Tuesday, October 29, 2013

Nimepata Wageni Leo

Leo nimepata bahati ya kutembelewa na wageni wawili. Mmoja ni Mchungaji John Mhekwa kutoka Tungamalenga, Iringa. Mwingine ni Profesa Paula Swiggum wa chuo cha Gustavus Adolphus, St. Peter, Minnesota.

Mchungaji Mhekwa hatukuwa tunafahamiana, lakini Profesa Swiggum tumefahamiana kwa miaka kadhaa, kwani katika programu yake ya kupeleka wanafunzi Tanzania, alinialika kuongea nao kuhusu masuala ya tofauti za tamaduni, kama maandalizi ya safari.

Wanafunzi walikuwa wanasoma kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Huo ulikuwa ni uamuzi wake. Mazungumzo yangu na hao wanafunzi yalihusu mambo niliyoandika katika kitabu hiki. Baada ya Profesa Swiggum kustaafu, profesa aliyemrithi, katika kuendesha programu hiyo, Barbara Zust, aliendelea na utaratibu huo.

Kifupi ni kwamba Profesa Swiggum tumeanza zamani kiasi kushirikiana katika nyanja hizo. Leo ilikuwa fursa ya pekee ya kufahamiana na huyu mgeni mwingine, Mchungaji Mhekwa. Nimemwambia kuwa Tungamalenga nilipita, mwezi Agosti mwaka 2011, nikiwa na wanafunzi tukiwa tunaelekea hifadhi ya Ruaha.

Sunday, October 13, 2013

Tamasha la Vitabu Twin Cities, Oktoba 12, Lilifana

Tamasha la vitabu, Twin Cities Book Festival, lililofanyika mjini St. Paul, Minnesota, jana, tarehe 12, lilienda vizuri. Niliondoka mapema asubuhi, yapata saa mbili, nikafika kwenye maaonesho saa tatu. Sikuwa nimechelewa, kwani wakati naandaa vitabu vyangu kwenye meza yangu, wengine nao walikuwa wakiandaaa, ingawa wengi walishapanga vitabu vyangu siku iliyotangulia
Meza niliyopata, baada ya kulipia dola 80, ilikuwa namba 12. Nilikuwa nimejisajili kwa jina la Africonexion, ambayo kampuni yangu ndogo inayohusika na uchapishaji na uuzaji wa vitabu vyangu, na pia kuratibu mihadhara yangu ya kuchangia maelewano baina ya watu wa tamaduni mbali mbali. Tangu nilipoisajili kampuni hii, shughuli zake zimekuwa zikifanyika zaidi hapa Marekani, lakini hatimaye, hasa nitakaporejea Tanzania baada ya kustaafu hapa Marekani, nataka kuijenga kampuni hii Tanzania, Africa Mashariki, na sehemu zingine.







 




Kama kawaida, watu walianza kuingia ukumbini tangu milango ilipofunguliwa. Ukiwaangalia wanavyojishughulisha kuangalia vitabu kwenye meza mbali mbali, unaona kabisa kuwa hao ni watu wanaothamini elimu. Kwa vigezo vyangu, hao ni watu walioelimika.











Inavutia kuona jinsi watu wanavyoacha shughuli zao nyingine ili kuja kwenye tamasha la vitabu. Ingekuwa ni Tanzania, watu hawangehudhuria. Hilo nimeshuhudia tena na tena, na nami, na wengine wengi, tumeandika sana kuhusu suala hilo. Kadiri miaka inavyopita, Tanzania inazidi kuwa taifa la wajinga. Hakuna sababu ya kubembelezana; ukweli lazima usemwe.









Ushahidi wa kuelimika ni kuwa na kiu isiyoisha ya kujifunza mambo. Ni dukuduku ya kutaka kujua, ambayo kwa ki-Ingereza huitwa "intellectual curiosity." Mtu asiye na "intellectual curiosity" hajaelimika, kwa sababu kuridhika na kile ambacho unadhani unajua, ambacho kwa kweli ni kidogo, ni ujinga. Ni wajibu wangu kama mwalimu kupambana na tabia za aina hiyo, bila kumwonea aibu mtu yeyote.








Kama kawaida, ushiriki wangu katika tamasha la Twin Cities Book Festival ulikuwa na mafanikio mazuri. Nilionana na kuzungumza na watu wengi waliofika kwenye meza yangu. Niliuza vitabu kadhaa. Niliitangaza kampuni ya Africonexion kwa kuwagawia watu chapisho la ukurasa moja ambalo linaelezea shughuli zake, na pia niliwapa kadi ya biashara ya Africonexion.

Binti yangu Zawadi alifika baadaye kunisaidia kwenye meza yangu, nami nikapata fursa ya kutembelea meza za wachapishaji na waandishi wengine. Nilielimika sana kwa kuongea na watu mbali mbali, kujionea shughuli za uchapishaji na maelfu ya vitabu vilivyokuwepo kwenye maonesho. Nilipata fursa ya kuwaelimisha wengine, kama mwalimu, mwandishi na mshauri katika masuala ya tofauti za tamaduni na athari zake.

Tuesday, October 8, 2013

Vijana Washikwa Mtwara Wakiwa Katika Mafunzo ya Al Shabaab na Al Qaida

1 
Stori ambayo ilishika namba 1 kwenye habari 10 za AMPLIFAYA ya Clouds FM October 7 2013 ni hii ya Polisi Mtwara kukamata vijana 11 ambao walikua wakifanya mazoezi ya kijeshi waliyokua wakijifunza kutoka kwenye cd za magaidi zilizokua na mafunzo kutoka kwa makundi ya Al Shabaab na Al Qaeda.
Taarifa zaidi unaweza kuzisoma hapo chini kwenye hiyo taarifa iliyotolewa na jeshi la polisi.
2 3

4 5 6


CHANZO: dj sek

0 comments:


Post a Comment

Tamasha Kubwa la Vitabu, Twin Cities, Oktoba 12

Lile tamasha maarufu kabisa la vitabu ambalo limefanyika mjini Minneapolis kwa miaka mingi, mara moja kwa mwaka, limekaribia kabisa. Kuanzia mwaka jana, tamasha limehamia mjii St. Paul, kwenye viwanja vya State Fairgrounds.

Hakuna tamasha kubwa zaidi ya hili katika eneo hili la Minnesota na majimbo ya jirani. Wanahudhuria watu yapata 7,000, wapenzi wa vitabu. Wanakuwepo waandishi, wachapishaji, wahariri, wachora picha za vitabuni, wahakiki, wauzaji wa vitabu na majarida. Wanahudhuria wazee, watu wazima, vijana, na watoto.

Nimeshiriki tamasha hili kwa miaka mingi, kama mwandishi wa vitabu na mwelimishaji katika chuo kikuu na jamii. Kila mara nimepata fursa ya kuongea na wasomaji wa maandishi yangu na watu ambao sijawahi kuwafahamu kabla. Wanakuja na maoni, taarifa, na uzoefu mbali mbali. Tunabadilishana mawazo. Inakuwa ni kama shule muhimu sana. Tamasha linapoisha, jioni, najiona nimeelimika sana.

Namshukuru Mungu kwa kuniwezesha kuandika vitabu na maandishi mengine. Namshukuru kwa namna ya pekee kwa kuniwezesha kuandika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ambacho najua kimesomwa na bado kinasomwa na maelfu ya watu hapa Marekani, ambao huguswa na mawazo na ushauri niliotoa katika kitabu hiki.

Kwenye kila tamasha, ambamo kunakuweko vitabu maelfu kwa maelfu, unawajibika kushangaa wadau wanafikiaje uamuzi wa kununua kitabu fulani au vitabu fulani. Nina bahati kuwa kitabu changu, ingawa kimekuwepo sokoni kwa miaka mingi kiasi, hakijachujuka bali kinawavutia wateja. Ninachoweza kusema ni kimoja, kwamba yote ni mipango ya Mungu.

Baadhi ya watu ninaokutana nao ni waandishi chipukizi. Huniulizia namna ya kuchapisha kitabu. Nami huwahamasisha kufuatilia hali ya uchapishaji wa leo, unaotumia tekinolojia tofauti na zile tulizozizoea. Kwa taarifa, na kwa manufaa ya watu wanaoongea ki-Swahili, nimetoa maelezo na uzoefu wangu kuhusu uchapishaji huo na mikakati mingine inayohusika, katika kitabu changu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii.

Nimeshajiandaa vizuri kwa tamasha la tarehe 12. Nakala za vitabu vyangu ninazo, pamoja na matangazo na machapisho mengine. Nangojea kwa hamu kukutana na kuongea na watu wengi. Kwa namna ya pekee, nangojea kuongea na watoto. Insh'Allah, nitaandika ripoti ya tamasha, kama ilivyo jadi yangu. Kwenye tamasha hili, nimejisajili kwa jina la kampuni yangu ndogo iitwayo Africonexion: Cultural Consultants, ambayo nimekuwa nikijitahidi kuitambulisha Tanzania. Unaweza kuona jina hilo katika orodha ya wauza vitabu, ambayo hi hii hapa.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...