Monday, August 31, 2015

Lowassa, CHADEMA na UKAWA

Kuhusu madai kwamba Lowassa ni fisadi, na kuhusu suala la CHADEMA kumkaribisha, na UKAWA kumteua kuwa mgombea wao wa urais, msimamo wangu ni kama ifuatavyo. Na napenda kuweka wazi kuwa mimi si mwanachama wala msemaji wa chama chochote cha siasa. Ni kiumbe huru, ninayetumia akili yangu na kuchambua mambo nipendavyo.
Kuna kitu kiitwacho haki za binadamu, na kuna kitu kiitwacho utawala wa sheria. Kwa mujibu wa tangazo la kimataifa la haki za binadamu, mtu yeyote anayetuhumiwa au kushtakiwa kwa kosa lolote ana haki ya kuhesabiwa kuwa hana kosa hadi mahakama ithibitishe vinginevyo.
Na hata huko mahakamani, inatakiwa uthibitisho wa hatia ya huyu mshtakiwa uwe wazi bila shaka ("reasonable doubt"). Pakiwa na hiyo "reasonable doubt," ni manufaa kwa mshtakiwa, yaani mahakama inapaswa kumwachia huru, arudi zake uraiani.
Haki hii unayo wewe, ninayo mimi, anayo Lowassa. Lowassa hajapelekwa mahakamani na kuthibitishwa ana hatia kwa vigezo nilivyotaja hapa juu.
Kwa msingi huo, CHADEMA hawajakosea kumkaribisha katika chama chao. UKAWA wamefanya jambo sahihi kumweka kama mgombea wao wa urais.
Ni kweli kuwa CHADEMA hao walikuwa wanamtukana sana Lowassa, wakamwita fisadi mkubwa, wakamweka hata kwenye orodha yao, maarufu kama "List of Shame."
Lakini nahisi CHADEMA wametambua kuwa walikosea, kwa maana kwamba hakuna mahakama iliyothibitisha kuwa Lowassa ni fisadi. Ni sahihi kwa CHADEMA kuwa na msimamo walio nao sasa juu ya Lowassa.
Wenye matatizo, wasiofuata haki, wahujumu wa haki za binadamu, ndio wanaendelea kuimba huu wimbo kuwa Lowassa ni fisadi. Wenye matatizo ni hao akina Samuel Sitta na Harrison Mwakyembe, wanaotangaza kuwa wanamtaka Lowassa aje kwenye mdahalo juu ya ufisadi wake. Akina Sitta na Mwakyembe wanafanya usanii na ulaghai. Watuhumiwa hatuwaiti kwenye mdahalo. Tunawapeleka mahakamani.
Nawashauri watu hao wajifunze kutoka kwa CHADEMA, kujirekebisha na kuzingatia utawala wa sheria na haki za binadamu.

Tuesday, August 25, 2015

Nimekikuta Kitabu Changu Kinameremeta Dukani

Mchana huu nimemaliza kusahihisha mtihani wa kumalizia muhula wa somo langu la "African Literature." Nimekwenda chuoni kuwarudishia wanafunzi daftari zao, nikiwa na furaha ya kuwa na wiki mbili tatu za "uhuru," kabla ya kuanza muhula mwingine.

Baada ya kurudisha daftari, niliingia katika duka la vitabu. Nilizunguka kidogo tu humo ndani nikaona kitabu changu cha Matengo Folktales kimewekwa mahali pa wazi, pamoja na vitabu vingine vichache. Kinaonekana pichani chenye rangi ya manjano na ramani ya Afrika.

Huu ni utaratibu wa duka letu la vitabu. Kila wakati wanachagua vitabu vichache na kuviweka sehemu hizo za wazi ili viweze kuonekana kirahisi kwa wateja. Kufuatana na utaratibu uliopo, kitabu kitakuwa hapo kwa siku kadhaa, na hata wiki kadhaa, kabla ya kurudishwa sehemu yake.

Katika duka hili la chuoni St. Olaf vinapatkana vitabu vyangu vyote. Mbali ya wanafunzi, waalimu, na wafanyakazi wengine wa chuo, wageni wanaokitembelea chuo hupenda kuingia katika hili duka la vitabu, ambalo huuza pia bidhaa mbali mbali, kama ilivyo kawaida katika maduka ya vitabu ya vyuo vya Marekani.

Kila ninapoviona vitabu vyangu katika duka hili, mawazo hunijia, hasa kuhusu namna vitabu hivi vinavyowafaidia wa-Marekani. Vinawafaidia kielimu, kwa kuwa vinatumika katika masomo. Vinawafaidia kibiashara, kwa kuviuza, na vinachangia ajira hata kama ni kiasi kidogo sana, kwa wachapishaji, wasafirishaji, na wahudumu wa duka kama hili la Chuo cha St. Olaf. Nawazia mambo ya aina hii.

Monday, August 24, 2015

Nimeimba Wimbo wa Taifa (Tanzania) Mjini Faribault

Juzi tarehe 22 Agosti, katika tamasha la kimataifa mjini Faribault, Minnesota, kulikuwa na muda wa wawakilishi wa nchi mbali mbali kuandamana hadi kwenye jukwaa kuu wakiwa wamebeba bendera za nchi zao. Baada ya kufika jukwaani, kila mmoja alipata fursa ya kusema machache kuhusu nchi yake na bendera yake, na wengine waliimba wimbo wa taifa lao.

Niliweka historia kwa kubeba bendera ya Tanzania, kusema machache kuhusu Tanzania, na kuimba wimbo wa Taifa. Pichani hapa kushoto ninaonekana nikiwa jukwaani na bendera yangu.

Kitendo hiki cha kuiwakilisha Tanzania hakijawahi kutokea mjini Faribault. Wala mimi sijawahi kusimama jukwaani mbele ya umati wa watu, iwe ni Tanzania au kwingineko, na kuimba wimbo wa Taifa peke yangu. Kutokana na upekee wa tukio hili, nimeona niweke kumbukumbu katika hii blogu yangu.

Niliwahi kuandika katika blogu hii nilivyoamua kununua bendera ya Tanzania ili niweze kuitumia katika matamasha na shughuli zingine hapa Marekani. Kwa kuwa katika tamasha la mwaka jana Faribault sikuwa na bendera, niliamua kuitafuta, kwa ajili ya baadaye.


Siku chache kabla ya tamasha la tarehe 22 Agosti nilimfahamisha mratibu wa tamasha kuwa tayari ninayo bendera. Aliniambia kuwa tayari wamepata bendera ya Tanzania.

Nilishangaa na kufurahi kwa mpigo. Niliona wamefanya heshima kubwa kwa Tanzania, nikizingatia kuwa walikuwa wanatarajia kuwa na bendera za nchi ishirini.

Hata hivi, siku ya tamasha, yaani hiyo juzi, nilibeba bendera yangu. Nilipofika kwenye uwanja wa tamasha, niliona wameshatundika bendera, zinapepea. Kwa hivi, yangu nilibaki nayo.

Bendera ya Tanzania pia ilikuwepo, ila kulikuwa na kasoro moja katika kuifunga mlingotini. Upande wa bluu ulikuwa juu, na upande wa kijani ulikuwa chini.

Kwa namna bendera zilivyofungwa, haikuwa rahisi kurekebisha. Na sikuwajulisha waandaaji dosari hiyo, kwa kuzingatia moyo wao wa kuienzi Tanzania. Niliamua kuwa nitatafuta wasaa muafaka, siku zijazo, kuwaelekeza namna ya kuitundika bendera yetu mlingotini.

Siku nzima katika tamasha, nilikuwa na furaha kuiona bendera yetu ikipepea hapo uwanjani, sambamba na bendera za nchi zingine. Niliandika taarifa zaidi katika blogu yangu ya ki-Ingereza.

Ninafanya mambo ya aina hii kwa ajili ya kuwaelimisha watu huku ughaibuni na kujifurahisha mwenyewe. Kama mtu mwingine yeyote, nami nina mambo ninayoyaona muhimu katika maisha yangu, na pia mambo yanayoniletea raha maishani. Hilo suala la bendera ya Taifa, kama nilivyolielezea, naliona kwa mtazamo huo. 

Saturday, August 22, 2015

Tamasha la Kimataifa Mjini Faribault Limefana

Nimerejea alasiri hii kutoka mjini Faribault, ambako nilishiriki tamasha la kimataifa. Mambo ya kusimulia ni mengi mno. Nategemea kusimulia kidogo kidogo siku zijazo.

Hata hivi, napenda niseme kuwa siku kadhaa kabla ya tamasha, nilipomwambia mratibu kuwa mwaka huu ninayo bendera ya Tanzania, aliniambia kuwa tayari wamenunua. Nilipatwa na mshangao wenye furaha.

Kuna nchi nyingi duniani, na nchi zilizotarajiwa kuwakilishwa na bendera ni ishirini na kidogo. Sikupata wasaa wa kuulizia walifikiaje uamuzi wa kununua bendera ya Tanzania. Ninahisi ni kwa sababu nilikuwa nimejisajili kama mshiriki wa tamasha, na pia kwa kuwa nina historia ndefu ya kushiriki matamasha mjini Faribault na majukumu mengine mjini Faribault.

Ulipofika wakati wa watu kuandamana na bendera za nchi zao, name nilijumuika nao. Tulienda kwenye jukwaa kuu, na kila mtu alisema maneno machache kuhusu nchi yake. Baadhi waliimba nyimbo za mataifa yao. Nami nilifanya hivyo hivyo.

Nilielezea kifupi Tanzania iko wapi na historia yake. Nilielezea maana ya rangi za bendera ya Tanzania, kasha nikaimba wimbo wa Taifa. Naamini kuwa hii ni mara ya kwanza kwa wimbo wa Taifa wa Tanzania kusikika mbele ya kadamnasi mjini Faribault. Nitakumbuka tukio hili.

Hapa naleta baadhi ya picha nilizopiga. Zinatoa fununu fulani za hali ilivyokuwa. Katika picha mojawapo, inaonekana meza yangu, yenye vitabu na "t-shirt" za manjano, na pembeni kuna bango la filamu ya Papa's Shadow, ambalo nililipeleka kwenye tamasha ili kuwaelezea watu kuhusu filamu hiyo ambayo iko njiani kuonyeshwa kwa walimwengu.

Sehemu kubwa ya filamu hiyo ni maongezi baina yangu na Mzee Patrick Hemingway kuhusu maisha, uandishi, na falsafa ya baba yake, mwandishi Ernest Hemingway. 

Kulikuwa na upepo sana muda wote wa tamasha, na vitu vyetu vilikuwa vinarushwa huko na huko. Hii ndio sababu ya meza yangu kuwa shaghalabaghala kama inavyoonekana.

Tamasha limefana sana. Nimekutana na kuongea na watu wa mataifa mbali mbali. Nimepanua mtazamo na ufahamu wangu kwa kuwasikiliza, na mimi nimewafahamisha mambo kadha wa kadha ambayo walikuwa hawayajui.

Kama nilivyogusia, hapa nimeweka picha mbali mbali, bali nategemea kuandika taarifa na kumbukumbu siku zijazo.

Thursday, August 20, 2015

Tumemaliza Warsha Kuhusu Jamii na Taaluma

Leo, hapa chuoni St. Olaf, tumemaliza warsha yetu kuhusu jamii na taaluma. Nimeshaandika kuhusu warsha hii katika blogu hii. Tumehitimisha warsha kwa kujadili kitabu cha George Yancey, Compromising Scholarship: Religious and Political Bias in American Higher Education. Lakini, kabla ya kuongelea mjadala wa leo, napenda kwanza kugusia mjadala wa jana.

Jana tulijadili sura za 1, 5, na 8 za Professors and Their Politics, kilichohaririwa na Neil Gross na Solon Simmons. Insha zilizomo katika kitabu hiki zinabainisha vizuri aina mbali mbali za mitzamo ya kisiasa inayoongoza fikra, utafiti, uongozi, na mambo mengine katika vyuo vikuu vya Marekani. Kitabu hiki kinajadili soshiolojia ya wanataaluma, kwa kuchambua mahusiano miongoni mwao na siasa zinazoendesha vyuo. Kinatoa mwanga juu ya mahusiano baina ya wanataaluma na jamii kwa ujumla, ikiwemo ushiriki wa waalimu na wahitimu katika masuala ya siasa za Marekani.

Tulisoma pia maandishi mengine ambayo hayamo katika kitabu hiki, tukayajumlisha katika mjadala. Andiko mojawapo ni "The Coddling of the American Mind." Mjadala ulikuwa wa kufikirisha na kuelimisha, sawa na mijadala ya siku mbili zilizotangulia.

Leo, tulijadili sura ya 2, 5, na 8 za Compromising Scholarship. Kwa kiasi fulani, mambo yaliyojitokeza leo ni mwendelezo wa yale tuliyoyajadili jana, ingawa kitabu hiki kinakwenda mbali katika kutufanya tujitambue kwamba tunapoangalia suala lolote, tunaliangalia kwa kutumia misingi, mitazamo, au kasumba tulizo nazo vichwani. Kwa mtu ambaye anafahamu angalau kiasi falsafa ya watu akina Immanuel Kant, au nadharia za kisasa za fasihi, msisitizo kwamba sisi sote tuna misingi hiyo vichwani mwetu, kitabu hiki si kigumu kukielewa.

Mjadala wa leo ulionekana kuamsha hisia za ndani na hamasa miongoni mwa wengi wetu. Labda ni kwa sababu ya aina ya masuala tuliyokuwa tunazungumzia, au labda ni kwa sababu tumezoeana baada ya siku tatu za kukaa pamoja na kujadili masuala, mjadala wa leo haukuwa wa kawaida. Ingekuwa warsha inaendelea kesho na keshokutwa, kwa mfano, joto la mjadala lingezidi kupanda.

Nimejifunza mengi katika warsha hii. Kama nilivyosema awali katika blogu hii, nafurahi kujipatia vitabu muhimu bila gharama, ambavyo nitavisoma kwa wakati wangu. Elimu ya bure namna hii, na vitabu muhimu, ni marupurupu adhimu ya ualimu.

Tuesday, August 18, 2015

Warsha Kuhusu Jamii na Taaluma Inaendelea

Siku chache zilizopia niliandika katika blogu hii kuhusu warsha tuliyokuwa tunaisibiri hapa chuoni St. Olaf juu ya jamii na taaluma. Warsha hiyo ilianza jana; tulijadili sura kadhaa za kitabu cha Martha C. Nussbaum, Not for Profit: Why Democracy Needs the Humanities.

Kitabu hiki kinaelezea namna mwelekeo wa elimu ya juu unavyochepuka kutoka katika hali yake ya asili na unavyoingia katika mkondo wa kibiashara. Malengo ya elimu, ambayo yanapaswa kuwa kumjenga mtu na jamii katika tabia ya kutafakari, kuhoji mambo, kujitambua, na kuwa na mahusiano mema, ya ushirikiano na kusaidiana, yamekuwa yakibadilika. Malengo hayo sasa ni kuwaandaa watu kwa ajira na uzalishaji wa mali.

Not for Profit kinaongelea umuhimu wa elimu katika demokrasia. Kwa kuiingiza elimu katika mfumo wa biashara, tunahujumu demokrasia na mahusiano bora ulimwenguni. Nilifurahi kusoma katika kitabu hiki nadharia za mabingwa niliowasoma nilipokuwa mwanafunzi Chuo Kikuu cha Dar es Salaam: Socrates, Jean Jacques Rousseau, Johann Pestalozzi, na John Dewey. Ningefurahi zaidi iwapo nadharia za Paulo Freire zingekuwemo pia, kwani huyu ni mwelimishaji maarufu aliyeonyesha njia ya kuifanya elimu kuwa nyenzo ya mapinduzi.

Nilifunguka akili niliposoma kuwa Rabindranath Tagore alikuwa mwelimishaji, sio tu kinadharia, bali kwa kuanzisha na kuendesha vyuo. Tangu zamani nilimfahamu Tagore kama mwandishi maarufu wa riwaya, tamthilia na mashairi, aliyepata tuzo ya Nobel mwaka 1913. Niliwahi kufundisha kitabu chake maarufu, Gitanjali, hapa chuoni St. Olaf. Lakini sikuwa nimefuatilia mchango wake ulivyoelezwa katika Not for Profit.

Leo tumejadili sura kadhaa za kitabu cha Stanley Fish, Versions of Academic Freedom: From Professionalism to Revolution. Fish anafafanua vizuri dhana ya uhuru wa taaluma, kwa kuangalia mitazamo mbali mbali iliyopo kuhusu dhana hiyo. Ameweka wazi masuali muhimu kuhusu dhana ya uhuru wa taaluma. Kwa mfano, uhuru wa taaluma ni haki ya kikatiba? Kwa nini waalimu katika elimu ya juu wanaamini wana haki ya kuwa na uhuru wa taaluma mpana kuliko uhuru walio nao wananchi wengine? Wanafunzi nao wanao au wanastahili uhuru huo?

Fish anaongelea pia masuala ya mtazamo wa kisiasa wa waalimu katika vyuo vikuu, na uhusiano wa maadili na uhuru wa taaluma. Tulipokuwa tunajadili suala hilo la maadili, profesa mwenzetu mmoja alielezea alivyowahi kukataa kuchora michoro ya kuboresha muundo wa ndege za kivita za jeshi la Marekani.

Kama ilivyokuwa jana, mjadala wa leo ulikuwa mzuri na wa kuelimisha. Nimefurahi kuvisoma vitabu viwili nilivyovitaja hapo juu. Kesho tutajadili Professors and their Politics, kitabu kilichohaririwa na Neil Gross na Solon Simmons.

Monday, August 17, 2015

Kumbukumbu ya Kuzaliwa

Leo ni kumbukumbu ya siku ya kuzaliwa kwangu, ambayo ni tarehe 17 Agosti, 1951. Familia yangu, ndugu, na marafiki wamejumuika nami kusherehekea siku hii. Kati ya hao marafiki, napenda kuwataja wawili wanaoonekana pichani hapa kushoto. Kulia anaonekana Larry Fowler, na kushoto anaonekana Bob Mitchell. Mwaka jana nilipokuwa nimelazwa hospitalini mjini Minneapolis, walifunga safari kuja kuniona. Zikipita wiki mbili tatu hatujaonana, hawakosi kunitafuta. Wanafurahi kupiga gumzo na michapo nami.

Waliniletea ujumbe siku zilizopita, wakisema kuwa siku ya kumbukumbu ya kuzaliwa kwangu wangependa kunipeleka mahali tukale chakula cha mchana. Siku zilivyopita, walikuwa wananikumbusha. Leo, nilipomaliza kufundisha, Larry alinifuata chuoni St. Olaf tukaenda kwenye hoteli ambapo tulipata chakula na kupiga michapo.

Namshukuru Mungu kwa kuniwezesha kuishuhudia siku hii. Ni neema ambayo sistahili. Napaswa kutambua kwamba kila siku katika maisha yangu ni dhamana, niitumie kwa mambo mema. Nizingatie wajibu wa kuvitumia kikamilifu vipaji alivyonipa Mungu kwa manufaa ya wanadamu.

Wengi hawakupata bahati ya kufikia umri niliofikia, lakini wamefanya makubwa, yasiyo kifani. Kama ilivyo kawaida yangu, nawakumbuka hasa waandishi maarufu, kama William Shakespeare, Alexander Pushkin, Ernest Hemingway, na Shaaban Robert. Hawakuishi miaka mingi kama yangu. Kuwafikiria watu kama hao kunanifundisha unyenyekevu. Siwezi kujivunia chochote nilichoweza kufanya, bali ni kumshukuru Mungu na kuendelea kumtegemea.

Inavyoonekana, kila ninaposherehekea kumbumbuku ya siku ya kuzaliwa kwangu, fikra zangu za msingi kuhusu maisha yangu zinajirudia. Ninajikuta nikifananisha mchango wangu ulimwenguni na ule wa watu maarufu, na kukiri kuwa, ingawa ninajitahidi, mchango wangu bado ni hafifu. Nimekuwa nikiandika hivyo katika blogu hii. Hii ni changamoto kwangu, daima na siku zijazo.

Sunday, August 16, 2015

CCM na Suala la Makapi na "Oil Chafu"

CCM inatuambia kuwa hao wanaotoka CCM na kuhamia UKAWA ni makapi au "oil chafu." Kila kukicha tunashuhudia hao wanaoitwa makapi na "oil chafu" wanavyoendelea kumwagikia UKAWA.

Kama hayo wanayosema CCM ni ukweli, basi ni kwamba CCM ni dampo kubwa la takataka. Ndio maana, pamoja na hayo makapi na hiyo "oil chafu" wanavyoendelea kumwagikia nje, CCM inasema iko imara. Kama kweli CCM iko imara, ni wazi CCM ni dampo kubwa la takataka. Unaweza ukachota mkokoteni mzima wa takataka na dampo likabaki salama.

Sasa suali linakuja. Kwa nini miaka yote hii CCM ilikuwa inajinadi kama chama makini, chama safi? Kwa nini CCM ilikuwa inatuambia kuwa ndio chama pekee kinachofaa kuiongoza Tanzania?

Hayo wanayosema CCM sasa yananikumbusha na yanathibitisha aliyoandika Mwalimu Nyerere miaka ya mwisho ya uhai wake, kwamba kuna uozo katika uongozi wa CCM, kwamba kuna kansa katika CCM. Anayetaka kufuatilia suala hilo asome kitabu cha Mwalimu Nyerere kiitwacho Uongozi Wetu na Hatima ya Tanzania, kilichochapishwa Harare mwaka 1993.

Mimi kama raia ambaye si mwanachama wa chama chochote ninachongojea ni Oktoba mwaka huu, CCM ing'olewe madarakani. Tujue moja.

Monday, August 10, 2015

Bendera ya Tanzania Itapepea Faribault, Minnesota, 22 Agosti

Tarehe 22 Agosti, nitashiriki tamasha la kimataifa mjini Faribault, Minnesota. Nimeshalipia gharama. Nitakuwa na meza ambapo nitaweka vitabu vyangu na machapisho mengine.

Hapo nitaongea na watu siku nzima kuhusu shughuli zangu za ufundishaji, utafiti, uandishi, na utoaji ushauri kuhusu athari za tofauti za tamadauni, ushauri ambao ninautoa kwa wanafunzi na waalimu wa vyuo vya Marekani na watu wengine waendao Afrika, taasisi na jumuia zenye mahusiano na wa-Afrika, na kadhalika.

Nitaweka pia mabango ya filamu ya "Papa's Shadow." Filamu hiyo, ambayo ni ya maelezo ("documentary"), kwa kiasi kikubwa ni mazungumzo baina yangu na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee wa Ernest Hemingway aliyebaki. Tunajadili maisha na maandishi ya Ernest Hemingway, hasa yale yanayohusu Afrika. Filamu hii itaanza kuonyeshwa hivi karibuni katika majumba ya sinema na itakuwa inapatikana katika DVD na kadhalika. Kwa taarifa zaidi tembelea tovuti ya Ramble Pictures.

Jambo jingine la pekee ni kuwa, kwa mara ya kwanza tangu kuanzishwa kwa tamasha la kimataifa mjini Faribault, bendera ya Tanzania itapepea, sambamba na bendera za mataifa mengine. Siku chache zilizopita, nilipeperusha bendera hii katika tamasha la Afrifest, mjini Brooklyn Park, kama nilivyoripoti katika blogu hii.

Ninapokuwa Tanzania, ninaweza kuiangalia bendera ya Tanzania nikawa ninaguswa kwa namna fulani, lakini hisia hizo huwa za pekee zaidi huku ughaibuni. Ingekuwa natoka Dar es Salaam kwenda kushiriki tamasha Mtwara, Chake Chake au Mbeya nisingeona sababu ya kubeba bendera ya Tanzania, labda kama tamasha ni la kimataifa. Na hata ningebeba, watu hawangekuwa na duku duku nayo au mshangao. Ni kitu walichozoea.

Lakini mambo ni tofauti huku ughaibuni. Sina namna ya kuelezea vizuri ninachomaanisha. Labda kwa kuwa niko mbali, nina hisia za pekee kuhusu kijiji changu cha Lituru, kata yangu ya Litembo, wilaya yangu ya Mbinga, mkoa wangu wa Ruvuma, na nchi yangu ya Tanzania.

Isipokuwa, jambo moja ni wazi, na linaelezeka: watu watakaohudhuria tamasha mjini Faribault wataiona bendera ya Tanzania. Bendera hii itatokea katika picha mbali mbali watakazopiga siku hiyo na kuzihifadhi, kuwapelekea marafiki au kuziweka mitandaoni.

Sunday, August 9, 2015

Shaaban Robert na Mbaraka Mwinshehe Waliongelea Umuhimu wa Shule

Nikiachilia mbali jinsi wazazi wangu walivyohimiza elimu, nikiachilia mbali jinsi Mwalimu Nyerere alivyohimiza elimu, naukumbuka kwa namna ya pekee mchango wa mwandishi Shaaban Robert na mwanamuziki Mbaraka Mwinshehe katika kuhimiza elimu.

Ninakumbuka jinsi baba yangu, nilipokuwa shule ya msingi, alivyokuwa ananitia msukosuko iwapo nilishindwa kupata 100% katika zoezi lolote au mtihani wowote. Ninakumbuka pia jinsi Mwalimu Nyerere alivyokuwa anahimiza elimu, kwa watu wote, kuanzia watoto hadi wazee, kama nilivyowahi kuandika katika blogu hii.

Shaaban Robert ni mtu anayenifanya nimkumbuke baba yangu. Nilijionea hayo niliposoma kitabu kiitwacho Barua za Shaaban Robert, ambacho habari zake niliziandika katika blogu hii. Humo tunaona jinsi Shaaban Robert alivyokuwa anamhamasisha mdogo wake Yusuf Ulenge afanye bidii katika elimu, akimtimizia mahitaji yote ya shule. Kwa wazazi na walezi, Shaaban Robert ni mfano wa kuigwa.

Mbaraka Mwinshehe, mwanamuziki ambaye wakati wa ujana wangu alitingisha Afrika Mashariki, ya Kati, na Kusini kwa nyimbo na muziki wake, aliimba wimbo maarufu wa kuwaasa vijana wazingatie elimu. Wimbo huo, "Enyi Vijana Sikilizeni," unaweza kuusikiliza hapa:

https://archive.org/details/EnyiVijanaSikilizeni

Saturday, August 8, 2015

Maajabu Katika Siasa Tanzania, 2015

Kuna maajabu mengi katika siasa Tanzania. Mimi si bingwa wa uchambuzi wa mambo hayo, na wala siamini kama kuna bingwa. Ila kila mtu ana uhuru wa kuchambua aonavyo. Oktoba tutaona tuko wapi, na kama uchaguzi utakwenda kiustaarabu, tutawajibika kuyapokea matokeo.

Hebu nirudi kwenye mada yangu ya maajabu ya siasa Tanzania. Edward Lowassa amejitoa CCM na kuibukia CHADEMA (UKAWA). Tayari amezua zogo. Watu wanarusha makombora kwake, kwa CHADEMA, na kwa UKAWA. Wanasema kwa nini CHADEMA impokee mtu ambaye wamekuwa wakimtukana kama fisadi mkubwa.

Ajabu ni kwamba hakuna mahakama yoyote ambayo imemwona Lowassa kuwa fisadi. Amehukumiwa na hisia za watu pamoja na majungu ya magazetini, katika blogu, na vijiweni. Amekosewa haki ya msingi, kwa mujibu wa tangazo la kimataifa la haki za binadamu, haki ya kwamba mtu anayetuhumiwa au kushtakiwa kwa kosa, lazima ahesabiwe kuwa hana kosa hadi mahakama ithibitishe vinginevyo.

Kwa hivi, wote wanaomwita Lowassa fisadi, au waliomwita fisadi (wakiwemo CHADEMA) wajirekebishe. Wamtendee haki Lowassa. Hadi mahakama ithibitishe, Lowassa ana haki ya kuonekana hana kosa, na kuingia kwake CHADEMA hakuna dosari.

Kwa CHADEMA na UKAWA kumkaribisha Lowassa ni sahihi kabisa. Ni jambo la busara CHADEMA wamwombe radhi kwa kumtukana kwa miaka mingi, yaishe. Na yeye ameonyesha roho nzuri kwa kuja kwenye chama chao, bila kinyongo. Ameonyesha moyo unaoendana na mafundisho ya dini yetu ya u-Kristu ya kuwasamehe wanaotutendea mabaya.

Kwa upande wa CCM ni kwamba Lowassa muda wote wamekuwa naye bega kwa bega. Alikuwa mkuu wa idara yao ya mambo ya nje. Hata baada ya kukatwa kwenye uchaguzi wa mgombea urais, hawakumtukana. Lakini ghafla, baada ya yeye kuhamia CHADEMA (UKAWA) wameanza kumtukana, kwamba ni kapi. Vigogo wa CCM wanaohamia upinzani wanatukanwa kwamba ni makapi.

Kwa maana hiyo, hao akina Asha Rose Migiro, Bernard Membe, Mizengo Pinda, January Makamba, Hamisi Kigwangwala, Emmanuel Nchimbi, na wengine, wakae chonjo. Wakae mkao wa kula. Wakitimkia upinzani, hapo hapo watajikuta wanaitwa makapi.

Haya ni kati ya maajabu ya siasa Tanzania

Tuesday, August 4, 2015

Mwandishi Seenaa Aongelea Kitabu Chake Mjini Minneapolis

Juzi Jumapili, nilipata ujumbe wa Facebook kutoka kwa rafiki yangu Peter Magai Bul wa Sudan aishiye Chicago kwamba kuna rafiki yake mwandishi, Seenaa Godana-Dulla Jimjimo, anakuja Minneapolis kuongelea kitabu chake, The In-Between: The Story of African-Oromo Women and the American Experience. Jana, baada ya kumaliza kufundisha na kupumzika kidogo nilikwenda Minneapolis kumsikiliza mwandishi huyu.

Ukumbi ulijaa watu, na karibu wote ni wa-Oromo wanaoishi hapa Minnesota. Nilifurahi kuonana na wanawake wawili na mwanamme mmoja ambao niliwahi kuwafundisha hapa chuoni St. Olaf. Tulifurahi kukutana.

Walikuwepo wazungumzaji watatu ambao waliongelea masuala yanayowahusu wa-Oromo kama vile ukandamizwaji wanaofanyiwa na jeshi la Ethiopia, harakati zao za ukombozi dhidi ya Ethiopia, unyanyaswaji na ukandamizwaji wa wanawake katika jamii ya wa-Oromo. Mzungumzaji mmojawao aliongelea juu ya mwandishi Seenaa na kitabu chake.

Baada ya hapo, mwandishi Seenaa alikaribishwa kuongea. Alielezea mambo muhimu yalyoathiri maisha yake, msukumo alioupata kwa mama yake katika elimu, kujitambua na kujiamini. Aligusiia umuhimu wa wa-Oromo kujituma katika kupigania haki zao na haki na usawa kwa wanawake, akawasihi viongozi wa dini wawe mstari wawemo katika kuihamasisha jumuia katika harakati hizo.  Kufuatia maongezi hayo, mwandishi alijibu masuali ya wasikilizaji.

Hatimaye mwandishi alikaribishwa kusaini vitabu vyake. Watu wengi tulijitokeza tukapanga foleni ya kununua vitabu ili kusainiwa. Nilipokaribia mezani, wanafunzi wangu walinizuia kulipia kitabu, wakalipia wao. Wakati wa kusaini, mwandishi alifurahi sana kuniona, kwani alishaelezwa habari zangu na Peter Magai Bul. Tulifurahi, tukapiga picha kabla na baada ya kusaini.

Nimeanza kukisoma kitabu. Nina hamu ya kujua mawazo na mtazamo wa dada huyu kuhusu masuala yanayowahusu wa-Oromo kuanzia kwao Oromia hadi huku ughaibuni. Inavyoonekana, kwa mujibu wa utangulizi wa kitabu, mwandishi anakwenda mbali ya kuwaongelea wa-Oromo tu. Kwa mfano, kuhusu suala la haki za wanawake, anawaongelea wanawake kwa ujumla, si wa-Oromo tu.

Niliguswa kuona jinsi shughuli ya kukutana na mwandishi na kuongelea kitabu ilivyowavutia watu wengi namna hii. Nilivutiwa na usikivu wao kwa wazungumzaji na masuali waliyouliza. Imenifanya nitambue kuwa hao wenzetu wameelimika na wanathamini elimu. Nimebaki ninajiuliza iwapo wanadiaspora wa ki-Tanzania tuna mwamko huo huo.

Sunday, August 2, 2015

Bendera ya Tanzania Katika Tamasha la Afrifest 2015

Jana, tarehe 1 Agosti, tamasha la Afrifest lilifanyika mjini Brooklyn Park, Minnesota. Hili ni tamasha ambalo huandaliwa mara moja kwa mwaka na bodi ya Afrifest Foundation ambayo mimi ni mwenyekiti wake. ili kuwakutanisha wa-Afrika, watu wenye asili ya Afrika waishio Marekani ya Kaskazini, Kati, na Kusini, pamoja na Caribbean, na pia watu wa mataifa mengine. Lengo kubwa ni kufahamiana, kuelimisha, na kuuenzi mchango wa watu weusi duniani kote, katika nyanja mbali mbali.

Hiyo jana ilikuwa ni mara ya kwanza kwa bendera ya Tanzania kupepea kwenye tamasha la Afrifest. Baada ya kushiriki matamasha na kujionea wenzetu wanavyotumia fursa kuzitangaza nchi zao, nilijiuliza kwa nini nisitafute bendera ya Tanzania, kama nilivyoeleza katika blogu hii.

Hatimaye, nilifanya uamuzi wa kununua bendera, niwe ninaipeperusha kwenye matamasha ninayoshiriki, maadam fursa zipo. Hapo kushoto naonekana na binti zangu Assumpta na Zawadi kwenye meza yetu, hiyo jana.
Sawa na kuweka vitabu mezani katika tamasha, ambavyo huwavutia watu waje kuulizia habari zake, sawa na kutundika bendera ya kampuni yangu ya Africonexion: Cultural Consultants, ambayo nayo huwavutia watu waje kuulizia maana ya Africonexion, bendera hiyo nayo ni kivutio na kianzio cha mazungumzo kuhusu Tanzania.

Miaka yote, nimekuwa nikishiriki matamasha chini ya kivuli cha kampuni yangu ya Africonexion: Cultural Consultants. Hata hivi katika kuelezea shughuli zangu, sikujiwekea mipaka, kwani utafiti wangu, ufundishaji, uandishi na utoaji ushauri katika masuala ya athari za tofauti za tamaduni, nagusia dunia yote, ikiwemo Tanzania. Lakini kuitundika bendera ya Tanzania kama nilivyofanya jana kunaongeza mwonekano wa nchi katika nchi za dunia.

Kwa kuwa bendera hiyo ilipepea hapo uwanjani siku nzima, kila mtu katika umati wa waliohudhuria tamasha aliiona. Wengi wa waliohudhuria walipiga picha hapo uwanjani, na haikwepeki bendera kuonekana katika baadhi ya picha.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...