Saturday, October 28, 2017

Papa's Shadow: Filamu Kuhusu Ernest Hemingway

Kampuni ya Ramble Pictures, ambayo inatengeneza filamu, imemaliza kutengeneza filamu inayohusu safari za mwandishi Ernest Hemingway Afrika Mashariki miaka ya 1933-34 na 1953-54. Nilishaandika taarifa za awali kuhusu filamu hiyo katika blogu hii.

Sehemu kubwa ya filamu hii ni mazungumzo baina ya Mzee Patrick Hemingway na mimi kuhusu safari hizo za Ernest Hemingway, falsafa yake juu ya maisha na sanaa. Patrick Hemingway ni moto pekee wa Ernest Hemingway aliye bado hai. Filamu inaelezea mambo juu ya mwandishi Ernest Hemingway ambayo yalikuwa hayafahamiki vizuri, hasa juu ya namna mwandishi huyu alivyoipenda Afrika.

Filamu hii inaitangaza Tanzania, kwa kuwa inaonyesha maeneo kadhaa ya nchi na watu wake, pamoja na safari ya kupanda Mlima Kilimanjaro. Chimbuko muhimu la filamu hii ni kozi niliyotunga na kufundisha iitwayo Hemingway in East Africa. Nilisafiri na wanafunzi 29 wa chuo cha St. Olaf, ninapofundisha, tukawa tunapita katika maeneo kadhaa ya Tanzania ambamo Ernest Hemingway alipita, huku tukisoma na kujadili maandishi yake kuhusu sehemu hizo.

Wakati filamu hiyo ilipokuwa inatengenezwa, niliweka taarifa mtandaoni, na nilipeleka taarifa sehemu kadhaa katika mfumo wa serikali ya Tanzania, kuelezea jinsi filamu hii itakavyoitangaza Tanzania. Nilifarijika kupata ujumbe kutoka Uwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, ukiafiki kuwa hii ni "fursa maridhawa ya kuitangaza Tanzania ulimwenguni" kama nilivyoelezea katika blogu hii.

Filamu inapatikana katika tovuti ya Ramble Pictures.

Wednesday, October 25, 2017

Ninangojea Mwaliko Kuelezea Tamaduni

Nimeona tangazo la chuo kimoja cha hapa Minnesota kwamba wanajiandaa kuwapeleka wanafunzi kwenye nchi moja ya Afrika. Ni programu ambayo wamekuwa nayo kwa miaka kadhaa. Kila mara, wamekuwa wakitumia kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences katika maandalizi hayo, ili kufahamu mambo ya msingi ya tofauti za tamaduni. Wamekuwa wakinialika kuongea nao kabla ya safari.

Nilivyoona tangazo nilijisemea kuwa hawa watu lazima watatafuta kitabu changu tena, na watanitafuta tena, kutokana na nilivyoona siku zilizopita. Nimejifunza tangu zamani kuwa unapotoa huduma kwa mteja, toa huduma bora kiasi cha kumfanya mteja asiwe na sababu ya kutafuta huduma kwingine.

Kwa upande wangu, nilijenga uhusiano huu na wateja kwa awamu. Mwanzoni, nilikuwa ninatoa ushauri tu, hasa katika program za kupeleka wanafunzi Afrika, zinazoendeshwa na vyuo mbali mbali vya Marekani. Baadaye, nilichapisha kitabu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences,  na hicho kikawa kinawavutia wateja wapya. Si kwamba kitabu hiki kina kila kitu. Vile vile, wanaonialika hawanialiki nikawasomee hiki kitabu. Wanakuwa wameshakisoma, ila wanakuwa na shauku ya kujua zaidi kutoka kwangu mwandishi. Kitabu ni kama chambo na kianzio cha mazungumzo.

Ninaandaa kitabu kingine cha kuendeleza yaliyomo katika Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Kitakuwa na mwelekeo ule ule na mtindo ule ule, ila kitaibua mambo mapya. Tayari nimeshakipa jina, Chickens in the Bus, ambacho ni kichwa cha sura mojawapo katika kitabu hiki.

Thursday, October 19, 2017

"Men Made Out of Words" ( Wallace Stevens)

Wallace Stevens ni mmoja wa washairi maarufu wa Marekani. Mara ya kwanza kupata fursa ya kuyasoma mashairi yake ni nilipokuwa ninasomea shahada ya uzamifu katika huo kikuu cha Wisconsin-Madison,1980-86. Nilichukua kozi kadhaa katika idara ya ki-Ingereza, mojawapo ikiwa "Poetry." Alitufundisha profesa John Brenkman.

Profesa Brenkman alikuwa na mtindo wa kufundisha ambao ulilifanya somo la "Poetry" livutie. Kwa uzoefu wangu wa kabla ya hapo, katika kusoma Tanzania, ushairi wa ki-Ingereza ndilo lilikuwa somo gumu kuliko mengine. Nilidokeza jambo hilo katika kijitabu changu cha Notes on Okot p Bitek's Song of Lawino.

Tangu nilipofundishwa na Profesa Brenkman, jina la Wallace Stevens limekuwa linanivutia, na daima niko tayari kusoma mashairi yake. Huu ni ushahidi wa jambo ambalo linafahamika vizuri, yaani namna mwalimu bora anavyoweza kumwathiri mwanafunzi. Jana nimeangalia kitabu changu cha mashairi, The Voice That is Great Within Us, na shairi moja lililonivutia ni "Men Made Out of Words," la Wallace Stevens. Ni shairi ambalo limeandikwa kwa uchache wa maneno na tamathali za usemi, na falsafa yake inachangamsha bongo.

MEN MADE OUT OF WORDS (Wallace Stevens)

What should we be without the sexual myth,
The human revery or poem of death?

Castratos of moon-mash--Life consists
Of propositions about life. The human

Revery is a solitude in which
We compose these propositions, torn by dreams,

By the terrible incantations of defeats
And by the fear that defeats and dreams are one.

The whole race is a poet that writes down
The eccentric propositions of its fate.


Thursday, October 12, 2017

Profesa Amekifurahia Kitabu

Ni kawaida yangu, kuchapisha maoni ya wasomaji wa vitabu vyangu. Leo nimepata ujumbe kutoka kwa profesa moja ambaye alihudhuria mkutano wa Africa Network nilioshiriki kuuandaa hapa chuoni St. Olaf.

Profesa huyu Mmarekani anawapeleka wanafunzi wa ki-Marekani Kenya na Rwanda. Katika mkutano wetu, aliongelea programu hiyo, akielezea jinsi tofauti za tamaduni zinavyojitokeza.

Nilivutiwa na mhadhara wake, kwa kuwa nami ni mzoefu wa programu hizi za kupeleka wanafunzi Afrika, ikiwemo Tanzania. Nilimpelekea kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, naye ameniandika ujumbe huu:

Dear Joseph,
There were several wonderful things that came from my attending the Africa Network conference. Meeting you and learning more is one. I just finished your book and enjoyed it so much. It made me laugh out loud and understand my Kenyan teaching colleague even more. I have been both to Rwanda and Kenya many times and am aware of many of the situations and misunderstandings you describe. I’ve shared my thoughts with Kitito and we hope to use your book in some way for our spring Cultural Identity course. 
Thanks again.

Ninashukuru kwamba kitabu hiki kinatoa mchango ambao nilipangia nilipokiandika, ikiwemo kuwaelimisha wanaohusika na programu za kupeleka wanafunzi Afrika. Msukumo wa kukiandika ulitoka katika mikutano ya jumuia ya vyuo iitwayo Associated Colleges of the Midwest (ACM), na baada ya kukichapisha, wahusika wa programu zingine nao wanakitumia. Mifano ni programu ya  chuo kikuu cha Wisconsin-Oshkosh na pia program ya chuo cha Gustavus Adolphus, ambayo nimeitaja mara kwa mara katika blogu hii.


Saturday, October 7, 2017

Tamasha la Kimataifa Mjini Faribault

Leo nilikuwa mjini Faribault kushiriki tamasha la kimataifa International Faribault Festival. Nimeshiriki tamasha hilo kwa miaka kadhaa kama mwalimu, mwandishi, na mtoa ushauri kuhusu masuala ya tofauti za tamaduni.

Hapa kushoto ni wanafunzi waliokuwa wanaongoza shughuli katika ukumbi mkuu wa tamasha. Shughuli hizo zilikuwa ni maonesho ya burudani, hasa ngoma za mataifa mbali mbali.


















































































































Watu wa kila rika walihudhuria, kama ilivyo kawaida katika matamasha haya hapa Marekani. Kulikuwa ni michezo mbali mbali ya watoto.


Nilikwenda na vitabu vyangu na machapisho mengine, kama inavyoonekana picha ya mwisho hapa kushoto. Kama kawaida, vitu hivyo huwa ni kivutio kwa watu na wanafika hapa mezani kuangalia na pia kuongea nami. Hiyo leo ilikuwa ni hivyo hivyo. Niliongea na watu wengi, kuanzi watoto hadi wazee.

Kwa mfano, huyu bibi anayeonekana kulia, mwenye nywele nyeupe, tuliongea sana. Alinieleza kuwa anamfadhili binti yatima aliyeko Ethiopia. Tuligusia tofauti za tamaduni, nikamweleza jinsi ilivyo muhimu kuzitafakari, kwani zinaathiri tabia, mawasiliano, na mengine. Mama mwingine aliyekuja hapa mezani pangu alisema anafundisha ki-Ingereza kwa wahamiaji kutoka nchi mbali mbali. Hapa Marekani, program hii inajulikana kama ESL, ambayo kirefu chake ni English as a Second Language. Basi, tuliongelea kidogo jinsi tofauti za tamaduni zinavyojitokeza katika programu hiyo, akanunua kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Friday, October 6, 2017

Mkutano wa Africa Network Chuoni St. Olaf

Tarehe 29 September hadi 1 Oktoba, palifanyika mkutano wa Africa Network, hapa chuoni St. Olaf. ambapo ninafundisha. Africa Network ni jumuia ya vyuo vyenye kujihusisha na uendelezaji wa masomo kuhusu Afrika, katika taaluma mbali mbali. Jumuia hiyo ilianzishwa mwaka 2004 na watu wachache  kutoka vyuo mbali mbali, na mwaka hadi mwaka imekuwa ikivutia watu kutoka vyuo vingine.

Tumekuwa tukifanya mikutano ya mara kwa mara. Miaka ya mwanzo tulikuwa tukifanya mkutano kila mwaka, lakini miaka michache iliyopita tuliamua kuwa tukutane mara moja katika miaka miwili.

Katika mkutano wetu wa mwaka 2015, nilipendekeza kuwa mkutano wa mwaka huu ufanyike hapa chuoni St. Olaf. Kwa hivyo, nilibeba jukumu la kufuatilia kwa karibu kila kipengele cha maandalizi hayo, na hatimaye tumefanya mkutano kwa mafanikio makubwa.

Tumejadili mada mbali mbali zilizowasilishwa, tukabadilishana uzoefu na mikakati kuhusu ufundishaji. Tumejadili mipango na mikakati ya kupeleka wanafunzi Afrika kimasomo na changamoto  zake. Tumejadili sio tu masuala ya ufanisi bali pia maadili katika shughuli hizo.

Baadhi ya wahudhuriaji ni wa tangu zamani, lakini wengi walikuwa wapya. Tumefanikiwa kuwavuta watu kutoka vyuo vya mbali, hadi Afrika Kusini, ambao wako Marekani kwa wakati huu. Tumejifunza na tumefundishana mengi, na pia tumejengea mahusiano mapya yatakayotupeleka mbele katika shughuli zetu.


Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...