Tuesday, December 4, 2018

Nashukuru Niliandika Kitabu Hiki

Nashukuru niliandika kitabu kiitwacho Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Nasema hivi kutokana na jinsi kinavyothaminiwa na watu wanaokitumia. Taarifa hizi ninazipata kutoka kwao.

Wiki hii kwa mfano, nimepata mawasiliano kutoka kwa waalimu wawili. Profesa Artika Tyner, kiongozi mojawapo wa Chuo Kikuu cha St. Thomas ameniandikia kuwa anahitaji nakala za kitabu hii, nami nimempelekea. Niliwahi kumwongelea katika blogu hii, baada ya kukutana naye kwa mara ya kwanza. Tangu tukutane, amekuwa mpiga debe wangu wa dhati. Namshukuru.

Nimepata pia ujumbe kutoka kwa Profesa Barbara Zust wa Chuo cha Gustavus Adolphus kunialika kwenda kuongea na wanafunzi anaowapeleka Tanzania katika programu ambayo imedumu miaka mingi. Kama ilivyo kawaida yake, ananiomba nikaongee na wanafunzi kuhusu masuala yaliyomo katika Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Kama kawaida, watakuwa wameskisoma na wanasubiri fursa ya kuniuliza masuali. Miaka yote nimefurahi kukutana na wanafunzi hao.

Ninafarijika na kushukuru kwamba nilijiingiza katika shughuli hii ya kuwasaidia watu kutafakari na kuelewa tofauti za tamaduni na athari za tofauti hizo, ili kujizatiti kabla na wakati wa kukutana na watu w utamaduni wa kigeni. Nashukuru niliandika kitabu hiki, ambacho  kimenirahishia kazi hiyo, na papo hapo ni chachu ya tafakari na mazungumzo ya kuelimisha. Nashukuru kuona kuwa wadau kama hao niliowataja, wenye wadhifa mkubwa katika jamii, wanaona umuhimu wa mchango wangu, nami sitawaangusha.

Saturday, November 24, 2018

Kumbukumbu ya Matengo Folktales Kutajwa Katika "Jeopardy."

Kipindi kama hiki, mwaka jana, kitabu cha Matengo Folktales kilitajwa katika kipindi maarufu cha televisheni kiitwacho Jeopardy." Ilikuwa tarehe 23 Novemba, nami niliandika taarifa katika blogu hii.

Tukio hili la kushtukiza lilinifungua macho nikatambua kuwa "Jeopardy" ni maarufu sana hapa Marekani. Bado sijui taarifa za kitabu changu zilifikaje kule, ila ninafurahia kuwaambia waMarekani taarifa hizo kila ninaposhiriki matamasha ya vitabu.

Thursday, November 22, 2018

Vitabu Kama Zawadi ya Sikukuu

Kwa watu wengi, huu ni wakati wa maandalizi ya sikukuu ya Krismasi. Pamoja na mengine, ni kununua zawadi kwa ajili ya ndugu, marafiki na kadhalika. Hapa Marekani, vitabu ni zawadi mojawapo inayothaminiwa.

Hapa kushoto ni picha niliyopiga tarehe 16 Novemba katika duka la vitabu la Barnes and Nobel mjini Burnsville. Inaonyesha kabati la vitabu vilivyopendekezwa na wahudumu wa duka. Nilipiga picha hiyo kwa sababu kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, kipo hapo. Kimekuwepo kwa wiki nyingi. Bila shaka kuna wateja wanaoingi na kuchungulia kwenye kabati hilo ili kupata wazo juu ya kitabu cha kununua, kwani tayari kimependekezwa na watu wazoefu wa vitabu.

Utamaduni wa kuvihesabu vitabu kama zawadi muafaka kwa sikukuu au mazingira yeyote mengine unanivutia, kama nilivyowahi kueleza katika blogu hii. Ninatamani utamaduni huu uote mizizi katika nchi yangu. Nawazia furaha watakayokuwa nayo watoto kwa kupewa vitabu kama zawadi, kwa sababu ninajua kuwa watoto wanapenda vitabu, kama nilivyowahi kuandika katika blogu hii.  Nawazia namna ambavyo mitazamo na fikra za watu zingeboreka kwa kuwa na utamaduni wa kuthamini na kusoma vitabu vya aina mbali mbali.

Saturday, November 10, 2018

Nimeongea na Lumen Christi Book Club

Miezi kadhaa iliyopita, nilipata mwaliko wa kwenda Lumen Christi Catholic Community kuongelea kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Aliyenialika ni Jackie ambaye alikuwa amekisoma kitabu hicho. Alisema kwamba jumuia ya waumini hao wana klabu yao ya usomaji vitabu, na kwa sasa wamejikita katika vitabu vinavyohusu Afrika.

Nilipoingia ukumbini, niliona meza imepangwa vizuri karibu na mlandoni, yenye vitabu vyangu na vya waandishi wawili ambao tunafahamiana: Maria Nhambu ambaye alizaliwa Tanzania, na Afeworki Ghorghis, jaji mstaafu wa mahakama kuu ya Eritrea.

Baada ya Jackie kunitambulisha, nilielezea kifupi nilivyokulia Tanzania, katika utamaduni wa wa-Matengo, na hatimaye nilivyokutana na utamaduni wa Marekani, nilipokuwa masomoni katika Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison, na kufikia kuwa mshauri kwa vyuo vinavyopeleka wanafunzi Afrika, kama nilivyoandika katika utangulizi wa kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Katika kuelezea uandishi wangu juu ya masuala ya utamaduni, nilianza na kitabu cha Matengo Folktales.

Baada ya hapo, Jackie alitaja vipengele vilivyomo kitabuni ili nielezee, na wengine waliniuliza masuali yao. Kati ya masuala tuliyoongelea ni "gifts" (sio kwa maana ya zawadi), uzee, na "African time." Nilielezea nilivyoandika kitabuni kuhusu masuala hayo. Klabu hii ya vitabu ni ya aina yake, kwa maana kwamba watu wanahudhuria hata bila kusoma kitabu kinachojadiliwa.

Mkutano ulikuwa mzuri na wenye manufaa. Binafsi, nilitoa shukrani kwa fursa ya kufahamiana na watu wapya, kwani inatajirisha maisha yangu. Nilifurahi kuweza kuwaelezea shughuli zangu kama mtoa ushauri chini ya mwavuli wa Africonexion.  Baada ya mimi kurejea nyumbani, Jackie aliniletea ujumbe kwamba atanitambulisha kwa mkurugenzi wa East Side Freedom Liabrary ambaye wakati huu anaandaa programu kuhusu Afrika. Sikuwa ninajua kuhusu maktaba hiyo. Ninasubiri.

Thursday, October 25, 2018

Nimepeleka Vitabu kwa wa-Matengo

Mwezi Julai mwaka huu nilikwenda Tanzania, nikiwa nimechukua vitabu vingi. Baadhi ni vile nilivyoandika mwenyewe, ambavyo niliviwasilisha katika maduka ya Kimahama, na A Novel Idea. Nilichukua pia nakala 16 za Matengo Folktales kwa ajili ya kuzipeleka kwa wa-Matengo, wilayani Mbinga, katika mkoa wa Ruvuma.

Ninasema hivyo, na kutaja kabila langu, nikijua kwamba kwetu wa-Tanzania, hii ni kauli tata, isiyopendeza, kwani inaashiria upendeleo au ubaguzi kwa msingi wa kabila. Utamaduni wa Tanzania, uliojengwa na chama cha TANU, hauafiki ubaguzi wa makabila au wa aina nyingine. Sasa kwa nini nimetoa kauli hiyo? Kwa nini niliamua kupeleka nakala hizi za Matengo Folktales kwa wa-Matengo? Napenda kuthibitisha kwamba nilifanya jambo muafaka.

Matengo Folktales ni mkusanyo wa hadithi za jadi ambazo nilizirekodi nyumbani u-Matengo miaka ya sabini na kitu. Nilizirekodi katika kaseti, kisha nikachagua hadithi kumi na kuzitafsiri kwa ki-Ingereza. Niliandika uchambuzi wa kila hadithi na nikaongezea insha ya kitaaluma kuhusu hadithi. Huu ukawa ni mswada ambao ulichapishwa kama Matengo Folktales.

Mimi ni mwanataaluma katika taaluma hii inayojulikana kama "Folklore." Kama ilivyo katika taaluma zingine, tuna taratibu na maadili ya utafiti, uandishi na uchapisahji. Kati ya hayo ni utaratibu wa kuwarudushia fadhila watu wanaowezesha utafiti wetu. Watafiti tusiwe tunachukua yale tunayopewa bila kuwarejeshea kwa namna moja au nyingine wale wanaotupa hayo tunayotafuta. Dhana hiyo huitwa "reciprocity" kwa ki-Ingereza.

Kuna nämna mbali mbali za kurudisha fadhila, kufuatana na mila na desturi za mahali husika na kufuatana na ridhaa ya mtu binafsi anayetuwezesha. Kuna namna mbali mbali za kutoa shukrani. Kwa upande wangu, na kwa watafiti wengi, namna bora kabisa ya kurudisha fadhila ni kuwapa nakala ya yale ninayorekodi na kuondoka nayo, kama vile kaseti au picha ninazopiga.

Kwa msingi huo, baada ya kuchapisha Matengo Folktales, nilijua kwamba nina wajibu wa kupeleka nakala kwa wa-Matengo. Kwa kuwa nimechapisha kitabu kwa ki-Ingereza, ilibidi nisubiri hadi ipatikane sehemu muafaka ya kupeleka.

Fursa imepatikana kwa kuwepo kwa shule za sekondari. Hizi nakala 16 nilimkabidhi mwalimu Frank Kinunda mjini Mbinga, baada ya mawasiliano naye, naye amezisambaza kwenye hizo shule. Zitawaelimisha vijana na walimu kuhusu utamaduni wa wahenga, na pia kuhusu taaluma ya "Folklore." Vile vile, kwa kuwa  nimeandika kwa uangalifu mkubwa kama mwalimu wa lugha ya ki-Ingereza, Matengo Folktales ni kitabu cha kujiongezea ujuzi wa ki-Ingereza. Kitabu hiki kinatumika kufundishia katika vyuo hapa Marekani, na ninafurahi kimeanza kuwa mikononi mwa wanafunzi na walimu Tanzania

Sunday, October 21, 2018

Minnesota Black Authors Expo Imekaribia

Bado siku sita tu hadi maonesho yaitwayo Minnesota Black Authors Expo yatakapofanyika. Hii ni mara ya pili kwa maonesho haya kufanyika. Mara ya kwanza ilikuwa mwaka jana.

Waandaaji waliniomba niwemo katika jopo la waandishi watakaoongelea masuala mbali mbali ya uandishi wa vitabu. Nilikubali. Jopo linategemewa kuwa kivutio kikubwa katika tamasha hilo.

Friday, October 19, 2018

Waandishi Marafiki Tumekutana

Tarehe 13 mwezi huu, nilishiriki tamasha la vitabu liitwalo Deep Valley Book Festival mjini Mankato, jimbo hili la Minnesota. Nilishahudhuria mara tatu tamasha hili linalofanyika mara moja kwa mwaka. Nilijua kuwa mmoja wa waandishi ambao walikuwa mbioni kushiriki ni rafiki yangu Becky Fjelland Brooks anayeonekana pichani kushoto.

Becky ni mwalimu katika South Central College hapa Minnesota. Tulianza kufahamiana wakati yeye na Profesa Scott Fee wa Minnesota State University Mankato waliponialika kwenda kuongea na wanafunzi waliokuwa wanawaandaa kwa safari ya masomo Afrika Kusini.

Watu wengi walihudhuria mhadhara wangu kuhusu tofauti za tamaduni, na nakala nyingi za kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences zilinunuliwa. Baada ya hapo, nimepata mialiko ya kwenda kuongea na wanafunzi hao kila mara wanapoandaliwa safari ya Afrika Kusini.

Mwalimu Becky ni mmoja wa wale wa-Marekani ambao wanaipenda Afrika na wanajibidisha kuwaelimisha wenzao kuhusu Afrika. Kuandaa programu za kupeleka watu Afrika ni kazi ngumu, yenye changamoto nyingi. Inahitaji ujasiri na uvumilivu. Nina uzoefu wa shughuli hizo, na ninawaenzi watu wa aina ya mwalimu Becky.

Mwalimu Becky ni mwandishi mwenye kipaji. Tayari ameshachapisha vitabu kadhaa, kwa ajili ya watoto, vijana, na watu wazima. Umaarufu wake unaongezeka mwaka hadi mwaka, na ameshatambuliwa na tuzo kama Midwest Book Awards. Ni faraja kwangu kwamba mwalimu Becky, mwandishi maarufu, anakipenda sana kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, na anaipenda mihadhara yangu, kama inavyonekana hapa na hapa.

Hii tarehe 13, kwa kuwa mwalimu Becky na mimi tulifahamu kuwa tungekutana, nilichukua nakala yangu ya kitabu chake kiitwacho Slider's Son ili anisainie. Ninavyo vitabu vyake vingine ambavyo alivisaini siku zilizopita. Tulifurahi kukutana. Ninajiona nimebarikiwa kuwa na rafiki kama huyu. Picha hiyo hapa juu aliiweka Facebook akiwa ameambatisha ujumbe huu: "With my dear friend Joseph Mbele, author of the enlightening and humorous book, "Africans and Americans," sharing stories and friendship at the Deep Valley Book Festival today...."

Thursday, October 18, 2018

Kitabu Bado Kiko Dukani Barnes and Noble

Juzi nilienda Apple Valley na Burnsville kuangalia maduka ya vitabu, kama nilivyoandika katika blogu hii. Kule Burnsvile, mji jirani na Apple Valley, nilitaka kuingia katika duka la Barnes and Noble ambamo kitabu changu kilikuwa kimewekwa sehemu maalum ya vitabu vilivyopendekezwa na wahudumu wa duka, kama nilivyoripoti katika blogu hii.

Sikujua kama ningekikuta, kwani sijui utaratibu wanaofuata katika kuvionesha vitabu hivyo sehemu hiyo. Nilidhani labda vinawekwa kwenye kabati hili kwa wiki moja hivi. Nilishangaa kukiona kitabu changu bado kipo, na kimewekwa juu zaidi ya pale kilipokuwepo kabla. Hapa kushoto ni picha niliyopiga wiki iliyopita, na kulia ni picha niliyopiga juzi. Ninafarijika na kufurahi kukiona hapa. Ninasubiri siku ya kwenda kukiongelea, kama nilivyodokeza.

Tuesday, October 16, 2018

Vitabu Nilivyonunua Leo

Leo niliamua kutembelea maduka ya vitabu kwenye miji ya Apple Valley na Burrnsville hapa Minnesota. Apple Valley, kwenye duka la Half Price Books,  nilinunua vitabu vitatu bila kutegemea. Nilipita sehemu ya vitabu vya Hemingway, ambapo sikuona kitabu kigeni kwangu. Nilienda sehemu ya bei nafuu, nikanunua vitabu vitatu.

Kimoja ni Essays and Poems cha Ralph Waldo Emerson, kilichohaririwa na Tony Tanner. Kwa miaka mingi nimefahamu jina la Emerson. Nilifahamu kuhusu insha yake "Self Reliance," ingawa sikuwa nimewahi kuisoma. Nilifahamu pia kuwa ameathiri sana falsafa na uandishi, sio tu Marekani, bali kwingineko. Kwa hali hiyo, sikusita kununua kitabu hiki, hasa baada ya kuona kuwa kina mashairi ya Emerson. Sikujua kuwa alitunga mashairi.

Kitabu kingine nilichonunua ni Collected Poems cha Edna St. Vincent Millay. Huyu ni mwandishi ambaye sidhani kama niliwahi kusikia hata jina lake. Lakini nilipoona hiki kitabu kikubwa sana chenye kurasa 757 na nyongeza ya kurasa 32, na halafu nikasoma taarifa za huyu mwandishi, kwamba alikuwa mwanamke mwenye kujiamini na uthubutu katika utunzi wa ma shairi, na mwanaharakati ambaye katika mazingira ya miaka ya 1920 kuelekea 1930 alikuwa akitetea uhuru wa mtu binafsi na hasa wanawake, na halafu nikaona alipata tuzo maarufu ya uandishi iitwayo Pulitzer Prize mwaka 1923, niliona lazima ninunue kitabu hiki, ili nifaidi utunzi wa mama huyu.

Si kawaida kukutana na tungo za wanawake wa zamani namna hiyo hapa Marekani. Tungo ya mwanzo kabisa ambayo nimewahi kusoma na kuifundisha ni The Awakening, ya Kate Chopin. Hiyo ni riwaya ya mwanzo mwanzo inayotambulika kama ya kifeministi. Kutokana na kufahamu kiasi fulani harakati za wakati ule, nilivutiwa na kitabu hiki cha mashairi ya Edna St. Vincent Millay, ambaye alikuja baada ya Kate Chopin.

Kitabu cha tatu nilichonunua ni The Mother, cha Maxim Gorky, kilichotafsiriwa na Hugh Aplin. Maxim Gorky ni mwandishi wa zamani wa Urusi. Nilipoona kitabu hiki, nilikumbuka enzi zangu kama mwanafunzi katika idara ya "Literature" ya chuo kikuu cha Dar es Salaam, ambapo mwalimu wetu Mofolo Bulane alitufundisha nadharia ya fasihi kwa mtazamo wa ki-Marxisti.

Katika mafundisho yale alituwezesha kufahamu kuhusu waandishi wengi, wakiwemo wa Urusi, kama vile Leo Tolstoy, Fyodor Dostoyevsky, Maxim Gorky, Vladimir Mayakovsky, Anna Akhmatova, na Mikhail Sholokhov. Tulijifunza kuwa Gorky ni moja wa waandishi waanzilishi wa mkondo wa "Socialist Realism," ambao ulifuatwa baadaye na akina Mayakovsky na Ana Akhmatova na wengine. Kutokana na kumbukumbu hizi za ujana wangu, niliamua kununua kitabu hiki ili niweze kukisoma nitakapopata wasaa. Baada ya kununua vitabu hivyo, nilielekea kwenye mji jirani wa Burnsville, kwenye duka la vitabu la Barnes Noble. Nitaandika juu ya safari hiyo wakati mwingine.

Saturday, October 13, 2018

Nimeshiriki Tamasha la Vitabu la Deep Valley

Leo nilienda Mankato, Minnesota, kushiriki tamasha la vitabu liitwalo Deep Valley Book Festival. Hii ilikuwa mara yangu ya nne kushiriki tamasha hilo. Ilikuwa fursa ya kuongea na watu kwa undani kuhusu mambo mbali mbali.

Kuna watu kadhaa ambao nawakumbuka zaidi. Mmoja aliniambia kuwa ana binti yake ambaye anafundisha ki-Ingereza kama lugha ya kigeni. Hapa Marekani somo hilo linajulikana kama English as a Foreign Language. Hufundishwa kwa wahamiaji ambao wanahijtaji kujia lugha hiyo, ambayo ndio lugha rasmi ya hapa Marekani. Nilichangia mada hiyo kwa kuelezea jinsi sgughuli ya kufundisha ESL inavyofungamana na suala la tamaduni. Hufundishi tu muuno, sarufi, istilahi, bali pia utamaduni wa mazungumzo.

Mama mmoja mzee, mwandishi, ambaye meza yake ilikuwa mbele yangu, alifika kunisalimia na kuongea. Nilimwuliza ameandika kuhusu nini, akaniambia kitabu chake kinahusu changamoto aliyopitita kufuatia binti yake kujitokeza kama mwenye silika ya mapenzi ya jinsia yake. Nilivyomwelewa huyu mama, ilikuwa ni changamoto kubwa kwake, na ndiyo aliyoandika kitabuni. Nilimwambia kuwa nami nilianza kuelewa suala hili la mapenzi ya jinsia moja nilipokuwa masomoni katika chuo kikuu cha Wisconsin-Madison, ambapo palikuwa na wana harakati wa aina mbali mbali. Nina nia ya dhati ya kukipata ta kiabu chake.

Kijana mmoja alikuja mezani pangu akaniambia kuwa anafuatilia habari za mwandishi Sinclair Lewis. Anamwigiza, yaani kujifanya yeye ndiye mwandishi huyo. Akaniuliza iwapo ataweza kupata wapi habari zaidi. Nikamwambia kuwa kwa bahati nzuri, Marekani ni Makini kwa kutunza taarifa za watu mashuhuri kama hao waandishi. Nilimwabia kuhus nyumba ya makumbusho ya Carl Sandburg, ambayo niliwahi kuitembelea, mjini, Galesburg, Illinois, na nyumba za makumbusho ya Ernest Hemingway ambayo niliwahi kutembelea mjini Oak Park, Illinois, na sehemu zingine, kama vile maktaba ya JF Kennedy ambayo niliwahi kuitembelea Boston.

Watu wamenieleza uzoefu wao wa kuishi na waAfrika hapa Marekani na kujione tofauti za tamaduni, kwa maana ya mienendo, namna ya kufikiri na kutenda. Mzee moja aliniambia kuwa ana jirani mSomali. Alinunua kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, nami nikamhimiza asikose kumwazimisha huyu mSomali asome.

Nami nimepata fursa ya kuwaeleza wat hao kuhu mialiko ninayopata kwenda sehemu mbali mbali kuelezea athari za tofauuti za tamaduni. Wakati wa kuongelea kitabu changu, nimeelezea mtindo wa uandishi niliotumia. Nimepata fursa ya kuongelea kitabu cha Matengo Folktales, pia, nilivyokiandaa kwa miaka mingi, tangu kurekodi hadithi hadi kuzitafsiri na kuzichambua, na hatimaye kuchapishwa. Sikukosa kuelezea kilivyotajwa mwezi November tarehe 23 katika kipindi cha TV ch Jeopardy. Nilikuwa nimechukua karatasi yenye tamko la Jeopardy a, ambao  hawakuweza kujibu/.

Mbali ya vitabu vyangu, nilichukua vitabu vya Bukola Oriola na kitabu cha mwanae Samuel Jacobs, mwenye umri wa miaka kumi na moja. Bukola Oriola niliwahi kumzungumzia katika blogu hii. Tangu nilipomwelekeza namna ya kuchapisha kitabu chake cha kwanza, amefika mbali. kwani aliteuliwa na Rais Obama kuwa katika United States Advisory Council on Human Trafficking.

Nimekutana na rafiki yangu Becky Fjelland Brooks, mwalimu wa South Central College, ambaye ni mpenzi mkubwa wa kitabu changu cha Africans and Americans, amewahi kunikalika mara kadhaa nikaongee na wanachuo wake. Akaandika taarifakadhaa, kama hii hapa na hii hapa.


Thursday, October 11, 2018

Mchakato wa Kwenda Kuongelea Kitabu

Leo nimepata ujumbe kutoka kwa Dan, ambaye hivi majuzi alikipigia debe kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, katika duka la Barnes and Noble, kama nilivyoelezea katika blogu hii. Anaendelea na juhudi yake. Ameandika:

Happy to spread the word about your book. Let me know if you are ever interested in doing a talk at our store. I can connect you with our manager.

Tafsiri yangu:

Ninafurahi kukitangaza kitabu chako. Nijulishe iwapo utapenda kuja kukiongelea katika duka letu. Nitaweza kukuunganisha na meneja wetu.

Kuwaalika waandishi kuongelea vitabu vyao ni utamaduni wa kawaida hapa Marekani. Ni fursa ya mwandishi kukutana na watu wanaotaka kujua mambo kama  historia ya mwandishi, changamoto za uandishi, falsafa na mawaidha yake kuhusu uandishi, na kadhalika. Vinakuwepo vitabu vya mwandishi, kwa watu kuvinunua na yeye kuvisaini. Wa-Marekani wanapenda kusainiwa vitabu, kama nilivyowahi kusema katika blogu hii.

Wednesday, October 10, 2018

Naambiwa Niongeze Bei ya Kitabu

Katika matamasha ya vitabu ninayoshiriki, ninakutana na mambo mengi, zikiwemo tabia na mitazamo ya wateja. Moja ambalo linanigusa zaidi ni pale mteja anaposhauri niongeze bei ya kitabu changu. Hiyo imetokea mara kadhaa, kuhusiana na vitabu vyangu viwili: Africans and Americans: Embracing Cultual Differences na Matengo Folktales.

Vitabu hivi ninaviuza kwenye matamasha kwa dola 14 kila kimoja. Kwa kujua kwamba watu wengine wanatoa  noti ya dola 20 au noti mbili za dola kumi kumi, ninajitahidi kuwa na chenji. Ajabu ni kwamba watu wengine hawasubiri chenji, na wengine wanakataa. Wanachotaka ni kitabu waende zao. Ninakumbuka watu waliowahi kutoa noti ya dola 20 bila kutaka chenji. Mmoja wa hao, nilipojiandaa kumpa chenji, alisema hiyo chenji ni shukrani yake kwangu kwa kuandika kitabu.

Tarehe 4 mwezi huu nilikutana na jambo jingine kabisa. Mama moja, Jackie, ambaye nimemfahamu miezi michache iliyopita na akasoma hivi vitabu vyangu viwili, alinialika kwenye mhadhara wa rafiki yake Maria kuhusu vitabu na maisha yake. Alikuwa ameniambi nije na nakala za vitabu vyangu, ili aweze kuvipeleka katika tamasha la vitabu. Baada ya mhadhara, wakati tulipokuwa tunajumuika kwa viburudisho na maongezi, Jackie akanulizia bei ya vitabu vyangu, nami nikamwambia kuwa ni dola 14. Alisema nipandishe iwe 15, kwa ulinganisho na kitabu cha dola 10 na pia kwa urahisi wa chenji.

Alinitambulisha kwa rafiki yake, akamwambia kuhusu hivi vitabu vyangu. Alivyokuwa akielezea hayo, akaniambia nivitoe kwenye begi, nikampa. Huyu rafiki alichagua Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, akapanda ngazi kwenda kuchukua hela akaja akanipa na kitabu akachukua. Dakika chache baadaye, mama huyu alinitambulisha kwa mama mwingine, na akamwambia kuhusu vitabu. Naye akanunua Matengo Folktales.

Kwa hivyo nimejikuta nikiafiki wazo la kuongeza bei ya vitabu vyangu. Hata hivyo, bei hiyo ni ndogo kulingana na bei za mahali pengine za vitabu hivyo. Ninaamini kuwa taarifa hii ina ujumbe kuhusu watu wanaothamini vitabu kuliko fedha. Kama nilivyowahi kusema tena na tena, blogu hii ni sehemu ambapo ninajiwekea mambo yangu binafsi, kama vile kumbukumbu, hisia, na mitazamo. Ikitokea haja, siku zijazo, ya kuandika kitabu kuhusu maisha na kazi zangu, blogu hii itakuwa chanzo muhimu cha taarifa.

Thursday, September 27, 2018

Nimenunua Tena Tungo Zote za Shakespeare

Tarehe 24 Septemba, nimenunua tena kitabu cha tungo zote za William Shakespeare.  Nilikinunua katika duka la Half Price Books mjini Apple Valley nilipotoka Burnsville kuangalia kitabu changu kama nilivyoelezea katika blogu hii.

Ingawa tayari nina vitabu vinne vyenye tungo zote za Shakespeare, sikuona tatizo kununua hiki pia. Kuwa na nakala mbali mbali za kitabu cha tungo za Shakespeare kuna mantiki nzuri kwa sababu tungo hizo zimehaririwa kwa namna mbali mbali. Hii imekuwa ni sehemu ya historia ya uchapishaji wa tungo za Shakespeare.

Mara kwa mara neno linaloonekana kwenye nakala fulani si lile linaloonekana kwenye nakala nyingine au limeandikwa kwa namna tofauti na lilivyo katika nakala nyingine. Hali hiyo ni ile inayoonekana katika miswada ya tungo za zamani, sehemu mbali mbali ulimwenguni, ikiwemo za huku kwetu, kama zile za Liongo Fumo.

Tofauti hazikwepeki, kwa sababu uandishi katika enzi za Shakespeare ulikuwa tofauti na wa leo. Leo kitabu kikichapishwa, tunategemea ni nakala sahihi ya mswada ulivyoridhiwa na mwandishi. Wakati wa Shakespeare, hapakuwa na utaratibu huo. Watu walikuwa wananakili andiko walivyoweza, na tofauti mbali mbali zilijidhihirisha kutoka kwa mnukuzi hadi mwingine.

Kadhalika waigizaji wa tamthilia majukwaani walikuwa wanatamka, pengine bila kujitambua, maneno yaliyofanana sauti, ingawa maneno ya mwandishi yalikuwa tofauti. Hiyo nayo ni sababu ya waandishi kuandika maneno tofauti.

Kwa hali hiyo, ni busara kuwa na nakala tofauti za kitabu hiki cha tungo zote za Shakespeare. Hata mtu ukiwa na kitabu cha tamthilia mojawapo tu, ni busara kuwa na nakala zilizohaririwa na wahariri tofauti wa kitabu hicho.

Faida nyingine ni kwamba baadhi ya nakala hizi zina maelezo ya wahariri juu ya mambo mbali mbali, yakiwemo maana za maneno na semi. Maelezo haya ni msaada mkubwa kwetu, kwani ki-Ingereza cha wakati wa Shakespeare kina tofauti nyingi na kiIngereza cha leo.

Monday, September 24, 2018

Nimekikuta Kitabu Changu Barnes and Noble

Baada ya kusikia kwamba kitabu changu kimewekwa sehemu maalum katika duka la Barnes and Noble, kama nilivyoandika katika blogu hii, leo nimeenda Burnsville kuangalia. Hapa kushoto linaonekana duka hilo, ambalo nimelitembelea mara kadhaa.





Hapa kushoto ndio mwonekano wa kabati ambapo huwekwa vitabu vilivyopendekezwa na wahudumu wa duka. Kitabu changu kinaonekana hapo chini. Duka lolote la Barnes and Noble huwa na vitabu vingi sana. Ni kama maktaba. Kwa hiyo, kitabu kuuzwa humo si jambo la ajabu. Hakunaajabu yoyote kwa kitabu changu kuuzwa Barnes and Noble. Kama nilivyoandika juzi, kitab changu hich kimekuwepo kwenye mtandao wa Barnes and Noble kwa muda mrefu.





Kitu cha pekee ni uamuzi wa mhudumu wa duka kukipendekeza kwa wateja, kama inavyooneka hapa chini ya kitabu:

Short and sweet. A wonderful read about the differences between Africans and Americans. I feel wiser to the world after reading it.
Tafsiri yangu:
Kifupi na kitamu. Andiko la kupendeza ajabu kuhusu tofauti za tamaduni baina ya waAfrika na waMarekani. Najiona nimejiongezea werevu mbele ya dunia baada ya kukisoma.

Ninafurahi kwa sababu huyu mhudumu, mwenye uzoefu katika maktaba amesema hivyo. hudumu wa maktaba hapa Marekani ni msomaji wa vitabu. Anapopendekeza kitabu hawezi kupendekeza kiholela. Aanajua kuwa wadau wanaofika humo ni wa kila aina. Wengine ni wasomi waliobobea. Anaweka heshima yake rehani, kwani wadau wakinunua wakaona si kitabu bora, ataaibika yeye kabla ya mwandishi. Hiyo ni sababu ya wazi ya mimi kufurahi.

Friday, September 21, 2018

Kitabu Kimeingia Barnes and Noble

Kwa wasomaji wa vitabu hapa Marekani, jina la Barnes and Noble si geni, kwani ni jina la kampuni inayomiliki maduka mengi ya vitabu yaliyoko nchi nzima. Maduka ya Barnes and Noble ni maarufu kiasi kwamba watu wanapoongelea maduka ya vitabu, huwazia kwanza Amazon na Barnes and Noble.

Leo nimepata ujumbe kutoka kwa mhudumu wa duka la Barnes and Noble Burnsville, mwendo wa nusu saa kutoka hapa ninapoishi. Ameandika:

Hi Joseph. Just letting you know I put your book on the staff recommendation display at the Barnes and Noble Burnsville where I work. The book about cultural differences between Africans and Americans. I really enjoyed it!

Tafsiri yangu:

Jambo Joseph. Nakufahamisha tu kwamba nimeweka kitabu chako sehemu vinapoonyeshwa vitabu vilivyopendekezwa na wahudumu wa duka la Barnes and Noble Burnsville ambapo ninafanya kazi. Kile kitabu juu ya tofauti za tamaduni baina ya wa-Afrika na wa-Marekani. Nilikifurahia sana!


Bwana huyu aliyeniandikia ujumbe alikuwa mhudumu wa duka la vitabu la hapa Chuo cha St. Olaf,  na ndipo alipokisoma kitabu changu. Yeye na wahudumu wenzake tulikuwa tukipenda kuongea. Kwa kuwa walikuwa wamesoma kitabu changu, walipokuwa wanaenda kujisaidia walipenda kusema, "kuchimba dawa," usemi waliouona kitabuni. Tulikuwa tukicheka. Nilikuwa nikivunjika mbavu na kujisikia raha kuwasikia hao wazungu wakiwa wa-Swahili namna hiyo. Niliona kitabu changu kimewagusa.

Nimefurahi kusikia kuwa kitabu changu kimeingia Barnes and Noble namna hiyo. Nasema ”namna hiyo” kwa maana ya kitabu kuwemo dukani, kwani, kwa miaka, kimekuwepo kwenye mtandao wa Barnes and Noble. Sitaki kusema mengi, nisije nikawa nahesabu vifaranga kabla havijaanguliwa, kama isemavyo methali ya ki-Ingereza. Nitasubiri nione.

Monday, September 10, 2018

Mdau Wangu Mpya

Juzi, tarehe 8, nilikwenda Coon Rapids, Minnesota, kuhudhuria uzinduzi wa jarida liitwalo L Magazine. Jarida hilo linalohusu zaidi masuala ya uandishi, uchapishaji, na uuzaji wa vitabu, limeanzishwa na Bi Bukola Oriola mwenye asili ya Nigeria anayeishi hapa Minnesota.

Kati ya watu waliohudhuria ni Dr. Artika Tyner, rafiki wa karibu wa Bi Oriola. Dr. Tyner ni "Vice President for Diversity and Inclusion" wa Chuo Kikuu cha St. Thomas. Anaonekana pichani akiwa ameshika tuzo alizopewa hiyo juzi kwa mchango wake kwa jamii.

Alipotambulishwa kwangu kwenye meza nilipoweka vitabu vyangu, tuliongea kiasi kuhusu shughuli zake na zangu. Alinunua vitabu vyangu, zikiwemo nakala 9 za Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Vile vile alielezea hamu yake ya kuendelea kuwasiliana nami ili tutafakari namna ya kushirikiana katika programu zinazohusu Afrika na watu wenye asili ya Afrika yaani wanadiaspora.

Nilitambua kuwa Dr. Tyner ni mmoja wa waMarekani Weusi ambao wana mapenzi ya dhati na Afrika. Hata mavazi yake yanaashiria hivyo. Ametembelea Afrika na anahamasisha programu za kupeleka watu Afrika. Dr. Tyner ni mtu maarufu, na kwa upande wangu kigezo kimoja ni kwamba ameshatoa mhadhara wa TED kuhusu elimu na mabadiliko ya jamii.


Ninafurahi kumpata mdau huyu mpya. Ninategemea kuendelea kubadilishana naye mawazo na uzoefu na kufanya shughuli mbali mbali za kuelimisha.

Thursday, August 30, 2018

Vitabu Nilivyonunua Nairobi

Nilisafiri tarehe 15 Julai kwenda Tanzania. Nilishukia Nairobi, kwa shughuli binafsi, ikiwemo kununua vitabu vya ki-Swahili. Kitabu nilichotamani zaidi ni Sauti ya Dhiki cha Abdilatif Abdalla ambacho nilitaka kukisoma kwa makini kuliko nilivyowahi kufanya kabla. Ninawazia pia kutafsiri kwa ki-Ingereza baadhi ya mashairi.

Nilivyoingia tu katika duka la vitabu la Textbbook Center, Kijabe Street, nilikitafuta kitabu cha Sauti ya Dhiki. Nilikiona, kikiwa na jalada tofauti na lile la mwaka 1973. Nilinunua pia Kichwamaji, Kaptula la Marx, Mzingile, na Dhifa, vya Euphrace Kezilahabi; Mashetani, tamthilia ya Ebrahim Hussein, na Haini, cha Adam Shafi.

Tangu zamani, nimekuwa na baadhi ya vitabu vya Kezilahabi, Ebrahim Hussein, na Adam Shafi. Ninafurahi kujipatia vile ambavyo sikuwa navyo. Hata hivi, nimegundua kuwa sasa nina nakala mbili za Mashetani na mbili za Kichwamaji.

Sunday, June 24, 2018

Maongezi ya Kina Leo na Msomaji Wangu

Leo nimekuwa na maongezi ya kina na msomaji wangu, mchungaji ambaye nilishamtaja katika blogu hii. Tulikutana mjini Hastings, Minnesota, tukaongeaa kwa saa mbili na robo. Tulikuwa tumeahidiana kwamba nikasaini nakala ya kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ambacho mchungaji alikuwa anampelekea mtu fulani wa karibu.

Tuliongea sana kuhusu shughuli zetu za kuelimisha na kuhamasisha jamii ya watu weusi juu ya masuala ya kujitambua. Mchungaji ameendelea kunifahamisha kuwa kitabu changu kinamsaidia kujitambua kama mtu mwenye asili ya Afrika, ingawa ana pia asili ya ki-Cherokee na ki-Faransa. Anataka kitabu hiki kitumike kuwaelimisha vijana wa-Marekani Weusi, waweze kujitambua na kujivunia walivyo na silika za u-Afrika, ili wasiwe wanabezwa na wazungu.

Nami naelewa vizuri tatizo lilivyo kwa hao vijana. Wanashinikizwa kubadili mwenendo, lugha, na mambo yao mengine, ili wafuate ya wazungu. Mashuleni wanashinikizwa, kudhibitiwa, na kuadhibiwa kwa mienendo yao ambayo mamlaka zinaitafsiri kama utovu wa nidhamu.

Jukumu lililopo, ili pawe na suluhu, ni kwa walimu na viongozi wa shule kufanya juhudi ya kujielimisha kuhusu utamaduni wa wa-Marekani Weusi ambao misingi yake kwa kiasi fulani, au kwa kiasi kikubwa, ni u-Afrika. Wa-Afrika walivyoletwa utumwani huku Marekani, walikuja na tamaduni zao, ambazo zimerithishwa tangu kizazi hadi kizazi, ingawaje zimekuwa zikiathirika na mabadiliko na mazingira kutoka kizazi hadi kizazi.

Hata hivyo, baadhi ya misingi na vipengele vya u-Afrika vimeendelea kuwepo. Kwa mfano, wa-Afrika tuna namna yetu ya kuongea, kama nilivyoelezea katika kitabu changu, hasa kurasa 32-39 na 44-45. Na nimeelezea kitabuni kwamba ninapokutana na wa-Marekani Weusi, ninatambua vipengele hivi vya u-Afrika katika tabia na mienendo yao.

Ninashukuru kufahamiana na mchungaji huyu ambaye ana tafakari za kina kuhusu masuala na ana ukarimu moyoni mwake wa kunielezea anavyojisikia na anavyowazia kuhusu ujumbe wowote uliomo katika kitabu changu. 

Friday, June 22, 2018

Nimehudhuria Mhadhara Kuhusu Frantz Fanon

Jioni hii nilikuwa St. Paul kuhudhuria mhadhara juu ya Frantz Fanon uliotolewa na Dr. Moustapha Diop. Mhadhara uliandaliwa na Nu Skool, jumuia ya wa-Marekani Weusi ambayo nimewahi kuiongelea katika blogu hii.

Niliona ni lazima nikahudhurie mhadhara huu, ambao mada yake ilikuwa "Becoming Fanon: A Portrait of the Decolonized" kwa kuzingatia umuhimu wa fikra za Fanon katika harakati za ukombozi sehemu mbali mbali za dunia, hasa ukombozi wa fikra.

Nilikutana  na fikra za Fanon kwa mara ya kwanza nilipokuwa mwanafunzi chuo kikuu cha Dar es Salaam, katika idara ya Literature, miaka ya 1973-76. Aliyetufundisha ni mwalimu Grant Kamenju, na vitabu vya Fanon alivyotumia ni The Wretched of the Earth na Black Skin White Masks. Katika kufundisha fasihi ya Afrika, ninaona umuhimu wa kurejea katika fikra za Fanon mara kwa mara. Sielewi utakosaje kurejea kwenye fikra za Fanon.

Katika mhadhara wake, Dr. Diop alielezea kifupi maisha ya Fanon, akajikita zaidi katika kufafanua jinsi baina ya mwaka 1956 hadi 1961 Fanon alivyobadilika na kuwa Fanon tunayemjua kama mwanamapinduzi. Fanon alikuja kuwa mwanaharakati hadi akafukuzwa nchini Algeria. Alikwenda Tunisia, ndipo alipoendesha harakati, ikiwemo kuwapiga msasa wapiganaji wazalendo wa Algeria kabla hawajaingia nchini mwao kupambana na jeshi la wakoloni.

Jambo jingine ambalo nimejifunza katika mhadhara huu ni kuwa The Wretched of the Earth hakukiandika, kutokana na hali ya afya yake, bali alimwelezea mke wake kwa mdomo, naye akaandika. Ilichukua miezi kadhaa. Dr. Diop alitoa muhtasari wa mambo muhimu aliyotufundisha Fanon na akawataja watu walioendeleza fikra  za Fanon Afrika na Marekani, wakiwemo Kwame Nkrumah na Steve Biko.

Tuesday, June 19, 2018

Vitabu Vinapobebana

Nadhani kila msomaji wa vitabu anatambua manufaa na raha ya kusoma vitabu vya aina mbali mbali. Hivi ninavyoandika, ninakaribia kumaliza kusoma Riding the Waves of Culture: Understanding Diversity in Global Business, kitabu ambacho nilikitaja siku kadhaa katika blogu hii.

Nimekifurahia sana kitabu hiki, kwa jinsi kinavyoongelea masuala ya tofauti za tamaduni, mada ambayo ninashughulika nayo sana. Kinanifanya nielewe undani wa yale niliyoandika katika Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Kwa mfano, sura ya kitabu hiki iitwayo "How We Manage Time," imenipa msamiati wa kuelezea yale niliyoelezea katika sura iitwayo "Time Flies But Not in Africa." Nimeelewa kwamba msimamo wetu wa-Afrika ni "synchronic" au "polychronic" na msimamo wa wa-Marekani ni "sequential." Tofauti zetu ambazo nimezielezea katika kitabu changu zimejengeka katika mitazamo hiyo miwili.

Nitoe mfano. Kama ninavyoeleza katika kitabu changu, sisi tunaonekana hatuna nidhamu ya kuchunga muda, katika mazingira yetu, wakati wa-Marekani wanachunga sana muda, katika mazingira yao. Hizi ni tofauti tu, wala si ishara kwamba utamaduni moja ni bora kuliko mwingine. Kila utamaduni una mantiki yake.

Dhana zilizomo katika Riding the Waves of Culture zimenipa mianya ya kufafanua yale niliyoandika katika kitabu changu. Tofauti kubwa kati ya vitabu hivi viiili ni kuwa Riding the Waves of Culture kimeandikwa kitaaluma na ni kikubwa, wakati Africans and Americans: Embracing Cultural Differences kimeandikwa kiwe rahisi kusomwa na yeyote na ni kifupi sana.

Thursday, June 14, 2018

Mwalimu Mwingine Aongelea Kitabu Changu

Ni jadi yangu kuwatambua wasomaji wanaosema neno kuhusu vitabu vyangu. Ni namna ya kuwashukuru kwa kutumia muda wao kukisoma kitabu na kutumia tena muda kuandika maoni yao. Ninatambua kwamba wanafanya hivyo kwa hiari, na wangeweza kutumia muda wao kwa namna nyingine. Ninawashukuru.

Wiki hii amejitokeza mwalimu Khalid Kitito, ambaye amekitumia kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences katika ufundishaji wake hapa Marekani, akaandka maoni kwenye mtandao wa PublicReputation:

Africans and Americans written by Joseph Mbele is an excellent book to read about cultural differences between Americans and Africans. He examined the deep culture and not surface culture. It brings out clearly the understanding as to why Americans and Africans have different perspective of time, relationships, work, family, love, respect among others. I used it to teach in my Culture and Identity Class and found it useful. The book provided a forum for insightful discussions and at the end of the course students were able to view other cultures as different and not weird. It is also easy to read and understand, thus suitable for general readers.

Napenda kugusia tathmini yake kuwa ninaibua "deep culture." Wanataaluma wa tamaduni wanasisitiza suala hili la "deep culture." Tunapokutana na utamaduni wowote, tunaona mambo mengi, lakini ili kuyaelewa yale tunayoyaona, tunatakiwa kuelewa msingi wake. Hii ndio "deep culture." Inachukua muda sana kuuelewa utamaduni kwa maana hiyo. Ndivyo ilivyokuwa kwangu, katika kutafakari utamaduni wa wa-Marekani. Ilinichukua miaka karibu ishirini ya kuishi na wa-Marekani kabla sijathubutu kuandika kitabu changu. Kwa upande mwingine, kwa kuwa mimi ni mtafiti na mwalimu wa fasihi na "folklore" na ni mw-Afrika, haikuwa shida kwangu kuelezea "deep culture" kwa upande wa wa-Afrika.

Pamoja na kumshukuru mwalimu Kitito, kwa kuandika maoni yake, ninatoa mwaliko kwa yeyote mwingine aliyesoma au kutumia kitabu changu chochote kuandika maoni yake katika ukurasa huu wa PublicReputation.

Friday, June 8, 2018

Tunasoma "Homegoing," Riwaya ya Yaa Gyasi


Tarehe 4 Juni, nilianza kufundisha kozi ya kiangazi hapa chuoni St. Olaf juu ya fasihi ya Afrika (African Litterature). Nimefundisha kozi hiyo mara kadhaa miaka iliyopita. Baada ya mimi kutoa utangulizi siku mbili za mwanzo, tulianza kusoma riwaya ya Yaa Gyasi iitwayo Homegoing.

Yaa Gyasi alizaliwa Ghana akakulia hapa Marekani. Nilikutana naye katika tamasha la Hemingway mjini Moscow, katika jimbo la Idaho akiwa ni mgeni rasmi wa tamasha kufuatia riwaya yake kushinda tuzo ya PEN/Hemingway kwa mwaka 2017.

Homegoing, inaturudisha nyuma karne tatu zilizopita, kwenye nchi ambayo leo ni Ghana. Tunaona jamii inavyoishi mila na desturi zake na mahusiano ya watu, lakini tunaona pia shughuli ya biashara ya utumwa. Tunaona jinsi watu walivyokuwa wakitekwa kufanywa watumwa na wengi kupelekwa pwani kwenye kasri ya Cape Coast kuhifdhiwa humo katika mazingira ya ovyo kupindukia, wakisubiri kuvushwa bahari kwenda Marekani.

Homegoing inafaa kusomwa sambamba na tamthilia ya The Dilemma of a Ghost, ya Ama Ata Aidoo, ambayo iliigizwa mara ya kwanza mwaka 1964, ikachapishwa mwaka 1965. Tungo hizi zinafaa kulinganishwa hasa kwa kuwa zinahusika na dhamira ya watu kuchukuliwa kutoka Afrika Magharibi kwenda utumwani Marekani. Vile vile zote zinatumia vipengele vya sanaa ya fasihi simulizi. Wanafunzi wangu nami bado tunaisoma riwaya hii, na tutajua mengi zaidi kadiri tunavyoendelea kusoma.

Sunday, June 3, 2018

Vitendea Kazi vya Kampuni Yangu

Mwaka 2002, nilianzisha na kusajili kampuni ambayo niliita Africonexion, kama nilivyoandika katika blogu hii. Nilisajili kama kampuni binafsi, usajili ambao hapa Marekani hujulikana kama "sole proprietorship." Niliamua kuanzisha na kusajili kampuni hii ya kutoaelimu na ushauri wa masuala ya utamaduni kwa kuwa tayari nilikuwa na uzoefu wa shughuli hizo, nikihudumia vyuo, makanisa, mashirika, jumuia na watu binafsi.

Shughuli zangu hizi zimekuwa na mafanikio makubwa, kwa maana kwamba nimewasaidia watu kuelewa na kuepukana na mambo ambayo yanaweza kusababisha migogoro na kutoelewana. Wale ambao tayari walishakumbana na migogoro na kutoelewana nimewasaidia kufahamu kwa nini walijikuta katika migogoro na kutoelewana. Lakini mimi mwenyewe nimefanikiwa pia kujifunza mengi katika shughuli zote hizo.

Napenda kuelezea siri moja kubwa ya mafanikio haya. Siri hiyo ni kujielimisha kwa kutumia vitabu. Vitabu ndio vitendea kazi vyangu. Sichoki kununua na kusoma vitabu. Kulingana na shughuli za kampuni yangu, ninanunua na ninasoma vitabu kuhusu masuala kama utandawazi, utamaduni, na saikolojia. Jana, kwa mfano, bila kutegemea, nilikiona kitabu kiitwacho Riding the Waves of Culture, katika duka la Half Price Books, mjini Apple Valley. Nilipokiona tu, nilitambua kuwa kitakuwa kitendea kazi muhimu.

Mbali na kutumia vitabu vya wengine, ninatumia pia kitabu nilichoandika mwenyewe, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Kitabu hiki kilitokana na uzoefu nilioongelea hapa juu. Si mimi tu ambaye ninakichukulia kitabu hiki kama kitendea kazi muhimu. Mifano ni profesa na mwandishi maarufu Becky Fjelland Brooks, ambaye aliakiongelea kitabu katika blogu yake. Mzee Patrick Hemingway, ambaye aliwahi kuishi Tanzania miaka yapata ishirini na tano, aliwahi kuniambia kuwa kitabu hiki ni "a tool of survival" yaani kimbilio la usalama.

Hili suala la kuviona vitabu kama vitendea kazi ni muhimu. Hainiingii akilini mtu aanzishe biashara, kwa mfano, halafu asitafute na kusoma vitabu au maandishi mengine juu ya uendeshaji wa biashara. Atafanikishaje malengo yake kama hafahamu vitu kama saikolojia ya binadamu, ambao ndio wateja wake? Atafanikiwaje kama hafahamu namna ya kuwasiliana na watu? Kama wateja wake ni wa tamaduni tofauti na utamaduni wake, ni muhimu mno afahamu tofauti hizo.

Nilivutiwa na msimamo wa Mama Barbro Finskas Mushendwa, mmiliki wa kampuni ya utalii ya J.M Tours, yenye makao yake Arusha, Tanzania. Baada ya kusoma kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, aliamua kununua nakala kadhaa kwa ajili ya wafanyakazi wake, ambao walikuwa ni madreva wa watalii. Aliona haraka kuwa kitabu hiki kinafaa kama kitendea kazi na madreva wake walinithibitishia hivyo, kama nilivyoripoti katika blogu ya ki-Ingereza.

Mmiliki wa kampuni yoyote anajua ulazima wa vitendea kazi kama vile magari na kompyuta, sawa na mkulima navyojua ulazima wa jembe na shoka. Lakini sijui ni wamiliki wa makampuni na wafanya biashara wangapi wa Tanzania wenye mtazamo kama wa Mama Mushendwa, wa kutambua kuwa vitabu ni vitendea kazi. Ninaona wanaanzisha kampuni au biashara na kuziendesha kimazoea,  au kwa kutegemea kudra ya Mungu au hata waganga wa kienyeji. Daima ninaona matangazo ya waganga wa kienyeji wakinadi dawa za mafanikio kibiashara.

Ninapoongelea mada hii ya vitabu kama vitendea kazi, ninakumbuka juhudi aliyofanya Mwalimu Nyerere katika kutekeleza kile alichoita elimu yenye manufaa. Aliwahimiza watu kujisomea ili kuboresha shughuli walizokuwa wanafanya. Chini ya uongozi wake, vilichapishwa na kusambazwa vitabu kuhusu kilimo, uvuvi, useremala, na kadhalika. Ninakumbuka kwamba kijijini kwangu, vitabu hivyo vilihifadhiwa katika nyumba ya baba yangu.

Pamoja na mimi kutumia vitabu vya wengine kama vitendea kazi, ninashukuru kwamba nami ni mwandishi. Ninapangia kuendelea kuandika ili kuchangia ufanisi katika shughuli zangu na za wengine.

Saturday, May 26, 2018

Nimekutana na Msomaji Mpya

Jana jioni nilikutana na msomaji mpya wa kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Nilikuwa mjini St. Paul kuhudhuria darasa la Nu Skool, ambayo ni jumuia ya wa-Marekani Weusi wanaokutana mara moja kwa mwezi kutafakari na kujadili masuala mbali mbali.

Kwa kawaida, kunakuwepo na mtoa mada na kunakuwepo na masuali ya watu kuyajadili. Wakati mwingine inaonyeshwa filamu ya kuelimisha, ambayo inafuatiliwa na mjadala pia. Mada ya mkutano wa jana ilikuwa "The Language of Black America."

Jana hiyo, tulipokuwa tumemaliza darasa na baadhi yetu tukawa tunaendelea kuongea na kutambulishana, mama moja aliniambia kuwa anasoma kitabu changu na kuwa kinamgusa sana. Mama huyu m-Marekani Mweusi alisema kuwa mambo ninayoelezea yanamwezesha kujitambua ni nani kiasili. Alisema anakisoma kitabu kidogo kidogo kwa makusudi ili kuupata ujumbe vizuri, bila pupa. Alisema kuwa, katika maisha yake kama m-Marekani Mweusi alikuwa na hisia mbali mbali, lakini hakuelewa chimbuko lake, ila kitabu kimemfunulia chanzo, yaani u-Afrika. Mama huyu amenigusa kwa kauli hiyo.

Nilimwuliza alisikiaje habari za kitabu hiki, kwani hiyo ni moja ya duku duku zangu. Aliniambia kuwa alihudhuria mhadhara wangu Nu Skool na ndipo alipofahamu kuhusu kitabu changu. Alikiagiza Amazon. Alisisitiza kuwa amekiweka chumbani na anasoma kidogo kidogo kwa makusudi.

Nimeshasema katika blogu hii kuwa tangu mwanzo nilipoandika na kisha kuchapisha kitabu hiki, nilikuwa na wasi wasi na duku duku kuhusu namna wa-Marekani Weusi watakavyokipokea, kwa kuwa ninagusia tofauti baina yao na wa-Afrika kwa namna ambayo huenda ikawakwaza baadhi yao. Lakini nimeshukuru kwamba hadi sasa, inaonekana kuwa hali ni shwari.

Nimeguswa na kauli za mama huyu. Nimeguswa na furaha aliyo nayo kutokana na kusoma niliyoandika. Sina namna ya kuelezea ninavyojisikia, kwani amenifanyia hisani kubwa kwa kunijulisha kuwa niliyoandika yana maana kubwa kwake, katika kujielewa na kumfariji. Ushuhuda kama huu ni motisha kwangu, niendelee kutafakari mambo na kuandika.

Tuesday, May 15, 2018

Mtanzania Afundishaye ki-Swahili Marekani Akifurahia Kitabu

Mimi kama mwandishi ninathamini maoni ya wasomaji juu ya maandishi yangu. Msomaji anapokuwa ametumia muda wake kusoma na kutafakari nilichoandika, halafu akatumia muda wake kuandika maoni, kwangu si jambo dogo. Ninashukuru. Katika blogu hii nina jadi ya kuwatambua wadau hao.

Hivi karibuni, nimeona andiko la Filipo Lubua katika ukurasa wake wa facebook kuhusu kitabu changu Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Huyu anafundisha ki-Swahili katika Chuo Kikuu cha Pittsburgh hapa Marekani. Anasema kwamba anakitumia kitabu hiki katika kozi juu ya Afrika Mashariki, na anasema ni kitabu kinachovutia sana. Ananishukuru kwa kukiandika kitabu hiki rahisi kusomeka juu ya mitazamo yetu, yaani sisi wa-Afrika na wenzetu wa-Marekani. Anasema kuwa wanafunzi wake wamo katika program ya masomo ambayo watasoma Tanzania. Watakuwa Dar es Salaam na Iringa kwa wiki yapata tano.

Katika mawasiliano ya ziada, mwalimu Lubua amesisitiza kuwa hiki kitabu muhimu sana hasa katika kufundishia utamaduni wa Kiswahili. Kauli yake hiyo imenikumbusha maelezo ya Leonce Rushubirwa, m-Tanzania mwingine mwalimu wa ki-Swahili Marekani, kuhusu matumizi ya kitabu hiki katika kufundishia ki-Swahili. Kuongea na wataalam wa aina hiyo ni fursa ya kujithibitishia ile dhana kwamba lugha imefungamana na utamaduni.

Tuesday, May 8, 2018

Nimeshiriki Amani Festival 2018

Tarehe 5 nilikuwa Carlisle, Pennsylvania, kushiriki katika tamasha liitwalo Amani Festival, ambalo nilishiriki mara ya mwisho mwaka 2005. Nilipata fursa ya kuonyesha baadhi ya vitabu vyangu na kuongea na watu mbali mbali, akiwemo mama mmoja ambaye alifanya kazi Afrika Kusini kwa miaka mitatu. Nilipata pia fursa ya kuhojiwa na mwandishi wa gazeti la Carlisle liitwalo The Sentinel.



















Kama kawaida, nilipanga vitabu mezani, na hicho kikawa kivutio. Watu wanafika hapo, na inakuwa ni fursa ya kuongea mambo mengi, kuhusu vitabu na yatokanayo.









Huyu mama alipopita mezani pangu alinyooshea kidole kitabu cha Matengo Folktales akisema "I have read that book!" akimaanisha amesoma kitabu hicho. Nilishangaa, nikaanzisha mazungumzo naye. Aliniambia kuwa alinunua kitabu hiki na kusainiwa nami miaka iliyopita, nikajua kuwa ni yapata miaka kumi na tano iliyopita, ambapo nilishiriki tamasha hili. Aliniambia kuwa yeye na mumewe ni wa kanisa moja hapa ambalo lina uhusiano na dayosisi ya Konde ya Kanisa la ki-Luteri Tanzania.Hapo nilijionea kuwa kumbe dunia hii ni ndogo sana.


















Hao ni wanafunzi wakicheza muziki wa Afrika.




























































Wadau hawajifichi







Wednesday, May 2, 2018

Wadau Niliokutana Nao Wikii Hii

Katika siku saba zilizopita, nimekutana na wadau wengi wa vitabu vyangu. Kwanza, nilipata barua pepe kutoka kwa mtu aliyejitambulisha kuwa ni m-Marekani anayefundisha ki-Ingereza Mwanza kwa kujitolea. Ameandika kuhusu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences:

Nimemaliza kitabu chako kuhusu tofauti za tamaduni zetu na nilikifurahia sana. Ulinichekesha mara nyingi. Aidha ukanieleza mambo mengi.

Aprili tarehe 28, niliongea na wanafunzi wa somo la Global Semester ambao watasafiri na kukaa sehemu mbali mbali za dunia, ikiwemo Arusha, Tanzania, ambako watakaa kwa mwezi moja. Profesa wao aliniomba nikawaeleze masuala ya tofauti za tamaduni. Yeye mwenyewe amesoma Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Tarehe 28 Aprili, nilikuwa Rochester, Minnesota, kushiriki tamasha la kimataifa linaloandaliwa kila mwaka na Rochester International Association. Hapo nilikutana na hao ndugu wawili wanaoonekana pichani hapa juu. Huyu wa kushoto ni daktari katika hospitali maarufu ya Mayo, mwenye asili ya Uganda, na huyu wa kulia ni m-Kenya ambaye alikuwa mwanafunzi wetu chuoni St. Olaf. Tuliongea kirefu. Daktari ndiye aliyetaka tupige hiyo picha tukiwa tumeshika vitabu vyangu.

Friday, April 27, 2018

Madaktari Wanafundishia Kitabu Hiki

Nilivyoandika kitabu changu Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, sikuwazia kingetumika kwa namna nyingi kama ilivyotokea baadaye. Kilichonishtua zaidi ni pale waalimu wa uuguzi wa chuo cha Gustavus Adolphus walipoamua kukitumia kufundishia, wakaanza, kila wanapofundisha kozi hiyo, kunialika kuongea na wanafunzi.

Baada ya muda si mrefu, Dr. Randy Hurley mwanzilishi na mhusika mkuu wa  na programu ya hospitali ya Ilula, mkoani Iringa, alinialika kuhutubia mkutano wa mwaka wa wadau wa hospitali hiyo. Ulikuwa ni mkutano wa kuchangisha fedha za kuendelezea programu. Hapo ndipo nikajua kuhusu programu ya kuelimisha wauguzi ambayo inafanyika Ilula, ikiwahusisha wa-Marekani na wa-Tanzania.

Nilijua kuwa wanatumia kitabu changu, bali sikuwa na taarifa zaidi. Lakini siku chache zilizopita nimeona jinsi kitabu hicho kinavyotajwa katika silabasi mpya ya kozi yao. Wanafunzi wanahimizwa kukisoma. Kwa kuwa mimi si mtaalam wa masuala ya uuguzi na matibabu, nilijiuliza masuali, kwa sababu baadhi ya mambo niliyoandika kitabuni ni tofauti na taaluma ya uuguzi na matibabu. Dukuduku yangu hii niliigusia katika blogu hii.

Hatimaye, nilikuja kuelewa vizuri mantiki ya madkatari na waalimu wa uuguzi kukitumia kitabu hiki. Ni kwa sababu kinaelezea utamaduni hauwezi kutenganishwa na masuala ya matibabu ba uuguzi. Madaktari na wauguzi wanatakiwa kuwafahamu wale wanaowahudumia, katika vipengele kama jadi, tabia, matarajio, miiko, imani, na hisia. Ni muhimu kwa muuguzi au daktari kuyafahamu na kuyazingatia wakati anatoa huduma. Kwa hivyo, sasa ninavyosikia kitabu kinatumiwa na watu katika taaluma hizo, sina masuali bali ninashukuru kwamba nimeweza kutoa mchango fulani wa manufaa.

Saturday, April 21, 2018

Mdau Amechagua Kitabu

Jana nimeona taarifa iliyonigusa kwa namna ya pekee. Mdau ameweka mtandaoni picha inayoonekana kushoto, akiwa ameambatanisha ujumbe: "Decided to bring some required reading with me." yaani anasema ameamua kubeba vitabu muhimu vya kujisomea. Hakusema kama anasafiri, lakini ujumbe wake unaashiria hivyo.

Niliguswa kuona kitabu changu Africans and Americans: Embracing Cultural Differences ni kimojawapo alichochagua, nikaandika "I am humbled that you have my "Africans and Americans" book on your list," yaani "nimeishiwa nguvu kuona kuwa umetaja kitabu changu katika orodha yako." Jibu aliloandika ni "Yes! I'm learning a lot. It's funny too. Thanks for the enlightenment," yaani "Ndio! Ninajifunza mengi. Kitabu kinachekesha pia. Asante kwa uelimishaji."

Nimeguswa kwa namna ya pekee kwa sababu mdau huyu, ambaye anaonekana nami pichani hapa kushoto, ni mtu mwenye ushawishi katika jamii, kama nilivyowahi kuelezea katika blogu hii. Ninafarijika kuwa kitabu changu ambacho nilikichapisha mwaka 2005 bado kinafanikisha malengo niliyokuwa nayo wakati nilipokuwa ninakiandaa na kukiandika. Lengo kuu lilikuwa ni kuwaelimisha watu, hasa wa-Afrika na wa-Marekani, kuhusu tofauti za tamaduni zao, iwe ni kinga ya kuzuia migongano na kutoelewana. Ila, kama huyu mdau anavyosema, kitabu hiki, pamoja na kuwa kinaelimisha, ni burudani pia.

Ninaweka taarifa hii hapa katika blogu yangu, kwa sababu hapa ni mahali ninapotunzia kumbukumbu zangu, kama nilivyowahi kuelezea.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...