Thursday, December 29, 2011

Mahojiano na Profesa Mbele, "Kombolela Show"

Nimeona niwaletee wadau mahojiano niliyofanyiwa katika "Kombolela Show," Oktoba 2, 2010. Mwendesha mahojiano alikuwa Metty Nyang'oro. Kwa jinsi mtandaoni kunavyofurika taarifa, nimeona si vibaya kuyaleta tena mahojiano haya, ili wadau wayasikie na kuyatafakari na kuchangia, endapo watajisikia kufanya hivyo, kwani elimu haina mwisho, wala haina mwenyewe.

Tuesday, December 27, 2011

Hadithi za wa-Matengo Zatamba Ughaibuni

Hivi karibuni, nilipata ujumbe kutoka kwa Profesa Paschal Kyoore wa Chuo cha Gustavus Adolphus kuwa anatunga kozi mpya, "The African Trickster," akaomba ushauri wangu, kwani mada hiyo ya "trickster" nimeifanyia utafiti na kuandika makala kwa miaka mingi.

Hatimaye, Profesa Kyoore ameniletea ujumbe kuwa ameshaagiza nakala za kitabu cha Matengo Folktales kwa ajili ya darasa hilo. Kisha angependa siku moja niende kuongea na wanafunzi wake, nami nimekubali.

Ninafurahi sana ninapoona watu wa ughaibuni wakipata fursa ya kujifunza mambo ya kwetu, na hadithi za jadi ni hazina mojawapo kubwa, kama nilivyoelezea hapa. Ni fursa kwetu na kwa walimwengu kutambua mchango wa wahenga wetu kwa utamaduni wa dunia, kwani katika hadithi zao, wahenga waliongelea na kutafakari kila aina ya suala linalomkabili binadamu, sawa na watu walivyofanya watu wa mataifa mengine.

Hadithi za wa-Matengo zinatumika katika vyuo mbali mbali hapa Marekani, kama nilivyoelezea hapa. Yapata miaka miwili iliyopita, nilipata pia ujumbe kutoka kwa mwalimu mmoja Uingereza, ambaye alikuwa anatafuta nakala ya Matengo Folktales kwa ajili ya kufundishia. Nilimpelekea.

Tunawajibika kuzirekodi hadithi hizi na masimulizi mengine, kwani vijana wa leo hawazielewi, na wanatekwa na tamaduni za nje, zinazoenezwa kwetu hasa kwa njia ya machapisho, televisheni, na mtandao wa kompyuta. Mimi nilirekodi hadithi za wa-Matengo nilipokuwa mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, miaka yapata 40 iliyopita. Halafu nilitumia miaka yapata 23 kuzishughulikia hadithi zilizomo katika Matengo Folktales, kwa maana ya kuzitafsiri na kuziandikia uchambuzi, ndipo nikachapisha kitabu. Lakini, shughuli hii haina mwisho, na kitabu kimoja hakitoshi. Ni kama changamoto tu. Kwa walioko Tanzania, kitabu kinapatikana Dar es Salaam, simu namba 0754 888 647 na 0717 413 073.

Friday, December 23, 2011

Maongezi na Wanafunzi Waendao Tanzania

Profesa Barbara Zust, wa Chuo cha Gustavus Adolphus, amenialika kwenda kuongea na wanafunzi anaowaandaa kwa safari ya Tanzania. Anafundisha masomo ya uuguzi, na mwezi Januari anawapeleka wanafunzi Tanzania kujifunza masuala ya afya na matibabu katika utamaduni tofauti na ule wa Marekani.

Profesa Zust ameshawapeleka wanafunzi Tanzania mara kadhaa. Katika kuwaandaa, hutumia kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences na pia hunialika nikaongee nao. Anajisikia vizuri sana ninapokutana na wanafunzi wake kujibu masuali yao na kuwapa maelezo mbali mbali, nami huwa nafurahi kukutana na wanafunzi hao wanaosomea taaluma ambayo sikusomea, ila ni wazi kuwa wanafaidika na mawazo yangu kuhusu jinsi tofauti za tamaduni zinavyohusika katika taaluma yao.

Hapa kushoto ni picha tuliyopiga na wanafunzi waliokuwa wanaenda Tanzania mwaka 2009. Tulikuwa kwenye chumba cha mkutano cha kanisa la Shepherd of the Valley, mjini Apple Valley. Habari za mkutano wetu niliziandika hapa.








Hapa kushoto ni picha tuliyopiga na wanafunzi waliokuwa wanakwenda Tanzania mwaka 2010. Tulikutana Mount Olivet Retreat Center, mjini Lakeville. Habari zaidi niliziandika hapa.

Wanafunzi hao na profesa wao wanapata fursa ya kuona sehemu mbali mbali za Tanzania, kama vile hospitali ya Ilula, kijiji cha Tungamalenga, na hifadhi ya Taifa ya Ruaha. Sehemu zote tatu ziko Iringa. Wanafunzi hao wanaguswa sana na ziara yao Tanzania. Nimeshasoma baadhi ya maoni yao.

Mwaliko wa sasa ni wa kuongea na wanafunzi tarehe 2 Januari. Insh'Allah, nitaleta picha na taarifa.

Tuesday, December 20, 2011

Mdau Mwingine, Mwanafunzi, Kaja

Mara kwa mara naandika habari za wasomaji wa maandishi yangu wanaonitembelea, au ninaokutana nao sehemu mbali mbali.

Jana, baada ya kumaliza kufanya mtihani wa mwisho wa somo langu la fasihi ya Afrika Kusini, kaja ofisini mwanafunzi Logan. Alikuja na nakala ya kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ili nikisaini. Nilisaini, tukaendelea na michapo. Logan alisoma somo langu jingine mwaka jana.

Chuo Cha St. Olaf kinaamini kuwa ni muhimu wanafunzi waufahamu ulimwengu nje ya Marekani. Kilinileta hapa, mwaka 1991, kuanzisha masomo katika idara ya ki-Ingereza juu ya uandishi wa ki-Ingereza kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Wanafunzi wanavutiwa na fursa hii ya kupanua upeo wao, kuzifahamu jamii na tamaduni mbali mbali.

Monday, December 19, 2011

Makari Hodari

Kwa sisi tuliosoma shule ya msingi zamani, Makari Hodari ni jina tunalolikumbuka sana. Tulisoma habari zake zilizotungwa na Padri Alfons Loogman, mwandishi wa vitabu vya Someni Bila Shida na Someni Kwa Furaha. Kwa kweli, padri huyu aliziteka nyoyo zetu watoto, akatufanya tupende kusoma. Aliandika vitabu kadhaa vya masomo ya ki-Swahili na hata mwongozo kwa walimu kuhusu kufundisha kusoma.

Nakumbuka kuwa katika shule yangu ya msingi ya Litembo, tulikuwa tunasoma hadithi ya Makari Hodari kwa kuiimba. Watoto wote darasani tulikuwa tunaimba kwa pamoja, kwa furaha. Hadi leo naweza kuimba tulivyoimba. Na mwalimu alikuwa akiimba nasi. Pamoja na utamu wa hadithi, tulivutiwa na picha.

Nikiitafakari hadithi ya Makari Hodari, naona kuwa ilijengeka katika mfumo wa zile hadithi za kale za mashujaa, ambazo zinasimuliwa katika tamaduni mbali mbali. Kwa mfano, Wa-Haya wana hadithi za mashujaa kama Mugasha, Rukiza, na Kilenzi. Wa-Chagga wana hadithi ya Mrile, wa-Swahili hadithi ya Liongo Fumo. Hadithi ya Makari Hodari imerahisisha na kufupisha masimulizi ili yawavutie watoto kwa umri wao. Lakini inataja vitendo vya ushujaa, majigambo, na nafasi ya mama katika maisha ya shujaa.

Leo ni mara ya pili kwangu kuandika kuhusu vitabu hivi vya Padri Loogman katika blogu hii. Nilipoandika mara ya kwanza, ujumbe wangu uliwafikia watu wengi, hasa baada ya kutokea katika blogu ya Michuzi. Leo nimeona niwaletee wadau hadithi ya Makari Hodari, waione pia picha yake na picha ya mama yake.

Saturday, December 17, 2011

Wanafunzi Wangu Wameondoka Tanzania

Mapema leo, wanafunzi niliowaleta Tanzania mwaka huu wameondoka nchini, baada ya kumaliza masomo ya miezi kadhaa Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam. Wanafunzi hao nami tunaonekana katika picha hapa kushoto, tuliyopiga kwenye hoteli ya Wilolesi, mjini Iringa, tarehe 10 Agosti.

Kama nilivyoelezea mara kadhaa katika blogu zangu, tulizunguka sehemu mbali mbali, kama vile Kalenga, Matema Beach, Lyulilo na Bagamoyo. Baada ya mizunguko hiyo niliwafikisha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, nami nikarejea Marekani kwani muhula wa masomo ulikuwa unaanza.

Ni faraja kuona wameondoka salama, kwani nilikuwa na wasi wasi kutokana na taarifa za migomo, vurugu na mabomu Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Kwa miaka yote niliyofundisha hapa Marekani nimekuwa mshauri katika programu kadhaa zinazopeleka wanafunzi Tanzania na nchi zingine za Afrika, kama nilivoelezea hapa. Huwa tunawaambia hao wanafunzi kuwa wasishiriki maandamano au migomo katika nchi husika. Kwa upande wa Tanzania, nimekuwa mwepesi kuwaeleza jinsi tulivyo nchi ya amani na utulivu.

Programu hizi zina manufaa mengi sio tu kwa hao wanafunzi, bali kwa wa-Tanzania humo mitaani. Kwa upande wa mahusiano baina ya nchi na nchi, programu hizi zinachangia maelewano baina ya Tanzania na Marekani. Marekani yenyewe kwa miaka mingi imewapokea na kuwaelimisha wa-Tanzania wengi, na wengi wao sasa ni watu wenye madaraka serikalini, katika taasisi mbali mbali, na katika jamii kwa ujumla. Hata kwa upande wa uchumi, mwanafunzi wa kigeni anayesoma Tanzania analiingizia Taifa hela nyingi za kigeni, kumzidi mtalii mara dufu.

Lazima niseme ukweli na kuelezea duku duku yangu. Kutokana na haya mabomu ya polisi ambayo yamekuwa jambo la kawaida vyuoni na mitaani nchini Tanzania, najiuliza kama inawezekana kuendelea kuipigia debe Tanzania kama nilivyozoea. Jambo la kufariji ni kuwa kwa ujumla, wanafunzi wa ki-Marekani wanaoenda Afrika wanaporudi Marekani wanasema kuwa pamoja na matatizo yote, wanakuwa wamejijengea upendo kwa Bara hili. Hii inatokana na ukarimu wanaoupata miongoni mwa watu vijijini, mitaani na mijini.

Friday, December 16, 2011

Vitabu Kama Zawadi ya Idd el Fitr na Krismasi

Hebu fikiria: sikukuu ya Idd el Fitr au Krismasi imewadia na unataka kuwapa zawadi ndugu na marafiki zako, wa-Tanzania wenzako. Unaamua kwenda kwenye duka la vitabu, na unawanunulia nakala za kitabu kama Kufikirika cha Shaaban Robert, au Binadamu na Maendeleo cha Mwalimu Nyerere, au kwa wanaojua ki-Ingereza, The Tempest cha Shakespeare. Unawafungia vizuri, kisha unawapelekea. Je, watajisikiaje hao wa-Islam na wa-Kristu wa Tanzania?

Miaka ya tisini na kitu, katika jumuia ya mawasiliano ya mtandaoni iitwayo Tanzanet, ambayo wanachama wake ni wa-Tanzania na marafiki wa Tanzania, niliwahi kuandika, kiutani, kwamba siku za usoni huenda nikaamua kwamba, kwenye mialiko ya arusi nisipeleke kreti ya bia, bali kreti ya vitabu. Ingawa ulikuwa ni mchapo, nilikuwa na jambo muhimu kichwani, kwani ni kweli kuwa vitabu ni hazina, na ni bora kuliko bia.

Hapa Marekani, ni kawaida watu kutoa au kupokea zawadi ya vitabu. Msimu kama huu wa Krismasi, watu wengi wananunua vitabu ili kuwapa zawadi wenzao. Hata kwenye arusi, mtu unaweza kutoa zawadi ya kitabu.

Je, ukimpa m-Tanzania zawadi ya kitabu wakati wa Idd el Fitr au Krismasi, itakuwaje? Tafakari hilo.

Thursday, December 15, 2011

Hatimaye Itabidi Nielezee Nilivyotoka Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam

Mwaka 1991 niliondoka Chuo Kikuu Dar es Salaam, nikaja kufundisha Chuo cha St. Olaf hapa Marekani. Kulikuwa na mlolongo wa masuala yaliyonifanya nikaondoka, baada ya kuwa mwalimu pale kuanzia mwaka 1976. Sijaelezea masuala hayo, ingawa yamo katika maandishi kwenye makabrasha, ambayo yalikuwa mawasiliano rasmi baina ya wahusika.

Mwaka jana, nikiwa maeneo ya Mwenge, Dar es Salaam, na marafiki zangu, nilikutana na Profesa Sam Maghimbi wa Chuo cha Elimu cha Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam. Nilishangaa alivyokumbushia nilivyotoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, na marafiki zangu wakasikia. Nilifarijika kuona kuwa kumbukumbu bado zipo kiasi hiki.

Wako wengi wanaokumbuka nilivyofundisha Chuo Kikuu Dar es Salaam, na jinsi nilivyoondoka. Lakini, kwa jinsi miaka inavyopita, wanafikia umri wa kustaafu, na wengine wamefariki. Nami natatizwa na fikra ya wa-Tanzania wengi za kudhani kila m-Tanzania anayeenda kufanya kazi nje hana sababu nyingine bali kufuata maslahi binafsi. Hata mafisadi waliozagaa nchini nao wanaimba wimbo huo huo waonekane wazalendo. Jambo hili linanikera, na ndio maana naona itabidi niandike habari zangu.

Tuesday, December 13, 2011

Leo Nimekuwa Marley Katika Hadithi ya Charles Dickens

Leo katika idara yetu ya ki-Ingereza tulifanya onesho la tamthilia kutokana na hadithi ya A Christmas Carol iliyotungwa na mwandishi maarufu Charles Dickens.

Watu tuliosoma shule zamani tunakumbuka sana vitabu vya Charles Dickens, hasa Oliver Twist. Ni nani asiyekumbuka wahusika wa hadithi hii, kama vile Oliver Twist mwenyewe, The Artful Dodger, na Fagin m-Yahudi? Ilikuwa raha kusoma miaka ile, na tulikuwa tunapenda hata kukariri baadhi ya kauli za hao wahusika.

Basi katika kipindi hiki cha kuelekea Krismasi, idara yetu ina jadi ya kufanya jambo la kumbukumbu na burudani. Kwa miaka kadhaa, tumekuwa tukiigiza mchezo huu unaotokana na riwaya hii ya Dickens. Katika A Christmas Carol kuna wahusika wakuu kadhaa, na Scrooge ndio kinara. Huyu ni mfanyabiashara bahili, ambaye zamani alikuwa na mshiriki wake wa kibiashara aliyeitwa Jacob Marley.

Wakati hadithi inapotokea, tunaambiwa kuwa Jacob Marley alifariki miaka saba iliyopita. Tunachoona ni mzimu tu wa Marley, ambao unamtokea Scrooge kwa namna ya kumfanya afadhaike. Ila mzimu wa Marley unamwachia maaagizo muhimu. Basi, nilipewa jukumu la kuigiza kama mzimu wa Marley. Nilishafanya hivyo pia mwaka juzi.

Tuliamua kuwa niwe Marley kwa namna ya mwanamuziki wa reggae Bob Marley, ili kuleta usasa na kunogesha hadithi. Nilivaa kofia iliyoshonewa rasta, ambayo ilinunuliwa Jamaica na profesa mstaafu wa idara yetu, Jonathan Hill. Nilionekana kama m-Jamaica kabisa. Wakati wote wa onesho nilijitahidi kuongea kama m-Jamaica, na watazamaji wa onesho letu walibaki hawana mbavu. Picha tuliyopiga leo baada ya onesho nimeiweka hapa. Kuna picha ambayo tulipiga mwaka juzi ila sijapata nafasi ya kuitafuta. Ningeiweka hapa pia.

Hadithi hii ya Dickens, kama hadithi zake zingine, inavutia na ina maadili mema, kwani, hatimaye Scrooge anabadilika. Mwanzoni alikuwa bahili na katili asiye na huruma kwa yeyote, na wala hataki hata kusikia maneno kama "Heri ya Krismas." Kwake zote hizo zilikuwa ni kero na upuuzi. Hatimaye, kutokana na mambo ya ajabu yanayomtokea, anabadilika na kuwa mtu mwenye roho njema ya kuvutia.

Posho za Wabunge Hazitoshi

Yapata mwaka 1997 nilipokuwa katika utafiti Mwanza, mimi na washiriki wa utafiti tulikutana na mbunge katika hoteli ya Ramada. Sikumbuki alikuwa ni mbunge wa sehemu gani nchini. Katika maongezi yetu, alilalamika kwa masikitiko kuwa wa-Tanzania wanaamini kuwa mbunge ni mtu mwenye hela sana. Akatoa mfano wa maisha yake mwenyewe, kwamba nyumbani kwake, watu wamejaa kwenye makochi muda wote. Mchana wako hapo, na usiku wanalala hapo. Na yeye anawajibika kuwalisha na kuwanywesha siku zote.

Wakati huu ambapo wa-Tanzania wanalumbana kuhusu kuongeza posho za wabunge, mimi nakumbuka kilio cha yule mbunge. Nasita kuwalaumu wabunge wanapodai kuongezewa posho. Naamini kuwa posho zao hazitoshi.

Tatizo ni sisi wa-Tanzania, sio wabunge. Mtu akishapata ubunge, tunamtegemea atufanyie mambo mengi sana yanayohitaji hela. Mbunge akiingia baa, tunategemea ofa zake, tena za uhakika, sio soda za reja reja. Tunamtegemea achangie hela nyingi kwenye vikao vya "send-off," kipaimara, arusi, na kadhalika. Asipochangia hela nyingi, hatutamhurumia. Na kama ana ndoto ya kugombea tena, anafanya bahati nasibu.

Mbunge asipotembelea eneo lake la uwakilishi, akaweza kujionea kila sehemu na kukutana na watu wote, tutamwona hafai. Bila hela nyingi, mbunge hawezi kutekeleza hayo. Na ukizingatia kuwa kila apitapo, anatakiwa kuchangia misiba, sherehe, na harambee, ni wazi kuwa hata akipewa posho ya laki tatu kwa siku, haitatosha.

Kwa kifupi, kitu cha kwanza kinachotakiwa ni kwa sisi wananchi kubadilika. Tusiwe mzigo kwa mbunge. Tukitekeleza hilo, tutakuwa na haki ya kuhoji ongezeko la posho za wabunge. Lakini kama tabia zetu ndio hizo nilizoelezea, za kutegemea mbunge achangie hela nzito kila shughuli, na utitiri wa watu kuhamia nyumbani kwa mbunge, malalamiko yetu kuhusu ongezeko la posho za wabunge ni unafiki.

Zaidi ya hayo niliyosema, wa-Tanzania wengi ni mbumbumbu. Wakati wa kampeni, tulijionea jinsi wagombea wa chama fulani walivyokuwa wanawahonga wapiga kura kwa khanga, ubwabwa, na kadhalika. Hao wa-Tanzania mbumbumbu wanaafiki na wanategemea hayo. Sasa basi, wabunge wa aina hii wakisema wanahitaji posho ziongezwe, huenda wanafanya maandalizi ya uchaguzi ujao, kwani wapiga kura mbumbumbu watategemea tena hizo khanga, ubwabwa na bia.

Hoja yangu inarudi pale pale, kwamba tatizo linaanzia kwa wananchi.

Saturday, December 10, 2011

Miaka 50 Baada ya Uhuru, Mtoto Albino Anaogopa Kwenda Shule

Jana ilikuwa ni kumbukumbu ya miaka 50 ya uhuru wa Tanganyika. Nilijaribu sana kuandaa makala kuhusu siku hiyo ya jana, lakini nilipata kigugumizi. Kwa upande moja, ninafahamu kuwa ndoto ya uhuru aliyokuwa nayo Mwalimu Nyerere, ya kuleta ukombozi wa kweli katika nyanja mbali mbali na kujenga taifa linalojitegemea, imezimishwa na sera zilizopo, ambazo zinaimarisha ukoloni mamboleo. Kama ningeandika makala jana kuhusu kumbukumbu za uhuru wa Tanganyika, pangekuwa hapatoshi.

Lakini jambo jingine lililonipa kigugumizi ni kuwa mawazo yangu yalikuwa yanarudi tena na tena kwenye taarifa niliyosoma wiki kadhaa zilizopita, kuhusu mtoto albino wa Ludewa ambaye anaogopa kwenda shule asije akauawa na watu wenye imani za kishirikina. Habari hii niliiweka hapa.

Siku nzima ya jana nilikuwa najiuliza, inakuwaje miaka 50 baada ya uhuru, mtoto huyu anaishi katika hofu ya kuuawa? Tumepiga hatua mbele au nyuma? Enzi za Mwalimu Nyerere, mtoto huyu angekuwa anaenda shule sawa na watoto wengine. Ndoto ya Mwalimu, wakati Tanganyika inapata uhuru, ilikuwa kwamba tupambane na maadui wakuu watatu: ujinga, umaskini, na maradhi. Leo, kushamiri kwa ujinga katika jamii yetu kunatishia maisha ya mtoto huyu albino.

Nimekuja ofisini asubuhi hii nikaona kwenye blogu ya Mtwara Kumekucha taarifa kuhusu mauaji ya albino. Inakuwa kama vile mawazo yetu yamefanana wakati huu. Naileta hiyo taarifa hapa.


Wednesday, December 7, 2011

Hifadhi za Historia Bagamoyo

Bagamoyo ni mji maarufu katika historia ya nchi yetu na dunia. Kwa mtu anayetaka kujifunza historia hiyo, napendekeza ziara Bagamoyo kuangalia hifadhi zilizopo. Mwaka huu, nilitembelea Bagamoyo, na wanafunzi kutoka Marekani, kama nilivyoelezea hapa. Mahali pamoja tulipotembelea ni Caravan Serai, hifadhi mojawapo ya historia. Hapa kushoto ninaonekana mbele ya mlango wa kuingilia Caravan Serai. Kuna sanamu ya mtumwa aliyebeba pembe ya ndovu.


Hapa kushoto tunaonekana katika eneo la Caravan Serai, tukiwa na mfanyakazi wa hifadhi hiyo, ambaye alikuwa anatuonyesha na kutuelezea yaliyomo.















Hapa anaonekana mtaalam wetu akitoa maelezo ya historia ya Caravan Serai.












Humo ndani kuna nyaraka, picha na vitu mbali mbali, kama vile vyombo vya nyumbani, na maelezo kuhusu vitu hivyo. Hapa kushoto, katika picha ya katikati, anaonekana Tippu Tip.










Hapa kushoto ni picha ya watumwa.













Hapa kushoto ni picha ya "bangili," kwa mujibu wa bandiko la maelezo, ambazo walikuwa wakivalishwa watumwa shingoni na kuunganishwa na watumwa wengine kwa mnyororo.










Hapa kushoto ni baadhi ya vitu vya nyumbani.













Vitu ni vingi katika hifadhi hii, na maandishi. Mtu ukiingia hapo, ukaangalia na kusoma yaliyomo, na kusikiliza maelezo, utajikuta umeelimika kutosha.

Hii Caravan Serai ni hifadhi mojawapo tu; kuna nyingine, kama vile ya Kanisa Katoliki, ambayo nimeisikia kwa miaka mingi, na niliiona kwa nje mwaka juzi. Napangia kuingia ndani yake na kuangalia siku za usoni.

Sunday, December 4, 2011

Barua za Shaaban Robert

Kitabu cha Barua za Shaaban Robert ni mkusanyiko wa barua alizoandika Shaaban Robert kwa mdogo wake Yusuf Ulenge baina ya mwaka 1931 na 1958. Yusuf Ulenge alifanya busara ya kuzihifadhi na sasa zimechapishwa kama kitabu, na Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Mhariri Profesa Mugyabuso Mulokozi amefanya kazi kubwa na watafiti wenzake katika kuzichapisha na kuziwekea maelezo.

Nilikinunua kitabu cha Barua za Shaaban Robert mwaka 2008 katika duka la Taasisi. Nilifurahi na pia kushtuka kugundua kuwa Yusuf Ulenge alikuwa mdogo wa Shaaban Robert. Jina la Yusuf Ulenge nililifahamu tangu kwenye mwaka 1964, nilipokuwa darasa la sita. Nilinunua kitabu kiitwacho Nguzo ya Maji na Hadithi Nyingine, kilichotungwa na Yusuf Ulenge. Miaka yote sikuwa na wazo hata kidogo kuwa huyu alikuwa mdogo wa Shaaban Robert.

Sasa, hizi barua zimenifungua macho kabisa, kwani nimejionea jinsi uhusiano wa hao ndugu wawili ulivyokuwa mkubwa na jinsi Yusuf Ulenge naye alivyokuwa mwandishi mahiri. Katika kitabu hiki kuna taarifa za maandishi mengi ya Yusuf Ulenge, vikiwemo vitabu alivyochapisha na vingine alivyopangia kuchapisha. Mzee Yusuf Ulenge alifariki tarehe 16 Desemba, 2002.

Shaaban Robert ni mfano wa mlezi bora, kwa jinsi alivyokuwa anamshauri na kumwongoza mdogo wake Yusuf katika masuala mbali mbali ya maisha, kama vile elimu. Siwezi kuelezea kwa ufasaha jinsi Shaaban Robert alivyothamini elimu na maadili mema, akawa anamwongoza Yusuf katika njia hiyo. Shaaban Robert alikuwa tayari kutoa gharama zozote zilizohitajika kumlipia Yusuf katika masomo yake, kuanzia daftari hadi usafiri. Ni mfano mzuri sana kwetu wazazi na walezi wa watoto.

Kitabu hiki kinaelimisha sana. Kinautikisa kabisa moyo wangu kwa undani na uzito wa maudhui yake. Kitabu hiki kinafaa kuwemo katika kila nyumba ya wa-Tanzania, ili kisomwe na wazazi na watoto. Hakuna kisingizio cha kutokuwa na kitabu kama hiki, na vitabu vingine vya Shaaban Robert, ambaye ndiye gwiji wa uandishi wa ki-Swahili, mwanafalsafa na mwalimu wa jamii. Hayo nimeyaelezea katika kitabu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii, uk. 30-41

Ingekuwa ni hapa Marekani, tukio la kuchapishwa kitabu kama hiki lingekuwa na kishindo, na watu wangepanga foleni kwenye maduka ya vitabu kukinunua. Kingezungumziwa magazetini na vyombo vingine vya habari. Wa-Tanzania tunapaswa kujiuliza iweje hatuna utamaduni wa aina hiyo. Iweje hatuna hata habari wala hamu ya kujua mwandishi kama Shaaban Robert alizaliwa wapi na aliishi wapi na mchango wake katika jamii na ulimwengu ni upi. Tuko wa-Tanzania yapata milioni arobaini. Ni nyumba ipi katika Tanzania, kuanzia nyumba za walalahoi hadi za hao tunaowaita viongozi, yenye vitabu vya mwandishi muhimu kama huyu?

Kwenye mtandao wa Facebook kuna ukumbi wa wadau na wapenzi wa Shaaban Robert, uitwao Ukumbusho wa Shaaban Robert. Walioanzisha ukumbi huu si wa-Tanzania, bali wa-Kenya. Hii ndio hali halisi, kwamba nabii hakosi heshima, isipokuwa katika nchi yake. Kuthibitisha zaidi jambo hili, jionee jinsi mwanafunzi m-Marekani alivyokichangamkia kitabu hiki cha Barua za Shaaban Robert, akakiandikia uchambuzi huu hapa.

Friday, December 2, 2011

Wadau Wamekuja Ofisini Kwangu

Leo, bila kutegemea, nimetembelewa na akina mama wawili ofisini kwangu. Walijitambulisha, wakasema wamekuja ili nisaini nakala za vitabu vyangu. Anayeonekana kushoto ni Mama Kay wa Lanesboro, Minnesota, na huyu wa kulia ni Mama Sandy wa maeneo ya St. Louis, Missouri.

Nimesaini nakala tatu za Matengo Folktales na moja ya Africans and Americans: Embracing Cultural Differences ambazo wamezinunua leo hapa Chuoni St. Olaf. Tumeongelea vitabu hivi na masuala mengine ya aina hiyo.

Kumbe, Mama Kay, tulishaonana miaka kadhaa iliyopita hapa St. Olaf, alipokuja na mumewe, ambaye ni marehemu sasa, pamoja na Mchungaji Gabriel Nduye, Mchungaji Mengele (ambaye sasa ni askofu) na mkewe, wote kutoka Njombe. Mama Kay ameshafika Tanzania.

Nimewaambia kuwa nimeguswa na ujio wao. Ninaguswa na namna wadau wanavyoyafuatilia maandishi yangu, na falsafa yangu ni kumshukuru Mungu kwa yote. Kama inavyoonekana katika picha, tumefurahi kukutana.

Wednesday, November 30, 2011

Makafiri

Ingawa watu wengi wanaamini kuwa masuala ya dini ni hatari kujadiliwa, blogu yangu haina kipingamizi kwenye kujadili masuala hayo, kama ilivyo kwa masuala mengine. Kama kuna tatizo, tatizo haliko kwenye mada, bali tatizo ni wahusika, kama nilivyoandika hapa.

Leo napenda kuongelea suala ambalo limenikera kwa muda mrefu. Ni suala la watu kuwaita wengine makafiri. Nimeshasoma taarifa kutoka sehemu mbali mbali za Tanzania ambazo zimenifanya niandike ujumbe huu.

Leo katika mtandao wa Facebook, nimeona taarifa kutoka Mbeya ambamo mtu analalamika kuwa kuna makafiri sana kule. Miezi kadhaa iliyopita, nilisoma taarifa kutoka Zanzibar, kwamba watu wa kijiji fulani walikuwa hawataki makafiri kwenye eneo lao. Ukipita mtandaoni, utaona kuwa jadi hii ya kuwaita wengine makafiri inajitokeza mara kwa mara miongoni mwa watu wa Visiwani.

Sijui hao wanaowaita wengine makafiri walipata wapi uwezo wa kufahamu undani wa watu wengine kiasi hicho. Nilidhani kuwa sote tunaosema tunamwamini Mungu tunafahamu kuwa mwenye uwezo wa kumhukumu binadamu, uwezo wa kujua yupi ni kafiri na yupi si kafiri, ni Mungu tu.

Hatujui ya Mungu, na bora tuwe wanyenyekevu. Hao wanaowaita wenzao makafiri huenda Mungu anawajua kuwa ndio makafiri wenyewe. Binafsi siwezi kumtambua kafiri, kwa sababu sina njia ya kuona yaliyomo moyoni au akilini mwa yeyote. Sithubutu kumwita yeyote kafiri, kwani nitaona kuwa kufanya hivyo ni kufuru, yaani kujifanya mimi ni Mungu.

Sunday, November 27, 2011

Taarifa ya Ikulu Kuhusu Mkutano wa JK na CHADEMA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete na ujumbe wa Serikali yake leo, Jumapili, Novemba 27, 2011, amekutana na kufanya mazungumzo na ujumbe wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).

Katika mazungumzo hayo yaliyofanyika Ikulu, Dar Es Salaam, yamefanyika katika mazingira ya urafiki na ujumbe wa CHADEMA umewasilisha mapendekezo yake kuhusu mchakato wa kuandika Katiba Mpya ya Tanzania. Serikali imepokea mapendekezo hayo.

Hata hivyo, pande zote mbili zimekubaliana kukutana tena asubuhi ya kesho, Jumatatu, Novemba 28, 2011, ili kuipa nafasi Serikali iweze kutafakari mapendekezo hayo.

Lakini pande hizo mbili zimekubaliana kuwa Katiba ya sasa ni Katiba nzuri iliyolilea Taifa kwa miaka 50 iliyopita kwa sababu ni Katiba ya sasa iliyoliwezesha Taifa la Tanzania kuwa na amani, utulivu na kupata maendeleo makubwa ambayo nchi yetu imepata mpaka sasa.

Pia pande zote mbili zimekubaliana kuhusu umuhimu wa kutunga Katibu Mpya kama Mheshimiwa Rais Kikwete alivyoliahidi taifa wakati wa salamu zake za mwaka mpya Desemba 31, mwaka jana, 2010, Katiba ambayo italiongoza Taifa la Tanzania kwa miaka mingine 50 ijayo.

Katika mazungumzo hayo, Mheshimiwa Rais aliwahakikishia wajumbe hao wa CHADEMA wakiongozwa na Mwenyekiti wa chama hicho, Mheshimiwa Freeman Mbowe kuwa ni dhamira yake na ya Serikali yake kuhakikisha kuwa Tanzania inapata Katiba mpya.

Katika mkutano huo, pande zote mbili zimekubaliana kuwa ni jambo muhimu sana kwa mchakato mzima wa kutungwa kwa Katiba Mpya kuendeshwa kwa namna ya kulinda na kudumisha tunu za taifa za amani, utulivu na umoja wa kitaifa.

Aidha, pande zote mbili zimekubaliana kuwa mchakato huo uendeshwe kwa kuzingatia misingi ya mambo mengine muhimu kwa taifa la Tanzania kama vile kujiepusha na vitendo vya uvunjifu wa amani, kuligawa Taifa kwa misingi ya udini na ukabila ama kutugawa kwa misingi ya maeneo.

IMETOLEWA NA:
KURUGENZI YA MAWASILIANO YA RAIS IKULU

NOVEMBA 27, 2011

Friday, November 25, 2011

Mahojiano na Profesa Joseph Mbele

Nimefanya mahojiano mara nyingi na watu mbali mbali, wakiwemo wa-Tanzania, kuhusu shughuli zangu katika jamii, kama vile maandishi na mihadhara. Hapa naleta mahojiano yaliyofanyika Septemba 2006, ili wale ambao hawajawahi kusikia sauti yangu au namna yangu ya kujieleza katika mazungumzo ya papo kwa papo, wapate fursa hiyo.

(Chanzo: Butiama.podomatic)







Tuesday, November 22, 2011

Nimekutana na Wadau wa New Hampshire

Leo nimebahatika kukutana na wadau wawili, mtu na mkewe, kutoka New Hampshire, ambako ni waumini wa Kanisa la Holy Trinity. Wamekuja hapa Minnesota kwa masuala ya shirika la Bega kwa Bega, ambalo linashughulikia ushirikiano na maendeleo katika mkoa wa Iringa.

Wadau hao, Mama Dot na Mzee Kurt, wanajiandaa kwenda Iringa, ambako wameshaenda mara kadhaa. Katika ujumbe wao wa mwanzo kwangu, walisema kuwa Profesa Joe Lugalla, ambaye wako wote New Hampshire, aliwahamasisha tukutane. Profesa Lugalla, kama mimi, anawasaidia wa-Marekani wanaokwenda Tanzania kwa kuwapa ushauri unaohitajika. Kwa msingi huo, amekuwa mdau mkubwa wa kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences" na amekipigia debe kwa watu hao tangu kilipokuwa mswada tu, mkusanyiko wa dondoo mbali mbali, usio na sura ya kitabu.

Wadau hao wawili nami tumeongea kwa karibu saa mbili. Maongezi yetu yalihusu shughuli wanazofanya Iringa katika mpango wa Bega kwa Bega, na hasa maandalizi wanayofanya ya kupeleka kikundi cha wa-Marekani Iringa katikati ya mwaka ujao. Mama Dot amewahi kufundisha Chuo Kikuu Cha Tumaini, na tuliongelea pia habari za chuo kile, ambacho nami nimekifahamu tangu mwanzo na ninafahamiana na baadhi ya viongozi na walimu wake. Tuliongelea sana tofauti za tamaduni baina ya wa-Marekani na wa-Afrika, kama nilivyozieleza katika kitabu changu, ambacho wamekisoma vizuri. Walikuja na nakala yao, na wakaniomba niisaini. Nami nilifanya hivyo.

Tumefurahi kukutana, na tumekumbushana kuhusu watu kadhaa wa Tanzania na Marekani ambao sote tunawafahamu, kuanzia walioko Chuo Kikuu cha Tumaini hadi walioko New Hampshire. Ni kweli, milima haikutani bali wanadamu hukutana.

Monday, November 21, 2011

Wizard of the Crow: Riwaya ya Ngugi wa Thiong'o

Siku hizi, katika darasa langu mojawapo, tunasoma Wizard of the Crow, riwaya ya Ngugi wa Thiong'o. Kama kawaida yake miaka hii, Ngugi huandika riwaya zake kwanza katika lugha ya Kikuyu. Ndivyo alivyofanya kwa riwaya hii, kisha akaitafsiri kama Wizard of the Crow.

Hatujamaliza kuisoma, bali tunakaribia katikati. Ni moja kati ya riwaya ndefu kabisa zilizowahi kuandikwa na wa-Afrika. Kwa kigezo hiki, riwaya hii inanikumbusha ile riwaya maarufu ya Bwana Myombekere na Bibi Bugonoka Ntulanalwo na Bulihwali iliyoandikwa na Aniceti Kitereza.

Katika riwaya hii, Ngugi si yule Ngugi ambaye tumezoea kumsoma kwa miaka yapata thelathini sasa, ambaye vitabu vyake katika kipindi hiki, tofauti kiasi fulani na miaka ya mwanzo, vimebeba hisia za kupambana na uonevu, unyonyaji, na ukoloni mamboleo bila mzaha. Kwa miaka mingi, Ngugi ameonekana kama mwandishi mwenye hasira, na wasomaji na wahakiki wengi wamekuwa wakilalamika kuwa hasira hizi zimedhoofisha sanaa katika uandishi wake.

Lakini Wizard of the Crow inavutia kwa kigezo cha sanaa. Ngugi amejidhihirisha kuwa msimuliaji wa hadithi mwenye uwezo wa kutumia kejeli na mizaha. Kwa upande wa dhamira, anaelezea hali halisi ya utawala na siasa inayoonekana sehemu nyingi za Afrika ya leo, ambamo wale tunaowaita viongozi ni mafisadi waliobobea katika majungu na ushirikina na uvunjaji wa haki za binadamu. Ingawa hali anayoelezea si ya kufurahisha, Ngugi anafanikiwa kuwaanika hao watu kwa mbinu mbali mbali za kisanii, kama nilivyogusia. Mtu unaposoma Wizard of the Crow, huwezi kujizuia kuwakumbuka madikteta kama vile Mobutu, Bokasa na Banda.

Ngugi wa Thiong'o amejipambanua kama mwandishi bora tangu zamani. Baadhi yetu tunaamini kuwa riwaya yake ya A Grain of Wheat ndio ilitia fora katika kazi zake zote, na wengine wanaihusisha pia Petals of Blood. Lakini naamini wasomaji na wahakiki sasa watakubali kuwa Wizard of the Crow ni bora kuliko zote ambazo Ngugi amewahi kuandika.

Saturday, November 19, 2011

Wabunge wa CCM Wanakera

Leo unatimia mwaka mmoja tangu nichapishe makala hii hapa chini. Kitu kimoja kilichonifanya niitafute na kuileta tena ni mjadala wa siku chache zilizopita katika Bunge la Tanzania kuhusu suala la Katiba. Niliwaona wabunge wakimjadili mtoa hoja, Mheshimiwa Tundu Lisu, au wakiongelea masuala ya kifamilia ya viongozi wa CHADEMA, badala ya kujadili hoja. Inakera. Na mimi ninayesema hivi ni raia ambaye si mwanachama wa chama chochote cha siasa.
-------------------------------------------------------

Chanzo: Hapakwetu

Wabunge wa CCM wanakera.

Tukianzia na wabunge hao walioapishwa safari hii, sitasahau kuwa hao ndio waheshimiwa waliotoroka midahalo wakati wa kampeni. Wote walitoroka midahalo, kitendo ambacho kimenikera. Mimi kama mwalimu, ninayetambua umuhimu wa midahalo, ninawashutumu hao waheshimiwa. Soma hapa.

Kila nitakapokuwa naona sura za hao waheshimiwa wa CCM, nitakuwa nakumbuka kitendo chao hiki cha kutoroka midahalo. Nitakuwa naangalia kama watajirekebisha au kama kitendo kile ni ishara ya tabia na mwenendo watakaofuata kwa miaka mitano ijayo.

Tukirudi nyuma, kwenye awamu iliyopita, wabunge wa CCM walikera. Ni nani atakayesahau yaliyotokea wakati Dr. Slaa alipoanza kutamka kuwa kuna ufisadi katika nchi yetu? Wabunge wote wa CCM walimpinga vikali na kumtupia shutuma nzito kwamba alikuwa mzushi.

Dr. Slaa hakuyumba, bali aliendelea kutoa madai yake. Hatimaye, ilianza kuthibitika kuwa aliyokuwa anayasema ni kweli, kwamba tuna mafisadi. Baada ya wananchi kuanza kuona ukweli huo, ukawa haupingiki tena, tuliwaona baadhi ya wabunge wa CCM wakijitokeza na kuanza kujinadi kuwa nao ni wapiganaji dhidi ya ufisadi. Sijui kama walikuwa wanaongea kwa dhati au kwa lengo jingine.

Tukirudi nyuma zaidi, tunakumbuka suala la machafuko yaliyotokea Visiwani mwaka 2001. Machafuko yale, yaliyotokana na CCM, chama tawala, kushindwa kutumia haki na busara, yaliiletea Tanzania aibu kubwa duniani. Kwa uthibitisho, soma hapa.

Lakini, pamoja na maovu yote yaliyofanyika Visiwani, pamoja na fedheha yote iliyoiangukia Tanzania, wabunge wa CCM hawakukubali kuwa serikali ya CCM ilikuwa na makosa, wala hawakukubali kuwa Tanzania ilikuwa inafedheheka. Wao waliitetea serikali ya CCM. Maadam palikuwa na suala lililohusu chama cha upinzani, yaani CUF, wabunge wa CCM waliamua kuikingia kifua serikali ya CCM, badala ya kusimamia haki za binadamu na heshima ya Tanzania.

Je, kuna kero kubwa zaidi ya hii ya kutojali maslahi ya Taifa na badala yake kuangalia maslahi ya kikundi fulani?

Mjengwablog Iliibua Kashfa ya Pan African Energy Mapema

Chanzo: Mjengwablog

Ndugu zangu,
Nafurahi kuwajulisha, kuwa Mjengwablog. com ndio iliyoibua kwa mara ya kwanza kashfa ya mradi wa gesi unaouhusisha kampuni ya Kisweden ya Pan African Energy , Tanesco na Wizara ya Nishati na Madini.

Habari kuhusu kashfa hiyo ziliripotiwa kwa mara ya kwanza hapa nchini na blogu hii Ijumaa ya Julai 15, 2011. Ni siku tatu kabla ya Waziri Ngeleja kuwasilisha bajeti ya Wizara ya Nishati Na Madini. Bila shaka yeyote, habari hiyo ilichangia kwenye kuongeza nguvu ya mjadala bungeni. Hapa chini ni habari husika niliyoiposti hapa globuni na kwenye mitandao mingine kama vile Global Publishers, Jamii Forums na Wanabidii. Pichani juu Waziri Ngeleja akipongezwa na wabunge wenzake wa CCM baada ya bajeti ya wizara yake kupitishwa. Ilikwamishwa ilipowasilishwa kwa mara ya kwanza.


Mheshimiwa Ngeleja, Sweden Kuna Kashfa Ya Nishati Yetu
Ndugu zangu,

Waziri wa Nishati na Madini Mheshimiwa William Ngeleja leo anawasilisha bajeti ya wizara yake huku kashfa ya nishati yetu ikiwa ni moja ya ajenda ya shirika la Misaada la Kimataifa la Action Aid lenye tawi lake nchini Sweden.

Shirika hili linaishinikiza Serikali ya Sweden kuacha kufadhili kwa kuyapa mitaji ya kuwekeza makampuni yenye kukwepa kodi kama ilivyo kwa kampuni ya Pan African Energy.

Kampuni hii Pan African Energy iliyosajiliwa kwenye visiwa viwili; Mauritius na Jersey inavuna gesi ya Songosongo huku ikiwa imeingia mkataba wa miaka 25 na TANESCO kupitia Shirika la Nishati ina Madini la Taifa TPDC. Ni mkataba wenye kuifanya kampuni hiyo kutokulipa kodi ya faida ya mapato wanayopata kutokana na mauzo ya umeme unaotokana na gesi asilia wanayovuna Songo Songo.

Kwa mujibu wa ripoti ya Shirika la Action Aid iliyotolewa mwezi Mei mwaka huu, tangu Pan African Energy waanze kuvuna gesi asilia kule Songo Songo mwaka 2004, kampuni hiyo imevuna faida ya zaidi ya dola za Kimarekani milioni 60. Nusu ya faida hiyo ilipatikana mwaka 2009 na kampuni hiyo ilitarajiwa kuongeza uzalishaji. Hivyo, kuvuna zaidi gesi yetu asilia ya Songosongo.

Mpaka kufikia sasa, Pan African Energy imefanikiwa kukwepa kodi inayokadiriwa kufikia dola za Kimarekani milioni 40. Hiki ni kiasi cha fedha kinachotosha kusomesha watoto wa Kitanzania 175,000 ( Laki moja na sabin ina tano elfu) kwa mwaka kwa mujibu wa ripoti ya Shirika la Action Aid.

Kwa kifupi tu, ripoti hii inadhihirisha namna ufisadi unavyochangia kutuacha Watanzania tukiwa katika hali ya giza linalotokana na mgawo wa umeme. Tukiwa katika hali ya uzalishaji duni kutokana na uhaba wa nishati ya umeme. Ufisadi umetuletea giza na umasikini.

Kampuni hii ya Pan African Energy inanufaika na ’mkataba wa kifisadi’ usiotanguliza maslahi ya taifa.
Ni wakati sasa wa Waheshimimiwa wabunge wetu ’ kumweka kikaangoni’ Waziri wa Nishati na Madini Mh. William Ngeleja ili atoe maelezo ya kina juu ya kashfa hii ya Pan African Energy. Na atwambie, ni hatua gani zitachukuliwa na lini kwa wote waliochangia kutufikisha kwenye kashfa hii. Hivyo basi, waliochangia kutufikisha katika giza hili tunalolishuhudia sasa kwa kukosa nishati hii muhimu kwa maana ya umeme.

Kama Mheshimiwa Waziri atashindwa kutoa majibu ya kuridhisha, basi, aombwe akae pembeni kupisha Watanzania wengine wenye uwezo wa kushika Wizara hiyo nyeti kwa taifa.

Nawasilisha.

Maggid
Knivsta, Sweden
Ijumaa, Julai 15, 2011
http://mjengwa.blogspot.com
( Unaweza kusoma ripoti ya Action Aid kwenye; http://www.actionaid.se)

Thursday, November 17, 2011

Nimekutana na Mdau Mjini Apple Valley

Leo nimekutana na mdau Dr. Mary Sheedy Kurcinka, mhadhiri na mwandishi maarufu wa masuala ya malezi ya watoto wachanga. Nilishamtaja siku chache zilizopita hapa. Tuliongea kwa saa moja na nusu mjini Apple Valley.

Mama huyu alishatembelea Nigeria na Ghana wakati wa ujana wake, akaandika kuhusu malezi ya watoto wachanga katika jamii ya wa-Yoruba. Sasa anapangia kwenda Tanzania, mwanzoni mwa mwaka ujao.

Mazungumzo yetu ya leo yalihusu suala hilo analofanyia utafiti. Aliponiandikia ujumbe wa kwanza, wiki kadhaa zilizopita, alisema alisikia habari zangu kutoka kwa muumini wa Shepherd of the Valley Lutheran Church.

Leo kaja na nakala ya kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ambacho alikinunua hivi karibuni. Amesema amekisoma na amekipenda sana. Kimemkumbusha aliyoyaona alipoishi Nigeria na Ghana. Kama ilivyo kawaida kwa wa-Marekani, aliniomba nisaini nakala yake, nami nikafanya hivyo.

Katika kuongea naye, nimepata motisha ya kufuatilia suala la malezi ya watoto wachanga, kwa kuzingatia saikolojia ya hao watoto wachanga, na changamoto zinazowakabili wazazi wao katika tamaduni mbali mbali. Leo tumejaribu kuongelea suala hilo tukizingatia tamaduni za wa-Marekani na wa-Afrika. Leo ulikuwa mwanzo, na tunategemea kuendelea kubadilishana mawazo.

Kwa vile sote wawili ni waandishi, tumepata fursa ya kuongelea masuala ya uandishi pia, kubadilishana uzoefu. Katika maongezi hayo, nilipata fursa ya kumweleza changamoto zilizonifanya nikaandika kitabu changu hiki, na pia nilivyojifunza kutokana na jinsi mwandishi Ernest Hemingway anavyofafanua dhana ya ukweli katika uandishi.

Wednesday, November 16, 2011

Mhadhara wa Jana Ulivyofanikiwa

Mhadhara wangu wa jana kwenye shule ya Mazingira, Apple Valley, ulifanikiwa sana. Ni umbali wa dakika 45 kutoka hapa ninapoishi. Niliongea kuanzia saa tatu hadi saa sita.










Leo Mwalimu Carlson ameniandikia ujumbe huu:

I have described the day to many of our faculty.... That was one of the best classroom sessions I have ever been a part of...the kids were buzzing for the rest of the day. Thank you so much
.

Nitafsiri kwa ki-Swahili:

Nimewaeleza walimu wetu wengi shughuli za leo.... Ni kati ya madarasa bora kabisa ambayo nimewahi kushiriki....vijana wamesisimka wakiongelea siku nzima. Asante sana.


Nahitimisha kwa kusema kuwa nilishagundua tangu zamani kuwa kuwaneemesha wengine kwa kuwafundisha ninayoyafahamu ni kitu kinachonipa raha mimi mwenyewe. Nafurahi kuwatajirisha vijana kitaaluma na kimtazamo. Mara kwa mara nafanya shughuli hizi kwa kujitolea, lakini sipungukiwi. Ninaamini ule usemi kuwa kadiri unavyotoa ndivyo unavyopewa.

Eti Tuupigie Mlima Kilimanjaro Kura, Kwa Lipi?

(Makala hii imechapishwa katika blogu ya kamalaluta)

eti tuupigie mlima kilimanjaro kura, kwa lipi?

sikuupigia kura mlima kilimanjaro na wala sikuwa na mpango wa kuupigia kura na nisingeweza kuupigia kura. ni kweli ungekuwa maajabu ya dunia tungepata pesa nyingi. lakini kwa nini kushiriki kuupigia kura mlima kilimanjaro??

Tanzania hupata pesa nyingi kutokana na utalii, ufadhili na vyanzo vingine.lakini pesa hizo huishia wapi?? tunazidi kukamuliwa kodi na kumasikinishwa. wakulima kama mimi tumekosa mitaji, huku rais wetu akionekana kila siku anawakaribisa matajiri kutoka nje ili wajekuchukua vijishamba vyetu kuwekeza eti.

mapato yoote hayo pamoja na utalii huishia wapi? hamna huduma za msingi za jamii, shule alizozijenga nyerere ndo bado zipo zinakaribia kuwaangukia wanafunzi.

pesa za kufisidi huwa hazikosi na mafisadi wako huru kuiba watakacho, anasa za watawala nazo hazikosagi pesa. wananunua magariya kitajiri, pinda eti anakataa gari la kitajiri kwa kuwa anaendesha gari la kitajiri then gari alilolikataa linapelekwa kwenye idara nyingine, kwa nini kuupigia kura mlima huu?

Tuesday, November 15, 2011

Mhadhara Katika Chuo cha Mazingira, Minnesota

Leo nilikwenda Apple Valley, kuongea na wanafunzi wa Chuo cha Msomo ya Mazingira. Nilialikwa na mwalimu Todd Carlson, na wanafunzi wake hao wamekuwa wakishughulika na mada ya falsafa za jadi.

Kwa miaka mingi, mwalimu Carlson amekuwa akinialika kuongea na wanafunzi hao.





Katika kuwaandaa, Mwalimu Carlson anawapa sehemu kadhaa za kitabu cha Matengo Folktales wasome. Kutokana na maandalizi hayo, wanafunzi hao wanakuwa na duku duku na masuali mengi ya kuniuliza. Ni wanafunzi makini sana. Wanaulizia kuhusu utafiti wa fasihi simulizi na changamoto za uandishi masimulizi hayo, tafsiri, maana, falsafa na kadhalika, wakizingatia yale niliyoandika katika Matengo Folktales.

Kila ninapotembelea Chuo hiki, nawasimulia hadithi angalau moja kutoka katika Matengo Folktales. Leo niliwasimulia hadithi ya "Jitu Katika Shamba la Mpunga," ambayo ni chemsha bongo ya aina yake, tukatumia muda kuiongelea.

Saturday, November 12, 2011

Vitabu Nilivyonunua Leo Apple Valley

Jioni ya leo nilipita kwenye duka la Half Price Books, mjini Apple Valley. Nilikuwa natoka Minneapolis.

Nilipoingia ndani, niliwakuta watu wengi humo, wanazunguka huko na huko wakiangalia vitabu. Kwenye sehemu ya kulipia, kulikuwa na foleni. Hii ni jioni ya Jumamosi, wikiendi, na wa-Marekani wamejazana katika duka la vitabu. Je, jambo hili linawezekana nchini mwetu?

Baada ya kuangalia vitabu vingi, nilichagua viwili. Kimoja ni The Hottentot Venus kilichotungwa na Rachel Holmes, na kingine ni The Time and the Place and Other Stories kilichotungwa na Naguib Mahfouz.

Hottentot Venus, ni habari ambayo nimeifahamu kwa miaka mingi. Ni jina alilopewa Saartje Baartman, mama mw-Afrika kutoka Afrika Kusini ambaye alipelekwa Ulaya kama kivutio, hasa kwa vile alikuwa na makalio makubwa sana, kutokana na desturi za kwao za kukuza makalio. Huko Ulaya alinyanyasika sana, kwani walimweka kwenye uzio kama mnyama, akitembezwa kwenye miji mbali mbali kwa maonyesho, na kukutana na adha za kila aina. Alifariki mwaka 1815.

Ni habari ya kusikitisha sana. Maiti yake iliwekwa katika jumba la makumbusho kwa miaka mingi, na hata ubongo na sehemu zake za siri zikiwa zimenyofolewa na kuwekwa kama kivutio cha aina yake. Hatimaye, serikali ya Mzee Mandela iliweka shinikizo kuwa masalia ya Saartje Baartman yarudishwe Afrika Kusini kwa mazishi sahihi. Mazishi hayo yalifanyika mwaka 2002.

Huo ni ufupi wa habari nilizozifahamu kwa miaka kadhaa. Lakini sasa nimenunua hiki kitabu, nitazifuatilia kwa undani zaidi.

Naguib Mahfouz ni kati ya waandishi maarufu waliopata kuishi. Alikuwa mtu wa Misri. Aliandika riwaya nyingi na hadithi fupi. Mwaka 1988 alipata tuzo ya Nobel kwa uandishi wake. Nimesoma na kufundisha baadhi ya vitabu vyake, kama vile Midaq Alley. Hiki kitabu nilichonunua leo ni kati ya vile ambavyo sikuwa navyo.

Mbeya Nchi, Raisi Sugu

Kabla ya yote, sherti niseme kuwa nasikitishwa na mambo yaliyotokea Mbeya siku mbili tatu hizi zilizopita na kusababisha uvunjifu wa amani. Natoa pole kwa waathirika. Kwa kuangalia habari zilizopatikana, tatizo limesababishwa na ukosefu wa busara za kiuongozi.

Kati ya taswira zilizotolewa kutokana na matukio haya ya Mbeya ni hili bango lisemalo Mbeya Nchi Raisi Sugu. Picha nimeipata kutoka blogu ya Francis Godwin. Bango hili naona lina ujumbe wa kufikirisha. Kwa upande mmoja, mtu anaweza kusema kuiita Mbeya nchi ni makosa na dharau kwa nchi ya Tanzania.

Lakini kwa upande mwingine, inakuwa vigumu kuthibitisha kosa liko wapi. Neno nchi limekuwa likitumika kwa namna nyingi katika maisha yetu. Miaka ya zamani na hadi leo, tunaposema u-Gogoni, au u-Sukumani, tunamaanisha nchi ya wa-Gogo na nchi ya wa-Sukuma. Hakuna ubaya wowote hapa. Katika hali hii, inakuwa vigumu kuwakosoa wenye hili bango lisemalo Mbeya Nchi.

Kuna wakati tulikuwa na nchi ya Tanganyika. Nchi hiyo ilipata Uhuru mwaka 1961 na mwaka 1964 ikatoweka. Pamoja na kuwa nchi ya Tanganyika haipo, mwaka huu kuna shughuli za kukumbuka uhuru wa nchi hiyo ambayo imetoweka.

Leo kuna nchi iitwayo Tanzania. Kesho na keshokutwa, watu wanaweza kuamua kuififisha nchi hiyo pia, kama walivyoififisha Tanganyika. Kwa mfano, wanaweza kuiunganisha hii Tanzania na nchi jirani, wakatunga nchi tofauti kabisa, na Tanzania ikafa kama ilivyokufa Tanganyika. Labda wenzetu wa Mbeya wanakazana kuhakikisha kuwa nchi yao haipotei kienyeji namna hiyo.

Kuhusu Mheshimiwa Mbunge wa Mbeya, maarufu kama Sugu, jambo moja lililojitokeza ni jinsi anavyokubalika na wananchi, hususan walalahoi. Nimeguswa na jinsi alivyokuja Mbeya wakati wa vurugu, na wakati viongozi wa serikali na polisi wakiwa wameshindwa kuzidhibiti, akaweza kuwahutubia wananchi na kuwatuliza. Napata picha kuwa ana akili na busara ya kiuongozi. Niliwahi kushiriki mjadala kuhusu Sugu hapa. Picha nimeitoa kwenye blogu ya mbeyayetu.

Taarifa tulizozipata ni kuwa wananchi wa Mbeya walikuwa hawataki kumsikiliza kiongozi yeyote isipokuwa Sugu. Hapo ikabidi Sugu aondoke kwenye vikao vya Bunge Dodoma na kuwahi Mbeya. Umati aliohutubia unaonekana kwenye hizi picha, ambazo nimeziona kwenye blogu ya mbeyayetu.

Friday, November 11, 2011

Nitakutana na Mteja Maarufu

Mara kwa mara napata fursa ya kukutana na wateja. Hao ni watu waliosoma vitabu vyangu au wanapangia kufanya hivyo au wamehudhuria mihadhara yangu. Wengine, ambao hatupati fursa ya kukutana uso kwa uso, wanawasiliana nami kwa barua pepe. Kwangu ni jambo la kushukuru, kwamba Mungu kanijalia uwezo na fursa hizo.

Siku chache zilizopita, nilipata ujumbe kutoka kwa mama mmoja akisema kuwa alipata taarifa zangu kutoka kwa mama mwingine wa Shepherd of the Valley Lutheran Church. Nilivyoangalia mtandaoni, nimegundua kuwa huyu aliyeniandikia ni mtu maarufu.

Wakati anaulizia kama tungeweza kukutana, alisema kuwa amenunua kitabu changu cha Africans and Americans na atakisoma hima. Anapangia kuandika kitabu kingine, na anapenda kusikia mawaidha yangu kuhusu masuala ya utamaduni katika malezi ya watoto.

Huyu namhesabu kama mteja maarufu, kwa vile anafahamika sana kutokana na shughuli zake za kuandika na kuelimisha umma. Nangojea siku tuliyopanga kukutana, wiki ijayo, nikizingatia kuwa mteja ni mfalme.

Nimalizie tu kwa kusema kuwa niliwahi kwenda Shepherd of the Valley kuongelea suala la tofauti za tamadununi. Kanisa hili lina ushirikiano na waumini wa Tungamalenga, Iringa. Nilifanya hiyo shughuli, na sikutegemea kuwa ingezua hayo niliyoeleza hapa juu. Ndivyo mambo yanavyokwenda hapa duniani. Unaweza kufanya jambo, usijue litazua nini, litaishia wapi au vipi.

Thursday, November 10, 2011

Maktaba Kuu ya Taifa, Dar es Salaam

Sijui ni wangapi kati ya mamilioni ya watu wanaoishi Dar es Salaam ambao wameingia katika Maktaba Kuu ya Taifa, au wana mazoea ya kuingia humo. Hapa siongelei wanafunzi, kwani hao wanaingia humo. Naongelea watu wasio wanafunzi.

Yawezekana wako ambao wana vijiwe vyao hapa nje ya maktaba, ambavyo wanahudhuria kila siku au kila wiki, lakini hawajawahi kukanyaga ndani ya maktaba hii.

Lakini, Mwalimu Nyerere alipofungua maktaba hii, tarehe 9 Desemba, 1967, alitoa ushauri wa maana, na baadhi ya maneno yake ni haya:

I am also forced to say that we shall probably not be able to go ahead as quickly as we would like, because even when a library service is run with the utmost economy, it still costs quite a lot of money. For a public library should not just be a place where books can be borrowed. It must also be a center for much wider adult education work of all kinds – ranging from the promotion of the desire for literacy by story telling and discussion, to the erudite lectures of visiting professors in our country. The libraries also have an important role to play in overcoming one of their own limitations; for a good librarian backed by a good library, can encourage people to write books as well as read them. Our traditional stories and histories can be written in Swahili so that the whole nation can read them; personal experiences, which are of wider interest, can be written as a story or a book; knowledge gained through practical development work can be written down so that it is shared. (…) (W)e can make our libraries into real cultural and community centers. It is up to us to provide them, to help them develop, and to use them to the full.

(Source: The Mwalimu Nyerere Foundation)

Hebu nijaribu kuyatafsiri kwa ki-Swahili:

Vile vile nalazimika kusema kuwa huenda hatutafanikiwa kusonga mbele kwa kasi ambayo tungependa, kwa sababu hata pale maktaba inapoendeshwa kwa umakini kabisa kimatumizi, bado inagharimu hela nyingi sana. Kwani maktaba ya umma isiwe tu mahali pa kuazimia vitabu. Sherti pawe pia mahali pa kutekelezea suala zima la elimu ya watu wazima kwa mapana yake--kuanzia kuhimiza kusoma na kuandika kupitia usimuliaji wa hadithi na uchambuzi wake, hadi mihadhara ya kisomi ya wahadhiri na maprofesa nchini mwetu. Maktaba pia zina wajibu muhimu wa kuchangia katika kurekebisha mapungufu yanayozikabili; kwani mkutubi bora awapo na maktaba bora, anaweza kuwahimiza watu kuandika vitabu sambamba na kuvisoma. Hadithi zetu za jadi na historia zinaweza kuandikwa kwa ki-Swahili ili Taifa zima liweze kuzisoma; taarifa za uzoefu wa watu binafsi, ambazo ni muhimu kwa jamii, zinaweza kuandikwa kama simulizi au kitabu; ujuzi upatikanao katika shughuli za maendeleo unaweza kuandikwa ili na wengine waupate. (...) (Tu)naweza kuzifanya maktaba zetu sehemu halisi za kuendeshea shughuli za kitamaduni na kijamii. Ni juu yetu kuzifanya ziwepo, kuchangia ustawi wake, na kuzitumia kikamilifu kabisa.

Wednesday, November 9, 2011

Hotuba ya Mwenyekiti wa CHADEMA, Novemba 9

Leo asubuhi, katika kufuatilia habari za mambo yanayotokea Arusha wiki hii, nimesoma kwamba wakati polisi wamewakamata CHADEMA eti kwa kufanya mkutano bila kibali, polisi hao hao hawajawakamata CCM ambao walifanya mkutano bila kibali cha polisi. Mimi kama raia ambaye si mwanachama wa chama chochote cha siasa nimeona kwa miaka na miaka jinsi vyombo vya dola Tanzania vinavyofanya umachinga kwa CCM, chama ambacho hatimaye, Mwalimu Nyerere alikiogopa, kama nilivyoelezea hapa.

Saturday, November 5, 2011

Maktaba ya Mkoa, Tanga

Maktaba ya mkoa, mjini Tanga, ilifunguliwa mwaka 1958. Wa-Ingereza, ambao walikuwa wanatawala Tanganyika, ndio waliojenga maktaba hii. Ni jengo zuri sana, kama inavyoonekana hapa kushoto.








Nimetembelea maktaba hii mara kadhaa. Ni mazoea yangu kutembelea maktaba, kama nilivyoeleza hapa na hapa. Tangu nilipofika hapo maktaba ya Tanga mara ya kwanza, miaka kadhaa iliyopita, nilipata fursa ya kufahamiana na mkurugenzi, ambaye anaonekana nami katika picha hapa kushoto. Nimepata fursa ya kuingia ndani na kuangalia vitabu na machapisho mengine, nikachangia nakala za vitabu vyangu.



Maktaba hii ilikuwa nzuri sana tangu ilipofunguliwa. Lakini leo, hali si nzuri, kama ilivyoelezwa hapa. Maktaba inahitaji ukarabati, vitabu vipya, majarida na kadhalika. Kwa nchi tajiri kama Tanzania, ambayo ina rasilimali kuliko nchi nyingi, haieleweki kwa nini isiwezekane kukarabati maktaba kama hii. Jawabu linaeleweka: ni ujinga, ufisadi na ukosefu wa uongozi kitaifa.





Uongozi wa maktaba unajitahidi sana kufanya kazi vizuri, ingawa mazingira ni magumu. Wanajitahidi kukidha mahitaji kufuatana na mabadiliko ya wakati. Kwa mfano, mara ya mwisho nilipoingia katika maktaba hii, nilionyeshwa sehemu ambayo imewekwa maalum kwa mahitaji ya wanafunzi wa chuo kikuu huria. Wanastahili pongezi.

Friday, November 4, 2011

Nakunywa Chai na Kahawa ya Tanzania

Ujumbe wangu wa leo ni kuwa wa-Tanzania tunapaswa kutumia bidhaa zinazotengezwa nchini mwetu kila inapowezekana. Iwe tuko Tanzania au nje, tufanye hivyo, kwani manufaa yake ni makubwa.

Nimepata wazo la kuandika ujumbe huu kutokana na ukweli kwamba hapa ughaibuni ninakunywa chai na kahawa ya Tanzania. Sibadili.

Kila ninapokuwa Tanzania, wakati wa kuondoka nahakikisha kuwa nimenunua chai na kahawa ya kunitosha hadi nitakapokuja tena. Mwaka huu, kwa mfano, wakati naenda kupanda ndege uwanja wa Julius Nyerere Dar es Salaam, nilimwambia dreva wa teksi anipeleke kwanza sehemu wanapouza chai na kahawa ya Tanzania. Ndivyo alivyofanya




Faida za kutumia bidhaa za nchini mwetu ni nyingi. Kwanza, tunachangia ajira katika nchi yetu. Kama wa-Tanzania wote, walioko nchini na nje, tungekuwa tunanunua vitu vinavyotengenezwa nchini, kama vile nguo, sabuni, sukari, soda, na viberiti, ajira zingeongezeka mara dufu. Waziri wa mambo ya nchi za nje hivi karibuni aliripotiwa akisema kuwa kuna waTanzania zaidi ya milioni mbili katika nchi za nje. Ni wazi kuwa hili ni soko kubwa sana kwa bidhaa za Tanzania, lakini tumekosa upeo wa kujitambua.


Wa-Tanzania wengi, ndani na nje ya nchi, tuna tatizo la kasumba na elimu duni. Tunashabikia vitu vya nje, hata bila sababu ya maana. Ukiwa Dar es Salaam, nenda mahali kama Mlimani City, kwa mfano. Hapo utawaona wa-Tanzania wakihangaika kununua juisi ya vikopo kutoka nje ya nchi, wakati maeneo ya jirani, kama vile Mwenge, yanauzwa mananasi, machungwa, mapapai na maembe.




Wa-Tanzania wanashabikia vitu vinavyoitwa vya mamtoni, bila kutambua kuwa kwa kufanya hivyo, wanawapa ajira watu wa nchi za nje. Tukiorodhesha vitu hivi vinavyotoka nje, wakati sio lazima tuviagize, tutaona jinsi tunavyochangia ukosefu wa ajira katika nchi yetu. Sina nafasi ya kuelezea kirefu suala hili hapa. Nimelielezea katika kitabu cha CHANGAMOTO.




Nina hakika kuwa kwa kununua vikopo na vikasha vya chai na kahawa vinavyoonekana kwenye hizi picha, nimechangia uchumi wa Tanzania, na ajira kwa wa-Tanzania kadhaa.

Thursday, November 3, 2011

Mwanafunzi Albino Aacha Shule Akihofia Kuuawa

Kila kukicha, zinajitokeza habari za kutia aibu, kusikitisha, na kutisha zinazothibitisha kuwa Tanzania ni kichwa cha mwendawazimu. Hapa ni habari mojawapo kutoka blogu ya Francis Godwin kuhusu mtoto albino. Taarifa hizi za uhayawani zinapojitokeza huwa najiuliza kama Tanzania ni nchi kweli, au imeshakuwa jehenam.

&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&


Mtoto Albino aliyeacha masomo akifanya mahojiano na waandishi wa habari

MWANAFUNZI wa darasa la pili shule ya msingi Bulongwa wilaya ya makete mkoani Iringa Emeliana Chaula (9)mwenye ulemavu wa ngozi (albino) ambeye pia ni yatima anayelelewa katika kituo cha watoto yatima cha ELCT Bulonga Wilayani Makete ameacha masomo yake kwa kuogopa kuuwawa.

Mwandishi wa mtandao huu kutoka Makete Cony Mpila anaripoti kuwa mkuu wa kituo hicho Dr. Mcheshi alisema mtoto huyo amesimama kwenda shuleni kutokana na vitendo vya kutishiwa usalama wake na baadhi ya watu kutokana na umbali wa kutoka kituo hicho na shuleni anakosoma Emeliana.
Dr. Mcheshi alisema kituo chao kimeshindwa kumlinda mtoto huyo kutokana na changamoto ya ukosefu wa mafuta ya kumpeleka shuleni mtoto huyo. Ili kumnusuru mtoto huyo kimaisha na kumuwezesha aendelee na masomo kituo kimeiandika barua katika ofisi ya Mkuu wa Wilaya Makete ingawa hakuna jitihada zozote zinazoendelea katika kumnusuru mtoto huyo kimaisha na kimasomo.
Dr huyo alieleza pia kituo chake kinakabiliwa na changamoto ya kuwalea watoto yatima wenye umri mdogo na kukosa msaada kutoka katika jamii na serikali pia.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...