Sunday, August 16, 2015

CCM na Suala la Makapi na "Oil Chafu"

CCM inatuambia kuwa hao wanaotoka CCM na kuhamia UKAWA ni makapi au "oil chafu." Kila kukicha tunashuhudia hao wanaoitwa makapi na "oil chafu" wanavyoendelea kumwagikia UKAWA.

Kama hayo wanayosema CCM ni ukweli, basi ni kwamba CCM ni dampo kubwa la takataka. Ndio maana, pamoja na hayo makapi na hiyo "oil chafu" wanavyoendelea kumwagikia nje, CCM inasema iko imara. Kama kweli CCM iko imara, ni wazi CCM ni dampo kubwa la takataka. Unaweza ukachota mkokoteni mzima wa takataka na dampo likabaki salama.

Sasa suali linakuja. Kwa nini miaka yote hii CCM ilikuwa inajinadi kama chama makini, chama safi? Kwa nini CCM ilikuwa inatuambia kuwa ndio chama pekee kinachofaa kuiongoza Tanzania?

Hayo wanayosema CCM sasa yananikumbusha na yanathibitisha aliyoandika Mwalimu Nyerere miaka ya mwisho ya uhai wake, kwamba kuna uozo katika uongozi wa CCM, kwamba kuna kansa katika CCM. Anayetaka kufuatilia suala hilo asome kitabu cha Mwalimu Nyerere kiitwacho Uongozi Wetu na Hatima ya Tanzania, kilichochapishwa Harare mwaka 1993.

Mimi kama raia ambaye si mwanachama wa chama chochote ninachongojea ni Oktoba mwaka huu, CCM ing'olewe madarakani. Tujue moja.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...