Monday, September 28, 2015

Kampeni za CCM Mwaka Huu

Najaribu kutafakari picha hii iliyopigwa katika moja ya mikutano ya kampeni za uchaguzi zinazoendelea Tanzania. Ina maana kwamba mwenye uwezo wa kupiga "push-up" nyingi ndio anafaa kuwa kiongozi? Je, ili uukwae ubunge, unatakiwa upige angalau "push-up" ngapi? Udiwani je? Na ili uwe waziri, unahitaji "push-up" ngapi? Na kwa uwaziri, ni sahihi tuwe na "push-up" tu au na kuruka viunzi pia? Na kwa kuzingatia uzito wa cheo cha uwaziri, kwa nini tusiongezee pia uwezo wa kunyanyua matofali angalau manne ya zege? Kwa kweli, tukifanya hivyo, tutapata serikali imara kabisa.

Sunday, September 27, 2015

Tumechangia Kanisa la Venezuela

Leo kanisani kwetu hapa mjini Northfield, kanisa Katoliki, tulikuwa na padri ambaye anatumikia kanisa fulani nchini Venezuela. Huyu padri ni m-Marekani, na kwa miaka yapata arobaini, mapadri wa-Marekani wamekuwa wamisionari katika kanisa hilo la Venezuela. Hata paroko wetu aliwahi kutumikia kanisa hilo kwa miaka mitano. Ananivutia kwa jinsi anavyoijua lugha ya ki-Hispania, na anawahudumia waumini hapa Northfield wanaotumia lugha hiyo.

Huyu padri mgeni alitoa mafundisho mazuri, na katika kuelezea utume wake Venezuela alituhimiza kwa maneno matatu: "Pray, say, pay." Alifafanua kwamba tusali kuwaombea waumini wa kanisa lile la Venezuela, tuwaeleze wengine kuhusu hali halisi na mahitaji ya kanisa lile, na tutoe mchango kulisaidia kanisa lile.

Niliguswa na maelezo yake, nikangojea muda wa kutoa mchango. Kilipopitishwa kijikapu cha mchango, nilikuwa tayari nimekwangua vijihela vilivyokuwemo katika pochi yangu nikavitumbukiza humo. Nilijisikia faraja na furaha kwamba vijihela hivyo vitakuwa na manufaa kwa kanisa lile la Venezuela, hasa kwa kuzingatia kuwa dola, hata zikawa chache, zinakuwa ni hela nyingi kwenye nchi kama Venezuela au Tanzania.

Mimi kama muumini wa dini, naiheshimu dini yangu, na dini zote. Ninafahamu kwamba zote ni njia wanazotumia wanadamu kuelekea kwa Mungu. Ni safari, kama safari ya kupanda Mlima Kilimanjaro. Kuna njia kadhaa za kufikia kileleni Kilimanjaro. Na itakuwa ni wendawazimu kwa watu wanaochukua njia tofauti kuanza kugombana na kupigana hadi kuuana kwa msingi wa tofauti za njia wanazochukua. Kwa mtazamo wangu, ni wendawazimu kwa watu wa dini mbali mbali kubezana au kugombana.

Ninaziheshimu nyumba za ibada za kila dini. Niliwahi kuelezea katika blogu hii nilivyozuru nyumba za ibada za wa-Hindu, nchini India. Leo nimechangia kanisa lililoko Venezuela. Lakini sibagui. Kuna wakati niliona taarifa kuwa wa-Islam wa sehemu fulani Tanzania walikuwa wanachangisha fedha za kukarabatia msikiti wao. Nilipeleka mchango wangu, kwa moyo mkunjufu, ingawa mimi si mu-Islam bali m-Katoliki. Nitaendelea kufanya hivyo.

Ninachojali ni kuwa wanadamu wote wameumbwa na Mungu, na Mungu hana ubaguzi, kama nilivyoandika katika blogu hii. Ninafurahi kumiliki blogu, kitu ambacho kinaniwezesha kueneza mawazo yangu na kupambana na mawazo ambayo nayaona ni sumu, hata kama yanaenezwa kwa jina la dini.

Saturday, September 26, 2015

Nimehojiwa Kuhusu Hemingway na "Papa's Shadow"

Leo nimekuwa na mahojiano na mwandishi wa gazeti la Manitou Messenger linalochapishwa hapa chuoni St. Olaf. Ni gazeti la wanafunzi, ambalo limekuwa likichapishwa kila wiki kwa miaka 125. Mahojiano yetu yalikuwa juu ya filamu ya Papa's Shadow. Katika ujumbe wa kuomba mahojiano, mwandishi aliandika:

...we are doing a feature article this week on the documentary, Papa's Shadow and Ramble Pictures. We learned that you were instrumental in the inspiration for and production of this film, and we were hoping you could answer a few quick questions.

Katika mahojiano, tumeongelea nilivyoanza kuvutiwa sana na mwandishi Ernest Hemingway, nilipoombwa na Thomson Safaris kuongoza msafara mkubwa wa wanafunzi, wazazi na walimu, katika safari ya Tanzania mwaka 2002. Hatimaye, baada ya miaka mitano ya kusoma maandishi na habari za Hemingway, nilitunga kozi Hemingway in East Africa, kwa ajili ya Chuo cha Colorado.

Baadaye, niliona niunde kozi hiyo kwa ajili ya wanafunzi wa Chuo cha St. Olaf. Nilifanya hivyo mwaka 2012. Wakati wa kuandikisha wanafunzi, alinifuata kijana aitwaye Jimmy Gildea, akaniomba nimruhusu kujiunga na kozi, kwa kuwa alimpenda Hemingway na alitaka kurekodi filamu ya kozi. Nilimsajili katika darasa.

Kozi ilikwenda vizuri, kama nilivyoandika hapa. Baada ya kurejea tena Marekani, baadhi yetu tulifunga safari ya jimbo la Montana kuonana na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee aliyebaki wa Ernest Hemingway. Tuliongea naye sana.

Jimmy alikuwa amenirekodi ofisini mwangu nikizungumza juu ya Hemingway, akachanganya mazungumzo haya na yale tuliyofanya na Mzee Patrick Hemingway,na akaongezea mambo mengine aliyorekodi Tanzania. Kwa bahati nzuri, tulipomaliza kozi, familia ya Jimmy walikuja kumchukua wakaenda kupanda Mlima Kilimanjao. Papa's Shadow inaonyesha safari yao ya kupanda mlima. Ni rekodi nzuri sana. Ninaamini itawavutia watalii.

Kuna mambo mengine niliyomwambia huyu mwandishi wa Manitou Messenger. Hasa, nilisisitiza azma yangu ya kuendelea kufanya kila juhudi kuuelimisha ulimwengu juu ya namna Hemingway alivyoipenda Afrika na namna maisha yake na fikra zake zlivyofungamana na Afrika. Nilimwambia pia kuwa Jimmy ni mfano murua wa kuigwa na wahitimu wengine wa vyuo. Alifuata na anaendelea kufuata anachokipenda moyoni mwake, yaani kutengeneza filamu za kuelimisha. Yeye na vijana wenzake katika Ramble Pictures wanajituma kwa roho moja katika shughuli zao na hawatetereshwi na magumu au vipingamizi vyovyote.

Thursday, September 24, 2015

"Papa's Shadow" Yapongezwa na Uwakilishi wa Kudumu wa Tanzania Umoja wa Mataifa

Tarehe 20 mwezi huu nilipeleka ujumbe Uwakilishi wa Kudumu wa Tanzania Umoja wa Mataifa kuhusu filamu ya Papa's Shadow. Sikuandika ujumbe mrefu, bali niliwatumia kiunganishi hiki.

Bila kuchelewa, tarehe 22 nilipata ujumbe kutoka kwao, ukiwa umeandikwa na Ndugu Noel Kabanda. Uwakilishi unaafiki kuwa Papa's Shadow ni "fursa maridhawa ya kuitangaza Tanzania ulimwenguni" na unasisitiza kuwa "Serikali inatambua mchango wa sanaa katika kuitangaza Tanzania katika sekta mbali mbali ikiwemo utalii na utamaduni."

Kwanza, kwa kuzingatia uwingi wa majukumu yanayowakabili wawakilishi wetu katika balozi zetu, nimeona ni muhimu kusema nilivyoguswa na jinsi Uwakilishi ulivyoushughulikia ujumbe wangu.

Pili, ujumbe wa Uwakilishi unawatia moyo wahusika wa Ramble Pictures, ambao ndio watengeneaji wa Papa's Shadow. Timu nzima ya Ramble Pictures ni vijana wa ki-Marekani, na baadhi yao walikuja Tanzania mwaka 2013 kwenye kozi yangu ya Hemingway Katika Afrika Mashariki. Ni furaha kwangu, na jambo la kujivunia, kuwaeleza vijana hao kuwa Uwakilishi wa Kudumu waTanzania Umoja wa Mataifa umeipokea Papa's Shadow kwa namna hii.

Papa's Shadow si filamu ya maigizo. Ni filamu ya kuelimisha kuhusu mwandishi Ernest Hemingway. Sehemu kubwa ya filamu hiyo ni maongezi baina yangu na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee aliyebaki wa mwandishi Hemingway. Tunaongelea maisha ya Hemingway, safari zake, uandishi wake, na fikra zake kuhusu masuala mbali mbali. Tunawafungua macho walimwengu kuhusu namna Hemingway alivyoipenda Afrika na alivyokuwa mtetezi wa Afrika.

Hemingway alisafiri na kuishi Afrika Mashariki mara mbili, mwaka 1933-34 na 1953-54. Aliandika hadithi, insha, barua na maandishi mengine ambayo ni hazina kubwa. Wenzetu katika nchi zingine ambako Hemingway alipita au kuishi na akaandika habari za huko, wametumia fursa hiyo kujitangaza, na wanawavutia watalii wengi sana. Mifano ni miji kama Paris (Ufaransa), Havana (Cuba), Oak Park (Illinois, Marekani), Key West (Florida, Marekani), na Pamplona (Hispania). Hemingway anapendwa ulimwenguni kote ambako watu wana utamaduni wa kusoma vitabu. Sina shaka kuwa Papa's Shadow italeta msisimko wa aina hiyo kwa kuwaelekeza mashabiki wa Hemingway nchini kwetu.

Hamu ya kuona Tanzania inafunguka macho kuhusu fursa hii ilinihamasisha kufanya utafiti juu ya safari za Hemingway katika nchi yetu na maandishi aliyoandika. Kozi niliyotunga ilikuwa na lengo hili. Nilitaka pia kuwasaidia walimwengu kuelewa umuhimu wa Afrika katika maisha na uandishi wa Hemingway. Kwa msingi huo huo, nilishiriki kikamilifu katika kufanikisha filamu ya Papa's Shadow.

Nimeeleza hayo yote ili kuweka wazi umuhimu wa ujumbe wa Uwakilishi wa Kudumu wa Tanzania Umoja wa Mataifa. Ni mfano wa mshikamano unaotakiwa baina yetu wanadiaspora, serikali, na wananchi wenzetu.

Tuesday, September 22, 2015

Nimenunua Kitabu cha Golding, "Lord of the Flies"

Zimepita siku nyingi kidogo tangu niandike ujumbe kuhusu vitabu nilivyonunua, au nilivyojipatia kwa namna nyingine. Viko vitabu kadhaa, hasa riwaya, ambavyo sikuvielezea.

Leo, baada ya kufundisha vipindi vyangu viwili, nilipita kwenye duka la vitabu la hapa chuoni. Niliangalia sehemu vinapouzwa vitabu kwa bei nafuu, nje ya duka, nikaona, kati ya vitabu vingi, kitabu cha William Golding, Lord of the Flies. Hapo hapo nilikumbuka miaka ya ujana wangu. Tulisoma kitabu hiki tulipokuwa kidatu tano Mkwawa High School, mjini Iringa. Huku nikikumbuka hayo yote, nilikinunua hima, ingawa nina hakika ninayo nakala nyingine niliyonunua zamani, ila itakuwa vigumu kuigundua ilipo katika utitiri wa vitabu vyangu.

Lord of the Flies ni riwaya niliyoipenda sana na ambayo ninaikumbuka sana. Ilinigusa kwa namna ya pekee kwa jinsi ilivyowachora wahusika, ambao ni watoto wa shule waliojikuta kwenye kisiwa peke yao baada ya ndege waliyokuwa wanasafiria kuanguka kisiwani humo na wao wakawa abiria pekee waliosalimika. Riwaya inaonyesha jinsi watoto hao, waliokulia katika jamii ya maadili na ustaarabu, walivyoanza kubadilika, wakawa wabaya na katili kupindukia.

Miaka ile, nilikuwa najikongoja katika uandishi wa hadithi fupi. Lord of the Flies ilinigusa kwa namna ya pekee, kwa ustadi wake wa kuelezea mazingira, ikachangia katika uandishi wa hadithi yangu, "A Girl in the Bus," ambayo ilichapishwa katika jarida la Busara. Hili lilikuwa ni jarida maarufu Afrika Mashariki, lililokuwa linachapishwa Nairobi.

Kuchapishwa kwa hadithi hii kulinipa furaha isiyoelezeka. Nilikuwa na mazoea ya kwenda katika maktaba ya mkoa Iringa, na daima nilikuwa napendezwa kuona jarida hili lenye hadithi yangu. Hata nilipoingia Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kusoma, mwaka 1973, nilikuwa najisikia raha kuliona jarida hili  katika maktaba.

Lord-Flies of the Flies ni riwaya iliyowagusa watu ulimwenguni. Wanadamu kwa ujumla tunaamini kuwa watoto wana silika ya wema na usafi wa moyo. Wanafalsafa kama Jean-Jacques Rousseau walichangia kujenga imani hiyo. Lakini William Golding, katika riwaya yake hii ameelezea jinsi watoto wanavyobadilika na kuwa wabaya. Ni hadithi iliyowashtua walimwengu kwa namna ilivyoihoji dhana ya kwamba watoto ni kama malaika.

Nikizingatia kuwa Lord of the Flies ni moja kati ya riwaya maarufu kabisa katika lugha ya ki-Ingereza, nitaisoma kwa furaha, nikikumbuka ilivyonigusa enzi za ujana wangu. Miaka ilivyopita, nimesoma hadithi na tamthilia mbali mbali ambazo zimeelezea dhamira hii ya watu waliopotelea kwenye kisiwa mbali na walimwengu. Mifano ni The Odyssey ya Homer, Robinson Crusoe ya Daniel Defoe, na mashairi kadhaa ya Derek Walcott, kama vile "The Castaway." Hata baadhi ya wanafalsafa wa mkondo wa "existentialism" wameongelea uwepo wetu hapa duniani kwa kuufananisha na upweke wa watu waliotupwa na kusahauliwa. Ni dhamira ambayo imekuwa na mashiko ya pekee katika fikra na hisia za wanadamu.

Monday, September 21, 2015

Tafsiri ya Sala ya Papa Francis

Katika ujumbe wangu wa jana,niliweka sala ya Baba Mtakatifu Francis ya kuiombea dunia. Sala hii inagusia na kujumlisha mambo mengi, kama vile upendo kwa wanadamu wote na viumbe vyote bila mipaka, kuwajali wasiojiweza, kuyatunza na kuyaboresha mazingira.

Sala hii inatuelekeza kumwomba Mungu atupe ufahamu wa thamani ya kila kiumbe, ufahamu na namna maisha yetu yalivyofungamana na maisha ya viumbe vyote. Aidha, sala inathimiza kumtegemea Mungu katika juhudi zetu za kutafuta haki, upendo, na amani.

Katika sala hii kuna mafundisho muhimu ya dini mbali mbali, matarajio ya wanaharakati wa masuala mbali mbali ya jamii, na matarajio ya wanamazingira. Ni sala inayofundisha busara za zamani za jamii mbali mbali, kama vile wenyeji wa asili wa Amerika ("Native Americans"). Wazo lililomo katika sala hii la kuviangalia viumbe vyote kwa uchaji linanikumbusha falsafa ya mwandishi Shaaban Robert. Kati ya sentensi zinazonigusa kwa namna ya pekee katika sala hii ni,

All-powerful God, you are present in the whole universe
and in the smallest of your creatures.

Kuhitimisha maelezo yangu, napenda kusema kwamba sala hii ilivyo katika ki-Ingereza ikiwa imesheheni uchaji, busara, na maudhui, imeundwa kwa lugha iliyotukuka. Ninajiuliza iwapo tunaweza kuitafsiri kwa ki-Swahili, tukahifadhi utukufu wake kwa msingi wa uhalisia wa ki-Swahili. Ninajiuliza hivyo pamoja na kufahamu jinsi suala la tafsiri lilivyo gumu na tata. Ninatarajia kujaribu kuitafsiri sala hii siku zijazo.

A prayer for our earth

All-powerful God, you are present in the whole universe
and in the smallest of your creatures.
You embrace with your tenderness all that exists.
Pour out upon us the power of your love,
that we may protect life and beauty.
Fill us with peace, that we may live
as brothers and sisters, harming no one.
O God of the poor,
help us to rescue the abandoned and forgotten of this earth,
so precious in your eyes.
Bring healing to our lives,
that we may protect the world and not prey on it,
that we may sow beauty, not pollution and destruction.
Touch the hearts
of those who look only for gain
at the expense of the poor and the earth.
Teach us to discover the worth of each thing,
to be filled with awe and contemplation,
to recognize that we are profoundly united
with every creature
as we journey towards your infinite light.
We thank you for being with us each day.
Encourage us, we pray, in our struggle
for justice, love and peace.

Sunday, September 20, 2015

Nimerejea Kutoka Kanisani

Nimetoka kanisani kusali, na ninaona ni sawa tu kuandika habari hiyo hapa katika blogu yangu. Hii si mara ya kwanza kwangu kuandika habari ya namna hiyo.

Kwanza napenda kuwajulisha ndugu, marafiki na wote wanaofuatilia habari zangu, kwamba afya yangu imeendelea kuwa bora. Zaidi ya huu mkongojo ninaotembea nao, uonekanao pichani, hakuna dalili ya tatizo. Naendesha gari mwenyewe, hata umbali mrefu. Natembea na mkongojo kwa kuwa daktari anataka nitembee nao. Nina kila sababu ya kumshukuru Mungu.

Kama ilivyo kawaida, katika ibada ya misa ya leo tumewaombea watu wote. Tumewakumbuka waumini wenzetu wanaosali makanisani, misikitini, na katika nyumba za ibada za dini zingine, tukiombea amani ulimwenguni. Wa-Katoliki hatujiombei wenyewe tu, bali wanadamu wote.

Kila Jumapili, tangu Baba Mtakatifu wa sasa, Papa Francis II, alipotoa waraka wake wa kichungaji, Laudato Si, tumekuwa tukisali sala yake ya kuiombea dunia:

A prayer for our earth

All-powerful God, you are present in the whole universe
and in the smallest of your creatures.
You embrace with your tenderness all that exists.
Pour out upon us the power of your love,
that we may protect life and beauty.
Fill us with peace, that we may live
as brothers and sisters, harming no one.
O God of the poor,
help us to rescue the abandoned and forgotten of this earth,
so precious in your eyes.
Bring healing to our lives,
that we may protect the world and not prey on it,
that we may sow beauty, not pollution and destruction.
Touch the hearts
of those who look only for gain
at the expense of the poor and the earth.
Teach us to discover the worth of each thing,
to be filled with awe and contemplation,
to recognize that we are profoundly united
with every creature
as we journey towards your infinite light.
We thank you for being with us each day.
Encourage us, we pray, in our struggle
for justice, love and peace.

Leo Papa Francis yuko upande huu wa dunia, ziarani Cuba, akiwa njiani kuja Marekani na kuhutubia bunge la Marekani na pia Umoja wa Mataifa. Kuna msisimko mioyoni mwa watu, wanapongojea kusikia mawaidha ya kiongozi huyu aliyejipambanua kwa kutetea wanyonge na uangalifu wa dunia hii ambayo ni msingi wa maisha yetu na ya viumbe vyote.

Wednesday, September 16, 2015

Filamu ya "Papa's Shadow:" Fursa ya Kuitangaza Tanzania

Nina furaha kuandika kuhusu filamu ambayo imeandaliwa iitwayo "Papa's Shadow," inayomhusu mwandishi maarufu Ernest Hemingway. Katika filamu hiyo, ninaonekana nikiongea na Mzee Patrick Hemingway, ambaye ni mtoto pekee wa Ernest Hemingway aliye hai. Ana umri wa miaka 87. Tunaongelea maisha, safari, maandishi na fikra za Hemingway, hasa kuhusu Afrika.

Sehemu nyingi hapa duniani ambako Hemingway alipita au kuishi na akaandika habari zake, zimejipatia umaarufu. na zinafaidika hasa katika utalii. Mifano ni Cuba na mji wa Pamplona nchini Hispania. Watu wa Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla tuna bahati hiyo, kwani Hemingway alikuja na kuishi kwetu mara mbili, mwaka 1933-34 na 1953-54, akaandika vitabu, hadithi, insha na barua kuhusu aliyoyaona.

Filamu ya "Papa's Shadow" ilitokana na kozi niliyofundisha Tanzania mwezi Januari mwaka 2013 juu ya Hemingway. Kozi ile ilimhamasisha Jimmy Gildea, mmoja wa wanafunzi wangu, kutengeneza filamu hiyo. Alianzisha kampuni, Ramble Pictures, akaanza kutegeneza hiyo filamu ya kuelimisha. Anaendelea kutengeneza filamu zingine zenye kuelimisha.

"Papa's Shadow" inaitangaza Tanzania kwa namna ya pekee. Kuna kampeni ya kuchangisha fedha za kumalizia malipo ya usajili na taratibu zingine kabla ya filamu kuonyeshwa na kusambazwa. Naleta hapa ujumbe ambao umeandikwa na binti yangu Zawadi, mmoja wa watu wanaojitolea katika Ramble Pictures, unaoelezea kampeni hiyo.

Nitapenda ujumbe huu uwafikie wa-Tanzania popote duniani, hasa wanadiaspora, ofisi za ubalozi, Wizara ya Maliasili na Utalii, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, na wadau wengine wote. Nilitumia miaka kadhaa kusoma maandishi ya Hemingway na kuandaa kozi ambayo ni chimbuko la filamu hii. Ninapangia kuendelea kufundisha kozi hiyo. Nawe m-Tanzania mwenzangu una fursa ya kutoa mchango wako. Tushirikiane. Tutafanikiwa. Sisi tuliokuwepo wakati Tanganyika ilipopata Uhuru tunakumbuka kauli mbiu ya Mwalimu Nyerere ya kuhimiza maendeleo ya Taifa jipya: "It can be done; play your part."

=====================================================

Hello!

My name is Zawadi Mbele, and I am contacting you today to let you know about an amazing project. Ramble Pictures, a Minneapolis-based, independent film company, recently launched a 30-day "Kickstarter" campaign in order to raise funds for the distribution of our completed documentary, Papa's Shadow.

Papa's Shadow is a personal film about Ernest Hemingway in East Africa. It explores his hunting expeditions and holds key dialogues on subjects such as race, language, and the cultures that distinguish us as citizens of the world. Featuring exclusive testimony by Ernest's only living son, Patrick Hemingway, as well as Tanzanian author and Hemingway scholar, Dr. Joseph Mbele, this documentary explores the integral role of two safaris in their shaping of an author and demise of a legend. 

Over the past four years, hard work and creative energy has been poured into making this feature-length documentary. The film has already been completed, however, we cannot show or distribute the film until we finish paying for copyright licensing. Again, please visit our Kickstarter webpage to learn more about how you can play an important role in bringing this documentary to distribution. Also, with Kickstarter, we are offering exclusive rewards with every donation, such as the new Hemingway Library Edition of "Greens Hills of Africa," signed by Patrick Hemingway. 

If there is someone else from your organization you would recommend contacting, we would be grateful to have our information passed along. If you can, please take the time to explore our webpage and let me know if you have any questions at all. You can email me directly or email Elizabeth Turner at elizabeth@ramblepictures.com.

Thank you for your time, and we look forward to hearing back from you!

Sincerely,

Zawadi Mbele
email: zawadi.mbele@gmail.com

Saturday, September 12, 2015

Wazo Kuhusu Kuchagua Kiongozi

Tunavyoelekea kwenye uchaguzi, mwezi ujao, nchini Tanzania, tunaona malumbano yanashamiri. Tunataka kujua nani anafaa kuwa kiongozi. Napenda kuchangia kifupi malumbano haya. Mchango wangu unasimama katika taaluma na utafiti.

Suala la uongozi linaingia moja kwa moja katika utafiti juu ya akili na saikolojia. Miaka yetu hii, watafiti wamekuwa wakituambia kuwa kuna aina nyingi za akili. Kuna maandishi mengi juu ya suala hilo, ambalo kwa ki-Ingereza linajulikana kama "multiple intelligence" au "multiple intelligences."

Kwa mujibu wa utafiti huo, uongozi unahitaji aina ya akili iitwayo "emotional intelligence." Ni akili inayomfanya mtu awe na mvuto kwa watu kwa haiba na mwenendo wake, uwezo wa kuunganisha watu, uwezo wa kuwafanya wafuate njia fulani kwa kutumia ushawishi, si vinginevyo. Mtu mwenye "emotional intelligence" kubwa ndiye anayefaa kuwa kiongozi.

Katika malumbano yanayoendelea miongoni mwa wa-Tanzania wakati huu wa kuelekea uchaguzi, sijaona dhana hii ya "emotional intelligence" ikitajwa. Sijaona kigezo hiki kikitajwa. Watu wanaongelea vitu kama uchapa kazi kama kigezo, lakini si "emotional intelligence." Watu wanaongelea uwezo wa kutoa hotuba ndefu, au uwezo wa kutembea kwa ukakamavu. Lakini hawaongelei "emotional intelligence."

Kwani kutoa hotuba ndefu ndio nini? Mtu unaweza kuongea kwa masaa lakini ukawa unasema umbea na upupu. Mtu mwingine anaweza kuongea kifupi, lakini akawa anatoa hoja thabiti.

Kwani nguvu za mwili na kifua kama cha mpiga ndondi ndio nini? Inahusiana vipi na uongozi? Lakini hivyo ndivyo vigezo vinavyoshabikiwa katika malumbano ya wa-Tanzania.

Hii haishangazi. Tanzania ni nchi ya watu wasio na utamaduni wa kusoma vitabu vya kuelimisha. Watanzania ni wavivu kutafuta elimu. Ndivyo walivyo, na ndivyo wanavyojiandaa kwa uchaguzi.

Wednesday, September 9, 2015

Vijana Wameonana Na Mzee Patrick Hemingway

Leo nimepata ujumbe na picha kutoka kwa Jimmy Gildea, anayeonekana kushoto kabisa pichani hapa kushoto, kwamba walikuwa mjini Bozeman, Montana, wakingojea kuonana na Mzee Patrick Hemingway na mkewe Mama Carol.

Jimmy alikuwa ni mmoja wa wanafunzi wangu katika kozi ya Hemingway in East Africaambayo nilifundisha Tanzania mwezi Januari mwaka 2013. Kutokana na kozi ile, na pia safari tuliyofunga kwenda Montana kuonana na Mzee Patrick Hemingway, Jimmy ametengeneza filamu iitwayo Papa's Shadow, ambayo kwa kiasi kikubwa inatokana na kozi ile.

Katika filamu hii, ambayo si ya maigizo, Mzee Patrick Hemingway na mimi tunaongelea maisha na maandishi ya baba yake, Ernest Hemingway, na tunaongelea kwa undani zaidi maisha na mizunguko yake Afrika Mashariki, miaka ya 1933-34 na 1953-54, na pia falsafa yake kuhusu masuala ya maisha na uandishi. Katika kutengeneza filamu hiyo, Jimmy ameshirikiana na hao vijana wanaoonekana pichani, na wengine ambao hawamo pichani.

Nimetamani sana kama nami ningekuwa Bozeman leo kuonana na Mzee Patrick Hemingway na Mama Carol. Hata hivi, nafarijika kwamba ninampigia simu wakati wowote nikipenda. Kwa kuwa aliishi miaka yapata 25 Tanganyika (na hatimaye Tanzania), ameniambia kuwa anafurahi kuongea na mimi, kwa kuwa hana watu wa kuongea nao kuhusu Tanzania na Afrika.

Kwa upande wangu, najifunza mengi kutoka kwa Mzee Patrick Hemingway, juu ya Ernest Hemingway, waandishi wengine, historia ya Tanganyika, na mambo mengine mengine. Pia ninaguswa kwa jinsi anavyokipenda kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Hata katika filamu ya Papa's Shadow anakitaja na kukinukuu. Katika hiyo picha ya pili, tuliyopiga nyumbani mwake mjini Craig, Montana, anaonekana Mzee na Mama Carol Hemingway, na kitabu kiko mezani hapo mbele yake.

Tuesday, September 8, 2015

Udini Katika Kampeni za Urais

Katika kipindi hiki cha kampeni za urais nchini Tanzania, tunashuhudia mengi. Kwa mfano, kwa siku mbili tatu hivi tumekuwa tukisikia shutuma nyingi dhidi ya mgombea wa UKAWA, Edward Lowassa kwamba anafanya udini. Chanzo cha shutuma ni kauli anayoonekana akitoa katika video alipokuwa anaongea na waumini wa ki-Luteri. Anasikika akiomba wamwunge mkono, awe m-Luteri wa kwanza kuwa rais.

Kauli hiyo imewasha moto miongoni mwa wapinzani wake, kwa mfano CCM. Wamekazana kupaaza sauti wakisema kuwa mgombea huyu hafai; anatugawanya kwa msingi wa dini, na atatuletea maafa akiwa rais.

Binafsi, sioni kama watu hao wana hoja ya msingi. Lowassa hana tabia hiyo inayosemwa. Tumemshuhudia kwa miaka anavyojumuika na waumini wa dini mbali mbali katika shughuli zao. Tumemwona akiongoza harambee za kuchangia misikiti na makanisa ya madhehebu mbali mbali sehemu mbali mbali za nchi. Kwa kufahamu alivyo na ushawishi mkubwa, viongozi na waumini wa dini mbali mbali wanafurahi kumwalika kwenye shughuli zao hizo.

Kwa kuizingatia hayo, ni wazi kuwa alichosema kwa waumini wenzake akiwaomba wampe kura siwezi kukiita udini. Siamini kama alikuwa na nia mbaya. Ni jambo la kawaida kabisa tunapokuwa na watu wa aina yetu tunazungumza kwa namna tofauti na tunapokuwa katika mazingira mengine.

Lowassa hakuwa anaongea na umma wa wa-Tanzania. Alikuwa anaongea na wa-Luteri wenzake, sawa na mimi ninavyoweza kuongea na wa-Matengo wenzangu au wa-Katoliki wenzangu, si kwa nia mbaya ya kibaguzi hata kidogo. Naweza kukubali kuwa labda Lowassa aliteleza katika kauli yake, lakini sikubali kuwa yeye anafanya udini.

Kinachonishangaza ni kuwa katibu mwenezi wa CCM, Nape Nnauye, ambaye ndiye, kama msemaji wa CCM, alitoa tamko la kumshutumu Lowassa, alisema siku kadhaa zilizopita kuwa CCM lazima ishinde uchaguzi, hata kwa goli la mkono. Aliwaambia hivyo wanahabari. Yaani aliitangazia dunia dhamira hii ya kuhatarisha amani. Ni tofauti na Lowassa ambaye alikuwa anaongea na wa-Luteri wenzake kanisani.

Nape Nnauye angekuwa ameongea na wanaCCM wenzake peke yao, huenda hata sisi wengine hatungesikia kauli yake. Hata kama tungesikia, yaani kama kauli yake ingevuja, kama ilivyovuja ya Lowassa, ningemhukumu kwa namna hiyo ninayomhukumu Lowassa. Lakini yeye amevuka mstari na kuutangazia ulimwengu dhamira ambayo ni mbaya kwa Taifa. Haoni hilo kosa lake kubwa, ila anajipa jukumu la kumshutumu Lowassa. Inanishangaza.

Friday, September 4, 2015

Gazeti la "MwanaHalisi" Lafunguliwa

Nimefurahi kuona taarifa kuwa mahakama kuu ya Tanzania imeamuru kufunguliwa kwa gazeti la MwanaHalisi ambalo serikali ya CCM ililifungia mwaka 2012. Ni ushindi kwa mmiliki wa MwanaHalisi, Saed Kubenea, na timu yake. Ni ushindi kwa watetezi wa uhuru wa vyombo vya habari.

Nilikuwa mmojawapo wa watu waliopinga wazi wazi hatua ya serikali ya kulifungia gazeti la MwanaHalisi. Ninasimamia uhuru wa kutoa mawazo, uhuru wa waandishi, kama ilivyofafanuliwa katika tangazo la kimataifa la haki za binadamu.

Taarifa tulizozipata leo ni kwamba mahakama imetamka kwamba ni juu ya Saed Kubenea kuamua kuendelea kuchapisha gazeti lake au kutoendelea. Vile vile, mahakama imeacha mlango wazi kwa Saeed Kubenea kuishtaki serikali na kudai fidia kwa kipindi chote ambapo gazeti lake lilikuwa limezuiwa.

Ni wazi kwamba, endapo Saed Kubenea atadai fidia, ambayo ni haki yake, walipa kodi wa Tanzania watabeba mzigo mkubwa. Labda watajifunza hasara ya kuiweka madarakani serikali isiyo makini, isiyoheshimu haki za binadamu ipasavyo, au kuwaweka madarakani watu wasio makini, wasioheshimu haki za binadamu ipasavyo. Tusifiche ukweli: kulifungia gazeti la MwanaHalisi, sawa na vitendo vingine vya uvunjwaji wa haki za binadamu, kumechafua jina la Tanzania.

 

Wednesday, September 2, 2015

Hotuba ya Dr. Wilbroad Slaa Kuacha Siasa

Kuhusu hotuba ya Dr. Slaa kwa waandishi wa habari akitangaza kuondokana na siasa, mengi muhimu yamesemwa na wenye upeo na tafakari nzito kunizidi. Ila nami kama raia mwingine yeyote, nina uhuru kamili wa kuongelea suala hili, kama mwananchi anavyoongea mtaani, ambayo ni haki yake.

Napenda nianze kwa kujikumbusha kwamba kwa miaka mingi, CCM wamekuwa wakimbeza Dr. Slaa, kwamba ni mzushi na mropokaji. Alipoanza kusema kuna ufisadi, CCM walimkatalia katakata, wakasema ni mzushi. Baadaye, vijana wa UVCCM wakawa wanafanya kibarua cha kumtukana Dr. Slaa.

Sasa, baada ya huyu mzushi na mropokaji kutema cheche juzi, mbele ya waandishi wa habari, nasubiri kuwasikia CCM wanasemaje. Wakisema tumpuuze kwa vile ni mzushi na mropokaji, basi ina maana kuwa UKAWA hawana sababu ya kukosa usingizi wala kujibishana naye. Kwa nini mtu ukose usingizi kwa sababu ya maneno ya mtu anayefahamika wazi kuwa ni mzushi na mropokaji?

Nitawashangaa CCM iwapo watashangilia mashambulizi ya Dr. Slaa dhidi ya Lowassa na UKAWA. Nitawashangaa.

Dr. Slaa amewaponda kabisa CCM. Sio tu kwa jinsi alivyoifananisha CCM na choo kichafu, bali kwa kauli yake kwamba serikali ya CCM ni waoga wa kuwachukulia hatua watuhumiwa wa ufisadi. Amesema kuwa CCM ni mfumo unaofuga mafisadi. Sio hivyo tu, bali amewaumbua pia wabunge wa CCM, kwamba hawasomi wanayopaswa kusoma.

Alivyosema hayo kuhusu wabunge wa CCM, nimekubaliana naye kabisa, kwani nami nilishaandika kuhusu wabunge hao nikiwaita mbumbumbu. Ushahidi ulikuwa jinsi walivyotoroka midahalo wakati wa uchaguzi wa mwaka 2010. Midahalo inaheshimiwa na watu wote wenye akili, lakini mbumbumbu hawaelewi umuhimu wake.

Umbumbumbu wa wabunge wa CCM umejidhihirisha tena na tena kwa tabia yao ya kuzomea Bungeni, na tabia ya kuunga mkono chochote kinachosemwa na serikali ya CCM. Kwa hayo yote, ninaichukulia kwa uzito upasao kauli ya Dr. Slaa kuwa wabunge wa CCM hawasomi.

Dr. Slaa hajawaonea CCM kwa hilo. Nakumbuka ule mwaka Mwalimu Nyerere alipojiandaa kung'atuka uenyekiti wa CCM, alizunguka nchi nzima akikagua uhai wa chama hicho. Inaonekana hakuridhika, kwani kuna siku alisema kuwa wako watu katika CCM ambao hata mtihani kuhusu "Azimio la Arusha" hawawezi kupasi. Kwa hivyo Mwalimu alishabaini umbumbumbu katika CCM tangu miaka ile ya katikati ya themanini na kitu.

Sasa, nikijumlisha hayo yote, nakuta kwamba Dr. Slaa ametuambia kuwa Tanzania inaendeshwa na mbumbumbu wasiosoma. Inaendeshwa na vipofu. Hilo ni janga kwa Taifa. Halafu ukiongezea na lile wazo la kuwa CCM ni kama choo kichafu, unaona wazi kuwa Dr. Slaa amemwaga hadharani mambo mazito dhidi ya CCM.

Sasa katika hali hii, nikiangalia wagombea wawili wa urais, yaani Magufuli na Lowassa, naona kuwa tafsiri ya kauli za Dr. Slaa ni kuwa UKAWA wamemtoa Lowassa chooni, lakini Magufuli ameng'ang'ania kubaki chooni. Ningekuwa mpiga kura, kura yangu ningempa huyu Lowassa aliyelopolewa kutoka chooni kuliko huyu Magufuli ambaye amepania kufia humo chooni.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...