Sunday, July 31, 2016

Ujumbe kwa Rais Magufuli: Shirikiana na UKAWA

Mheshimiwa Rais Magufuli, salaam na pole kwa majukumu ya kutumbua majipu. Mimi ni raia wako, ambaye si mwanachama wa chama chochote cha siasa. Nimeona nikuandikie, ingawa ninajua kuwa jadi ya ovyo iliyojengwa na chama chako cha CCM ni ya kutotambua uwepo wa sisi raia tusio na vyama. CCM imekuwa na historia ya kutotambua kuwa sisi tusio na chama ni raia wenye haki sawa katika nchi yetu, na wenye akili na mitazamo kuhusu mustakabali wa nchi yetu. Achana na hii jadi. Itakuponza.

Ninaandika ujumbe huu kukushauri ushirikiane na UKAWA. Nina sababu za kukushauri hivyo. Kwanza, kumbuka kwamba tangu ulipoingia madarakani kama rais, UKAWA walionyesha mapenzi yao kwako kwa dhati, wakadiriki kutangaza mara kwa mara kwamba ulikuwa unatekeleza ajenda yao. Mheshimiwa Rais Magufuli, hakuna hazina kubwa kwa kiongozi kama kukubalika kiasi hiki. Na katika nchi yenye wapinzani, kuweza kuwakonga nyoyo zao kama ulivyofanya ni jambo la pekee. Ni baraka uliyojaliwa. Tafadhali usiifuje.

Sisemi ujiunge na UKAWA. Wewe ni mwana-CCM, na una uhuru na haki kikatiba ya kubaki CCM. Lakini kumbuka uliyokuwa umeyaona katika CCM wakati wa kampeni za urais. Ulitamka tena na tena kwamba ndani ya CCM wako ambao ni CCM mchana, lakini usiku wanakuwa UKAWA. Kwa maana hiyo, uko katika chama ambacho ni kitendawili.

Nimepata taarifa kuwa siku za karibuni umekuwa ukisema kwamba hao ndumilakuwili waliomo CCM utawafagia kwa fagio la chuma. Laiti kama ungeweza kufanya hivyo. Laiti kama ningekuwa na namna ya kukusaidia kufanikisha azma hiyo. Kwa bahati mbaya, sina uwezo kabisa. Kwa bahati mbaya, nawajibika kukueleza kuwa hata wewe itakuwia shida sana kuwagundua ndumilakuwili hao.

Hao ni ndumilakuwili wazoefu. Wamekubuhu katika sanaa ya kujivika ngozi ya kondoo. Ni wazoefu wa kupalilia unga. Watakuhadaa daima kwa kujifanya ni watu wako, kumbe usiku wanakubomoa. Kumbuka usemi wa wahenga, kwamba kikulacho ki nguoni mwako. Hii ndio sababu nyingine ya mimi kukushauri ushirikiane na UKAWA.

Wewe mwenyewe, na sisi wote tunafahamu, kuwa wako CCM wenzako ambao ni wafuasi wa Lowassa. Wamejichimbia CCM. Wanaendelea kula bata huko CCM, ilhali ni wafuasi wa Lowassa. Lowassa mwenyewe amethibitisha kuwa ana wafuasi wake huko CCM na amewahimiza waendelee mshikamano naye na kumpa taarifa.

Sasa, Mheshimiwa Rais, unahitaji ushahidi gani zaidi kwamba huko CCM umekalia kuti bovu? Hata hivyo, kama nilivyosema, ninatambua haki na uhuru wako wa kuwemo katika chama ukipendacho. Una haki na uhuru wa kuwemo CCM. Siwezi kuingilia haki yako na uhuru wako.

Lakini ushauri wangu kwamba ushirikiane na UKAWA unaweza kuwa ndio njia bora ya wewe kufanikisha majukumu yako uliyoazimia. Ukiwa karibu na UKAWA, UKAWA wataendelea kukuunga mkono kama walivyofanya tangu ulipoingia madarakani.

Ninahisi kwamba kadiri watakavyozidi kukuamini, itakuwa rahisi kwako kuwashawishi wakutajie hao ndumilakuwili waliomo CCM, ambao wamevaa magwanda na vikofia vya CCM, lakini ni wakereketwa "orijino" wa Lowassa. Tafakari hilo, Mheshimiwa Rais Magufuli. Ninaona kuna mazuri mbele ya safari, iwapo utaanza kushirikiana na UKAWA.

Halafu, kumbuka kwamba hao UKAWA si maadui zako. Wanacholilia ni wewe kuwaacha wafanye shughuli zao kwa mujibu wa katiba, ikiwemo mikutano na maandamano ya amani. Ni hicho tu, Mheshimiwa Rais. Wanachohitaji ni demokrasia kama ilivyotamkwa katika katiba.

Kumbuka, Mheshimiwa Rais, ulikula kiapo cha kuilinda na kuitetea katiba ya Tanzania. Kwa kuwa wanachotaka UKAWA ni wewe kuzingatia katiba ambayo uliapa kuilinda na kuitetea, tatizo liko wapi? Ulikula kiapo cha kuitetea katiba, lakini kwa jinsi CCM, vyombo vya dola, na wewe mwenyewe mnavyosuasua, mtu anaweza kudhani kuwa labda wewe na serikali yako mlikula kiapo cha kutetea kitabu cha hadithi za Abunuwasi.

Sasa hivi, CCM wanaonekana wakijibidisha kutekeleza kauli mbiu yako ya Hapa Kazi Tu. Tunawashuhudia wanavyoshindana katika kupiga huu mzigo. Lakini, kama nilivyosema, kumbuka kuwa si wote wako nawe kwa dhati. Wako ambao ni wazoefu wa kupalilia unga. Wanakuwa CCM mchana, na usiku wanakuwa UKAWA.

Saturday, July 30, 2016

Serikali ya CCM na Mikutano ya Kisiasa

Katika siku hizi chache, tumeshuhudia ubabe wa CCM na serikali ya CCM ambao ni hujuma dhidi ya haki za binadamu. Baada ya UKAWA kutangaza azma yao ya kufanya mikutano na maandamano ya amani nchi nzima (Tanzania) tumesikia kauli za vitisho kutoka kwa CCM na serikali yake.


Napenda kusema kuwa ninapinga msimamo wa CCM na serikali ya CCM kuhusu suala hilo kwa sababu ni hujuma dhidi ya haki za binadamu. Katiba ya Tanzania, ya mwaka 1977, 20 (1) imeweka wazi msimamo wake:

Every person has the freedom to freely and peaceably assemble, associate and cooperate with other persons, and for that purpose, express views publicly and to form and join with associations or organizations formed for purposes of preserving or furthering his beliefs or interests or any other interests.

Tamko hili la katiba ya Tanzania linaendana na tangazo la kimataifa la haki za binadamu ("The Universal Declaration of Human Rights"), vifungu namba 18, 19, 20, na 21. Nashauri kila mtu ajisomee, kwani tangazo liko sehemu mbali mbali mtandaoni.

Tumemsikia msemaji wa CCM akitoa vitisho kwa watu wa UKAWA kuhusu azma yao ya kuandamana, na amesema kuwa watakaofanya hivyo waende na wake na watoto wao kwenye mstari wa mbele wa maandamano. Kisha amewaagiza polisi wajiandae.


Huyu mheshimiwa anahitaji kuelimishwa. Asome maneno ya katiba ya Tanzania niliyonukuu hapa juu, na mengine ambayo sijanukuu, ambayo yanatamka wazi kuwa mtu hashurutishwi kushiriki mambo ya vyama vya siasa. Ni hiari. Kwa maana hiyo, kauli ya huyu msemaji wa CCM ni ya kijinga.


Mtu akiwa mwanachama wa chama cha siasa hana uwezo wala ruhusa kwa mujibu wa katiba ya Tanzania kumshinikiza mwenzake. Kila mtu ana uhuru wake na haki zake. Anaweza kuwa mke wa mtu wa chama fulani, lakini yeye akawa wa chama kingine, au akawa hana chama. Kauli ya msemaji wa CCM ni ya kijinga.


Msemaji wa CCM anadhihirisha jinsi alivyo na fikra za kimfumo dume, kwamba mume ni kama mtawala mwenye wadhifa wa kuamuru mke wake afuate anayotaka yeye. Dunia ya leo inasisitiza kuheshimu haki sawa kwa wanawake na wanaume. Huyu msemaji wa CCM anawafundisha nini watoto wa Tanzania? Lakini huyu ndiye ambaye CCM imemwona kuwa anafaa kuwa msemaji wake. Ni mpeperusha bendera wa CCM. Ni shida kweli.


Msemaji huyu amedhihirisha wazi kuwa anayahusisha maandamano na vurugu na hata umwagaji damu. Hajatoa mfano wowote kuthibitisha jambo hilo. Ni lini waandamaji wa Tanzania waliandamana wakiwa na silaha, wakasababisha vurugu na umwagaji damu? Wenye historia ya kubeba silaha na kuvuruga maandamano ya kisiasa ambayo ni ya amani, na hata kujeruhi na kuua waandamanaji wasio na hatia wanafahamika.


Juu ya yote, msemaji wa CCM anapaswa kuwa mstari wa mbele kuwaelimisha raia juu ya haki na wajibu wao katika maandamano. Asisitize kuwa katiba ya Tanzania inatambua haki na uhuru wa watu kufanya mikutano na maandamano kwa amani. Serikali ya CCM iheshimu katiba ya Tanzania. Iheshimu haki za binadamu.


Tanzania ni nchi yenye heshima tangu ilikotoka. Uvunjwaji wa haki za binadamu unaiharibia heshima nchi yetu, na mzalendo yeyote hawezi kuafiki jambo hilo.

Wednesday, July 27, 2016

Tumejadili "Valley Song," Tamthilia ya Athol Fugard

Leo katika darasa langu la African Literature, tumejadili Valley Song, tamthilia ya Athol Fugard, mwanatamthilia maarufu wa Afrika na ulimwenguni. Alizaliwa Afrika Kusini mwaka 1932. Ametunga tamthilia nyingi ambazo kwa ujumla wake ni kama rekodi ya yale ambayo Afrika Kusini imepitia kisiasa, kijamii, na kitamaduni. Kitabu chake cha Notebooks: 1960-1977 ni hazina ya kumbukumbu zake za kukua kwake kama msanii, falsafa yake ya sanaa, na tathmini yake ya wasanii mbali mbali kama vile Samuel Beckett, Bertolt Brecht, na Albert Camus.

Nimefundisha tamthilia kadhaa za Fugard, na ninaguswa zaidi na zaidi na kazi zake. Miaka ya karibuni, kwa mfano, nimejikuta ninafundisha Sorrows and Rejoicings tena na tena. Baadaye niliamua kufundisha tamthilia ambayo sikuwahi kuifundisha, nikachagua Valley Song.

Valley Song inahusu familia ya Buks, mkulima chotara nchini Afrika Kusini . Anaonekana tangu mwanzo akiwa ameshika mbegu za maboga. Ni mkulima anayefurahia kuona mbegu zinavyoota shambani, kustawi na kuzaa mazao. Lakini, anakabiliana na matatizo kadhaa. Kwa mfano, binti yake alitorokea mjini, ambako alifariki katika mazingira ya kutatanisha, akiwa ameacha mtoto mchanga aitwaye Veronika.

Ana wasi wasi kwamba atapoteza shamba na nyumba yake kutokana na kishawishi cha wazungu wenye fedha wanaofika fika kuangalia shamba na nyumba hiyo.  Juu ya yote, Veronika, ambaye sasa ni msichana mkubwa, anasema tena na tena kuwa anataka kwenda mjini akawe mwimbaji maarufu. Hapendi kuendelea kuishi shamba ambapo anaona hakuna fursa kama mjini.

Ndoto hii ya Veronika inamsumbua Buks, kwani anawazia jinsi binti yake alivyotorekea mjini na kufariki huko.  Hata hivyo, baada ya kumsikiliza sana Veronika, anamwacha aende. Dhamira ya jinsi mbegu za maboga zinavyoota na kustawi na kuzaa maboga makubwa makubwa inahusishwa na ndoto ya Veronika ya kukuza kipaji chake cha uimbaji na kisha kuwa na mafanikio makubwa.

Valley Song inaishia kwa matumaini ya namna hiyo, ambalo ni jambo jema lenye kugusa mioyo yetu. Tamthilia hii, ingawa fupi, ni uthibitisho mwingine wa kipaji cha Fugard kama msanii mwenye ufahamu wa kina wa uhalisia wa maisha, majaribu yake na uwezo wa binadamu wa kupambana nayo.

Friday, July 22, 2016

CCM: Ni Chama cha Mapinduzi?

Makala ninayoleta hapa niliichapisha mwaka 2008 katika blogu hii. Ninaileta tena hapa ili kuchochea tafakari, hasa kwa wakati huu ambapo mkutano mkuu wa CCM unafanyika Dodoma.
-------------------------------------------------------------------------------------------------------------

CCM: Ni Chama cha Mapinduzi?

Sielewi kwa nini watu wanaamini kuwa CCM ni chama cha mapinduzi. Sijawahi kuelewa na bado sielewi kwa nini. Dhana ya mapinduzi ilielezwa vizuri na TANU, katika "Azimio la Arusha," "Mwongozo," na maandishi, hotuba na mahojiano mbali mbali ya Mwalimu Nyerere. Matokeo ya yote hayo ni kuwa Watanzania tulifahamu vizuri na kukubali dhana na maana ya mapinduzi katika nchi yetu. Yeyote ambaye hajasoma maandishi hayo, au kusikiliza hotuba hizo, ningemshauri afanye hivyo, ili aweze kufahamu msingi wa ujumbe wangu.

CCM ilipoanza, ilijinadi kuwa ni chama cha mapinduzi. Lakini baada ya muda si mrefu, mwelekeo wake ulijionyesha kuwa si wa mapinduzi. Badala ya kuendeleza fikra na mwelekeo wa "Azimio la Arusha," "Mwongozo" na mengine yote niliyoyataja hapo juu, CCM ilitoa "Azimio la Zanzibar." Ingawa CCM haikutoa fursa iliyostahili kwa wananchi kuliangalia na kulijadili "Azimio la Zanzibar," habari zilizojitokeza ni kuwa Azimio hili lilikiuka yale yaliyokuwemo katika "Azimio la Arusha." Mwalimu Nyerere alilishutumu "Azimilo la Zanzibar" kwa msingi huo.

Kitu kimoja kilichokuja kufahamika wazi ni kuwa "Azimio la Zanzibar" lilibadilisha masharti ya uongozi yaliyokuwemo katika "Azimio la Arusha" na "Mwongozo." Kwa mfano, "Azimio la Zanzibar" liliondoa miiko ya uongozi iliyokuwepo.

Baada ya CCM kuvunja misingi ya mapinduzi, kilichofuatia ni kuimarika kwa ubepari, matabaka, na ufisadi. Chini ya himaya ya CCM, "Azimio la Arusha" halisikiki, "Mwongozo" hausikiki, wala maandishi na hotuba zingine zilizofafanua maana ya mapinduzi hazisikiki. Inaonekana kuwa CCM ilikusudia tangu mwanzo kuwafanya watu wasahau hayo yote, ili iendelee na sera za kujenga ukoloni mamboleo nchini mwetu.

Inakuwaje basi CCM ijiite chama cha mapinduzi wakati inahujumu mapinduzi? Inakuwaje Watanzania hawahoji jambo hilo? Elimu ni ufunguo wa maisha; bila elimu kuna hatari ya kurubuniwa na kuburuzwa kama vipofu.

CHANZO: blogu ya hapakwetu.

Wednesday, July 20, 2016

Ki-Ingereza cha Shakespeare

Miaka mia nne imepita tangu alipofairki Walliam Shakespeare. Lakini dunia haiwezi kumsahau, kwa mchango wake uliotukuka katika utunzi wa tamthilia na mashairi. Leo, ninarejea tena kwenye mada hii ya mchango wa Shakespeare, ambayo nimekuwa nikiiongelea katika blogu hii. Napenda kujikumbusha suala la ki-Ingereza cha Shakespeare.

Kumbukumbu hii imenijia leo kwa sababu maalum. Leo, katika kozi yangu ya African Literature, nimeanza kufundisha The Dilemma of a Ghost, tamthilia ya Ama Ata Aidoo. Nimeongelea mistari nane ya mwanzo ya "Prologue," yaani utangulizi, nikataja mambo mengi, kuanzia "folklore" hadi tamthilia za Shakespeare. Mistari hiyo ni hii:

I am the Bird of the Wayside--
The sudden scampering in the undergrowth,
Or the trunkless head
Of the shadow in the corner.
I am the asthmatic old hag
Eternally breaking the nuts
Whose soup, alas,
Nourished a bundle of whitened bones--

Miaka yetu, tulipokuwa tunasoma sekondari,  ambayo kwangu ilikuwa ni 1967-70, tulisoma na kuelewa ki-Ingereza cha Shakespeare. Tulipokutana na maneno magumu au misemo isiyoeleweka, tulifuatilia hadi kuelewa. Aghalabu, maelezo yalikuwemo katika vitabu tulivyokuwa tunasoma. Vinginevyo, tuliangalia kamusi. Tulikuwa na tabia ya kujituma.

Utamu wa ki-Ingereza cha Shakespeare unaonekana katika maandishi yake yote. Humo tunaona nidhamu ya hali ya juu katika matumizi ya maneno na uundaji wa sentensi. Kila neno lina umuhimu, na limewekwa mahali panapostahili. Hakuna sehemu inayolegalega.

Kumsoma Shakespeare ni chemsha bongo. Ni kunoa akili, sio tu kutokana na namna Shakespeare anavyotumia lugha bali pia kutokana na ukweli kuwa Shakespeare ndiye aliyekuwa na msamiati mkubwa kuliko mtumiaji mwingine yeyote wa ki-Ingereza. Hapa naleta mfano kutoka katika tamthilia yake ya Hamlet, ambayo nimeikumbuka leo kwa namna ya pekee, ili angalau wale tuliosoma zamani tujikumbushe enzi zile, ambapo shule ilikuwa shule kweli:

ACT I SCENE III A room in Polonius' house.
[Enter LAERTES and OPHELIA]
LAERTESMy necessaries are embark'd: farewell:

And, sister, as the winds give benefit

And convoy is assistant, do not sleep,

But let me hear from you.
OPHELIADo you doubt that?
LAERTESFor Hamlet and the trifling of his favour,

Hold it a fashion and a toy in blood,

A violet in the youth of primy nature,

Forward, not permanent, sweet, not lasting,

The perfume and suppliance of a minute; No more.
OPHELIANo more but so?
LAERTESThink it no more;10

For nature, crescent, does not grow alone

In thews and bulk, but, as this temple waxes,

The inward service of the mind and soul

Grows wide withal. Perhaps he loves you now,

And now no soil nor cautel doth besmirch

The virtue of his will: but you must fear,

His greatness weigh'd, his will is not his own;

For he himself is subject to his birth:

He may not, as unvalued persons do,

Carve for himself; for on his choice depends20

The safety and health of this whole state;

And therefore must his choice be circumscribed

Unto the voice and yielding of that body

Whereof he is the head. Then if he says he loves you,

It fits your wisdom so far to believe it

As he in his particular act and place

May give his saying deed; which is no further

Than the main voice of Denmark goes withal.

Then weigh what loss your honour may sustain,

If with too credent ear you list his songs,30

Or lose your heart, or your chaste treasure open

To his unmaster'd importunity.

Fear it, Ophelia, fear it, my dear sister,

And keep you in the rear of your affection,

Out of the shot and danger of desire.

The chariest maid is prodigal enough,

If she unmask her beauty to the moon:

Virtue itself 'scapes not calumnious strokes:

The canker galls the infants of the spring,

Too oft before their buttons be disclosed,40

And in the morn and liquid dew of youth

Contagious blastments are most imminent.

Be wary then; best safety lies in fear:

Youth to itself rebels, though none else near.

Sunday, July 17, 2016

Nimealikwa Maoneshoni Faribault, Minnesota

Jana nilipigiwa simu ambayo sikutegemea. Ilitoka kwa mjumbe wa kamati ya maandalizi ya International Festival Faribault. Hayo ni maonesho ya tamaduni za kimataifa yanayofanyika kila mwaka mjini Faribault, Minnesota. Mtu aliyenipigia simu alikuwa ananiulizia iwapo ninapangia kushiriki maonesho mwaka huu, ili wanitengee meza.

Nimewahi kuhudhuria maonesho haya miaka iliyopita, na nimekuwa nikiandika taarifa zake katika blogu hii. Nimekuwa nikishiriki kama mwandishi na mwalimu, nikiwa na meza ya vitabu vyangu na machapisho mengine. Hapo ninaongea na watu juu ya shughuli zangu za uandishi, ufundishaji, na utoaji ushauri kuhusu tofauti za tamaduni na athari zake katika ulimwengu wa utawandazi wa leo.

Kila mara, nimekuwa nikifuata utaratibu wanaofuata washiriki wengine, yaani kupeleka maombi kabla kwa kujaza fomu na kuipeleka, pamoja na malipo. Kutokana na jadi hiyo, niliguswa kupigiwa simu jana. Nilipata hisia kuwa waandaaji wa maonesho wanathamini ushiriki wangu, nami nitakuwa nao bega kwa bega.

Nitaandaa vitabu vyangu na machapisho mengine, na nitapata fursa ya kukitangaza kwa mara ya kwanza kwenye tamasha hili kitabu changu kipya, mwongozo wa Song of Lawino. Vile vile, kwa kuwa tamasha hili ni fursa kwa watu kuzitangaza nchi na tamaduni zao, nitachukua pia bendera ya Tanzania, ambayo niliitafuta kwa madhumuni ya aina hiyo, kama nilivyowahi kuandika katika blogu hii.

Tuesday, July 12, 2016

Hemingway Auneemesha Mji wa Pamplona kwa Utalii

Wiki hii mji wa Pamplona nchini Hispania unafurikwa na maelfu ya watalii kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Ni kwa nini? Ni kwa sababu ya jadi ya tangu karne kadhaa zilizopita ya kusherehekea tamasha liitwalo San Fermin. Sherehe hizi hufanyika kila mwaka wakati huu wa Julai. Kati ya mambo yanayofanyika ni michezo ya kukimbizana na mafahali ("running of the bulls") na michezo ya kupambana na mafahali ("bull-fighting"), kama nilivyogusia katika blogu hii.

Ingawa jadi hii iko katika miji mingi nchini Hispania, dunia inafahamu zaidi Pamplona. Hii inatokana na mwandishi maarufu Ernest Hemingway. Baada ya kushuhudia tamasha hili mjini Pamplona kuanzia mwaka 1923, hasa hiyo "running of the bulls" na "bull-fighting," alivutiwa sana, akaielezea kwa ustadi katika riwaya yake ya kwanza The Sun Also Rises.

Ingawa ilikuwa ni riwaya yake ya kwanza, The Sun Also Rises ilimjengea Hemingway umaarufu kama mwandishi. Ulimwengu ulivutiwa na bado unavutiwa na usimuliaji wake, na hapo ndipo umaarufu wa tamasha la Pamplona ulipozuka na kusambaa. Tangu mwaka ule 1926 ilipochapishwa The Sun Also Rises hadi leo, mji wa Pamplona umeendelea kuifunika miji mingine kwa kuvutia watalii.

Hii si mara yangu ya kwanza kuongelea jinsi watu wengine ulimwenguni wanavyoneemeka kwa kutumia maandishi na jina la Hemingway kama kivutio cha utalii. Cuba ni mfano mojawapo. Hemingway huyu huyu alitembelea Tanganyika na sehemu zingine za Afrika Mashariki. Aliandika kitabu maarufu cha Green Hills of Afrika kuhusu mizunguko yake nchini Tanganyika, akiwinda kwenye mbuga kama Serengeti, Ngorongoro, Manyara, na Tarangire, akapita maeneo kama Babati, Kondoa, Handeni, na Tanga. Hiyo ilikuwa katika mizunguko yake ya mwaka 1933-34.

Katika mizunguko yake ya mwaka 1953-54, Hemingway alipita kwenye maeneo mengine pia kama vile Iringa na Mwanza. Katika barua zake, ziko ambazo zilitumwa kutoka kwenye posta za Tanganyika, kama vile John's Corner na Arusha. Hivi karibuni, nilipokwenda kuzuru maktaba ya J.F. Kennedy, lengo langu moja lilikuwa kuziona barua ambazo Hemingway aliandika alipokuwa maeneo haya. Nilikuwa nimezisoma zikiwa zimepigwa chapa vitabuni, lakini nilitaka kuona hati ya mkono wake.

Hizi ni taarifa ambazo zinahitaji utafiti na kisha kuzitumia kama wanavyofanya wenzetu. Nimepata hamasa ya kuandika ujumbe huu leo kwa kuwa huu ni wakati muafaka, ambapo ninafuatilia mambo yanayofanyika Pamploma wiki hii.


Sunday, July 10, 2016

Kumbukumbu na Picha Nilizopiga na Edwin Semzaba

Naleta kumbukumbu na picha za Edwin Semzaba nami, tulizopiga Chuo kikuu Dar es Salaam, mwaka 2010. Tulipiga picha hizi nje ya ofisi yake kwenye majengo ambayo miaka tulipokuwa tunasoma katika chuo hicho, 1973-76, yalikuwa idara ya "Estates."

Semzaba tulisoma darasa moja, tangu Mkwawa High School, 1971-72, ambapo tulikuwa katika kikundi cha michezo ya kuigiza. Semzaba alikuwa na kipaji sana cha kuigiza. Kuna picha tulipiga tukiwa wanafunzi wengi, ambao baadhi yao nawakumbuka, kama vile Rajabu Mwajasho, Yusuf Ngororo, Jumbe, Hashim Mvogogo, Edwin Semzaba, Edward Jambo, Mathias Chikawe, na Gondwe.

Kimasomo, Mkwawa ilikuwa maarufu. Nusu ya darasa letu tuliingia Chuo Kikuu Dar es Salaam, mwaka 1973. Semzaba na mimi tulisoma "Literature," tukifundishwa na Grant Kamenju, Mofolo Bulane, Gabriel Ruhumbika, William Kamera,  Keorapetse Kgositsile. Kulikuwa pia wahadhiri chipukizi: Ismael Mbise, Clement Ndulute, na Christon Mwakasaka.
  
Walikuja pia walimu kama Stephen Arnold wa Chuo Kikuu cha Alberta, Canada; Stephen Sorkin wa Chuo Kikuu cha Indiana, Marekani; na Phanuel Egejuru. kutoka Nigeria. Pia tulitembelewa na kufundishwa na Stanley Mitchell wa Uingereza, Alex La Guma, mwandishi maarufu wa Afrika Kusini aliyekuwa anaishi u-Ingereza, na George Lamming, mwandishi maarufu wa Barbados aliyekuwa anaishi u-Ingereza.

Tukiwa wanafunzi wa mwaka wa pili, tulisoma riwaya ya Lamming, In the Castle of my Skin katika kozi aliyotufundisha Grant Kamenju. Wakati Lamming alipokuwa anatufundisha kuhusu uandishi wa Caribbean, ninakumbuka kuwa nilifanya mahojiano naye, nikishirikiana na Semzaba, na mahojiano haya yalichapishwa katika gazeti la "Sunday News," kama sikosei.

Nakumbuka tulipiga picha ya darasa zima, tukiwa na George Lamming na mwalimu wetu Grant Kamenju. Tulikuwa sisi wanafunzi wa mwaka wa pili na wengine wa mwaka wa tatu. Baadhi ya hao wa mwaka wa tatu walikuwa wa-Tanzania, kama vile Mugyabuso Mulokozi na wa-Kenya kama vile Alice Bulogosi. Bahati mbaya sijui nakala yangu ya picha ile iko wapi.

Pamoja na "Literature," Semzaba alisomea "Theatre Arts," akifundishwa na Bob Leshoai, Ebrahim Hussein, Louis Mbughuni, Penina Mhando, Godwin Kaduma, na Amandina Lihamba. Mimi sikusomea "Theatre Arts," bali ki-Ingereza, nikifundishwa na waalimu kama Pauline Robinson, Trevor Hill, na Derek Nurse.

Katika somo la "Literature," tulikuwa tunapenda sana kunukuu misemo maarufu na ile ya kuchekesha iliyokuwemo katika riwaya kama The Ragged Trousered Philanthropists ya Robert Tressell, na tamthilia kama Purple Dust ya Sean O'Casey. Semzaba alikuwa anapenda sana jambo hilo.

Maongezi na Semzaba daima yalikuwa ya kuburudisha roho na akili, kwani alikuwa na kipaji cha kuongea, kuchekesha, na kucheka. Kicheko chake kilisababisha wengine mcheke. Hata kama mtu ulikuwa na wingu mawazoni, kama ulikutana na Semzaba, ilikuwa lazima uburudike na kufurahi. Mungu alimjalia haiba hiyo.

Tulihitimu shahada ya kwanza mwaka 1976, tukaajiriwa kufundisha pale pale Chuo Kikuu, Semzaba akiwa idara ya "Theatre Arts" na mimi idara ya "Literature." Kwa bahati mbaya, muda mfupi tu baada ya kuajiriwa, Semzaba alianza kuugua akiwa na matatizo ya miguu. Ilibidi aende nyumbani kuuguzwa kwa miezi mingi.

Familia yake walikuwa wanaishi Dar es Salaam, katika jengo mojawapo la ghorofa pembeni mwa barabara ya Morogoro, linalotazamana na kituo cha zimamoto. Nilikwenda hapo kumjulia hali, nikafahamiana vizuri na mdogo wake ambaye jina lake nimesahau.

Nimeona niandike kumbukumbu hizi chache za rafiki yangu Edwin Semzaba. Baada ya mimi kuja kufundisha Chuo cha St. Olaf huku Marekani, nilipata fursa ya kumleta Semzaba huko Pacific Lutheran University katika programu ya LCCT mwaka 1999. Alikuwa rafiki yangu tangu ujana wetu hadi mwisho wa maisha yake.

Nilipokuwa ninakwenda Tanzania na kufika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, nilikuwa ninampitia Semzaba. Alikuwa ananielezea habari za uandishi wake na hali ya vitabu, uchapishaji, na kadhalika nchini Tanzania. Siku tulipopiga picha hizi, kwenye mwezi Julai au Agosti, 2010, alinielezea tuzo alizopata, na ndiyo siku aliponipa nakala ya kitabu chake, Marimba ya Majaliwa, kama nilivyoandika katika blogu hii. Ninaonekana nimeshika kitabu hicho katika picha hapa kushoto.

Sunday, July 3, 2016

Ninasoma " The Sun Also Rises"

Kwa  sasa, katika usomaji wangu wa maandishi ya Ernest Hemingway, ninatumia muda mwingi zaidi katika kusoma The Sun Also Rises. Hii ni baada ya kusoma A Moveable Feast, ambayo niliiongelea katika blogu hii.

Ingawa sikuwahi kusoma The Sun Also Rises, nilikuwa nimesoma habari zake. Nilikuwa ninafahmu umaarufu wa riwaya hii na niliwahi kuiongelea katika blogu hii. Nilifahamu, kwa mfano, kwamba riwaya hii inawaongelea wa-Marekani waliokuwa wanaishi Paris na walijulikana kama "the lost generation," yaani kizazi kilichopotea. Katika A Moveable Feast, nilisoma kuwa Gertrude Stein aliwaita hivyo wa-Marekani hao.

Nilikuwa ninafahamu pia kuwa The Sun Also Rises ndio riwaya iliyoupa umaarufu mji wa Pamplona wa Hispania, kwa jinsi Hemingway alivyoielezea jadi ya mji huo ya sikukuu ya San Fermin, ambapo kunafanyika mchezo wa kukimbizana na mafahali ("running of the bulls") na mchezo wa kupambana na mafahali ("bull fighting.") Katika "running of the bulls," mafahali huachiwa katika mtaa mwembamba mjini kuwafukuza watu waliojazana humo, ambao hutimka mbio, huku mafahali wakiwafukuza na kuwashambulia. Watu wengi huumizwa na baadhi kubaki mahututi na mara moja moja hata kufa. Ni mchezo unaopendwa sana.

Katika mchezo wa kupambana na mafahali, wanaume waitwao "matador" hutokea uwanjani kwa utaratibu maalum, na kukabiliana na fahali kwa mbinu mbali mbali kama inavyoeleza hapa. Taratibu na sheria za mchezo huu zimekuwa zikibadilika na kutofautiana katika vipindi mbali mbali vya historia na sehemu mbali mbali za dunia. Hutokea fahali anafanikiwa kumjeruhi "matador," pengine vibaya sana. Hemingway aliipenda sana michezo hii ya hatari, kwani alithamini na kusifia ushujaa.

Sasa ni fursa yangu kujisomea mwenyewe The Sun Also Rises, riwaya ambayo imeufanya mji wa Pamplona kuwa maarufu wenye kuvutia idadi kubwa ya watalii. Tayari nimeona jinsi Hemingway anavyoelezea mji wa Paris na maisha ya watu miaka ile ya elfu moja mia tisa na ishirini na kitu. Maelezo yake yananikumbusha A Moveable Feast. Nimekuta pia sehemu katika The Sun Also Rises ambapo mhusika mkuu anamwambia mwenzake kuhusu Afrika. 

Kutokana na jinsi ninavyofuatilia uhusiano wa Hemingway na Afrika, nimefurahi kukutana na taarifa hii katika The Sun Also Rises. Wakati alipoandika riwaya hii, Hemingway alikuwa bado hajasafiria Afrika, bali alikuwa anafahamu habari zake kutokana na kusoma vitabu kama Batouala cha Rene Maran na maandishi ya rais wa Marekani mstaafu Teddy Roosevelt ambaye, mwaka 1909, alikuwa amefanya safari ya miezi mingi ya uwindaji nchini Kenya.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...