Friday, June 29, 2012

Kugombana na Madaktari ni Uchuro

Mgomo wa madaktari umeanza tena, siku chache zilizopita. Inasikitisha kuona kuwa tumefikia hali hiyo. Ukiniuliza nani namhesabu kama mwajibikaji mkuu aliyesababisha tatio hili, nitakuambia kuwa ni serikali ya CCM. Huo umekuwa msimamo wangu tangu pale ulipotokea mgomo wa mwanzo wa madaktari wiki kadha zilizopita. Nilieleza msimamo huo hapa.

Siku chache zilizopita, nilimsikiliza mwenyekiti wa madaktari wanaogoma, Dr.Stephen Ulimboka, akiongelea jinsi uhaba wa vitendea kazi ulivyo. Alitaja mfano wa kifaa cha "CT-scan" ambacho kimeharibika Muhimbili yapata miezi mingi iliyopita.

Kama nilivyosema katika makala yangu ya mwanzo, sera za serikali ya CCM zinasabisha upotevu mkubwa wa mali ya Tanzania, kama vile madini. Serikali yenyewe imekiri kuwa mikataba ya madini ya siku zilizopita ilikuwa ni ya hasara kwa Taifa. Lakini je, serikali imeshamwajibisha yeyote aliyehusika katika kusaini mikataba hiyo?

Je, ni kweli kuwa nchi hii haiwezi kununua hicho kifaa cha "CT-scan"? Kutokana na sera mbovu za CCM, makampuni kama Barrick yanafaidika sana na dhahabu yetu wakati sisi, ukifananisha na mapato wanayopata wao, sana sana tunaambulia mapato duni sawa na njugu kiganjani, na tunaambulia uharibifu wa mazingira na afya za watu wanaoishi maeneo ya migodini,

Kitu kimoja kinachokera katika mgogoro huu baina ya serikali na madaktari ni jinsi madai ya madaktari yanavyopotoshwa. Wako ambao wanaongea kama vile wanachodai madaktari ni posho na maslahi yao tu. Ukweli ni kuwa madaktari wana madai ya msingi ya kuwatetea wananchi. Kuna uchakachuaji wa makusudi unaofanywa kuhusu jambo hilo, ili ionekane kuwa madaktari hawajali maishai ya wananchi.

Ni kweli kuwa mgomo huu unaathiri maisha ya wa-Tanzania. Hili si jambo jema. Lakini serikali haina haki ya kuwashutumu madaktari kwa hoja hii ya kutojali maisha ya wa-Tanzania, wakati serikali hiii hiii inawakumbatia hao wanaoitwa wawekezaji ambao wengi wao wanahujumu maisha na afya za wa-Tanzania, achilia mbali kuharibu mazingira maeneo ya migodini. Serikali ingekuwa haifanyi hayo, ingekuwa na haki ya kuwaandama madaktari kwa hoja hii ya kuathiri maisha ya wa-Tanzania.

Katika mgogoro baina ya serikali na madaktari, kuna pia suala la serikali kutumia mwanya wa sheria na uamuzi wa mahakama. Serikali haifanyi haki inapokwepa kuwajibika kwa yale yanayodaiwa na madaktari, madai ambayo ni ya kweli, na yako katika uwezo wa serikali na nchi yetu hii ambayo ina utajiri mkubwa. Kama suala ni sheria na maamuzi ya mahakama, sote tunakubali kuwa sheria ichukue mkondo wake.

Lakini kinachokera ni kuwa serikali inatumia mwanya huu kufunika kile ambacho sisi wengine tunakiona ni uzembe na kutowajibika kwa serikali yenyewe. Madai ya madaktari ni ya msingi, na yako katika uwezo wa serikali hii. Kwa serikali kutowajibika hapo na kukimbilia mahakamani kuwabana madaktari kwa kipengele cha sheria tu, sio jambo la haki na haliiweki serikali katika sura nzuri, kwa mtazamo wangu.

Kama nilivyosema katika makala yangu ya mwanzo, kugombana na madaktari si jambo jema. Nilikumbushia usemi wa wahenga kuwa tusidharau wakunga na uzazi ungalipo. Napenda kuongezea kwa dhati kabisa kuwa kugombana na madaktari si dalili njema bali ni uchuro.

Wednesday, June 20, 2012

Nimetua Bondeni, kwa Madiba

Tarehe 14, nilitua Johannesburg, kuhudhuria mkutano ulioandaliwa na American Council of Learned Societies (ACLS). Mkutano tumefanyia katika chuo Kikuu cha Witwatersrand, ukiwa umehudhuriwa na watafiti kutoka Afrika Kusini, Ghana, Marekani, Nigeria, na Tanzania. Tulijadili mada za utafiti zilizowasilishwa na watafiti mbali mbali. Utafiti huo hugharamiwa na ACLS, kwa wale ambao miradi yao ya utafiti inaonekana kuwa ya kiwango kinachotakiwa. Mada zote zilikuwa katika nyanja mbali mbali za sayansi ya jamii.

Friday, June 8, 2012

Mama Shakila, Mwimbaji Maarufu

Mama Shakila ni mwimbaji maarufu wa taarab. Imepita miaka yapata 22 tangu nilipobahatika kumtembelea na kuongea naye kuhusu maisha yake na masuala ya sanaa na jamii. Laiti ningekuwa nimepata fursa zaidi ya kuongea naye hadi kuandika makala za kiwango cha juu kitaaluma, au hata kitabu  cha aina hiyo. Mama Shakila, sawa na wasanii wetu wengi, ametoa mchango mkubwa kwa jamii yetu na ulimwengu kwa ujumla. Lakini, jamii yetu ina tatizo la kutowaenzi watu hao ipasavyo. Kufanya utafiti na kuandika habari zao na tathmini ya mchango wao ingekuwa namna moja ya kuwaenzi, pia kuhakikisha kuwa wanapata kipato wanachostahili kutokana na kazi zao. Ingebidi wasomi wawe wanaandika makala na vitabu kuchambua kazi za wasanii hao; wanafunzi vyuoni wawe wanaandika tasnifu, na pawe na mijadala, makongamano, ya kuchambua mchango wa watu hao. Lakini jamii yetu, pamoja na kufaidika kutokana na juhudi za watu hao, ina jadi ya kutowajali kimaslahi, na kisha kuwasahau.

Tuesday, June 5, 2012

Mahojiano: Jacton Manyerere na wana-Uamsho (Zanzibar)

Mwandishi wa gazeti la JAMHURI, Manyerere Jackton (pichani katikati), amefanya mahojiano ya ana kwa ana na Amiri Mkuu wa Jumuiya ya Maimamu Zanzibar, Sheikh Farid Hadi Ahmed, aliyeeleza lengo kuu la Jumuiya hiyo ya Kiislamu.

JAMHURI: Ni nini chanzo cha vurugu za Mei 26?

Sheikh Farid: Kilichotokea hapa kwa muda mrefu, japo inasikika Jumuiya ya Uamsho ndiyo inayofanya mihadhara, lakini ni Umoja na Jumuiya za Kiislamu ambazo zimekuwa zinaendesha mihadhara. Tumefanya mihadhara zaidi ya mia moja hadi sasa - mikutano zaidi ya mia pamoja na makongamano tofauti. Na lengo zaidi hapo awali lilikuwa ni kuwaelimisha watu kujua Sheria ya Mabadiliko ya Katiba na kuona ni jinsi gani inawabana Wanzibari na haijawapa ile haki yao ya kuujadili Muungano. Na baada ya hapo kilichokuwa kinazungumzwa zaidi ni kuwaelimisha wananchi kujua haki yao, kujua mustakabali wa nchi yao na umuhimu wa kuuhoji Muungano au kuujua Muungano. Wazanzibari wao kama washirika na Watanganyika wana haki ya kuuhoji Muungano. Sasa hii mihadhara imeendelea kwa muda mrefu na ilikuwa inakwenda misafara ya mbali mingine hadi shamba. Na ilikuwa misafara mikubwa inaweza ikabeba magari mia mbili, mia mbili na zaidi, kuna mapikipiki, watu wanakwenda wanarudi kwa usalama wala hakuna tabu na matatizo yoyote. Hayo yote ndiyo kwa jumla yamefanyika. Sasa kilichojitokeza hivi karibuni ni kuwa lilifanyika kongamano. Katikati ya lile kongamano watu waliamua kutembea, kama ni matembezi tu lakini si maandamano hasa. Maandamano ni kitu ambacho kimeandaliwa, kina slogan yake, kina ujumbe, kinaenda maeneo maalumu kufikisha ujumbe maalumu. Haikuwa hivyo.

JAMHURI: Je, Polisi walivamia?

Sheikh Farid: Polisi hawakuvamia, hawakuwahi kuvamia. Na walipokuja kwa kweli walikuja matembezi yameanza kutoka maeneo ya Lumumba. Watu wote wameacha baiskeli zao, vifaa vyao palepale na walinzi walibaki eneo lile. Watu wametoka wametembea mpaka hapa Michenzani, katika roundabout, wameshuka chini mpaka maeneo ya Kariakoo. Kwa hiyo watu wakaenda moja kwa moja wakarudi kwenye kile kiwanja walichoanzia. Wakarudi palepale wakataa kitako. Wakawa wanaendelea na shughuli zao. Wakazungumza, wakazungumza mpaka wakamaliza. Walipomaliza kuzungumza wakatawanyika wakaenda majumbani mwao salama salmini. Nashangaa sasa alipokuja Waziri, Jeshi la Polisi wamemdanganya. Na alipokuja IGP wamemdanganya wamemwambia uongo. Wanamwambia kuwa Jeshi la Polisi limejaribu kuzima fujo, lakini si kweli. Ni uongo huo. CD zipo zinauzwa kila pahali. Wazi kabisa. Zinaonyesha maandamano kitu mbali, na zile fujo kitu mbali kabisa. Hayo matembezi kitu mbali na hizo fujo kitu mbali kabisa.

JAMHURI: Nini chanzo kilichosababisha fujo?

Sheikh Farid: Fujo ilisababishwa na Jeshi la Polisi kukosa utaratibu, kuchukua mazoea yale yale ya uhuni na mabavu. Ndicho kilichofanyika kwa sababu kati ya mmoja wa watu waliohudhuria pale kwenye viwanja palipokuwa na mdahalo ni Maalim Musa Juma, yeye ni mmoja katika wahadhiri wala si kiongozi wa Jumuiya ya Uamsho, lakini ni mwalimu ambaye anahadhiri, anafundisha. Sasa siku ile yeye alikuwa si mzungumzaji, alikuwa mkaribishaji wa wazungumzaji. Walichokifanya wakati wa majira ya saa moja na kidogo usiku, yumo msikitini mwake anasomesha, alikwenda mtu ana shida naye. Alipomwita, kutoka nje kuwafuata wale watu wakamkamata kwenye kiuno, na wengine watano wamekuja wamemzoa wamemshindilia kwenye gari wakampeleka kituo cha Polisi. Wale vijana waliokuwa pale - wanafunzi na watu ambao wanampenda, na sasa kimekuwa kitu sensitive kwa sheikh kumdharau. Sasa hii dharau iliyofanyika, wananchi hawakukubali kwa hiyo wakaanza kupigiana simu wote kwamba Sheikh wetu kakamatwa, twendeni tukamdai kwanini kakamatwa, na tujue. Kama kumchukulia dhamana tumchukulie.

JAMHURI: Lipi jina sahihi la Jumuiya hii? Ni Uamsho au Muamsho?

Sheikh Farid: Hizi harakati zinazoendelea hapa nchini (Zanzibar) zinafanywa na Umoja wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu. Ndiyo wanaofanya hizi harakati zote. Isipokuwa katika utaratibu wa mambo ya mihadhara, Jumuiya pekee ina uzoefu mkubwa kwenye mihadhara ni Jumuiya ya Uamsho.

JAMHURI: Taasisi ya kidini kwanini ijikite kwenye siasa?

Sheikh Farid: Hakuna tatizo lolote. Hakuna tatizo kikatiba, hakuna tatizo kidini yetu, hakuna tatizo kimtazamo sahihi wa wanasiasa. Kote hakuna tatizo. Mtazamo sahihi wa wanasiasa. Tumchukue Rais wetu wa hapa Zanzibar, Mheshimiwa Jumbe ameandika kitabu na kuna sura maalumu anaita “Dini na Siasa”. Kaeleza mengi. Kaeleza jinsi watu wengine walivyo katika dini zao, lakini akaelezea ama upande wa Uislamu huwezi kutenganisha dini na siasa. Hilo moja. Basi kama watu wanajua wanasiasa, huyu mwanasiasa anatamka kwenye kinywa chake. Alikuwa Rais wa Zanzibar, Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Makamu wa Kwanza wa Rais wa Tanzania. Alikuwa pia Makamu wa Mwenyekiti wa CCM na kaeleza wazi kabisa kwenye Uislamu huwezi kutenganisha na siasa. Ukija kwenye Koran, Uislamu unahesabu kuwa dini ni mfumo kamili wa maisha ya mwanadamu, ikiwamo sehemu ndogo inayoitwa “siasa”. Siasa kwenye Uislamu au kwenye lugha ya Kiarabu, neno hilo hilo siasa kama lilivyo, maana yake ni “uongozi”, kwa hiyo uongozi ni sehemu ndogo, ni mlango katika maisha ya mwanadamu au katika dini ya Kiislamu. Kwa hiyo sisi kuzungumza siasa ni sahihi kabisa.

JAMHURI: Nyuma ya Uamsho kuna msukumo wa kisiasa?

Sheikh Farid: Uamsho haina uhusiano na CUF. Hili suala limeanza ilipokuja hii rasimu ya Katiba, ilipokuja kama rasimu, Serikali nzima iliikataa, Wazanzibari waliikataa wakaona wamedharauliwa. Iliporudi ikaja na dharau nyingine, badala ya kuletwa kama rasimu ikaletwa kuwa ni sheria sasa…kinguvu. Unaposema sheria maana yake ni nguvu, utake usitake. Ikaletwa kama sheria na ilikuwa iletwe kama rasimu. Hilo tatizo la mwanzo. Tatizo la pili, ndani ya rasimu ile kama alivyosema Mheshimiwa Kikwete mwenyewe wakati anazindua Tume, hakuna mjadala wa Muungano mle ndani yake, ni kwenda mbele tu kuuboresha, lakini suala la kutazama mustakabali wa Zanzibar je, inafaidika na Muungano? Hilo hakuna. Imeshapita miaka 48 na hawajawahi kuulizwa huko nyuma. Sasa sisi hapa ndipo tulipoona kuna haja ya kuulizwa, na njia ya kufanya hivyo ni kupitia kura ya maoni.

JAMHURI: Kuna umuhimu wa kuwapo Muungano wa Tanganyika na Zanzibar?

Sheikh Farid: Sisi tunachotaka ni kura ya maoni. Wazanzibari waseme wenyewe. Hakuna mtu amepewa kibali cha kumsemea mtu. Hakuna Mtanganyika wala Mzanzibari. Kila mtu aseme mwenyewe na hiyo ndiyo demokrasia, kwa hiyo sisi kama Jumuiya ya Taasisi za Kiislamu tunasema iitwe kura ya maoni. Nisiseme mie, mie nitasema kwenye karatasi. Kila Mzanzibari atasema kwenye karatasi. Kura ya maoni ni nyepesi tu.

JAMHURI: Mbona hamjasikika mkilaani kuchomwa makanisa? Mnaunga mkono kitendo hicho?

Sheikh Farid: Tumeshatoa taarifa nyingi sana. Tatizo unajua hakuna uadilifu kwenye uandishi wa habari. Hakuna uadilifu hata kwenye hii TV yetu iliyopo hapa (ZBC), hata redio zilizoko hapa hakuna uadilifu bwana. Hii ni kwa mtu anachukia kitu anakuwa si mwadilifu. Na haya ndiyo yanayosababisha matatizo kama haya kuzuka. Mtu unamnyima haki yake anafika mahali hawezi kustahamili. Kwa hiyo sisi kiufupi tunalaani vibaya sana suala zima la kuchoma makanisa, dini haisemi hivyo. Si dini yetu wala si nyingineyo, haisemi hivyo. Lakini tunashangazwa vilevile, tumechoma makanisa, sisi ameuliwa imam ndani ya msikiti na Jeshi la Polisi…ameuliwa imam ndani ya msikiti, huko Mwembechai kwenu huko Dar es Salaam ameuliwa Muislamu ndani ya msikiti. Acha kuchoma makanisa. Sisi tunalaani uvunjifu wa amani wa aina yoyote - ikiwa wa ubaguzi wa kidini wa kuchoma makanisa, ikiwa wa kuwahujumu watu, tukubali haya si mafunzo maana hata kwenye nyumba yangu wamekuja wamehujumu ndani, wamepiga mabomu ndani ya nyumba, wamevunja mlango.

JAMHURI: Mambo gani ambayo Zanzibar haitendewi haki ndani ya Muungano?

Sheikh Farid: Ni mamlaka kamili ya kimaamuzi ya kimataifa, ya ndani na nje ya nchi. Hiki ndicho tunachokosa Zanzibar. Wanaita Sovereignty, Zanzibar inakosa sovereign yake kwa hiyo tunataka sovereign state. Kama ni Zanzibar iheshimike, kama ni Rais wa Zanzibar aheshimike, Serikali ya Zanzibar iheshimike ndani na nje ya nchi. Iwe na mamlaka kamili. Na wao wenyewe (Wazanzibari) wataona utaratibu nini watafanya. Kwa hiyo wananchi waulizwe, chepesi tu hakina tabu. Si waliulizwa kwenye Serikali ya Umoja wa Kitaifa na hakupigwa mtu?

JAMHURI: Marekani majimbo yale ni nchi - ni Muungano, mbona majimbo hayana mamlaka kamili kama nchi?

Sheikh Farid: Mbona upo muungano tofauti na huo. Kama Umoja wa Ulaya si upo? Upo vipi? Katika Umoja wa Mataifa si kila nchi ina kiti?

JAMHURI: Huo si muungano ni kama jumuiya tu.

Sheikh Farid: Huo ni muungano, si wameungana katika vitu maalumu? Wamarekani wameamua wao vile. Sisi tumeamua hivi. Wao hatuwasemei. Sie tunaamua tunachotaka sie. Na sisi hawezi kutulazimisha mtu tuamue kwa akili za Kimarekani. Wamarekani wataamua wao wenyewe Kimarekani, haki za Kizanzibari zitaamuliwa Kizanzibari-Zanzibari.

JAMHURI: Ungependa Muungano wa uwe wa namna gani?

Sheikh Farid: Mie ninachosema ule mchakato wa Katiba imekuwa sawa na kumchukua ng’ombe na gari ya ng’ombe halafu ng’ombe ukamweka nyuma gari ya ng’ombe ukaweka mbele. Au mashine ukaweka nyuma, gari ukaweka mbele. Sijui itakwenda vipi. Sasa tunashangaa, watu wataalamu wana akili lakini inaonyesha akili zao zimefika mahali wanatuona sisi wapumbavu. Sisi bwana tunasema ilivyo kitu kinachowafungamanisha Wazanzibari na Watanganyika ni Muungano. Ninyi mnataka kujadili Katiba ya Muungano, hili tatizo la Muungano kwanini msilizungumze mwanzo? Hili la kuzungumza mwanzo. Kwanza, lizungumzwe hili kwanza mpaka likae sawasawa halafu ndiyo tuzungumze Katiba. Sasa unasema mimi na wewe tunataka kufanya biashara njoo tufunge mkataba mimi na wewe. Si tuzungumze tukubaliane kwanza halafu ndiyo tuandike mkataba kwa sababu Katiba ndiyo umefunga kila kitu. Kitu kinachotufungamanisha tukizungumze mwanzo. Wananchi wapewe fursa wazungumze mwanzo. Watu wanapewa fursa hizo wasiokuwa na nchi mwanzo…hii ni nchi. Hii ni nchi. Ilikuwa ni nchi tena kubwa mpaka Dar es Salaam yote ilikuwa yetu ile, tena mikataba ipo ya kimataifa ya kuonyesha Dar es Salaam yote ile ni yetu sisi. Na kuingia ndani huko maili 10.

JAMHURI: Je, mtaidai Dar es Salaam?

Sheikh Farid: Hatuna shida nayo hiyo. Tutakuachieni. Sisi watu makarimu sana sie. Tutawaachieni. Nashangaa nyie tu hizi kilomita za mraba ngapi zinakushughulisheni nyie wakati mna mapori tele kule juu, na mna ardhi ya kwenda na kurudi, mashamba ya kwenda na kurudi mnang’ang’ania hiki tu!

JAMHURI: Muungano ukivunjika, nini hatima ya Wazanzibari wanaoishi/waliowekeza Bara?

Sheikh Farid: Jawabu moja, wewe huwajui Watanzania wanaofanya biashara Kenya? Uganda? Hatima yao ipo vipi? Sasa ninyi inaonyesha kuna watu wana fikra mbovu katika vichwa wanaona maana yake tukiwa hivi (tukitengana) tutakuwa maadui, hata! Udugu lazima utabakia. Tumeoa kule. Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar usingizi wake (mkewe) ni wa kule (Bara) au hujui wewe? Hatuwezi kuachana bwana, watu watabakia, mapenzi yapo, undugu upo, ujirani mwema kabisa, waliokuwapo hapa Watanganyika watabakia, Wakristo hapa watabakia, itakuwa kila kitu kina utaratibu. Si maana yake kwamba mmetengana muwadhulumu wale ndugu zenu (walio Bara). Mkiwadhulumu sawa! Sisi kawaida yetu hatuko hivyo.

Chanzo: Mjengwa Blog.

Monday, June 4, 2012

Kanisa Lilivyoungua Zanzibar

Kati ya uharibifu uliofanyika Zanzibar wakati wa vurugu za hivi karibuni makanisa yalichomwa moto. Hapa kushoto ni picha ya kanisa likiungua. Nimeipata hapa. Kutokana na kauli mbali mbali mtandaoni, ni wazi kuwa wako watu ambao wamefurahishwa na uchomaji moto wa haya makanisa, pamoja na vitabu vilivyokuwemo humo, kuanzia vya sala hadi Biblia. Wako ambao wanasema kuwa Zanzibar ni nchi ya ki-Islam na u-Kristo hautakiwi kule. Kwa maana hiyo, kuchoma moto makanisa ni kuwakomoa wa-Kristo.

Maajabu ya dunia hayaishii hapa, kwani wako pia watu ambao wanauchukia u-Islam na wanataka kuwakomoa wa-Islam. Wangeikaribisha fursa ya kuichoma moto misikiti. Miezi kadhaa iliyopita, tulipata taarifa za kikundi cha wa-Marekani waliotangaza kuwa watachoma moto Quran. Kabla ya hapo, tulisikia kwamba kule kwenye jela ya Guantanamo, kulikuwa na kitendo cha kuikojolea Quran. Bila shaka, lengo ni kuwakomoa wa-Islam.

Wenzetu ndio hao. Kweli, dunia ina mambo.


Saturday, June 2, 2012

Watafiti wa ki-Tanzania Tumekutana Ughaibuni

Kila siku ni ya pekee, lakini kuna siku ambazo ni za pekee zaidi. Leo nilienda Luther Seminary, St. Paul, kuonana na wachungaji wawili, ambao ni Rev. Dr. Falres Ilomo (aliye katikati pichani) na Rev. Dr. Andrea Mwalilino (hapo kulia). Mchungaji Mwalilino, ambaye tumefahamiana kwa miaka kadhaa, alikuwa ameniarifu kuwa kuna huyu mgeni kutoka Tanzania, ambaye yuko kwa kipindi tu hapa Luther Seminary. Tulitafuta fursa ya kuonana, na leo imewezekana.


Mchungaji Mwalilino, ambaye alihitimu shahada ya uzamifu Luther Seminary, tuko wote hapa Minnesota, ingawa miji mbali mbali. Mgeni wetu, ambaye alihitimu shahada ya uzamifu katika Chuo Kikuu cha Augustana, Ujerumani, ni mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Tumaini, Iringa. Mimi mwenye blogu hii nilihitimu shahada ya uzamifu katika Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison. Mjadala wetu ulikuwa wa kiwango cha juu kitaaluma. Tumeongelea utafiti katika tamaduni na dini za jadi za wa-Afrika, lengo moja muhimu likiwa ni kutafakari namna ya kuziweka dhana na falsafa za jadi za ki-Afrika kwenye uwanja wa mijadala na uchambuzi katika dunia ya leo, tukizingatia kuwa wa-Afrika wa tangu zamani wana mchango ambao unastahili kutambuliwa na kutumiwa.

Katika utafiti huo, tuna wajibu wa kuangalia lugha, kwani lugha ndio chombo kinachobeba na kuwakilisha dhana mbali. Utafiti wa lugha utatuwezesha kujua sio tu dhana za ndani katika falsafa za wa-Afrika, bali pia namna ya kuwasilisha kwa wa-Afrika mafundisho ya dini yetu ya u-Kristo ambayo yalikuja kwetu kutoka kwenye lugha za kigeni. Suala hilo si kwa u-Kristo tu, bali pia kwa u-Islam. Tumebaini kwamba kutokana na tofauti za lugha, dhana nyingi katika dini hizo hazijaelezwa au kueleweka ipasavyo. Tutawezaje kuziwasilisha kwa wa-Afrika, dhana za hizo dini, ambazo huko zilikotoka zilikuwa katika lugha ambazo sio zetu? Hili ndilo suala, na inabidi tuzame katika kulitafakari. Tafakari hii ni lazima ifanyike na iwe endelevu. Mada hii tumeiongelea na kuichambua kwa karibu saa mbili tulizokuwa pamoja, na sote tunakiri tumefanya kazi nzito, ya kufikirisha. Tumekubaliana kuendeleza tafakari na mawasiliano siku za usoni.

Friday, June 1, 2012

Tamko la Maaskofu Kuhusu Machafuko na Hali ya Vitisho Zanzibar

Sisi Maaskofu, Mapadre, Wachungaji na Waumini tunaoishi Zanzibar,
tumekutana leo tarehe 30 Mei 2012 kufutia hali ya machafuko, uvunjifu
wa amani, uchomaji wa Makanisa, uharibifu wa mali za Kanisa na vitisho
dhidi ya Wakristo na mali zao.

Tumekutana na tunatoa tamko baada ya muda mrefu wa kimya na uvumilivu
tuliosafiri nao kwa takribani miaka 11, kwa kumbukumbu zetu tangu
mwaka 2001. Tunajua na tunauambia umma wa wapenda amani kuwa matukio
ya tarehe 26 hadi 28 Mei 2012 ni matokeo ya mahubiri na mihadhara
ambayo imekuwa ikiendeshwa iliyolenga kwa makusudi kuutukana na
kuukashifu Ukristo hapa visiwani Zanzibar na hivi kupandikiza hofu
miongoni mwa waumini wa dini ya Kikristo. Tunashawishika kusema kuwa
ufadhili na ushawishi wa vurugu na vitisho hivi vina udhamini wa ndani
au nje ya nchi yetu.

Tumefikia hatua hiyo baada ya matukio mbalimbali yaliyokuwa yanafanywa
dhidi ya Kanisa na mali zake tangu mwaka 2001 hadi hivi majuzi
yalikuwa yakitolewa taarifa kwenye vyombo vya Ulinzi na Usalama hapa
visiwani Zanzibar lakini ushirikiano umekuwa mdogo na kwa sehemu kubwa
dhaifu sana. Kwa maelezo na vielelezo ni kwamba, jumla ya makanisa
yasiyopungua 25 yamevunjwa na kuchomwa moto tangu mwaka 2001, pamoja
na ahadi za Serikali na vyombo vya ulinzi na usalama katika maeneo
yote yaliyopata kutolewa taarifa hakuna hata moja lililothibitika
wahusika kukamatwa, kufikishwa mahakamani na kuchukuliwa hatua za
kisheria.

Kumekuwa pia na vitendo vya kuchoma magari huko Pemba na hapa Unguja,
na Serikali kwa upande wake imeshiriki hata kupora ardhi na majengo ya
Kanisa hapa Unguja na huko Pemba.

Tumebaini pia hasa baada ya matukio ya vurugu za tarehe 26 hadi 28 Mei
2012 kuwa kuna mikakati ya makusudi ya kuwafanyia Wakristo vurugu.

Mikakati hiyo inajumuisha mambo kama vile kuchoma Makanisa zaidi,
kuharibu mali za Makanisa yakiwemo mashule, vituo mbalimbali vya
Kanisa vinavyotoa huduma za kijamii hapa Visiwani.

Mkakati au mpango huo umepangwa na unakusudiwa kutekelezwa kati ya
tarehe 1 na 2 Juni, na tarehe 8 na 9 Juni mwaka huu. Tunazo taarifa
tunazoweza kuzithibitisha kuwa baadhi ya Wakristo wamekuwa wakitumiwa
jumbe za simu za mkononi (SMS) zikiwatisha na kuwataka waondoke
visiwani humu mara moja hata kama ni wazawa.

Sehemu ya pili ya mkakati ni kuwasaka Wakristo nyumba kwa nyumba kwa
ajili ya kuwaangamiza, kuwabaka na kuwalawiti.

Chakusikitisha zaidi ni pale ambapo baadhi ya walinzi wa Usalama wa
raia hasa Polisi wenye asili ya hapa Visiwani Zanzibar kusikika
wakisema kuwa wataunga mkono vurugu kila zitakapotokea.

Kufuatia maelezo hayo yote, Sisi Maaskofu, Wachungaji, Mapadre na
waumini tuliokutana leo, tunapenda kwanza kutoa neno la shukrani kwa
uongozi wa Serikali kwa ushirikiano iliyotuonyesha kufutia matukio ya
hivi majuzi, na hasa kwa kupewa fursa za kukutana na viongozi na
kusikilizwa.

Tunatamka kuuelezea umma wa wapenda Amani wote tukisema, tumechoswa
kuishi na kuchukuliwa kama raia wa daraja la pili katika nchi yetu.

Tunaonya kuwa hatuko tayari tena kuvumilia vitendo vya uvunjaji wa
amani na haki zetu na tabia za kufanywa tuishi kwa hofu.

Kadhalika tunaiomba seriakli yetu ituhakikishie usalama wa maisha
yetu, mali zetu pamoja na majengo yetu ya ibada.

Wito wetu kwa viongozi wa dini mbalimbali hapa nchini ni kuwa, kila
mmoja anawajibu mkubwa wa kuhakikisha kwamba nchi yetu inatawaliwa kwa
mujibu wa sheria za nchi na kwmba kila mmoja ahubiri kwa lengo la
kukuza amani, utulivu na usalama wa kila mtu na mali zake.

Mwisho, tunapenda kuhitimisha tamko letu kwa kuwaalika wakristo wote
kuiombea nchi yetu amani, utulivu na mshikamano ambazo ni tunu
tulizoachiwa na waasisi wetu.

Ni imani yetu pia kwamba viongozi wetu wataendeleza wajibu wao na
mamlaka waliyopewa na Mungu pasipo upendeleo wa aina yoyote.

Mungu Ibariki Tanzania, Mungu Ibariki Zanzibar.

Kwa niaba ya Wakristo wote;

Ni sisi Maaskofu wenu

1. Michael Hafidh
Askofu wa Kanisa Anglikana Zanzibar

2. Augustine Shao
Askofu wa Jimbo Katoliki Zanzibar

3. Pastor Timothy W. Philemon
Makamu Mwenyekiti wa Ushirika wa Wachungaji wa Makanisa ya Pentekoste
Zanzibar

SOURCE: Kiongozi [Toleo Na: 22 Juni 01-07,2012 (uk 2)].

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...