Friday, June 8, 2018

Tunasoma "Homegoing," Riwaya ya Yaa Gyasi


Tarehe 4 Juni, nilianza kufundisha kozi ya kiangazi hapa chuoni St. Olaf juu ya fasihi ya Afrika (African Litterature). Nimefundisha kozi hiyo mara kadhaa miaka iliyopita. Baada ya mimi kutoa utangulizi siku mbili za mwanzo, tulianza kusoma riwaya ya Yaa Gyasi iitwayo Homegoing.

Yaa Gyasi alizaliwa Ghana akakulia hapa Marekani. Nilikutana naye katika tamasha la Hemingway mjini Moscow, katika jimbo la Idaho akiwa ni mgeni rasmi wa tamasha kufuatia riwaya yake kushinda tuzo ya PEN/Hemingway kwa mwaka 2017.

Homegoing, inaturudisha nyuma karne tatu zilizopita, kwenye nchi ambayo leo ni Ghana. Tunaona jamii inavyoishi mila na desturi zake na mahusiano ya watu, lakini tunaona pia shughuli ya biashara ya utumwa. Tunaona jinsi watu walivyokuwa wakitekwa kufanywa watumwa na wengi kupelekwa pwani kwenye kasri ya Cape Coast kuhifdhiwa humo katika mazingira ya ovyo kupindukia, wakisubiri kuvushwa bahari kwenda Marekani.

Homegoing inafaa kusomwa sambamba na tamthilia ya The Dilemma of a Ghost, ya Ama Ata Aidoo, ambayo iliigizwa mara ya kwanza mwaka 1964, ikachapishwa mwaka 1965. Tungo hizi zinafaa kulinganishwa hasa kwa kuwa zinahusika na dhamira ya watu kuchukuliwa kutoka Afrika Magharibi kwenda utumwani Marekani. Vile vile zote zinatumia vipengele vya sanaa ya fasihi simulizi. Wanafunzi wangu nami bado tunaisoma riwaya hii, na tutajua mengi zaidi kadiri tunavyoendelea kusoma.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...