Sunday, August 22, 2010

Kukutana kwa Wanablogu

Katika ziara yangu Tanzania mwaka huu, pamoja na mengi mengine, nilipata fursa ya kukutana na wanablogu. Tarehe 7 Agosti nilikutana na Kamala na Chacha pale Sinza kama inavyoonekana katika picha hii.
Tuliongea na kubadilishana mawazo ya aina aina, kama alivyoeleza Kamala katika blogu yake. Chacha naye aliandika ujumbe kuhusu mkutano wetu. Bofya hapa.

Tarehe 17 Agosti, hapo hapo Sinza, nilikutana na mwanablogu Maggid Mjengwa. Bofya hapa.Tuliongea kuhusu mambo mengi, kuanzia gazeti la Kwanza Jamii, masuala ya blogu, yakiwemo masuala ya faida na kero zake.

Tuliongelea, kwa mfano, namna ya kuyachukulia maudhi ya baadhi ya watoa maoni kwenye hizi blogu. Tangu tulipokuwa tunaandika katika Kwanza Jamii, sisi wawili tumekuwa na msimamo kwamba ni bora kuwaacha watu waseme hata kama wanachosema kinaudhi, kwa msingi kuwa labda wanahitaji kufanya hivyo kwa manufaa yao kisaikolojia, mbali na kwamba tunazingatia suala la uhuru wa kutoa maoni na fikra. Ni msimamo mgumu unaohitaji uvumilivu, lakini labda ni bora kuwa na msimamo huu kuliko msimamo wa kuwazuia watu uhuru. Msimamo huu nimeuelezea kinaganaga katika kitabu changu cha CHANGAMOTO.

Naona kuwa suala la kukutana na wanablogu wenzangu Tanzania linazidi kuwa jadi. Nilianza kufanya hivyo mwaka jana, nilipokutana na mwanablogu maarufu Issa Michuzi. Waliofanya juhudi kuniunganisha na Issa Michuzi ni Maggid Mjengwa na Frederick Mboma. Hatimaye, Ndugu Mboma ndiye aliyenifikisha ofisini kwa Michuzi, tukaongea kuhusu masuala ya aina aina, hasa blogu. Bofya hapa.

Mikutano hii ya wanablogu ina manufaa mengi, kama walivyosema wanablogu wengine. Ni fursa ya kufahamiana na kubadilishana mawazo kuhusu masuala ya blogu na mengine. Katika mkutano wangu na Chacha na Kamala, jambo moja lililosisitizwa ni suala la kujitambua. Hao wawili wanajibidisha katika kufuatilia mada hii wakijumuika na wengine. Nami niliona ni vema nasi wanablogu tuwe tunatakafakari suala hili la kujitammbua. Kwa hivi, niliuliza suali: kwa nini tunablogu? Bofya hapa.

Mwaka jana, wazo la kuwakutanisha wanablogu wa Tanzania lilipendekezwa na kujadiliwa. Ingawa mkutano huu haukufanyika, wazo linastahili kufanyiwa kazi na kutekelezwa.

3 comments:

Fadhy Mtanga said...

mie nawapongezeni sana kwa kukutana. Kukutana ni jambo la muhimu sana, kwani zaidi ya kufahamiana kuna mambo mengi ya kujadiliana.

Yasinta Ngonyani said...

Kwa kweli kublog ni raha sana yaani sasa tumekuwa kama familia moja. Inafurahisha sana kwa ukutanaji mfanyao na tunashukuru kwa kugana nasi mambo mnayojadili.Upendo Daima.

Simon Kitururu said...

Tuko Pamoja!

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...