Showing posts with label mafanikio. Show all posts
Showing posts with label mafanikio. Show all posts

Sunday, June 3, 2018

Vitendea Kazi vya Kampuni Yangu

Mwaka 2002, nilianzisha na kusajili kampuni ambayo niliita Africonexion, kama nilivyoandika katika blogu hii. Nilisajili kama kampuni binafsi, usajili ambao hapa Marekani hujulikana kama "sole proprietorship." Niliamua kuanzisha na kusajili kampuni hii ya kutoaelimu na ushauri wa masuala ya utamaduni kwa kuwa tayari nilikuwa na uzoefu wa shughuli hizo, nikihudumia vyuo, makanisa, mashirika, jumuia na watu binafsi.

Shughuli zangu hizi zimekuwa na mafanikio makubwa, kwa maana kwamba nimewasaidia watu kuelewa na kuepukana na mambo ambayo yanaweza kusababisha migogoro na kutoelewana. Wale ambao tayari walishakumbana na migogoro na kutoelewana nimewasaidia kufahamu kwa nini walijikuta katika migogoro na kutoelewana. Lakini mimi mwenyewe nimefanikiwa pia kujifunza mengi katika shughuli zote hizo.

Napenda kuelezea siri moja kubwa ya mafanikio haya. Siri hiyo ni kujielimisha kwa kutumia vitabu. Vitabu ndio vitendea kazi vyangu. Sichoki kununua na kusoma vitabu. Kulingana na shughuli za kampuni yangu, ninanunua na ninasoma vitabu kuhusu masuala kama utandawazi, utamaduni, na saikolojia. Jana, kwa mfano, bila kutegemea, nilikiona kitabu kiitwacho Riding the Waves of Culture, katika duka la Half Price Books, mjini Apple Valley. Nilipokiona tu, nilitambua kuwa kitakuwa kitendea kazi muhimu.

Mbali na kutumia vitabu vya wengine, ninatumia pia kitabu nilichoandika mwenyewe, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Kitabu hiki kilitokana na uzoefu nilioongelea hapa juu. Si mimi tu ambaye ninakichukulia kitabu hiki kama kitendea kazi muhimu. Mifano ni profesa na mwandishi maarufu Becky Fjelland Brooks, ambaye aliakiongelea kitabu katika blogu yake. Mzee Patrick Hemingway, ambaye aliwahi kuishi Tanzania miaka yapata ishirini na tano, aliwahi kuniambia kuwa kitabu hiki ni "a tool of survival" yaani kimbilio la usalama.

Hili suala la kuviona vitabu kama vitendea kazi ni muhimu. Hainiingii akilini mtu aanzishe biashara, kwa mfano, halafu asitafute na kusoma vitabu au maandishi mengine juu ya uendeshaji wa biashara. Atafanikishaje malengo yake kama hafahamu vitu kama saikolojia ya binadamu, ambao ndio wateja wake? Atafanikiwaje kama hafahamu namna ya kuwasiliana na watu? Kama wateja wake ni wa tamaduni tofauti na utamaduni wake, ni muhimu mno afahamu tofauti hizo.

Nilivutiwa na msimamo wa Mama Barbro Finskas Mushendwa, mmiliki wa kampuni ya utalii ya J.M Tours, yenye makao yake Arusha, Tanzania. Baada ya kusoma kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, aliamua kununua nakala kadhaa kwa ajili ya wafanyakazi wake, ambao walikuwa ni madreva wa watalii. Aliona haraka kuwa kitabu hiki kinafaa kama kitendea kazi na madreva wake walinithibitishia hivyo, kama nilivyoripoti katika blogu ya ki-Ingereza.

Mmiliki wa kampuni yoyote anajua ulazima wa vitendea kazi kama vile magari na kompyuta, sawa na mkulima navyojua ulazima wa jembe na shoka. Lakini sijui ni wamiliki wa makampuni na wafanya biashara wangapi wa Tanzania wenye mtazamo kama wa Mama Mushendwa, wa kutambua kuwa vitabu ni vitendea kazi. Ninaona wanaanzisha kampuni au biashara na kuziendesha kimazoea,  au kwa kutegemea kudra ya Mungu au hata waganga wa kienyeji. Daima ninaona matangazo ya waganga wa kienyeji wakinadi dawa za mafanikio kibiashara.

Ninapoongelea mada hii ya vitabu kama vitendea kazi, ninakumbuka juhudi aliyofanya Mwalimu Nyerere katika kutekeleza kile alichoita elimu yenye manufaa. Aliwahimiza watu kujisomea ili kuboresha shughuli walizokuwa wanafanya. Chini ya uongozi wake, vilichapishwa na kusambazwa vitabu kuhusu kilimo, uvuvi, useremala, na kadhalika. Ninakumbuka kwamba kijijini kwangu, vitabu hivyo vilihifadhiwa katika nyumba ya baba yangu.

Pamoja na mimi kutumia vitabu vya wengine kama vitendea kazi, ninashukuru kwamba nami ni mwandishi. Ninapangia kuendelea kuandika ili kuchangia ufanisi katika shughuli zangu na za wengine.

Wednesday, June 7, 2017

Umuhimu wa Kumpigia Mbuzi Gitaa

Katika jamii yetu wa-Tanzania, usemi kwamba usimpigie mbuzi gitaa unachukuliwa kuwa ni ukweli usiopingika, busara isiyo na walakini. Ni kile kinachojulikana kama busara ya kawaida, yaani "common sense," kwa ki-Ingereza. Lakini je, mtazamo huu ni sahihi? Hili ndilo suala ninalopenda kulijadili hapa, kwa mtazamo wangu kama msomi, mtafiti na mwalimu.

Napenda kutamka wazi kuwa kwa msomi au mwalimu au mtafiti, "common sense" ni kitu cha kujihadhari nacho. Kazi ya msomi, mwalimu au mtafiti si kuzingatia, kuafiki, au kuhalalisha "common sense," bali kuhoji na kudadisi "common sense." Ndivyo alivyofanya mwelimishaji maarufu Socrates. Kuna wengi wengine, kama vile Galileo. Jamii yote ilielewa kuwa jua linaizunguka dunia, kwani kila mtu alijionea mwenyewe. Ilikuwa ni "common sense." Lakini Galileo, akiendeleza mawazo ya Copernicus, alisema kuwa ni dunia ndio inayolizunguka jua. Jamii ya Galileo ilimtia matatani, kama vile jamii ya Socrates ilivyomtia matatani.

Turudi kwenye suala la kumpigia mbuzi gitaa. Ninapenda kusema kuwa ni wajibu wa msomi, mtafiti, au mwalimu kuhoji hii busara ya jamii kwamba kumpigia mbuzi gitaa ni kupoteza muda au ni ujinga. Msimamo huu wa jamii una walakini mkubwa. Ukipiga gitaa, inatoa sauti. Je, jamii inamaanisha kuwa mbuzi hana uwezo wa kutambua na kuguswa na sauti? Kama jamii inaamini hivyo, inakosea.

Sisi ambao tulikulia kijijini tukichunga mbuzi tunajua kuwa mbuzi wana milio yao ambayo wanatumia kuwasiliana. Hata wakati wa kuchunga, tulikuwa tunaweza kutambua mlio wa mbuzi mwenye dhiki. Tulikuwa tunawaita mbuzi kwa majina tuliyowapa au kwa kupiga mluzi. Kwa hivi, jamii inakosea iwapo inaamini kuwa mbuzi hawana uwezo wa kujieleza, kutambua au kuguswa na sauti.

Suala la kulitafakari ni sauti ipi ambayo mbuzi anaitambua na kuguswa nayo, na ipi hawezi kuitambua na kuguswa nayo. Kinachohitajika si hiyo "common sense" kwamba usimpigie mbuzi gitaa, bali utafiti. Tunatakiwa kumpigia mbuzi gitaa tena na tena, kwa mitindo mbali mbali.

Utafiti hauwekewi kikomo. Hata pale tunapodhani tumepata ufumbuzi wa suala, hatupigi marufuku utafiti zaidi wa suala hilo. Badala ya kuridhika na busara ya jamii kuwa tusimpigie mbuzi gitaa, mtafiti au msomi huwaza: kwa nini nisimpigie mbuzi gitaa? Itakuwaje nikimpigia mbuzi gitaa? Ngoja nimpigie mbuzi gitaa nione kitakachotokea. Huu ndio mtazamo wa mtafiti, msomi, na mwalimu. Hii duku duku ya kujua huitwa "intellectual curiosity" kwa ki-Ingereza.

Msomi au mtafiti au mwalimu ni mtu anayetafuta elimu muda wote. Thomas Edison, mvumbuzi maarufu, alifanya majaribio ya kuvumbua na kuunda vitu akashindwa mara nyingi sana, lakini hatimaye alivumbua balbu ya umeme. Huu ndio moyo unaohitajika katika suala hili la kumpigia mbuzi gitaa. Tukitaka mfumo wa elimu wa kweli, inatubidi tujenge mtazamo na mwelekeo huu wa kutambua umuhimu kumpigia mbuzi gitaa.

Unapofanya utafiti kwa ajili ya kuchunguza suala fulani huwezi kujua matokeo yatakuwa yepi. Unaweza kupata matokeo ambayo hukutegemea. Katika majaribio yake ndani ya maabara, mwaka 1928 Alexander Fleming aliona kitu kimejitokeza kwenye kisahani kimojawapo alimoweka vitu vya kuvichunguza. Kitu hicho kilikuwa kimejitokeza bila yeye kutegemea, lakini ndicho kilikuja kubainika kuwa ni penicillin.

Kwa hivyo, mtu ukianza kumpigia mbuzi gitaa, ukawa anafuatilia kwa makini kila kinachotokea, huenda utajifunza mambo ambayo hakutegemea kuhusu tabia na hisia za mbuzi. Inawezekana ukipiga gitaa mara ya kwanza usione lolote likitokea. Lakini je, unajuaje kama hakutakuwa na mabadiliko yoyote ukimpigia mara kumi, au mara mia, au zaidi?

Kama unadhani ninatania, napenda tujikumbushe utafiti na uvumbuzi aliofanya Ivan Pavlov akitumia mbwa. Pavlov alifanya majaribio ambayo yalitoa mchango mkubwa katika taaluma ya saikolojia. Nashauri msomaji utafute taarifa za Pavlov na majaribio yake na uvumbuzi aliofanya. Huenda utakubaliana nami kuwa suala la kumpigia mbuzi gitaa si la kupuuzwa. Ni muhimu.

Sunday, May 21, 2017

"Contagious Success," Kitabu Muhimu

Nina furaha wakati huu kwa kuwa ninasoma kitabu kiitwacho Contagious Success: Spreading High Performance Throughout Your Organization. Nilinunua kitabu hiki siku chache zilizopita, kama nilivyoripoti katika blogu hii. Sikupoteza fedha zangu.

Mwandishi wa kitabu hiki, mwenyekiti wa Hudson Highland Center for High Performance, ni mwenye ujuzi na uzoefu mkubwa. Kitabu chake hiki ni matokeo ya utafiti ulioshirikisha watu wa sehemu mbali mbali ulimwenguni, ambao ni wafanyakazi katika sekta zinazotegemea na kuendeshwa na ujuzi na maarifa. Kwa ki-Ingereza, watu hao huitwa "knowledge workers." Hii ni dhana muhimu katika dunia ya leo na kesho, ambayo inaendelea kuwa dunia ya "knowledge economy."

Tangu mwanzo, kitabu hiki kina mafundisho muhimu kwa viongozi, mameneja, wamiliki wa biashara, watoa huduma na kadhalika. Ujumbe mahsusi ni namna ya kuyaeneza mafanikio katika shirika, kampuni, taasisi, au jamii. Mwandishi anasema: "Every company has high-performing workgroups that both make money for the business and develop new products, services, or markets. These work groups create environments in which results are achieved and people flourish."

Jambo muhimu kabisa ni kujenga mazingira ya kuwezesha ufanisi. Hata kama mtu ni hodari namna gani, hawezi kufanikiwa ipasavyo katika mazingira yasiyo muafaka. Mazingira ni msingi wa mafanikio, na ufanisi wa kikundikazi au vikundikazi unapata fursa ya kuenea katika kampuni au shirika zima.

Mwandishi ananukuu kauli za wataalam waliofafanua mawazo hayo: "According to Daniel Gilbert, Professor of psychology at Harvard University, 'Four decades of scientific research have shown that situations are powerful determinants of human behavior--and much more powerful determinants than most of us realize.'"

Baada ya maelezo, mwandishi analeta nukuu nyingine: "'Changing the situation and shaping the environment--that's what leadership is all about,' noted Linda Ginzel, clinical professor of managerial psychology at the University of Chicago Graduate School of Business."

Mwandishi anaelezea zaidi wazo hilo, na halafu analeta mawazo ya ziada. Kwanza, nyakati zimebadilika. Dunia ya leo si ile ya wakati mapinduzi ya viwanda ("Industrial Age") ambapo wafanyakazi walisimama katika mstari na uzalishaji wa bidhaa ulikuwa unatiririka kama mnyororo ("assembly line"). Wakati ule maamuzi ya namna kuendesha kiwanda yalikuwa mepesi na wazi kuliko sasa. Ushindani haukuwa mkubwa kama leo. Amri zilikuwa zinatoka juu kwa viongozi na kwenda chini, bila matatizo. Wafanya kazi waliwajibika kutii walichoambiwa. Hawakuhitaji kuwa wabunifu.

Leo mambo yamebadilika. Wafanyakazi hawatakiwi wawe watu wa kufuata tu maelekezo. Lazima watumie akili na ubunifu, kukabiliana na mazingira ya leo. Mazingira haya yanahitaji pia mabadiliko ya mtindo wa uongozi: "The strategies that worked in the Industrial Age are no longer effective. Leaders need to be honest about their own strengths and weaknesses. They must recognize that they can't be or do everything and, therefore, should make sure the people around them have complementary strengths."

Anaendelea kufafanua, kwa kunukuu kauli ya Carol Hymowitz katika Wall Street Journal:  "Arrogance is out of fashion in the executive suite. So are autocratic executives who rule by intimidation, think they have all the answers and don't believe they need to be accountable to anyone."

Kuhitimisha suala hili la uongozi mpya, mwandishi anasema kuwa uongozi ni lazima uwe unawathamini watu, unathamini ubunifu na uthubutu, na uwe mwepesi kuzitambua na kuzikamata fursa zinazojitokeza.

Nilivyokuwa ninasoma haya mawazo, nimejikuta nikiwazia Tanzania na malengo ya serikali ya kujenga nchi ya viwanda. Nimeona wazi kuwa ili tufanikiwe, lazima tujiweke sawa kwa mambo mengi, kama haya ya kuwathamini watu, kuweka mazingira muafaka na kuzingatia rasilimali watu, ambayo inakwenda sambamba na kuwapa watu uhuru wa kufikiri, kuwa wabunifu na watundu, hata kama kwa utundu wao wanaishia kufanya makosa. Watu wakiwa na uoga wa kufanya makosa, mafanikio yanaweza kuwa shida kupatikana.

Kitabu hiki cha Contagious Success nimekifurahia sio tu kwa sababu kinaelimisha sana, bali pia, kwa kiasi kikubwa, kwa sababu kimenikumbusha kitabu kingine, Leading Beyond the Walls, ambacho ninacho na nilikiongelea katika blogu hii.

Monday, January 30, 2017

Kitabu Nilichonunua Leo: "The Highly Paid Expert"

Leo nilikwenda Minneapolis na wakati wa kurudi, nilipita Mall of America, kuangalia vitabu katika duka la Barnes & Noble. Nilitaka hasa kuona kama kuna vitabu vipya juu ya mwandishi Ernest Hemingway.

Niliangalia scheme vinapowekwa vitabu vya fasihi, nikakuta kitabu kipya juu ya Ernest Hemingway, Everybody Behaves Badly: The Backstory to 'The Sun Also Rises.' kilichoandikwa na Lesley M.M. Blume. Kwa kuwa nimezama sana katika uandishi wa Hemingway, maisha na falsafa yake, na kwa kuwa nimeshasoma The Sun Also Rises, nilitamani kukinunua kitabu hiki, ambacho, kwa maelezo niliyoyaona, kinazungumzia yaliyo nyuma ya pazia.

Sikuwa na hela za kutosha, kwa hivyo nikaamua kuangalia vitabu vingine. Nilitumia muda zaidi katika sehemu ya "Business/Management." Huwa ninapenda sana kununua na kusoma vitabu vya taaluma hii, kwani vinanifundisha mengi kuhusu mambo ya ujasiriamali na biashara. Taaluma hii inanisaidia katika kuendesha shughuli za kampuni yangu ya Africonexion: Cultural Consultants.

Hatimaye, nilikiona kitabu kilichonivutia kwa namna ya pekee, The Highly Paid Expert, kilichoandikwa na Debbie Allen.  Kwa mujibu maelezo nyuma ya kitabu, huyu mwandishi ni mtaalam maarufu katika mambo ya biashara na ujasiriamali. Niliangalia ndani, nikaona mada anazoongelea ni za kuelimisha kabisa, kama vile matumizi ya tekinolojia za mawasiliano na mitandao.

Niliona anatoa ushauri wa kusisimua. Kwa mfano, anasema kuwa ni lazima mtu unayetaka mafanikio katika shughuli zako, uwasaidie wengine kufanikiwa. Unavyowasaidia wengine wafanikiwe, unajijengea mtandao wenye manufaa kwako pia. Ubinafsi na uchoyo wa maarifa haukuletei mafanikio. Kitabu hiki kinavutia kwa jinsi mwandishi anavyothibitisha mawazo yake, ambayo kijuu juu yanaonekana kama ya mtu anayeota ndoto.

Kwa bahati niliweza kuimudu gharama ya kitabu hiki, nikakinunua na kuondoka zangu, kwani nilikuwa sina hela iliyosalia. Sijutii kununua vitabu. Vitabu vinavyoelimisha ni mtaji, kwani hakuna mtaji muhimu zaidi ya elimu. Kwa wajasiriamali, wafanya biashara, watoa huduma, na kwa kila mtu, elimu ni tegemeo na nguzo muhimu. Ulazima wa kununua vitabu ni sawa na ilivyo lazima kwa mkulima kununua pembejeo.

Wednesday, March 23, 2016

Watu Wanaofanikiwa na Wale Wasiofanikiwa

Katika vitabu vinavyohusu mafanikio na maendeleo binafsi na pia kuinufaisha jamii, kuna mambo yanayoelezwa tena na tena. Mambo hayo tunaweza kuyaita mbinu au siri za mafanikio.

Picha nilizoweka hapa zinaorodhesha mambo hayo. Kwa upande mmoja kuna mambo wanayofanya watu wenye mafanikio au wanaotaka mafanikio. Ni mambo ambayo ni sehemu ya tabia ya watu hao.

Kwa upande wa pili, yanatajwa mambo wafanyayo watu wasio na mafanikio, au wasiofahamu njia au siri ya mafanikio. Hao ni watu wa kushindwa.

Mambo wanayofanya watu wenye mafanikio au wanaotaka mafanikio ni kama kusoma kila siku, kuwa wepesi wa kuyapokeo mabadiliko, wepesi wa kuwasamehe wenzao, wanaongelea fikra na mawazo, wanajifunza muda wote, ni wenye shukrani, wanajiwekea malengo na wanayatekeleza, wanawatakia wenzao mafanikio, wanayasifia mafanikio ya wenzao.

Watu wasio na mafanikio au wasiofahamu siri ya mafanikio ni wakosoaji wakubwa na walalamishi,  wanaogopa mabadiliko, wana visirani, wanawaongelea watu, wanajiona wajuaji, wanawalaumu wengine kwa lolote, wanadhani wanastahili kila watakacho, hawajiwekei malengo, hawakiri udhaifu wao au makosa yao, hawatambui mazuri ya wenzao, wanataka sifa hata wasipostahili, wanaangalia televisheni kila siku.

Katika kuyatafakari mambo hayo, nimeona wazi matatizo ya wa-Tanzania wengi. Wengi wamo katika hili kundi la wasiofanikiwa. Tabia ya kukaa vijiweni na kulumbana kuhusu vilabu vya mpira vya Ulaya, kuhusu vituko vya mastaa, kulalamikia hili au lile, ni tabia iliyoshamiri. Muda wanaokaa vijiweni wangeweza kuutumia kwa kusoma vitabu. Lakini huwaoni wakifanya hivyo, wala nyumbani, wala maktabani. Wasipofanikiwa, hawajitathmini na kutambua dosari zao, bali wanatafuta visingizio na wachawi.

Friday, June 19, 2015

Mteja Nimefurahia Huduma

Leo nilipeleka gari langu kwenye kituo cha Car Time hapa mjini Northfield kubadilishiwa "oil." Kwa hapa Marekani, inashauriwa kubadili "oil" kila baada ya kuendesha gari maili 3000. Sijui utaratibu wa Tanzania.

Kama ilivyo kawaida, nilipokewa vizuri, nikakaa sehemu ambapo wateja hungojea huduma. Baada ya dakika kama ishirini hivi, mtu aliyenipokea sehemu ya mapokezi alifika nilipokaa akachuchumaa kwa heshima zote na kuniambia kuwa mafundi walikuwa wamegundua kuwa gari langu linahitaji pia "tire rotation."

Kwa kuogopa kuwa labda ingekuwa gharama ambayo sikujiandaa kuimudu, nilimwuliza kwa utaratibu iwapo itakuwa gharama kiasi gani. Alinijibu kuwa hiyo "tire rotation" haitanigharimu. Nilimjibu kuwa nashukuru kwa huduma hiyo.

Dakika kama kumi tu baadaye. huyu jamaa aliiniita, kuniambia kuwa gari lilikuwa tayari. Alinikabidhi ufunguo na bili yangu, nikalipia, kisha nikashukuru na kuondoka zangu.

Huu ndio utamaduni niliouona hapa Marekani wa kuhudumia wateja. Nimewahi kuandika kuhusu huduma ya Car Time katika blogu hii,. Kila mahali nilipopita, hapa Marekani nimeona utamaduni huu wa kumjali mteja.

Sio mimi pekee mwenye uzoefu huo. Katika mahojiano yangu na Deus Gunza, m-Tanzania mwenzangu, tuliongelea suala hilo, tukakubaliana kuwa huu ndio utamaduni tunaouona hapa Marekani. Kwa upande wangu, nimejionea kuwa hata ukiingia baa, kama mhudumu yuko sehemu nyingine, ni kawaida kumwona meneja anakuja kwenye meza yako, kusafisha na kukuhudumia.

Katika baa za Tanzania, sijawahi kumwona meneja akifanya jambo kama hilo. Utamwona amekaa mahali anapiga gumzo na ulabu na marafiki zake, na akiona mteja umeingia na unangojea huduma, atakachofanya ni kuwaita wahudumu na kuwafokea kwa kukukalisha bila huduma. Sijawahi kumwona meneja akichukua kitambaa na kusafisha meza kwa ajili ya mteja na halafu kumletea kinywaji. Ni kama mwiko.

Kwa nini ninasimulia yote hayo? Ni kwa sababu nina nia ya dhati ya kuwasaidia wafanya biashara na watoa huduma wa Tanzania. Huduma bora kwa mteja ni msingi muhimu wa mafanikio. Hii imani kwamba mafanikio yanatokana na kwenda kwa mganga kusafisha nyota au kupata dawa ya mafanikio ni upuuzi.

Sijaona kampuni yoyote hapa Marekani inayoenda kwa waganga kutafuta dawa. Dawa muhimu ya uhakika ni kumridhisha au kumfurahisha mteja. Kama unauza bidhaa, uhakikishe bidhaa yako ni bora. Na kama biashara yako ni ya kutoa huduma, kama ile ushauri, uhakikishe huduma yako ni bora. Kwa vyovyote vile hakikisha mteja ameridhika au amefurahi. Huyu atakuwa mpiga debe wako. Ukimwudhi ataeneza habari kwa wengine na biashara yako itadhurika. Wataalam wanasema kuwa matangazo haya ya mdomo wanayofanya wateja ni msingi mkuu wa kufanikiwa au kuanguka kwa biashara.

Leo, niliporejea kutoka Car Time, nimemwelezea binti yangu Zawadi na mama watoto yote yaliyojiri, kwa furaha kubwa. Halafu jionee nilivyoandika hapa katika blogu. Nimekuwa mpiga debe wa Car Time bila wao kunilipa. Na ndivyo ilivyo katika maisha yetu. Utamsikia m-Tanzania anaisifia simu yake mpya ya "iPhone" au "smartphone" au "laptop" yake au kitu kingine, bila kutambua kuwa anaipigia debe kampuni ambayo haimlipi chochote, haimjui na wala haichangii uchumi wa Tanzania bali inajitajirisha. Tuna uwezo mkubwa sisi wateja. Laiti tungeutumia kuzitangaza bidhaa na huduma za ki-Tanzania.

Nimejifunza mengi katika kuishi hapa Marekani. Hili nililolieleza ni jambo moja. Ni elimu ambayo ninaitumia katika kuendeleza kampuni yangu ya ushauri ya Africonexion. Ninazingatia sana umuhimu wa kutoa huduma bora, kama nilivyowahi kuandika katika blogu hii.

Thursday, May 21, 2015

Kusonga Mbele na Kutoyumbishwa

Naandika makala hii kuwapa moyo wengine, hasa vijana, wanaojituma kujiendeleza katika fani yoyote na kimaisha kwa ujumla. Kwa ujumla, mawaidha haya yanapatikana vitabuni.

Katika vitabu vinavyoelezea mikakati ya mafanikio, kitu kimoja kinachosisitizwa ni kutambua kwamba unaposonga mbele, kuna watu watakaokuandama kwa mategemeo ya kukukatisha tamaa na kukurudisha nyuma. Watabeza shughuli zako na mafanikio yako.

Kwa mujibu wa vitabu hivyo, hao ni watu wa kuwapuuza. Ni muhimu pia kuwapuuza wale wasio na mtazamo wa maendeleo yao wenyewe. Badala ya kupoteza muda kuwa na watu wa namna hiyo, andamana na watu waliomo katika njia ya mafanikio, au waliofanikiwa. Utajifunza kutoka kwao.

Watu wenye mafanikio, wanajiamini, na hawaoni shida kuwashauri au kuwasaidia wengine nao wafanikiwe. Napenda kunukuu maneno ya Henry Rogers mtu maarufu aliyeanzisha na kuendesha Rogers & Cowan, kampuni ya mahusiano ya jamii:

Not only is it essential to make someone feel important, the art of psychorelations demands that we also make the person feel at ease. As I reflect back on my life, I find that powerful and important people have always made an effort to make me feel comfortable. My experience has been that the more important they are, the more gracious they are. Could it be that their ability to reach out graciously to others has helped make them important? I believe so. (Henry C. Rogers, Rogers' Rules for Success, uk. 44.)

Sijui kama wewe ni mmoja wa hao wanaobeza au wanaohimiza juhudi na mafanikio ya wenzao. Siku chache tu zilizopita, nilisoma kauli za Wema Sepetu, dada m-Tanzania maarufu katika maigizo ya filamu. Alielezea jinsi watu wanavyombeza, kumtukana, na kufanya kila juhudi ya kumkatisha tamaa, hadi amewahi kufikiria kuwa hakuna sababu ya kuendelea kuishi.

Ni ushuhuda ambao ulinigusa sana. Ni ukweli usiopingika kwamba wako wa-Tanzania wengi wa ovyo kama ilivyoelezwa hapa juu. Hata mimi wananiandama kwa kejeli na mabezo humo mitandaoni, lakini hawajitambulishi. Kwa mfano, nimekumbana na watu wanaokibeza kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences ambacho kinapendwa na kutumiwa sana, hasa hapa Marekani, na ni msingi mojawapo wa mialiko ya mara kwa mara ya kwenda kutoa mihadhara, kama inavyoonekana pichani hapo juu, katika Chuo cha South Central, Minnesota.

Lakini, utakuta mtu anajitokeza na kutoa kauli ya kubeza bila maelezo wala ushahidi, ili mradi amerusha maneno yanayoweza kukatisha tamaa. Wala hatoi ushauri muafaka, kama anaona mapungufu, ili kuisaidia jamii. Ukitaka mfano, soma ujumbe huu. Kuna wakati hao waropokaji niliamua kuwapa vidonge vyao, kama tunavyosema, kwa kuwaambia waandike vitabu vyao, tuone.

Kwa upande wangu, watu wa namna hiyo wanajisumbua bure. Wanapoteza muda ambao wangeutumia kujiendeleza kwa kusoma. Bora hata wangenitafuta niwape mawazo na uzoefu kama wanavyonitafuta wa-Marekani. Ninawaheshimu wa-Marekani kwa hilo. Ni wasikivu wanapoelezwa mambo wasioyafahamu, kama haya ninayowalezea kuhusu athari za tofauti za tamaduni katika dunia ya utandawazi wa leo. Ni watu wanaotaka mafanikio katika ulimwengu huu.

Hao watu aliowaongelea Wema Sepetu na ambao nami ninawaongelea, nawaonea huruma. Labda siku itafika watakapoanza kuwa na mtazamo mpya. Binafsi nina furaha maishani kwa kuwa ninazingatia malengo niliyojiwekea, na mafanikio ninayaona, hasa katika kuwagusa watu na kuwaneemesha. Nimeshasema kabla kuwa lengo langu kuu ni hilo, sio utajiri wa fedha.

Sunday, December 21, 2014

Kitabu Kingine: "A Goal is a Dream With a Deadline"

Usiku wa kuamkia leo, nimemaliza kusoma kitabu kiitwacho A Goal is a Dream With a Deadline, ambacho nilikinunua siku za karibuni. Mwandishi wake, Leo B. Helzel, amekusanya kauli za watu mbali mbali wenye ujuzi na uzoefu, ili kuwaelimisha wajasiriamali, mameneja, na watu werevu kwa ujumla, wenye mitazamo ya kimaendeleo.

Kitabu hiki ni tofauti na vingine kwani ni mkusanyo wa misemo ya busara kuhusu mambo kama kujiwekea malengo, kustahimili matatizo, kutafuta masoko au wateja, kujiwekea maamuzi na kuyatekeleza kwa dhati na bila kuchelewa, kuwasikiliza wateja kwa makini na kuwahudumia vizuri, kuzingatia ubunifu, kupunguza urasimu, na kujiamini. Hayo ni baadhi ya yaliyomo katika kitabu hiki.

Sura zote za kitabu hiki zina mambo muhimu. Kwa vile mimi ninashughulika na kutoa ushauri kwa jumuia, taasisi, makampuni, na watu binafsi kuhusu tofauti za tamaduni na athari zake, nimevutiwa sana na sura ya kitabu hiki iitwayo "Going Global." Baadhi ya mawaidha yaliyomo katika sura hii ni haya: "Never assume that business is conducted in a foreign country just as it is at home" (uk. 146), "Learn about your host's people by reading about their history and culture" (uk. 147), " "Always assume that time will be handled differently in a foreign country" (uk. 147), "Latin Americans may refuse to do business with you if you are too serious. So lighten up and slow down" (uk. 151), "In Asia, learn when "maybe" really means "no" (uk. 151).

Mawaidha haya yanafanana na yale ninayotoa na kuyafafanua katika mihadhara na warsha zangu. Yamo katika kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, na pia mara moja moja katika blogu hii.

Nimejifunza mambo kadhaa muhimu katika kusoma A Goal is a Dream With a Deadline, na nakipendekeza kwa yeyote anayetaka mabadiliko yenye manufaa katika fikra, shughuli, maisha yake na ya jamii.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...