Tuesday, December 13, 2011

Posho za Wabunge Hazitoshi

Yapata mwaka 1997 nilipokuwa katika utafiti Mwanza, mimi na washiriki wa utafiti tulikutana na mbunge katika hoteli ya Ramada. Sikumbuki alikuwa ni mbunge wa sehemu gani nchini. Katika maongezi yetu, alilalamika kwa masikitiko kuwa wa-Tanzania wanaamini kuwa mbunge ni mtu mwenye hela sana. Akatoa mfano wa maisha yake mwenyewe, kwamba nyumbani kwake, watu wamejaa kwenye makochi muda wote. Mchana wako hapo, na usiku wanalala hapo. Na yeye anawajibika kuwalisha na kuwanywesha siku zote.

Wakati huu ambapo wa-Tanzania wanalumbana kuhusu kuongeza posho za wabunge, mimi nakumbuka kilio cha yule mbunge. Nasita kuwalaumu wabunge wanapodai kuongezewa posho. Naamini kuwa posho zao hazitoshi.

Tatizo ni sisi wa-Tanzania, sio wabunge. Mtu akishapata ubunge, tunamtegemea atufanyie mambo mengi sana yanayohitaji hela. Mbunge akiingia baa, tunategemea ofa zake, tena za uhakika, sio soda za reja reja. Tunamtegemea achangie hela nyingi kwenye vikao vya "send-off," kipaimara, arusi, na kadhalika. Asipochangia hela nyingi, hatutamhurumia. Na kama ana ndoto ya kugombea tena, anafanya bahati nasibu.

Mbunge asipotembelea eneo lake la uwakilishi, akaweza kujionea kila sehemu na kukutana na watu wote, tutamwona hafai. Bila hela nyingi, mbunge hawezi kutekeleza hayo. Na ukizingatia kuwa kila apitapo, anatakiwa kuchangia misiba, sherehe, na harambee, ni wazi kuwa hata akipewa posho ya laki tatu kwa siku, haitatosha.

Kwa kifupi, kitu cha kwanza kinachotakiwa ni kwa sisi wananchi kubadilika. Tusiwe mzigo kwa mbunge. Tukitekeleza hilo, tutakuwa na haki ya kuhoji ongezeko la posho za wabunge. Lakini kama tabia zetu ndio hizo nilizoelezea, za kutegemea mbunge achangie hela nzito kila shughuli, na utitiri wa watu kuhamia nyumbani kwa mbunge, malalamiko yetu kuhusu ongezeko la posho za wabunge ni unafiki.

Zaidi ya hayo niliyosema, wa-Tanzania wengi ni mbumbumbu. Wakati wa kampeni, tulijionea jinsi wagombea wa chama fulani walivyokuwa wanawahonga wapiga kura kwa khanga, ubwabwa, na kadhalika. Hao wa-Tanzania mbumbumbu wanaafiki na wanategemea hayo. Sasa basi, wabunge wa aina hii wakisema wanahitaji posho ziongezwe, huenda wanafanya maandalizi ya uchaguzi ujao, kwani wapiga kura mbumbumbu watategemea tena hizo khanga, ubwabwa na bia.

Hoja yangu inarudi pale pale, kwamba tatizo linaanzia kwa wananchi.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...