Tuesday, December 25, 2012

Milima Haikutani

Wa-Swahili husema, milima haikutani bali binadamu hukutana. Hayo yalinipata mjini Karatu mwaka 2008 nilipokutana na mzee ambaye anaonekana nami pichani.

Siku hiyo ilikuwa siku ya mnada mjini Karatu, siku ambayo hutokea mara moja kwa mwezi. Katika umati mkubwa wa watu, yeye na mimi tulijikuta uso kwa uso. Yeye alinitambua mara moja, akauliza: "Profesa Mbele?" Nilimwambia ndio mimi. Tulifurahi sana, tukaanza michapo.

Mzee huyu nilimfahamu mwaka 1996 wakati nafanya utafiti wa masimulizi ya jadi kuhusu shujaa wa wa-Iraqw aitwaye Saygilo Magena. Utafiti huu ulinipeleka kwenye miji na vijijini kama vile Mbulu, Mamaisara, na Karatu.

Kati ya watu walionisaidia sana ni huyu mzee ambaye jina lake ni John Qamlali. Baada ya kufahamiana kule Mbulu, tulikutana tena mjini Arusha, tukaongea sana. Anajua sana habari za wa-Iraqw na ameshawasaidia watafiti wengine wa mataifa mbali mbali. Ninazo kanda za maongezi yetu.

Kukutana tena mwaka 2008, miaka zaidi ya kumi tangu tulipokutana mara ya kwanza, ilikuwa ni ajabu na pia jambo la kushukuru.

Maaskofu Watoa Tamko Juu Ya Masuala Mbali Mbali

TANZANIA CHRISTIAN FORUM (TCF) MKUTANO MKUU WA NNE WA JUKWAA LA WAKRISTO TANZANIA (TCF)

TAMKO RASMI “ATUKUZWE MUNGU JUU MBINGUNI, NA DUNIANI IWE AMANI KWA WATU ALIOWARIDHIA”

Utangulizi Katika Mkutano Mkuu wa Nne wa Jukwaa la Wakristo Tanzania, Tanzania Christian Forum – TCF, uliofanyika katika Kituo cha Mikutano na Mafunzo cha Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) Kurasini jijini Dar es Salaam, tarehe 6 Desemba, 2012; Wajumbe walitafakari kwa undani juu ya kuzorota kwa mahusiano baina ya Dini mbili za Ukristo na Uislamu nchini Tanzania, pamoja na kutathmini juu ya wajibu wa Kanisa na Utume wake wa Kinabii kwa taifa letu.

Jukwaa la Wakristo Tanzania (TCF) linajumuisha taasisi kuu za Umoja wa Makanisa nchini kama ifuatavyo;- Jumuiya ya Kikristo Tanzania - CCT Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania - TEC Jumuiya ya Makanisa ya Kipentekoste Tanzania - PCT Kanisa la Waadventisti Wasabato – SDA (observers)

Tafakari Tafakari yetu ilianza kwa kujiuliza yafuatayo:

1. Ni mwenendo gani uliotusibu hivi karibuni kusababisha kukutana kwetu hapa? Vikundi vya kihalifu vikiongozwa chini ya mwavuli wa waamini wa Kiislamu vimekuwa vikishambulia kwa ukali na kikatili sana imani, mali, majengo na makanisa ya Wakristo kwa jeuri na kujiamini.

2. Kwa mwenendo huo ni kitu gani kilicho hatarini? Vitendo na mienendo yote ya namna hiyo inahujumu sana Amani, Mapatano na Uelewano kati ya watu wote nchini mwetu. Tunaelewa kwamba ni waamini wachache tu wenye kutenda maovu hayo, lakini mienendo ya kikatili ya namna hii huchochea shari miongoni mwa walengwa wa ukatili husika na kutaka kulipiza kisasi hata kusababisha uvunjifu wa amani.

3. Ni athari gani kwa nchi, katika muda ujao, iwapo mienendo hiyo haitadhibitiwa na kukomeshwa kabisa?

Katika nyakati zetu hizi, tunashuhudia fadhaa na migogoro mingi ya kijamii. Kuna hasira kubwa ya chinichini inayotokana na kasoro nyingi za kiutendaji katika mihimili mikuu ya uongozi na utando mkubwa wa ufukara wa kutupwa kwa wananchi wengi usio na matumaini ya kumalizika hivi karibuni. Hatari ya hali hii ni dhahiri kwamba makundi nyemelezi (kisiasa, kiuchumi na kidini), kwa kutumia vikundi halifu vilivyo katika hali ya ufukara na migogoro, yatavielekeza kimapambano na kiharakati kutetea kijeuri ajenda hasimu za wale walio madarakani au washindani wao kwa maslahi ya wanyemelezi. Hali tunayoelezea sio ya kufikirika kwani ndiyo inayotokea huko nchini Nigeria, Kenya na nchi za Afrika ya Kaskazini hivi sasa. Tanzania haina kinga ya kipekee kuiepusha kukumbwa na maovu ya namna hiyo bila utaratibu na vyombo thabiti kuhimili mienendo hasi kama hii. Kutokana na matukio na kauli zinazotolewa na watu mbalimbali hapa nchini, inawezekana tayari wanyemelezi wako kazini wakiongoza vikundi kusukuma ajenda za kutekeleza maslahi yao.

4. Masuala yanayotakiwa kufafanuliwa na kudhibitiwa na Dola mapema ili yasiendelee kupotoshwa:

Hali ya mahusiano kuzorota pamoja na kashfa dhidi ya Kanisa.

Huu ni wakati wa kukubali kwamba misingi ya Haki, Amani na Upendo katika Taifa letu imetikiswa kwa kiwango kikubwa. Uchochezi, kashfa, matusi na uchokozi wa wazi na makusudi unaofanywa na baadhi ya waamini wa dini ya Kiislamu, ukiendeshwa na kuenezwa kupitia vyombo vyao vya habari vya kidini (redio na magazeti) mihadhara, kanda za video, CD, DVD, vipeperushi, makongamano, machapisho mbalimbali na kauli za wazi za viongozi wa siasa na hata viongozi wa dini husika (ushahidi wa mambo yote haya tunao) pasipo Serikali kuchukua hatua yeyote huku bali imekuwa ikibakia kimya tu. Ukimya huu unatoa taswira ya Serikali kuunga mkono chokochoko hizi. Jambo hili linavyoendelea kuachwa hivi hivi linaashiria hatari kubwa ya kimahusiano siku zijazo.

Hadhi ya Baba wa Taifa kuhifadhiwa.

Huyu ni kiongozi aliyetoa maisha yake kwa ajili ya ustawi wa nchi yetu akitetea Watanzania wote bila ubaguzi wowote, akiimarisha umoja wa Kitaifa, amani na upendo kwa watu wote. Kashfa, kejeli na habari za uongo dhidi yake ni kukipotosha kizazi hiki na hata vizazi vijavyo kwa kuondoa moja ya alama muhimu ambazo kiongozi huyo alisimamia kwa ajili ya umoja wa kitaifa.

“Memorandum of Understanding” (M.o.U) ya mwaka 1992, kwa ajili ya huduma za kijamii zitolewazo na Makanisa kwa Watanzania wote, ikiwa ni pamoja na huduma za hospitali, vituo vya afya na zahanati na shule mbalimbali zinazoendeshwa na Makanisa nchini kote. Ni vema ikaeleweka wazi kwamba makubaliano hayo (M.o.U) yalikuwa ni kati ya Makanisa ya Tanzania na Makanisa ya nchini Ujerumani ambapo Serikali ya Tanzania ilihusishwa tu, kwa vile raia wake ndio wangenufaika na misaada hiyo ambayo nchi ya Ujerumani ingeitoa kupitia Makanisa hayo. Kanisa limeendelea kujishughulisha na huduma hizi kwa jamii hata kabla ya uhuru na baada ya uhuru pasipo ubaguzi. Ikibidi ni vema kuondoa hali hii, ya Kanisa kuendelea kutukanwa, chuki na kukashifiwa viongozi wake kutokana na huduma hizi kwa jamii yote. Jukwaa la Wakristo Tanzania tunaitaka Serikali itoe tamko la ufafanuzi juu ya M.o.U hiyo, maana yake, makusudi yake na manufaa yake kwa Watanzania wote.

Hujuma ya kuchomwa Makanisa na mali za Kanisa, ni tukio la uvamizi na uchokozi wa wazi, ulioyakuta makanisa yetu na waamini wake wakiwa hawana habari na bila maandalizi yoyote. Ni muhimu kuanzia sasa, Wakristo wote wakae macho na wawe waangalifu zaidi.

Dhana ya kuwa Tanzania inaendeshwa kwa mfumo Kristo ni potofu na potevu.

Maneno hayo ni ushahidi wa uwepo wa ajenda za waamini wenye imani kali na waliojiandaa kwa mapambano maovu kutetea dhana potovu kinzani na misingi ya demokrasia na haki za binadamu kama ilivyotangazwa na Umoja wa Mataifa na kuridhiwa na Serikali yetu. Jukwaa la Wakristo nchini tunakanusha wazi wazi na kueleza bayana kuwa, nchi hii haiongozwi kwa mfumo Kristo!. Kwa watu walio makini hakuna kificho kuwa viongozi wote waandamizi wa ngazi ya juu Serikalini awamu ya sasa, asilimia 90 ni Waislamu (Rais wa Nchi na Amiri Jeshi Mkuu, Makamu wa Rais, Mkuu wa Usalama wa Taifa, Jaji Mkuu, Mkuu wa Jeshi la Polisi). Kwa mantiki hiyo haiingii akilini kueleza watu kuwa nchi hii inaendeshwa kwa mfumo Kristo! Kwa upande wa Zanzibar asilimia 100 ya viongozi ngazi za juu Serikalini ni Waislamu, na sio kweli kwamba Zanzibar hakuna Wakristo wenye sifa za kuongoza. Kisha, hata uwakilishi wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, theluthi mbili ya wajumbe wake ni Waislamu. Tunayo mifano mingine mingi iliyo wazi, na hii ni baadhi tu. Watanzania wanapaswa kuelewa wazi kuwa, nchi hii inaongozwa kwa misingi ya Utawala wa Kisheria na sio vinginevyo.

Matumizi hasi ya Vyombo vya Habari vya Kidini:

Vyombo vya habari vya kidini vinatumiwa na viongozi wa dini ya Kiislam kuukashifu Ukristo na kuwachochea Waislamu hadharani kupitia vyombo hivyo wakiwataka wawaue Maaskofu na Wachungaji, iwe kwa siri au hadharani. Japo Serikali imesikia kashfa na uchochezi huo hatarishi, imendelea kukaa kimya, na kuwaacha wachochezi hao wakiendelea kuhatarisha amani bila kuwadhibiti. Jambo hili linatia mashaka makubwa juu ya umakini wa Dola kuhusu usalama wa wananchi nchini mwao. Imani kali za namna hii huchochea vitendo viovu vya uasi na hujuma sio tu dhidi ya waamini na viongozi wa dini fulani, bali hata na kwa Serikali na viongozi waliopo madarakani, endapo waamini wa dini fulani katika taifa kama Tanzania lililo na waamini wa dini nyingi tofauti, hawataheshimu na kutendeana kiungwana baina yao na wale wasio wa dini na mapokeo yao. Hali hii inapelekea kujiuliza kama je,huu ni wakati mwafaka kwa kila raia au kiongozi wa dini kujilinda yeye mwenyewe na waamini wake dhidi ya wenye imani kali?

Matukio yanayosababisha hasira na kutenda maovu:

Tumejionea matukio kadhaa ambayo kwayo vikundi vya watu wenye hasira vilisababisha hujuma na uharibifu mkubwa wa mali za watu wengine. Hivyo ni viashiria tosha vya uchovu na unyonge mkubwa katika jamii yetu, ambamo jambo dogo tu na hata la kupuuzwa, likitendwa na afikiriwaye kuwa hasimu wa watu fulani, wahalifu hujipatia fursa ya kuonesha hasira yao kwa vitendo vya hujuma na shari, wakiharibu hata kuteketeza mali na nyenzo za maisha ya jamii. Suala hili lataka uchambuzi yakinifu na wa kiroho ili kupata majibu na maelezo sahihi na wala sio kwa kutumia nguvu za ziada za kijeshi au kwa majibu mepesi ya kisiasa. Hili ni suala lihusulo tunu na maadili ya jamii yote ya Watanzania katika ujumla wao. Kila mmoja wetu ni mhusika na sote tukitakiwa kuwajibikiana katika ujenzi wa amani iletayo mapatano na uelewano kati yetu.

Mapendekezo: Kutokana na muono wetu huo tunapendekeza yafuatayo:

Tabia na mienendo ya kukashifiana ikomeshwe kabisa na badala yake tujengeane heshima/staha tukizingatia utu wa kila mmoja katika utofauti wetu.

Tumwendee Mungu wetu na kumwomba atuongoze sote kufuata utashi wake tukitafuta huruma yake iliyo sheheni upendo wake mkuu, ili atujalie umoja wa kuishi pamoja kwa amani nchini mwetu.

Tunaitaka Serikali yetu na vyombo vyake vya usalama, sheria na amani kutenda mara moja na bila kuchelewa, katika nyakati ambazo vikundi halifu kisiasa au kidini vinapoanza uchochezi ili kupambanisha wanajamii. Tabia ya kuachia uchochezi wa kidini kuendelea pasipo hatua mathubuti kuchukuliwa na Dola ni udhaifu mkubwa wa uongozi na uwajibikaji. Ikithibitika kwamba uharibifu uliofanywa ulitokana na kikundi mahususi chini ya uongozi wa dini au chama cha kisiasa au asasi isiyo ya kiserikali, basi taasisi husika iwajibishwe na kulipa fidia kwa uharibifu uliofanywa.

Lianzishwe Baraza mahsusi lililo huru lisiloegemea chama chochote cha kisiasa wala dini yoyote na litamkwe na kuwezeshwa kikatiba likiwa na dhumuni kuu la kuilinda na kuiongoza Serikali kuto fungamana na dini yoyote na kuhakikisha kwamba dira na dhana ya utu katika mfumo wa uchumi wenye kujali maslahi ya wote havipotoshwi. Baraza hilo liwe na uwezo wa kuvichunguza vyombo vya sheria na usalama itokeapo matatizo makubwa yaashiriayo uvunjifu wa haki na kuteteresha usalama wa nchi.

Na sisi viongozi wa dini za Kikristo, Kiislam, Kihindu na nyinginezo tuwajibike katika kufundisha, na katika majiundo ya waamini wetu, hasa vijana, ili kuwajengea uelewa na utashi wa kuvumiliana kwa upendo. Katika kushuhudia na kuadhimisha imani na ibada zetu sote tutambue , tulinde na kukuza maadili, tunu na desturi za imani za watu wengine wanazo ziheshimu na kuzitukuza. Vikundi vya imani kali na pambanishi kwa kutumia kashfa potoshaji sharti vidhibitiwe kwa weledi mkubwa wa viongozi wa dini husika wakisaidiana na usalama wa taifa. Stahamala [kustahimiliana] ni fadhila inayopaswa kufundishwa na kupenyezwa katika mifumo ya uongozi na maisha ya jamii na ihifadhiwe kwa kufuatiliwa kwa karibu sana.

Hitimisho: Kwa sasa Kanisa liko katika vita vya Kiroho, hivyo ni vyema Waamini wote wakakumbuka kuwa, katika mapambano kama hayo Mungu mwenyewe, Mwenye enzi yote ndiye mlinzi wa watu wake na Kanisa lake. JIBU LITAPATIKANA TU, KWA NJIA YA SALA, KUFUNGA NA MAOMBI!

Hivyo siku ya Jumanne tarehe 25 Desemba 2012, inatangazwa rasmi nchini kote kuwa siku ya sala na maombi kwa Wakristo wote na Makanisa yote nchini, pamoja na watu wote wenye mapenzi mema, kuomba kwa imani, amani katika nchi yetu, na kumkabidhi Mungu ashughulikie mipango yoyote iliyopo, ya wazi na ya kisirisiri ya kutaka kuondoa amani ya taifa hili na kuyashambulia Makanisa nchini Tanzania ishindwe na kuanguka pamoja na wale wote walio nyuma ya mipango hiyo.

1. Askofu Bruno Ngonyani (TEC) - Mwenyekiti
2. Askofu Dkt. Israel Mwakyolile (CCT) - Mjumbe (Mwenyekiti Mwenza)
3. Askofu Daniel Aweti (PCT) - Mjumbe (Mwenyekiti Mwenza)
4. Askofu Oscar Mnung’a (CCT) - Mjumbe
5. Askofu Elisa Buberwa (CCT) - Mjumbe
6. Askofu Stephen Mang’ana (CCT) - Mjumbe
7. Askofu Dkt. Peter Kitula (CCT) - Mjumbe
8. Askofu Alinikisa Felick Cheyo (CCT) - Mjumbe
9. Askofu Christopher Ndege (CCT) - Mjumbe
10. Askofu Michael Hafidh (CCT) - Mjumbe
11. Askofu Charles Salala (CCT) - Mjumbe
12. Askofu Dismus Mofulu (CCT) - Mjumbe
13. Mchg. Conrad Nguvumali (CCT) - Mjumbe
14. Mchg. Ernest Sumisumi (CCT) - Mjumbe
15. Mchg. William Kopwe (CCT) - Mjumbe
16. Askofu Thaddaeus Ruwa’ichi (TEC) - Mjumbe
17. Askofu Paul Ruzoka (TEC) - Mjumbe
18. Askofu Norbert Mtega (TEC) - Mjumbe
19. Askofu Severine Niwemugizi (TEC) - Mjumbe
20. Askofu Michael Msonganzila (TEC) - Mjumbe
21. Askofu Castorl Msemwa (TEC) - Mjumbe
22. Askofu Eusebius Nzigilwa (TEC) - Mjumbe
23. Askofu Renatus Nkwande (TEC) - Mjumbe
24. Askofu Bruno Ngonyani (TEC) - Mjumbe
25. Fr. Antony Makunde (TEC) - Mjumbe
26. Fr. Sieggried Rusimbya (TEC) - Mjumbe
27. Fr. Ubaldus Kidavuri (TEC) - Mjumbe
28. Askofu Dkt. Paul Shemsanga (PCT) - Mjumbe
29. Askofu Ability Samas Emmanuel (PCT) - Mjumbe
30. Askofu Nkumbu Nazareth Mwalyego (PCT) - Mjumbe
31. Askofu Batholomew Sheggah (PCT) - Mjumbe
32. Askofu Dkt. Mgullu Kilimba (PCT) - Mjumbe
33. Askofu Renatus Tondogosso (PCT) - Mjumbe
34. Askofu Emmanuel Mhina (PCT) - Mjumbe
35. Askofu O.S. Sissy (PCT) - Mjumbe
36. Askofu Jackson Kabuga (PCT) - Mjumbe


CHANZO: Mjengwa Blog

Monday, December 24, 2012

Shaaban Robert na Nyerere: Waandishi Muhimu kwa Kila m-Tanzania

Kwa miaka michache iliyopita, wakati nimejitosa katika kusoma maandishi ya Shaaban Robert, nimejiwa na mawazo mbali mbali ambayo naona ni muhimu. Kwa bahati nzuri, nimechapisha makala mbili juu ya Shaaban Robert, moja katika Encyclopedia of African Literature, na nyingine katika CHANGAMOTO: Insha za Jamii.

Napenda kunukuu machache niliyoandika katika Encyclopedia of African Literature:

Shaaban Robert displayed profound awareness of the human condition; he opposed injustice, championed freedom, and extolled the dignity of labour. He was sensitive to the condition of women. He wrote poems celebrating women, and a biography of Siti Binti Saad, the famous female taarab singer, recounting the meteoric rise to fame of this woman from a humble rural background in a male-dominated world which put incredible obstacles in her path. He was proud of his Swahili language and culture, which he understood very well, appropriated, and celebrated in and through his writings. However, he deeply respected other languages and cultures and appropriated whatever he could from them. If colonialism had not limited his educational opportunities, he would have explored this dimension to the fullest. He greatly admired world writers like Shakespeare, whose artistic mind he described as a great ocean whose waves touched the shores of the whole world....[Shaaban] Robert's poetic sensibility was deep and intertwined with his moral and ethical principles. Sensitive to the condition and plight of all creatures, he held that all things moved with the rhythm of poetry: the birds, streams, the sea, the wind and the thunderstorms, the seasons....His vision of a just society was part of the shaping of the dream for an egalitarian society, which became his country's policy. (p. 463)

Katika kusoma na kutafakari maandishi ya Shaaban Robert, ilifikia wakati nikajenga wazo kuwa kuna uwiano mzito baina ya mafundisho ya Shaaban Robert na yale ya Mwalimu Nyerere. Wakati Nyerere anaongelea sana masuala ya siasa, uchumi, nadharia mbali mbali kuhusu jamii na maendeleo yake, Shaaban Robert aliongelea masuala ya aina hiyo hiyo kwa kutuingiza katika hisia na mahusiano baina ya binadamu na binadamu mwenzake.

Kama Nyerere, Shaaban Robert alikuwa mchambuzi wa jamii na mwanafalsafa, lakini aliongelea masuala kwa kutumia wahusika maalum na matendo na masahibu yao, na hivi kutugusa moja kwa moja. Ningekuwa na madaraka ya kuamua masuala ya mfumo wa elimu Tanzania, ningehakikisha kuwa Shaaban Robert na Nyerere wamekuwa nguzo ya elimu ya kila m-Tanzania.

Friday, December 21, 2012

Habari Njema: Kitabu cha "Hemingway and Africa" Kimefika

Leo nina furaha sana. Kisa? Kitabu nilichoagiza, Hemingway and Africa, kimefika leo.

Kila ninapojipatia kitabu kipya ninafurahi. Ukizingatia kuwa hadi sasa nina vitabu zaidi ya elfu tatu, utaona kuwa nimekuwa mwenye furaha, tena na tena. Huenda nitaishi miaka kadhaa ya ziada kutokana na hiyo furaha.

Pamoja na hayo yote, hiki kitabu cha Hemingway and Africa ni cha pekee. Mwanzo kukiona ni pale nilipokiazima kutoka maktaba ya Chuo Kikuu cha Minnesota, nikakisoma. Kilinigusa kwa namna ya pekee, kwa jinsi kilivyosheheni taarifa na uchambuzi mpya, nikaamua lazima niwe na nakala.

Kama unavyoniona pichani, nimekishika kitabu hiki nikiwa nimefurahi sawa na mtu aliyejishindia kreti ya bia. Ninataja bia kwa makusudi. Kitabu hiki, chenye kurasa 398, bei yake ni dola 80 ambayo kwa madafu ni zaidi ya 120,000. Ukienda baa na hela hizo, unapata kreti mbili za bia, kuku mzima, na nauli ya teksi ya kukurudisha kwenu Mbagala. Kama wewe si mtu wa baa, hizo hela ni mchango tosha wa sherehe kama vile "send-off."

Sasa inakuwaje Krismasi yote hii mtu ufurahie kitabu cha bei mbaya, badala ya kujichana na bia? Ukweli ni kwamba kila mtu ana udhaifu wake. Udhaifu wangu mojawapo ni kuvipenda sana vitabu.

Kuhusu mwandishi Hemingway, ni kwamba kwa miaka na miaka nimekuwa msomaji na shabiki mkubwa wa maandishi yake: kuanzia riwaya na hadithi fupi, hadi insha na barua. Nayapenda kwa namna ya pekee maandishi yake yanayohusu uhusiano wake na Afrika, kwani alitembelea na kuishi miezi mingi Afrika Mashariki, hasa Kenya na Tanganyika. Aliandika kuhusu mazingira ya nchi hizo, kuhusu watu na tamaduni zao, na kuhusu wanyama katika mbuga za hifadhi, kwa kiwango cha ustadi ambacho sisi wenyewe hatujakifikia. Alituachia hazina kubwa katika maandishi yake, hazina ambayo hatujafunguka macho na kuitumia.

Monday, December 17, 2012

Hongera JWTZ Kwa Kufungua Maktaba


Nimevutiwa sana na taarifa juzi kuwa Rais Kikwete, Amiri Jeshi wa Tanzania, amefungua maktaba ya kisasa kwenye chuo cha mafunzo cha Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) Monduli. Ni habari njema kabisa.

Mimi ni mdau mkubwa wa maktaba na katika blogu hii ninaziongelea mara kwa mara. Mifano ni maktaba za TangaDar es SalaamSongeaLushotoMoshiIringa, na Southdale.

Kwa miaka mingi sijawahi kusikia rais au kiongozi mwingine wa kitaifa Tanzania akifungua maktaba, ukiachilia mbali tarehe 9 Desemba, 1967, ambapo Mwalimu Nyerere alifungua Maktaba Kuu ya Taifa, Dar es Salaam.

Pita katika maktaba yoyote Tanzania, utaona kuwa maktaba ni kitu ambacho wa-Tanzania hawakithamini sana, isipokuwa labda wanafunzi. Na hao wanafunzi wanaonekana maktabani endapo wamebanwa sana na mwalimu au wanakabiliwa na mitihani.

Wakaazi wa Tanga, kwa mfano, wamekuwa na bahati ya kuwa na maktaba tangu mwaka 1958, kabla ya Uhuru. Ingebidi wawe juu kabisa kitaifa kwenye suala la elimu. Lakini wapi, ukiingia katika maktaba ile, hutawaona. Je, unadhani kuwa ukimwuliza mkaazi wa Arusha au Songea akuonyeshe maktaba iko wapi, ataweza kukuambia? Jaribu uone.

Tanzania tumezoea kusikia kuhusu ufunguzi wa baa, sio maktaba. Kama unafungua baa maarufu, unaweza kabisa kumleta waziri akawa mgeni rasmi. Kutokana na utamaduni huo, kitendo cha JWTZ cha kufungua maktaba ya kisasa ni cha pekee. Ni kitendo kinacholeta matumaini kuwa labda tutashtuka na kuelewa umuhimu wa maktaba. Natoa pongezi kwa JWTZ.

Sunday, December 16, 2012

Serikali Yapongeza Kuanzishwa Kitivo cha Udaktari Songea

Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Ndugu Said Mwambungu akisalimia wananchi baada ya kuwasili Peramiho. Kushoto kwake ni ASKOFU Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Songea, Norbert Mtega akifuatiwa na Mratibu wa Kitivo cha Udaktari Peramiho Chuo cha Mt Augustino Tawi la Songea Padre Dunstan M. Mbano
Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Ndugu Said Mwambungu akikagua maeneo ya kitivo cha udaktari Peramiho. Kushoto kwake ni Joseph Joseph Mkirikiti na kulia kwake ni ASKOFU Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Songea, Norbert Mtega akifuatiwa na Mratibu wa Kitivo cha Udaktari Peramiho Padre Dunstan Mbano



Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Ndugu Said Mwambungu akielekezwa jambo na ASKOFU Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Songea, Norbert Mtega.

Jengo la utawala ambalo bado halijaanza kutumika
Jengo la hosteli ya wanafunzi ambalo bado halijaanza kutumika
Jengo la Maabara Kitivo cha Udaktari Peramiho baada ya ukarabati ambalo bado halijaanza kufanya kazi kutokana na ukosefu wa vifaa vya kufundishia

Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Ndugu Said Mwambungu akihutubia wananchi wa Peramiho
Serikali imepongeza uamuzi wa Chuo Kikuu cha Mt Augostino Tanzania kuanzisha kitivo cha udaktari katika kituo chake cha Songea. Hayo yalisemwa jana tarehe 15.12.2012 na Mkuu wa mkoa wa Ruvuma ndugu Said Thabit Mwambungu alipofanya ziara ya kukagua maendeleo ya chuo hicho kilicho katika eneo la Peramiho.  Amesema kuanzishwa chuo hicho ni ukombozi kwa Mkoa wa Ruvuma ambao awali haukuwa na vyuo vya elimu ya juu.

“Kuanzishwa kwa chuo cha Tiba ni lulu kwa mkoa wa Ruvuma kwa vile kitapunguza usumbufu kwa wananchi wa ukanda huu ”alisema Mwambungu.

Aidha, akijibu risala ya chuo kuhusu tatizo la ardhi kwa ajili ya upanuzi wa eneo la chuo, Mwambungu amewataka watendaji walio chini yake wakae na uongozi wa chuo kwa ufumbuzi. Alisisitiza kuwa anaamini liko ndani ya uwezo wao.

“Watendaji kuanzia kijiji kaeni na viongozi wa chuo kupata ufumbuzi wa tatizo hili nanaamini hata likiwashinda, ofisi ya Mkuu wa Wilaya itawasaidia” alisema ndugu Mwambungu.

Akizungumzia tatizo la maji, amekemea tabia ya wananchi kuharibu mazingira na vyanzo vya maji na kusababisha tatizo la maji. Amewataka wananchi waache tabia hii mara moja. Akifafanua zaidi amewataka viongozi wa dini waisaidie serikali kutoa elimu kwa wananchi kuhusu tatizo la uharibifu wa mazingira na athari zake.

“Nawaomba viongozi wa dini mzungumze na waumini wenu kuhusu tatizo hili wakati serikali inasimamia sheria kuhusu waharibifu na uharibifu mazingira” Alisema Mwambungu.

Kwa upande wa umeme alisema watakaa na pande zote zinazohusika ili kupata ufumbuzi kwa vile linaigusa serikali pia.

Awali mratibu wa Kitivo cha Udaktari Peramiho Chuo cha Mtakatifu Agustino Tawi la Songea Padre Dunstan M. Mbano alisema Padre Mbano alisema chuo kina wanafunzi 39 wa mwaka wa kwanza wanaosoma masomo ya udaktari ambao wamelazimika kupelekwa kwa muda katika Chuo cha Ifakara-Morogoro kilicho chini ya Chuo Mama cha Mtakatifu Augustino wakisubiri kukamilika kwa miundo mbinu. Alisema, hata hivyo, wanafunzi hawa kiutawala bado wako chini ya Chuo Kikuu cha Mt Augustino Kituo cha Songea. Alisema Kituo cha Songea kilizinduliwa Novemba mwaka 2011 na kina jumla ya wanafunzi 631. Wanafunzi wa shahada ya kwanza ualimu kwa mwaka wa kwanza na wa pili ni 592 na wanaosoma udaktari ni 39.


Padre Mbano alisema ujenzi wa chuo umegawanyika katika awamu tatu. Awamu ya kwanza ilihusu ukarabati wa majengo ya iliyokuwa hospitali ya wakoma, nyumba ya Mkuu wa Chuo, jengo la utawala na hostel kwa ajili ya wanafunzi. Awamu ya pili na tatu zitahusisha ujenzi wa hostel mbili, ukumbi, maktaba, ,adarasa na nyumba za walimu.

Padre Mbano alisema chuo kinakabiliwa na changamoto za ukosefu wa umeme, maji na samani na vifaa vya kufundishia. Kuhusu umeme, alisema zinahitajika shilingi za Kitanzania milioni 178.3 kuufikisha umeme katika eneo hilo na kwa upande wa samani na vifaa vya kufundishia zinahitajika shilingi za Kitanzania milioni 57.3.

Habari na mwanablog CHANZO: Azimioletu Blog

Tuesday, December 11, 2012

Mungu ni Mmoja: Anaitwa Allah, Brahman, Chiuta, Ruwa na Kadhalika

Uzuri wa kuwa na blogu yako ni kuwa hutawaliwi na mtu katika kuamua nini cha kuandika. Uamuzi wote ni wako. Nimesema kabla kuwa katika blogu yangu hii, masuala ambayo yanasemwa kuwa ni nyeti, kama dini, ni ruksa kujadiliwa. Tena sio tu ruksa, bali muhimu kujadiliwa.

Leo napenda kutoa hoja kuwa Mungu ni mmoja: anaitwa Allah, Brahman, Chiuta, Ruwa, na kadhalika, kutokana na kuwepo kwa lugha nyingi hapa duniani. Huyu ndiye aliye juu ya yote, mwenye uwezo wote, kama inavyosemwa katika ki-Arabu, "Allahu akbar." Ni dhana ya msingi katika dini zetu.

Kama wewe ni mu-Islam, halafu unasema kuwa Allah ni tofauti na Mungu wanayemwabudu wa-Kristu, au Mungu wanayemwabudu wa-Hindu, jichunguze upya, kwani utakuwa unasema kuna miungu zaidi ya mmoja. Utakuwa unaongelea kuwepo kwa mungu mwingine zaidi ya Allah. U-Islam hautambui kuwepo kwa Mungu mwingine zaidi ya Allah.

Kama wewe ni m-Kristu, halafu unasema kuwa Mungu unayemwabudu ni tofauti na Allah, basi inabidi ujichunguze, kwa misingi hiyo hiyo. U-Kristu hautambui kuwepo kwa mungu zaidi ya huyu ambaye sisi wa-Kristu tunayemwabudu, ambaye kwa ki-Arabu huitwa Allah. Usishangazwe na jina Allah. Wa-Kristu ambao ni wa-Arabu nao hutumia jina Allah, wakimaanisha Mungu, kama nilivyowahi kusema katika blogu hii.

Huyu Mungu mmoja anatajwa kwa majina mbali mbali kufuatana na lugha. Wa-Tumbuka wa Malawi na Zambia humwita Chiuta. Wa-Hindu humwita Brahman. Wa-Kamba na wa-Kikuyu humwita Ngai. Wachagga humwita Ruwa.

Hoja yangu ni kuwa majina yote hayo yanamtaja Mungu huyu huyu. Muumini anayeamini kuwa kuna Mungu mmoja tu, sherti akubali na azingatie hilo. Ni ushahidi kuwa Mungu alijitambulisha kwa wanadamu duniani kote tangu mwanzo kabisa.

Nimeona nitoe mawazo yangu, kwa uhuru kabisa, kwani ni haki yangu. Kama kuna anayetaka kuyajadili au kuyapinga, namkaribisha kwa mikono miwili kufanya hivyo.

Monday, December 10, 2012

Baridi Kali Minnesota

Jimbo la Minnesota ni moja ya sehemu zinazopata baridi kali kuliko zote Marekani, wakati wa miezi ya baridi. Jana imeanguka theluji nyingi, kama inavyoonekana pichani, katika eneo la Chuo cha St. Olaf.

Wakati kama huo ni hatari kuendesha magari, na ajali huwa nyingi, yaani magari kugongana barabarani, au kuteleza na kutumbukia mitaroni.













Baridi hii haizoeleki hata kama mtu umepambana nayo miaka na miaka. Inapokuja, ni bora kubaki nyumbani, kama huna sababu ya lazima ya kwenda nje, na kama unakwenda nje, ni lazima kujizatiti kwa mavazi yatakiwayo. Vinginevyo, baridi hii itakuletea madhara. Kuna watu wanaokufa kutokana na kuwa nje kwenye baridi hii.

Katikati ya picha hapa kushoto linaonekana gari maalum ambalo kazi yake ni kusafisha njia na barabara kutokana na kufunikwa na theluji.

Saturday, December 8, 2012

Simba wa Tsavo

Leo napenda kuongelea habari ya simba wa Tsavo. Ni habari iliyokuwa inatusisimua sana tulipokuwa shuleni, baina ya darasa la tano na la nane. Kulikuwa na kitabu, Simba wa Tsavo, ambacho kilichapishwa mwaka 1966. Ni tafsiri ya kitabu cha J.H. Patterson kilichoitwa The Man Eaters of Tsavo.

Kitabu hiki kilielezea matukio ya kutisha wakati ujenzi wa daraja la reli kwenye mto Tsavo, nchini Kenya, miaka mia na kitu iliyopita. Kilielezea namna simba walivyokuwa wakiwavizia, kuwadaka na kuwaua wafanya kazi kwenye eneo la hili daraja wakawaua watu zaidi ya mia, hadi, hatimaye, Patterson alipofanikiwa kuwaua, mwezi Desemba 1898. Hiyo ndio habari tuliyosoma tukiwa shuleni, miaka hiyo ya sitini na kitu.

Lakini, kwa miaka hii ya karibuni, yapata miaka kumi, nimekutana na taarifa nyingine nyingi kuhusu simba wa Tsavo. Je, unajua wale simba waliishia wapi? Katika kusoma habari za mwandishi Ernest Hemingway, ambaye alizaliwa mwaka 1899 eneo la jirani na Chicago, nimegundua kuwa alipokuwa mtoto alipelekwa na baba yake katika hifadhi ya Field Museum of Natural History mjini Chicago. Hapo alipata kuziona maiti za wanyama mbali mbali kutoka Afrika ambazo zilikuwa zimehifadhiwa kitaalam ili zionekane kama vile ni wanyama hai.

Kati ya wanyama hao ni wale simba wa Tsavo, ambao picha yao inaonekana hapa juu. Habari hii ilinishtua sana, kwani sikujua kabisa kuwa simba wa Tsavo wamehifadhiwa na kwamba wako Chicago. Hiyo ni faida ya wazi ya kusoma vitabu, kwamba mtu unagundua mambo ambayo hukuyajua. Pamoja na kuangalia wanyama hao waliohifadhiwa, mtoto Hemingway alisoma kitabu cha The Man Eaters of Tsavo. Hayo yote yalichangia katika kumjengea Hemingway mapenzi makubwa aliyokuwa nayo juu ya Afrika kwa maisha yake yote.

Mwaka 1933, Hemingway na mke wake Pauline walifunga safari wakitokea Ulaya, wakaja Afrika Mashariki. Walishuka meli Mombasa, wakapanda treni kuelekea Nairobi. Walipita Tsavo, wakaenda hadi Machakos, kisha Tanganyika. Kuhusu safari yake ya Tanganyika, Hemingway aliandika kitabu maarufu kiitwacho Green Hills of Africa, ambacho ni kimoja ya vitabu vyake ambavyo nimevisoma na kuwafundisha wanafunzi.

Wednesday, December 5, 2012

Barua za Ernest Hemingway, 1907-1922

Leo nimekipata kitabu cha barua za Hemingway ambacho nilikitaja katika blogu hii siku chache zilizopita. Kama nilivyoandika, nilikiona kwa mara ya kwanza katika duka la vitabu hapa Chuoni St. Olaf. Lakini nakala ile ilinunuliwa hima, ikabidi niagize.

Hemingway alikuwa mwandishi makini wa barua. Hata mwanae, Mzee Patrick Hemingway, amethibitisha hivyo. Kwa ujumla, Hemingway hakutaka wala kutarajia kuwa barua zake zichapishwe. Alikuwa na mazoea ya kuandika barua zake kwa uwazi na hata kutumia lugha ambayo inaonekana kali au yenye kukiuka maadili.

Baada ya Hemingway kufariki, mwaka 1961, suala la kuchapisha au kutochapisha maandishi ya Hemingway ambayo alikuwa hajayachapisha lilijitokeza na kuwa kubwa. Maandishi yake mengine alikuwa hajamaliza kuyarekebisha. Barua zake alikuwa hajaazimia zichapishwe. Suala likawa nini kifanyike.

Wasomaji wa maandishi ya Hemingway walisukumwa na kiu ya kutaka kusoma maandishi yake yote. Wahariri na watafiti walitaka hivyo pia. Familia yake ilikuwa katika mtihani mgumu. Lakini hatimaye, iliamuliwa kuwa bora kuchapisha maandishi hayo, hata barua zake. Ndivyo tulivyovipata vitabu vya Hemingway kama vile The Garden of Eden, Islands in the Stream, A Moveable Feast, na Under Kilimanjaro. Ni matokeo ya maamuzi magumu, na juhudi za wahariri kuhariri miswada aliyoicha Hemingway ikiwa haijakamilika, wakiongozwa na wazo kwamba bila shaka Hemingway mwenyewe angeafiki uhariri huo.

Tunaposoma vitabu hivi bado tunajiuliza iwapo kama Hemingway angeishi zaidi, angerekebisha vipi maandishi haya, hasa ikizingatiwa kuwa alikuwa mwandishi mwenye nidhamu ya hali isiyo ya kawaida katika kusahihisha na kuboresha maandishi yake. Alitaka kila neno liwe mahali pake na liwe kweli ni neno hilo, si jingine, na kila sentensi iwe imekamilika kwa kiwango cha juu kabisa.

Leo nilitaka nikumbushie pia kitabu cha barua za Shaaban Robert, ambacho niliandika habari zake katika blogu hii. Nilitaka nivijadili vitabu hivi vya barua kwa pamoja, kuelezea umuhimu wa vitabu vya aina hii, ambamo tunapata kuwafahamu waandishi hao maarufu kupitia njia ya barua walizoandika. Barua hizi ni kioo muhimu cha kutuwezesha kuyafahamu mambo ambayo pengine hatungeyafahamu kwa kuangalia tu vitabu vyao vingine. Nangojea nipate wasaa wa kuandika na kuzihusianisha barua za Hemingway na zile za Shaaban Robert.

Tuesday, December 4, 2012

Wa-Kristu Wasilimu; Wa-Islam Waingia u-Kristu

Dini ni moja ya mada ambazo nazizungumzia sana katika blogu yangu. Leo napenda kugusia tena mada ya mtu kubadili dini. Niliwahi kuandika kuhusu mada hiyo, nikatamka kuwa kubadili dini ni haki ya mtu, kwa mujibu wa dhamiri yake. Soma hapa.

 Dini ni safari ambayo binadamu anasafiri. Kwa wengine ni safari ngumu yenye vikwazo vingi. Kwa wengine ni safari nyepesi, kwa maana kwamba wametulia kabisa katika imani yao. Namshukuru Muumba kwamba mimi ni mmoja wa hao waliotulia, ingawa nilipokuwa kijana nilihangaika na kutetereka kiasi fulani.

Ukiangalia mtandaoni, kama vile YouTube, utaona taarifa nyingi za watu wanaobadili dini, kutoka u-Islam kuingia u-Kristu, kutoka u-Kristu kuingia u-Islam, na kadhalika. Maelfu ya watu wanafanya hivyo muda wote. Katika YouTube utawaona wengi wakitoa ushuhuda kuhusu walivyohamia dini nyingine na nini kiliwafanya wahame.  Kwa mtazamo wangu, hayo ni mambo yao binafsi, baina yao na Muumba. Hayaongezi wala kuteteresha imani yangu.

Hapa chini ni taarifa ya watu kuingia u-Islam hivi karibuni nchini Burundi. Hakuna mwenye haki ya kuwazuia, iwapo watu hao wanajisikia ndani ya moyo wao kuwa kwa kubadili dini wanakuwa karibu zaidi na Muumba. Nawatakia mema katika safari hii ya kiroho.
.

Hapa chini ni taarifa ya wa-Islam kuingia u-Kristu nchini Pakistan. Hakuna mwenye haki ya kuwazuia, iwapo watu hao wanajisikia ndani ya moyo wao kuwa kwa kubadili dini wanakuwa karibu zaidi na Muumba. Nawatakia mema katika safari hii ya kiroho.

Nimekutana na Kobina Aidoo

Siku chache zilizopita, Kobina Aidoo kutoka Ghana alitembelea hapa Chuoni St Olaf kutoa mhadhara kama sehemu ya maazimisho ya Africa Weeks. Maazimisho hayo huandaliwa kila mwaka na jumuia ya wanafunzi iitwayo Karibu.

Sikuwa nimesikia jina la Kobina Aidoo, ila nilihudhuria mhadhara wake. Ni kijana mwenye kipaji anayeinukia katika nyanja za filamu na uanaharakati katika kuelimisha jamii.

Aliongelea suala la nani ni mw-Amerika Mweusi, akaleta changamoto nyingi zinazowakabili watu weusi wanaoishi hapa Marekani katika kujitambua na kujitambulisha. Baada ya kusema machache, alituonyesha DVD yake ambayo imajaa kauli na mitazamo ya watu weusi wanaoishi Marekani, wakiwa wametokea nchi mbali mbali za Afrika na bara la Marekani.

Ni mitazamo inayofikirisha na kuchangamsha akili. Inatupanua mawazo kuhusu utata wa suala hilo la nani ni m-Marekani Mweusi, na kwa ambaye hakufahamu, inashtua kuona migogoro baina ya waMarekani weusi wa asili na watu weusi ambao ni wahamiaji wa miaka ya karibuni nchini Marekani.

Katika picha hapo juu ninaonekana na Kobina, baada ya mhadhara wake. Tulipiga picha hii mara baada ya mimi kumkabidhi nakala ya kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ambayo anaonekana ameishika, na yeye akawa amenikabidhi nakala ya DVD yake.

Sunday, December 2, 2012

Naiwazia Songea

Nyumbani ni nyumbani. Leo nimeikumbuka Songea, nikaamua kuleta picha mbili tatu nilizopiga mwaka huu. Hapa kushoto ni barabara itokayo stendi kuu kuelekea bomani, hatua chache tu kutoka duka la vitabu la Kanisa Katoliki. Nyuma ya haya majengo ndipo kilipo Chuo Kikuu cha Kanisa Katoliki.











Hapa ni taswira ya uwanja wa Maji Maji, kutoka juu. Nilipiga picha hii kutoka ghorofa ya tatu ya hoteli niliyofikia, ng'ambo ya barabara kutoka kituo kikuu cha polisi. Kule ng'ambo ni kitongoji cha Lizaboni, njiani kuelekea Peramiho, Mbinga, na Mbamba Bay.
Hapa kushoto ni stendi kuu nikiwa na dada yangu na mdogo wangu.

Saturday, December 1, 2012

Mwandishi Hemingway: Vitabu Vipya

Ernest Hemingway ni kati ya waandishi maarufu kabisa duniani. Alizaliwa mwaka 1899 karibu na mji wa Chicago, akafa kwa kujipiga risasi nyumbani kwake kwenye jimbo la Idaho mwaka 1961. Katika maisha yake, aliandika sana, akianzia kama ripota wa gazeti la Kansas City Star. Maandishi yake ni pamoja na riwaya, hadithi fupi, insha, masimulizi ya safari zake, barua magazetini, mashairi, na maelfu ya barua. Tangu wakati wa uhai wake hadi leo, watu wengi sana wamechambua maandishi yake na kuelezea maisha yake.


Vitabu kumhusu Hemingway vinaendelea kuchapishwa. Miezi ya karibuni, vimechapishwa vitabu kama Hemingway and Africa, Hemingway's Boat, na The Letters of Ernest Hemingway: Volume 1,1907-1922.

Kitabu cha The Letters of Ernest Hemingway: Volume 1, 1907-1922 nilikiona kwa mara ya kwanza miezi michache iliyopita katika duka la vitabu la Chuo cha St. Olaf. Ni kitabu muhimu sana kwa jinsi kinavyojumlisha kila barua ya Hemingway inayojulikana kwa kipindi cha miaka iliyotajwa. Ninapangia kujipatia nakala.

Ninayo nakala ya kitabu cha mwanzo cha barua za Hemingway, kiitwacho Ernest Hemingway: Selected Letters: 1917-1961. Lakini hiki cha sasa kinafunika kila kitu. Ni juzuu la kwanza, na inategemewa kwamba kutachapishwa majuzuu mengine, hadi kukamilisha maisha yote ya Hemingway.

Wakati wa maonesho ya vitabu yaliyofanyika wiki chache zilizopita mjini Minneapolis, mzee mmoja alifika kwenye meza yangu, na katika mazungumzo yetu nilimtaja Hemingway. Hapo hapo mzee akaniuliza kama nimeshasoma Hemingway's Boat.

Niligutuka kuona mzee huyu keshasoma kitabu hiki ambacho kimetoka karibuni tu. Lakini papo hapo nikakumbuka kuwa hapa ni Marekani, sio Tanzania. Usomaji wa vitabu hapa ni jambo la kawaida kabisa. Nilimwambia kuwa kitabu hicho nimekiona katika duka la vitabu Chuoni St. Olaf, na kwamba nimekiangalia angalia, ila sijakisoma. Hata hivi, tuliendelea na mazungumzo kuhusu mambo ya aina hiyo.

Kitabu cha Hemingway and Africa nilikiazima kutoka maktaba ya Chuo Kikuu cha Minnesota nikakisoma. Niko njiani kujipatia nakala. Hiki ni kimoja kati ya vitabu muhimu sana vinavyochambua uhusiano wa Hemingway na Afrika. 

Najihesabu kama mmoja wa wapenzi na wafuatiliaji wakubwa wa Hemingway. Nimefanya na naendelea kufanya utafiti juu yake na maandishi yake, hasa uhusiano wake na Afrika. Imekuwa ni furaha kwangu kuwapeleka wanafunzi Tanzania, kwa somo hilo.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...