Monday, July 28, 2014

Vitabu Nitakavyoonesha Katika Tamasha la Afrifest, Agosti 2

Kila mwaka wakati wa tamasha Afrifest, ninakuwa na meza ambapo naonesha vitabu vyangu na machapisho mengine. Meza ya vitabu huwavuta watu waje hapo. Kwa kawaida, mbali ya kutaka kunifahamu na kufahamu shughuli zangu, watu wanaofika hapo huwa na hamu ya kujua vitabu vinahusu nini. Wengi huvishika wao wenyewe na kuangalia ndani.

Kwa mawazo yangu, hiyo si fursa ya kuvipigia debe vitabu hivyo. Ninachofanya ni kujibu masuali niulizwayo. Kama suali linahusu kitabu au vitabu moja kwa moja, naelezea pia chimbuko la kitabu na uhusiano wake na shughuli zangu.

Ninaposema shughuli zangu, ninamaanisha ufundishaji wa fasihi na lugha ya ki-Ingereza, utafiti katika masimulizi ya jadi, uandishi, utoaji wa ushauri kuhusu tofauti za tamaduni kwa wa-Marekani waendao Afrika. Pia naongelea kuhusu kuwaandaa wanafunzi na kuwapeleka katika safari za masomo Afrika.

Kwa namna moja au nyingine, masuala ya aina hiyo yanajitokeza katika vitabu vyangu. Ni kawaida kwamba mtu anayekuja kwenye meza yangu anakuwa na hamu zaidi ya mada fulani, na hiyo inamfanya aulizie zaidi kuhusu kitabu fulani, na huamua kukinunua.

Tarehe 2 Agosti, katika tamasha la Afrifest litakalofanyika North View Junior High School, Brooklyn Park, hapa Minnesota, nitapeleka vitabu vifuatavyo.

Kimoja ni Matengo Folktales, ambacho ni mkusanyo wa hadithi kumi za jadi za wa-Matengo, nilizorekodi miaka ya katikati ya sabini na kitu, nikazitafsiri kwa ki-Ingereza na kuziandikia uchambuzi.

Kitabu hiki nimekiandika kwa namna ya kuweza kusomwa na yeyote, na pia katika masomo ya kiwango chochote, hadi chuo kikuu.













Kitabu kingine ni Notes on Achebe's "Things Fall Apart". Maelezo ya historia ya kitabu hiki niliyaandika katika blogu hii.

















Kitabu kingine  ni Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Wasomaji wa blogu hii watakuwa wamekisikia, na wengine wamekisoma.

Kitabu hiki nilikiandika katika mazingira maalum. Nikiwa mmoja wa washauri katika pogram za Associated Colleges of the Midwest za kupeleka wanafunzi Afrika, nilikuwa nikiongelea sana, kwenye mikutano yetu masuala ya athari za tofauti za tamaduni, kwani wanafunzi wanaporudi kutoka Afrika, wanakuwa na masuali mengi kuhusu mambo waliyoyaona kule. Mengine yalikuwa ya kustaajabisha na mengine ya kukera, na mengine ya kukanganya akili. Kazi yangu ilikuwa kufafanua, kwa sababu nawafahamu kutosha wa-Marekani na wa-Afrika. Basi washauri wenzangu katika program hizi walinishawishi niandike mwongozo, uweze kutumiwa nao na wanafunzi wao wanapokwenda Afrika.








Kingine ni CHANGAMOTO: Insha za Jamii. Ni mkusanyo wa insha kuhusu masuala ya siasa, uchumi, elimu, na utamaduni, kwa kuzingatia hasa hali ya Tanzania.

Lengo lilikuwa kuwajibu wale waliokuwa wananiuliza kwa nini siandiki kwa ki-Swahili, ili wa- Tanzania walio wengi waweze kusoma. Pamoja na kukubaliana na mtazamo wao, sherti niseme pia kuwa wa-Tanzania waache kujiziuka; wajifunze ki-Ingereza na ikiwezekana, lugha zingine pia. Kiswahili kina manufaa, lakini hakitawafikisha mbali katika dunia ya utandawazi wa leo. Shaaban Robert, ambaye wa-Tanzania hupenda sana kuunukuu usemi wake kuwa titi la mama li tamu, akimaanisha lugha yake ya ki-Swahili, hakuwa mvivu kama walivyo wa-Tanzania wa leo. Pamoja na kuwa hakuwa na fursa kama tulizo nazo leo, alijitahidi akajifunza ki-Ingereza na hata kukitumia. Aliziheshimu lugha na tamaduni za kigeni.

Kitabu kingine ni Africans in the World. Hiki ni kijitabu kidogo sana. Kinahusu historia ya wa-Afrika na wengine wenye asili ya Afrika, pamoja na siasa, utamaduni, na mengine kama hayo. Kilitokana na Afrifest ya kwanza mwaka 2007. Niliandaa magango kumi, kila bango likiwa linaelezea kipengele fulani. Hatimaye, yaliyomo kwenye mabango niliyachapisha kwa umbo la hiki kijitabu. Hakuna tofauti yoyote kati ya yale mabango na hiki kijitabu, isipokuwa ukubwa tu. Ufundishaji wangu wa somo la "Africa and the Americas," chuoni St. Olaf, ulinirahizishia kazi ya kuandika kazi hii.

Friday, July 25, 2014

Kitabu Kimefika Salama Dar es Salaam

Leo nimefurahi kumsikia mwanablogu Bwaya akielezea kuwa amepata kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ambacho nilimpelekea Dar es Salaam, tarehe 14 Julai. Ameandika taarifa hii kwenye ukurasa wake wa Facebook na pia katika blogu yake, na sehemu zote mbili ameambatanisha picha inayoonekana hapa kushoto. Ni picha ya kitabu na pia bahasha ambayo nilitumia kitabu hiki.

Nimefurahi kwamba kitabu kimefika salama, kwani jana nilianza kuwa na wasi wasi kuwa labda kimepotelea njiani.

Namshukuru Ndugu Bwaya kwa kutoa taarifa hima alipopata, kama alivyoahidi. Kwa taarifa zaidi, pitia blogu ya Jielewe

Monday, July 21, 2014

Leo ni Kumbukumbu ya Kuzaliwa Hemingway

Leo ni siku ya kumbukumbu ya kuzaliwa Ernest Hemingway. Alizaliwa tarehe 21 Julai, 1899, Oak Park, kitongoji cha Chicago.

Hemingway ni mwandishi maarufu pengine kuliko wote walioandika ki-Ingereza katika karne iliyopita, na bado yuko juu sana. Anasifika kwa mengi, ikiwemo kuasisi mtindo wa uandishi ambao wengi wameufuata, hasa msisitizo katika uandishi wa sentensi fupi.

Haiwezekani kwa mtu yeyote kukumbuka tarehe za kuzaliwa kwa kila mtu maarufu. Imekuwa bahati tu kuwa nimekumbuka kuwa leo, tarehe 21 Julai, ndio tarehe ya kuzaliwa Hemingway.

Hemingway ni mwandishi ambaye maandishi yake nayasoma sana, pia maandishi ya wengine kumhusu yeye, na tahakiki mbali mbali za maandishi yake.

Kitu kimoja kinachonivutia sana ni kauli mbali mbali za Hemingway kuhusu masuala kadha wa kadha ya maisha, uandishi, falsafa, na kadhalika. Ukizingatia kwamba Hemingway alipenda sana kunywa, hebu fikiria, kwa mfano usemi wake huu: "I drink to make other people more interesting."

Alisema mengi kuhusu hali halisi ya uandishi, kwa mfano: "There is nothing to writing. All you do is sit down at a typewriter and bleed." Mengine machache nimeyanukuu katika makala yangu, "Writing as hard Labour."

Aliipenda sana Afrika, na alisema mengi kuhusu hilo, ambayo nimeyasoma hapa na pale, kwa mfano katika kitabu chake cha The Green Hills of Africa. Jana, katika kupitia kitabu cha Papa Hemingway, kilichoandikwa na rafiki yake A.E. Hotchner, nimeona kauli ya Hemingway ambayo sikuwa nimeiona kabla. Hemingway alikuwa katika mipango ya kwenda tena Afrika, na Hotchner, ambaye alikuwa New York, alimwuliza kama angepitia New York. Hemingway alijibu:

Sure, I'll see you before we leave, either in New York or here if we by-pass New York. Going back to Africa after all this time, there is the excitement of a first adventure. I love Africa and I feel it's another home, and any time a man can feel that, not counting where he's born, is where he's meant to be.

Wasomaji wa blogu yangu hii na ile ya ki-Ingereza, watakuwa wanafahamu kuwa mimi ni msomaji na mfuatiliaji mkubwa wa Hemingway. Nina ndoto ya kuandika kitabu kumhusu Hemingway, kitakachohusu uhusiano wake na Afrika.

Juzi hapo, tarehe 15 mwezi huu, nilipoongea na Mzee Patrick Hemingway, ambaye anafahamu ninavyomheshimu Hemingway kwa uandishi na msimamo wake kuhusu Afrika, nilimwambia kuwa ninapangia, hatimaye, kuandika kitabu, ambacho nitakiita "Hemingway's Africa." Mzee Hemingway aliafiki, akisema kuwa itakuwa bora kwa vile mimi ni mw-Afrika.

Ningeweza kuandika sana kuhusu mada hii, lakini leo nilitaka tu kujikumbusha kuwa tarehe kama hii, yaani Julai 21, ndio tarehe aliyozaliwa Hemingway.

Saturday, July 19, 2014

Tunajiandaa kwa Tamasha la Afrifest, Agosti 2

Kila mwaka, tangu mwaka 2007, nahudhuria tamasha la Afrifest, ambalo hufanyika hapa Minnesota, Marekani.

Imewahi kutokea kwamba nilikuwa Tanzania wakati wa tamasha hilo. Binti zangu wananiwakilisha.Wanafahamu vizuri shughuli zangu, na wanawaeleza watu wanaoulizia kuhusu shughuli zangu na vitabu vyangu.

Hizo "ti-sheti" tulizovaa zina nembo ya kikampuni changu kiitwacho Africonexion: Cultural Consultants, ambacho najaribu kukijenga.





Hapa kushoto anaonekana Deta, binti yangu wa kwanza. Siku hiyo sikuwepo.













Hapa kushoto anaonekana Zawadi, binti yangu wa mwisho, akiwa anangojea watu. Hapo ni wakati alipokuwa mdogo. Alianza kuipenda shughuli hii tangu alipokuwa mdogo sana. Alikuwa akifuatana nami kwenye matamasha ya utamaduni, akinisikiliza ninapoongea na watu. Tangu akiwa na umri ule mdogo, aliweza kuwaeleza watu kuhusu shughuli zangu na kuhusu vitabu vyangu. Kwa mfano, katika mji wa Faribault kulikuwa na tamasha la tamaduni, nami nikiwa Tanzania. Zawadi alihudhuria mwenyewe. Alihojiwa na gazeti la Faribault Daily News, akatoa maelezo vizuri kabisa.





Shughuli kama Afrifest ni fursa ya watu kutoka sehemu mbali mbali za dunia na tamaduni mbali mbali kukutana. Naamini kuwa kwa watu wazima, vijana, na watoto, hii ni elimu bora kabisa.Hapa kushoto Zawadi anaonekana akiwa na watu wawili kutoka visiwa vya Caribbean.



Hapa kushoto wanaonekana Deta na Zawadi wakihojiwa. Kila mwaka, habari za Afrifest zimekuwa zikitangazwa katika vyombo vya habari vya hapa Minnesota. Mahojiano na waandaaji na washiriki huwa sehemu ya taarifa hizo.
Kwa mtoto au kijana, kuhojiwa namna hii ni kujijengea tabia ya kujiamini na pia uwezo wa kujieleza.






Hapa naonekana nikiwa na mama mmoja aliyekuja kwenye meza yangu. Nilimweleza yale aliyoulizia. Hata hivi, kwa kumwangalia usoni, hakuonekana anavutiwa na yale niliyokuwa nasema. Niligundua hatimaye kuwa dhana yangu haikuwa sahihi, kwani, bila mimi kutegemea, alitoa pochi yake, akalipia vitabu viwili: Africans and Americans: Embracing Cultural Differences na Matengo Folktales.Baada ya kuchukua hivyo vitabu, akajiondokea zake, kimya kimya. Nilizidi kuamini kuwa huyu mama sio mzungumzaji sana.


Mwaka huu, Afrifest itafanyika North View High School katika mji wa Brooklyn Park, Minnesota, tarehe 2 Agosti. Lakini shughuli za mwanzo zitafanyika siku moja kabla, yaani Agosti 1, kama unavyoona katika tangazo hapa chini. Kwa taarifa zaidi, tembelea www.afrifest.org

Thursday, July 17, 2014

Ninasoma Vitabu Vitatu kwa Mpigo

Siku hizi, nimekuwa nikisoma vitabu vitatu kwa mpigo. Kitabu kimojawapo ni A Moveable Feast cha Ernest Hemingway. Hiki ni kati ya vitabu vya Hemingway vilivyochapishwa baada ya kufariki kwake. Mswada wa kitabu hiki ulihaririwa kwanza na Mary Welsh, mke wake wa nne na wa mwisho, ukachapishwa mwaka 1964.

Mimi ninasoma toleo jipya la mswada huu, ulivyohaririwa na Sean Hemingway, na kuandikiwa utangulizi na Patrick Hemingway. Toleo hili lilichapishwa mwaka 2009. Miaka ya 1921 hadi 1926 Hemingway aliishi Paris, na kitabu kinaelezea mambo ya wakati ule, yakiwemo mahusiano yake na waandishi mashuhuri kama Gertrude Stein, ambaye alichangia sana kumkomaza kijana Hemingway katika uandishi. Bado ninakisoma, isipokuwa habari zake nimezifahamu kwa miaka kadhaa.

Kitabu kingine ninachosoma ni Nomad (New York: Free Press, 2011), kilichotungwa na Ayaan Hirsi Ali. Kinahusu maisha yake. Huyu ni mama aliyezaliwa Somalia, akalelewa katika u-Islam. Baadaye aliacha dini hiyo, kitendo ambacho kilisababisha awe mkimbizi, kwani kuacha u-Islam ni kosa kubwa, naye amelazimika kuishi kama mkimbizi Ulaya na sasa Marekani, akihofia kuuawa. Msimamo wa Ayaan Hirsi Ali ni kwamba u-Islam ni dini katili na kandamizi, hasa kwa wanawake. Ayaan anasema hana dini. Binafsi, ningependa watu wakisome kitabu chake, na kama wanaweza kuupinga msimamo wake, tutafaidika sana, hasa sisi ambao si wa-Islam.

Kitabu cha tatu ninachosoma ni The Pearl (New York: Bantam, 1973), kilichotungwa na John Steinbeck, mwandishi maarufu m-Marekani, aliyepata tuzo ya Nobel mwaka 1962. Binafsi,  nisikiapo jina la Steinbeck, nawazia kwanza riwaya zake za The Grapes of Wrath na  Of Mice and Men. Vile vile, jina la Steinbeck linanirudisha kwenye miaka ya sitini na kitu, nilipokuwa nasoma sekondari. Nilisoma riwaya yake ya The Moon is Down, ambayo ilinigusa sana, ikazitawala hisia zangu kwa namna ambayo nashindwa kuelezea.

Huu ni wakati wa likizo. Nina muda mwingi wa kujisomea vitabu ninavyopenda, bila kusukumwa na mahitaji ya shule. Panapo majaliwa, nikishamaliza kusoma vitabu hivi ninavyovisoma wakati huu, nitaviongelea katika blogu hii.

Wednesday, July 16, 2014

Madreva Wetu Katika Kozi ya "Hemingway in East Africa, 2013"

Katika safari zetu, wanafunzi wangu nami, nchini Tanzania, mwezi Januari mwaka 2013, tulitumia kampuni ya utalii ya Shidolya, yenye makao yake Arusha. Hapa naleta picha ya madereva wetu, kutoka kwenye kampuni hiyo.

Tulisafiri salama kila mahali: Arusha, Longido, Mto wa Mbu, Karatu, Ngorongoro, Serengeti, Manyara, Babati, na Tarangire. Tulikuwa na bahati; hatukupata tatizo.

Nimeona ni jambo jema kuwakumbuka madereva. Kwa bahati mbaya sina picha ya wapishi wetu, ambao nao walituhudumia vizuri kabisa.

Tuesday, July 15, 2014

Leo Nimeongea Tena na Mzee Patrick Hemingway

Leo, saa kumi na dakika hamsini na mbili, nilimpigia simu Mzee Patrick Hemingway. Niliona tu nimpigie, baada ya kimya cha miezi mingi, wakati nilipozidiwa na homa. Sasa, kwa vile najisikia nafuu sana, niliamua kumpigia Mzee Hemingway. Nilimweleza kuwa nimekuwa kimya kwa muda mrefu kwa sababu ya kuugua, ila sasa hali yangu ni nafuu sana na inaendelea kuimarika. Tumeongea hadi saa kumi na mbili na robo.

Baada ya kusalimiana tu, Mzee alinifahamisha kuwa yeye na ndugu yake Sean Hemingway wamechapisha toleo jipya la kitabu cha Hemingway, The Sun Also Rises. Nami hapo hapo nikamwambia kuwa nimempigia simu leo baada ya kusikiliza, jana, mahojiano baina ya mtangazaji wa redio na Sean Hemingway, kuhusu kuchapishwa kwa toleo hili

Mada hii tumeiongelea kwa muda mrefu, tukijumlisha pia mawazo na maandishi mengine ya Hemingway, kama vile True at First Light na Under Kilimanjaro. Tuliongelea kuhusu wahakiki wa Hemingway na jinsi Hemingway alivyokuwa hawapendi. Mzee Hemingway aliniambia kuwa kuna makala yenye mawazo mazuri kuhusu Hemingway ambayo ameisoma mtandaoni, iliyoandikwa na mhakiki wa Iran.

Hiyo mada ya uhakiki nayo tumeiongelea kwa muda mrefu, na Mzee Hemingway akasisitiza kuwa waandishi wengi hawatumii ki-Ingereza vizuri. Hapo hapo akaongezea kuwa mimi ni tofauti; naandika vizuri. Nimefurahi sana kumsikia akisema hivyo, na baadaye katika maongezi yetu alirudi tena kwenye suala hili, akasema anakipenda kitabu changu na anakiongelea kwa watu. Hilo nalo limenifurahisha. Nilijua kuwa Mzee Hemingway anakipenda kitabu changu, lakini amenishtua leo kwa kukiongelea wakati ambapo tulikuwa tunaongelea mambo mengine.

Kama kawaida, tumeongelea pia habari za kuishi kwake Tanganyika (hatimaye Tanzania). Nilimwuliza zaidi kuhusu suala hilo, nikimkumbushia kuwa nilishamwambia napangia kwenda Iringa kufanya utafiti. Hii mada nayo tumeiongelea kwa muda mrefu, na amenipa dokezo zaidi kuhusu yale ninayotaka kutafiti.

Amenielezea kuhusu waandishi, tukaongelea nadharia ya Hemingway juu ya uwindaji wa kweli, na nadharia ya ukweli katika uandishi. Nilimwambia kuwa kadiri siku zinavyopita, na kadiri ninavyozidi kusoma maandishi ya Hemingway, napata picha kuwa itabidi nisome maandishi yake yote, kwani mara kwa mara kuna vipengele vinavyojitokeza tena na tena katika vitabu vmbali mbali.

Nilimwambia kuwa moja ya ndoto zangu ni kuandika kitabu "Hemingway's Africa," naye akasema itakuwa vizuri, hasa kwa vile mimi ni mw-Afrika. Nami nakubaliana naye. Amenisikiliza tangu tulipofahamiana mara ya kwanza, jinsi ninavyomwenzi Hemingway kwa jinsi alivyoandika kuhusu nchi yangu na Afrika Mashariki kwa ujumla, juu wa mazingira ya nchi, watu, na wanyama, na jinsi alivyoipenda sehemu hii ya dunia, akafanya kila juhudi ya kuwashawishi wanafamilia waende kule. Nilishamwambia Mzee Hemingway jinsi ninavyomshukuru Hemingway na jinsi nilivyo na msimamo tofauti katika masuala mengi yanayomhusu Hemingway, tofauti na watafiti wengine.

Ninafurahi kwa jinsi Mzee Patrick Hemingway anavyonisaidia kufahamu zaidi mambo ya Hemingway. Ni bahati ya pekee kwangu, na kwa yeyote yule, kwamba tuna fursa ya kuongea na huyu Mzee, ambaye ndiye motto pekee wa Hemingway aliye bado hai. Ana umri wa miaka 87 sasa. Kama kawaida yake, Mzee Hemingway amenieleza mambo ya kusisimua kuhusu watafiti wa kigeni waliofika Afrika na kukaa muda mfupi tu, wakarudi wakijifanya ni wataalam wa mambo ya Afrika.

Ili kugusia kila mada tuliyoongelea, itabidi niandike insha ndefu, na hapa sio mahali pake. Kumbukumbu zangu za maongezi ya leo nitaziandika mahali pengine, panapo majaliwa.

Monday, July 14, 2014

Vitabu Nilivyonunua Leo

Leo mchana, wakati binti yangu Deta ananirudisha kutoka hospitalini, tulisikia katika redio ya garini mahojiano na Sean Hemingway, mjukuu wa Ernest Hemingway. Mahojiano yalihusu toleo jipya la kitabu cha Ernest Hemingway, The Sun Also Rises. Ilikuwa ni mwanzo kwangu kusikia kuwa Sean amehariri  toleo jipya la kitabu cha The Sun Also Rises.

Sikushangaa kusikia kuwa kampuni ya Scribner ndiyo imechapisha. Nimefahamu tangu zamani kuwa Scribner ni kampuni kongwe ambayo ilichapisha vitabu vya Hemingway tangu zamani.

Niliposikiliza mahojiano hayo, niliamua hapo hapo kwenda kutafuta nakala ya hili toleo jipya. Tulipita kwenye duka la vitabu la chuo cha St. Olaf na nikaambiwa kuwa tayari wanacho kitabu hiki. Niliwaambia waniwekee, ili nije kununua.

Wakati huo huo, niliamua kutafuta nakala ya toleo la mwanzo la The Sun Also Rises. Katika kusoma maandishi ya Hemingway, kwa miaka, nilifahamu kuwa The Sun Also Rises ni kitabu kilichompa Hemingway umaarufu miaka yake ya mwanzo kama mwandishi. Kilichapishwa mwaka 1926, na kiliupa umaarufu mji wa Pamplona ulioko Hispania. Nilikuwa sijakisoma kitabu hiki, na bado sijakisoma, lakini kwa miezi mingi kimekuwa ni kipaumbele katika maazimio yangu ya vitabu vya kuvisoma mapema iwezekanavyo.

Mahojiano niliyoyasikia redioni yalidhihirisha kuwa toleo hili jipya la The Sun Also Rises lina mambo kadhaa ambayo hayakuwemo katika toleo la mwanzo. Jambo hili lilinizidishia hamu ya kupata nakala ya toleo la mwanzo, ili nitakaposoma, niweze kufananisha. Basi, tulipitiliza hadi mji wa Apple Valley, kutafuta hili toleo la mwanzo la kitabu, katika duka la Half Price Books. Kwa bahati mbaya hawakuwa na nakala.

Badala yake, nilinunua vitabu vingine vinne. Kitabu kimojawapo ni Papa Hemingway, kilichoandikwa na A.E. Hotchner. Huyu alikuwa rafiki wa karibu wa Ernest Hemingway. Nilinunua nakala ya kitabu hiki miaka kadhaa iliyopita, lakini leo nimeona toleo lenye picha ya Hemingway kwenye jalada, nikavutiwa. Kwa hivi, ninazo nakala mbili za kitabu hiki.

Kitabu kingine nilichonunua leo ni Leaf and Bone, kilichohaririwa na Judith Gleason. Ninacho kitabu hiki tangu zamani, "hard cover," na nimekisoma mara kadhaa na kukitumia katika somo la "folklore." Lakini leo nilivyoliona toleo la "paperback" niliamua kununua. Kwa hivi, ninazo nakala mbili za kitabu hiki.

Kitabu kingine nilichonunua leo ni Shalimar the Clown, riwaya ya Salman Rushdie. Ingawa nina vitabu kadhaa vya Salman Rushdie, hiki sikuwa nacho. Mwaka jana nilifundisha riwaya maarufu ya Salman Rushdie, Midnight's Children. Sio riwaya rahisi kuielewa, ila ina mvuto wa aina yake.

Wakati wa kufundisha kitabu hiki, nilikuwa nashangaa kwa nini watu walikuja juu na kulaani riwaya yake ya Satanic Verses, wakati staili aliyotumia katika Satanic Verses, na pia baadhi ya kejeli ni zile zile katika Midnight's Children. Kwa mujibu wa nadharia ya fasihi, sio sahihi kumshambulia mwandishi kwa yale yanayosemwa na wahusika katika kitabu chake, kama vile haya ndio mawazo au msimamo wa mwandishi mwenyewe.

Ni mbaya pia pale wanaomshambulia ni watu ambao hawajasoma alichoandika. Mtu unaweza kujiuliza: kati ya maelfu walioandamana kulaani kitabu cha Satanic Verses, ni wangapi walikuwa wamekisoma? Ni wangapi wanaojua ki-Ingereza na fasihi kiasi cha kuweza kukielewa kitabu hiki?

Kitabu cha nne nilichonunua leo ni English Fairy Tales, mkusanyiko wa hadithi za jadi za wa-Ingereza. Ninazo baadhi ya hadithi hizo katika vitabu vyangu vingine. Lakini nilipenda kuwa na kitabu hiki, ambacho, kwenye jalada, kimesemwa kuwa ni "Complete and Unabridged," yaani ni mkusanyiko kamilifu, bila marekebisho ya kuzirahisisha hadithi zilizomo. Ningependa kujadili dhana ya "fairy tales" na kuitofautisha na "folk tales," kama wengi tuliomo katika taaluma ya "folklore" tunavyotofautisha. Lakini kwa leo, nitaishia hapa.

Tuesday, July 8, 2014

Karatu: Baada ya Darasa Kumalizika

Hapa ni Karatu, Tanzania, mwezi Januari, mwaka 2013.  Ilikuwa mara tu baada ya kumaliza kipindi katika kozi yangu ya "Hemingway in East Africa." Hapa wanaonekana wanafunzi, mimi, na wenyeji watatu waliokuja kujumuika nasi. Sote tulifurahi kujumuika nao.

Huyu bwana aliyeshika kitabu changu ni mwanasheria. Aliweza kuongea na baadhi ya wanafunzi, wakamweleza manufaa ya kitabu hiki kwao. Ninayo video inayowaonyesha wakiongea. Hao akina mama wawili, mmoja mwenye khanga na mwingine mwenye "jeans" ni mahakimu.

Sunday, July 6, 2014

Hemingway: "True at First Light"

Tulipomtembelea Mzee Patrick Hemingway, kule Montana, alituzawadia nakala za kitabu cha Ernest Hemingway, True at First Light. Tayari nilikuwa na nakala mbili hivi za kitabu hiki, na nilikuwa nimekisoma. Pia ni kitabu kimojawapo ambacho nilikitumia katika kozi yangu ya "Hemingway in East Africa."

Hata hivi, zawadi hii kutoka kwa Mzee Patrick Hemingway ilinigusa sana. Jalada lake tu lilinivutia kwa namna ambayo siwezi kuelezea. Pili, ilikuwa ni bahati ya pekee kupata nakala kutoka kwa mhariri wa kitabu.

Ernest Hemingway aliandika mswada mrefu sana kutokana na safari yake ya pili Afrika Mashariki. Alisafiri na kuishi kule miezi kadhaa, kuanzia mwaka 1953 hadi 1954. Hakuuchapisha mswada huu, bali aliuhifadhi Cuba, ambako aliishi miaka mingi. Alisema kuwa ni urithi kwa watoto wake.

Miaka ya hivi karibuni, mswada huu ulitayarishwa na kuchapishwa kitabu, Under Kilimanjaro. Ni kitabu kikubwa sana, ila nilikuwa nimekisoma. Humo, Hemingway anaelezea vizuri hali ilivyokuwa miezi aliyokaa Afrika Mashariki, akiwa na Mary Welsh, mke wake wa nne, na wa mwisho. Anaelezea vizuri maisha ya wenyeji, hasa wa-Kamba na wa-Maasae.

Mzee Patrick Hemingway ametufanyia msaada mkubwa kwa kuuhariri mswada ule upya na kuchapisha True at First Light, ambacho ni kitabu cha wastani, sio kikubwa kama Under Kilimanjaro. Katika kozi yangu ya "Hemingway in East Africa," nilijaribu kutumia Under Kilimanjaro, lakini niliona kuwa ni kazi nzito mno kwa wanafunzi, na muda haukutosha. Lakini kwa sisi watafiti, ni wajibu kulisoma na kulitafakari buku hili lote.

Jambo jingine la peke kwangu ni kuwa Mzee Patrick Hemingway alisaini nakala hizo alizoutuzawadia. Hapa naleta picha ya kumbukumbu hiyo adhimu. Kwa watu wenye uzoefu wa vitabu, ni bahati ya pekee kusainiwa nakala ya kitabu chako na mwandishi au mhariri.

Nimalizie tu kwa kusema kuwa baada ya kurejea kutoka Montana, nilikuwa na dukuduku ya kufahamu zaidi kuhusu mchapishaji wa hili toleo tulilozawadiwa na Mzee Patrick Hemeingway.

Nilishaona, mwanzoni mwa kitabu, kuwa mchapishaji ni Arrow Books wa Uingereza. Katika kutafuta zaidi mtandaoni,  niliona pia picha ya hilo jalada inayoonekana hapa juu, ambayo sikuwa nimeionaa popote kabla. Kama ilivyo kwa vitabu vingi, kitabu cha True at First Light kimechapishwa kikiwa na majalada tofauti.

Thursday, July 3, 2014

Naulizwa Kama Nafundisha ki-Swahili Hapa Marekani

Mara kwa mara, ninapokutana na wa-Tanzania wasionifahamu vizuri, au wasionifahamu kabisa, wasikiapo kuwa nafundisha kwenye chuo fulani Marekani, wanauliza iwapo nafundisha ki-Swahili.

Suali hili linaweza kuonekana kuwa rahisi, lakini kwangu ni suali tata. Kifupi ni kuwa mimi nafundisha katika idara ya ki-Ingereza ya Chuo cha St. Olaf, hapa Minnesota. Idara hii ilinialika kuja hapa kuanzisha kozi katika somo la "Post-Colonial Literature," na pia kufundisha uandishi wa ki-Ingereza. Nilichukuliwa, mwaka 1991, kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, ambapo nilikuwa nafundisha katika idara ya "Literature."

Hakuna kozi ya ki-Swahili katika chuo hiki cha St. Olaf. Mbali ya ki-Ingereza, lugha zinazofundishwa hapa ni ki-Jerumani, ki-Japani, ki-China, ki-Spaniola, ki-Norway, ki-Latini, na ki-Griki cha kale.

Ninapotafakari suala la kufundisha ki-Swahili, najutia kwa nini sina ujuzi utakiwao, nikizingatia kuwa hii kwangu ni lugha karibu sawa na lugha mama. Nimeifahamu na kuitumia tangu utotoni. Lakini, lazima nikiri kuwa sina utaalam wa kuifundisha. Ningejivunia kuweza kufundisha ki-Swahili. Wazo hilo nimelielezea pia katika kitabu changu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii.

Mtu huwezi kukurupuka tu, ukafundisha ki-Swahili chuoni, au hata katika shule ya msingi. Lazima ujue mambo mengi yanayohusu lugha hiyo na uwe na utaalamu wa kuifundisha, ambao una vipengele vingi kufuatana na kiwango cha wanafunzi. Sikusomea taaluma hiyo, kwa hivyo siwezi kujitupa katika uwanja ambao siufahamu itakiwavyo.

Kwa kawaida, hao watu wanaoniuliza kama nafundisha ki-Swahili hapa Marekani nadhani wanaamini kuwa kwa mtu kama mimi kufundisha ki-Swahili Marekani ni jambo rahisi tu. Hawaonekani kufahamu hayo niliyosema hapa juu, kwamba inahitaji elimu ya pekee ya lugha husika na ufundishaji wake.

Wanashtuka ninapowaeleza kuwa nafundisha ki-Ingereza. Hawategemei kusikia m-Swahili anawafundisha wa-Marekani ki-Ingereza, ambayo ni lugha yao. Kwa upande wangu, kila ninapoulizwa kama nafundisha ki-Swahili hapa Marekani, huwa najichekea moyoni, ingawa sionyeshi kwao kwamba suali lao linanichekesha. Sio vizuri, wala uungwana kumcheka mtu, na kumfanya ajisikie vibaya, kwa suali kama hilo.

Wednesday, July 2, 2014

Mandhari ya Mto wa Mbu na Ziwa Manyara

Mwezi Januari, 2013, katika mizunguko yangu Tanzania na wanafunzi wa Chuo cha St. Olaf, tukiwa tunafuatilia safari na maandishi ya Ernest Hemingway, niliamua tusimame kwenye mlima juu ya Mto wa Mbu, pembeni ya barabara iendayo Karatu.

Mkisimama hapo, mnauona mji wa Mto wa Mbu kule bondeni, na kwa mbali kule mbele mnaliona ziwa la Manyara.








Hata miaka iliyotangulia, wakati nasafiri na wanafunzi kutoka Chuo cha Colorado, tulifika mahali hapa. Mimi kama mwalimu naona ni muhimu kwa wanafunzi kufika sehemu hiyo na kuangalia sehemu hizi ambazo Hemingway alizielezea vizuri katika kitabu chake cha Green Hills of Africa. Inavutia kusoma maelezo ya Hemingway wakati mpo mahali hapa, anavyouelezea mji, mto unaopita hapo, duka la m-Hindu na uzuri wa Ziwa Manyara.

Nina imani kuwa sina haja ya kueleza kuwa anayeonekana hapo kushoto ni mimi.

Tuesday, July 1, 2014

Ngorongoro

Hapa ilikuwa ni mwezi Januari, 2013. Niko katika bonde la Ngorongoro, mmoja ya vivutio vikubwa vya utalii Tanzania. Nimebahatika kufika sehemu hiyo mara kadhaa. Kila wakati naguswa na uzuri na upekee wa mahali hapo.



Mara ya kwanza kufika hapo nilikuwa kiongozi wa wanafunzi na wazazi wao kutoka shule ya Shady Hill, Boston. Nilikuwa nimeombwa na kampuni ya Thomson Safaris kuongoza msafara huu.







Miaka iliyofuata nimefika hapo na wanafunzi kutoka vyuo vya Marekani vya Colorado na St. Olaf, tukiwa katika kozi ya "Hemingway in East Africa," ambayo niliitunga. Nimeandika makala kadhaa kuhusu kozi hiyo, na makala ya hivi karibuni kabisa ni hii hapa

Kila wakati naguswa na uzuri na upekee wa mahali hapo. Kuna wanyama wa aina aina, kama vile samba, pundamilia, twiga, tembo, vifaru na nyati.

Mara zote, tulitembelea pia hifadhi za Serengeti, Manyara, na Tarangire. Zote hizo ni utajiri mkubwa wa nchi yetu, kwa sasa na kwa vizazi vijavyo.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...