Tuesday, December 13, 2011

Leo Nimekuwa Marley Katika Hadithi ya Charles Dickens

Leo katika idara yetu ya ki-Ingereza tulifanya onesho la tamthilia kutokana na hadithi ya A Christmas Carol iliyotungwa na mwandishi maarufu Charles Dickens.

Watu tuliosoma shule zamani tunakumbuka sana vitabu vya Charles Dickens, hasa Oliver Twist. Ni nani asiyekumbuka wahusika wa hadithi hii, kama vile Oliver Twist mwenyewe, The Artful Dodger, na Fagin m-Yahudi? Ilikuwa raha kusoma miaka ile, na tulikuwa tunapenda hata kukariri baadhi ya kauli za hao wahusika.

Basi katika kipindi hiki cha kuelekea Krismasi, idara yetu ina jadi ya kufanya jambo la kumbukumbu na burudani. Kwa miaka kadhaa, tumekuwa tukiigiza mchezo huu unaotokana na riwaya hii ya Dickens. Katika A Christmas Carol kuna wahusika wakuu kadhaa, na Scrooge ndio kinara. Huyu ni mfanyabiashara bahili, ambaye zamani alikuwa na mshiriki wake wa kibiashara aliyeitwa Jacob Marley.

Wakati hadithi inapotokea, tunaambiwa kuwa Jacob Marley alifariki miaka saba iliyopita. Tunachoona ni mzimu tu wa Marley, ambao unamtokea Scrooge kwa namna ya kumfanya afadhaike. Ila mzimu wa Marley unamwachia maaagizo muhimu. Basi, nilipewa jukumu la kuigiza kama mzimu wa Marley. Nilishafanya hivyo pia mwaka juzi.

Tuliamua kuwa niwe Marley kwa namna ya mwanamuziki wa reggae Bob Marley, ili kuleta usasa na kunogesha hadithi. Nilivaa kofia iliyoshonewa rasta, ambayo ilinunuliwa Jamaica na profesa mstaafu wa idara yetu, Jonathan Hill. Nilionekana kama m-Jamaica kabisa. Wakati wote wa onesho nilijitahidi kuongea kama m-Jamaica, na watazamaji wa onesho letu walibaki hawana mbavu. Picha tuliyopiga leo baada ya onesho nimeiweka hapa. Kuna picha ambayo tulipiga mwaka juzi ila sijapata nafasi ya kuitafuta. Ningeiweka hapa pia.

Hadithi hii ya Dickens, kama hadithi zake zingine, inavutia na ina maadili mema, kwani, hatimaye Scrooge anabadilika. Mwanzoni alikuwa bahili na katili asiye na huruma kwa yeyote, na wala hataki hata kusikia maneno kama "Heri ya Krismas." Kwake zote hizo zilikuwa ni kero na upuuzi. Hatimaye, kutokana na mambo ya ajabu yanayomtokea, anabadilika na kuwa mtu mwenye roho njema ya kuvutia.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...