Wednesday, September 7, 2011

wa-Marekani Wajifunza u-Islam Kalenga

Mwaka huu, wanafunzi niliowaleta Tanzania kutoka Marekani wamepata fursa ya kujifunza kuhusu u-Islam kutoka kwa wahusika wa dini hiyo. Nilitaka wapate fursa hiyo, ili wapate mwanga angalau kidogo kuhusu dini hiyo, na pia waifahamu Tanzania kama nchi yenye dini mbali mbali, na waweze kujua tunavyoishi pamoja.

Mimi kama m-Kristo, ninaweza kuelezea masuala ya u-Kristo Tanzania kwa kiwango cha kuridhisha. Vile vile, kutokana na juhudi zangu za kujielimisha kuhusu dini mbali mbali, ningeweza kutoa maelezo kuhusu u-Islam, kama ninavyofanya ninapofundisha fasihi.

Lakini niliona ni muhimu kuwapa wanafunzi hao fursa ya kukutana na kujifunza kutoka kwa viongozi wa dini ya ki-Islam. Fursa nzuri ilijitokeza tulipokuwa Kalenga, mkoani Iringa, kwenye Makumbusho ya Mkwawa. Hiyo ilikuwa ni tarehe 11 Agosti. Baada ya ziara ya makumbusho, niliona msikiti, nikamwambia mkurugenzi wa makumbusho, ndugu Nicholaus Kulanga, kuwa ningependa kuonana na imam wa msikiti, ili anisaidie kuwaelimisha wanafunzi wangu kuhusu u-Islam. Mkurugenzi aliahidi kututambulisha.

Siku ya pili, alasiri, tulienda tena Kalenga, tukapata fursa ya kuongea na Imam Zuberi Suleiman. Nilimweleza lengo na madhumuni yangu, yaani kuwapa wanafunzi wangu fursa ya kuelewa kidogo kuhusu u-Islam, kwani fursa za aina hiyo ni nadra Marekani, na wa-Marekani wengi hawaelewi chochote au wana mawazo potofu kuhusu u-Islam.

Imam, anayeonekana pichani amevaa kanzu na kofia, alivutiwa na ombi hilo, akatuongoza hadi kwenye msikiti wa mwanzo wa Kalenga. Wakati anajiandaa kuongea nasi, alimwita pia mwenzake, ambaye ni Ustaadh Maneno, akajumuika nasi.

Imam na Ustaadh walitoa maelezo ya chimbuko la u-Islam na misingi yake kwa ufasaha kabisa. Hata mimi ambaye ninaelewa mambo kadha wa kadha kuhusu u-Islam nilipata mwanga mpya. Imam alinionyesha kitabu kiitwacho "Tafsiri ya Sehemu ya Kumi ya Mwisho ya Qur'an Tukufu." Nilivutiwa na kitabu hiki, na nitakinunua.

Sote tulifurahi kupata fursa hii ya kuongea. Nilijisikia vizuri pale Imam na Ustaadh waliposema wamefurahishwa kuwa nafahamu mengi kuhusu u-Islam. Wakati tunaagana, Ustaadh Maneno aliwapa majina mapya hao wanafunzi: huyu mvulana jina lake ni Abdi Karim na huyu dada jina lake ni Bi Aisha. Jambo hili lilitufurahisha wote, tukacheka kwa furaha. Niliwaeleza hao wanafunzi heshima ya majina hayo katika u-Islam, na kuanzia siku ile nimekuwa nikiwaita kwa majina hayo.

Tumejenga uhusiano mzuri hapo Kalenga. Mwakani, Insh'Allah, natawapeleka wanafunzi wengine hapo.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...