Saturday, May 16, 2015

Vitabu Nilivyonunua Karibuni

Napenda kujiwekea hapa kumbukumbu za vitabu nilivyonunua katika siku chache zilizopita. Ni faraja kuweza kupita tena katika maduka ya vitabu, baada ya miezi ya kuwa katika hali ngumu kiafya.

Yapata wiki moja iliyopita,  katika duka la vitabu la hapa Chuoni St. Olaf, ambamo daima kunakuwa na vitabu vingi ambavyo sijawahi kuviona, niliguswa kukiona kitabu cha Terry Eagleton, How to Read Literature, ambacho nilikuwa sijawahi hata kukisikia.
Terry Eagleton ni mwananadharia wa fasihi ambaye ni maarufu kabisa. Nilinunua vitabu vyake kadhaa na kuvisoma miaka ya 1980-86 nilipokuwa masomoni Chuo Kikuu Cha Wisconsin Madison. Nimeanza kusoma na kuvutiwa na How to Read Literature.

Juzi tarehe 14, wakati narudi kutoka Columbia Heights, nilipitia Apple Valley, nikaingia katika duka la vitabu la Half Price Books ambalo nimelitaja mara nyingi katika blogu hii. Nilinunua vitabu vitatu.

Kimoja ni Without a Name and Under the Tongue. Hizi ni riwaya mbili ambazo zimechapishwa katika hiki kitabu kimoja. Mtunzi ni Yvonne Vera wa Zimbabwe, ambaye ni kati ya waandishi wa kizazi kipya wa Zimbabwe. Nilishafundisha riwaya yake Butterfly Burning, na nilivyokiona kitabu chake hiyo juzi, nilifikiwa na hamu ya kusoma zaidi uandishi wake, nisikie tena sauti ya mwandishi anayeandika kuhusu nchi ya karibu na nyumbani Tanzania.

Kitabu kingine nilichonunua, Bluest Eye/Sula/Song of Solomon nacho kimejumlisha vitabu vitatu vya Toni Morrison. Ninahisi ninavyo vitabu hivi, ila sina hakika, kwani nina vitabu vingi sana. Toni Morrison ni mwandishi mmojawapo maarufu kabisa duniani. Alipata tuzo ya Nobel. Nina kitabu chake Playing in the Dark, ambacho kina fikra pevu kuhusu athari za utamaduni na fasihi ya wa-Marekani Weusi katika historia ya fasihi ya Marekani.

Kitabu cha tatu nilichonunua ni Great Expectations, cha Charles Dickens. Ninacho kitabu hiki, pamoja na vingine vya mwandishi huyu maarufu. Lakini hii haikunizuia kununua nakala nyingine. Labda, huko mbele ya safari, nitaweza kukijumlisha katika vitabu ambavyo nimekuwa nikitoa kwa vyuo, taasisi, na watu binafsi Tanzania.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...