Wednesday, December 30, 2015

Nimekutana na Mdau wa Miaka Mingi

Leo nimekutana na mdau wangu wa miaka mingi, Dr. Barbara Poole Galyen, ambaye anaishi California. Kwa siku chache hizi za Krismasi na Mwaka Mpya, yuko hapa Minnesota kwa ndugu zake. Kwa kupitia facebook tuliwasiliana na leo nilikwenda mjini Lakeville alikofikia.

Dr. Galyen na mimi tulifahamiana mwaka 1995, wakati nilipokuwa natafiti masimulizi ya jadi na tamaduni mkoani Mwanza. Utafiti huo ambao nilifanya tangu mwaka 1993 hadi 1996 uligharamiwa na shirika la Earthwatch. Dr. Galyen alikuwa mmoja wa watu kutoka nchi mbali mbali waliokuwa wanakuja Tanzania kushiriki utafiti wangu. Yeye alikuja wakati wa utafiti kisiwani Ukerewe.

Kwa kauli yake mwenyewe, huu ulikuwa mwanzo na msingi wa yeye kuipenda Afrika, hadi akaenda kufanya kazi Kenya katika United States International University, ambapo nilimtembelea mwaka 1997. Hatimaye alianzisha kampuni ya ushauri kuhusu masuala tamaduni ulimwenguni. Shughuli hizi, ambazo zinafanana na zangu, zimempa fursa ya kuzunguka sehemu mbali mbali za dunia na kujenga mtandao wa kimataifa wa washiriki.

Leo imekuwa furaha kubwa kuonana tena baada ya miaka mingi, kubadilishana mawazo na kupiga michapo. Nilimchukulia nakala ya kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ambamo nimegusia mambo yaliyotokana na utafiti wangu wa Earthwatch.

Dr. Galyen mwenyewe katika ukurasa wake wa facebook, ameandika kuhusu kukutana kwetu leo:

I enjoyed a wonderful visit with Dr. Joseph Mbele who was the one who originally introduced me to Africa in 1995 on an "Earthwatch" adventure. I give him credit for changing my life completely after I moved to Kenya as a result of our fascinating studies on a remote island in Lake Victoria, TZ. Born in Tanzania, Dr. Mbele is currently a professor at St. Olaf College in MN where he continues to work on special projects around the world! He's inspiring me again to get more involved in heart-felt projects globally.

Monday, December 28, 2015

Kitabu Juu ya Charles Dickens

Siku chache zilizopita, niliingia katika gereji yangu ambayo imefurika vitabu. Katika kufukua fukua, nilikiona kitabu Dickens, kilichotungwa na Peter Ackroyd. Sikumbuki nilikinunua lini na wapi, ila niliamua kukichukua, kwa lengo la kukipitia angalau juu juu. Nina vitabu kadhaa vilivyotungwa na Dickens. Baadhi nimevisoma na baadhi sijavisoma.

Dickens ni kati ya waandishi ambao watu wa rika langu tuliwasoma miaka ya ujana wetu Tanzania, tukawapenda sana. Kutokana na mvuto huu, nimeandika juu ya Dickens mara kadhaa katika blogu hii. Mifano ni hapa, na hapa. Kwa hivyo, nilivyokigundua kitabu cha Dickens katika gereji,  nilifurahi, nikakichukua hima.

Nilikuwa nafahamu jina la mwandishi Peter Ackroyd, ingawa sikumbuki kama nimewahi kusoma kitabu chake chochote. Katika kupitia taarifa kwenye jalada la kitabu chake cha Dickens, nimeona orodha ya vitabu alivyoandika na umaarufu wake. Kwa mfano, amejijengea heshima kubwa kwa kuandika vitabu vya historia na wasifu wa waandishi kama William Shakespeare na William Blake .

Kitabu cha Dickens ni wasifu wa Dickens, maelezo kuhusu maisha yake na maandishi yake, pamoja na maelezo kuhusu jamii alimoishi na kuandika. Ni kitabu kilichosheheni uchambuzi wa maandishi ya Dickens, sambamba na uchambuzi wa uhusiano baina ya maandishi hayo na jamii. Ni matunda ya utafiti wa kina na mpana. Dickens ni hazina kubwa, kitabu chenye kurasa 1195.

Nimekuwa nikikipitia kwa mshangao juu ya juhudi na umakini uliotumika katika utafiti na uandishi wake. Ninafahamu kuwa wenzetu wa nchi kama za Ulaya na Marekani wana jadi ya kufanya utafiti wa kina na kuandika kwa umakini kuhusu waandishi wao maarufu. Kwa mfano, kuna vitabu vya aina hiyo juu ya William Shakespeare, Johann Wolfgang von Goethe, Henrik Ibsen, Leo Tolstoy, Mark Twain, Ernest Hemingway, na William Faulkner.

Tukijifananisha na hao wenzetu, sisi wa-Tanzania tumefanya utafiti gani na tumeandika nini juu ya waandishi wetu maarufu kama Mgeni bin Faqihi na Shaaban Robert? Hakuna chochote ambacho tumefanya kinachoweza kufananishwa na majuzuu makubwa aliyoandika Michael Reynolds juu ya Ernest Hemingway, achilia mbali majuzuu waliyoandika wengine juu ya huyu huyu Charles Dickens. Labda, kwa kutafakari hayo tutagundua na kukiri kuwa tuna njia ndefu mbele yetu.

Saturday, December 26, 2015

Jólabókaflóð: Mafuriko ya Vitabu Nchini Iceland

Nchi ya Iceland inaongoza ulimwenguni kwa usomaji wa vitabu, na pia kwa asilimia ya watu wanaochapisha vitabu. Hilo linatosha kuipambanua nchi ile. Lakini kuna pia jadi iitwayo Jólabókaflóð, yaani mafuriko ya vitabu, ambayo hutokea majira ya Krismasi.

Kila mwaka, kuanzia mwezi Septemba hadi Desemba, pilika pilika zinazohusiana na vitabu zinapamba moto. Wachapishaji wa vitabu wanaongeza juhudi ya kutangaza vitabu, na jamii nzima huwa katika heka heka ya kununua vitabu. Mazungumzo na malumbano kuhusu vitabu hushamiri kila mahali.

Mwezi Novemba, katalogi kubwa ya vitabu iitwayo bókatíðindi inachapishwa na kugawiwa bure karibu kila nyumba. Katalogi hii huorodhesha vitabu karibu vyote vilivyochapishwa katika mwaka husika. Kadiri Krismasi inavyokaribia, shughuli ya kuzawadiana vitabu inapamba moto. Kilele huwa ni tarehe 24 Desemba, ambayo ni mkesha wa Krismasi. Watu hutumia mkesha wa Krismasi wakisoma vitabu.

Taarifa hizo sikuwa ninazifahamu, hadi leo. Sikujua kuwa utamaduni wa Iceland umefungamana na vitabu kiasi hicho. Nimejikuta ninawazia hali ilivyo nchini mwangu Tanzania. Nimekumbuka makala niliyoandika katika blogu hii nikiwazia ingekuwaje iwapo wa-Tanzania tungeanzisha utamaduni wa kupeana vitabu kama zawadi ya Idd el Fitr au Krismasi.

Je, sisi wa-Tanzania tunaweza kuthubutu kuwapelekea wa-Tanzania wenzetu vitabu kama zawadi ya sikukuu au ya sherehe kama arusi? Tafakari mwenyewe.

Wednesday, December 23, 2015

Ninajivunia Binti Huyu: Bukola Oriola

Nimefurahi kupata taarifa kuwa Rais Obama amemteua Bukola Oriola, kuwa mjumbe katika tume ya kumshauri kuhusu masuala ya usafirishwaji wa ghilba na utumikishwaji wa binadamu, kama ilivyotangazwa katika taarifa hii. Bukola ni binti kutoka Nigeria anayeishi hapa Minnesota, Marekani. Nimemfahamu tangu mwaka 2009, kwa kusoma taarifa zake katika magazeti ya wa-Afrika hapa Minnesota.

Niliguswa kwa namna ya pekee niliposoma kauli yake kuwa alikuwa ameandika mswada wa kitabu bali hakujua auchapishe vipi. Kwa kuwa nilikuwa na uzoefu wa kujichapishia vitabu, dhamiri yangu ilinisukuma niwasiliane naye ili nimsaidie. Nilielezea kisa hicho katika blogu hii.

Baada ya kitabu chake, Imprisoned: The Travails of a Trafficked Victim kuchapishwa, niliendelea kumhamasisha. Kwa mfano, nilimwalika kwenye tamasha la vitabu mjini Minneapolis tarehe 10 Oktoba, 2009, ambalo nilikuwa nashiriki. Nilitaka yeye kama mwandishi chipukizi aone na kujifunza kazi inayomngoja mwandishi baada ya kuchapisha kitabu. Alikuja, tukapiga picha inayoonekana hapa kushoto tukiwa kwenye meza yangu.

Kitabu kilimfungulia milango. Alikuwa anazunguka sehemu mbali mbali kutoa mihadhara kuhusu utumwa na mateso wanayopata wanawake wanaorubuniwa, kutoroshwa, kutekwa, na kisha kutumikishwa na kunyanyaswa. Alianzisha kipindi cha televisheni na pia taasisi aliyoiita The Enitan Story. Yote hayo ni kwa ajili ya kuwasaidia waathirika na kuielimisha jamii kuhusu tatizo hili ambalo limeota mizizi duniani.

Ninafurahi kwa mafanikio ya binti huyu. Naye, kwa kukumbuka nilivyomsaidia, aliandika ifuatavyo katika utangulizi wa kitabu chake:

     I would also like to thank those who worked with me to get this book published. My profound gratitude goes to Prof. Joseph Mbele of St. Olaf College, Northfield, Minnesota, who showed me how to get my book published, otherwise it would have been another Word Document on my computer. It would have not been able to give the message of hope to the hopeless. God bless you sir.

Kitendo cha Rais Obama kumteua Bukola kwenye tume hiyo ni heshima kubwa kwake. Hapa Minnesota na Marekani kwa ujumla watu wamezipokea taarifa hizi kwa furaha. Nchini kwake Nigeria taarifa hii imekuwa kishindo katika vyombo vya habari. Kwa upande wangu, naona fahari kuwa niliitikia wito wa dhamiri yangu nikamwelekeza namna ya kuchapisha kitabu ambacho kilichangia na bado kinachangia mafanikio yake. Mungu ni mkubwa.

Bukola mwenyewe anatambua kuwa kuna mkono wa Mungu katika mambo anayopitia na kuyashuhudia maishani. Anaamini kuwa ana wajibu mbele ya Mungu wa kuwasaidia wanyonge, na kuwa mtetezi wa wanaonyanyaswa na kudhulumiwa. Msikilize anavyojieleza:

Saturday, December 19, 2015

Kuchapisha Vitabu Mtandaoni

Kutokana na taarifa ninazoandika katika blogu hii, na sehemu zingine, watu wengi wanafahamu kuwa nimechapisha vitabu vyangu mtandaoni. Nimeshawasaidia waandishi kadhaa wa mataifa mbali mbali kuchapisha vitabu vyao kwa mtindo huo. Kwa upande wa Tanzania, niliwahi kuongea na wanataaluma wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kuhusu suala hilo, na nilinukuliwa katika gazeti la Mwananchi.

Mara kwa mara, watu huniulizia kuhusu kuchapisha vitabu vyao. Napenda kuongelea tena suala hili, hasa matokeo ya kuchapisha vitabu mtandaoni. Kwanza, ni muhimu kufahamu kwamba kuna njia nyingi za kuchapisha vitabu mtandaoni. Ni juu ya mwandishi kuchagua. Binafsi, ninatumia njia ambayo ni rahisi kabisa, isiyo na gharama, au yenye gharama ndogo kiasi kwamba haiwi kizuizi kwangu.

Kuchapisha kwa namna hii ni rahisi sana. Mbali ya kutokuwa na gharama, haichukui muda, ili mradi mswada umeshaandaliwa kama faili la kielektroniki. Kinachobaki ni kuuingiza mswada kwenye tovuti ya kuchapishia, na haichukui dakika kumi kumaliza shughuli hii na kitabu kikawa tayari kununuliwa na watu popote ulimwenguni.

Jambo moja linalovutia sana katika kuchapisha vitabu mtandaoni kwa namna nifanyavyo ni kwamba vitabu hupatikana bila kikomo. Vinahifadhiwa kama mafaili ya kielektroniki, na huchapishwa kama kitabu halisi pale tu mdau anapoagiza nakala. Akiagiza nakala moja, inachapishwa hiyo hiyo. Akiagiza mia au elfu ni hivyo hivyo. Hakuna udhia wa kutunza shehena ya vitabu ghalani na kungojea wateja, huku vikiwa katika hatari ya kuharibiwa na unyevu, mende, au panya.

Hata hivi, nimeona kuna matatizo. Kwanza kwa upande wa mnunuzi. Ni lazima awe na namna ya kununua mtandaoni. Kwa kawaida hii inamaanisha awe na "credit card" kama vile VISA na Mastercard. Jambo la pili ni bei. Nikiangalia vitabu vyangu, naona wazi kuwa kama vingechapishwa mahali kama Tanzania kwa mtindo wa jadi, vingekuwa na bei nafuu kuliko ilivyo sasa.

Lakini, kwa upande mwingine, kama kitabu kinachapishwa kama kitabu pepe, yaani "e-book," kinaweza kuuzwa kwa bei ndogo sana, kuliko bei ya kuchapisha kwa mtindo wa jadi. Mdau anatakiwa awe na kifaa cha kuhifadhia na kusomea kitabu pepe, yaani "e-reader" au "e-book reader," kama vile Kindle au Nook.

Pamoja na kuwepo kwa vitabu pepe na vifaa vya kuhifadhia na kusomea vitabu hivyo, imethibitika tena na tena kwamba wadau wengi bado wanavitaka vitabu vya jadi, yaani vya karatasi na majalada. Mazoea haya na mapenzi ya vitabu vya jadi yamejengeka na hayaonekani kutoweka mioyoni mwa wengi.

Tekinolojia ya kuchapisha vitabu mtandaoni inawaathiri wachapishaji wa jadi kwa namna mbali mbali. Kadiri siku zinavyopita, wengi wao wanaona faida ya kuchapisha vitabu mtandaoni. Tekinolojia hii mpya inawasukuma kwenda na wakati ili wasipoteze biashara katika mazingira ya ushindani na mabadiliko yasiyoisha.

Thursday, December 17, 2015

Mdau Kanishukuru kwa Kutafsiri "Kimbunga"

Ninavyoandika katika blogu hii na blogu ya ki-Ingereza huwa sina namna ya kujua ni nani atasoma nilichoandika. Siwezi hata kujua kama niandikacho kitasomwa na yeyote. Ni kubahatisha. Kwa kutambua hilo, nimediriki kusema kwamba ninapoandika katika blogu, ninajiandikia mwenyewe.

Hata hivi, ukweli unajitokeza kuwa kuna watu wanaosoma niandikayo. Katika blogu kuna sehemu ambapo ninafuatilia na kuona takwimu za utembeleaji wa blogu na orodha ya makala zinazosomwa au kupitiwa siku hadi siku.

Nimefurahi kusoma leo ujumbe wa mdau akinishukuru kwa tafsiri yangu ya "Kimbunga," shairi la Haji Gora Haji. Ameandika:

Thank you so much for translating this poem. I'd been searching to read poems originally written in Swahili. Immense gratitude Joseph.

Nimefurahi kuwa nimempa mdau huyu angalau tone la kutuliza kiu yake kuhusu mashairi ya ki-Swahili. Amenipa motisha ya kuendelea kutafsiri tungo za ki-Swahili, ili afaidike zaidi kwa kutambua utajiri wa jadi ya tungo za ki-Swahili ambayo imekuwepo na kustawi kwa karne kadhaa.

Ninamkumbuka pia mtunzi Haji Gora Haji. Nikiweza, kwa idhini yake, kutafsiri mashairi yake na kuyachapisha kama kitabu, kama alivyofanya Clement Ndulute kwa mashairi ya Shaaban Robert, itakuwa ni jambo la manufaa katika kumtangaza na kuuelimisha ulimwengu.

Wednesday, December 16, 2015

Nimeitafsiri Sala ya Papa Francis

Nilielezea katika blogu hii nia yangu ya kuitafsiri sala ya Papa Francis ambayo ni sehemu ya waraka wake wa kitume, "Laudato Si." Papo hapo, ninafahamu vizuri kuwa kutafsiri ni suala tata. Katika ujumbe wangu, niliandika kuwa

"napenda kusema kwamba sala hii ilivyo katika ki-Ingereza ikiwa imesheheni uchaji, busara, na maudhui, imeundwa kwa lugha iliyotukuka. Ninajiuliza iwapo tunaweza kuitafsiri kwa ki-Swahili, tukahifadhi utukufu wake kwa msingi wa uhalisia wa ki-Swahili. Ninajiuliza hivyo pamoja na kufahamu jinsi suala la tafsiri lilivyo gumu na tata. Ninatarajia kujaribu kuitafsiri sala hii siku zijazo."

Hata hivi, nimejaribu kutafsiri sala ya Papa Francis, ili kuwapa angalau fununu wale ambao hawajui ki-Ingereza. Ni bora kufanya hivyo, kuliko kuacha kabisa. Ye yote anayekijua ki-Ingereza vizuri, na pia anakijua ki-Swahili vizuri, ataona kuwa nimejipa mtihani mgumu. Ninamhimiza naye ajaribu kutafsiri.

A prayer for our earth

All-powerful God, you are present in the whole universe
and in the smallest of your creatures.
You embrace with your tenderness all that exists.
Pour out upon us the power of your love,
that we may protect life and beauty.
Fill us with peace, that we may live
as brothers and sisters, harming no one.
O God of the poor,
help us to rescue the abandoned and forgotten of this earth,
so precious in your eyes.
Bring healing to our lives,
that we may protect the world and not prey on it,
that we may sow beauty, not pollution and destruction.
Touch the hearts
of those who look only for gain
at the expense of the poor and the earth.
Teach us to discover the worth of each thing,
to be filled with awe and contemplation,
to recognize that we are profoundly united
with every creature
as we journey towards your infinite light.
We thank you for being with us each day.
Encourage us, we pray, in our struggle
for justice, love and peace.

Sala Kuiombea Dunia Yetu

Mungu mweza yote, upo kila mahali

na hata katika viumbe vyako vidogo kabisa.
Unakumbatia kwa upole wako kila kilichopo.
Tufurikie nguvu ya upendo wako
ili tuuhifadhi uhai na uzuri.
Tujaze amani, ili tuishi
kama kaka na dada, bila kumdhuru yeyote.
Ee Mungu wa maskini,
tusaidie kuwanusuru waliotelekezwa na kusahauliwa katika dunia hii,

ambao wana thamani isiyo kifani machoni mwako.
Tuletee uponyaji maishani mwetu,
ili tuihifadhi dunia badala ya kuwania kuipora,
ili tustawishe uzuri, si uchafuzi na uharibifu.
Gusa mioyo
ya wale wanaowania maslahi yao tu
yanayowagharimu maskini na dunia.
Tufundishe kuibaini thamani ya kila kitu,
kujawa na uchaji na tafakari,
kutambua
 kuwa tumefungamana
na kila kiumbe
tunavyoelekea kwenye nuru yako isiyo na mwisho.
Tunakushukuru kwa kuwa nasi kila siku.

Tuhimize, tunakuomba, katika juhudi zetu
za kutafuta haki, upendo na amani.

Wednesday, December 9, 2015

Mtunzi Haji Gora Haji

Leo nimeamua kuongelea kifupi utunzi wa Haji Gora Haji wa Zanzibar, mmoja wa waandishi maarufu wa ki-Swahili wa zama zetu hizi. Nafurahi kuwa niliwahi kuonana naye mjini Zanzibar na kuzungumza naye. Panapo majaliwa, nitaandika taarifa ya mazungumzo yetu, ambayo yalihusu maisha yake katika sanaa. Ni muhimu kuutangazia ulimwengu kazi murua inayofanywa na watu wetu wenye vipaji kama Haji Gora Haji.

Nina vitabu vyake vinne: Kimbunga (Dar es Salaam: Dar es Salaam University Press, 1994), Utenzi wa Visa vya Nabii Suleiman Bi Daudi (A.S.) (Zanzibar: Al-Khayria Press Ltd, 1999), Kamusi ya Kitumbatu (Zanzibar: Express Printing Services, 2006), na Siri ya Ging'ingi (Dar es Salaam: Taasisi ya Taaluma za Kiswahili Chuo Kikuu Dar es Salaam, 2009).

Kadiri siku zinavyopita, wasomaji na wahakiki wanajitokeza na kuongelea uandishi wa Haji Gora Haji. Mifano ya kutambuliwa huko ni taarifa ya Amanda Leigh Lichtenstein, ya Ridder Samson, na ya Pascal Bacuez. Nami nimetafsiri mashairi yake mawili nikayachapisha hapa, hapa, na hapa.

Haji Gora Haji, kama walivyo watunzi wengi, wa zamani hadi leo, wamejengeka katika jadi ya fasihi simulizi. Wanaitumia jadi hii katika utunzi wao, iwe ni mashairi kama walivyofanya W.B. Yeats na Derek Walcott, au riwaya, kama walivyofanya Charles Dickens na Chinua Achebe, au tamthilia, kama walivyofanya William Shakespeare, Wole Soyinka na Ebrahim Hussein, au hadithi fupi, kama walivyofanya Lu Hsun na Ama Ata Aidoo.

Ni hivyo hivyo kwa Haji Gora Haji, kama nilivyowahi kutamka. Utumiaji wa mbinu, miundo, na hata dhamira zitokanazo na fasihi simulizi kunachangia uwezo wa tungo kugusa fikra na hisia za hadhira kwa namna ya pekee kutokana na kwamba fasihi simulizi ni urithi wa wanadamu wote. Maudhui yatokanayo na fasihi simulizi ni ya thamani kwa wanadamu wote.

Kuthibitisha zaidi namna Haji Gora Haji alivyojengeka katika fasihi simulizi, sikiliza anavyosimulia hadithi ya Paa na Pweza.


Monday, December 7, 2015

Nimesaini Vitabu Kwa Ajili ya Filamu ya "Papa's Shadow"

Wakati wa kampeni ya Ramble Pictures ya kuchangisha fedha kulipia gharama za filamu ya Papa's Shadow, nilichangia fedha kiasi na pia nakala za kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Walikuwa wameweka viwango mbali mbali vya michango ambavyo viliendana na vizawadi na vivutio kwa wachangiaji. Waliochangia dola 200 au zaidi waliahidiwa nakala ya kitabu changu kama zawadi.

Leo, Jimmy Gildea, mwanzilishi wa Ramble Pictures na mtengenezaji wa Papa's Shadow, ambaye alikuwa mwanafunzi katika kozi yangu ya Hemingway, alinifuata hapa chuoni St. Olaf, nikasaini nakala tano za kitabu changu, na kumkabidhi.

Tulipata fursa ya kuongelea habari za Ernest Hemingway, ziara yetu ya Montana, msisimko na mafanikio ya kampeni ya kuchangisha fedha, na kadhalika. Vile vile, Jimmy alinirekodi nikiwa nasoma kitabu cha Green Hills of Africa na pia nikiwa natembea katika sehemu iliyoonyesha vizuri mandhari ya chuo. Jimmy aliniuliza iwapo nina picha za ujana na utoto wangu. Anakusanya hayo ili kuyatafutia nafasi katika filamu ya Papa's Shadow, ingawa tayari ni nzuri sana, kwa jinsi nilivyoiona.

Papa's Shadow inategemewa kupatikana wiki chache kuanzia sasa, labda mwezi Februari. Si filamu ya kuigiza bali ni mazungumzo juu ya maisha, uandishi, na falsafa, ya Ernest Hemingway, hasa inavyohusiana na safari zake Afrika Mashariki, miaka ya 1933-34 na 1953-54. Sehemu kubwa ya filamu hii ni mazungumzo baina yangu na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee wa Ernest Hemingway aliye bado hai. Ni filamu inayoelimisha, si burudani.

Saturday, December 5, 2015

Kuwalea Watoto Kupenda Vitabu

Kati ya mambo yanayonivutia sana hapa Marekani ni namna wazazi wanavyowalea watoto katika utamaduni wa kupenda kusoma vitabu. Katika matamasha ya vitabu, maduka ya vitabu, na maktaba, ninawaona wazazi wakiwa na watoto. Nimewahi kuandika kuhusu suala hilo katika blogu hii. Lakini kwa kuwa hii ni mada ninayoitilia maanani sana, nimeamua kuiongelea tena.

Picha ya juu hapa kushoto ilipigwa mwaka 2008, niliposhiriki sherehe za kumbukumbu ya uhuru wa Nigeria hapa Minnesota. Nilikuwa na meza ya vitabu vyangu. Nakumbuka vizuri jinsi huyu mama m-Nigeria anayeonekana pichani alivyokuja mezani pangu na binti yake. Tulisalimiana, wakaangalia na kuvifurahia vitabu vyangu, kama inavyoonekana pichani.

Picha ya pili hapa kushoto nilipiga katika tamasha la vitabu la Deep Valley, mjini Mankato, Minnesota. Nilivutiwa na namna hao watoto walivyokuwa wanafuatana na mama yao kutoka meza hadi meza wakiangalia vitabu.

Picha ya tatu hapa kushoto nilipiga mwezi Agosti mwaka huu mjini Brooklyn Park, Minnesota, katika tamasha la Afrifest. Huyu bwana, m-Marekani Mweusi, alikuja na watoto wake kwenye meza yangu, kuangalia vitabu. Watoto hao ni wadogo sana, na sijui kama walikuwa wanajua kusoma, lakini, nilivutiwa na kitendo cha baba yao kuwaleta kuangalia vitabu.

Kwa wa-Marekani, umri wa mtoto si tatizo. Wanawasomea vitabu hata watoto wadogo sana, hasa kabla ya kulala. Watoto wanapenda kusomewa vitabu. Hapa naikumbuka video ya kusisimua inayomwonyesha mtoto mdogo akisomewa vitabu, halafu anavyoangua kilio kila anapoambiwa kuwa hadithi imeisha. Hebu iangalie.


Thursday, December 3, 2015

Kuhusu Kublogu

Nimekuwa mwanablogu tangu mwaka 2008. Ninaendesha blogu hii ya Hapa Kwetu na nyingine ya ki-Ingereza. Kublogu kuna mambo mengi. Kublogu kunanipa fursa ya kujieleza kwa uhuru. Hili ni jambo la msingi, kama alivyoelezea mwanablogu Christian Bwaya.

Lakini kublogu kuna matokeo yenye manufaa. Kumeniwezesha kuwafikia watu mbali mbali ambao wanatembelea blogu zangu. Siwezi kujua wanapata ujumbe gani katika maandishi yangu. Kama taaluma inayotufundisha, hili ni suala tata.

Ujumbe wa andiko ni zao la kazi anayofanya msomaji juu ya andiko. Na kwa kuwa wasomaji wana akili zinazotofautiana, na wana nidhamu na uzoefu tofauti wa kusoma, kila mmoja anaibuka na ujumbe tofauti, kwa kiwango kidogo au kikubwa.

Niliwahi kuelezea kwa nini ninablogu, lakini sidhani kama nilikuwa na majibu ya uhakika. Baadaye, katika kutafakari suala hili, nilifikia hatua ya kutamka kwamba ninablogu kwa ajili yangu mwenyewe. Labda huu ndio ukweli wa mambo.

Imani iliyojengeka katika jamii ni kuwa mwandishi anawaandikia wasomaji. Tumezoea kuona waandishi wakiulizwa wanamwandikia nani, nao wanaelezea walengwa wao. Jadi hii na imani hii imekosolewa kwa uhodari na Roland Barthes katika makala yake, "The Death of the Author."

Makala hii ya Barthes naona inaipa uzito hoja yangu kuwa ninapoblogu ninajiandikia mwenyewe. Sijui ni nani atasoma au anasoma ninachoandika. Kusema kwamba ninawaandikia wasomaji ni kama kuota ndoto. Ni kujiridhisha kwa jambo ambalo halina uhakika bali ni bahati nasibu. Nikisema ninajiandikia mwenyewe ninasema jambo la uhakika.

Tuesday, December 1, 2015

Nilitembelea Duka la Vitabu la Amkal

Tarehe 23 Mei, 2015, nilitembelea duka la vitabu la Amkal mjini Minneapolis, kama nilivyoripoti katika blogu hii. Ni duka la wa-Somali ambalo linauza zaidi vitabu vinavyohusu dini ya ki-Islam. Siku hiyo nilinunua kitabu kiitwacho Jesus: Prophet of Islam. Ninapenda kuongelea, kwa kifupi na wepesi kabisa, mawazo yanayonijia ninapokumbuka ziara yangu katika duka lile.

Jambo la msingi kwamba katika kuishi kwangu hapa Marekani, nimeona jinsi wa-Afrika wa nchi mbali mbali wanavyovithamini vitabu. Kwa mfano, nimewahi kuwaongelea wa-Kenya.

Wa-Somali ni mfano mwingine. Nimekutana na wa-Somali wanaoishi hapa Minnesota ambao wanaandika vitabu. Nimejionea wanavyojitokeza kuwasikiliza waandishi wa vitabu wa ki-Somali. Mfano ni Nuruddin Farah, ambaye huonekana hapa Minnesota mara kwa mara, ingawa makao yake kwa miaka hii ni Afrika Kusini. Wanamheshimu kwa jinsi anavyowakilisha taifa lao katika ulimwengu wa uandishi.

Kwa ujumla, hao wa-Somali ni wakimbizi au wahamiaji. Lakini pamoja na kadhia hiyo, pamoja machungu waliyoyapitia, wameshikilia umuhimu wa vitabu na elimu. Katika vyuo vya hapa Minnesota, kama vile Chuo Kikuu cha Minnesota, Metropolitan State University. Mankato State University, South Central College, na Minneapolis Community and Technical College, wanafunzi wa ki-Somali ni wengi. Wanawekeza katika elimu. Wanajijengea mtaji ambao wataweza kuutumia kwa maendeleo ya nchi yao.

Suala la elimu wanalishughulika kwa namna nyingine pia, kama vile magazeti na vituo vya televisheni. Hali hii nimeiona pia miongoni mwa wa-Afrika wengine, kama vile wa-Kenya na wa-Ethiopia. Kwa kutumia njia hizo, wanazitangaza nchi zao na shughuli zao, kama vile biashara. Ninawaona ni mfano wa kuigwa.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...