Thursday, October 25, 2018

Nimepeleka Vitabu kwa wa-Matengo

Mwezi Julai mwaka huu nilikwenda Tanzania, nikiwa nimechukua vitabu vingi. Baadhi ni vile nilivyoandika mwenyewe, ambavyo niliviwasilisha katika maduka ya Kimahama, na A Novel Idea. Nilichukua pia nakala 16 za Matengo Folktales kwa ajili ya kuzipeleka kwa wa-Matengo, wilayani Mbinga, katika mkoa wa Ruvuma.

Ninasema hivyo, na kutaja kabila langu, nikijua kwamba kwetu wa-Tanzania, hii ni kauli tata, isiyopendeza, kwani inaashiria upendeleo au ubaguzi kwa msingi wa kabila. Utamaduni wa Tanzania, uliojengwa na chama cha TANU, hauafiki ubaguzi wa makabila au wa aina nyingine. Sasa kwa nini nimetoa kauli hiyo? Kwa nini niliamua kupeleka nakala hizi za Matengo Folktales kwa wa-Matengo? Napenda kuthibitisha kwamba nilifanya jambo muafaka.

Matengo Folktales ni mkusanyo wa hadithi za jadi ambazo nilizirekodi nyumbani u-Matengo miaka ya sabini na kitu. Nilizirekodi katika kaseti, kisha nikachagua hadithi kumi na kuzitafsiri kwa ki-Ingereza. Niliandika uchambuzi wa kila hadithi na nikaongezea insha ya kitaaluma kuhusu hadithi. Huu ukawa ni mswada ambao ulichapishwa kama Matengo Folktales.

Mimi ni mwanataaluma katika taaluma hii inayojulikana kama "Folklore." Kama ilivyo katika taaluma zingine, tuna taratibu na maadili ya utafiti, uandishi na uchapisahji. Kati ya hayo ni utaratibu wa kuwarudushia fadhila watu wanaowezesha utafiti wetu. Watafiti tusiwe tunachukua yale tunayopewa bila kuwarejeshea kwa namna moja au nyingine wale wanaotupa hayo tunayotafuta. Dhana hiyo huitwa "reciprocity" kwa ki-Ingereza.

Kuna nämna mbali mbali za kurudisha fadhila, kufuatana na mila na desturi za mahali husika na kufuatana na ridhaa ya mtu binafsi anayetuwezesha. Kuna namna mbali mbali za kutoa shukrani. Kwa upande wangu, na kwa watafiti wengi, namna bora kabisa ya kurudisha fadhila ni kuwapa nakala ya yale ninayorekodi na kuondoka nayo, kama vile kaseti au picha ninazopiga.

Kwa msingi huo, baada ya kuchapisha Matengo Folktales, nilijua kwamba nina wajibu wa kupeleka nakala kwa wa-Matengo. Kwa kuwa nimechapisha kitabu kwa ki-Ingereza, ilibidi nisubiri hadi ipatikane sehemu muafaka ya kupeleka.

Fursa imepatikana kwa kuwepo kwa shule za sekondari. Hizi nakala 16 nilimkabidhi mwalimu Frank Kinunda mjini Mbinga, baada ya mawasiliano naye, naye amezisambaza kwenye hizo shule. Zitawaelimisha vijana na walimu kuhusu utamaduni wa wahenga, na pia kuhusu taaluma ya "Folklore." Vile vile, kwa kuwa  nimeandika kwa uangalifu mkubwa kama mwalimu wa lugha ya ki-Ingereza, Matengo Folktales ni kitabu cha kujiongezea ujuzi wa ki-Ingereza. Kitabu hiki kinatumika kufundishia katika vyuo hapa Marekani, na ninafurahi kimeanza kuwa mikononi mwa wanafunzi na walimu Tanzania

Sunday, October 21, 2018

Minnesota Black Authors Expo Imekaribia

Bado siku sita tu hadi maonesho yaitwayo Minnesota Black Authors Expo yatakapofanyika. Hii ni mara ya pili kwa maonesho haya kufanyika. Mara ya kwanza ilikuwa mwaka jana.

Waandaaji waliniomba niwemo katika jopo la waandishi watakaoongelea masuala mbali mbali ya uandishi wa vitabu. Nilikubali. Jopo linategemewa kuwa kivutio kikubwa katika tamasha hilo.

Friday, October 19, 2018

Waandishi Marafiki Tumekutana

Tarehe 13 mwezi huu, nilishiriki tamasha la vitabu liitwalo Deep Valley Book Festival mjini Mankato, jimbo hili la Minnesota. Nilishahudhuria mara tatu tamasha hili linalofanyika mara moja kwa mwaka. Nilijua kuwa mmoja wa waandishi ambao walikuwa mbioni kushiriki ni rafiki yangu Becky Fjelland Brooks anayeonekana pichani kushoto.

Becky ni mwalimu katika South Central College hapa Minnesota. Tulianza kufahamiana wakati yeye na Profesa Scott Fee wa Minnesota State University Mankato waliponialika kwenda kuongea na wanafunzi waliokuwa wanawaandaa kwa safari ya masomo Afrika Kusini.

Watu wengi walihudhuria mhadhara wangu kuhusu tofauti za tamaduni, na nakala nyingi za kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences zilinunuliwa. Baada ya hapo, nimepata mialiko ya kwenda kuongea na wanafunzi hao kila mara wanapoandaliwa safari ya Afrika Kusini.

Mwalimu Becky ni mmoja wa wale wa-Marekani ambao wanaipenda Afrika na wanajibidisha kuwaelimisha wenzao kuhusu Afrika. Kuandaa programu za kupeleka watu Afrika ni kazi ngumu, yenye changamoto nyingi. Inahitaji ujasiri na uvumilivu. Nina uzoefu wa shughuli hizo, na ninawaenzi watu wa aina ya mwalimu Becky.

Mwalimu Becky ni mwandishi mwenye kipaji. Tayari ameshachapisha vitabu kadhaa, kwa ajili ya watoto, vijana, na watu wazima. Umaarufu wake unaongezeka mwaka hadi mwaka, na ameshatambuliwa na tuzo kama Midwest Book Awards. Ni faraja kwangu kwamba mwalimu Becky, mwandishi maarufu, anakipenda sana kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, na anaipenda mihadhara yangu, kama inavyonekana hapa na hapa.

Hii tarehe 13, kwa kuwa mwalimu Becky na mimi tulifahamu kuwa tungekutana, nilichukua nakala yangu ya kitabu chake kiitwacho Slider's Son ili anisainie. Ninavyo vitabu vyake vingine ambavyo alivisaini siku zilizopita. Tulifurahi kukutana. Ninajiona nimebarikiwa kuwa na rafiki kama huyu. Picha hiyo hapa juu aliiweka Facebook akiwa ameambatisha ujumbe huu: "With my dear friend Joseph Mbele, author of the enlightening and humorous book, "Africans and Americans," sharing stories and friendship at the Deep Valley Book Festival today...."

Thursday, October 18, 2018

Kitabu Bado Kiko Dukani Barnes and Noble

Juzi nilienda Apple Valley na Burnsville kuangalia maduka ya vitabu, kama nilivyoandika katika blogu hii. Kule Burnsvile, mji jirani na Apple Valley, nilitaka kuingia katika duka la Barnes and Noble ambamo kitabu changu kilikuwa kimewekwa sehemu maalum ya vitabu vilivyopendekezwa na wahudumu wa duka, kama nilivyoripoti katika blogu hii.

Sikujua kama ningekikuta, kwani sijui utaratibu wanaofuata katika kuvionesha vitabu hivyo sehemu hiyo. Nilidhani labda vinawekwa kwenye kabati hili kwa wiki moja hivi. Nilishangaa kukiona kitabu changu bado kipo, na kimewekwa juu zaidi ya pale kilipokuwepo kabla. Hapa kushoto ni picha niliyopiga wiki iliyopita, na kulia ni picha niliyopiga juzi. Ninafarijika na kufurahi kukiona hapa. Ninasubiri siku ya kwenda kukiongelea, kama nilivyodokeza.

Tuesday, October 16, 2018

Vitabu Nilivyonunua Leo

Leo niliamua kutembelea maduka ya vitabu kwenye miji ya Apple Valley na Burrnsville hapa Minnesota. Apple Valley, kwenye duka la Half Price Books,  nilinunua vitabu vitatu bila kutegemea. Nilipita sehemu ya vitabu vya Hemingway, ambapo sikuona kitabu kigeni kwangu. Nilienda sehemu ya bei nafuu, nikanunua vitabu vitatu.

Kimoja ni Essays and Poems cha Ralph Waldo Emerson, kilichohaririwa na Tony Tanner. Kwa miaka mingi nimefahamu jina la Emerson. Nilifahamu kuhusu insha yake "Self Reliance," ingawa sikuwa nimewahi kuisoma. Nilifahamu pia kuwa ameathiri sana falsafa na uandishi, sio tu Marekani, bali kwingineko. Kwa hali hiyo, sikusita kununua kitabu hiki, hasa baada ya kuona kuwa kina mashairi ya Emerson. Sikujua kuwa alitunga mashairi.

Kitabu kingine nilichonunua ni Collected Poems cha Edna St. Vincent Millay. Huyu ni mwandishi ambaye sidhani kama niliwahi kusikia hata jina lake. Lakini nilipoona hiki kitabu kikubwa sana chenye kurasa 757 na nyongeza ya kurasa 32, na halafu nikasoma taarifa za huyu mwandishi, kwamba alikuwa mwanamke mwenye kujiamini na uthubutu katika utunzi wa ma shairi, na mwanaharakati ambaye katika mazingira ya miaka ya 1920 kuelekea 1930 alikuwa akitetea uhuru wa mtu binafsi na hasa wanawake, na halafu nikaona alipata tuzo maarufu ya uandishi iitwayo Pulitzer Prize mwaka 1923, niliona lazima ninunue kitabu hiki, ili nifaidi utunzi wa mama huyu.

Si kawaida kukutana na tungo za wanawake wa zamani namna hiyo hapa Marekani. Tungo ya mwanzo kabisa ambayo nimewahi kusoma na kuifundisha ni The Awakening, ya Kate Chopin. Hiyo ni riwaya ya mwanzo mwanzo inayotambulika kama ya kifeministi. Kutokana na kufahamu kiasi fulani harakati za wakati ule, nilivutiwa na kitabu hiki cha mashairi ya Edna St. Vincent Millay, ambaye alikuja baada ya Kate Chopin.

Kitabu cha tatu nilichonunua ni The Mother, cha Maxim Gorky, kilichotafsiriwa na Hugh Aplin. Maxim Gorky ni mwandishi wa zamani wa Urusi. Nilipoona kitabu hiki, nilikumbuka enzi zangu kama mwanafunzi katika idara ya "Literature" ya chuo kikuu cha Dar es Salaam, ambapo mwalimu wetu Mofolo Bulane alitufundisha nadharia ya fasihi kwa mtazamo wa ki-Marxisti.

Katika mafundisho yale alituwezesha kufahamu kuhusu waandishi wengi, wakiwemo wa Urusi, kama vile Leo Tolstoy, Fyodor Dostoyevsky, Maxim Gorky, Vladimir Mayakovsky, Anna Akhmatova, na Mikhail Sholokhov. Tulijifunza kuwa Gorky ni moja wa waandishi waanzilishi wa mkondo wa "Socialist Realism," ambao ulifuatwa baadaye na akina Mayakovsky na Ana Akhmatova na wengine. Kutokana na kumbukumbu hizi za ujana wangu, niliamua kununua kitabu hiki ili niweze kukisoma nitakapopata wasaa. Baada ya kununua vitabu hivyo, nilielekea kwenye mji jirani wa Burnsville, kwenye duka la vitabu la Barnes Noble. Nitaandika juu ya safari hiyo wakati mwingine.

Saturday, October 13, 2018

Nimeshiriki Tamasha la Vitabu la Deep Valley

Leo nilienda Mankato, Minnesota, kushiriki tamasha la vitabu liitwalo Deep Valley Book Festival. Hii ilikuwa mara yangu ya nne kushiriki tamasha hilo. Ilikuwa fursa ya kuongea na watu kwa undani kuhusu mambo mbali mbali.

Kuna watu kadhaa ambao nawakumbuka zaidi. Mmoja aliniambia kuwa ana binti yake ambaye anafundisha ki-Ingereza kama lugha ya kigeni. Hapa Marekani somo hilo linajulikana kama English as a Foreign Language. Hufundishwa kwa wahamiaji ambao wanahijtaji kujia lugha hiyo, ambayo ndio lugha rasmi ya hapa Marekani. Nilichangia mada hiyo kwa kuelezea jinsi sgughuli ya kufundisha ESL inavyofungamana na suala la tamaduni. Hufundishi tu muuno, sarufi, istilahi, bali pia utamaduni wa mazungumzo.

Mama mmoja mzee, mwandishi, ambaye meza yake ilikuwa mbele yangu, alifika kunisalimia na kuongea. Nilimwuliza ameandika kuhusu nini, akaniambia kitabu chake kinahusu changamoto aliyopitita kufuatia binti yake kujitokeza kama mwenye silika ya mapenzi ya jinsia yake. Nilivyomwelewa huyu mama, ilikuwa ni changamoto kubwa kwake, na ndiyo aliyoandika kitabuni. Nilimwambia kuwa nami nilianza kuelewa suala hili la mapenzi ya jinsia moja nilipokuwa masomoni katika chuo kikuu cha Wisconsin-Madison, ambapo palikuwa na wana harakati wa aina mbali mbali. Nina nia ya dhati ya kukipata ta kiabu chake.

Kijana mmoja alikuja mezani pangu akaniambia kuwa anafuatilia habari za mwandishi Sinclair Lewis. Anamwigiza, yaani kujifanya yeye ndiye mwandishi huyo. Akaniuliza iwapo ataweza kupata wapi habari zaidi. Nikamwambia kuwa kwa bahati nzuri, Marekani ni Makini kwa kutunza taarifa za watu mashuhuri kama hao waandishi. Nilimwabia kuhus nyumba ya makumbusho ya Carl Sandburg, ambayo niliwahi kuitembelea, mjini, Galesburg, Illinois, na nyumba za makumbusho ya Ernest Hemingway ambayo niliwahi kutembelea mjini Oak Park, Illinois, na sehemu zingine, kama vile maktaba ya JF Kennedy ambayo niliwahi kuitembelea Boston.

Watu wamenieleza uzoefu wao wa kuishi na waAfrika hapa Marekani na kujione tofauti za tamaduni, kwa maana ya mienendo, namna ya kufikiri na kutenda. Mzee moja aliniambia kuwa ana jirani mSomali. Alinunua kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, nami nikamhimiza asikose kumwazimisha huyu mSomali asome.

Nami nimepata fursa ya kuwaeleza wat hao kuhu mialiko ninayopata kwenda sehemu mbali mbali kuelezea athari za tofauuti za tamaduni. Wakati wa kuongelea kitabu changu, nimeelezea mtindo wa uandishi niliotumia. Nimepata fursa ya kuongelea kitabu cha Matengo Folktales, pia, nilivyokiandaa kwa miaka mingi, tangu kurekodi hadithi hadi kuzitafsiri na kuzichambua, na hatimaye kuchapishwa. Sikukosa kuelezea kilivyotajwa mwezi November tarehe 23 katika kipindi cha TV ch Jeopardy. Nilikuwa nimechukua karatasi yenye tamko la Jeopardy a, ambao  hawakuweza kujibu/.

Mbali ya vitabu vyangu, nilichukua vitabu vya Bukola Oriola na kitabu cha mwanae Samuel Jacobs, mwenye umri wa miaka kumi na moja. Bukola Oriola niliwahi kumzungumzia katika blogu hii. Tangu nilipomwelekeza namna ya kuchapisha kitabu chake cha kwanza, amefika mbali. kwani aliteuliwa na Rais Obama kuwa katika United States Advisory Council on Human Trafficking.

Nimekutana na rafiki yangu Becky Fjelland Brooks, mwalimu wa South Central College, ambaye ni mpenzi mkubwa wa kitabu changu cha Africans and Americans, amewahi kunikalika mara kadhaa nikaongee na wanachuo wake. Akaandika taarifakadhaa, kama hii hapa na hii hapa.


Thursday, October 11, 2018

Mchakato wa Kwenda Kuongelea Kitabu

Leo nimepata ujumbe kutoka kwa Dan, ambaye hivi majuzi alikipigia debe kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, katika duka la Barnes and Noble, kama nilivyoelezea katika blogu hii. Anaendelea na juhudi yake. Ameandika:

Happy to spread the word about your book. Let me know if you are ever interested in doing a talk at our store. I can connect you with our manager.

Tafsiri yangu:

Ninafurahi kukitangaza kitabu chako. Nijulishe iwapo utapenda kuja kukiongelea katika duka letu. Nitaweza kukuunganisha na meneja wetu.

Kuwaalika waandishi kuongelea vitabu vyao ni utamaduni wa kawaida hapa Marekani. Ni fursa ya mwandishi kukutana na watu wanaotaka kujua mambo kama  historia ya mwandishi, changamoto za uandishi, falsafa na mawaidha yake kuhusu uandishi, na kadhalika. Vinakuwepo vitabu vya mwandishi, kwa watu kuvinunua na yeye kuvisaini. Wa-Marekani wanapenda kusainiwa vitabu, kama nilivyowahi kusema katika blogu hii.

Wednesday, October 10, 2018

Naambiwa Niongeze Bei ya Kitabu

Katika matamasha ya vitabu ninayoshiriki, ninakutana na mambo mengi, zikiwemo tabia na mitazamo ya wateja. Moja ambalo linanigusa zaidi ni pale mteja anaposhauri niongeze bei ya kitabu changu. Hiyo imetokea mara kadhaa, kuhusiana na vitabu vyangu viwili: Africans and Americans: Embracing Cultual Differences na Matengo Folktales.

Vitabu hivi ninaviuza kwenye matamasha kwa dola 14 kila kimoja. Kwa kujua kwamba watu wengine wanatoa  noti ya dola 20 au noti mbili za dola kumi kumi, ninajitahidi kuwa na chenji. Ajabu ni kwamba watu wengine hawasubiri chenji, na wengine wanakataa. Wanachotaka ni kitabu waende zao. Ninakumbuka watu waliowahi kutoa noti ya dola 20 bila kutaka chenji. Mmoja wa hao, nilipojiandaa kumpa chenji, alisema hiyo chenji ni shukrani yake kwangu kwa kuandika kitabu.

Tarehe 4 mwezi huu nilikutana na jambo jingine kabisa. Mama moja, Jackie, ambaye nimemfahamu miezi michache iliyopita na akasoma hivi vitabu vyangu viwili, alinialika kwenye mhadhara wa rafiki yake Maria kuhusu vitabu na maisha yake. Alikuwa ameniambi nije na nakala za vitabu vyangu, ili aweze kuvipeleka katika tamasha la vitabu. Baada ya mhadhara, wakati tulipokuwa tunajumuika kwa viburudisho na maongezi, Jackie akanulizia bei ya vitabu vyangu, nami nikamwambia kuwa ni dola 14. Alisema nipandishe iwe 15, kwa ulinganisho na kitabu cha dola 10 na pia kwa urahisi wa chenji.

Alinitambulisha kwa rafiki yake, akamwambia kuhusu hivi vitabu vyangu. Alivyokuwa akielezea hayo, akaniambia nivitoe kwenye begi, nikampa. Huyu rafiki alichagua Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, akapanda ngazi kwenda kuchukua hela akaja akanipa na kitabu akachukua. Dakika chache baadaye, mama huyu alinitambulisha kwa mama mwingine, na akamwambia kuhusu vitabu. Naye akanunua Matengo Folktales.

Kwa hivyo nimejikuta nikiafiki wazo la kuongeza bei ya vitabu vyangu. Hata hivyo, bei hiyo ni ndogo kulingana na bei za mahali pengine za vitabu hivyo. Ninaamini kuwa taarifa hii ina ujumbe kuhusu watu wanaothamini vitabu kuliko fedha. Kama nilivyowahi kusema tena na tena, blogu hii ni sehemu ambapo ninajiwekea mambo yangu binafsi, kama vile kumbukumbu, hisia, na mitazamo. Ikitokea haja, siku zijazo, ya kuandika kitabu kuhusu maisha na kazi zangu, blogu hii itakuwa chanzo muhimu cha taarifa.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...