Showing posts with label Lugha. Show all posts
Showing posts with label Lugha. Show all posts

Saturday, May 27, 2017

"Witchcraft by a Picture" (John Donne)

Juzi, nilinunua kitabu cha mashairi kiitwacho The Works of John Donne, kama nilivyosema katika blogu hii. John Donne aliishi Uingereza, hasa London, miaka ya 1572-1631.

Katika kuyasoma mashairi yake, nimeona kuwa yanahitaji utulivu wa pekee, na tafakari, kwani matumizi yake ya lugha yanaonyesha uangalifu mkubwa. Ki-Ingereza chake ni cha miaka ile, ambayo ni miaka ya William Shakespeare, si cha leo. Hapa naleta shairi mojawapo, "Witchcraft by a Picture." Labda siku moja nitapata ujasiri wa kujaribu kulitafsiri kwa ki-Swahili.



         Witchcraft by a Picture

I fixe mine eye on thine, and there
     Pitty my picture burning in thine eye,
My picture drown'd in a transparent teare,
     When I looke lower I espie;
          Hadst thou the wicked skill
By pictures made and mard, to kill,
How many wayes mightst thou performe thy will?

But now I have drunke thy sweet salt teares,
     And though thou poure more I'll depart;
My picture vanish'd, vanish feares,
     That I can be endamag'd by that art;
          Though thou retaine of mee
One picture more, yet that will bee,
Being in thine owne heart, from all malice free.

Wednesday, March 15, 2017

Maktaba ya Chuo Kikuu cha Minnesota

Mara kwa mara, ninaandika kuhusu maktaba ninazozitembelea, hapa Marekani na Tanzania. Mifano ni maktaba ya John F. Kennedy,  ya Brookdale, ya Southdale, ya Moshi, ya Tanga, ya Iringa, ya Dar es Salaam, na ya Songea.

Jana, nilikuwa Minneapolis kwa shughuli binafsi. Baadaye niliingia katika maktaba ya Wilson. Nimezoea kwenda kusoma katika maktaba hii, ambayo ni moja ya maktaba za Chuo Kikuu cha Minnesota. Kati ya hizo, hii ndio inayonihusu zaidi, kwa sababu humo ndimo kuna majarida, vitabu, na hifadhi za lugha na fasihi.

Ingawa chuoni St. Olaf ninapofundisha pana maktaba kubwa, ambayo imeunganishwa na maktaba ya chuo cha Carleton, maktaba ya Wilson ni kubwa zaidi.

Picha zinazoonekana hapa nilipiga jana. Hiyo ya juu ni ubavuni mwa maktaba, na hiyo ya chini ni sehemu ya mbele, kwenye mlango. Ardhini inaonekana theluji, kwani ni bado kipindi cha baridi.


Saturday, February 25, 2017

Tafsiri Yangu ya "A Time to Talk" (Robert Frost)

Leo nimetafsiri shairi fupi la Robert Frost, "A Time to Talk." Hili ni shairi nililolisoma kwa mara ya kwanza miaka mitatu iliyopita, baada ya binti yangu Zawadi kuninunulia kitabu cha mashairi ya Frost, Robert Frost: Selected Poems. Kama nilivyoelezea katika blogu hii, nilikuwa nimelazwa hospitalini mjini Minneapolis, na binti yangu, kwa kujua ninavyopenda vitabu, alininunulia hiki kitabu kinisaidie kukabili hali niliyokuwemo.

Shairi hili la "A Time to Talk" lina mawaidha mazito kuhusu maisha. Linatukumbusha umuhimu wa uungwana na ukarimu katika mahusiano yetu binadamu. Tuache fikra ya kwamba hatuna muda wa kujumuika na wenzetu, kujuliana hali, na kadhalika. Robert Frost anavyoelezea mambo katika shairi hili ananikumbusha maisha ya vijijini, ambayo niliishi tangu utotoni. Kusalimiana ni wajibu, na watu hutumia muda kujuliana hali.

Bila shaka, Frost anaukosoa utamaduni wa ubinafsi, na utamaduni wa kila mtu na maisha yake. Anaikosoa hali ambayo wanafalsafa kama Karl Marx na wafuasi wake wameiongelea vizuri kwa kutumia dhana ya "alienation." Anavyoongelea kuhusu kuwa na muda wa kuongea na wenzetu, ninaona kuwa Frost anaikejeli jamii ambayo imejiaminisha kuwa muda ni hela ("time is money"). Ninavyosema hayo mambo yanayohusu utamaduni, kama yalivyoelezwa katika shairi hili, ninakumbuka nilivyoyaelezea katika kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Kwa kumalizia, napenda nirudie jambo ambalo ninalitamka daima. Kutafsiri kazi ya fasihi ni shughuli ngumu yenye mitego na vipingamizi vingi. Nilivyojaribu kulitafsiri shairi la Frost, simaanishi kuwa tafsiri yangu ndio kilele cha ufanisi. Msomaji makini anayezifahamu vizuri sana lugha za ki-Ingereza na ki-Swahili, na sio lugha tu, bali lugha ya kifasihi, bila shaka ataona vipengele ambayo vingeweza kuboreshwa. Kwa mfano, katika mstari wa pili, utatafsirije "a meaning walk," ili uziwasilishe kwa ki-Swahili dhana zilizomo katika huo usemi wa ki-Ingereza?
------------------------------------------------------------------------------------------------------------

A TIME TO TALK (Robert Frost, 1874-1963)

When a friend calls to me from the road
And slows his horse to a meaning walk,
I don't stand still and look around
On all the hills I haven't hoed,
And shout from where I am, What is it?
No, not as there is a time to talk.
I thrust my hoe in the mellow ground,
Blade-end up and five feet tall,
And plod: I go up to the stone wall
For a friendly visit.

MUDA WA MAONGEZI

Rafiki anaponiita kutoka barabarani
Huku akipunguza kwa makusudi mwendo wa farasi wake,
Sisimami tu na kuangalia huko na huko
Kubaini idadi ya vilima ambavyo bado sijalima
Na kisha kupaaza sauti pale nilipo, Vipi?
Hapana, hapana kwani kuna muda wa kuongea.
Nasimika jembe langu katika ardhi tepetepe,
Ubapa wa jembe ukiwa juu futi tano toka ardhini,
Na ninatembea taratibu: ninaelekea kwenye ukuta wa mawe
Kukutana na rafiki.

Wednesday, November 2, 2016

Nimenunua Webster's Concise Dictionary and Thesaurus

Jana nilinunua nakala ya Webster's New World Concise Dictionary and Thesaurus, iliyochapishwa mwaka 2014. Hili ni toleo jipya la kitabu hiki ambacho kimekuwa kikichapishwa kwa miaka mingi. Kitabu hiki ni hazina ya pekee kwa kuwa kinajumlisha kamusi na "thesaurus."

Kwa wale wasiofahamu tofauti za vitu hivi viwili, napenda kusema kwa kifupi kwamba kamusi hutoa tafsiri za maneno. "Thesaurus," badala ya kutoa tafsiri ya neno, huorodhesha maneno ambayo maana zake zinafanana au kukaribiana na neno hilo.

Kwa mfano, katika kitabu nilichonunua leo, sehemu ya thesaurus, neno "docile" limewekewa maneno yafuatayo: "meek, mild, tractable, pliant, submissive, accommodating, adaptable, resigned, agreeable, willing, obliging, well-behaved, manageable, tame, yielding, teachable, easily influenced, easygoing, usable, soft, childlike."

Mfano huu unaonyesha wazi ubora na upekee wa "thesaurus." Kwa kuyaorodhesha maneno yenye maana zinazofanana au kukaribiana, mtu unakumbushwa msamiati wa lugha. Kama ni mzoefu wa kusoma unayeyatambua maneno hayo na unapenda kuchagua neno la kulitumia, kazi yako inakuwa imerahisishwa. Inatakiwa uwe na ufahamu wa tofauti ndogo ndogo za maana au msisitizo zilizomo katika maneno kama zile ambazo kwa ki-Ingereza huitwa "denotation" na "connotation" ili uweze kuchagua neno lifaalo kuliko mengine katika muktadha wa uandishi wako.

Nimenunua Webster's New World Concise Dictionary and Thesaurus ingawa ninazo "thesaurus" tangu zamani, nilipokuwa sekondari, ambapo niliifahamu Roget's Thesaurus. Kwa nini nimenunua "thesaurus" nyingine leo? Ni kwa kuwa ni toleo jipya. Vile vile, mara kwa mara ninanunua kitabu ambacho nakala yake ninayo, kama nilivyowahi kueleza katika blogu hii.

Nakala za ziada za vitabu muhimu ni baraka. Ninapokwenda Tanzania, huwa sikosi kuchukua vitabu kadhaa kuzigawa kwenye maktaba za jamii au vyuo. Kwa miaka mingi, nimekuwa na wazo kwamba ukipeleka kamusi ya ki-Ingereza, kwa mfano, kwenye shule yoyote, ni kama unaanzisha mapinduzi katika ufundishaji wa somo la ki-Ingereza katika shule hiyo. Unakuwa umemwezesha mwalimu kufahamu uandishi sahihi wa maneno ya ki-Ingereza. Vile vile, kwa kuwa kamusi kwa kawaida hutoa pia mifano ya matumizi ya maneno, unakuwa umemjengea mwalimu fursa ya kujiongezea ufahamu wa lugha. Unakuwa umeweka msingi wa kuboresha somo la ki-Ingereza kwa wanafunzi.

Kitabu ni rasilimali na pia ni mtaji. Kupeleka kitabu muhimu popote nchini kikasomwe ipasavyo ni aina ya uwekezaji. Hilo ni jambo linaloeleweka kwa yeyote anayefahamu kuwa dunia inaingia zaidi na zaidi katika enzi za uchumi unaoendeshwa na elimu na maarifa. Hiyo ndiyo dhana ya "knowledge economy." 

Monday, October 10, 2016

Ki-Ingereza Kama Lugha ya Ulimwengu

Jana, katika blogu hii, nilikiongelea kitabu cha Charles Derber, People Before Profit, ambacho kinahusu utandawazi. Katika kukisoma kitabu hiki, nilivutiwa na maelezo yake, na nikapata hamasa ya kufuatilia mada ya utandawazi kwa namna nyingine.

Nilikumbuka kwamba nina kitabu cha David Crystal, English as a Global Language, ambacho nilikinunua miaks michache iliyopita, ila nilikuwa nimekipitia juu juu tu. Leo nimeamua kukisoma, na ninaona jinsi maelezo yake kuhusu lugha ya ki-Ingereza yanavyofungamana na suala la utandawazi. Kwa mfano, katika utangulizi wake, mwandishi anasema,

"We have as yet no adequate typology of the remarkable range of language contact situations which have emerged as a consequence of globalization, either physically (e.g. through population movement and economic development or virtually (e.g. through Internet communication and satellite broadcasting)." (xi)

Kitu kimoja kilichonifanya nikumbuke kitabu cha David Crystal ni kuwa huyu ni mtaalam maarufu ulimwenguni wa masuala ya lugha. Nilipokuwa mwanafunzi katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kuanzia mwaka 1973, nikisomea "Literature" na "English," ndipo niliposoma maandishi ya Crystal, sambamba na mabingwa wengine, kama vile Frank R. Palmer, John Lyons, Noam Chomsky, Sydney Greenbaum, na Randolph Quirk. Kumbukumbu hiyo ndiyo ilinifanya ninunue kitabu cha Crystal, English as a Global Language miaka michache iliyopita. Sasa, kwa kuwa ninafuatilia suala la utandawazi, ninaona nilifanya vizuri kununua kitabu hiki.

Pamoja na kuelezea jinsi ki-Ingereza kilivyofanikiwa kuenea duniani na kinavyoendelea kuiteka dunia kama lugha ya mawasiliano ulimwenguni iliyo muhimu kuliko zote, Crystal anabainisha pia kuwa hatuwezi kuwa na uhakika kama hali hii itaendelea hivi siku za usoni. Kama nilivyoeleza katika ujumbe wa jana, nikinukuu kitabu cha People Before Profit, utandawazi hausambai bila upinzani kutoka katika jamii na tamaduni mbali mbali zinazotaka kulinda jadi na misingi yao.

Ni hivi hivi katika kuenea kwa ki-Ingereza. Crystal anatuelekeza kwenye kitabu cha Tom McArthur, The English Language, na anatumabia kuwa McArthur

"adopted a more synchronic perspective, moving away from a monolithic concept of English. His primary focus was on the kinds of variation encountered in the language as a consequence of its global spread. He suggested that English was undergoing a process of radical change which would eventually lead to fragmentation into a 'family of languages.'" (x)

Hilo wazo la ki-Ingereza kugawanyika katika vilugha mbali mbali linasisimua akili. Lakini, hata kama ki-Ingereza kitaishia kuwa vilugha vingi, ninategemea kuwa bado kutakuwa na misingi itakayodumu katika vi-Ingereza hivyo na kuendelea kuwawezesha watumiaji kuwasiliana na kuelewana. Hata wakati huu, tayari ki-Ingereza kina lahaja nyingi, sawa na ki-Arabu, ki-China, ki-Swahili, na lugha zingine.

Jambo la muhimu la kuzingatia, kwa nchi kama Tanzania, ni hoja ya msingi ya English as a Global Language, kwamba hakuna namna ya kukizuia ki-Ingereza kutawala dunia kama lugha ya mawasiliano. Tupende tusipende, lazima tutafute namna ya kuhakikisha kuwa tunaijua lugha hiyo. Tusipumbazwe na siasa reja reja zilizovaa gwanda la utaifa, tukasahau kwamba ki-Ingereza ndiyo nyenzo na silaha itakiwayo katika mapambano ya ulimwengu wa utandawazi wa leo na kesho.

Wednesday, July 20, 2016

Ki-Ingereza cha Shakespeare

Miaka mia nne imepita tangu alipofairki Walliam Shakespeare. Lakini dunia haiwezi kumsahau, kwa mchango wake uliotukuka katika utunzi wa tamthilia na mashairi. Leo, ninarejea tena kwenye mada hii ya mchango wa Shakespeare, ambayo nimekuwa nikiiongelea katika blogu hii. Napenda kujikumbusha suala la ki-Ingereza cha Shakespeare.

Kumbukumbu hii imenijia leo kwa sababu maalum. Leo, katika kozi yangu ya African Literature, nimeanza kufundisha The Dilemma of a Ghost, tamthilia ya Ama Ata Aidoo. Nimeongelea mistari nane ya mwanzo ya "Prologue," yaani utangulizi, nikataja mambo mengi, kuanzia "folklore" hadi tamthilia za Shakespeare. Mistari hiyo ni hii:

I am the Bird of the Wayside--
The sudden scampering in the undergrowth,
Or the trunkless head
Of the shadow in the corner.
I am the asthmatic old hag
Eternally breaking the nuts
Whose soup, alas,
Nourished a bundle of whitened bones--

Miaka yetu, tulipokuwa tunasoma sekondari,  ambayo kwangu ilikuwa ni 1967-70, tulisoma na kuelewa ki-Ingereza cha Shakespeare. Tulipokutana na maneno magumu au misemo isiyoeleweka, tulifuatilia hadi kuelewa. Aghalabu, maelezo yalikuwemo katika vitabu tulivyokuwa tunasoma. Vinginevyo, tuliangalia kamusi. Tulikuwa na tabia ya kujituma.

Utamu wa ki-Ingereza cha Shakespeare unaonekana katika maandishi yake yote. Humo tunaona nidhamu ya hali ya juu katika matumizi ya maneno na uundaji wa sentensi. Kila neno lina umuhimu, na limewekwa mahali panapostahili. Hakuna sehemu inayolegalega.

Kumsoma Shakespeare ni chemsha bongo. Ni kunoa akili, sio tu kutokana na namna Shakespeare anavyotumia lugha bali pia kutokana na ukweli kuwa Shakespeare ndiye aliyekuwa na msamiati mkubwa kuliko mtumiaji mwingine yeyote wa ki-Ingereza. Hapa naleta mfano kutoka katika tamthilia yake ya Hamlet, ambayo nimeikumbuka leo kwa namna ya pekee, ili angalau wale tuliosoma zamani tujikumbushe enzi zile, ambapo shule ilikuwa shule kweli:

ACT I SCENE III A room in Polonius' house.
[Enter LAERTES and OPHELIA]
LAERTESMy necessaries are embark'd: farewell:

And, sister, as the winds give benefit

And convoy is assistant, do not sleep,

But let me hear from you.
OPHELIADo you doubt that?
LAERTESFor Hamlet and the trifling of his favour,

Hold it a fashion and a toy in blood,

A violet in the youth of primy nature,

Forward, not permanent, sweet, not lasting,

The perfume and suppliance of a minute; No more.
OPHELIANo more but so?
LAERTESThink it no more;10

For nature, crescent, does not grow alone

In thews and bulk, but, as this temple waxes,

The inward service of the mind and soul

Grows wide withal. Perhaps he loves you now,

And now no soil nor cautel doth besmirch

The virtue of his will: but you must fear,

His greatness weigh'd, his will is not his own;

For he himself is subject to his birth:

He may not, as unvalued persons do,

Carve for himself; for on his choice depends20

The safety and health of this whole state;

And therefore must his choice be circumscribed

Unto the voice and yielding of that body

Whereof he is the head. Then if he says he loves you,

It fits your wisdom so far to believe it

As he in his particular act and place

May give his saying deed; which is no further

Than the main voice of Denmark goes withal.

Then weigh what loss your honour may sustain,

If with too credent ear you list his songs,30

Or lose your heart, or your chaste treasure open

To his unmaster'd importunity.

Fear it, Ophelia, fear it, my dear sister,

And keep you in the rear of your affection,

Out of the shot and danger of desire.

The chariest maid is prodigal enough,

If she unmask her beauty to the moon:

Virtue itself 'scapes not calumnious strokes:

The canker galls the infants of the spring,

Too oft before their buttons be disclosed,40

And in the morn and liquid dew of youth

Contagious blastments are most imminent.

Be wary then; best safety lies in fear:

Youth to itself rebels, though none else near.

Thursday, October 29, 2015

Shairi la "Kimbunga" (Haji Gora Haji)

Kutafsiri kazi ya fasihi ni kazi ngumu ya kuchemsha bongo. Inahitaji ufahamu wa hali ya juu wa lugha husika, na pia hisia makini za kifasihi. Tofauti na inavyoeleweka katika jamii, kutafsiri ni suala pana kuliko kuwasilisha ujumbe kutoka lugha moja kwenda lugha nyingine, bali ni kutunga upya kazi ya fasihi inayotafsiriwa. Hili suala linajadiliwa sana na wataalam wa lugha, fasihi, na falsafa.

Pamoja na matatizo yote, ninapenda kuchemsha akili yangu kwa kutafsiri kazi za fasihi. Kwa mfano, nimetafsiri hadithi za ki-Matengo, na shairi la Mama Mkatoliki.

Hapa naleta shairi la Haji Gora Haji, mshairi maarufu wa Zanzibar, ambaye niliwahi kukutana naye. Shairi hilo ni "Kimbunga" ambalo limo katika kitabu chake kiitwacho Kimbunga. Jisomee shairi hilo na ujionee nilivyopambana na lugha katika kutafsiri. Ni mapambano, na kuna wakati unajikuta umepigwa butwaa au mwereka.
-----------------------------------------------------------------------------------------------------------------

                               Kimbunga

1.     Kimbunga mji wa Siyu, kilichowahi kufika
       Si kwa yule wala huyu, ilikuwa patashika
       Kimeing'owa mibuyu, minazi kunusurika
       Nyoyo zilifadhaika.

2.     Yalizuka majabali, yakabirukabiruka
       Zikadidimia meli, ngarawa zikaokoka
       Kimbunga hicho kikali, mavumbi hayakuruka
       Nyoyo zilifadhaika.

3.     Nyumba kubwa za ghorofa, siku hiyo zimeruka
       Zikenenda kwa masafa, kufikia kwa kufika
       Vibanda vyao malofa, vyote vikasalimika
       Nyoyo zikafadhaika.

4.     Chura kakausha mto, maji yakamalizika
       Pwani kulikuwa moto, mawimbi yaliyowaka
       Usufi nusu kipeto, rikwama limevunjika
       Nyoyo zikafadhaika.

5.     Kuna kikongwe ajuza, viumbe kimewateka
       Hicho kinamiujiza, kila rangi hugeuka
       Wataokiendekeza, hilaki zitawafika
       Nyoyo zikafadhaika.


                                 A Hurricane

1.     A hurricane once arrived in Siyu town
       Sparing neither that one nor this one, it was sheer mayhem
       It uprooted babobab trees, the coconut trees surviving
       Hearts went panicking.

2.     Big rocks turned up, tumbling over and over
       Ships were sinking, while mere boats survived
       Fearsome as the hurricane was, it raised no dust
       Hearts went panicking

3.     Great storied houses were blown away that day
       They flew quite a distance, landing wherever they landed
       The huts of the lowly, all survived intact
       And hearts went panicking

4.     The frog drained the river, the water all dried up
       On the shore was conflagration, of the waves flaming
       Half a container of kapok, broke the coolie's cart
       And hearts went panicking

5.     A wizened hag there was, who held beings captive
       She is given to magical powers, changing hues at will
       Those who let her be, perdition will be their lot
       And hearts will go panicking.

Sunday, June 7, 2015

Nimetoka Kanisani Kusali

Ni Jumapili, saa sita na kidogo mchana. Nimetoka kanisani kusali. Mimi ni m-Kristu wa kawaida, m-Katoliki. Namwabudu Mungu na ninaamini kuwa yeye ndiye anayeongoza maisha yangu. Katika raha na matatizo, ninamtegemea yeye. Ninamshukuru kwa kunipa uhai siku hadi siku.

Namshukuru Mungu kwa kunipa akili na utashi nitafakari mambo na kujiamulia. Ninamshukuru kwa jinsi anavyotuneemesha, kwa kuwaumba wanadamu wa kila aina, wenye dini mbali mbali, tamaduni na lugha mbali mbali. Dunia inapendeza kwa tofauti hizo, sawa na maua yanavyopendeza, kwa uwingi wa tofauti za rangi.

Namshukuru Mungu kwa yote aliyoyaweka duniani: nchi kavu, bahari, milima, mabonde, mito, miti, majani na maua. Ametuwekea wanyama wa kila aina, ndege na wadudu, jua, mwezi na nyota, mvua na upepo, vitu vinavyoonekana na visivyoonekana.

Vyote ni mazao ya uumbaji wa Mungu. Ninaomba niwe na moyo wa kuwapenda wanadamu wote na vyote alivyoumba Mungu. Ninaomba niwe mtu mwema, mwenye kutambua na kuzingatia kila siku kuwa Mungu amenipa uhai, akili, na vipaji, si kwa ajili yangu, bali kwa manufaa ya walimwengu bila kujali tofauti zao, za taifa, kabila, dini, jinsia, umri, utamaduni, lugha, na kadhalika.

Kuwa kanisani, kujumuika na waumini wenzangu, ni fursa ya kujikumbusha imani ya dini yangu, kuwaombea walimwengu wote, wabarikiwe. Sasa, baada ya kutoka kanisani, ninajisikia mwenye faraja, moyo mkunjufu, na ari ya kuendelea na majukumu yangu.

Saturday, February 21, 2015

Lugha na Mwamko wa Elimu Tanzania

Katika kuendelea kutekeleza ombi nililopata kutoka kwa mdau wa blogu hii, juu ya sera ya lugha ya kufundishia nchini Tanzania, napenda kuongelea suala la lugha na mwamko wa elimu. Huu ni mwendelezo wa ujumbe nilioandika katika makala yangu, "Tatizo si Lugha ya Kufundishia, ni Uzembe." ambayo niliichapisha katika blogu hii.

Kwanza, nasisitiza mtazamo wangu kuwa tatizo si lugha ya kufundishia, bali uzembe.

Mimi kama mwelimishaji, nimeshuhudia tatizo hili lilivyo katika jamii ya wa-Tanzania. Nitaanza kwa kutoa mfano. Mwaka 1980, nilipokuwa mhadhiri katika idara ya "Literature" ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, nilifika kusomea shahada ya uzamifu katika Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison, Marekani.

Niliondoka Tanzania wakati jamii ikiwa bado inazingatia mafundisho ya Mwalimu Nyerere kuhusu elimu. Kwa miaka sita niliyokuwa masomoni, nilifanya bidii katika masomo na pia nilinunua vitabu vingi sana, nikijua kuwa ndio nyenzo itakayonifanya nifundishe kwa kiwango cha juu kabisa pindi nitakaporejea tena Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Nilipohitimu masomo, nilirejea nchini nikiwa na shehena yangu ya vitabu. Badala ya kuniulizia kuhusu masomo niliyosomea au elimu niliyoipata, watu waliniuliza kama nimeleta "pick-up." Walinishangaa kwa kuleta vitabu badala ya gari. Haikutegemewa kuwa mtu ukae "majuu" miaka yote ile halafu usirudi na gari.

Hapo nilitambua wazi kabisa kuwa mwamko wa elimu, ambao alikuwa ameuchochea Mwalimu Nyerere, ulikuwa umedidimia. Niliendelea kufundisha katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam huku nikishuhudia mwamko wa elimu ukiendelea kudidimia nchini.

Jadi ya kuthamini mali na vitu badala ya elimu iliendelea kushamiri. Wasomi wakipata fursa ya kwenda nje, inayojulikana kama "sabbatical," walitegemea na walitegemewa kutumia fursa hiyo kujitafutia vitu, hasa magari. Mwenye kuleta gari au magari alionekana ndiye msomi bora. Ni tofauti kabisa na hapa Marekani, ambapo profesa unathaminiwa kwa ujuzi wako, hata kama unatembelea baiskeli au unapekua kwa miguu. Binafsi, kwa kuwa kipaumbele changu elimu na taaluma nimeridhika kufundisha hapa Marekani, tangu nilipoanza, mwaka 1991.

Tanzania, ilikuwa ni jambo la kawaida kwa walimu kushughulikia shughuli zao za kujipatia pesa hata kama walipaswa wawe darasani wakifundisha. Jambo hili limekuwa likitajwa na wanafunzi wetu wa ki-Marekani tunaowapeleka kusoma Tanzania, kwani katika vyuo vyao hapa Marekani, profesa hawezi kukosa kuingia darasani bila sababu ya maana kama vile kuumwa. Na akikosa kipindi, hufanya mpango wa kukifidia.

Katika jamii ya wa-Tanzania, nilishuhudia kushamiri utamaduni wa kutafuta vyeti kwa njia yoyote, badala ya kutafuta elimu. Nilishuhudia jinsi watu walivyokuwa tayari kutafuta hata vyeti feki. Hata baadhi ya wale wanaoitwa viongozi wamejipatia hivyo vyeti feki, kutoka  vyuo ambavyo havina hadhi itambulikanayo katika ulimwengu wa taaluma.

Kama ambavyo nimekuwa nikilalamika tena na tena katika blogu hii, utamaduni wa kununua na kusoma vitabu umekosekana katika jamii ya wa-Tanzania. Wazazi, ambao wangetegemewa kuwa wanunuaji wa kuaminika wa vitabu na wawe wanawasomea vitabu watoto wao, kama wafanyavyo wa-Marekani, hawafanyi hivyo.

Hao tunaowaita viongozi Tanzania, na wa-Tanzania wengine wengi, hutembelea nchi za nje. Sijui ni wangapi wanatumia fursa hii kununua vitabu na kurudi navyo Tanzania. Katika miji wanayopita na katika viwanja vya ndege, kuna maduka ya vitabu. Sijui ni wangapi wanapita katika maduka hayo na kununua vitabu. Nimewahi kusafiri mara kwa mara na wa-Tanzania, na nimeona kuwa zawadi wanazonunua ni vitu kama vipodozi, marashi, na mizinga ya vinywaji vikali. Wa-Tanzania hupenda zawadi za aina hiyo. Vitabu je? Jibu mwenyewe.

Sijui ni nyumba zipi katika Tanzania ambazo zina maktaba. Sijui ni nyumba ngapi ambazo zina vitabu angalau 50 au 100, kwa ajili ya watoto na wazazi. Kutegemea kuwa utamwona m-Tanzania amekaa sebuleni, bustanini, ufukweni, ndani ya basi au ndege, anasoma kitabu, ni kama kutegemea kumwona jogoo amevaa suruali.

Niliwahi kuhudhuria tamasha la vitabu Dar es Salaam, mwaka 2004. Watoto walikuwepo, na waalimu, lakini watu wazima walikuwa wachache sana. Hata hao wanaoitwa viongozi, wa ngazi yoyote, hawakuwepo. Watoto walifanya maonesho mbali mbali na waliimba nyimbo. Katika wimbo mmojawapo, waliwasihi wazazi wawe wananunua vitabu na kusoma pamoja na watoto wao majumbani. Wazazi wenyewe hawakuwepo kwenye tamasha. Lakini jioni, nilipokuwa naelekea nyumbani, niliwaona hao watu wazima wamekusanyika kwenye mabaa.

Katika hali hii, tatizo linalohitaji kushughulikiwa ni mwamko wa elimu. Bila mwamko wa elimu, hata lugha ya kufundishia ikibadilishwa mara ngapi, hata tukisema tutumie lugha zetu za ki-Nyaturu, ki-Nyasa, ki-Zaramo, na kadhalika, tusitegemee kuwa tutaleta mapinduzi yatakiwayo. Kinachohitajika ni mwamko wa elimu. Huu ndio msingi, ambao tumeuharibu.

Tuesday, February 17, 2015

Tatizo si Lugha ya Kufundishia, ni Uzembe

Jana, katika blogu hii, mdau mmoja aliniomba niandike makala kuhusu lugha ya kufundishia nchini Tanzania. Aliandika hivi:

Prof Mbele. Pole na kazi za kila siku.
Ningependa kujua nini maoni yako kuhusu kutumia kiswahili kama lugha kuu ya kufundishia mpaka chuo kikuu. Je unalionaje hili, unaona kutakuwa na athari zozote kutokana na elimu?. Je ni kweli tutakuwa tumejitenga na dunia?.

Ningeomba kama ungepata nafasi basi ukaliandika hili kama post katika blog na wala si comment. Nakutakia siku njema


Kwa kweli mada hii ya lugha ya kufundishia Tanzania imejadiliwa sana, katika vitabu, majarida, magazeti, mitandao, mikutano, na kadhalika. Siamini kama ninaweza kusema lolote ambalo halijasemwa. Hata hivi, nina mtazamo wangu, kama watu wengine.

Ninaamini kwa dhati kuwa tatizo si lugha ya kufundishia bali uzembe. Ingekuwa watu wanatambua umuhimu wa elimu, kwa maana halisi ya elimu, hawangekuwa wanatoa visingizio au lawama kama wanavyofanya. Hawangekuwa wanatumia muda wao katika kulalamika. Wangeelekeza nguvu zao na akili zao katika kutatua matatizo yoyote na kusonga mbele.

Kwamba mwanafunzi anafanya vizuri akifundishwa kwa lugha yake, ni hoja inayovutia, lakini sina hakika kama ninaikubali sana. Ingekuwa ninaikubali sana au kabisa, ningesema basi tuwafundishe watoto wetu kwa ki-Nyakyusa, ki-Sukuma, ki-Yao, na kadhalika. Kwa wengi, ki-Swahili ni lugha yao ya pili. Sisi hatukufundishwa kwa lugha mama, bali tulifundishwa kwa lugha ngeni ya ki-Swahili na baadaye ki-Ingereza, na hatukutetereka. Kwa nini mambo yawe kinyume leo, kama si uzembe?

Kama lugha ya ki-Ingereza ni tatizo, jawabu ni kufanya bidii kujifunza lugha hiyo. Kusema kwamba tuache kufundishia kwa ki-Ingereza eti kwa vile ufahamu wa ki-Ingereza ni mdogo ni kuhalalisha uzembe. Kinachotakiwa ni kufanya bidii kujifunza lugha hiyo kama tulivyokuwa tunafanya sisi.

Uzembe umetufikisha hapa tulipo. Kwa nini majirani zetu wa Malawi, Kenya, na Uganda hawatoi visingizio kama wanavyotoa wa-Tanzania? Ki-Ingereza sio lugha ya wenzetu hao, bali ki-Chewa, ki-Yao, ki-Ganda, ki-Acholi, ki-Kamba, Kikuyu, na kadhalika, kama ilivyo kwetu ki-Pare, ki-Luguru, ki-Makonde na kadhalika.

Kwa nini hao majirani zetu wawe wanatumia ki-Ingereza hadi chuo kikuu bila malalamiko kama wanayotoa wa-Tanzania? Enzi zetu, tulikuwa tunasomeshwa kwa ki-Ingereza sekondari (au kabla?)na kuendelea. Tulisoma chuo kikuu na hao wenzetu kutoka nchi za jirani, kwa ki-Ingereza bila matatizo. Leo ki-Ingereza kimekuwa shida. Ni nini kimetokea, kama si uzembe?

Ingawa nina mengine ya kusema, ninaamini kuwa blogu ni mahali pa makala fupi fupi, tofauti na kitabu. Kwa leo naona niishie hapa. Nitaendelea kuandika, ili kuongelea vipengele vya ujumbe wa mdau ambavyo sijavigusia hapa.

Wednesday, December 3, 2014

Wazo la Kutafsiri Kitabu

Kwa wiki kadhaa, nimekuwa nikiwazia kutafsiri kitabu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii. Siku chache zilizopita, niliandika kuhusu kitabu hiki katika blogu hii.

Nawazia kuzirekebisha insha zilizomo, na kuchapisha kitabu cha ki-Ingereza. Kufanya hivyo kutakipa kitabu hadhira kubwa zaidi kuliko ile ya wajuao ki-Swahili. Nina hakika, kwa mfano, kuwa wa-Marekani watakitafuta na kukisoma. Kwa ujumla wasomaji wa vitabu vyangu ni wa-Marekani.

Ninaposhiriki matamasha hapa Marekani, watu kadha wa kadha huja kwenye meza yangu na kuangalia vitabu, kuvinunua, au tu kuongea nami. Wako wanaoniuliza kama nimechapisha kitabu kingine, kwani vile vilivyopo mezani, vya ki-Ingereza, wanavyo au wamevisoma. Kauli hizi hata binti zangu, ambao hushirikiana nami, wamezisikia tena na tena.

Kwa miaka kadhaa, sijachapisha kitabu kipya. Sababu kubwa ni kuwa kuandika kitabu huchukua muda. Yaweza kuwa miezi au miaka. Kwa mfano, ilichukua miaka 23 hivi kuandaa kitabu cha Matengo Folktales. Vile vile, muda mwingi natumia katika kufanya utafiti na kuandika makala. Kutafsiri kitabu cha CHANGAMOTO, ni njia moja ya wazi ya kupatikana hicho kitabu kingine.

Kutafsiri CHANGAMOTO sio jambo la haraka. Kuna kitabu kingine katika lugha ya ki-Ingereza ambacho nataka kumaliza kukiandika kabla ya kuanza kutafsiri CHANGAMOTO. Hata hivi, siwezi kusema kuwa ni lazima ningoje. Muda wote ninakuwa na kazi kadhaa ninazoandika, na huwa sio rahisi kujua ni ipi itamalizika kabla ya ipi. Wanadamu tumejaliwa uwezo wa kufanya shughuli nyingi kwa pamoja, "multitasking" kwa ki-Ingereza. Ninachoombea ni uzima na akili timamu.

Saturday, January 29, 2011

Mikataba Bomu Itaendelea Kutumaliza

Wa-Tanzania wanalalamika sana kuhusu mikataba bomu ambayo inalisababishia Taifa hasara kubwa. Tafsiri yao, kwa ujumla, ni kwamba tunaingizwa katika janga hili na mafisadi ambao wanasaini kwa makusudi mikataba hii, kwamba hao ni wa-Tanzania wenye ubinafsi na uroho, na hawana uchungu na nchi, bali wanatafuta namna ya kunufaika wao. Mafisadi wetu hao wanashirikiana na mafisadi wa nje kuitafuna nchi yetu.

Kwa ujumla, nami nina hisia hizo. Kwanza kuna ukweli usiopingika kuwa maadili katika nchi yetu yanazidi kuporomoka. Vile vile nazingatia usemi wa wahenga kuwa lisemwalo lipo, na kama halipo laja. Pia tunaona taarifa kutoka sehemu mbali mbali za dunia kuhusu uozo wa rushwa katika masuala ya mikataba, zabuni, na kadhalika.

Lakini msimamo wangu hauishii hapa. Naamini kuwa hata kama tukiondoa kabisa rushwa na ufisadi, tukawa na watu wanaojali maslahi ya nchi na hao ndio wakawa wanaosaini mikataba yetu, bado tutaendelea kulizwa na mikataba bomu.

Kitakachosababisha janga hili ni kuanguka kwa elimu katika Tanzania. Kama ninavyosema daima katika blogu hii na sehemu zingine, wa-Tanzania tumejichimbia kaburi kwa kutothamini elimu ipasavyo. Ushahidi ni ufahamu wa lugha ulivyo duni, na utamaduni wa kununua na kusoma vitabu ulivyofifia au kutoweka miongoni mwetu.

Nikifafanua suala la lugha na kulihusisha na suala la mikataba, napenda kusema kuwa tupende tusipende, mikataba ya kimataifa itaendelea kuandikwa kwa ki-Ingereza, nasi tutajikuta tunasaini bila kuelewa vizuri kilichomo. Kuna matapeli wengi duniani, ikiwamo katika uwanja wa biashara na uwekezaji.

Wajanja, kwa kutambua umbumbumbu wetu, watachukulia mwanya huu kama mbinu ya kutukomoa. Laiti tungekumbuka msisitizo wa Mwalimu Nyerere pale tulipopata Uhuru, kuhusu maadui watatu tuliopaswa kupambana nao: umaskini, maradhi na ujinga.

Mwaka jana, serikali ya CCM ilitamka mara kwa mara kwamba imefanya marekebisho katika mikataba ya madini, ili kuziba mianya iliyokuwepo, iliyokuwa inatukosesha mapato tunayostahili. Sasa hapo nina suali. Ni nini kilichotufanya tusione hizo dosari tangu mwanzo? Kama si ufisadi, labda ni huu ujinga ninaoongelea. Binafsi, nakerwa kwamba serikali haijatuelezea undani wa suala hilo.

Wednesday, January 19, 2011

Andika ki-Swahili; ki-Ingereza Hatuelewi

Kuna tabia katika jamii ya wa-Tanzania ya kulalamika pale mtu anapoandika ki-Ingereza. Malalamiko haya yanaonekana mara kwa mara katika blogu ya Michuzi, kwa mfano, ambayo inasomwa sana na wa-Tanzania, pale inapotokea makala iliyoandikwa kwa ki-Ingereza.

Walalamikaaji wanakumbushia kuwa wa-Tanzania wengi hawajui ki-Ingereza, na kwa hivi wanataka mwandishi awafikirie hao kwa kuandika kwa ki-Swahili, lugha wanayoifahamu. Ujumbe unaojitokeza katika malalamiko hayo ni kwamba ni jambo la uzalendo kwa mwandishi kuwafikiria hao wa-Tanzania walio wengi, ili nao wapate kufaidika na yale yanayoandikwa.

Sijawahi kuona malalamiko hayo yakipingwa. Inaonekana kuwa hoja inayotolewa katika malalamiko hayo inakubalika miongoni mwa wa-Tanzania.

Katika kulitafakari suala hili, naona kuna haja ya kuwakosoa hao walalamikaji. Ingawa ni kweli kuwa mtu akiandika kwa ki-Swahili anawafikia wananchi wasiojua ki-Ingereza, kuna pia tatizo la uvivu katika jamii yetu.

Malalamiko hayo ni sehemu ya tatizo hili la uvivu ambalo naliongelea tena na tena katika blogu hii na zingine, na pia katika maandishi mengine. Wa-Tanzania wanapenda kutafuta visingizio na kuwalaumu wengine. Kwa nini wa-Tanzania waridhike na hali yao, ya kujua ki-Swahili tu, badala ya kujifunza lugha zingine?

Kama wa-Tanzania wanataka kudekezwa, ni bora wajue kuwa dunia hii ya ushindani haidekezi mtu. Wasipojituma katika masuala ya elimu, ikiwemo elimu ya lugha mbali mbali, sio tu watabaki nyuma, bali wataumia. Mawasiliano ya kimataifa yatakuwa mtihani mkubwa ambao watashindwa. Mikataba ya nje watashindwa kuielewa.

Wakati huu tunanyoosheana vidole kutokana na mikataba tunayohisi waTanzania wenzetu wanaisaini kifisadi. Lakini, kwa jinsi tunavyoendekeza uvivu ninaoongelea, tutaendelea kusaini mikataba mibovu kwa kutojua lugha. Nchi itaendelea kuumia.

Hata kama watu hawana vitabu, kuna maktaba katika miji mbali mbali. Mtu yeyote anaweza kujipangia utaratibu wa kwenda kusoma vitabu vilivyomo, akajiongezea angalau ufahamu wa ki-Ingereza. Lakini wa-Tanzania wako radhi kukaa kwenye kijiwe nje ya maktaba, siku hadi siku, wiki hadi wiki, mwezi hadi mwezi, mwaka hadi mwaka, bila kuingia humo maktabani. Hili ni tatizo kubwa katika nchi yetu.

Thursday, November 25, 2010

Kuendesha Blogu Mbili

Nina blogu mbili: ya ki-Swahili na ya ki-Ingereza. Kuendesha blogu moja ni kazi, blogu mbili ni zaidi. Kwa nini naendesha blogu mbili?

Nimewahi kuelezea kwa nini ninablogu. Labda nisisitize tu kuwa blogu yangu ya ki-Swahili inanipa fursa ya kujiongezea uzoefu wa kuandika kwa ki-Swahili, na pia kuwasiliana na wa-Tanzania wengi, wakiwemo wale wasiojua ki-Ingereza. Ninafahamu pia kuwa wako wasomaji wa blogu hii ambao si wa-Tanzania. Kuna hata wa-Marekani ambao wameniambia kuwa wanaisoma. Wanajikumbusha mambo ya Tanzania na pia lugha ya ki-Swahili.

Katika blogu yangu ya ki-Ingereza siandiki sana masuala ya Tanzania. Kadiri siku zinavyozidi kwenda, napata hisia kuwa ninaandika kwa ajili ya walimwengu kwa ujumla. Naona jinsi ninavyozingatia masuala ya taaluma, hasa fasihi. Naamini natoa mchango kwa wale wapendao fasihi au wenye duku duku ya kuifahamu. Hapo nawafikiria sana wa-Tanzania.

Katika kuongelea kazi za fasihi, siandiki makala ndefu, bali nagusia vipengele muhimu, na pia natoa dokezo ambazo ni changamoto kwa yeyote, aweze kuzifanyia utafiti na tafakari. Naamini kuwa kwa namna hii, yeyote atajiongezea ufahamu wa fasihi.

Labda nijieleze zaidi kwa wa-Tanzania wenzangu: siandiki kwa ajili ya wale ambao lengo lao kuu ni kupasi mtihani. Naandika kwa ajili ya wale wenye kupenda fasihi au wenye duku duku ya kujifunza fasihi. Pia kama nilivyosema kabla, naandika kwa ki-Ingereza ili kutoa mfano wa uandishi bora wa ki-Ingereza, jambo ambalo linahitajika katika jamii yangu ya wa-Tanzania.

Ingawa kuendesha hizi blogu mbili si kazi rahisi, nitajitahidi kuzimudu kwa kadiri ya uwezo wangu. Kazi ya kuendesha blogu hizi inaniwekea aina ya nidhamu katika maisha yangu. Kuandika katika blogu hizi mara kwa mara imeshakuwa kama deni na wajibu, lakini naona manufaa yake kwangu, kwa jinsi ninavyotumia muda wangu na akili yangu kwenye shughuli ya maana.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...