Showing posts with label mikutano. Show all posts
Showing posts with label mikutano. Show all posts

Monday, June 1, 2015

Blogu Zangu Zimenisaidia

Hapa Chuoni St. Olaf kuna utaratibu unaomtaka kila mwalimu kuandika ripoti ya shughuli alizofanya katika mwaka wa shule unaoisha. Hizo ni shughuli za kitaaluma, yaani vitabu ulivyochapishwa, makala ulizochapisha, ushiriki wako katika mikutano ya kitaaluma, kazi ulizofanya katika uongozi wa vyama vya kitaaluma, kozi ulizotunga na kufundisha, uhariri katika majarida ya kitaaluma. Vile vile unaorodhesha huduma ulizotoa katika jamii nje ya chuo, kama vile ushauri ("consultancy"), na mihadhara katika mikutano ya vikundi na jumuia.

Nimekuwa na jadi ya kuandika mambo ya aina hiyo katika blogu hii ya hapakwetu na blogu ya ki-Ingereza. Katika kuandika ripoti yangu ya mwaka unaoisha, blogu zangu zimekuwa hazina ya kumbukumbu na taarifa nilizohitaji. Huu ni uthibitisho wa manufaa ya shughuli ninayofanya ya kublogu. Ninakumbuka kuwa niliwahi kuelezea namna blogu ilivyonisaidia darasani.

Watu wengine wanaandika kumbukumbu zao katika "diary." Lakini mimi kwa vile sina mazoea ya kufanya hivyo, nitaendelea kublogu kama ninavyofanya. Lengo ni kuhifadhi kumbukumbu. Tena, kwa kuwa nimezoea kuelezea shughuli zangu kwa upana, tangu chimbuko hadi matokeo, taarifa zangu zitaweza kutumika hata kwa kuandika kitabu. Ndoto ya kuandika kitabu cha aina hiyo nimekuwa nayo kitambo. Panapo majaliwa, nitaitekeleza.

Sunday, August 22, 2010

Kukutana kwa Wanablogu

Katika ziara yangu Tanzania mwaka huu, pamoja na mengi mengine, nilipata fursa ya kukutana na wanablogu. Tarehe 7 Agosti nilikutana na Kamala na Chacha pale Sinza kama inavyoonekana katika picha hii.
Tuliongea na kubadilishana mawazo ya aina aina, kama alivyoeleza Kamala katika blogu yake. Chacha naye aliandika ujumbe kuhusu mkutano wetu. Bofya hapa.

Tarehe 17 Agosti, hapo hapo Sinza, nilikutana na mwanablogu Maggid Mjengwa. Bofya hapa.Tuliongea kuhusu mambo mengi, kuanzia gazeti la Kwanza Jamii, masuala ya blogu, yakiwemo masuala ya faida na kero zake.

Tuliongelea, kwa mfano, namna ya kuyachukulia maudhi ya baadhi ya watoa maoni kwenye hizi blogu. Tangu tulipokuwa tunaandika katika Kwanza Jamii, sisi wawili tumekuwa na msimamo kwamba ni bora kuwaacha watu waseme hata kama wanachosema kinaudhi, kwa msingi kuwa labda wanahitaji kufanya hivyo kwa manufaa yao kisaikolojia, mbali na kwamba tunazingatia suala la uhuru wa kutoa maoni na fikra. Ni msimamo mgumu unaohitaji uvumilivu, lakini labda ni bora kuwa na msimamo huu kuliko msimamo wa kuwazuia watu uhuru. Msimamo huu nimeuelezea kinaganaga katika kitabu changu cha CHANGAMOTO.

Naona kuwa suala la kukutana na wanablogu wenzangu Tanzania linazidi kuwa jadi. Nilianza kufanya hivyo mwaka jana, nilipokutana na mwanablogu maarufu Issa Michuzi. Waliofanya juhudi kuniunganisha na Issa Michuzi ni Maggid Mjengwa na Frederick Mboma. Hatimaye, Ndugu Mboma ndiye aliyenifikisha ofisini kwa Michuzi, tukaongea kuhusu masuala ya aina aina, hasa blogu. Bofya hapa.

Mikutano hii ya wanablogu ina manufaa mengi, kama walivyosema wanablogu wengine. Ni fursa ya kufahamiana na kubadilishana mawazo kuhusu masuala ya blogu na mengine. Katika mkutano wangu na Chacha na Kamala, jambo moja lililosisitizwa ni suala la kujitambua. Hao wawili wanajibidisha katika kufuatilia mada hii wakijumuika na wengine. Nami niliona ni vema nasi wanablogu tuwe tunatakafakari suala hili la kujitammbua. Kwa hivi, niliuliza suali: kwa nini tunablogu? Bofya hapa.

Mwaka jana, wazo la kuwakutanisha wanablogu wa Tanzania lilipendekezwa na kujadiliwa. Ingawa mkutano huu haukufanyika, wazo linastahili kufanyiwa kazi na kutekelezwa.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...