Thursday, May 21, 2015

Kusonga Mbele na Kutoyumbishwa

Naandika makala hii kuwapa moyo wengine, hasa vijana, wanaojituma kujiendeleza katika fani yoyote na kimaisha kwa ujumla. Kwa ujumla, mawaidha haya yanapatikana vitabuni.

Katika vitabu vinavyoelezea mikakati ya mafanikio, kitu kimoja kinachosisitizwa ni kutambua kwamba unaposonga mbele, kuna watu watakaokuandama kwa mategemeo ya kukukatisha tamaa na kukurudisha nyuma. Watabeza shughuli zako na mafanikio yako.

Kwa mujibu wa vitabu hivyo, hao ni watu wa kuwapuuza. Ni muhimu pia kuwapuuza wale wasio na mtazamo wa maendeleo yao wenyewe. Badala ya kupoteza muda kuwa na watu wa namna hiyo, andamana na watu waliomo katika njia ya mafanikio, au waliofanikiwa. Utajifunza kutoka kwao.

Watu wenye mafanikio, wanajiamini, na hawaoni shida kuwashauri au kuwasaidia wengine nao wafanikiwe. Napenda kunukuu maneno ya Henry Rogers mtu maarufu aliyeanzisha na kuendesha Rogers & Cowan, kampuni ya mahusiano ya jamii:

Not only is it essential to make someone feel important, the art of psychorelations demands that we also make the person feel at ease. As I reflect back on my life, I find that powerful and important people have always made an effort to make me feel comfortable. My experience has been that the more important they are, the more gracious they are. Could it be that their ability to reach out graciously to others has helped make them important? I believe so. (Henry C. Rogers, Rogers' Rules for Success, uk. 44.)

Sijui kama wewe ni mmoja wa hao wanaobeza au wanaohimiza juhudi na mafanikio ya wenzao. Siku chache tu zilizopita, nilisoma kauli za Wema Sepetu, dada m-Tanzania maarufu katika maigizo ya filamu. Alielezea jinsi watu wanavyombeza, kumtukana, na kufanya kila juhudi ya kumkatisha tamaa, hadi amewahi kufikiria kuwa hakuna sababu ya kuendelea kuishi.

Ni ushuhuda ambao ulinigusa sana. Ni ukweli usiopingika kwamba wako wa-Tanzania wengi wa ovyo kama ilivyoelezwa hapa juu. Hata mimi wananiandama kwa kejeli na mabezo humo mitandaoni, lakini hawajitambulishi. Kwa mfano, nimekumbana na watu wanaokibeza kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences ambacho kinapendwa na kutumiwa sana, hasa hapa Marekani, na ni msingi mojawapo wa mialiko ya mara kwa mara ya kwenda kutoa mihadhara, kama inavyoonekana pichani hapo juu, katika Chuo cha South Central, Minnesota.

Lakini, utakuta mtu anajitokeza na kutoa kauli ya kubeza bila maelezo wala ushahidi, ili mradi amerusha maneno yanayoweza kukatisha tamaa. Wala hatoi ushauri muafaka, kama anaona mapungufu, ili kuisaidia jamii. Ukitaka mfano, soma ujumbe huu. Kuna wakati hao waropokaji niliamua kuwapa vidonge vyao, kama tunavyosema, kwa kuwaambia waandike vitabu vyao, tuone.

Kwa upande wangu, watu wa namna hiyo wanajisumbua bure. Wanapoteza muda ambao wangeutumia kujiendeleza kwa kusoma. Bora hata wangenitafuta niwape mawazo na uzoefu kama wanavyonitafuta wa-Marekani. Ninawaheshimu wa-Marekani kwa hilo. Ni wasikivu wanapoelezwa mambo wasioyafahamu, kama haya ninayowalezea kuhusu athari za tofauti za tamaduni katika dunia ya utandawazi wa leo. Ni watu wanaotaka mafanikio katika ulimwengu huu.

Hao watu aliowaongelea Wema Sepetu na ambao nami ninawaongelea, nawaonea huruma. Labda siku itafika watakapoanza kuwa na mtazamo mpya. Binafsi nina furaha maishani kwa kuwa ninazingatia malengo niliyojiwekea, na mafanikio ninayaona, hasa katika kuwagusa watu na kuwaneemesha. Nimeshasema kabla kuwa lengo langu kuu ni hilo, sio utajiri wa fedha.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...