Tuesday, June 30, 2015

Mambo ya Tamasha la Vitabu Mankato

Kila tamasha la vitabu au utamaduni ninaloshiriki huwa na mambo mengi ya kuelimisha na kuburudisha akili. Kukutana na watu na kuongea nao ni sababu muhimu ya ushiriki wangu katika matamasha hayo. Juzi katika tamasha la Deep Valley Book Festival, binti yangu Zawadi nami, tunaoonekana pichani hapa kushoto, tulikutana na kuongea na watu mbali mbali.

Kati ya hao alikuwepo mama mmoja ambaye si rahisi kumsahau. Alifika mezani petu, na wakati tunasalimiana alinyanyua nakala ya Matengo Folktales, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, Notes on Achebe's Things Fall Apart, na Africans in the World, akasema anavinunua.

Wakati wote alikuwa anatuelezea kuwa alikuwa na binti yake ambaye aliishi China kwa miaka nane kisha akaenda Namibia, na kwamba ameipenda Namibia tangu  mwanzo. Alituambia tumwekee vitabu vyake, na kwamba binti yake angefika baadaye.

Yapata nusu saa kabla ya tamasha kwisha, huyu binti alikuja. Tuliongea naye, akatuambia jinsi alivyoipenda Namibia akifananisha na China. Mama yake naye akaja. Akaulizia vile vitabu tulivyomwekea, tukavichukua chini ya meza tulipovihifadhi, tukampa. Aliziangalia "t-shirt," akainyanyua moja na kuilipia. Kwa kuwa alinunua vitu vyote hivi: vitabu vinne na "t-shirt," tulimpunguzia bei, ingawa hakutegemea. Tulisahau kupiga picha pamoja naye na binti yake, kwa kumbukumbu.

Huyu mama hapa kulia ni mwalimu Becky Fjelland Davis wa Chuo cha South Central, Mankato. Ni mpenzi wa kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences na mpiga debe wake mkuu. Nami nilinunua kitabu chake, Jake Riley: Irreparably Damaged.

Huyu mwenzake alijitambulisha kwangu na binti yangu hiyo jana, akasema kwamba alihudhuria mhadhara wangu Chuoni South Central, "Writing About Americans." Huku akiusifia mhadhara ule, alinunua kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.


Nimeona niiongelee tena picha hiyo hapa kushoto, ingawa nilishaigusia juzi. Huyu mama ni Becky, ambaye nimemwongelea hapa juu. Huyu bwana, Paul Dobratz, ambaye alikuwa katika msafara wa Becky wa Afrika Kusini, alitusisimua, akishirikiana na Becky, kwa habari kem kem na michapo ya safari yao.

Hii ilikuwa ni mara ya kwanza kwa Paul kwenda Afrika, lakini Afrika iliuteka moyo wake kiasi kwamba anataka kwenda tena. Nimekutana au kuwasiliana na wa-Marekani wengi ambao wakishafika Afrika wanatekwa mioyo hivi hivi. Mwandishi Ernest Hemingway alikumbwa na hali hiyo wakati alipokuwa akizunguka Tanganyika mwaka 1933-34, kama alivyoandika katika Green Hills of Africa. Yeye na mke wake Pauline walijawa na hisia za kuipenda sana Tanganyika, kiasi kwamba hawakupenda kuondoka. Kwa maneno yake mwenyewe: "We had not left it, yet, but when I would wake in the night I would lie, listening, homesick for it already.”

Sunday, June 28, 2015

Tamasha la Vitabu Mankato Limefana

Leo, nikiwa na binti yangu Zawadi, tulikwenda Mankato kushiriki tamasha la vitabu, Deep Valley Book Festival. Niliandika habari za tamasha hilo katika blogu yangu ya ki-Ingereza. Nilipeleka vitabu vyangu vinavyoonekana mtandaoni, pamoja kijitabu kiitwacho Africans in the World. Vile vile tulipeleka "t-shirt" kama hizo tulizovaa pichani, zenye nembo ya kampuni yangu ndogo Africonexion: Cultural Consultants. Tunajifunza mengi katika kukutana na watu wanaofika kwenye meza yetu. Hatujui nini kitamvutia mtu fulani na kwa nini. Lakini watu hujieleza. Tunasikia habari nyingi, nyingine za kushangaza, zinazomfanya mtu anunue hiki au kile.

Inatufurahisha kuwaangalia watu wakipita kwenye meza mbali mbali kuangalia vitabu, kuongea na waandishi, wachapishaji na wengine wanaokutana nao katika tamasha. Nasi tunapata fursa ya kukutana na watu mbali mbali. Leo, kwa mfano, wamefika watu kwenye meza yetu ambao wametuambia wamefika Afrika: Botswana, Tanzania, na Namibia. Tunahisi walivutiwa na "t-shirt" tulizovaa, zenye ya ramani ya Afrika. Kila mmoja ametusimulia habari za safari yake. Tulijua kuwa tutakutana na baadhi ya watu tuliokutana nao wakati nilipotoa mihadhara katika Chuo cha South Central, katika maandalizi ya safari ya Afrika Kusini. Kama tulivyotarajia, walikuwepo watu kadhaa.



Hapa kushoto anaonekana kiongozi wa safari ya Afrika Kusini, mwalimu Becky Fjelland Davis, ambaye ni mwandishi. Alishiriki tamasha. Mwingine ni Paul Dobratz ambaye alihudhuria shughuli zote nilizofanya wakati wa ziara yangu Chuoni South Central. Naye alikuwemo katika safari ya Afrika Kusini. Binti yangu nami tulifurahi sana kusikia habari za safari.




Kama ilivyo kawaida hapa Marekani, watu wa rika mbali mbali huhudhuria matamasha haya ya vitabu. Wanayathamini sana, na mahudhurio huwa makubwa.

Daima ninaguswa ninapowaona wazazi wakiwa na watoto wao. Ninaguswa na jinsi wanavyowalea watoto wao katika utamaduni wa kupenda kusoma vitabu.






Imekuwa siku ya furaha sana kwa binti yangu na mimi. Tumefurahi kukutana na kuongea na watu wa aina aina, tuliowafahamu na ambao hatukuwafahamu. Tumerudi na kumbukumbu nyingi.

Thursday, June 25, 2015

Habari ya Malipo ya Mhadhara Chuoni Winona

Jumanne wiki hii, nilikwenda Chuo Kikuu cha Winona kutoa mhadhara, kama nilivyoandika katika blogu hii. Katika safari kama hii, kuna mambo mengi, na haiwezekani kuyaongelea yote. Hata hivi, naona ni vizuri tu kuelezea angalau yale yenye umuhimu Fulani kwangu na labda kwa wengine. Napenda kuongelea suala la malipo ya mhadhara ule.

Wakati nilipoombwa kwenda kutoa mhadhara, mhusika aliniuliza malipo yangu ni kiasi gani. Huu ni utaratibu hapa Marekani, nami kama ilivyo kawaida yangu, nilimwambia kuwa siweki kipaumbele kwenye malipo, bali kutoa huduma itakiwayo. Kama wanaonialika wana uwezo wa kunilipa, kwangu ni sawa, kama wana uwezo kidogo, kwangu ni sawa, na kama hawana uwezo, kwangu ni sawa pia. Niko tayari kuitikia mwito kwa hali yoyote. Nilidhani suala lilikuwa limeishia hapo.

Siku kadhaa baadaye, mhusika alinielezea tena habari ya malipo, akataja kiasi ambacho angeweza kunilipa, kutokana na bajeti yake. Nilimjibu kuwa sina tatizo, nikamshukuru. Alipoleta mkataba, ambao ulitaja kiasi hicho cha malipo, niliusaini bila kusita, nikamrudishia.

Siku ilipofika, yaani hiyo tarehe 23 Juni, binti yangu Zawadi nami tulikwenda Chuoni Winona. Tulikaribishwa vizuri, tukaingia kwenye ukumbi wa mkutano wakati huo huo wanafunzi walipokuwa wanaingia. Baada ya kila mtu kuketi, mwenyeji wangu alisimama kunitambulisha. Alisema tunaye mgeni hapa, Dr. Mbele, profesa wa Chuo cha St. Olaf. Ni mtu ambaye nimemfahamu kwa miaka kadhaa, na nimemwomba aje atoe mhadhara.

Hadi hapo, sikuona kitu cha pekee, kwani huo ni utaratibu wa kawaida. Kilichokuwa cha pekee ni pale alipoanza kuelezea mazungumzo yetu juu ya malipo. Aliwaambia wanafunzi kuwa Dr. Mbele aliniambia kuwa hajali kama nina malipo kiasi gani ya kumpa, angekuja tu. Nasikitika kuwa kiasi nilichoweza kumwekea hakifanani na umaarufu wake. Niko njiani kutafuta hela kwa program nyingine, niweze kumwalika na kumlipa kiwango anachostahili.

Kwa kweli, sikutegemea angesema yote hayo, na nilimsikiliza kwa kumhurumia kwa jinsi alivyoonekana kujisikia vibaya kwamba ameshindwa kunitayarishia malipo ninayostahili. Nilifarijika alipomaliza maelezo yake na kunikaribisha nitoe mhadhara.

Baada ya mhadhara, mwenyeji wangu aliniongoza kwenda ofisini kwake, akanipa fomu ya malipo nisaini. Kisha akanipa cheki. Nilishangaa kuona cheki ilikuwa imezidi kile kiwango alichoniambia mwanzo. Nikaona kuwa alikuwa amejitahidi alivyoweza kuvuka kile kiwango tulichokubaliana. Na bado aliendelea kulalamika kuwa angeridhika kama angenilipa ninavyostahili.

Nimeona niongelee jambo hili, kwani ni kati ya mambo ambayo sitayasahau. Pia ni jambo lenye maana kwangu. Nimetamka tena na tena kuwa siweki pesa mbele, bali huduma. Hata hivi, ninafahamu jinsi wa-Marekani wanavyojali malipo. Wanazingatia umuhimu wa kumlipa mtu kile wanachoona ni haki yake.

Ningeweza kusema kuwa ninapaswa kuzingatia umuhimu wa kufuata utamaduni wa mahali nilipo. Lakini suala hili la malipo bado ni mtihani kwangu, kama nilivyowahi kuandika katika blogu hii. Ninaamini kuwa kwa kuzingatia huduma kwa wanadamu, badala ya ubinafsi, sipotezi chochote. Badala yake, Mungu ananibariki. Ninaishi na raha moyoni. Ninafurahi kwamba binti yangu alishuhudia yote niliyoeleza hapo juu. Labda yatamsaidia maishani.

Wednesday, June 24, 2015

Uzinduzi wa Filamu ya "Papa's Shadow"

Jana ilikuwa siku ya pekee kwangu. Nilihusika na matukio mawili muhimu sana, kama nilivyoripoti katika blogu hii. Napenda kuongelea tukio mojawapo: uzinduzi wa filamu ya "Papa's Shadow." Habari ya filamu hii nimezungumzia kabla katika blogu hii, lakini imeelezwa pia, vizuri kabisa, kwenye tovuti ya Ramble Pictures.

Jana ilikuwa siku tuliyoingojea kwa hamu kubwa. Ilikuwa ni siku ya kuonyeshwa filamu ya "Papa's Shadow" hadharani, ingawa wote walikuwa waalikwa. Kwa kuwa mimi ni mhusika mkuu katika filamu hiyo kama mzungumzaji sambamba na Mzee Patrick Hemingway, uwepo wangu ulikuwa muhimu.

Nilijikuta niko miongoni mwa kadamnasi iliyoniona maarufu. Nina hakika kuwa huu utakuwa mzigo maishani, kwani nitategemewa kujua mengi juu ya Hemingway kuliko inavyowezekana. Hiyo jana tu masuali magumu yalikuwa yanaelekezwa kwangu. Hata hivi, hii ni changamoto nzuri ya mimi kuendelea kujielimisha.

Baada ya filamu kuonyeshwa, watu walikuja na kunishukuru sana kwa mengi niliyosema juu ya Hemingway. Mtu mmoja, kwa mfano, aliyejitambulisha kwangu kama mwalimu wa "high school," alinionyesha daftari ambamo alikuwa ameandika mambo yaliyomgusa zaidi katika filamu, na alisema kuwa amepata hamasa ya kuanza kusoma tena maandishi ya Hemingway.

Nilifurahi kuwa binti zangu walikuwepo kushuhudia uzinduzi. Kwa bahati mbaya mama yao hakuweza kujiunga nasi kwa kuwa alikuwa kazini.

Hapa kushoto niko na binti yangu wa kwanza, Deta, ambaye hajawa na fursa nyingi za kushuhudia shughuli zangu. Hii ni kutokana na majukumu ya kazi, sawa na mama yake. Lakini jana ilikuwa fursa nzuri, na sote tulifurahi.











Hapa kushoto niko na binti yangu wa pili, Assumpta. Huyu ndiye aliyeanzisha utani kuwa baada ya filamu hii ya "Papa's Shadow," nijiandae kutua Hollywood.

















Hapa kushoto niko na Zawadi binti yangu wa tatu. Huyu amekuwa akifuatana nami katika shughuli zangu tangu utoto wake. Anafahamu vizuri mawazo yangu, na anaweza kuniwakilisha katika matamasha bila mimi kuwapo.









Hapa kushoto tuko na Jimmy Gildea, mtengeneza filamu. Alikuwa mmoja wa wanafunzi 29 waliokuja Tanzania kwenye kozi yangu ya "Hemingway in East Africa," Januari, 2013.

Nimefanikiwa katika mambo mengi maishani, hasa katika masomo, na yote yameniletea furaha. Lakini nimefurahi zaidi kwa uzinduzi wa filamu hii na kwa jinsi nilivyowashirikisha watoto wangu. Waliyojionea na kuyasikia hiyo jana watayakumbuka.

Tuesday, June 23, 2015

Imekuwa Siku ya Mafanikio Makubwa

Leo imekuwa siku ya mafanikio makubwa. Kwanza nilienda Chuo Kikuu cha Winona na binti yangu Zawadi nikatoa mhadhara. Nilitumia hadithi za jadi kujadili namna wahenga wetu walivyozielewa dhana za uongozi na uwajibikaji.

Baada ya kuelezea kwa ufupi jinsi Afrika ilivyokuwa chimbuko la binadamu, lugha, sayansi, tekinolojia, na falsafa, nilisimulia hadithi mbili zilizomo katika kitabu changu cha Matengo Folktales, kuthibitisha namna wahenga wetu walivyoyatafakari masuala ya jamii. Hadithi hizo ni "The Monster in the Rice Field" na "Nokamboka and the Baby Monster."

Baada ya kurejea kutoka Winona, tulijiandaa kwenda Excelsior, kuhudhuria uzinduzi wa filamu ya "Papa's Shadow." Filamu hii inamhusu mwandishi Ernest Hemingway, na kwa kiasi kikubwa ni mazungumzo baina yangu na Mzee Patrick Hemingway, kuhusu maisha, uandishi, na fikra za Hemingway.

Matokeo ya mazungumzo yetu yalivyo katika filamu yamewasisimua sana watazamaji. Nilitegemea hivyo, kutokana na kwamba inaleta mtazamo mpya juu ya Hemingway.


Mtengenezaji wa filamu ni Jimmy Gildea, ambaye alikuwa mwanafunzi wangu katika kozi ya "Hemingway in East Africa," niliyofundisha Tanzania mwezi Januari mwaka 2013. Anaonekana pichani hapa kushoto akiwa nami na binti zangu.





Monday, June 22, 2015

Ernest Hemingway, a bridge between cultures

An excellent opportunity to learn why Ernest Hemingway fell in love with Cuba, was how Julián González, Cuban Minister of Culture, described the 15th International Colloquium dedicated to the author of The Old Man and the Sea, an academic event which began yesterday, June 18, in the presence of researchers and followers of the life and work of the great writer.
The Minister spoke to the press regarding the number of U.S. scholars who attend each edition of the event and how their interest in the life of the winner of the Nobel Prize for Literature also brings them closer to the social and cultural life of the island.

What made Hemingway fall in love with our country, he noted, were the characteristics of the people, as “he was an enemy of formalities and here he found a suitable setting for his work, without the usual protocol of other big capitals. This spontaneity is multiplied in the cultural level of our people, in the way that they appreciate the arts in general and literature in particular.”

He highlighted the role of Hemingway as a bridge between two cultures, “today more than ever because once Americans are able to travel to Cuba freely, a great incentive will be to discover what it was the writer found here, what he saw in our people that made him established himself here and take to Cuba as a second home.”

The opening day of the conference began with a tribute to René Villareal, Hemingway’s butler at his Finca Vigía home, and who the bestselling author called his Cuban son.
Villareal was the confidant of the famed writer for 14 years, but their relationship dated from his childhood, when in 1939 the Pulitzer Prize winner rented the property because in it he found the peace to write.

The tribute was followed by the presentation of the book, The Last Lion, by Argentine Professor Richard Koon, which in six parts takes a journey through the life of the remarkable writer from his childhood in Illinois until his death in Idaho.

Koon noted that the research for the book had taken some four decades and it brought together the testimonies of people who in various ways were linked to the life and work of Hemingway, including the Catalan artist Joan Miró and the writer Rafael Alberti.

The program for the coming days of the event, which ends Sunday, includes celebrations for the 80th anniversary of the first edition of Green Hills of Africa, and the 90th anniversary of the publication of his book of short stories In Our Time.

A panel entitled, Hemingway and Martha Gellhorn: In love and war, led by Professor Sandra Spanier, University of Pennsylvania, and the book launch of Hemingway: the unknown, by Cuban Enrique Cirules, will also feature.

Fotos con pies y créditos:
Ricardo Koon, author of the book The Last Lion. Photo: Padrón, Abel

Chanzo: Granma

El legado de Ernest Hemingway es celebrado en Cuba

La vigencia del célebre autor también está en las películas basadas en sus obras / El evento resaltó la vida y obra del Premio Nobel de Literatura


Caracas, 22 de junio de 2015.- Considerado el Dios de Bronce de la literatura norteamericana, expertos sostienen que la vigencia de sus obras no ha palidecido.

Este domingo culminó el XV Coloquio Internacional Ernest Hemingway realizado en Cuba, con la participación de expertos de diferentes partes del mundo. Un estudioso cubano participante del evento resaltó la vida y obra del Premio Nobel de Literatura y manifestó que la personalidad del célebre autor ha creado una serie de mitos, sitios y plazas en los lugares donde él vivió.

"La efigie de Hemingway (1899-1961) flota en un limbo, que va desde La Habana a Paris, Nueva York, España, Italia, el Caribe, desde Tanzania a Centroáfrica, y al parecer no va a desaparecer todavía" declaró un participante del Coloquio. En 1954, Hemingway le entregó la medalla del Premio Nobel a la Patrona de Cuba, La Virgen de la Caridad del Cobre, como reconocimiento al pueblo cubano, inspirador de su obra El viejo y el mar.

La vigencia de Hemingway también está en las películas basadas en sus obras, como “Adiós a las armas”, “Por quien doblan las campanas” y “Forajidos”, entre otras, que fueron interpretadas por prestigiosos actores y actrices. Una buena parte de la distensión entre Cuba y Estados Unidos está apoyada en las relaciones entorno a la vigencia de Hemingway en la Isla. MCM

VTV /TeleSur

(Chanzo: Venezolana de Televison)

Sunday, June 21, 2015

Niliyoyaona Maktabani Brookdale, Minnesota

Jana, kama nilivyoandika katika blogu hii, nilihudhuria mkutano Brooklyn Park, ambao tulifanyia katika maktaba ya Brookdale. Hapa kushoto ni picha ya upande wa Mbele wa maktaba hii, inavyoonekana kabla hujaingia ndani. Jana ilikuwa ni mara yangu ya kwanza kufika hapa, na niliona jinsi jengo lilivyo tofauti na majengo ya maktaba zingine ambazo nimeingia hapa Minnesota.



Nilivyoingia ndani, nilijikuta sehemu hii inayoonekana kushoto, ingawa ni kubwa na pana zaidi ya hii inayoonekana pichani. Wakutubi wengi wapo katika eneo hilo, tayari kuwasiaida wateja, na sehemu ya maulizo ambayo ni kubwa pia, iko eneo hili. Unapokuwa sehemu hii, kwa mbele yako na pembeni kuna maeneo yenye vitabu, majarida, kompyuta nyingi na hifadhi mbali mbali za taarifa, kama vile CD, DVD na na kaseti.

Niliulizia kilipo chumba cha mkutano, nikapita katikati ya makabati ya vitabu vya kila aina hadi mwishoni kabisa.




Baada ya mkutano, nilirejea tena sehemu hii na kuchungulia katika makabati mbali mbali, hasa ya fasihi. Kuna utajiri mkubwa wa vitabu, vya masomo na taaluma mbali mbali, vya watoto na watu wazima, na vitu vingine vingi. Inapendeza kuona wenzetu wanavyowekeza katika vitu vya namna hii, kuelimisha jamii.

Hiyo jana ilikuwa ni Jumamosi, na ilikuwa ni alasiri. Jua lilikuwa linawaka vizuri, na walikuwepo watu wengi katika maktaba, watu wa kila rangi, na kila rika. Wwnginw walikuwa wanasoma vitabu, wengine wanaazima, wengine wanatumia kompyuta, na wengine walikuwa wanarudufu maandishi.

Nilivyoangalia hali hii, ya watu wengi kuwemo maktabani wakati wa alasiri, Jumamosi, niliwazia hali ya Tanzania. Nilijiuliza ni wapi katika Tanzania unaweza kuona hali hii, tena Jumamosi mchana. Ni wapi unaweza kuwaona watu wa rika mbali mbali wamejaa maktabani wanajisomea. Hata huyu dada Latonya  niliyekutana naye jana hapo nje ya maktaba alikuwa anakuja maktabani na akina dada wenzake.

Ningekuwa na uwezo, ningebadili mioyo ya wa-Tanzania, wawe kama hao wa-Marekani, wenye kupenda kusoma. Ningehamasisha ujenzi wa maktaba zaidi. Kwa mji kama Dar es Salaam, ningependa ziwepo maktaba Sinza, Kinondoni, Buguruni, Kigamboni, Kawe, Kimara, Ukonga na sehemu zingine. Ingekuwa ni Marekani, mji wa ukubwa wa Dar es Salaam ungekuwa na maktaba nyingi. Lakini, miaka hamsini na zaidi tangu tupate uhuru, maktaba ni hiyo hiyo moja. Si jambo la kujivunia.

Saturday, June 20, 2015

Msomaji Amenilalamikia

Leo alasiri nilikwenda Brooklyn Park, Minnesota, kuhudhuria mkutano wa bodi ya Afrifest Foundation ambayo mimi ni mwenyekiti wake. Tulifanyia mkutano wetu katika maktaba ya Brookdale.

Baada ya mkutano, nilipotoka nje kuelekea sehemu nilipopaki gari, alinikimbilia dada Latonya anayeonekana katika picha hapa kushoto, ambayo tulipiga miaka mitano iliyopita kwenye tamasha la Afrifest. Ni m-Marekani Mweusi kutoka Chicago, ila anaishi Minneapolis. Tulifahamiana miaka ile kwa kuwa naye alikuwa katika bodi ya Afrifest Foundation.

Hatukutegemea kama tungeonana leo, ghafla namna ile. Kwa hivi tulifurahi sana. Lakini hakupoteza muda, alianza kunihoji kwa nini siandiki sana katika blogu yangu ya ki-Ingereza kama zamani. Alisema, akimaanisha maandishi yangu ya kiSwahili, "Tunaona unaandika sana, na tunajua unaandika mambo ya maana, ila hatujui unachoandika. Inakuwa kama unatusahau marafiki zako wa-Marekani Weusi."

Kwa kweli, ingawa mazungumzo yalikuwa ya kirafiki, na hata kiutani, niliona kuwa alikuwa anaongea kwa dhati. Na sisi wa-Afrika ambao tunaishi Marekani tunafahamu kuwa wako wa-Marekani Weusi wengi ambao wanategemea sisi wa-Afrika tuwe na mshikamano nao, kama ndugu. Kwa hivi, sikuyachukulia malalamiko ya Latonya kama mzaha. Nilijikuta nikikiri kosa na kuahidi kuwa nitakuwa naandika kama zamani. Alivyowataja wa-Marekani Weusi hakuwa anatunga hadithi. Ninafahamu kuwa wanasoma maandishi yangu.

Latonya mwenyewe ni mmoja wa wafuatiliaji wa dhati wa maandishi yangu. Hapo pichani, anaonekana ameshika kitabu changu cha Africans and Americans:Embracing Cultural Differences, mara baada ya kukinunua. Maneno aliyoniambia leo yameniingia. Nilimwambia hivyo, nikaahidi kujirekebisha.

Friday, June 19, 2015

Mteja Nimefurahia Huduma

Leo nilipeleka gari langu kwenye kituo cha Car Time hapa mjini Northfield kubadilishiwa "oil." Kwa hapa Marekani, inashauriwa kubadili "oil" kila baada ya kuendesha gari maili 3000. Sijui utaratibu wa Tanzania.

Kama ilivyo kawaida, nilipokewa vizuri, nikakaa sehemu ambapo wateja hungojea huduma. Baada ya dakika kama ishirini hivi, mtu aliyenipokea sehemu ya mapokezi alifika nilipokaa akachuchumaa kwa heshima zote na kuniambia kuwa mafundi walikuwa wamegundua kuwa gari langu linahitaji pia "tire rotation."

Kwa kuogopa kuwa labda ingekuwa gharama ambayo sikujiandaa kuimudu, nilimwuliza kwa utaratibu iwapo itakuwa gharama kiasi gani. Alinijibu kuwa hiyo "tire rotation" haitanigharimu. Nilimjibu kuwa nashukuru kwa huduma hiyo.

Dakika kama kumi tu baadaye. huyu jamaa aliiniita, kuniambia kuwa gari lilikuwa tayari. Alinikabidhi ufunguo na bili yangu, nikalipia, kisha nikashukuru na kuondoka zangu.

Huu ndio utamaduni niliouona hapa Marekani wa kuhudumia wateja. Nimewahi kuandika kuhusu huduma ya Car Time katika blogu hii,. Kila mahali nilipopita, hapa Marekani nimeona utamaduni huu wa kumjali mteja.

Sio mimi pekee mwenye uzoefu huo. Katika mahojiano yangu na Deus Gunza, m-Tanzania mwenzangu, tuliongelea suala hilo, tukakubaliana kuwa huu ndio utamaduni tunaouona hapa Marekani. Kwa upande wangu, nimejionea kuwa hata ukiingia baa, kama mhudumu yuko sehemu nyingine, ni kawaida kumwona meneja anakuja kwenye meza yako, kusafisha na kukuhudumia.

Katika baa za Tanzania, sijawahi kumwona meneja akifanya jambo kama hilo. Utamwona amekaa mahali anapiga gumzo na ulabu na marafiki zake, na akiona mteja umeingia na unangojea huduma, atakachofanya ni kuwaita wahudumu na kuwafokea kwa kukukalisha bila huduma. Sijawahi kumwona meneja akichukua kitambaa na kusafisha meza kwa ajili ya mteja na halafu kumletea kinywaji. Ni kama mwiko.

Kwa nini ninasimulia yote hayo? Ni kwa sababu nina nia ya dhati ya kuwasaidia wafanya biashara na watoa huduma wa Tanzania. Huduma bora kwa mteja ni msingi muhimu wa mafanikio. Hii imani kwamba mafanikio yanatokana na kwenda kwa mganga kusafisha nyota au kupata dawa ya mafanikio ni upuuzi.

Sijaona kampuni yoyote hapa Marekani inayoenda kwa waganga kutafuta dawa. Dawa muhimu ya uhakika ni kumridhisha au kumfurahisha mteja. Kama unauza bidhaa, uhakikishe bidhaa yako ni bora. Na kama biashara yako ni ya kutoa huduma, kama ile ushauri, uhakikishe huduma yako ni bora. Kwa vyovyote vile hakikisha mteja ameridhika au amefurahi. Huyu atakuwa mpiga debe wako. Ukimwudhi ataeneza habari kwa wengine na biashara yako itadhurika. Wataalam wanasema kuwa matangazo haya ya mdomo wanayofanya wateja ni msingi mkuu wa kufanikiwa au kuanguka kwa biashara.

Leo, niliporejea kutoka Car Time, nimemwelezea binti yangu Zawadi na mama watoto yote yaliyojiri, kwa furaha kubwa. Halafu jionee nilivyoandika hapa katika blogu. Nimekuwa mpiga debe wa Car Time bila wao kunilipa. Na ndivyo ilivyo katika maisha yetu. Utamsikia m-Tanzania anaisifia simu yake mpya ya "iPhone" au "smartphone" au "laptop" yake au kitu kingine, bila kutambua kuwa anaipigia debe kampuni ambayo haimlipi chochote, haimjui na wala haichangii uchumi wa Tanzania bali inajitajirisha. Tuna uwezo mkubwa sisi wateja. Laiti tungeutumia kuzitangaza bidhaa na huduma za ki-Tanzania.

Nimejifunza mengi katika kuishi hapa Marekani. Hili nililolieleza ni jambo moja. Ni elimu ambayo ninaitumia katika kuendeleza kampuni yangu ya ushauri ya Africonexion. Ninazingatia sana umuhimu wa kutoa huduma bora, kama nilivyowahi kuandika katika blogu hii.

Monday, June 15, 2015

Namshukuru Msomaji

Napenda kuweka kumbukumbu nyingine katika hii blogu yangu, kama ilivyo desturi. Wikiendi hii nimeona ujumbe kuhusu kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Ujumbe huu, ulioandikwa na Ruth Ann Baker kwenye mtandao wa Amazon, unasema:

Learned some things I don't think I could find elsewhere. There is Lots of info on relationships and social etiquette.

Nimenakili ujumbe kama ulivyoandikwa. Nimefurahi kusikia maoni ya mtu ambaye amekisoma kitabu. Namshukuru kwa kutumia muda wake adimu kuandika maoni yake, katika ukumbi ambapo watu duniani kote wanaweza kuusoma.

Ni faraja kwangu ninapoona kuwa mtu baada ya kutumia fedha zake kukinunua kitabu, na muda wake katika kukisoma, anaona hajapoteza fedha wala muda. Ningejisikia vibaya sana iwapo hali ingekuwa kinyume, kama msomaji angeona amepoteza fedha zake na muda wake.

Nimeona niandike hayo, kwani ni jadi yangu kufanya hivyo, kuwahakikishia wasomaji wa vitabu vyangu kwamba ninawaheshimu na ninawashukuru kwa maoni yao. Maoni yao ni tunu wanayonipa, bila mimi kuwalipa chochote. Ni motisha kwangu, niendelee kuandika. Malipo muafaka ninayoweza kuwalipa ni kuendelea kuandika na kujitahidi kuandika kwa ubora zaidi muda wote.

Nimefurahi pia kuona msomaji huyu amenunua toleo la Kindle la kitabu hicho. Nimewahi kuandika kuwa kitabu hiki kinapatikana kama kitabu pepe katika Kindle na pia lulu.com. Ninajifunza katika kufuatilia jinsi wasomaji wanavyokwenda na wakati katika tekinolojia ya uchapishaji wa vitabu.

Saturday, June 13, 2015

Nimepata Kitabu "Infidel" cha Ayaan Hirsi Ali

Leo nimepata kitabu Infidel cha Ayaan Hirsi Ali ambacho nilikinunua mtandaoni tarehe 3 Juni. Ayaan alizaliwa Somalia, akakulia Somalia, Saudi Arabia, Ethiopia na Kenya. Kisha alihamia u-Holanzi, ambako aliwahi hata kuwa mbunge.

Katika kukua kwake alianza kuhoji malezi ya ki-Islam aliyoyapata, na hatimaye alijitoa katika dini hii na kuwa mtu asiye na dini. Hayo amekuwa akisimulia katika vitabu na mihadhara yake. Kitabu chake cha kwanza, ambacho sina, ni The Caged Virgin: An Emancipation Proclamation for Women and Islam, ambacho Salman Rushdie amekielezea hivi:

This is an immensely important book--passionate, challenging, and necessary. It should be read as widely as possible, because it tells the truth--the unvarnished, uncomfortable truth.

Mtazamo wa Ayaan Hirsi Ali umemletea matatizo makubwa tangu mwanzo. Anatafutwa kuuawa. Alikuwa chini ya ulinzi u-Holanzi na hatimaye alihamia Marekani. Bado anaandika, anatoa mihadhara na anafanya mahojiano.

Baada ya kusikia habari zake kwa miaka kadhaa, niliamua kutafuta ukweli mimi mwenyewe. Nilinunua kitabu chake kiitwacho Nomad, nikakisoma, kama nilivyoandika katika blogu hii. Nilifahamu kuwa kitabu chake kingine kinachofahamika sana ni Infidel. Sikuwa na haraka nacho, kwani ninanunua na kusoma vitabu vingine muda wote.  Lakini, hatimaye, nimeamua kukinunua nikisome. Sijui anasema nini katika kitabu hiki, na duku duku inanisukuma nisome.

Nimenunua "Muhammad:" Kitabu cha Deepak Chopra

Jana nilipita kwenye duka la vitabu hapa Chuoni St. Olaf nikanunua kitabu kiitwacho Muhammad kilichotungwa na Deepak Chopra. Nilikiona juzi, nikawa nakiwazia, na jana nikaenda kukinunua.

Deepak Chopra ni mwandishi maarufu, ambaye mawazo yake na mtazamo wake huwagusa watu sana. Ni mhamasishaji na mtoa ushauri kuhusu masuala mbali mbali ya maisha. Ninajua hayo, ingawa sina na wala sijasoma kitabu chake hata kimoja.

Katika kukiangalia kitabu hiki cha Muhammad, nimeona kuwa Deepak Chopra ameandika pia kitabu juu ya Yesu na Buddha. Nikizngatia umaarufu wa mwandishi huyu, naona nijitahidi kusoma angalau hiki nilichonunua.

Ninacho kitabu kingine kiitwacho Muhammad: A Biography of the Prophet, kilichotungwa na Karen Armstrong. Nilikipenda, na niliwahi kuandika juu yake katika blogu hii. Nikiona kitabu hiki cha Deepak Chopra kimenifaa, nitakiongelea pia.

Blogu yangu hii ni uwanja huru kwa yoyote kutoa maoni yake. Ni uwanja huru kwa mijadala ya mada yoyote. Mara kwa mara ninaandika kuhusu vitabu, vyangu na vya wengine, vikiwemo vitabu vya dini. Nina msimamo wangu kuhusu dini mbali mbali, kuhusu misahafu na kuhusu umuhimu wa mijadala ya dini. Ninasema hayo ili mgeni katika blogu hii aelewe kwa nini leo ninaleta taarifa kuhusu kitabu kinachohusu dini tofauti na yangu.

Friday, June 12, 2015

Siku ya Mhadhara Chuo Kikuu Winona Inakaribia

Siku hazikawii. Zimebaki siku kumi na moja tu kufikia siku ya mhadhara wangu Chuo Kikuu cha Winona, utakaotokana na utafiti wangu juu ya falsafa zilizomo katika masimulizi ya jadi kama inavyodhihirika katika kitabu changu cha Matengo Folktales. Niliandika taarifa ya awali ya mhadhara huu katika blogu hii.

Leo nimeamka nikiwa nauwazia mhadhara huu kwa dhati. Nimejikuta nikijikumbusha mambo muhimu. Ninataka kwenda kutoa mhadhara madhubuti, wa kusisimua na kuelimisha. Hili huwa ni lengo langu kila ninapokubali mwaliko kama huu wa kwenda kutoa mhadhara popote.

Ninatambua wajibu wangu wa kuitendea haki taaluma. Ni wajibu wangu kama mtafiti na mwalimu kuitendea haki taaluma. Ni wajibu wangu kuwa mfano wa kuigwa na vijana wanaotafuta elimu, kama hao vijana watakaonisikiliza Chuoni Winona.

Ninatambua wajibu wangu wa kuwathibitishia wanaonialika kwamba hawakukosea kwa kunialika. Ninataka wasikilizaji wangu wakiri kuwa uamuzi wa kunialika ulikuwa sahihi. Sitaki wanaonialika na wanaonisikiliza niwaache wakisema kuwa afadhali wangemwalika mtu mwingine. Sitaki. Nataka wote wakiri kuwa mimi ndiye niliyefaa kutoa mhadhara ule. Wakiri kuwa mimi ndiye niliyefaa kujibu au kujadili masuali yao.

Ninatambua wajibu wangu mbele ya Mungu. Uhai wangu siku hadi siku, akili timamu, na vipaji alivyonipa Mungu ni dhamana kwa faida ya wanadamu. Ninapovitumia vipaji hivi ipasavyo, ninatimiza wajibu wangu kwa Mungu. Ninamtukuza Mungu. Ni furaha kwangu kutambua kwamba kutumia vipaji kwa namna hii ni kumtukuza Mungu, sawa na kusali.

Hayo ndiyo mawazo ambayo yamekuwa yakizunguka akilini mwangu tangu asubuhi. Ni aina ya mawazo yanayonisukuma nyakati kama hizi, ninapojiandaa kutekeleza mialiko. Ninapokubali mwaliko, ninafanya hivyo kwa dhati. Nikiona sitaweza kwa vigezo nilivyofafanua hapa juu, huwa nakiri tangu mwanzo ili wahusika wamtafute mtu mwingine, hata kama kwa kufanya hivyo ninajikosesha malipo yanayoendana na mwaliko.

Thursday, June 11, 2015

Kesi ya Raif Badawi: Mwanablogu wa Saudi Arabia

Raif Badawi ni mwanablogu wa Saudi Arabia ambaye anafahamika sana duniani kutokana na kuhukumiwa kifungo cha miaka kumi gerezani na viboko 1000. Alihukumiwa kwa kile kilichoitwa kuitukana dini ya u-Islam. Amekaa gerezani miaka miwili na tayari alishapigwa viboko 50 nje ya msikiti mjini Jeddah. Adhabu hiyo si nyepesi; inaweza kusababisha kifo.

Watu wengi duniani wanalaani hukumu hiyo. Wengi hawaoni ni kwa vipi Raif Badawi ameutukana u-Islam. Wengi wamechukizwa na hukumu hiyo kwa kuwa ni hujuma dhidi ya uhuru wa kutoa mawazo.

 Mawazo ya Raif Badawi yaliyosababisha hukumu dhidi yake ni ya kawaida sana kwa vigezo vyetu wa-Tanzania na wengine duniani. Lakini wahusika nchini Saudi Arabia wameendelea kusisitiza kuwa Raif Badawi anastahili hukumu hiyo. Kuna tetesi kuwa huenda akashtakiwa upya ili apewe hukumu kali zaidi, kukatwa kichwa, hukumu ambayo hutekelezwa sana Saudi Arabia.

Kesi ya Raif Badawi imeibua masuala ya ukiukwaji wa haki za binadamu nchini Saudi Arabia. Kuna mengi yanayoongelewa. Kwa mfano, ni marufuku Saudi Arabia kutoa mawazo yanayopingana na yale ya watawala na viongozi wa dini. Ni marufuku kwa watu wasio wa-Islam kujenga nyumba za ibada zao, kama vile makanisa, katika ardhi ya Saudi Arabia. Ni marufuku kuhubiri dini tofauti na u-Islam. Ni marufuku kwa wanawake kuendesha gari. Ni marufuku kwa wanawake kusafiri bila kibali cha mume au ndugu wa kiume.

Kuna kampeni kubwa sehemu mbali mbali duniani kulaani hukumu dhidi ya Raif Badawi. Sisi wanablogu wa Tanzania tunasimama wapi? Ni vema kukumbushana kuwa ukiona mwenzako ananyolewa, wewe tia maji.

Tuesday, June 9, 2015

"Song of Lawino:" Utungo wa Okot p'Bitek

Sisi tuliosoma sekondari miaka ya mwishoni ya sitini na kitu na kuendelea tunaukumbuka utungo wa Okot p'Bitek, Song of Lawino, ambao ulichapishwa na East African Publishing House, mwaka 1966. Ni utungo uliotusisimua sana kwa namna mhusika wake mkuu, Lawino, alivyozielezea tofauti baina ya utamaduni wa asili wa kabila lake la Acholi, akifananisha na utamaduni wa ki-zungu ambao mume wake anaukumbatia. Lawino ana mtazamo wa aina yake, na anatumia lugha ya ucheshi na kejeli.

Tuliosoma somo la"Literature" katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam miaka ya sabini na kitu tulikuwa na bahati ya kufundishwa utungo huu na mwalimu Grant Kamenju wa Kenya, ambaye ufundishaji wake ulikuwa wa kusisimua fikra. Alitumia nadharia za akina Karl Marx, Frantz Fanon, Eldridge Cleaver, na wengine wa kimapinduzi katika kuchambua ujumbe wa Lawino.

Alitujengea msimamo wa kuutambua ukoloni mamboleo kama alivyouelezea Fanon, hasa katika The Wretched of the Earth na Black Skin, White Masks. Kitabu cha Cleaver, Soul on Ice, kiliibua masuala yanayowasibu wa-Marekani Weusi kwa ustadi na namna ya kusisimua sawa na alivyofanya Fanon. Kiungo cha yote kilikuwa Song of Lawino.

Mambo mengi yanayotokea leo Tanzania, Afrika, na kwingineko katika hii inayoitwa "Dunia ya Tatu," katika nyanja kama uchumi, siasa, na utamaduni, yalielezwa vizuri na Frantz Fanon. Baadaye yameelezewa vizuri na wengine pia, kama vile Walter Rodney na Ngugi wa Thiong'o.

Nimeamua kuleta ujumbe huu leo kwa sababu maalum. Kwa siku kadhaa, nimekuwa nikiurekebisha mswada wangu, "Notes on the Song of Lawino," ambao ninatarajia kuuchapisha baada ya siku chache. Niliuandika miaka ya mwanzoni ya tisini na kitu, nikawa nnaurekebisharekebisha, na kisha nikauweka kando mwaka 1994. Siku chache zilizopita, nilipata hamasa ya kuanza kuushughulikia tena hadi niuchapishe, kwa kufuata mkondo wa Notes on Achebe's Things Fall Apart.

Monday, June 8, 2015

Nimerekebisha Kitabu Changu

Kwa zaidi ya wiki moja, nimekuwa nikikipitia kitabu changu cha Matengo Folktales kwa ajili ya kukiboresha. Rekebisho moja nililofanya ni kuongeza ukubwa wa herufi ili kitabu kisomeke kwa urahisi zaidi. Nilikuwa pia naangalia kama kuna kosa lolote katika uandishi wa maneno. Nimerekebisha dosari zilizoziona katika maneno yapata matano

Ingawa nimetumia masaa mengi katika shughuli hiyo, kwangu si kitu, nikifananisha na kazi niliyofanya kwa miaka yapata ishirini na tatu katika kukiandaa kitabu hiki, tangu kuzitafuta na kuzirekodi hadithi, kuziandika kwa kuzitafsiri kwa ki-Swahili, kuzitafsiri kwa ki-Ingereza, kuzichambua, kusoma nadharia mbali mbali ili kutajirisha uchambuzi, na kurekebisha tafsiri na uchambuzi tena na tena.

Bahati ni kwamba miaka ya sabini na kitu, nilianza pia kufundisha somo la fasihi simulizi ("Oral Literature") na nadharia ya fasihi (Theory of Literature") katika idara ya "Literature" ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Katika kufundisha nilijionea mwenyewe kuwa hapakuwa na kitabu nilichoona kinafaa kwa somo la fasihi simulizi kwa wanafunzi wa kiwango cha chuo kikuu. Kuna usemi kuwa kama kitabu unachosoma huridhiki nacho, andika hicho kitabu unachokitaka.

Hali hiyo ya kukosekana kitabu kilichofaa katika ufundishaji wangu ilinihamasisha kutafakari masuala niliyokuwa nakumbaba nayo katika kuandika kitabu changu. Nilipania kuwa kiwe kinafaa kwa kufundishia. Miaka ilipita, nami nikawa natafiti, natafakari, na kuandika kiasi nilivyoweza. Wakati huo huo, nilikuwa nahangaika kuziboresha tafsiri za hadithi katika muswada. Shughuli hii ilinifundisha mengi kuhusu tafsiri, kama nilivyogusia katika makala iliyochapishwa katika jarida la Metamorphoses.

Historia ya kitabu hiki ni ndefu, na labda nitaweza kuiandika kiasi fulani siku za usoni. Ninakumbuka, kwa mfano, kwamba nilipokuwa nasomea masomo ya juu katika Chuo Kikuu cha Wisconsin, 1980-86, nilichukua somo la nadharia ya fasihi katika idara ya "Comparative Literature" lililofundishwa na Professor Keith Cohen. Kati ya nadharia tulizojifunza ni "Structuralism." Professor Cohen alitupa "homework" ya kuchambua hadithi yoyote kwa kutumia nadharia ya "Structuralism."

Nilitumia fursa hii kuichambua hadithi ya "The Tale of Two Women," ambayo imo katika Matengo Folktales. Mtu anayefahamu angalau kidogo nadharia ya "Structuralism" ataona athari zake, japo kidogo,  katika uchambuzi wangu.

Baada ya harakati za aina aina kwa miaka mingi, nilichapisha kitabu hiki mwaka 1999. Ndoto yangu ya kuandika kitabu cha kutumiwa katika ufundishaji wangu Chuo Kikuu cha Dar es Salaam haikutimia nilivyotarajia. Niliondoka Tanzania mwaka 1991, nikaja kufundisha katika idara ya ki-Ingereza Chuoni St. Olaf, huku  nikiwa bado naufanyia kazi mswada wangu. Kwa hivi kitabu kilichapishwa huku Marekani, na wanaokisoma ni wa-Marekani, kuanzia katika jamii hadi vyuoni, kama nilivyoelezea hapa na  hapa.

Masimulizi ni mengi, na kama nilivyogusia, labda nitafute wasaa miaka ijayo niandike kumbukumbu zangu za historia ya kitabu hiki.

Mhadhiri wa Algeria Amefurahi Kupata Kitabu

Jana, niliporejea kutoka kanisani, nilikuta ujumbe katika ukurasa wangu wa Facebook kutoka kwa Samir Zine Arab, mhadhiri wa "African Literature and Listening Skills" katika chuo kikuu cha Hassiba Ben Bouali Chlef, Algeria. Alikuwa anashukuru kupata nakala ya kijitabu changu, Notes on Achebe's Things Fall Apart ambayo nilimtumia siku kadhaa zilizopita.

Ujumbe wake, ulioambatana na picha inayoonyesha kitabu pamoja na bahasha niliyotumia, kama inavyoonekana hapa kushoto, ameusambaza kwa marafiki zake wa Facebook ambao mimi ni mmoja wao. Amenigusa kwa namna alivyoandika:

Dear friends, brothers and sisters! Today I'm the happiest man on earth! This morning I received a lovely book from a great professor Joseph Mbele! Thank you so much dear!!

Pamoja na ujumbe huu, Mwalimu Samir ameniandikia pia ujumbe binafsi ambao nao umenigusa sana. Kwake na kwangu imekuwa ni furaha. Ninavutiwa na watu wa aina ya huyu mwalimu, ambao wana duku duku ya kutafuta elimu. Aliposikia tu kuhusu kijitabu changu, alikitaka.

Ninafurahi kuwa wanafunzi Algeria watapata fursa ya kuyafamu na kuyatafakari mawazo niliyoandika katika kijitabu hiki, ambacho Mwalimu Samir alikitamani tangu nilipokitaja katika Facebook, tarehe 11 Mei. Taarifa zaidi za kijitabu hiki niliandika katika blogu hii. Tangu nilipoandika taarifa hiyo, kuna kitu cha ziada ambacho nimefanya. Nimechapisha kijitabu hiki kama kitabu pepe, yaani "ebook."

Sunday, June 7, 2015

Nimetoka Kanisani Kusali

Ni Jumapili, saa sita na kidogo mchana. Nimetoka kanisani kusali. Mimi ni m-Kristu wa kawaida, m-Katoliki. Namwabudu Mungu na ninaamini kuwa yeye ndiye anayeongoza maisha yangu. Katika raha na matatizo, ninamtegemea yeye. Ninamshukuru kwa kunipa uhai siku hadi siku.

Namshukuru Mungu kwa kunipa akili na utashi nitafakari mambo na kujiamulia. Ninamshukuru kwa jinsi anavyotuneemesha, kwa kuwaumba wanadamu wa kila aina, wenye dini mbali mbali, tamaduni na lugha mbali mbali. Dunia inapendeza kwa tofauti hizo, sawa na maua yanavyopendeza, kwa uwingi wa tofauti za rangi.

Namshukuru Mungu kwa yote aliyoyaweka duniani: nchi kavu, bahari, milima, mabonde, mito, miti, majani na maua. Ametuwekea wanyama wa kila aina, ndege na wadudu, jua, mwezi na nyota, mvua na upepo, vitu vinavyoonekana na visivyoonekana.

Vyote ni mazao ya uumbaji wa Mungu. Ninaomba niwe na moyo wa kuwapenda wanadamu wote na vyote alivyoumba Mungu. Ninaomba niwe mtu mwema, mwenye kutambua na kuzingatia kila siku kuwa Mungu amenipa uhai, akili, na vipaji, si kwa ajili yangu, bali kwa manufaa ya walimwengu bila kujali tofauti zao, za taifa, kabila, dini, jinsia, umri, utamaduni, lugha, na kadhalika.

Kuwa kanisani, kujumuika na waumini wenzangu, ni fursa ya kujikumbusha imani ya dini yangu, kuwaombea walimwengu wote, wabarikiwe. Sasa, baada ya kutoka kanisani, ninajisikia mwenye faraja, moyo mkunjufu, na ari ya kuendelea na majukumu yangu.

Friday, June 5, 2015

Ninaombwa Tafsiri ya Kitabu Changu

Mara kadhaa, wa-Marekani wameniuliza iwapo kitabu changu Africans and Americans: Embracing Cultural Differences kimetafsiriwa kwa ki-Swahili au wameniomba nikitafsiri. Hao ni watu ambao wameishi au wanaishi Afrika Mashariki, hasa kwa shughuli za kujitolea.

Tangu nilipoanza kupata maulizo au maombi hayo, nimekuwa na wazo la kukitafsiri kitabu hiki. Mwanzoni kabisa, kwa kuzingatia uwingi wa wa-Somali walioingia na wanaendelea kuingia hapa Minnesota, ambao nimekuwa nikiwasaidia katika kuufahamu utamaduni wa Marekani, niliwazia kumwomba mmoja wa marafiki zangu wa ki-Somali atafsiri kitabu hiki kwa ki-Somali. Ninao marafiki kadhaa wa ki-Somali ambao, sawa na wa-Afrika wengine, wamekisoma na wanakipenda kitabu hiki. Lakini bado sijalitekeleza wazo hilo.

Jana nimepata ujumbe wa aina hiyo kutoka kwa mama mmoja m-Marekani, ambaye simfahamu. Ninanukuu sehemu ya ujumbe wake, na nimeweka nukta nne mahali ambapo kuna maneno ambayo sijayanukuu:

....I hope one day that you will translate your wonderful book. It is such a wealth of knowledge for me, and I know my Tanzanian friends would feel the same. Of course most good people would never mean to hurt or offend a new acquaintance, but sometimes when we are lucky enough to make a friend from a different country, we can use a little guidance on how to be respectful of each others cultural differences. Your book has given me that gift, and so I thank you for that!....Last year I went to Africa for the wildlife, but I found it was the Tanzanian people who stole my heart. This year I will return and visit Eli's village and meet his family. I am so excited about my visit. That is why it is so important to me to do my best to not be the classic "UGLY AMERICAN". Thank you again for your response. I hope you will consider writing the Kiswahili version of your book in the future. I know there would be many people who would find it both helpful and fascinating, as I did....

Natafsiri ujumbe huu ifuatavyo:

....Natumaini siku moja utakitafsiri kitabu chako murua. Ni hazina kubwa ya maarifa kwangu, na ninajua kuwa marafiki zangu wa-Tanzania watakiri hivyo. Ni wazi kuwa watu wengi wenye roho nzuri hawanuii kumuumiza au kumkosea mtu pindi wanapofahamiana, lakini mara nyingine tunapobahatika kumpata rafiki kutoka nchi nyingine tunaweza kunufaika na mwongozo wa namna ya kuheshimiana kutokana na tofauti za tamaduni zetu. Kitabu chako kimekuwa tunu ya aina hiyo, na nakushuru kwa hilo....Mwaka jana nilikwenda Afrika kuwaona wanyama mbugani, lakini waliouteka moyo wangu ni wa-Tanzania. Mwaka huu nitaenda tena kijijini kwa Eli na kukutana na familia yake. Ninafurahi sana ninavyoingojea safari hiyo. Ndio maana ni muhimu sana kwangu kujitahidi kwa namna yoyote kutokuwa yule anayefahamika kama "M-MAREKANI WA OVYO." Narudia kukushukuru kwa jawabu lako. Ninatumaini utalichukulia maanani suala la kuandika toleo la ki-Swahili la kitabu chako siku zijazo. Ninajua kitabu hiki kitawasaidia na kuwasisimua wengi kama ilivyokuwa kwangu....

Kwa wale ambao hawafahamu, hii dhana ya "Ugly American" imejengeka sana katika mawazo ya wa-Marekani wanaoamini kuwa tabia ya wa-Marekani wanapokuwa nje za kigeni si nzuri. Dhana hiyo ilishamiri baada ya kuchapishwa kwa kitabu cha Eugene Burdick na William J. Lederer kiitwacho The Ugly American.

Sina la nyongeza la kusema kwa leo, bali kujiuliza: mimi ni nani niyapuuze maombi ya watu? Ninapaswa kuchukua hatua stahiki, nikizingatia ule usemi maarufu wa ki-Latini: "Vox Dei vox populi," yaani sauti ya umma ni sauti ya Mungu.

Thursday, June 4, 2015

Kitabu "Africans and Americans" Kiko Manyara

Kitabu changu Africans and Americans: Embracing Cultural Differences ambacho kinafahamika kwa wasomaji wa blogu hii na blogu yangu ya ki-Ingereza, sasa kinapatikana Burunge Visitors Center(BVC) mkoani Manyara.

BVC ilianzishwa kwa ajili ya kuratibu uhifadhi wa mazingira na kuendesha shughuli za utalii kwa manufaa ya jamii. BVC inatoa elimu kwa jamii na wageni kuhusu mazingira, historia, na utamaduni.

Kwa mujibu wa shughuli zangu kama mtoa ushauri na mwelimishaji wa masuala ya utamaduni, ushirikiano na BVC ni jambo lenye mantiki ya wazi. Kwa hivi, tumechukua hatua hii ya BVC kujipatia vitabu vyangu ninavyovichapisha kwa jina la  kampuni yangu ya Africonexion: Cultural Consultants ili kiviuza katika duka lao.

Watu walioko Tanzania wanaohitaji vitabu hivi wanaweza kutuma barua pepe: info@burungevisitorscentre.or.tz au imborutours@gmail.com au kupiga simu zilizoorodheshwa kwenye tovuti:  http://www.burungevisitorscentre.or.tz/

Wednesday, June 3, 2015

Nadharia ya Uandishi

Uandishi ni nini? Je, kila uandishi ni uandishi wa kweli? Uandishi wa kweli ni nini? Naona haya ni masuali ya msingi. Ningependa tuyatafakari. Waandishi wengi maarufu wameandika kuhusu masuala hayo. Katika kitabu chake, Letters to a Young Novelist, Mario Vargas Llosa, mwandishi maarufu kutoka Peru, aliandika:

The defining characteristic of the literary vocation may be that those who possess it experience the exercise of their craft as its own best reward, much superior to anything they might gain from the fruits of their labors. That is one thing I am sure of amid my many uncertainties regarding the literary vocation: deep inside, a writer feels that writing is the best thing that ever happened to him, or could ever happen to him, because as far as he is concerned, writing is the best possible way of life, never mind the social, political, or financial rewards of what he might achieve through it.

Nitafsiri kwa ki-Swahili:

Utambulisho mahsusi wa wito wa uandishi labda ni kwamba wale wenye wito huo huutambua uandishi kama tunu kubwa kuliko zote, bora kuliko chochote wanachoweza kukipata kutokana na juhudi yao. Hiki ni kitu kimoja ambacho nina uhakika nacho ingawa nimezingirwa na masuali yaletayo wasiwasi kuhusu wito wa uandishi: ndani ya nafsi yake, mwandishi hujisikia kuwa uandishi ni kitu bora kabisa kumtokea au kinachoweza kumtokea, kwa sababu kwa mtazamo wake, uandishi ni mkondo bora kabisa wa maisha, bila kujali manufaa ya kijamii, kisiasa, au kifedha anayoweza kuyapata kwa uandishi.

Kama ilivyo tafsiri yoyote, tafsiri yangu hainasi kila kipengele cha ujumbe wa mwandishi, hasa tukizingatia kuwa tafsiri yangu ni tafsiri ya tafsiri, kwani Mario Vargas Llosa aliandika kwa ki-Hispania. Hata hivi naamini kuna mambo muhimu yanayojitokeza. Mfano ni msisitizo kuwa uandishi kwa wenyewe ni tunu ya thamani kuliko zote. Ni kama kusema kuwa uandishi wa kweli ni ule unaomletea mwandishi faraja kamili na kumfanya asijali matokeo mengine ya uandishi wake, kama vile sifa na fedha.

Nilipokinunua kitabu hiki cha Mario Vargas Llosa, miaka michache iliyopita, nilianza kukisoma nikakutana na dhana fulani ambazo nilishakutana nazo katika maandishi ya Shaaban Robert. Waandishi maarufu wa lugha yoyote ni watu wenye utajiri wa fikra. Hili ni fundisho kwa waandishi chipukizi.

Wakati huu ninaposoma Letters to a Young Novelist, ninasoma pia The Naïve and the Sentimental Novelist, kitabu cha Orhan Pamuk, ambacho nilikinunua hivi karibuni. Orhan Pamuk ni mwandishi maarufu wa U-Turuki, ambaye alipata tuzo ya Nobel. Kitabu chake hiki nacho kinaelezea mtazamo wake kuhusu uandishi. Niliwahi kumtaja mwandishi huyu katika blogu hii, katika kulalamika kuwa maisha hayaturuhusu kusoma vitabu vyote muhimu.

Monday, June 1, 2015

Blogu Zangu Zimenisaidia

Hapa Chuoni St. Olaf kuna utaratibu unaomtaka kila mwalimu kuandika ripoti ya shughuli alizofanya katika mwaka wa shule unaoisha. Hizo ni shughuli za kitaaluma, yaani vitabu ulivyochapishwa, makala ulizochapisha, ushiriki wako katika mikutano ya kitaaluma, kazi ulizofanya katika uongozi wa vyama vya kitaaluma, kozi ulizotunga na kufundisha, uhariri katika majarida ya kitaaluma. Vile vile unaorodhesha huduma ulizotoa katika jamii nje ya chuo, kama vile ushauri ("consultancy"), na mihadhara katika mikutano ya vikundi na jumuia.

Nimekuwa na jadi ya kuandika mambo ya aina hiyo katika blogu hii ya hapakwetu na blogu ya ki-Ingereza. Katika kuandika ripoti yangu ya mwaka unaoisha, blogu zangu zimekuwa hazina ya kumbukumbu na taarifa nilizohitaji. Huu ni uthibitisho wa manufaa ya shughuli ninayofanya ya kublogu. Ninakumbuka kuwa niliwahi kuelezea namna blogu ilivyonisaidia darasani.

Watu wengine wanaandika kumbukumbu zao katika "diary." Lakini mimi kwa vile sina mazoea ya kufanya hivyo, nitaendelea kublogu kama ninavyofanya. Lengo ni kuhifadhi kumbukumbu. Tena, kwa kuwa nimezoea kuelezea shughuli zangu kwa upana, tangu chimbuko hadi matokeo, taarifa zangu zitaweza kutumika hata kwa kuandika kitabu. Ndoto ya kuandika kitabu cha aina hiyo nimekuwa nayo kitambo. Panapo majaliwa, nitaitekeleza.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...