Thursday, December 29, 2016

Vitabu Tulivyosoma Mwaka 2016

Zikiwa zimebaki siku mbili tu kabla ya kwisha mwaka 2016, nimeona wa-Tanzania kadhaa wakijitokeza katika mtandao wa Facebook na kutaja vitabu walivyosoma mwaka huu. Jambo hili limenifurahisha, nikizingatia kuwa nimekuwa nikihamasisha usomaji wa vitabu, kwa kutumia blogu yangu hii, blogu za wengine, na pia katika kitabu changu, CHANGAMOTO: Insha za Jamii.

Ninawapongeza watu hao kwa kuonyesha mfano mzuri. Ninawapongeza pia wasomaji waliojitokeza na kuchangia suala hili kwa namna mbali mbali, kama vile kuvijadili vitabu hivyo, kuulizia upatikanaji wake, au kupendekeza vitabu vingine. Kuhusu upatikanaji wa vitabu, watu wamepeana taarifa za maduka ya vitabu, na pia upatikanaji wa vitabu pepe mtandaoni. Ni jambo la kuvutia kwamba kuna wa-Tanzania wanaotambua matumizi ya manufaa ya tekinolojia ya mtandao.

Mazungumzo haya yameonyesha mambo kadhaa. Jambo moja ni kuwa wako wa-Tanzania wanaojibidisha kusoma vitabu. Jambo jingine ni kuwa wanasoma vitabu vya aina mbali mbali, kama vile vya siasa, ujasiriamali, fasihi, na maendeleo ya jamii au ya mtu binafsi. Vile vile wanasoma vitabu vya waandishi wa mataifa mbali mbali, vya ki-Swahili na vya ki-Ingereza. Jambo jingine ni kuwa wahusika wameonyesha moyo mkubwa wa kusaidiana, kama vile kwa kufahamishana vitabu bora na hata kuazimishana vitabu.

Ninawaenzi watu hao. Huenda wakawa chachu ya kustawisha utamaduni wa kusoma vitabu nchini Tanzania. Laiti watu wengi zaidi wangejumuika katika safari hii. Laiti kama watu maarufu nchini mwetu, kama vile wanasiasa na wasanii, wangejiunga na kuwa wahamasishaji wa usomaji wa vitabu. Kutokana na mvuto wa wasanii wetu, kwa mfano, wangeweza kuwa wahamasishaji wa watoto na vijana katika kupenda kusoma vitabu.

Kwa upande wangu, naona sihitaji kuorodhesha vitabu nilivyosoma mwaka 2016. Mara kwa mara, katika blogu hii au blogu ya ki-Ingereza, ninaandika taarifa za baadhi ya vitabu ninavyosoma. Vingine ni vile ninavyofundisha chuoni St. Olaf, na vingine ni vile ninavyojisomea mwenyewe. Ninapoandika  taarifa, ninajitahidi kuelezea upekee au ubora wa vitabu hivyo.

Tuesday, December 27, 2016

Nimejutia Kusoma "Hamlet" Wakati wa Sikukuu

Siku kadhaa zilizopita, nilianza kusoma Hamlet, tamthilia ya Shakespeare, kama nilivyoandika katika blog ya ki-Ingereza. Tamthilia hii haikuwa ngeni kwangu. Ni moja ya tungo za Shakespeare ambazo nimezifahamu au kuzisoma tangu ujana wangu.

Lakini kuna jambo ambalo sikulizingatia nilipoamua kusoma Hamlet wakati huu, ambao ni wa sikukuu ya Krismasi. Ulikuwa si wakati muafaka wa kusoma Hamlet, hadithi yenye matukio ya kusikitisha. Mkondo mkuu wa hadithi hii ni jinsi baba ya Hamlet alivyouawa na ndugu yake, mfalme Claudius, ambaye miezi miwili tu kufuatia msiba huo alimwoa mama yake Hamlet. Mambo haya yanampa Hamlet msongo mkubwa wa mawazo.

Mzimu wa marehemu baba yake unamtokea Hamlet na kumweleza ufedhuli uliofanyika na kisha kumwelekeza alipize kisasi. Hamlet anatafakari afanye nini. Hasira na huzuni zake anazieleza kwa hisia na ufasaha tena na tena, kwa mfano katika tamko hili:

Ham. O that this too too solid flesh would melt
Thaw and resolve itself into dew!
Or that the Everlasting had not fixed
His canon 'gainst self-slaughter! O God! God!
How weary, stale, flat, and unprofitable
Seem to me all the uses of this world!
Fie on't! ah, fie! 'Tis an unweeded garden
That grows to seed; things rank and gross in nature
Possess it merely. That it should come to this!
But two months dead--nay, not so much, not two!
So excellent a king, that was to this
Hyperion to a satyr; so loving to my mother
That he might not beteem the winds of heaven
Visit her face too roughly. Heaven and earth!
Must I remember? Why, she would hang on him
As if increase of appetite had grown
But what it fed on; and yet, within a month--
Let me not think on't! Frailty, thy name is woman!
....
              Act I. Sc. II

Tafakari yake inamfanya hata ajiulize kama aendelee kuishi na kupambana na masaibu ya maisha kwa mategemeo ya kuyamaliza, au atoe uhai wake, kama tunavyomsikia katika tamko hili maarufu sana:

Ham. To be, or not to be, that is the question:
Whether 'tis nobler in the mind to suffer
The slings and arrows of outrageous fortune
Or to take arms against a sea of troubles,
And by opposing end them. To die--to sleep--
No more; and by a sleep to say we end
The heartache, and the thousand natural shocks
That flesh is heir to. 'Tis a consummation
Devoutly to be wished. To die--to sleep.
To sleep--perchance to dream: ay, there's the rub!
For in that sleep of death what dreams may come
When we have shuffled off this mortal coil,
Must give us pause....
                                              Act. III. Sc. I

Ili kuzipata vizuri hisia za Hamlet, tushuhudie jinsi Laurence Olivier alivyoliigiza tamko hili la pili, katika filamu ya mwaka 1948, ambayo niliiangalia kwa mara ya kwanza mwaka 1971, nilipokuwa Mkwawa High School, Tanzania:

Tuesday, December 20, 2016

Zawadi ya Krismasi

Siku tatu zilizopita, jirani yangu m-Marekani, mama mwenye umri zaidi yangu, aliniomba nimsainie nakala za kitabu cha Africans and Americans Embracing Cultural Differences. Alikuwa amevinunua kwa ajili ya kuwapelekea rafiki zake, wa-Marekani wenzake, kama zawadi ya Krismasi.

Jambo hili lilitosha kunifanya niandike ujumbe katika blogu yangu, kwani linadhihirisha jadi ninayoiona hapa Marekani, kama nilivyowahi kudokeza katika blogu hii. Lakini nimehamasika kuandika baada ya kusoma makala ambayo ameichapisha Christian Bwaya katika blogu yake. Ameelezea umuhimu wa zawadi kwa watoto na mambo ya kuzingatia katika kutoa zawadi kwa watoto.

Kati ya mifano ya zawadi alizotaja ni vitabu. Ni jambo muhimu, nami kama mwalimu ninaliafiki moja kwa moja. Nimejionea jinsi watoto wanavyopenda vitabu, sio tu hapa Marekani, bali pia Tanzania. Nimeandika mara kwa mara umuhimu wa kuwasomea watoto vitabu na kuwajenga watoto katika utamaduni wa kusoma vitabu. Huwa ninafarijika ninaposoma taarifa za uhamasishaji wa suala hilo.

Tutakuwa tumepiga hatua kubwa iwapo tutajijengea utamaduni wa kuwanunulia watoto vitabu kama zawadi, kwani wanavipenda vitabu. Tutakuwa tumepiga hatua iwapo vijana wetu na watu wa kila rika watakuwa na utamaduni wa kuthamini zawadi ya vitabu.

Friday, December 16, 2016

Dunia Yetu ya Maigizo

Shakespeare alisema, tena na tena, kuwa dunia ni jukwaa la maigizo ambapo kila mtu hujitokeza na kuigiza nafasi yake na kisha hutoweka zake. Maelezo haya naona ni kianzio muafaka cha kutafakari mambo ya dunia yetu. Ili kuchangia tafakari hiyo, nanukuu Hamlet, tamthilia maarufu ya Shakespeare, kutoka onyesho la 2, sehemu ya 2, ambapo tunasikia maongezi baina ya Polonius na Hamlet:

   Pol. My lord, I have news to tell you.
   Ham. My lord, I have news to tell you: when Roscius was an actor in Rome--
   Pol. The actors are come hither, my lord.
   Ham. Buzz, buzz!
   Pol. Upon my honor--
   Ham. Then came each actor on his ass--
   Pol. The best actors in the world, either for tragedy, comedy, history, pastoral, pastoral-comical, historical pastoral, tragical-historical, tragical-comical-historical-pastoral; scene individable, or poem unlimited, Seneca cannot be too heavy, nor Plautus too light. For the law of writ and the liberty, these are the only men.

Tangu zamani, nimevutiwa na ufafanuzi wa Polonius wa aina za maigizo. Kwa upande moja, naona kama analeta dhihaka nyepesi au kejeli, ingawa siwezi kudai kuwa ninaweza kuthibitisha jambo hilo. Ila kwa kweli anasisimua akili yangu.

Katika taaluma ya fasihi, inaeleweka kuwa ni juu ya kila msomaji kutumia ufahamu wake kuchambua kazi ya fasihi. Ufahamu huo unaweza kujumlisha mambo mengi, kama vile ufahamu wa fasihi, falsafa, na saikolojia. Matokeo ya kuchambua kazi ya fasihi hayabashiriki, na kwa kuwa kila msomaji ana upeo tofauti wa ufahamu, ni wazi kuwa kila msomaji wa kazi ya fasisi ataielewa kwa mtazamo tofauti.

Ukiwauliza wasomaji mbali mbali maana ya kazi fulani ya fasihi, utegemee kusikia majibu na maelezo tofauti, isipokuwa kama hao wasomaji wanafanya ukasuku. Kwa bahati mbaya, ukasuku huu umeshamiri miongoni mwa wengi. Hata katika blogu hii ya hapakwetu, wanajitokeza watu wanaoulizia maana ya kazi ya sanaa. Wanategemea niwape uchambuzi, kwa imani kwamba fasihi ni kama dini, ambamo kuna imamu au padri mwenye majawabu ya masuali ya waumini.

Baada ya maelezo haya, narejea tena kwenye ujumbe wangu wangu wa awali hapo juu, pamoja na nukuu niliyoiweka kutoka katika tamthilia ya Hamlet. Ninaona ni changamoto na kichocheo murua cha fikra.


Wednesday, December 14, 2016

Wosia wa Rabindranath Tagore Kuhusu Uhuru wa Kutoa Maoni

Rabindranath Tagore ni mmoja wa waandishi maarufu kabisa waliowahi kuishi. Alizaliwa mwaka 1861 Calcutta na kufariki 1941. Aliheshimika duniani kote wakati wa uhai wake na bado anaheshimika. Aliandika mashairi, tamthilia, insha, riwaya, hadithi fupi, na pia maelfu ya barua. Niliwahi kufundisha utungo wake maarufu Gitanjali, hapa chuoni St. Olaf.

Tagore alikuwa mwalimu aliyetukuka, kioo cha ubinadamu wa kweli ("humanism"), mwenye fikra pevu na nzito juu ya maisha na maadili. Watu maarufu kama W.B. Yeats, Mahatma Gandhi na Albert Einstein, walimmwenzi sana. Mwaka 1913 alipata tuzo ya Nobel katika fasihi. Nina vitabu vyake vitatu, kimojawapo kikiwa Rabindranath Tagore: An Anthology.

Kutoka katika kitabu hiki nimenukuu sehemu ya ujumbe wa tarehe 25 Septemba, 1930, kwa gazeti la Izvestia la Urusi. Ni ujumbe unaopaswa kutafakariwa na kuzingatiwa, tunaposhuhudia ukandamizaji wa uhuru wa watu kujieleza. Ili kuufikisha ujumbe kwa watu wasiojua ki-Ingereza, nimejaribu kuutafsiri.

     There must be disagreement where minds are allowed to be free. It would not only be an uninteresting but sterile world of mechanical regularity if all our opinions were forcibly made alike. If you have a mission which includes all humanity, you must, for the sake of that living humanity, acknowledge the existence of differences of opinion. Opinions are constantly changed and re-changed only through the free circulation of intellectual forces and moral persuasion. Violence begets violence and blind stupidity. Freedom of mind is needed for the reception of truth; terror hopelessly kills it. The brute cannot subdue the brute. It is only the man who can do it.

Tafsiri

     Lazima pawepo na kutokubaliana mahali ambapo akili zinaruhusiwa kuwa huru. Dunia itakuwa sio tu haipendezi bali tasa yenye kwenda kwa mwendo ule ule kama mashine, iwapo maoni yetu yote yatalazimishwa kufanana. Kama watu mna malengo yanayowahusu wanadamu kwa ujumla wao, sherti, kwa manufaa ya uhai wa jamii hiyo ya wanadamu, kutambua uwepo wa tofauti za maoni. Maoni hubadilishwa bila ukomo pale tu panapokuwa na mzunguko huru wa nguvu za akili na ushawishi wa mwenendo wa kimaadili. Mabavu huzaa mabavu na ujinga mithili ya upofu. Uhuru wa akili unahitajika ili ukweli upokelewe, na vitisho huua kabisa ukweli huo. Hayawani hawezi kumdhibiti hayawani. Ni binadamu tu ndiye anaweza.

Monday, December 12, 2016

Leo Nimemaliza Kufundisha Muhula wa Kwanza

Leo nimemaliza kufundisha muhula wa kwanza. Nilikuwa ninafundisha kozi tatu: "First Year Writing," "African Literature," na "Muslim Women Writers." Nilihitimisha ufundishaji wa "First Year Writin"g wiki iliyopita, ili kuwapa wanafunzi muda wa kuandika insha kuu ya mwisho. Katika kozi hii, ninafundisha uandishi bora wa ki-Ingereza, na uangalifu unaotakiwa katika vipengele vyote , kuanzia neno, hadi sentensi, hadi insha.

Katika African Literature tumemalizia muhula tukisoma riwaya ya Mia Couto, The Tuner of Silences. Mia Couto ni mwandishi wa Msumbiji, ambaye ni maarufu sana. Amepata sifa na tuzo kem kem, ikiwemo tuzo ya Neustadt. The Tuner of Silences ni riwaya inayosisimua akili kwa jinsi ilivyosheheni ubunifu wa kisanaa na kifikra.

Kuna mengi ya kutafakari katika riwaya hii, hasa yatokanayo na dini, fasihi linganishi, historia, falsafa kama vile "existentialism," na mikondo ya falsafa ya sanaa kama vile "surrealism."  Vile vile, taaluma ya saikolojia, kama vile mkondo wa "psychoanalysis," inasaidia kutafakari dhamira zilizomo. Kuisoma na kuufaidi utajiri wa riwaya kama The Tuner of Silences kunahitaji upeo mpana wa mawazo ambao unatokana na kusoma kwingi, sio tu fasihi bali taaluma mbali mbali.

Katika kuiongelea The Tuner of Silences darasani, nimesisitiza jambo hilo, Nimefundisha wanafunzi umuhimu wa kuzingatia nadharia za usomaji kama zilivyoelezwa na Cleanth Brooks katika insha yake, "The Language of Paradox," na pia zilivyoelezwa na Roland Barthes katika kitabu chake kiitwacho S/Z: An Essay.

Katika kozi ya "Muslim Women Writers," tumemalizia muhula tukisoma riwaya ya Monica Ali, Brick Lane. Ni riwaya ndefu, inayoelezea maisha ya watu wa Bangladesh ambao wanaishi Uingereza. Ni jamii ya ki-Islam, na tunaiona inavyojitahidi kustahimili na kustawi katika mazingira ya ugenini.

Hii ni jamii kama jamii zingine, yenye watu wenye maadili mema na ari ya kuwa mfano kwa wengine, na pia wako ambao tabia zao zina walakini. Wanapenda kufuatilia habari za wenzao, na ni wapiga majungu. Tofauti baina ya utamaduni wao na ule wa wa-Ingereza zinajitokeza, na pia tofauti baina ya vijana na watu wazima au wazee. Vijana wanaonekana kuiga mambo ya vijana wa kizungu, yakiwemo ambayo si mazuri.

Kufundisha kazi ya fasihi kutoka Bangladesh imekuwa ni fursa ya kuelezea historia ya fasihi ya nchi hiyo, ukiwemo mchango mkubwa wa Rabindranath Tagore, mwandishi wa mashairi, tamthilia, riwaya, na insha, ambaye aliitwaa tuzo ya Nobel mwaka 1913. Kwa bahati nzuri, Tagore ametajwa katika Brick Lane, kwa jinsi alivyo hazina kwa watu wa Bangladesh. Lakini jambo la kuzingatia ni kuwa Tagore ni mwamba katika fasihi ya ulimwengu, aliyeheshimiwa na miamba wenzake kama vile W.B. Yeats wa Ireland, aliyekuwa na urafiki na mawasiliano na Tagore.

Leo, katika kuhitimisha kozi yetu ya "Muslim Women Writers," nimewaomba wanafunzi ushauri juu ya kuitumia tena riwaya hii siku za usoni, nitakapofundisha kozi hii. Wameniambia kuwa ni riwaya muhimu sana, ingawa inachukua muda sana kuisoma. Wameshauri kwamba nitakapofundisha tena kozi hii, Brick Lane iwe mwanzoni, wakati wanafunzi wakiwa bado hawajachoka na masomo. Riwaya zingine, ambazo ni fupi fupi, zije baadaye. Nimewashukuru kwa ushauri huo wa wanafunzi ambao wamepitia kozi yangu, nikizingatia kuwa adhabu ya kaburi aijuaye maiti.

Friday, December 9, 2016

The Rime of the Ancient Mariner: Samuel Taylor Coleridge

Jana na leo nimesoma The Rime of the Ancient Mariner, utenzi maarufu wa Samuel Taylor Coleridge, ambao ni moja ya tungo za ki-Ingereza nilizokuwa ninazipenda wakati wa ujana wangu, kama nilivyoandika katika blogu hii. Nimefurahi kuusoma tena, baada ya miaka mingi, wakati ambapo akili yangu imepevuka zaidi kutokana na kusoma tungo nyingi za fasihi.

Katika kusema hivi, ninakumbuka kauli ya mshairi William Wordsworth, katika shairi lake maarufu, "Lines Written a Few Miles Above Tintern Abbey," anavyoongelea namna alivyotembelea, katika utu uzima wake, eneo ambalo alilizoea alipokuwa kijana. Matokeo ya kufanya hivyo ni kwamba, ingawa hawezi tena kuyaona mazingira yale kwa hisia za ujanani, sasa anayaona kwa kutumia akili ya kiutu uzima. Aina zote mbili za maono anazienzi, ingawa zinatofautiana.

Nami ninajisikia hivyo hivyo katika kusoma wakati huu The Rime of the Ancient Mariner. Nimeweza kuuweka utungo huu katika mkabala wa tungo nilizosoma kwa miaka ya baina ya ujana wangu na umri nilio nao sasa. Ninawazia hadithi ya kale ya Misri iitwayo, "The Tale of the Shipwrecked Sailor," utenzi wa Odyssey wa Homer, hadithi za baharia Sindbad, riwaya ya Daniel Defoe, Robinson Crusoe; riwaya ya Herman Melville, Moby Dick; na Utenzi wa Masaibu.

Papo hapo, kutokana na utafiti na ufundishaji wa somo la "Folklore," nimetilia maanani vipengele vya The Rime of the Ancient Mariner kama usimuliaji wa hadithi, imani mbali mbali ambazo tunaziita ushirikina. Kuna imani kama vile juu ya macho kuwa na nguvu ya kichawi. Dhana hiyo inajitokeza mara kadhaa katika utenzi huu. Kwa mfano, mwanzoni kabisa mwa utenzi tunasoma:

It is an ancient Mariner,
And he stoppeth one of three.
'By thy long grey beard and glittering eye,
Now wherefore stopp'st thou me?

'The Bridegroom's doors are opened wide,
And I am next of kin;
The guests are met, the feast is set:
May'st hear the merry din.'

He holds him with his skinny hand,
'There was a ship,' quoth he.
'Hold off! unhand me, grey-beard loon!'
Eftsoons his hand dropt he.

He holds him with his glittering eye--
The Wedding-Guest stood still,
And listens like a three years' child:
The Mariner hath his will.

Kuanzia hapo, huyu baharia mkongwe anamsimulia kijana yaliyomsibu katika safari baharini, yeye na mabaharia wenzake. Ni kisa cha mikosi, majanga na vifo vya wenzake wote akasalimika yeye, na tangu hapo katika maisha yake, hupatwa na maumivu fulani nafsini mwake ambayo suluhu yake ni kumnasa mtu wa kumsimulia kisa chake.

The Rime of the Ancient Mariner ni kisa cha kusisimua. Coleridge anazisukuma hisia zetu kupitia hali mbali mbali: mshangao, hofu, masikitiko, na huruma. Pamoja na kwamba hatimaye tunafarijika kwa jinsi mzee huyu alivyonusurika, tunabaki na majonzi kwa vifo vya mabaharia wenzake. Baada ya kuelewa kisa kizima, tunaelewa kwa nini mzee huyu anamteka kwa uchawi wa macho yake kijana anayekwenda arusini na kumfanya asikilize kisa chake hadi mwisho.


Thursday, December 8, 2016

Tamko la CUF Kuelekea Maadhimisho ya Uhuru wa Tanganyika


Kesho, Alhamisi, tarehe 9 Disemba, 2016 ni siku ya maadhimisho ya miaka 55 ya Uhuru wa Tanganyika, Watanzania tunaadhimisha miaka 55 ya kuwa huru baada ya harakati za miaka mingi ya kudai uhuru wa nchi yetu kutoka kwa wakoloni waliotutawala.

The Civic United Front (CUF-Chama Cha Wananchi) kinaungana na wananchi wote katika kuadhimisha siku hii muhimu katika historia ya nchi yetu, na kutoa wito kwao kuendelea kusimamia malengo, dhamira, na nia za viongozi wetu katika kupigania Uhuru kama yalivyowahi kusema na kuainishwa kuwa ni kupambana na maadui wakubwa watatu ambao ni Umasikini, Ujinga, na Maradhi.

Sambamba na siku ya uhuru wa Tanganyika, tarehe 9 Disemba, ni siku ya maadhimisho ya kimataifa kuhusiana na waathirika wa mauaji ya halaiki na kuzuia jinai zake, (International Day of Commemoration and Dignity of the Victims of the Crime of Genocide and of the Prevention of this Crime) kama ilivyotangazwa na Umoja wa Mataifa (UN) kwa tamko lake namba (A/RES69/363). Tarehe hii ya 9 Disemba pia ni siku ya kimataifa kuadhimisha juhudi za kupinga na kupambana na rushwa, (Internatinal Anti Corruption Day) kama ilivyotangazwa na Umoja wa Mataifa (UN) kwa tamko lake namba (A/RES/58/4).

THE CIVIC UNITED FRONT (CUF-Chama Cha Wananchi) kinaungana na mataifa yote duniani kuadhimisha siku hizi na kuiahidi Jumuiya ya Kimataifa kuwa itaipa kila aina ya ushirikiano ili kufikia malengo ya kuanzishwa kwa maadhimisho ya siku hizo. Kwa kutumia mifano michache ya maadhimisho ya siku kama hizi za kimataifa juu ya jinai dhidi ya ubinadamu na kutamalaki kwa rushwa, na kufuatilia mwenendo wa matukio yanayoendelea kutokea katika nchi yetu kwa pande zote mbili za Muungano (Tanganyika na Zanzibar), inabainika kuwa malengo halisi ya mapambano ya kudai uhuru hayajafikiwa kama ilivyodhamiriwa na viongozi na majemedari walioongoza harakati za kudai uhuru na ukombozi wa nchi yetu. Kwa hakika, mapambano ya kudai Uhuru yamefanikiwa kwa kiwango kidogo mno cha kumuondosha mkoloni mzungu, na badala yake ndugu zetu na wananchi wenzetu wamejiweka katika nafasi hiyo kwa kuendeleza yaleyale aliyokuwa akiyafanya Mkoloni kwa takribani nchi zote za kiafrika. 

Wakati huu nchi yetu ikiwa inatimiza miaka 55 ya kuwa huru, kumeshuhudiwa uvunjifu mkubwa wa Haki za binaadamu, Ukandamizaji wa demokrasia uliochupa mipaka ikiwa ni pamoja na kupuuzwa na kuminywa kwa maamuzi ya kidemokrasia ya wananchi kuchagua viongozi wanaowataka, uvamizi, ushambuliaji na utekaji wa viongozi wa kisiasa, na utawala usiozingatia matakwa ya kisheria katika kuongoza kwake.

Katika siku za hivi karibuni hali imeendelea kuwa mbaya zaidi ambapo vyombo vya Ulinzi na Usalama, vyenye wajibu na jukumu la kulinda Raia na Mali zao, vimekuwa vikikubali kupokea amri na kutumiwa na wanasiasa wa Chama tawala na vibaraka wao kushiriki jinai mbalimbali kama vile kunyanyasa na kudhalilisha wananchi wasio na hatia kwa kuwabambikizia kesi, kuvamia, kupiga na kujeruhi wananchi na au kutoa ulinzi na kufanikisha njama za matukio hayo, kama inavyofanywa na kikosi cha askari kinachojulikana kwa jina la ‘Mazombi’ kisiwani Zanzibar na kushindwa kwa vyombo hivyo kuchukuwa hatua zozote za kisheria kwa wahusika wa uratibu na utekelezaji wa jinai hizi zinazofanywa wazi wazi.

Vitendo vyote hivi vinaashiria namna Viongozi wa CCM na Serikali yake walivyoshindwa kusimamia nia, dhamira na malengo ya Viongozi wetu waliopigania Uhuru. Bila ya shaka haya yote ni dalili na mwelekeo mbaya wa kuvurugika kwa amani ndani ya nchi yetu. The Civic United Front (CUF-Chama Cha Wananchi) inatowa wito kwa Serikali na viongozi wa CCM, kuheshimu na kuzingatia misingi ya HAKI, USAWA, DEMOKRASIA NA KUFATA UTAWALA WA SHERIA ili kuiepusha nchi yetu kuingia katika majanga yanayoweza kuepukika.

HAKI SAWA KWA WOTE

SALIM BIMANI

MKURUGENZI WA HABARI, UENEZI NA MAHUSIANO NA UMMA

MAWASILIANO: 0777 414 112 / 0752 325 227

Saturday, December 3, 2016

Msikilize Rais Yahya Jammeh Anavyokubali Ushindi wa Mpinzani

Msikilize Rais Yahya Jammeh wa Gambia anavyokubali matokeo ya uchaguzi wa urais ambayo mpinzani ameshinda. Rais Jammey, bila kusita, anasema kuwa kwa kura zao, wananchi wa Gambia wamenena, naye anayapokea matokeo. Anampongeza mpinzani kwa ushindi wake, na anaahidi kumpa ushirikiano kuanzia kipindi hiki cha mpito. Anamwombea baraka za Allah katika kuiongoza nchi ya Gambia, na anawashukuru watu wa Gambia.

Friday, December 2, 2016

Ndugu wa Uganda Anataka Kitabu

Kama ilivyo kawaida katika blogu hii, ninapenda kujiwekea kumbukumbu mbali mbali. Jana niliwatembelea akina mama wawili wa-Kenya waishio Brooklyn Park, Minnesota, ambao walitaka tukutane ili niweze kuwapa ushauri kuhusu fursa za kujiendeleza kielimu ya juu na katika ajira. Wakati tulipokuwa katika maongezi, waliwasiliana na bwana mmoja wa kutoka Uganda, wakamwita kuja kuungana nasi.

Tulizungumza kuhusu masuala mbali mbali, yakiwemo masuali waliyoniuliza juu ya ufundishaji na uandishi wangu. Mmoja wa hao akina mama nilikuwa nimemwahidi kumpa nakala ya kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Huyu jamaa wa Uganda aliniulizia namna ya kukipata kitabu kile, nikamweleza kuwa anaweza kukipata mtandaoni Amazon.com au lulu.com/spotlight/mbele, au kutoka kwangu. Nikamshauri kwamba kwa upnde wa gharama, ni rahisi zaidi kukinunua Amazon.com. Lakini yeye alisisitiza kuwa nimpelekee, akanipa na anwani yake.
,
M-Ganda huyu amenikumbusha wa-Ganda wengine niliokutana nao hapa Minnesota, wakajiptia kitabu changu. Mmoja ni Steven Kaggwa ambaye alikuwa anamiliki mgahawa wa Tam Tam. Baada ya kukisoma kitabu hiki, aliniambia kuwa aliwaelezea wafanya kazi wake. Mmoja wao, Sally, hakuishia tu kujinunulia nakala, bali alinunua nakala nyingine ambayo aliniambia alikuwa anampelekea mkuu wake wa kazi, ambaye ni m-Marekani. Niliguswa na taarifa ya huyu mama, kama nilivyoguswa miaka michache baadaye, wakati mama mmoja kutoka Togo alivyonunua nakala za kitabu hiki kwa ajili ya wakuu wa kazini kwake, kama nilivyoripoti katika blogu hii.

M-Ganda mwingine ninayemkumbuka nilikutana naye katika tamasha la vitabu ambalo nilikuwa ninashiriki. Alikuwa amefika kikazi hapa Minnesota, lakini alikuja kwenye tamasha hilo, na ndipo tulipofahamiana. Bila kusita alinunua kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differenes, akaenda zake. Yeye na hao wengine wameniacha nikitafakari jinsi hao wenzetu walivyo. Ninaona kuwa sio tu wameenda shule, bali wameelimika, kwani uthibitisho wa kuelimika ni kuwa na hamu ya kutafuta elimu hata baada ya kumaliza shule.

Thursday, December 1, 2016

Maandalizi ya Wanachuo wa Gustavus Adolphus Waendao Tanzania

Jana nilipata ujumbe kutoka kwa Profesa Barbara Zust wa Chuo cha Gustavus Adolphus akiulizia iwapo nitaweza kwenda kuongea na wanafunzi wanaojiandaa kwenda naye Tanzania kwa safari ya kimasomo. Ameniambia kuwa watakuwa na kikao cha maandalizi ya safari tarehe 2 na 3 Januari, katika kituo cha mikutano cha Mount Olivet. Nimefanya mazungumzo hayo tena na tena miaka iliyopita.

Katika ujumbe wake, Profesa Zust amekumbushia kuwa, kama ilivyo jadi, wanafunzi hao watakuwa wameshasoma kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Pia amekumbushia jinsi wanafunzi wanavyoshukuru na kufurahia kwamba wanapokuwa Tanzania wanakutana na yale ambayo ninakuwa nimewaeleza kitabuni na katika mazungumzo.

Taarifa hii ni muhimu kwangu, na ndio maana ninaiweka hapa katika blogu yangu, kama kumbukumbu. Kwa kuzingatia umuhimu wa suala hili, nimeitika mwaliko wa Profesa Zust na kumwambia kuwa nitakwenda kukutana nao tarehe 2 Januari. Kama kawaida, panapo majaliwa, nitaandika taarifa katika blogu hii.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...