Saturday, September 26, 2015

Nimehojiwa Kuhusu Hemingway na "Papa's Shadow"

Leo nimekuwa na mahojiano na mwandishi wa gazeti la Manitou Messenger linalochapishwa hapa chuoni St. Olaf. Ni gazeti la wanafunzi, ambalo limekuwa likichapishwa kila wiki kwa miaka 125. Mahojiano yetu yalikuwa juu ya filamu ya Papa's Shadow. Katika ujumbe wa kuomba mahojiano, mwandishi aliandika:

...we are doing a feature article this week on the documentary, Papa's Shadow and Ramble Pictures. We learned that you were instrumental in the inspiration for and production of this film, and we were hoping you could answer a few quick questions.

Katika mahojiano, tumeongelea nilivyoanza kuvutiwa sana na mwandishi Ernest Hemingway, nilipoombwa na Thomson Safaris kuongoza msafara mkubwa wa wanafunzi, wazazi na walimu, katika safari ya Tanzania mwaka 2002. Hatimaye, baada ya miaka mitano ya kusoma maandishi na habari za Hemingway, nilitunga kozi Hemingway in East Africa, kwa ajili ya Chuo cha Colorado.

Baadaye, niliona niunde kozi hiyo kwa ajili ya wanafunzi wa Chuo cha St. Olaf. Nilifanya hivyo mwaka 2012. Wakati wa kuandikisha wanafunzi, alinifuata kijana aitwaye Jimmy Gildea, akaniomba nimruhusu kujiunga na kozi, kwa kuwa alimpenda Hemingway na alitaka kurekodi filamu ya kozi. Nilimsajili katika darasa.

Kozi ilikwenda vizuri, kama nilivyoandika hapa. Baada ya kurejea tena Marekani, baadhi yetu tulifunga safari ya jimbo la Montana kuonana na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee aliyebaki wa Ernest Hemingway. Tuliongea naye sana.

Jimmy alikuwa amenirekodi ofisini mwangu nikizungumza juu ya Hemingway, akachanganya mazungumzo haya na yale tuliyofanya na Mzee Patrick Hemingway,na akaongezea mambo mengine aliyorekodi Tanzania. Kwa bahati nzuri, tulipomaliza kozi, familia ya Jimmy walikuja kumchukua wakaenda kupanda Mlima Kilimanjao. Papa's Shadow inaonyesha safari yao ya kupanda mlima. Ni rekodi nzuri sana. Ninaamini itawavutia watalii.

Kuna mambo mengine niliyomwambia huyu mwandishi wa Manitou Messenger. Hasa, nilisisitiza azma yangu ya kuendelea kufanya kila juhudi kuuelimisha ulimwengu juu ya namna Hemingway alivyoipenda Afrika na namna maisha yake na fikra zake zlivyofungamana na Afrika. Nilimwambia pia kuwa Jimmy ni mfano murua wa kuigwa na wahitimu wengine wa vyuo. Alifuata na anaendelea kufuata anachokipenda moyoni mwake, yaani kutengeneza filamu za kuelimisha. Yeye na vijana wenzake katika Ramble Pictures wanajituma kwa roho moja katika shughuli zao na hawatetereshwi na magumu au vipingamizi vyovyote.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...