Saturday, November 30, 2019

Wadau wa Utalii wa Kielimu Tumekutana

Tarehe 2 Novemba nilikutana na mama Georgina, ambaye anatoka Ghana na ni mmiliki wa kampuni iitwayo African Travel Seminars. Anapeleka wasafiri kwenda nchi za Afrika, kuanzia kaskazini, hadi kusini, mashariki hadi magharibi, na Tanzania imo. Mbali ya kuwaonesha vivutio vya utalii, anawaelimisha kuhusu maisha na tamaduni za waAfrika.

Niliifahamu kuhusu kampuni yake kuanzia miaka ya tisini na kitu, nikaona jinsi shughuli zake zinavyofanana na zangu, ambazo zimeelezwa katika tovuti ya Africonexion. Hivi karibuni nilianza kuwasiliana na huyu mama, na tukapanga kukutana.

Kabla hatujakutana, mama huyu alisoma kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Ameamua awe anawapa wageni anaowapelea Afrika. Yeye nami tunafahamu kuwa hii itawawezesha wageni kuelewa mwenendo na tabia za waAfrika na pia kujielewa namna wao wenyewe wanavyoeleweka kwa mtazamo wa waAfrika.

Tumejithibitishia kuwa malengo yetu yanafanana. Tunapenda kuendeleza elimu kuhusu Afrika kwa waMarekani na tunapenda kujenga maelewano baina ya waMarekani na waAfrika. Yeye nami tuna uzoefu wa kuongelea masala haya hapa Marekani, kwa wanafunzi na walimu, watu wanaoenda Afrika kwa shughuli za kujitolea, watalii, nakadhalika.

Thursday, November 14, 2019

Kijana Msomali Amekipenda Kitabu Hiki

Jana, nilikuwa posta hapa chuoni nikipata huduma. Ghafla nikasikia kwa nyuma ninaitwa, "Professor Mbele!" Nilipinduka nikamwona kijana mmoja, mwanafunzi wetu mSomali ananisogea. Aliniambia amesoma kitabu changu, akimaanisha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Nilifurahi, ila sikujua nimwambie nini, ila aliongezea kuwa alitamani kipatikane kama "audio book" ili mama yake aweze kusikiliza. Niliguswa sana, kwa sababu ninaelewa hali ya waSomali hapa Minnesota na Marekani kwa ujumla.

Wako wengi sana, wakimbizi au wahamiaji kutoka nchini kwao. Jimbo hili la Minnesota lina idadi kubwa ya waSomali kuliko sehemu nyingine duniani ukiachilia mbali Somalia yenyewe.

Ninafahamu pia kuwa waSomali hawakuwa na jadi ya maandishi. Utamaduni wao ni wa masilimuzi. Walipata mwafaka wa namna ya kuandika lugha yao mwaka 1972. Watu wazima wengi hawajui kuandika na kusoma, na wazee ndio kabisa.

Wote hao wako hapa Marekani, ambapo utamaduni ni wa maandishi. Ninafahamu changamoto zinazowakabili, kwani nina uzoefu katika masuala yao, ikiwemo fasihi simulizi na elimu. Kijana huyu alivyoniambia kuhusu mama yake, niliguswa sana. Nimeshampelekea ujumbe rafiki yangu mSomali kumwelezea suala hilo. Huyu tulishaongelea kutafsiri kitabu changu kwa kiSomali. Nimemwambia kuwa kutokana na kauli ya huyu kijana ya kutaka mama yake asome kitabu hiki, inabidi tukamilishe tafsiri halafu irekodiwe kama "audio book." Itachukua muda, lakini hii si hoja.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...