Sikuwa nimesikia jina la Kobina Aidoo, ila nilihudhuria mhadhara wake. Ni kijana mwenye kipaji anayeinukia katika nyanja za filamu na uanaharakati katika kuelimisha jamii.
Aliongelea suala la nani ni mw-Amerika Mweusi, akaleta changamoto nyingi zinazowakabili watu weusi wanaoishi hapa Marekani katika kujitambua na kujitambulisha. Baada ya kusema machache, alituonyesha DVD yake ambayo imajaa kauli na mitazamo ya watu weusi wanaoishi Marekani, wakiwa wametokea nchi mbali mbali za Afrika na bara la Marekani.
Ni mitazamo inayofikirisha na kuchangamsha akili. Inatupanua mawazo kuhusu utata wa suala hilo la nani ni m-Marekani Mweusi, na kwa ambaye hakufahamu, inashtua kuona migogoro baina ya waMarekani weusi wa asili na watu weusi ambao ni wahamiaji wa miaka ya karibuni nchini Marekani.
Katika picha hapo juu ninaonekana na Kobina, baada ya mhadhara wake. Tulipiga picha hii mara baada ya mimi kumkabidhi nakala ya kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ambayo anaonekana ameishika, na yeye akawa amenikabidhi nakala ya DVD yake.