Tuesday, July 25, 2017

Busara za Seneta McCain Muhimu kwa Tanzania

Ninavyoona, Tanzania sio tu inaelekea kubaya katika siasa na mahusiano ya jamii, bali imeshafikia pabaya. Taifa limepasuka. Badala ya siasa za kizalendo, zinazozingatia umuhimu wa umoja wa Taifa, hata wakati wa kutofautiana mitazamo, nchi imegubikwa na uhasama. Serikali imesahau wajibu wake wa kuunganisha nguvu za umma ili kuleta maendeleo.

Tutajengaje nchi wakati kila mahali watu wanaangaliana kiuhasama kutokana na tofauti za mitazamo ya ksiasa? Ili serikali itambue wajibu wake wa kuunganisha Taifa ili kutumia uwezo wa kila mwananchi katika kuleta maendeleo, busara za Seneta John McCain wa Marekani, alizozitoa katika hotuba yake leo tarehe 25 Julai, 2017, ni muhimu.

Dakika za mwisho za hotuba hii zinawahusu zaidi wa-Marekani. Lakini, ukiachilia mbali sehemu hiyo, hotuba hii ina busara muhimu za kuinusuru Tanzania.

 

Tuesday, July 18, 2017

Mhadhiri wa Algeria Amekifurahia Kitabu

Mimi kama mwandishi, ninaguswa na maoni ya wasomaji. Leo nimepata ujumbe kutoka kwa mhadhiri wa chuo kikuu kimoja cha Algeria, Samir, ambaye tumewasiliana kwa miaka michache, na nilimpelekea nakala ya kijitabu changu, Notes on Achebe's Things Fall Apart.

Nanukuu sehemu ya ujumbe wake:

I hope this finds you safe. I am so pleased to let you know that your book on Achebe's TFA is very helpful!! It really helped me. It is a pleasure also to inform you that I am citing you in my phd thesis on Gender in Ngugi's fiction. Your name will also be cited in my Acknowledgements and Dedications. Thank you so much....We love you much.

Kwa wale wasiojua ki-Ingereza, napenda kuelezea anachosema mhadhiri huyu kwa ujumla. Anasema kuwa anategemea ujumbe wake utanifikia nikiwa salama. Amefurahi sana kunifahamisha kuwa kitabu changu kuhusu riwaya ya Achebe ya Things Fall Apart ni mchango mkubwa sana na kimemsaidia sana. Anafurahi kunifahamisha vile vile kuwa ananukuu kitabu changu katika tasnifu yake ya uzamifu kuhusu jinsia katika riwaya za Ngugi wa Thiong'o. Jina langu litatajwa katika orodha ya watu waliochangia tasnifu hii. Anahitimisha kwa kusema, "Asante sana....Tunakupenda sana."

Ujumbe wowote kutoka kwa wasomaji makini una manufaa kwangu kama mwandishi. Ninayachukulia maanani maoni yao, hasa nikijua kuwa wametumia hela zao kununua kitabu changu. Kuna wengine ambao ninakuwa nimewapa nakala ya bure. Hao wanaponiandikia maoni yao juu ya kitabu ninaona kama wamelipa fadhila. Maoni yao ni muhimu kwangu kuliko hela.

Kitabu hiki na vingine vinapatikana hapa

Monday, July 17, 2017

Nina Mashairi Yote ya John Donne

Nimegundua kuwa nina mashairi yote ya John Donne. Huyu ni mshairi mmoja maarufu sana katika ki-Ingereza, ambaye aliishi miaka ya 1572-1631, na niliwahi kumtaja katika blogu hii. Niliandika habari zake siku niliponunua kitabu kiitwacho The Works of John Donne.

Lakini wikiendi hii, katika kuangalia katika msitu wa vitabu vyangu ofisini, nimegundua kitabu kiitwacho The Complete English Poems of John Donne, kilichohaririwa na C.A. Patrides. Hiki kina mashairi yake yote.

Katika utangulizi wake, Patrides amesema mambo ambayo yamenifungua macho na kunifikirisha. Amesema, kwa mfano, "The text of Donne's poetry can vex an editor into nightmares." Anamaanisha kuwa maandishi ya Donne yanaweza kumchanganya akili mhariri akaishia katika majinamizi. Hii ni kwa sababu miswada ya mashairi ya Donne ni mingi na inahitilafiana.

Niliposoma utangulizi huu, nimewazia maandishi ya William Shakespeare, ambaye aliishi wakati ule ule wa John Donne. Maandishi ya Shakespeare, hasa tamthilia, nayo yanapatikana katika miswada inayohitilafiana, na kwa miaka yote wahariri wamekuwa wakijaribu kurekebisha na kuwasilisha kile ambacho wanaamini ni andiko sahihi la Shakespeare.

Tofauti hizi katika maandishi ya Donne na Shakespeare, haziko katika maneno na sentensi tu, bali pia katika alama kama vile nukta na mikato katika sentensi. Kwa hivyo, tunavyosoma andiko la Shakespeare, tunapaswa kuzingatia kuwa kuna vitu kadha wa kadha ambavyo vimeingizwa na wahariri wa karne moja hadi nyingine.

Hata hivi, kama nilivyosema katika ujumbe wangu wa mwanzo, nimeona nisome kwa makini mashairi ya Donne, hasa kwa kuzingatia kuwa nilikulia nikiwa nimesikia sana kwamba mashairi yake ni magumu. Nimepata mwamko mpya, wa kutaka kujipima akili kwa kuyakabili haya mashairi yanayosemekana ni magumu. Tena basi, nitapenda hata kujaribu kutafsiri baadhi ya mashairi haya kwa ki-Swahili, kama nilivyowahi kutamka katika blogu hii.

Wednesday, July 12, 2017

Mazungumzo Global Minnesota Kuhusu Fasihi





Leo nilikwenda Minneapolis, kwa mwaliko wa taasisi iitwayo Global Minnesota, kutoa mhadhara juu ya fasihi simulizi na andishi wa Afrika, kuanzia chimbuko lake barani Afrika hadi Marekani, ambako hii fasihi simulizi ililetwa na watu waliosafirishwa kutoka Afrika kama watumwa. Watoa mada tulikuwa wawili, mwingine ni Profesa Mzenga Wanyama anayefundisha katika chuo cha Augsburg.


Pichani hapa kushoto, tunaonekana kama ifuatavyo. Kutoka kushoto ni Tazo kutoka Zambia, ambaye alihitimu chuo cha St. Olaf  mwaka jana, na amajiriwa kwa mwaka huu moja na Global Minnesota. Wa pili ni Carol, rais wa Global Minnesota. Wa tatu ni Profesa Wanyama. Wa nne ni mimi, na wa tano ni Tim, mkurugenzi wa programu wa Global Minnesota, ambaye alikuwa mtu wa kwanza kuniuliza kama ningekuwa tayari kutoa mhadhara Global Minnesota, wakati tulipokutana katika tamasha la Togo miezi michache iliyopita.


















Hapa kushoto ninaonekana nikiongea. Sina kawaida ya kusoma hotuba, hata kama nimeandika vizuri. Ninashindwa kuangalia karatasi badala ya kuangalia watu. Hata darasani, sisomi nilichoandaa kimaandishi. Katika kujiandaa kwa ajili ya kutoa mihadhara, ninaandika sana hoja na maelezo yangu. Lakini wakati wa kutoa mhadhara, ninatumia kumbukumbu tu ya yale niliyoandika.

Kwa hivyo, katika mhadhara wa leo, nimeongelea chimbuko la binadamu ambalo liliendana na uwezo kutembea wima kwa miguu tu, kutumia lugha, na  kutumia na kutengeneza zana za kazi. Hayo yote kwa pamoja yalisababisha kuumbika kwa kiumbe aitwaye binadamu kimwili, kiakili, na kadhalika. Huu ndio msingi wa kukua kwa lugha na fasihi, ambayo ilihitaji ubunifu, kumbukumbu, na uwezo wa kutambua na kuunda sanaa,  ikiwemo fasihi, ambayo ni sanaa inayotumia lugha.

Maendeleo ya tekinolojia, ambayo ilianzia na kutengeneza zana za mawe au miti, yalifikia hatua ya binadamu kuvumbua maandishi. Hapo ndipo ikawezekana kuandika yale yaliyokuwa katika fasihi simulizi, na ushahidi tunauona katika Misri ya miaka yapata elfu nne au tano iliyopita. Hadithi zilizoandikwa wakati ule ni kama "The Tale of Two Brothers," "The Story of Sinuhe," na "The Tale of the Ship-wrecked Sailor."

Lakini pia, uandishi ulimwezesha binadamu kutunga fasihi kimaandishi. Waandishi, hasa wa mwanzo, walikuwa wamelelewa katika fasihi simulizi, kiasi kwamba kazi zao andishi zilibeba athari za wazi za fasihi simulizi. Mifano kutoka Afrika ni The Golden Ass (Apuleus), Chaka (Thomas Mofolo), The Palm Wine Drinkard (Amos Tutuola), Things Fall Apart (Chinua Achebe), The Dilemma of a Ghost (Ama Ata Aidoo). Waandishi weusi wa bara la Marekani kama vile Zora Neal Hurston, Toni Morrison, na Edwidge Dandicat.




Baada ya mimi kuongea, alifuata Profesa Mzenga Wanyama, kama inavyoonekana pichani hapa kushoto. Yeye aliongelea zaidi waandishi weusi wa Marekani, akianzia na Phyllis Wheatley. Aliongelea elimu na itikadi aliyofundishwa msichana na hata alipoandika mashairi yake, akawa anaelezea pia waandishi wa ki-Afrika kama vile Achebe na Ngugi wa Thiong'o, na Chimamanda Ngozi Adichie. Kati ya masuala aliyosisitiza ni utumwa wa fikra na umuhimu wa kujikomboa. Baada ya hotuba zetu, palikuwa na muda mfupi wa masuali na majibu.









Baada ya kikao kwisha, hawakosekani wahudhuriaji wenye kupenda kuongea zaidi na mtoa mada. Hapa kushoto niko na profesa mstaafu wa College of St. Benedict, Minnesota. Ni mzaliwa wa India. Nilimwambia kuwa nilishawahi kualikwa kwenye chuo kile kutoa mihadhara.













Hapa kushoto anaonekana Carol, rais wa Global Minnesota, na binti yangu Assumpta, ambaye aliwahi kufanya kazi na Carol, wakati taasisi ilipokuwa inaitwa International Institute of Minnesota.















Hapa kushoto niko na mama moja kutoka Brazil, ambaye ni mfanyakazi katika Minnesota Department of Human Services. Sikumbuki kama nimewahi kuongea na mama yeyote wa Brazil mwenye asili ya Afrika. Kwa hiyo, hiyo ilikuwa ni kumbukumbu ya pekee.
















Hapa kushoto niko na vijana wawili waliohitimu masomo chuo cha St. Olaf ambapo ninafundisha. Huyu wa kushoto kabisa ni raia wa Swaziland, na huyu wa kulia ni Tazo wa Zambia anayeonekana katika picha ya kwanza hapo juu.













Hapo kushoto niko na binti zangu, Assumpta na Zawadi. Ninafurahi wanapokuja kunisikiliza katika mihadhara. Wataweza kuelezea habari zangu kwa yeyote atakayependa kuelewa zaidi shughuli zangu katika jamii.

Nimalizie kwa kusema kuwa wakati tulipokuwa tunaagana, viongozi wa Global Minnesota walielezea nia yao ya kuniita tena kwenye program nyingine. Tim aliongezea kuwa kama  angekuwa amekumbuka, vitabu vyangu vingekuwepo kwa ajili ya watu waliohudhuria mkutano wa leo. Nami nilikuwa sijawazia jambo hilo. Siku zijazo litaweza kufanyika.

Monday, July 10, 2017

Nitawasilisha Mada Global Minnesota

Nimealikwa na taasisi iitwayo Global Minnesota kutoa mada tarehe 12 Julai juu ya mwendelezo wa fasihi ya ki-Afrika kuanzia chimbuko lake kama fasihi simulizi hadi fasihi andishi ya leo. Mael"ezo zaidi yako mtandaoni

--------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------
Global Conversations: African Folktales to Contemporary Authors

JULY 12 @ 6:00 PM CDT / Free

From ancient oral traditions to contemporary literature, African stories reflect wisdom, cultural identities, and social values developed over countless generations. Join us, St. Olaf College Associate Professor Joseph Mbele, and Augsburg College Associate Professor Mzenga Wanyama for an exploration of how these stories find expression today, both in Africa and in the African diaspora.

Speakers
Joseph Mbele, Associate Professor of English at St. Olaf College, is a folklorist and author. His writings, including Matengo Folktales, illuminate the underlying values that shape cultures. Dr. Mbele has done fieldwork in Kenya, Tanzania, and the U.S., and has given lectures and presented conference papers in Canada, Finland, India, Israel, Kenya, Tanzania, Uganda, and the U.S. After earning a Ph.D. from the University of Wisconsin and before coming to St. Olaf in 1990 to teach post-colonial and third-world literature, he taught in the Literature Department at the University of Dar es Salaam, Tanzania. Over the years, he has taught courses such as Swahili Literature, Theory of Literature, African Literature, Sociology of Literature, Postcolonial and Third World Literature, The Epic, and African-American Literature.

Mzenga Aggrey Wanyama, Associate Professor of English at Augsburg College, was born and raised in Kenya where he received his bachelor’s of education and master’s degrees from the University of Nairobi and then taught English language and literature in Kenyan High schools and at Kenyatta University. In the United States, he had a two-year stint in the graduate program at Howard University in Washington, D.C. before attending the University of Minnesota where he earned a Ph.D. in English. Mzenga also worked as an Assistant Professor of English at St. Cloud State University where he taught courses in literature and writing. His areas of focus are Postcolonial theory and literature and African American literary history.

Presented in partnership with the Friends of the Minneapolis Central Library.

Global Conversations: African Folktales to Contemporary Authors
Wednesday, July 12, 2017
6:00 PM

Sunday, July 9, 2017

Wole Soyinka na Madikteta wa Afrika

Wole Soyinka ni mmoja wa waandishi bora kabisa kutoka Afrika. Ameandika tamthilia, riwaya, mashairi, insha, na wasifu wake. Pia ametafsiri riwaya ya ki-Yoruba ya D.O. Fagunwa. Tafsiri hiyo inaitwa Forest of a Thousand Daemons: A Hunter's Saga.

Pamoja na umahiri wake katika kubuni visa na katika kuimudu lugha ya ki-Ingereza, Soyinka anachota sana mbinu na vipengele vingine vya sanaa na masimulizi ya jadi, hasa ya wa-Yoruba, lakini pia ya mataifa mengine, akienda mbali hadi u-Griki ya kale. Umahiri wake kama mwandishi umetambuliwa kwa namna mbali mbali, ikiwemo tuzo ya Nobel katika fasihi, ambayo alitunukiwa mwaka 1986.

Katika kazi zake, anashughulikia masuala ya aina mbali mbali, kama vile siasa, itikadi, ukoloni, ukoloni mambo leo, utamaduni, na fasihi ya Afrika na kwingineko. Udikteta ni mada ambayo Soyinka ameishughulikia tangu zamani, sio tu katika maandishi na mahojiano, bali pia kama mwanaharakati. Tamthilia ya Kongi's Harvest ni mfano mzuri. Tamthilia hii tuliisoma nilipokuwa mwanafunzi katika idara ya "Literature," Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, 1973-76.

Wiki hii nimesoma A Play of Giants. Ni tamthilia ambayo inazama zaidi katika mada ya madikteta wa Afrika. Nilifahamu jambo hilo tangu zamani, kama nilivyoelezea siku chache zilizopita katika blogu hii. Soyinka anawaumbua madikteta hao. Anatumia kejeli kuelezea fikra na matendo yao, ulevi wa madaraka, uduni wa akili zao, na ukandamizaji wa haki za binadamu. Uduni wa akili zao unadhihirika kwa namna wanavyoongelea mambo yasiyo na maana, na kama wanaongelea mambo ya maana, hoja zao ni za ovyo kupindukia.

Madikteta hao wanaongelea jinsi wanavyoweza kudumu madarakani. Wanabadilishana mawazo na uzoefu wao. Wazo moja ni kutawala kwa mkono wa chuma na kuwafanya raia waishi kwa hofu. Hofu inaweza kujengwa mioyoni mwa raia kwa kutumia ushirikina na kuwafanya waamini kuwa mtawala anaona kila kinachoendelea nchini, Kwa njia hiyo, raia wanaogopa hata kuwazia kupinga utawala, kwani wanaamini kuwa mtawala atajua.

Udikteta ni mada ambayo imeanishwa katika kazi za fasihi tangu zamani sana. Tunaisoma katika The Epic of Gilgamesh, kwa mfano, na katika baadhi ya tamthilia za Shakespeare. Katika kusoma A Play of Giants, nimewazia sana riwaya ya Ngugi wa Thiong'o, Wizard of the Crow, ambamo dikteta anaumbuliwa pamoja na mfumo wa utawala wake kwa njia ya kejeli, sawa na anavyofanya Soyinka.

Ingawa kuna matumizi ya kejeli, A Play of Giants si tamthilia ya kufurahisha, bali inatibua akili na kunifanya nijiulize binadamu tunawezaje kuishi katika himaya ya udikteta. Kejeli ya mwandishi inanifanya mimi msomaji nicheke, lakini si kicheko cha furaha, bali dhihaka juu ya madikteta na aibu juu yetu wanadamu.

Friday, July 7, 2017

Wadau Wangu Wapya

Nina furaha kama mwandishi kuwa nimejipatia wadau wapya, na ninawatambulisha hapa kama ilivyo kawaida yangu. Hao ni Brian Faloon na mkewe Kristin, wenyeji wa Rochester, Minnesota. Brian ni rais wa Rochester International Association (RIA). Kristin na mimi ni wanabodi katika bodi ya RIA, ambamo nilijiunga mwaka jana kama nilivyoelezea katika blogu hii.

Baada ya mimi kujiunga na bodi, nilipata fursa ya kutoa mhadhara katika chuo kikuu cha Minnesota Rochester, mada ikiwa "Folklore as Expression of Ethics," kama nilivyoeleza katika blogu ya ki-Ingeeza. Brian alihudhuria.

Brian aliuongelea mhadhara ule katika mkutano uliofuata wa bodi ya RIA. Baada ya muda, nilipata mwaliko wa kutoa mhadhara chuo kikuu cha Winona, mwaliko ambao niliuelezea katika blogu hii. Kristin aliniuliza iwapo itawezekana yeye kuhudhuria. Niliwasiliana na waandaaji, kuwauliza iwapo ninaweza kumwalika mgeni kuhudhuria, nikajibiwa kuwa ni ruksa. Nilimweleza Kristin hivyo.

Nilisafiri tarehe 27 Juni hadi Winona, mwendo wa saa mbili. Nilivyoingia ukumbini, niliwakuta Kristi na Brian wameketi, pamoja na wasikilizaji wengine yapata 50. Nilitambulishwa na wenyeji wangu, nikatoa mhadhara kama nilivyoelezea katika blogu ya ki-Ingereza. Nilivyomaliza mhadhara na muda wa masuali na majibu, Kristin na Brian walinisogelea tukaongea. Walifurahia mhadhara. Nilivyowashukuru kwa kusafiri mwendo mrefu na kuhudhuria, walinijibu kuwa wao ni mashabiki wangu. Walichosema ni ukweli, kwani walianza kuwa wadau tangu waliposoma kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Tarehe 4 Julai, nilipata ujumbe kutoka kwa Kristin. Kati ya mambo aliyoandika ni haya:

We greatly enjoyed hearing your presentation and thought it was very good! Thank you for letting us attend! I believe it would be an excellent presentation to do in our community and schools here in Rochester as we have the same tensions between the two groups....I would like to coordinate something when we have time. We can discuss it at the next meeting if you're interested.

Ninajivunia hao wadau wangu wapya. Moyo wangu wa kutumia ujuzi wangu kwa manufaa ya walimwengu unaniletea fursa kama hii anayoongelea Kristin. Ninazipokea fursa hizi kwa moyo mkunjufu. Ninaamini ni mipango ya Mungu, wala sijali suala la kulipwa au kutolipwa fedha, kama nilivyoelezea katika blogu hii. Mungu ana mipango yake, na anasawazisha mambo.

Monday, July 3, 2017

Ninapenda Muziki wa Reggae

Ukivaa kofia kama hii niliyovaa pichani hapa kushoto, halafu useme hupendi reggae, hakuna atakayekuelewa. Kofia, sawa na vazi lolote, inawasilisha ujumbe. Ni tamko. Kofia hii niliyovaa inawafanya watu wafikirie vitu kama Rastafari, reggae, Bob Marley, na Jamaica, ambako muziki wa reggae ulianzia.

Muziki wa reggae umeenea sana duniani, kuanzia visiwa vya Pacific, hadi Afrika Kusini; Senegal hadi Sweden. Reggae haichagui kabila, taifa, wala utamaduni. Niliwahi kwenda chuo kikuu cha Arizona, Tucson, nikaambiwa kuwa Wahindi Wekundu wanaipenda reggae. Siku moja, nilitembea katika mtaa mdogo mjini Tel Aviv, Israel, nikaona mbele yangu bango kubwa la picha ya Bob Marley.

Kwa hiyo, kutokana na kwamba siwezi kujumlisha habari za muziki wa reggae ulimwengu mzima, ninawazia zaidi Jamaica. Kutokana na kusoma vitabu juu ya Rastafari na reggae, ninavutiwa na jinsi muziki wa reggae ulivyounganika na itikadi ya Rastafari, ukawa ni sauti ya walalahoi dhidi ya unyonyaji, ukandamizaji, na dhulma za kijamii, kiuchumi, na kadhalika, ndani na nje ya Jamaica.

Saturday, July 1, 2017

Vitabu Nilivyonunua Leo

Ninaamini kuwa kila mtu ana kitu anachokipenda sana. Kuna watu wanaopenda sana soka. Ni mashabiki ambao daima wanafuatilia mechi. Wako tayari kukopa hela ili waende uwanjani kuangalia mechi. Wengine wanapenda bia. Katika baa za Tanzania, nimeona watu wanaokunywa na kuandikiwa deni walipe baadaye. Kama huku kupenda kitu namna hii ni ugonjwa, basi vitabu ndio ugonjwa wangu. Ndio maana katika blogu hii ninaandika mara kwa mara habari za vitabu.

Mtu anaweza kuuliza, inakuwaje katika ulimwengu huu wa vitabu pepe, tuko watu ambao tunaendelea kung'ang'ania vitabu vya jadi? Je, hatuoni udhia wa kubeba vitabu hivyo, na pia udhia wa kuvitafutia sehemu ya kuviweka, badala ya kutumia kifaa cha kuhifadhia vitabu pepe, ambacho kinaweza kubeba mamia ya vitabu au zaidi? Ukweli ni kwamba, mazoea yana taabu. Sio rahisi kuachana na mazoea.

Leo nilikwenda Minneapolis, na wakati wa kurudi, nilipita katika duka la vitabu la Half Price Books, mjini Apple Valley. Kama kawaida, niliangalia kwanza sehemu vinapowekwa vitabu vya Ernest Hemingway au vitabu juu ya Hemingway. Sikuona kipya, nikaelekea sehemu vinapouzwa vitabu vya bei rahisi kabisa. Hapo nilichagua vitabu vinne.

Kitabu kimoja ni Gilgamesh: A Verse Narrative, cha Herbert Mason. Wafuatiliaji wa fasihi simulizi za kale wanafahamu juu ya Gilgamesh, mtu maarufu katika masimulizi ya watu wa himaya ya Sumer, katika nchi ambayo leo inaitwa Iraq, na pia nchi zingine za Mashariki ya Kati. Masimulizi haya hatimaye yaliandikwa, katika lugha kadhaa za wakati ule, kwa hati iitwayo "cuneiform," ambayo ni tofauti kabisa na hizi hati tunazotumia leo, kama vile ya ki-Rumi, au ki-Arabu. Ugunduzi wa maandishi yale ulitokana na juhudi za wana akiolojia.

Lakini baada ya ugunduzi, hakuna aliyeweza kusoma hati ya "cuneiform." Baadaye sana siri ya hati hii iligunduliwa na usomaji wake ukawezekana. Tafsiri za masimulizi ya Gilgamesh zikaanza. Kwa upande wangu, kwa miaka mingi nimefundisha masimulizi ya Gilgamesh kwa kutumia tafsiri ya N. K. Sandars. Nilifahamu, hata hivyo, kwamba ziko tafsiri zingine pia. Kwa hivyo, leo niliona ninunue hii tafsiri ya kishairi ya Herbert Mason.

Kitabu kingine nilichonunua leo ni A Play of Giants, ambayo ni tamthilia ya Wole Soyinka. Nimesoma na kufundisha maandishi ya Soyinka kwa miaka mingi, kuanzia tamthilia, riwaya, mashairi na insha. Ninavyo vitabu vyake kadhaa, lakini si A Play of Giants. Hata hivyo, nilifahamu tangu zamani kuwa tamthilia hii inawaumbua madikteta wa Afrika. Sasa nitaisoma.

Kitabu cha tatu nilichonunua ni Theban Plays of Sophocles. Ni tafsiri ya David R. Slavitt ya tamthilia tatu za Sophocles. Huyu ni mwanatamthilia maarufu wa u-Griki ya kale. Ninazo tatsiri tofauti za tamthilia hizo, lakini niliamua kununua hii pia. Ni jambo bora kusoma tafsiri mbali mbali za kazi ya fasihi, kwani kila tafsiri inaleta ladha tofauti na hata tofauti za ujumbe.

Kitabu cha nne nilichonunua ni Speaking of Books: The Best Things Ever Said About Books and Book Collecting, kilichohaririwa na Rob Kaplan na Harold Rabinowitz. Hicho sikuwahi hata kukisikia, lakini nilivyoangalia ndani, nilivutiwa. Ni mkusanyiko wa kauli za watu mbali mbali kuhusu vitabu, usomaji, uandishi, waandishi, wasomaji, na kadhalika. Nilikuwa ninafahamu baadhi ya mambo ambayo yamewahi kusemwa kuhusu vitabu, kama vile kauli ya Ernest Hemingway, "There is no friend as loyal as a book," yaani hakuna rafiki wa kweli kama kitabu. Kutokana na kupendezwa kwangu na mambo hayo, niliona ninunue kitabu hiki.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...