Saturday, June 24, 2017

Eti Tundu Lissu Anapinga Kila Kitu

Kuna wa-Tanzania wanaomlalamikia au kumshambulia Tundu Lissu eti anapinga kila kitu. Napenda kusema kuwa malalamiko na mashambulio haya ni ujinga.

Kutoa mawazo na kujieleza ni haki ya kila binadamu, ambayo imetambuliwa katika tangazo la kimataifa la haki za binadamu na imetambuliwa katika katiba ya Tanzania. Tundu Lissu anatumia haki yake. Haingilii wala kuzuia haki ya mtu yeyote kutoa mawazo. Watu wajibu hoja zake. Watu wenye akili hufanya hivyo.

Kama Tundu Lissu hakubaliani na yale wanayosema wengine, na anahoji au kupinga muda wote, tatizo liko wapi? Masuala yenyewe yanahusu maslahi ya Taifa. Kila mzalendo anawajibika kutoa mchango kadiri ya uwezo wake. Mawazo ni mchango mmoja wapo. Na hiki ndicho Tundu Lissu anachofanya. Akae kimya kwa nini? Hata mimi sikai kimya ninapoona maslahi ya nchi hayafuatiliwi ipasavyo au yanahujumiwa. Kutoa mawazo ni muhimu, na kukosoana, inapobidi.

Ni ujinga kutotambua kuwa anavyofanya Tundu Lissu anatoa changamoto ya kuwafanya watu wafikiri nje ya upeo waliozoea au nje ya upeo wanaouwazia wao. Elimu haisongi mbele kama hakuna watu wachochezi wa fikra kama Tundu Lissu. Watu wanaohoji fikra zinazokubalika na jamii wanaipa jamii fursa ya kufungua milango mipya ya fikra. Siafiki uwekaji wa mipaka katika kufikiri na kutafuta ukweli. Elimu haiwekewi mipaka.

Mimi kama mwalimu ninawajibika kuwalea vijana wawe watu wa kuhoji mambo bila ukomo. Vinginevyo, kuna sababu gani ya kujiita mwalimu? Kuna sababu gani ya kuwa na vyuo na kusema kuwa tunaelimisha? Watu makini ulimwenguni kote wanatambua kuwa dunia inazidi kuwa ya "knowledge economy." Bila tabia ya udadisi usiokuwa na mipaka, tutajengaje "knowledge economy"? Kwa maana hiyo, ninamwona Tundu Lissu kama mtu muhimu kwa maendeleo ya nchi, na ni mfano wa kuigwa.

Monday, June 19, 2017

Mzalendo Tundu Lissu Aliyasema Haya Mambo

Leo nimeona taarifa za kufikishwa mahakamani watuhumiwa wakuu wawili wa ufisadi mkubwa nchini Tanzania. Watuhumiwa hao ni Harbinder Singh Sethi na James Rugemalira. Wananchi wengi tunalichukulia jambo hili kama mwendelezo wa juhudi za Rais Magufuli kusafisha nchi. Lakini kitu kimoja kinachonikera ni jinsi watu wengine wanavyojaribu kupindisha historia ya suala hili. Hapa naleta hotuba ya Tundu Lissu aliyoitoa Bungeni kabla ya ujio wa Rais Magufuli.

Wednesday, June 7, 2017

Umuhimu wa Kumpigia Mbuzi Gitaa

Katika jamii yetu wa-Tanzania, usemi kwamba usimpigie mbuzi gitaa unachukuliwa kuwa ni ukweli usiopingika, busara isiyo na walakini. Ni kile kinachojulikana kama busara ya kawaida, yaani "common sense," kwa ki-Ingereza. Lakini je, mtazamo huu ni sahihi? Hili ndilo suala ninalopenda kulijadili hapa, kwa mtazamo wangu kama msomi, mtafiti na mwalimu.

Napenda kutamka wazi kuwa kwa msomi au mwalimu au mtafiti, "common sense" ni kitu cha kujihadhari nacho. Kazi ya msomi, mwalimu au mtafiti si kuzingatia, kuafiki, au kuhalalisha "common sense," bali kuhoji na kudadisi "common sense." Ndivyo alivyofanya mwelimishaji maarufu Socrates. Kuna wengi wengine, kama vile Galileo. Jamii yote ilielewa kuwa jua linaizunguka dunia, kwani kila mtu alijionea mwenyewe. Ilikuwa ni "common sense." Lakini Galileo, akiendeleza mawazo ya Copernicus, alisema kuwa ni dunia ndio inayolizunguka jua. Jamii ya Galileo ilimtia matatani, kama vile jamii ya Socrates ilivyomtia matatani.

Turudi kwenye suala la kumpigia mbuzi gitaa. Ninapenda kusema kuwa ni wajibu wa msomi, mtafiti, au mwalimu kuhoji hii busara ya jamii kwamba kumpigia mbuzi gitaa ni kupoteza muda au ni ujinga. Msimamo huu wa jamii una walakini mkubwa. Ukipiga gitaa, inatoa sauti. Je, jamii inamaanisha kuwa mbuzi hana uwezo wa kutambua na kuguswa na sauti? Kama jamii inaamini hivyo, inakosea.

Sisi ambao tulikulia kijijini tukichunga mbuzi tunajua kuwa mbuzi wana milio yao ambayo wanatumia kuwasiliana. Hata wakati wa kuchunga, tulikuwa tunaweza kutambua mlio wa mbuzi mwenye dhiki. Tulikuwa tunawaita mbuzi kwa majina tuliyowapa au kwa kupiga mluzi. Kwa hivi, jamii inakosea iwapo inaamini kuwa mbuzi hawana uwezo wa kujieleza, kutambua au kuguswa na sauti.

Suala la kulitafakari ni sauti ipi ambayo mbuzi anaitambua na kuguswa nayo, na ipi hawezi kuitambua na kuguswa nayo. Kinachohitajika si hiyo "common sense" kwamba usimpigie mbuzi gitaa, bali utafiti. Tunatakiwa kumpigia mbuzi gitaa tena na tena, kwa mitindo mbali mbali.

Utafiti hauwekewi kikomo. Hata pale tunapodhani tumepata ufumbuzi wa suala, hatupigi marufuku utafiti zaidi wa suala hilo. Badala ya kuridhika na busara ya jamii kuwa tusimpigie mbuzi gitaa, mtafiti au msomi huwaza: kwa nini nisimpigie mbuzi gitaa? Itakuwaje nikimpigia mbuzi gitaa? Ngoja nimpigie mbuzi gitaa nione kitakachotokea. Huu ndio mtazamo wa mtafiti, msomi, na mwalimu. Hii duku duku ya kujua huitwa "intellectual curiosity" kwa ki-Ingereza.

Msomi au mtafiti au mwalimu ni mtu anayetafuta elimu muda wote. Thomas Edison, mvumbuzi maarufu, alifanya majaribio ya kuvumbua na kuunda vitu akashindwa mara nyingi sana, lakini hatimaye alivumbua balbu ya umeme. Huu ndio moyo unaohitajika katika suala hili la kumpigia mbuzi gitaa. Tukitaka mfumo wa elimu wa kweli, inatubidi tujenge mtazamo na mwelekeo huu wa kutambua umuhimu kumpigia mbuzi gitaa.

Unapofanya utafiti kwa ajili ya kuchunguza suala fulani huwezi kujua matokeo yatakuwa yepi. Unaweza kupata matokeo ambayo hukutegemea. Katika majaribio yake ndani ya maabara, mwaka 1928 Alexander Fleming aliona kitu kimejitokeza kwenye kisahani kimojawapo alimoweka vitu vya kuvichunguza. Kitu hicho kilikuwa kimejitokeza bila yeye kutegemea, lakini ndicho kilikuja kubainika kuwa ni penicillin.

Kwa hivyo, mtu ukianza kumpigia mbuzi gitaa, ukawa anafuatilia kwa makini kila kinachotokea, huenda utajifunza mambo ambayo hakutegemea kuhusu tabia na hisia za mbuzi. Inawezekana ukipiga gitaa mara ya kwanza usione lolote likitokea. Lakini je, unajuaje kama hakutakuwa na mabadiliko yoyote ukimpigia mara kumi, au mara mia, au zaidi?

Kama unadhani ninatania, napenda tujikumbushe utafiti na uvumbuzi aliofanya Ivan Pavlov akitumia mbwa. Pavlov alifanya majaribio ambayo yalitoa mchango mkubwa katika taaluma ya saikolojia. Nashauri msomaji utafute taarifa za Pavlov na majaribio yake na uvumbuzi aliofanya. Huenda utakubaliana nami kuwa suala la kumpigia mbuzi gitaa si la kupuuzwa. Ni muhimu.

Sunday, June 4, 2017

Vitabu Vinavyopinga Dini

Ingawa mimi ni muumini wa dini, m-Katoliki, ninapenda kuzifahamu dini zingine. Sijiwekei mipaka. Sina tatizo na watu wa dini tofauti na yangu, wala watu wasio na dini. Ninajifunza kutoka kwao. Mtu unajifunza mengi kutoka kwa watu wenye mawazo tofauti na yako.

Ninasoma vitabu vya dini zingine, kama nilivyowahi kueleza katika blogu hii. Vile vile ninasoma vitabu vinavyohoji au kupinga dini. Fikra za wapinga dini zinafikirisha. Mfano ni kauli ya Karl Marx: "Religion is the sigh of the oppressed creature, the heart of a heartless world, and the soul of soulless conditions. It is the opium of the people."

Ninaipenda kauli hiyo ya Marx kwa kuwa inafikirisha na kusisimua akili. Kuna ubaya gani kwa mtu kuiponda dini namna hii? Kuna sababu gani ya mimi muumini kumchukia mtu wa aina hiyo? Kama vile mimi ninavyotetea haki na uhuru wa kuwa na mawazo yangu, naye ana haki na uhuru wa kuwa na mawazo tofauti na yangu. Ana uhuru wa kujieleza na kusambaza mawazo yake.

Ninavyo vitabu vinavyohoji u-Kristu. Mifano ni Jesus: Prophet of Islam, kilichotungwa na Muhammad Ata Ur-Rahim na Ahmad Thomson; The Gnostic Gospels, kilichotungwa na Elaine Pagels; na The Essential Gnostic Gospels, Including the Gospel of Thomas & The Gospel of Mary, kilichotungwa na Alan Jacobs. Nina vitabu vinavyouhoji u-Islam, vya waandishi kama Ayaan Hirsi Ali na Nawaal el Saadawi. Kuna vingine ambavyo bado sina, ila nitavinunua, kama vile vya Wafa Sultan na Ibn Warraq.

Kama mtu umejengeka katika dini yako na unatambua umuhimu na maana yake, kuna sababu gani ya kuvichukia vitabu vinavyoihoji dini? Jazba au masononeko ya nini, kama si ishara ya udhaifu na ubabaishaji wako mwenyewe? Binafsi, niko imara, na wahenga walisema, kelele za chura hazimzuii ng'ombe kunywa maji.

Fikra zinazohoji dini ninaziona kuwa zenye manufaa. Mimi kama muumini ninazichukulia hizo kama fursa ya kuimarisha imani, sawa na misukosuko inavyomkomaza mtu. Wakristu tunafundishwa uvumilivu, na hii ni njia ya kujipima tuna imani kiasi gani. Kama kawaida, nakaribisha maoni.

Friday, June 2, 2017

Kitabu Kimependekezwa na Africa International University

Nimeona leo kuwa kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, kimependekezwa na Africa International University (AIU) kwa ajili ya wanafunzi wa kigeni. Chuo hiki kiko Karen, nchini Kenya.

Nimevutiwa na maelezo yaliyotolewa kama Information for International Students juu ya hali halisi anayokumbana nayo mtu anapojikuta katika utamaduni wa kigeni:

Moving to a different cultural environment is a very stressful experience – that’s why it is sometimes referred to as “culture shock”. You will likely go through a difficult period of adjustment and homesickness after the initial excitement wears off. This is normal. As you learn your way around the campus and its unique culture, you will be more comfortable at AIU. Soon you will be helping other new international students adjust to AIU and Kenya. If you are willing to learn, you will learn a great deal about yourself and others who are different from you. You will leave here enriched and transformed.

Still, it is wise to take time before coming to prepare yourself and your family for the cultural adjustments that will be necessary. By reading as much as you can about cultural adjustment and talking to other international students, you can learn what to expect. Then you will better understand the feelings and frustrations you deal with as you adjust to your new environment. Since academics will demand a great deal of you at AIU, any preparation you can do before coming will help all of your adjustments once you arrive on campus....Due to cultural differences, you may feel somewhat confused when talking with fellow students. “What do they mean?” Communication in Africa is inferential rather than direct, so you will need to become adept at listening for what is being communicated between the lines.... Students at AIU are coming from all over Africa and the world. They will appreciate the time you invest in learning about the uniqueness of their own cultures—e.g. what communicates respect.

Maelezo na mawaidha haya yanahusiana na yaliyomo katika kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Ni masuala yasiyokwepeka, hasa katika dunia ya utandawazi wa leo. Yanawahusu sio tu wanafunzi, bali pia wafanya biashara, wanadiplomasia, na kadhalika, kama ninavyoelezea mara kwa mara katika blogu hii.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...