Sunday, July 28, 2013

Wageni Kutoka Tanzania


Wiki hii nimekuwa na bahati hapa Minnesota ya kukutana na wageni wawili kutoka Tanzania. Mgeni wa kwanza, Ndugu Charles Mpanda kutoka Arusha, tulionana tarehe 25 mjini Rochester, tukapiga picha inayoonekana hapa kushoto. Habari ya tukio hili niliandika hapa. Nitaandika zaidi katika blogu hii ya "hapakwetu."










Leo nimeenda mjini New Prague, kuonana na mgeni mwingine, Fr. Setonga, ambaye naonekana naye katika hiyo picha ya chini. Fr. Setonga tumewasiliana kwa miaka mingi kidogo, kwa simu na barua pepe, ila hatukuwahi kuonana. Leo imekuwa bahati ya kuonana.

Tumeongelea masuala mbali mbali, kuhusu dini yetu, kuhusu juhudi na mafanikio ya Kanisa Katoliki katika sekta ya elimu, sehemu mbali mbali duniani, kwa karne hadi karne, kuanzia shule za msingi hadi vyuo vikuu. Hii inatokana na msimamo wa Kanisa Katoliki wa kuthamini sana elimu. Kwangu mimi niliyesomeshwa katika shule za Kanisa Katoliki, ni jambo la kujivunia na kushukuru kwamba walinifundisha maadili na nidhamu ya kazi ya kiwango cha juu kabisa, pamoja na kuzingatia vipaji na uwezo tunapata kutoka kwa Mungu, na kwa ajili ya kuwahudumia wengine.

Tuligusia mfano hai wa jinsi Kanisa Katoliki linavyokazana kufungua matawi ya chuo kikuu cha Mtakatifu Augustin nchini Tanzania. Nilimdokezea Fr. Setonga kuwa ninawazia kwenda kufundisha katika chuo hiki, kama njia moja ya kutoa shukrani kwa Kanisa.

Kati ya mambo mengine tuliyoongelea kwa undani, tukakubaliana, ni umuhimu wa sisi waumini wa Tanzania kuwa wafadhili wa kanisa letu na shughuli zake mbali mbali. Itakuwa ni faraja na jambo la kujivunia iwapo tutabeba majukumu ambayo aghalabu yamebebwa na wafadhili kutoka nchi za nje, hasa Ulaya na Marekani.

Friday, July 26, 2013

Mwaliko Mkutanoni Finland

Nimepata mwaliko kwenda kushiriki mkutano wa wanataaluma Finland, katika chuo kikuu cha Turku. Mkutano ufanyika kuanzia tarehe 19 hadi 24 Agosti na mada yake itakuwa The Role of Theory in Folkloristics and Comparative Religion." Nitakuwa mmoja wa watoa mada wateule, na mhadhara wangu utahusu "The Epic as Discourse on National Identity," kama ilivyotajwa katika programu hii hapa.

Mkutano huu wa wanataaluma umeandaliwa kwa kumbukumbu ya marehemu Profesa Lauri Honko, mmoja wa wataalam wakubwa kabisa duniani katika. Wa-Tanzania labda watafurahi kusikia kuwa Profesa Honko alifanya utafiti sehemu mbali mbali za dunia, ikiwemo Tanzania. Niliwahi kumwona,  na kuwa naye kwa wiki kama mbili hivi, wakati nilipohudhuria warsha ya watafiti ambayo aliiendesha Turku mwaka 1991. Alikuwa ni mtaalam sana, aliyekuwa anaongea kwa kujiamini kabisa, lakini mtu mtaratibu na mpole. Ukisoma vitabu vyake na makala zake, unaona wazi kabisa kuwa alikuwa mwenye mawazo mazito yenye kutoa mchango mkubwa kwa taaluma.

Kati ya mambo mengi aliyofanya, ikiwa ni pamoja na kuandika vitabu na makala na kutoa mihadhara, Profesa Honko aliisaidia UNESCO kwa kuandaa sera ya kuhifadhi utamaduni.

Sio jambo geni kwangu kupata mialiko ya aina hii. Najisikia raha kwenda kuuelezea ulimwengu fikra, mitazamo, na matokeo ya utafiti wangu. Papo hapo ni fursa ya kukutana na wataalam wengine na kubadilishana mawazo na uzoefu. Ndivyo taaluma inavyokua na kustawi.

Hata hivi, sitakuwa na raha sana kwenye mkutano huu wa Turku, kwani nitakuwa namkumbuka Profesa Honko.  Ni jambo jema kwamba mkutano utakuwa ni kwa kumkumbuka, lakinii papo hapo masikitiko ya kutokuwa naye yatakuwepo. Mungu amweke mahali pema Peponi.

Thursday, July 18, 2013

Kiu ya Kusoma Vitabu

Daima nina kiu ya kusoma vitabu.  Sio rahisi unikute sina kitabu. Hii sio tu kwa vile mimi ni mwalimu. Ni tabia ambayo nilijengeka nayo tangu nikiwa kijana mdogo.

Kuwa mwalimu kumenipa motisha zaidi ya kusoma sana vitabu. Wakati huu ninapoandika, wanafunzi wangu na mimi tumemaliza kusoma Half of a Yellow Sun kilichoandikwa na Chimamanda Ngozi Adichie. Sote tumekifurahia sana. Lakini, mwandishi huyu amechapisha hivi karibuni na kitabu kingine kiitwacho Americanah, ambacho tayari kinazungumziwa sana miongoni mwa wapenda vitabu. Kwa hivi, nami najipanga kujipatia kitabu hiki, nikisome.

Kitabu kingine ambacho tumekimaliza katika darasa tofauti siku chache zilizopita ni Midnight's Children cha Salman Rushdie.  Kitabu hiki ni kama chemsha bongo, kwa jinsi kilivyotumia mbinu mbali mbali za kuelezea maisha ya mhusika mkuu Saleem Sinai. Maisha hayo yamefungamana na historia ya India, tangu dakika ile India ilipopata uhuru, usiku wa manane, mwaka 1947. Rushdie amechanganya matukio ya historia na ubunifu wake wa ajabu katika kitabu hiki.

Midnight's Children ni kitabu kinachokutegemea msomaji uwe na ufahamu fulani wa mila, desturi na dini za India, hasa u-Hindu, u-Islam, u-Kristu, na u-Parsi. Uwe na ufahamu fulani wa historia ya India hasa katika karne ya ishirini, inayojumlisha viongozi maarufu kama Mahatma Gandhi, Jawaharlal Nehru, Muhammad Ali Jinnah, na Indira Gandhi. Ujue mazingira yaliysababisha kuzaliwa kwa nchi mbili za India na Pakistan, na mgogoro wa Kashmir, ambao bado unaendelea. Kwa bahati nzuri, katika miaka niliyofundisha hapa chuoni St. Olaf, nimefundisha sana fasihi ya India na hayo yote niliyoyataja.

Tulipofikia ukurasa wa mwisho wa kitabu hiki, tulijisikia kama washindi wa mashindano magumu. Kwa upande wangu, baada ya kupambana na Midnight's Children hadi mwisho, nimejawa na hamasa ya kusoma kitabu kingine cha Rushdie Satanic Verses, ambacho nilikinunua zamani, nikajaribu kukisoma, bila kufika mbali. Ninahisi kuwa kwa kusoma Midnight's Children nimejiandaa vilivyo kukabiliana na Satanic Verses. Au labda nianzie na kitabu chake kiitwacho The Enchantress of Florence, ambacho nimekuwa nacho kwa miaka kadhaa, bila kukisoma.

Ni jambo jema kujaribu kusoma maandishi mbali mbali ya mwandishi yeyote, sio kitabu kimoja tu. Kwa mfano, kwa upande wa Tanzania, utawakuta watu wakitaja kitabu cha Hamza Njozi kuhusu mauaji ya Mwembechai lakini hawajui kuwa mwandishi huyu amechapisha vitabu vingine pia, na makala nyingi, kuhusu u-Islam na fasihi.

Vile vile, wengi wakisikia jina la Salman Rushdie, wanalihusisha na kitabu cha Satanic Verses tu. Huu nao ni uzembe, kwani mwandishi huyu amechapisha vitabu vingi, kuanzia riwaya hadi insha kuhusu masuala mbali mbali ya sanaa, siasa na utamaduni. Kumtendea haki Rushdie ni lazima tusome maandishi yake mbali mbali.

Akili zetu zinapaswa ziwe na duku duku isiyoisha ya kujua mambo. Njia moja kuu ya kujaribu kukidhi kiu hii ni kusoma sana vitabu. Hapo utaona kwamba, tofauti na imani ya jamii yetu ya Tanzania, wajibu wa kusoma vitabu ni wa watu wote, sio wanafunzi tu.

Wednesday, July 17, 2013

Chezea Arusha Weye

Katuni hii imenipendeza. Sina zaidi, bali niseme tu haka kajibwa kanatisha. Tena usiombee kukutana nako.

Ingawa mchoraji hajataja mambo ya uchaguzi wa madiwani uliofanyika siku chache zilizopita, katuni inayapeleka mawazo yetu kwenye uchaguzi huo, ambao matokeo yake yamekuwa CHADEMA kushinda kata zote nne zilizokuwa zinashindaniwa.

Matokeo hayo hayakunishangaza. Kwa miaka kadhaa, katika pitapita zangu Arusha, nikiongea na madereva wa teksi, mafundi viatu, na wauza mitumba, nimejionea nguvu za CHADEMA katika mji ule. Nilithubutu hata kuandika makala kuhusu nguvu ya CHADEMA mjini Arusha. Makala hiyo ni hii hapa. Niliandika hayo, na leo ninaandika tena, ingawa mimi si mwanachama wa chama chochote cha siasa.

Thursday, July 11, 2013

Tumeanza Kusoma "Abyssinian Chronicles"

Baada ya kumaliza kitabu cha Half of a Yellow Sun, darasa langu la fasihi ya Afrika tumekuwa tukisoma Abyssinian Chronicles, riwaya ya Moses Isegawa.

Moses Isegawa ni kijana aliyezaliwa na kukulia Uganda. Lakini mwaka 1990 aliondoka Uganda akaenda kuishi Netherlands, akiwa amechukua uraia wa nchi ile.

Nilikuwa nimesikia habari za kitabu chake hiki kwa miaka kadhaa. Nilinunua nakala, ila sikupata fursa ya kukisoma, ingawa nilikipitia juu juu. Hata hivyo katika kukipitia hivyo, niliona wazi kabisa kuwa ni kitabu murua, kilichoelezea kwa ufasaha na mvuto mkubwa maisha ya leo ya watu wa Uganda, kuanzia kijijini hadi mjini.

Nilipokuwa naandaa kozi yangu hii, miezi michache iliyopita, niliamua kitabu hiki kiwemo katika orodha yangu. Tumesoma karibu kurasa 100 tu,  wakati kitabu kina kurasa 480. Kiasi tulichosoma kimetupa fursa ya kuongelea dhamira mbali mbali zinazojitokeza, kama vile mila na desturi za arusi, masuala ya wahusika, na sanaa.

Kwa upande wangu, nimekuwa nikiwaambia wanafunzi kuwa maelezo ya maisha ya vijijini yamenikumbusha maisha yangu mwenyewe, maana nilizaliwa na kukulia nilikulia kijijini.

Moses Isegawa alikiandika kitabu hiki kwa lugha ya kidachi (Dutch), na jina lake lilikuwa Abessijnse kronieken, ambacho kilichapishwa Amsterdam mwaka 1998. Nakala 100,000 ziliuzwa hima, ingawa idadi ya watu wa nchi ile ni yapata milioni 16 tu.

Mwandishi alikiweka kitabu chake hiki katika lugha ya ki-Ingereza. Kwa kawaida, tunasema alikitafsiri. Lakini kwa mujibu wa falsafa za leo, dhana ya tafsiri ni dhana tata, na kile tunachokiita tafsiri sio tafsiri kwa kweli, bali utungo mpya. Huo ndio mtazamo wangu kuhusu Abyssinian Chronicles.

Muhula wetu umeisha leo, na mategemeo yangu ni kuwa wanafunzi na mimi mwenyewe tutaendelea kukisoma kitabu hiki hadi ukurasa wa mwisho. Sioni kama kuna tatizo kufikia mwisho wa muhula bila kumaliza kusoma kitabu. Dhana ya kumaliza kusoma kitabu nayo ni dhana tata na naweza kusema ni dhana muflisi. Kwa kutafakari kwa undani maana ya kusoma ni nini, na nini kinafanyika tunaposema tunasoma kitabu, nimejionea kuwa huwezi kumaliza kusoma kitabu chochote, hata kama umefika ukurasa wa mwisho na sentensi ya mwisho. Hilo ni suala jingine la falsafa, ambalo nalifafanua wakati wa kufundisha fasihi.

Abyssinian Chronicles ni kitabu kinachoelezea mambo ya miaka ya karibuni, ya sabini na kitu hadi themanini na kitu. Kinavutia sana. Ni ushahidi mwingine wa jinsi wenzetu wa nchi jirani, na wa nchi zingine za Afrika, walivyo katika anga za juu sana katika uandishi kwa lugha hizi za kigeni.

Wednesday, July 10, 2013

Taasisi ya Sir Emeka Offor Yachangia Vitabu

Sir Emeka Offor Foundation of Nigeria donates $600,000 to St. Paul-based Books for Africa; Largest donation ever

E-mail Print PDF
books for africa photo-3238792 orig
Books for Africa photo
The Nigeria-based Sir Emeka Offor Foundation has donated $600,000 to Books For Africa (BFA), which will support the shipment of more than a million books to the children of Nigeria and across Africa.

"This donation represents the largest single donation we have ever received at Books For Africa, so naturally we are quite excited," said Patrick Plonski, executive director of BFA. "The generosity of Sir Emeka Offor in advancing education across the African continent is an outstanding example for others to follow."

Tom Warth, who founded BFA in 1988, said that the "benefits that will accrue to the young people of Africa through this generous donation are immeasurable. We at Books For Africa struggle every day to convince folks of the wisdom of education in the advancement of African nations. Over our 25 years many have agreed with us but to have your generous donation as an example in the future will make our task easier."

In a unique partnership with BFA that began in 2010, the Sir Emeka Offor Foundation has agreed to sponsor major shipments of books to Nigeria and The Gambia. In 2010, the Foundation sponsored eight containers to students in Nigeria and in 2011, another 16 containers, a total of about 530,000 books.

In 2012, the foundation sponsored the shipment 110,000 books for school children as part of Books For Africa's "Million Books to The Gambia" campaign.

The $600,000 donation will support the shipment of an additional one million books to the children of Africa. With funding provided by this grant, planning is currently under way to distribute an additional 1.1 million books to Nigeria, the Gambia, Somalia, Liberia, Tanzania, Namibia, Senegal, Ethiopia, Kenya, Rwanda, Botswana, South Africa, sierra Leone, Malawi and Egypt.

The Sir Emeka Offor Foundation is a non-governmental philanthropic organization whose founder, Sir Emeka C. Offor, began in the 1990s to positively render assistance to the needy in society in various ramifications irrespective of tribe, creed, religion and nation.

Books For Africa is the world's largest shipper of donated text and library books to the African continent. It has shipped over 28 million books to 49 African countries over the past 25 years.

CHANZO: InsightNews.com

Thursday, July 4, 2013

Tumemaliza Kusoma "Half of a Yellow Sun"

Kwa wiki hizi sita, katika kipindi hiki cha "summer," nimekuwa nikifundisha kozi juu ya fasihi ya Afrika. Jana tumemaliza kusoma Half of a Yellow Sun, riwaya ya Chimamanda Ngozi Adichie wa Nigeria.  Huyu ni mwandishi chipukizi, lakini tayari ameshajipatia umaarufu sana na nyota yake inazidi kung'ara.

Amechapisha vitabu kadhaa akianzia na Purple Hibiscus na The Thing Around Your Neck. Ninavyo vitabu hivyo, na nimeshawahi kufundisha Purple Hibiscus.  Hivi karibuni, amechapisha Americanah, kitabu ambacho kinaongelewa sana miongoni mwa wasomaji, walimu, na wahakiki.

Kilipochapishwa kitabu cha Half of a Yellow Sun, nilisoma taarifa zake. Taarifa hizi zilielezea kuwa kitabu hiki kinahusu vita ya wenyewe kwa wenyewe nchini Nigeria, ambapo sehemu ya kusini mashariki ilijitenga na kutangaza kuwa imekuwa taifa huru la Biafra.

Mwaka 2008 Chimamanda Ngozi Adichie alikuwa mmoja wa waandishi walioalikwa kuhudhuria tamasha la vitabu Minneapolis. Alikuja kuzindua kitabu cha Half of a Yellow Sun. Nilihudhuria, nikasikiliza hotuba yake, kisha nikajumuika na umati wa watu waliokuwa wananunua nakala na kusainiwa na mwandishi. Nilipata pia fursa ya kupiga naye picha inayoonekana hapa kushoto.

Pamoja na kuwa nilinunua nakala ya Half of a Yellow Sun siku hiyo, sikupata fursa ya kukisoma. Lakini miaka yote hii nilikuwa na nia ya kufanya hivyo, na nimefanya hivyo katika kufundisha somo la fasihi ya Afrika.

Wote tumependezwa sana na Half of a Yellow Sun. Chimamanda Ngozi Adichie ana kipaji kikubwa sana cha kubuni na kusimulia hadithi. Yeyote anayesoma maandishi yake na anakijua ki-Ingereza vizuri, atakiri kuwa mwandishi huyu anaimudu vizuri sana lugha hiyo. Ni kweli kuwa kwa ujumla Half of a Yellow Sun inahusu vita ya Biafra, 1966-1970, lakini kwanza inaongelea maisha ya kila siku ya watu, hasa katika mazingira ya Chuo Kikuu cha Nsukka. Chimamanda alizaliwa na kukulia hapo, na katika maandishi yake hupenda kuongelea maisha ya wasomi na familia zao chuoni pale.

Hata katika mazingira ya vita, Half of a Yellow Sun inatuonyesha watu wakijitahidi kuendelea na shughuli zao za kawaida, kama vile kuelimisha watoto, hata kama ni chini ya mti. Tunawaona watu wakitafuta riziki za maisha. Na tunawaona watoto wakicheza michezo, pamoja na dhiki kubwa ya magonjwa na njaa. Pamoja na ukatili mkubwa uliojitokeza katika vita ya Biafra, Chimamanda Ngozi Adichie amejiepusha na kishawishi cha kuangalia suala zima kama suala la aina mbili tu ya watu, yaani wabaya na wema. Anaonyesha jinsi binadamu tulivyo na uwezo wa kuwa wabaya, sawa na wale ambao tunawaona ndio wabaya.

Half of a Yellow Sun imefuata vizuri mtiririko wa matukio yaliyotangulia vita na matukio ya vita yenyewe. Kwangu mimi kama m-Tanzania, nimeguswa na jinsi Chimamanda Ngozi Adichie alivyoelezea mchango wa Tanzania katika kuiunga mkono Biafra. Ameelezea furaha ya watu wa Biafra na heshima waliyokuwa nayo kwa Tanzania na Mwalimu Nyerere. Wakati nasoma kitabu hiki na suala hili la Tanzania, nilikumbuka kitabu kipya cha Chinua Achebe kiitwacho There Was a Country. Humo Achebe ameelezea vizuri sana jinsi msimamo wa Tanzania ulivyoshangiliwa na watu wa Biafra. Jina la Tanzania lilikuwa linatajwa kila mahali. Miziki ya Tanzania ilipigwa kila mahali. Katika Half of a Yellow Sun, kuna baa ambayo ilibadilishwa jina ikaitwa Tanzania Bar.

Kwa wasiofahamu napenda kusema kuwa sehemu iliyoitwa Biafra ni sehemu wanayoishi zaidi watu wa kabila la Igbo. Kutokana na siasa za Nigeria, ambamo ukabila una nafasi kubwa sana, dhuluma dhidi ya waIgbo, ikiwemo wengi kuuawa, hasa sehemu za kaskazini mwa Nigeria, ndio kitu kilichosababisha wakakimbilia kwao na kujitangaza kuwa ni taifa huru la Biafra. Chinua Achebe, ambaye alifariki hivi karibuni, na Chimamanda Ngozi Adichie ni wa kabila hilo.

Kwa kumalizia, bora niseme tu kwamba kuliko kusimuliwa, ni bora mtu ujipatie nakala ujisomee. Nasema hivyo nikijua fika kwamba ushauri huu hauna maana kwa jamii ya wa-Tanzania, kwani utamaduni wa kununua vitabu na kuvisoma haupo. Kuna uwezekano mkubwa kwamba ushauri wangu utazingatiwa na watu wa nchi zingine kama vile Kenya, ambayo ni makini kwa masuala ya aina hiyo.

Monday, July 1, 2013

Makala ya "New York Times" Yaongelea Udhalimu Tanzania

Nicholas Kulish wa gazeti la New York Times amechapisha makala kuhusu vitendo viovu ambavyo vimekuwa vikifanyika Tanzania, vitendo ambavyo ni ukiukwaji wa haki za binadamu. Isome makala hiyo hapa

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...