tamaa. Hii ndio habari yangu ya leo, habari binafsi ambayo naamini itawapa moyo wengine, hata kama ni wachache. Inatosha.

Wednesday, March 2, 2011

Orijino Komedi Wamtangaza Yesu



Kibao hiki cha Orijino Komedi kiliniacha hoi kabisa tangu nilipokiona mara ya kwanza. Mimi ni m-Katoliki. Kila ninapokiangalia kibao hiki, naishiwa nguvu, kwa jinsi Orijino Komedi wanavyoimba na kukatika. Ni balaa babu kubwa. Papo hapo wanawasilisha ujumbe kwa namna isiyosahaulika. Najikuta nikisema Mungu asifiwe kwa vipaji alivyowajalia Orijino Komedi.

Nashukuru kwamba miaka zaidi ya kumi iliyopita niliamua kuanza kumtafakari Yesu mimi mwenyewe. Ninaamini kwa dhati kuwa, kwa jinsi alivyokuwa karibu na watu na pia mpenda michapo, Yesu angeafiki jinsi Orijino Komedi wanavyotangaza neno lake kwa huo mtindo wao wa kuyaruka majoka.

Nawashukuru sana Orijino Komedi kwa kuleta neno la Yesu kwa namna hii ya kuvutia na kugusa moyo.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...