Wednesday, December 30, 2009

CHANGAMOTO: Insha za Jamii

Leo nimechapisha kitabu kipya. Kinaitwa CHANGAMOTO: Insha za Jamii. Ni mkusanyiko wa makala mbali mbali nilizoandika mwaka 2009, juu ya masuala ya uchumi, siasa, jamii, na utamaduni yanayoihusu Tanzania na dunia kwa ujumla.

Hiki ni kitabu changu cha kwanza katika lugha ya ki-Swahili. Naamini kuwa uzoefu niliopata utanisaidia siku zijazo.

Kwa kuanzia, kitabu hiki kinapatikana mtandaoni, pamoja na vitabu vyangu vingine. Bofya hapa.

Wednesday, December 23, 2009

KWA KINA NA PROF. JOSEPH MBELE

Ili kuwapa mwanga zaidi wasomaji wa blogu hii kuhusu fikra zangu, naleta tena mahojiano ambayo niliwahi kufanyiwa na blogu maarufu ya Bongo Celebrity. Bofya hapa.

Sunday, December 20, 2009

Bia za Kuzindulia Kitabu

Miaka michache iliyopita, nilichapisha kijitabu kuhusu Things Fall Apart. Nilimtumia ujumbe rafiki yangu aliyekuwa anaishi Dar es Salaam, kuhusu kuwepo kwa kijitabu hicho, naye akaniandikia hima. Nanukuu sehemu ya ujumbe wake:

Kuhusu habari ya kitabu nitajitahidi ili niweze kujulisha watu ila, naomba kitu kimoja ukija Tanzania tutafanya kitu kinachoitwa uzinduzi maana yake tutaalika waandishi wa habari jambo ambalo ni rahisi sana hapa kwetu ili mradi kinywaji kipatikane na tunaweza kualika kundi moja la mziki basi.

Aliendelea kufafanua mkakati huo, ikiwa ni pamoja na kuwaalika wageni muhimu, kama vile waziri wa elimu au naibu wake.

Wazo ambalo lilinata kichwani mwangu zaidi ni hili la kuandaa kinywaji. Kwa maneno mengine, nilitegemewa kununua bia nyingi. Bado sijafanya huu uzinduzi wa kufa mtu, nikinukuu usemi wa mitaani. Badala yake, najiuliza nchi yetu inakwenda wapi.

Wazo la bia za kuzindulia vitabu linaelezea vizuri hali halisi ya jamii ya Tanzania. Tumefikia mahali ambapo bia ndio njia ya kuwavutia watu kwenye shughuli mbali mbali. Nimewahi kuhudhuria maonesho ya kimataifa ya biashara Dar es Salaam. Nimejionea jinsi bia zinavyofurika kwenye viwanja vya maonesho, mwaka hadi mwaka. Inakuwa kama vile baa za Dar es Salaam zinahamia kwenye viwanja hivyo.

Nimehudhuria pia tamashala la Taifa la vitabu Dar es Salaam. Kama nilivyosema tena na tena katika blogu hii, mahudhurio kwenye tamasha hilo huwa ni duni sana, isipokuwa watoto wa shule na walimu. Sitashangaa iwapo tutaanza utaratibu wa kusogeza bia kwenye tamasha la vitabu ili kuwavutia watu. Bila shaka tutafikia mahali ambapo zitahitajika bia kuwavutia watu waende vyuoni.

Wednesday, December 2, 2009

Darasa Chini ya Mti

Makala hii, inayotokana na picha inayoonekana hapa chini, ilichapishwa katika gazeti la KWANZA JAMII. Ni makala ya pili. Kusoma makala ya kwanza, bofya hapa.


Darasa Chini ya Mti

Na Profesa Joseph L. Mbele

Nimeona picha kwenye blogu kadhaa ambayo inamwonyesha mwalimu na watoto wa darasa la kwanza, chini ya mbuyu. Ubao wa kuandikia umepigiliwa kwenye mbuyu. Kama inavyotegemewa, Watanzania wanalalamikia hali hiyo. Wanauliza kwa nini watoto wasome katika mazingira ya aina hii. Wengine, kama kawaida, wanaishutumu serikali.

Napenda kuliangalia zaidi suala la darasa kufanyika chini ya mti. Je, ni balaa kama tunavyodai au kunaweza kukawa na mtazamo mwingine?

Kuna vijiji na jumuia nyingi nchini mwetu ambazo hazina shule. Sababu moja ni kuwa idadi ya watu katika nchi yetu inaongezeka muda wote. Vijiji vinaenea sehemu za mbali ambazo zamani zilikuwa mapori au mashamba. Watoto wanatembea mwendo mrefu kwenda shuleni. Na kadiri watu wanavyoendelea kujenga mbali na shule, mwendo wa kutembea hadi shuleni unaongezeka.

Sasa je, ni bora watoto hao waendelee kwenda mwendo mrefu kila siku hadi kwenye shule au ni bora wapate fursa ya kusoma chini ya mti, hapo kijijini pao? Je, wangoje hadi wajengewe shule ya matofali iliyoezekwa bati, au ni bora wapewe fursa ya kuanza masomo chini ya mbuyu hapa hapa kijijini?

Katika vijiji vingi Tanzania, vikiwemo hivi vinavyoendelea kujitokeza, watu wana dhiki kifedha. Wanaishi kwenye nyumba za makuti na hawana kipato cha uhakika. Hawana uwezo kifedha lakini wanataka watoto wao waanze angalau kujifunza kusoma na kuandika. Wanafurahi kumpata mwalimu na wako tayari kuanzisha darasa chini ya mti. Kwa mtazamo wangu, watu hao wakifanikiwa kumpata mwalimu akaanzisha shule chini ya mti, ni hatua moja mbele.

Tuliangalie suala hili kwa mtazamo wa wanakijiji. Bila shaka walikaa, wakatathmini hali ya kijiji chao na mahitaji ya watoto wao, wakaamua kuanzisha shule. Walimtafuta mwalimu, wakatafuta huo ubao, na pia wakasogeza mbao za kukalia watoto. Walipitisha uamuzi kila mzazi atafute sare ya shule. Kwa kipato cha watu wa hapo, huenda huu mradi wa sare ulikuwa mgumu sana. Lakini wamejitahidi, na kila mtoto ana sare.

Hapo ubaoni zinaonekana hesabu za kujumlisha. Haya ni maendeleo kwa hao watoto na kwa hicho kijiji. Si sahihi kupuuzia ukweli huu. Tuwape wanakijiji wa hapo heshima wanayostahili, kwa juhudi waliyofanya hadi sasa. Sisemi turidhike na hali. Nasema kuwa wanakijiji hao wamepiga hatua inayostahili kutambuliwa.

Katika elimu, jambo la msingi si jengo. Wakristu tunafahamu kuwa Yesu alifundisha watu popote, na mafanikio yake hayakuathirika kwa sababu ya kukosa jengo. Watu wengi maarufu katika nchi yetu walianza shule chini ya mti. Marehemu Oscar Kambona, kwa mfano, alisoma shule ya msingi chini ya mwembe kijijini kwake Kwambe, karibu na Mbamba Bay. Mwembe huo bado uko.

Mwalimu Nyerere alipohamasisha kisomo cha watu wazima na kisomo chenye manufaa hakusema kuwa lazima pawe na majengo. Wengi walisoma chini ya mwembe au mkorosho.

Mambo mengi muhimu, kama vile mazungumzo na mijadala, yanaweza kufanyika chini ya mti. Mwalimu Nyerere alipoongelea demokrasia ya enzi za wahenga wetu, alisema kuwa wazee walikuwa wanakaa chini ya mti na kujadiliana hadi wakubaliane. Hakusema kuwa walikaa katika jumba la mikutano, nasi hatujawahi kulaumu kwa nini walikaa chini ya mti. Iweje suala la darasa kuwa chini ya mti litukera namna hii?

Katika kufundisha kwangu Marekani, nimeona kuwa nyakati ambapo jua linawaka vizuri, wanafunzi wanaomba tukafanyie darasa nje, chini ya mti. Ingawa mwanzoni, kutokana na mazoea, sikuwa napenda kuondoka darasani, hatimaye nilizoea. Siku inapokuwa nzuri, ni kawaida kuona madarasa yakifanyika chini ya miti. Ingawa Wamarekani hawafanyi darasa chini ya mti sababu ya kukosa majengo, hoja yangu ni kuwa kufanyia darasa chini ya mti haimaanishi kuwa elimu inadunishwa. Kuna mambo kadha wa kadha ya kuangalia kabla ya kutoa hukumu kama tunayotoa tunapoona watoto wakisoma chini ya mti.

Watanzania tunapoongelea elimu tuwe tunatofautisha kati ya mambo ya msingi na yasiyo ya msingi. Tukiona watoto wanasoma chini ya mti, tusitoe hukumu za upesi bila tafakari. Jambo la msingi ni somo au elimu, sio kuwepo au kutokuwepo kwa jengo. Jengo linaweza kuchangia ubora wa elimu katika mazingira fulani, lakini sio kila penye jengo bora pana elimu bora.

Tabia hii ya kutoangalia mambo ya msingi inajitokeza kwa namna nyingine pia katika nchi yetu. Watanzania wengi wanaamini kuwa watoto wakifundishwa kwa kiIngereza, elimu inakuwa bora. Wengi wanaamini kuwa watoto wakiweza kuongea kiIngereza wanakuwa wameelimika vizuri. Ndio maana kuna utitiri wa shule zinazotumia kiIngereza.

Siku hizi umezuka mtindo wa watoto kuvaa majoho na vikofia maalum wakati wanapohitimu shule. Majoho na vikofia vinachukuliwa kama dalili ya shule bora au elimu bora. Ukweli ni kuwa elimu si majoho wala vikofia. Watoto wanaweza kuwa wameelimika vizuri hata kama wanavaa kaptula na shati siku ya kuhitimu. Vivyo hivyo, kusoma chini ya mti si hoja. Cha msingi ni masomo yenyewe.

Ninaposema hayo yote simaanishi kuwa majengo hayana umuhimu. Lakini si vizuri kusema kuwa kila jamii ingoje hadi ijenge majengo mazuri ndipo watoto waanze kufundishwa na mwalimu. Ni bora mwalimu aanze darasa chini ya mti. Kama watoto wana daftari na kalamu, na mwalimu wao ana ubao na chaki, inatosha, kwa kuanzia.
Kadiri kijiji kinavyopata nguvu, kinaweza kujikongoja na shughuli ya majengo na mahitaji mengine.

Friday, November 27, 2009

Elimu ya Kijijini

Makala hii ilichapishwa katika gazeti la KWANZA JAMII

Profesa Joseph L. Mbele

Mara kwa mara nakumbuka elimu niliyopata kijijini, kabla ya kuanza shule. Wengi wetu tulipitia njia hiyo. Ni elimu gani hiyo? Tangu utotoni, tulipata maelekezo kutoka kwa wazazi kuhusu mambo mbali mbali, kufuatana na umri, kuanzia namna ya kuvaa hadi namna ya kula kwa adabu na kuwasalimia watu.

Baadaye wavulana tulijifunza kuchunga mbuzi na ng’ombe, na kutandika nyasi kwenye zizi la ng’ommbe, na kukamua maziwa. Wasichana walifundishwa kazi za jikoni na kulea watoto.

Kama ilivyo kwa watoto wengine, baba na mama walikuwa wananituma kufanya shughuli hii au ile. Hata majirani walikuwa wanatutuma sisi watoto kuwasaidia shughuli mbali mbali. Yote hii ilikuwa ni sehemu ya elimu yetu.

Nilipokua kidogo nilianza kushiriki katika kilimo. Nilijifunza kulima, kupanda, kupalilia, na kuvuna mazao. Nilijifunza kuchuma kahawa na kuishughulikia baada ya hapo. Shughuli hizi ziliniwezesha kufahamu zaidi habari za udongo, nyasi, na magugu. Niliwafahamu wadudu wanaoishi mashambani, kama ni wadudu salama kwa mimea au ni adui wa mimea. Nilizijua tabia za wadudu mbali mbali, kuanzia siafu hadi sisimizi na mchwa. Nilijua kama wanauma au hawaumi. Tulijifunza namna ya kuwanasa kumbikumbi, ambao walikuwa ni chakula.

Katika kuchunga mbuzi na ng’ombe tulipata fursa ya kujifunza mambo mengi, sio tu kuhusu tabia za hao wanyama, bali pia elimu ya mimea na nyasi, zikiwemo nyasi ambazo ni chakula cha mbuzi au ngombe na kadhalika. Huko porini tulijifunza pia aina mbali mbali za mboga za porini, matunda, uyoga, na kadhalika. Tuliweza kutofautisha uyoga ambao unalika na binadamu na ule ambao ni sumu.

Katika kukua kwetu kijijini, tulisikiliza hadithi na nyimbo, tukaweza kusimulia hadithi hizi na kuimba nyimbo. Hadithi hizi zilisheheni falsafa, maarifa, na maadili. Tulishiriki katika ngoma, tukaweza kupiga ngoma na ala zingine za muziki, kucheza na kuimba. Mbali ya kwamba hii ilikuwa ni burudani, ilikuwa pia elimu ya sanaa. Ilikuwa ni elimu kuhusu namna ya kushirikiana na wengine, kwani ngoma inahitaji nidhamu na ushirikiano.

Kwa kuwa nilisoma shule ya msingi nikiwa bado naishi kijijijini, niliendelea kuipata elimu ya kijijini hata baada ya kuanza shule. Baada ya masomo shuleni, niliporudi nyumbani, niliendelea na shughuli ya kuchunga mbuzi na ng’ombe, na kusaidia shughuli mbali mbali za nyumbani ambazo ziliendelea kuimarisha elimu yangu ya kijijini.

Baada ya kumaliza darasa la nne, mambo yalibadilika sana. Nilikwenda shule ya bweni, mbali kabisa na nyumbani kwangu. Elimu niliyoipata kule ilikuwa ya vitabuni zaidi. Ingawa tulifanya pia shughuli za nje, kama vile shambani na bustanini, muda mwingi zaidi tulitumia katika kujifunza yaliyomo vitabuni. Elimu ya vitabuni ilishamiri kichwani mwangu nilivyozidi kuendelea na madarasa, hadi chuo kikuu Dar es Salaam, na hatimaye Marekani.

Kadiri nilivyoendelea na elimu ya shuleni, nilizidi kusahau elimu ya kijijini. Kusoma sana kuliendana na kufifia kwa elimu niliyoipata kijijini. Leo hii, sikumbuki majina ya mimea mingi, wala ya aina nyingi za majani niliyojifunza kijijini. Nimesahau majina na tabia za wadudu, wanyama, na ndege mbali mbali. Sina tena ufahamu mzuri wa miti na majani ambayo ni dawa, miti ambayo ni bora kwa kuni na ile ambayo si bora, kwa vile labda haishiki moto haraka au inatoa moshi mwingi. Hii ni hasara kubwa.

Elimu ya kijijini ni elimu thabiti. Ni elimu ambayo imekusanya ujuzi na maarifa kutoka enzi za zamani. Vizazi kwa vizazi vimechuja na kuhifadhi yale yaliyo muhimu tu. Kila kinachofundishwa kina maana katika maisha. Ndio elimu ya kijijini.

Hapakuwa na vitabu wala maktaba. Kila kitu kilihifadhiwa akilini na kurithishwa kutoka kizazi hadi kizazi kwa maneno ya mdomo na kwa vitendo. Elimu ya kijijini haikuwa inakaa maktabani, bali watu walitembea nayo vichwani. Kutokana na ulazima wa kuhifadhi kila kitu katika akili ya binadamu, hapakuwa na nafasi kubwa ya kuhifadhi lolote ambalo halikuwa na maana au umuhimu. Hii ni tofauti na leo, ambapo tunatumia zaidi vitabu. Tunao uwezo wa kuhifadhi vitabu kiasi chochote, hata kama havina maana.

Hakuna ubishi kuwa vitabu vingi ni muhimu, kwani vinabeba elimu ya aina aina. Lakini, kuna pia vitabu ambavyo havina uhusiano na maisha ya wale wanaosoma. Katika shule, kuanzia enzi za ukoloni hadi leo, tunawafundisha vijana mambo mengine ambayo hayana mantiki wala umuhimu katika hali na mahitaji ya jamii zetu. Wakoloni walianzisha mtindo wa kufundisha mambo ya kwao bila kuzingatia umuhimu au uhalali wake katika mazingira ya kwetu. Walizipotosha akili za vijana, na kwa bahati mbaya upotoshaji wa aina mbali mbali bado unaendelea, kama walivyoelezea watalaam kama Franz Fanon na Mwalimu Nyerere. Hii ni tofauti na elimu ya kijijini, ambayo ilienda sambamba na maisha na mahitaji ya wahusika.

Kwa vile elimu ya shuleni inadhihirishwa kwa vyeti, wako ambao wanatafuta njia za mkato, zisizo halali, kupata hivyo vyeti. Wengine wanaiba mitihani. Huu ni udhaifu wa mfumo wa elimu ya shule. Elimu ya kijijini haikuwa na mwanya wa namna hiyo. Hapakuwa na njia za mkato. Hapakuwa na mitihani ya kuiba. Kama ilikuwa ni kwenda kwenye unyago na jando, kila mhusika alitimiza yaliyohitajika.

Tujiulize suali moja: Je, kuna sababu yoyote ya kuendelea kuisahau au kuififisha elimu ya kijijini kwa vile tu mtu anaendelea na elimu ya shuleni? Je, haingekuwa bora kuiingiza elimu ya kijijini mashuleni ili kuhifadhi na kudumisha hazina hii ya urithi wetu?

Tuesday, November 24, 2009

Utamaduni na Utandawazi

Makala hii ilichapishwa katika KWANZA JAMII.

Profesa Joseph L. Mbele

Tangu mwaka jana, nimekuwa naendesha warsha hapa Tanzania kuhusu utamaduni na utandawazi. Mwaka jana nilifanya hivyo Arusha, na mwaka huu nimeendesha warsha Tanga na Dar es Salaam. Warsha hizi zimehudhuriwa na watu kutoka Tanzania, Kenya, Cameroon, Uingereza, Sweden, na Marekani. Hao wa nchi za nje ni watu waliokuwepo Tanzania kwa shughuli mbali mbali.

Niliamua kuanza kuendesha warsha hizi hapa Tanzania kutokana na kutambua kuwa ni muhimu katika dunia ya leo inayozidi kuwa kijiji. Watu wa tamaduni mbali mbali wanazidi kukutana kwa sababu mbali mbali, kama vile biashara, masomo, utalii, na uwekezaji. Watu wa tamaduni mbali mbali wanajikuta wakifanya kazi pamoja viwandani, maofisini, na kadhalika. Wanafunzi, watafiti, na walimu, wanajikuta wakishughulika na watu wa tamaduni mbali mbali.

Hali hii inaweza kusababisha migogoro ya aina aina, kwani kila mtu ana namna yake ya kuongea, kufikiri, kufanya mambo, ambayo inatokana na utamaduni wake. Bila kuelewa utamaduni wa wengine, matatizo lazima yatatokea, kama vile kutoelewana na kugombana.

Kwa miaka mingi katika kufundisha Marekani, nimehusika pia katika kutoa ushauri kwa waMarekani kuhusu utamaduni wa waAfrika. Wamarekani hao ni wale wanaokuja Afrika, iwe ni kwa masomo, utalii, shughuli za kidini, au za kujitolea. Nimehusika pia katika kutoa ushauri kwa waAfrika waishio Marekani, kuwasaidia kuulewa utamaduni wa Mmarekani.

Uzoefu huu umenifungua macho kuhusu umuhimu wa suala hili la kuelewa tamaduni mbali mbali, hasa kwa kuwa dunia inabadilika na kuwa kijiji. Hatutaweza kukwepa maingiliano baina ya tamaduni mbali mbali. Wafanya biashara watahitaji kutafuta masoko katika nchi za mbali, au watahitaji kutafuta washiriki kutoka nchi za mbali, au watahitaji kutafuta malighafi kutoka nchi za mbali. Makampuni yatahitaji kuwaajiri watu kufanya shughuli zake sehemu mbali mbali duniani, na katika kufanya hivyo, yatawajibika kuwaajiri watu wa tamaduni mbali mbali.

Kutokana na uzoefu huu nilioupata Marekani, niliona niko tayari kufanya warsha Tanzania. Nilikuwa na hamu ya kukutana na waTanzania na kuona nitafanikiwa vipi kuleta ujumbe wangu.

Jambo la kwanza nililofanya katika warsha hizi ni kuelezea maana ya utamaduni na maana ya utandawazi. Utamaduni, kama nilivyogusia, ni dhana inayojumlisha tabia, mwenendo, hisia na taratibu za maisha. Hata namna ya kuzungumza hutofautisha utamaduni mmoja na mwingine, kiasi kwamba, kwa mfano Mmarekani akisema jambo, linaweza kuonekana kuwa ni maudhi kwa Mwafrika au utovu wa heshima, wakati kwa utamaduni wa Mmarekani, ni usemi wa kawaida au wa heshima. Kadhalika, Mwafrika anaweza kusema jambo ambalo ni la kawaida au la heshima katika utamaduni wake, lakini likawa kero kwa Mmarekani.

Kuhusu utandawazi, dhana yangu ni kuwa utandawazi haukuanza miaka yetu hii, kama wengi wanavyofikiri. Ni jambo lililoanza zamani sana, tangu enzi za binadamu wa mwanzo kabisa. Utandawazi ulianza pale binadamu waliposambaa kutoka Afrika, ambako ndiko walikoanzia, na kuenea duniani. Kuenea huku kwa binadamu kuliandamana na kuenea kwa ujuzi, maarifa, lugha, na mambo mengine mengi.

Utandawazi ulichukua sura mbali mbali kadiri historia ilivyosonga mbele. Katika enzi zetu, utandawazi umetawaliwa na kuenea kwa ubepari, ambao umeathiri uchumi, siasa, utamaduni, na mambo mengine mengi.

Pamoja na hayo, bado tunazo tofauti za tamaduni ambazo zinaweza kuwa kipingamizi tunapokutana na watu wa nchi mbali mbali. Hapo ndipo ulipo umuhimu wa kujielimisha kuhusu tofauti hizi.

Baada ya kuongelea masuala haya ya jumla na kinadharia katika warsha hizi, niliingia katika kutoa mifano ya matatizo ambazo makampuni yamekumbana nayo wakati wa kujaribu kupeleka shughuli zao katika nchi za mbali, kwenye utamaduni tofauti. Makampuni ya Marekani, kwa mfano, yamewahi kupata matatizo katika nchi za Ulaya na Asia. Hata namna ya kutangaza biashara inaweza kuwa chanzo cha matatizo. Tangazo ambalo linavutia wateja katika utamaduni fulani linaweza kuwa kero kwa watu wa utamaduni tofauti. Hata rangi zinazotumika katika tangazo zinaweza kuwa na maana tofauti au kuleta hisia tofauti katika tamaduni mbali mbali.

Kwa bahati nzuri, washiriki wa warsha hizi wamevutiwa na wamesisitiza kuwa ni muhimu warsha hizi ziendelee siku za usoni, kwenye mashirika, vyuo, na taasisi mbali mbali. Kwa upande wangu, nimefurahi kupata fursa ya kuongea kwa undani na waTanzania ambao tulikuwa hatufahamiani. Nimefurahi kuanza kuamsha fikra za masuala haya muhimu miongoni mwa waTanzania. Nimefurahi kuanza kujenga mtandao wa watu ambao tutaweza kuchangia kwa namna fulani maendeleo katika jamii yetu.

Katika kuthibitisha zaidi hoja hizi, nimekuwa nikiongelea mifano hai ya jinsi utamaduni wa Mmarekani unavyotofautiana na utamaduni wa Mwafrika, kama nilivyojionea mimi mwenyewe katika kuishi kwangu na waMarekani. Katika kufanya hivyo, nimekuwa nikitumia kitabu ambacho nimeandika, na ambacho kinatumika na waMarekani wanaofika Afrika, na pia waAfrika wanaoishi Marekani. Ninaandika muda wote, na hii ni njia ya kuendelea kujifunza mimi mwenyewe na kuendelea kutoa mchango wangu katika masuala haya muhimu.

Kitu kimoja ambacho nimekuwa nikisisitiza ni kuwa hili ni suala la elimu, na elimu haina mwisho. Tunawajibika kuanza kujielimisha na kuendelea hivyo bila kuchoka. Warsha moja au mbili haitoshi, bali ni mwanzo. Ni mwanzo mzuri, na nangojea kuendelea kuendesha warsha hizi siku zijazo.

Tuesday, November 17, 2009

Maprofesa Hatuvunji Msitu, ni Mwalimu wa Shule ya Msingi

Picha hii ilichapishwa tarehe 15 Novemba katika blogu ya Haki Ngowi, pamoja na maelezo haya: Mwalimu, Albert Juakali wa shule ya msingi Iboma iliyopo kijiji cha Udinde Wilaya ya Chunya Mkoani Mbeya akifundisha wanafunzi wa darasa la kwanza chini ya Mti wa Mbuyu kama alivyokutwa na Mpigapicha wetu. Picha na Brandy Nelson
Nina mengi ya kusema kuhusu picha hii. Kwa leo napenda kumwongelea huyu mwalimu, kwa kuirejesha makala yangu iliyotokea katika gazeti la KWANZA JAMII.

Maprofesa hatuvunji msitu, ni Mwalimu wa Shule ya Msingi


Na Profesa Joseph L. Mbele

TUNAONGELEA sana mfumo wa elimu. Kitu kimoja ninachoona hatukizungumzii ipasavyo ni wadhifa wa mwalimu wa shule ya msingi. Jamii haimwoni mwalimu wa shule ya msingi kama mtu wa pekee sana. Lakini, akitokeza mwalimu wa chuo kikuu, kama mimi, jamii inafungua macho na kutega masikio. Jamii inamwona mwalimu wa chuo kikuu, profesa, kuwa mtu wa pekee sana, kumzidi mwalimu wa shule ya msingi.

Kwa miaka kadhaa sasa, nimejjijengea mtazamo tofauti kuhusu suala hilo. Hii ndio mada ya makala yangu hii. Hoja yangu ni kuwa, mwalimu wa shule ya msingi anastahili heshima ya pekee. Tunaposema shule ya msingi, tuzingatie neno msingi.

Neno msingi tunalitumia sana tunapoongelea ujenzi wa nyumba. Basi, tuchukulie mfumo wa elimu kama nyumba. Tunapowazia kujenga nyumba, tunazingatia sana msingi, kuhakikisha kuwa ni imara. Kila mtu anajua kuwa ukishafanya hivyo, nyumba yako itakuwa imara. Basi, na elimu ni hivyo hivyo. Ili iwe imara, ni lazima tuanzie kwenye msingi. Na hapo ndipo tunamkuta mwalimu wa shule ya msingi. Yeye ni kama yule fundi mjenzi tunayemtegemea kutujengea msingi imara. Hapo tunaanza kuelewa maana halisi ya dhana ya shule ya msingi.

Tunaweza kutoa mfano mwingine. Tukichukulia ualimu kama kazi ya ukulima, basi mwalimu wa shule ya msingi ni sawa na yule mkulima anayevunja msitu. Sisi walimu tunaokuja baadaye kwa mfano chuo kikuu, tunakuta shamba limeshatayarishwa. Kazi yetu ni nyepesi tukiichukulia kwa mtazamo huu wa kumkumbuka aliyevunja msitu. Ni lazima tumwenzi mvunja msitu, ambaye ni mwalimu wa shule ya msingi. Ni msitu gani huo anaovunja?

Mwalimu wa darasa la kwanza ana jukumu la kuleta mapinduzi katika akili ya mtoto. Anamtoa katika fikra na mazoea ya kucheza siku nzima na kuwinda ndege na kumwingiza katika ulimwengu wa ukurasa wa daftari na kitabu. Huu ni ulimwengu mwingine kabisa, na mapinduzi yanayofanyika hapa ni makubwa. Mtoto alikotoka anajua lugha ya kuongea na kusikia. Lakini mwalimu wa darasa la kwanza anambadilisha na kumfanya aifahamu lugha andishi. Maneno ambayo mtoto alizoea kuyasema tu na kuyasikia, sasa anapaswa ayaone na ayaelewe yanakuwaje kimaandishi. Ajifunze kuandika na kusoma, sio kusema tu na kusikia. Ajifunze namna ya kupanga kila herufi, neno, na sentensi kwenye mstari ulionyooka. Afahamu ukurasa unapangwaje: aanzie juu kwenda chini, si vinginevyo. Maneno ayaandike vipi, nukta na mkato aziweke wapi, na alama za kuuliza na kushangaa aziweke wapi. Haya ni mapinduzi makubwa ya akilini.

Katika mapinduzi hayo, mtoto anaanza kukiona kila kitu kwa mtazamo wa maandishi. Akiona kiti, anajua namna ya kuandika neno kiti. Akiona mnyama au mdudu, anajua namna ya kuandika mnyama au mdudu. Akili ya kuielewa lugha kama kitu cha kusema na kusikia tu inapanuliwa. Akili hiyo inakutana na lugha kwa kutumia macho. Hii ni lugha andishi.

Baada ya mwalimu wa shule ya msingi kufanya hayo mapinduzi akilini mwa mtoto, ndipo sisi walimu wa madarasa yanayofuata tunaletewa huyu mtoto. Sisi hatuleti mapinduzi. Hatuvunji msitu, wala kujenga msingi. Tunaingia darasani na kuongea sana, na wanafunzi wanaandika wanachosikia. Tunawaambia waende maktabani wakasome. Lakini hayo yanawezekana tu kwa vile mwalimu wa shule ya msingi alishawafundisha hao wanafunzi kuandika na kusoma. Bila hivyo, sisi tungekwama. Kwa bahati mbaya, tunasahau jambo hilo. Tunamsahau aliyevunja msitu na tunadhani kusoma na kuandika kuliwezekana au kulijitokeza kiurahisi tu.

Huwa najiuliza, je, nikiambiwa nikafundishe darasa la kwanza, nitaweza? Nina hakika nitaumia kichwa. Bahati nzuri, kwa miaka kadhaa nimekuwa nawatafuta walimu wa shule za msingi sehemu mbali mbali za Tanzania na kuongea nao. Wamenifungua macho kuhusu mambo kadhaa, kama vile saikolojia na tabia ya watoto. Wamenielimisha kuwa watoto wana saikolojia tofauti kufuatana na umri: watoto wa darasa la kwanza wana tabia hii na hii, na unapaswa unapowafundisha ufanye hivi au hivi. Ukifanya vile au vile, hutafanikiwa katika kuwafundisha. Mimi sikujua hayo, lakini walimu wa shule ya msingi wamenifundisha.

Walimu hao wameniambia kuwa unapowafundisha watoto wadogo, uangalie unatumia muda gani kwa kitu kimoja, ili ubadili na kufanya kitu kingine. Usijaribu kuwafundisha kitu kimoja kwa muda mrefu. Ukitoa maelezo kwa dakika kadhaa, unabadili; labda uwaimbishe wimbo. Baada ya dakika kadhaa, labda wachukue daftari na kuchora; baadaye wasome, na kadhalika. Usijaribu kutoa mhadhara kwa muda mrefu, kama tunavyofanya chuo kikuu. Elimu hii nimeipata kutoka kwa walimu wa shule za msingi. Kwa maana nyingine, ningekurupuka tu na kwenda kufundisha kule, ningeharibu mambo. Sijui maprofesa wangapi wanajua hayo.

Kitu kimoja tunachohitaji ni kumtambua mwalimu wa shule ya msingi kwa kazi anayofanya na kumpa fursa kamili ya kufanya kazi yake. Katika Tanzania, tangu miaka ya mwanzo ya Uhuru, tuna jadi ya kuwatwisha walimu majukumu ambayo si ya lazima. Kwa mfano, kwenye sherehe za kitaifa au mapokezi ya viongozi, walimu wametegemewa kuwaandaa watoto wa shule katika gwaride, nyimbo, ngoma, au halaiki. Maofisa kilimo, wahasibu na watumishi wengine ambao wangeweza kabisa kufanya shughuli hizo, hawaguswi. Kwa nini hao wasifanye hizo shughuli za magwaride, ngoma, na halaiki, kama ni shughuli muhimu? Walimu wametumika katika shughuli nyingine pia, kama vile kusimamia kura na hata kuwapikia viongozi. Hizi ni kero zisizo na sababu. Walimu wana kazi nyingi: kuandaa masomo, kufundisha, na kusahihisha daftari za wanafunzi au mitihani..

Baadhi ya matatizo yanayoendelea kuwepo kutokana na walimu wa ngazi mbali mbali kutokuwa na mshikamano. Ingekuwa bora iwapo walimu wa shule za msingi na wale wa sekondari, hadi wa vyuo vikuu, wawe na mshikamano thabiti, na mawasiliano ya daima. Kama nilivyogusia hapo juu, mwalimu wa shule ya msingi ana mengi ya kutufundisha sisi wengine. Anao uwezo wa kutupa mwanga kuhusu njia waliyosafiri wanafunzi tunaowafundisha vyuoni.

Naamini, ingekuwa bora pia kwa walimu wa vyuo vikuu kujaribu kufundisha shule ya msingi. Ingekuwa njia nzuri ya kujielimisha. Ninafahamu kuwa profesa akienda kufundisha shule ya msingi, waTanzania watamshangaa, na huenda wakadhani amechanganyikiwa. Lakini kuna mengi muhimu ambayo profesa anaweza kujifunza kwa kufundisha shule ya msingi, angalau mara moja moja.

Monday, November 16, 2009

Ziara Katika Shule ya Sayansi ya Mazingira

Kwa miaka yapata kumi, nimekuwa nikialikwa kila mwaka kwenda kwenye shule ya sayansi ya mazingira mjini Apple Valley, Minnesota, kutoa mhadhara kwenye somo la falsafa za jadi na mazingira.Mimi kama mtafiti wa masomo yahusuyo masimulizi na falsafa za jadi na utamaduni kwa ujumla, nimetumia fursa hii kuwaeleza wanafunzi namna binadamu, tangu mwanzo wake hapa duniani, alivyoweza kuyatafakari, kuyatathmini na kuyaelezea mazingira. Tangu enzi za mwanzo binadamu aliunda lugha kama chombo mahsusi cha kumwezesha kufanya yote hayo. Uundaji wa lugha halikuwa jambo rahisi, tangu kuvipa majina viumbe na vitu vyote vilivyomzunguka hadi kusema na kuelewana na binadamu wengine.

Kila mwaka, mwalimu Todd Carlson, ambaye amekuwa akinialika, anawaelezea wanafunzi kuhusu utafiti wangu juu ya fasihi simulizi na falsafa za jadi, na anawasomesha kitabu changu cha Matengo Folktales. Hadithi, nyimbo na semi ni baadhi ya mikondo aliyotumia binadamu kuyaelezea mazingira yake na kukidhi duku duku ya akili yake kuhusu yote yaliyomzunguka. Historia ya binadamu imeenda sambamba na upanuaji na utajirishaji wa urithi huo. Hakuna kitu wala kiumbe ambacho binadamu hakukipa angalau jina. Jina ni simulizi ambalo linapambanua kitu au kiumbe kimoja na kingine. Kutoka kwenye kiwango cha majina, binadamu ametunga hadithi, nyimbo, na semi kuhusu misitu, wanyama, ndege, maporomoko ya maji, tufani, ukame, na kadhalika. Hadithi, nyimbo, na semi hizo zimeelezea pia mahusiano ya binadamu na yote hayo. Kuna pia maombezi na matambiko, na njia zingine za kumsaidia binadamu kukabiliana na mazingira na hali mbali mbali za maisha.Mwalimu Carlson anaonekana katika picha hapo juu upande wa kulia kabisa, akiwa ameweka mkono kiunoni. Wanafunzi wa shule hii wanajifunza mambo ya msingi yanayohusu mazingira na namna ya kuyahifadhi. Wanapata fursa ya kutembelea nchi za nje pia, kujifunza.
Katika kutembelea kwangu shule hii nimeona jinsi wanafunzi walivyo makini na wenye duku duku ya kujua mambo. Ni wanafunzi hodari kabisa. Kila ziara imekuwa ya kuridhisha sana. Taarifa na picha hizi zinatokana na ziara yangu ya tarehe 10 Novemba, 2009.

Sunday, November 8, 2009

Watanzania jitokezeni kwenye mijadala ya elimu

Habari hii imechapishwa katika gazeti la Habari Leo

Imeandikwa na Na Simon Nyalobi; Tarehe: 7th November 2009

WATANZANIA wametakiwa kujenga tabia ya kuandika machapisho ya utafiti wao na kujitokeza katika mijadala ya kimataifa kuhusu elimu badala ya kuogopa na kukaa pembeni.

Mwito huo ulitolewa jana Dar es Salaam na Ofisa Mipango ya Elimu wa Shirika la Oxfam tawi la Tanzania, Mary Soko wakati wa akifunga warsha ya siku tatu ya Jumuiya ya Utendaji wa Elimu nchini iliyokuwa na washiriki 40 kutoka maeneo mbalimbali nchini.

Soko alisema kuwa Wataznania wengi hawajitokezi katika makongamano ya kimataifa kuonesha utafiti wao ikilinganishwa na mataifa mengine hususani Nigeria ambayo raia wake hujitokeza kila kongamano la usomaji wa vitabu linapotokea.

Alisema kuwa hata makongamano yanayofanyika hapa nchini, hayana muamko kwa kuwa watanzania wengi wamekuwa nyuma kushiriki. Kutokana na hali hiyo, amewataka sasa kujitokeza kila yanapotokea makongamano ya usomaji wa vitabu ili kuiweka nchi katika ramani ya wasomi kwani uwezo wa kufanya hivyo wanao.

Hata hivyo aliasa tabia ya kusoma iboreshwe katika jamii hususani wadau wa elimu, ili waongeze maarifa ya kuandika utafiti wao kwa usahihi.

Pia aliwataka walimu kuacha kulala na badala yake waihamasishe serikali kuhusu mustakabali wa elimu ili kudumisha kiwango cha elimu nchini kwani wakishindwa wao taifa nalo litashindwa.

Katika hatua nyingine alilitaka Baraza la Mitihani Tanzania (NECTA), Taasisi ya Ukuzaji wa Mitaala na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kushirikiana kwa pamoja ili kuboresha kiwango cha elimu nchini.

Vitabu Bila Karatasi

Kitu kimoja ambacho kinampambanua mwanadamu na viumbe wengine ni tekinolojia. Chimbuko la binadamu lilifungamana na uwezo wake wa kutengeneza na kutumia zana mbali mbali, kuanzia zana za miti na mawe, hadi chuma na leo zana zinazoendeshwa na umeme au nguvu za nyuklia. Katika maendeleo haya ya tekinolojia, binadamu amegundua na kuweza kutumia nishati mbali mbali, kama vile maji, upepo na jua.

Uandishi na uchapishaji vimefungamana na maendeleo ya tekinolojia. Tangu binadamu wa kwanza alivyoandika michoro kwenye miamba au kuta za mapango, kwenye ngozi za wanyama, vibao vya udongo, au karatasi, yote hayo ni matunda ya tekinolojia. Leo kuna mashine na mitambo ya aina aina ya kuchapisha magazeti na vitabu.

Maendeleo ya tekinolojia ya uchapishaji yametufikisha mahali ambapo uchapishaji sasa unaweza kufanyika bila karatasi. Vitabu vinaandikwa na kusomwa bila kutumia karatasi, bali kwa mtindo wa digitali. Kwa mtindo huu wa digitali, mtu anaandika kitabu chake kwa kutumia kompyuta, na anakihifadhi mtandaoni. Mwenye kutaka kukisoma kitabu hiki anatumia kifaa maalum kiitwacho "e-reader" au "e-book reader." Kuna vifaa vingine pia. Mtu huyu anaingiza kitabu kutoka mtandaoni katika kifaa chake na kukisoma kwenye skrini ya kifaa hicho. Anaweza kuhifadhi vitabu vingi katika kifaa hicho.

Hatua hii ni muhimu, kwani kati ya faida zake nyingi ni kuwa inachangia kuhifadhi miti na misitu ambayo ilikuwa inaharibiwa ili kutengeneza karatasi. Tekinolojia hii ya digitali ni baraka kwa waandishi na wasomaji. Waandishi hawalazimiki tena kuwategemea wachapishaji. Wasomaji hawalazimiki kwenda kwenye duka la vitabu, au kuagiza kitabu na kukingoja kisafirishwe. Wanakipata papo kwa papo mtandaoni. Baadhi ya vitabu vangu, sasa vinapatikana kwa mtindo huo, kama inavyoonekana hapo upande wa kulia.

Saturday, November 7, 2009

Tutajengaje Utamaduni wa Kusoma Vitabu?

Leo asubuhi nilienda kwenye mji wa Brooklyn Park, Minnesota, kuhudhuria kikao cha kamati inayojishughulisha na masuala ya kujenga na kuboresha mahusiano baina ya waAfrika na waMarekani Weusi. Baada ya kikao, wakati narudi kwenye mji ninapoishi, nilipita kwenye mji wa Apple Valley, nikaingia katika duka la vitabu la Half Price Books. Ni duka ambalo nimelitembelea mara nyingi. Half Price Books ni mtandao mkubwa wa maduka ya vitabu hapa Marekani, ambao una maduka katika miji mingi kama inavyoonekana hapa.

Kama kawaida, ninapoingia katika maduka ya vitabu hapa Marekani, nawakuta watu wa kila aina wakizungukazunguka kutafuta vitabu, wakivisoma, na wakivinunua. Kuna maduka mengi ya vitabu hapa Marekani ambamo watu wanaleta vitabu vyao kuviuza, na wengine wanakuja kununua. Unaweza kuja kuuza vitabu vyako na kununua vitabu vingine. Nimewahi kufanya hivyo. Maduka ya Half Price Books yanafuata mtindo huo. Kwa hivi, daima utawaona watu wakija na mifuko au makasha ya vitabu vya kuuza, wakati huo huo unawaona watu wakinunua vitabu.

Leo, kama ilivyo kila ninavyoingia katika maduka haya, niliona jinsi Wamarekani wanavyojali utamaduni wa kusoma vitabu. Niliwaona wazee, watu wazima, wake kwa waume, vijana, na watoto. Niliwaona wazazi wakiwa na wamekuja na watoto wao. Niliwasikia wakiongea na watoto kuhusu vitabu, wakiwasomea watoto vitabu, wakijibu masuali ya watoto, na kadhalika.

Nilijisikia vibaya kukumbuka hali ilivyo nchini mwetu Tanzania. Leo ni Jumamosi. Je, ni mzazi gani Mtanzania ambaye siku kama ya leo anaenda kwenye duka la vitabu? Ni mzazi gani ambaye anampeleka mtoto wake kwenye duka la vitabu?

Sasa, kama watoto wa wenzetu wanalelewa hivyo, je, tunaweza kutegemea kuwa Taifa letu litaweza kushindana na hao wenzetu katika ulimwengu huu wa leo na wa kesho ambao unategemea elimu na maarifa? Ni lini na vipi waTanzania tutajenga utamaduni wa kusoma vitabu? Hatima ya Taifa letu itakuwaje?

Tuesday, November 3, 2009

Kijitabu Kuhusu "Things Fall Apart"

Riwaya ya Chinua Achebe, Things Fall Apart, inafahamika duniani kote. Inatumika sana mashuleni. Mimi kama mwalimu wa fasihi nimefundisha riwaya hii kwa miaka mingi, hadi nikaandika mwongozo kwa wasomaji, wanafunzi, na walimu. Mwongozo huu ni kijitabu ambacho kinapatikana mtandaoni. Bofya hapa.

Lakini, kama watu wasemavyo, tunakwenda na wakati. Tarehe 1 Novemba, 2009 nimekichapisha kijitabu hiki kama "e-book." Yeyote mwenye kifaa kiitwacho "e-reader," au "e-book reader," anaweza kukiingiza katika kifaa hicho, akakisoma. Bofya hapa.

Saturday, October 31, 2009

KWANZA JAMII limetua Mwanza


Gazeti la KWANZA JAMII linapatikana Mwanza, kwa mujibu wa picha hizi zilizotoka katika blogu ya Mjengwa tarehe 29 Oktoba, 2009 na 30 Oktoba, 2009. Nami napenda kufuatilia maendeleo ya gazeti hili.

Wednesday, October 28, 2009

KWANZA JAMII Mikumi

Picha hii imechapishwa tarehe 28 Oktoba, 2009, katika blogu ya Mjengwa. Maggid Mjengwa amepiga picha hii Mikumi. Mimi kama mwandishi katika gazeti la KWANZA JAMII nafurahi kuona gazeti hili, ambalo bado changa, linavyojikongoja na kuendelea kuenea nchini, hadi kwenye miji midogo na vijijini. Siku chache zilizopita tulipata habari za KWANZA JAMII kufika kijijini Roya. Bofya hapa. Kama wahenga walivyosema, pole pole ya kobe humfikisha mbali.

Friday, October 16, 2009

Warsha Dar es Salaam: Utamaduni na Utandawazi


Tarehe 5 Septemba, mwaka huu, niliendesha warsha Dar es Salaam, kuhusu Utamaduni na Utandawazi. Warsha hii iliandaliwa na Tanzania Discount Club. Siku chache kabla, tarehe 29 Agosti, niliendesha warsha nyingine Tanga, kuhusu Utamaduni, Utandawazi na Maendeleo. Warsha hii, ambayo ilihudhuriwa na watu wa mataifa mbali mbali, nimeiongelea kidogo hapa na hapa.

Warsha hii ya Dar es Salaam ilinipa fursa ya kukutana na waTanzania kutoka sekta binafsi, taasisi mbali mbali na Ubalozi wa Marekani.
Warsha ilidumu kuanzia saa nne na nusu asubuhi hadi saa 11 jioni. Sehemu ya kwanza ilihusu masuala ya jumla: dhana ya utamaduni, kama nilivyoielezea katika kitabu changu Africans and Americans, na dhana ya utandawazi. Kwa mtazamo wangu, utandawazi ni jambo ambalo lilianza zamani kabisa, pale binadamu wa mwanzo walivyosambaa duniani wakitokea Afrika Mashariki. Hapo ndipo utandawazi ulipoanzia, na baada ya hapo, kumekuwa na aina na awamu mbali mbali za utandawazi, hadi kufikia zama zetu hizi, ambazo zimeshuhudia utandawazi wa ubepari ambao uliongelewa vizuri na Karl Marx na Frederick Engels katika Communist Manifesto. Leo hii, tekinolojia, na hasa tekinolojia ya mawasiliano, inawezesha aina nyingine za utandawazi, ambazo hata akina Karl Marx hawakuziwazia, kwani hazikuwepo. Utandawazi unajitokeza katika uchumi, siasa, utamaduni, na mambo mengine mengi.
Baada ya maelezo haya ya jumla niliingia kwenye suala la nafasi ya utamaduni katika utandawazi, nikielezea jinsi kuwepo kwa tamaduni mbali mbali duniani kunavyoathiri au kuathirirwa na utandawazi. Nilitoa mifano ya athari hizi. Kutokana na utafiti na uzoefu wangu, niliongelea kwa undani masuala yanayojitokeza katika mahusiano baina ya Wamarekani na Waafrika, kama nilivyoeleza katika kitabu changu.
Washiriki wote walifurahiwa na warsha hii na walitaka warsha za aina hii zifanyike siku za usoni, katika vyuo na taasisi mbali mbali.
Kwa upande wangu, nilifurahi kupata fursa ya kuongea na waTanzania wenzangu na kuwaeleza yale ambayo nimekuwa nawaeleza waMarekani kwa miaka kadhaa. Imenipa motisha ya kuendelea kufanya warsha za aina hii.
Jambo mmoja nililosisitiza ni kuwa ni muhimu warsha kama hii iwe ni sehemu ya elimu endelevu, ni muhimu tuendelee kuwasiliana. Baadhi ya washiriki walijipatia nakala za kitabu changu. Siku zijazo itawezekana kufanya warsha juu ya yaliyomo na yatokanayo na kitabu hiki, kama ambavyo inafanyika huku Marekani. Kitabu kinapatikana Dar es Salaam, simu namba 0717 413 073 au 0754 888 647

Kadiri dunia inavyoendelea na utandawazi, ni muhimu tujizatiti kwa kuelewa yanayotokea na kujiweka sawa ili kukabiliana na kuitumia hali inayojitokeza. Kwa wale ambao wamelala, utandawazi unaweza kuwa tishio na kipingamizi, lakini kwa walio makini utandawazi unaweza kuwa fursa ya kufanya mambo ya maana.

Wednesday, October 14, 2009

Mwalimu Angerudi Leo Angejisikiaje?

Makala hii imechapishwa katika KWANZA JAMII, Oktoba 13-19, 2009

Profesa Joseph L. Mbele

Imetimia miaka kumi tangu Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere, alipofariki London, Oktoba 14, 1999. Ni jambo jema kutumia muda huu kumkumbuka kwa namna ya pekee, kwa mchango wake kwa Tanganyika (na baadaye Tanzania), Afrika na dunia kwa ujumla. Ni vizuri pia kutumia muda huu kutafakari mwenendo wa nchi yetu, tukilinganisha na makusudio aliyokuwa nayo Mwalimu wakati wa uhai wake.

Mchango wa Mwalimu katika harakati za kupigania Uhuru wa Tanganyika unatambulika. Akishirikiana na viongozi wengine wa sehemu mbali mbali za nchi, wa dini na rangi mbali mbali, na wananchi kwa ujumla, Mwalimu Nyerere aliongoza Tanganyika kufikia Uhuru, Desemba 9, 1961.

Hapo alitoa hotuba ambayo maneno yake ni vigumu kusahaulika, kwa jinsi yalivyoelezea kwa ufasaha hisia na matumaini ya Taifa letu changa. Mwalimu alisema, “Sisi tunataka kuwasha mwenge, na kuuweka juu ya Mlima Kilimanjaro, ili umulike hata nje ya mipaka yetu, ulete tumaini pale ambapo hakuna matumaini, upendo mahali palipo na chuki, na heshima palipojaa dharau.”

Hotuba hii ilikuwa ni kielelezo kizuri cha malengo aliyokuwa nayo Mwalimu kwa nchi yetu. Ilisisimua nchi nzima na kuleta changamoto kwa wananchi katika ari ya kulijenga Taifa lao. Katika hotuba na maandishi yake mbali mbali, miaka yote ya maisha yake, Mwalimu Nyerere alifafanua masuala na wajibu mbali mbali wa wananchi, viongozi, na Taifa kwa ujumla. Aliweka sera ya kujenga uchumi wa kijamaa, ambamo njia kuu za uchumi zinamilikiwa na umma, kupitia serikali yao, kwa manufaa ya umma. Alielezea wajibu wa kila mtu kufanya kazi, na kupata kipato kutokana na mchango wake. Aliongelea kutokomeza unyonyaji, iwe ni wa mtu dhidi ya mwingine, au tabaka la jamii dhidi ya tabaka jingine.

Kuhusu elimu alifundisha kuwa elimu ni haki ya kila binadamu, itolewe kwa watu wote, bure. Mwalimu alifafanua wajibu wa wasomi kuwa ni kuutumikia umma. Elimu ilitakiwa iwe inayochochea udadisi wa kifikra, na kujitegemea. Alisisitiza kuwa elimu haina mwisho. Alijenga utaratibu wa elimu ya watu wazima na kisomo chenye manufaa, ili watu waweze kujiendelea katika fani mbali mbali, iwe ni ukulima, uvuvi, useremala, na kadhalika. Pamoja na kuona elimu kuwa ni namna ya kupambana na adui ujinga, elimu ilihesabiwa kuwa njia ya kuondokana na utumwa wa kimawazo na ukoloni mambo leo.

Mwalimu alijali suala la huduma za afya na matibabu, akiyachukulia mambo hayo kuwa ni haki ya kila mtu. Ingekuwa uwezo wa nchi kuwa mdogo, huduma zingepelekwa kila mahali. Na katika kuwazia hilo, akaona kuwa vijiji vya ujamaa ndio mfumo muafaka wa kuwezesha huduma kama elimu, afya, na burudani kuwafikia wananchi.

Kisiasa, Mwalimu Nyerere alisimama kidete kutetea wanyonge na kujenga misingi ya demokrasia ya wakulima na wafanyakazi. Muda mfupi tu baada ya Uhuru, Mwalimu aliandaa na kutangaza Azimio la Arusha na miongozo mbali mbali ya kujenga usawa katika nchi yetu.

Mwalimu Nyerere alishughulikia utamaduni pia, akihamasisha watu kuuthamini utamaduni wao, maadili, lugha, na sanaa. Mwalimu aliipa kipaumbele lugha ya kiSwahili akaifanya lugha ya Taifa. Aliitumia katika hotuba na maandishi yake, kuanzia insha hadi mashairi. Alitafsiri tamthilia za Shakespeare: “The Merchant of Venice” na “Julius Caesar” kwa kiSwahili, akathibitisha utajiri wa lugha ya kiSwahili na pia kuwafungulia waTanzania milango waone utajiri uliomo katika falsafa na uandishi wa bingwa huyu ambaye alisifiwa pia sana na Shaaban Robert.

Mwalimu alitambua kuwa nchi yetu msingi wake mkuu ni wakulima. Kwa hivi alijibidisha kujenga sera ya kuleta maendeleo vijijini. Kufuata na hali halisi ya nchi yetu, aliona kuwa njia muafaka ni viijiji vya ujamaa. Sera hii ilikuwa na lengo la kuleta maendeleo vijijini katika usawa na kujitegemea. Ni sera aliyoifafanua mara kwa mara, kuanzia pale alipotangaza Azimio la Arusha.

Taifa letu lilihitaji kuwa na sera kuhusu uhusiano wetu na nchi zingine na nafasi yetu duniani. Mwalimu alisisitiza kuwa nchi yetu ni huru na haifungamani na upande wowote. Tuko tayari kuwa marafiki na nchi yoyote kwa misingi ya kuheshimiana. Hatumruhusu rafiki yetu kutuchagulia maadui zetu.

Kwa vile watu wengi Afrika na duniani walikuwa bado wanapigania uhuru na ukombozi, nchi yetu ilikuwa na msimamo wa kuunga mkono harakati za ukombozi duniani kote. Tulikuwa bega kwa bega na wenzetu katika nchi za kusini mwa Afrika, Palestina, Sahara Magharibi. Tuliunga mkono harakati za Wamarekani weusi, na kadhalika.

Maisha yake yote, Mwalimu alizingatia mwelekeo huo. Hakuwahi kuchepuka kutoka kwenye imani yake juu ya Ujamaa. Wako ambao wanadai kuwa aliwahi kusema kuwa Ujamaa umeshindwa. Madai hayo hayana ukweli. Hakuna ushahidi ambao umetolewa kwamba Mwalimu aliwahi kusema kuwa Ujamaa umeshindwa. Ni uzushi tu ambao wengi wameusikia na wanaurudia kama vile ungekuwa ukweli.

Leo hii Tanzania haifuati mwelekeo wa Mwalimu. Wazo la kujenga uchumi unaojitegemea limetupwa kando. Badala ya kuendeleza malengo ya Azimio la Arusha, kuyaweka katika hali ya kuendana na mazingira ya leo, chama tawala cha CCM kilileta Azimio la Zanzibar, ambalo Mwalimu Nyerere alilishutumu. Azimio la Zanzibar lililegeza masharti ya uongozi yaliyowekwa miaka iliyotangulia.
Leo tunaongelea kukua kwa uchumi, lakini si mgawanyo wa mali katika jamii. Nchi yetu ina matabaka, na tofauti kati ya matajiri na maskili inazidi kuwa kubwa. Hii ni hali ya hatari kwa siku za usoni.

Kwa sera zake, kama zilivyotamkwa katika Azimio la Zanzibar, CCM ilifungua milango ambayo hatimaye imeuwezesha ufisadi kuota mizizi na kustawi katika nchi yetu. CCM haishughuliki katika kudumisha urithi wa Mwalimu Nyerere. Inaonekana wazi kuwa CCM ingependa fikra za Mwalimu Nyerere zisahaulike, kutokana na ukweli kuwa CCM imeachana na fikra hizo, na pia kwa miaka mingi kabla hajafariki, Mwalimu Nyerere alikuwa anaishutumu na kuikosoa CCM.

Mara kwa mara zinapatikana taarifa za namna watu sehemu mbali mbali za dunia wanavyomwenzi Mwalimu Nyerere. Lakini tukifananisha na Tanzania tunaona kuwa nabiii huheshimiwa, isipokuwa nchini kwake. Hata hivi, tunayo fursa ya kujirekebisha, na dalili za kuleta matumaini zipo. Kwa mfano katika maadhimisho ya kifo cha Mwalimu Nyerere mwaka huu, Taasisi ya Mwalimu Nyerere itatoa vitabu kadhaa vya maandishi ya Mwalimu, yakiwemo maandishi ambayo hayajawahi kuchapishwa. Habari hii inaleta matumaini.

Napenda kumalizia kuwa niliyoandika hapa ni dondoo tu. Kila kipengele kinastahili makala ya pekee, hata kitabu. Lakini nina suali: je, leo hii Watanzania tunaweza kudiriki kusema kuwa tuwashe mwenge na kuuweka juu ya Mlima Kilimanjaro kwa lengo la kuleta matumaini, upendo na heshima kwa wenzetu ulimwenguni? Ni nani duniani anayetuangalia leo akatamani kuwa kama tulivyo? Mwalimu Nyerere angerudi nchini leo, angejisikiaje?

Sunday, October 11, 2009

Tamasha la Vitabu, Minneapolis, 2009

Jana, tarehe 10 Oktoba, nilishiriki tamasha la vitabu mjini Minneapolis. Tamasha hili hufanyika kila mwaka mara moja. Nimeshahudhuria mara kadhaa miaka iliyopita, lakini hali ni mpya kila mwaka. Kwa mfano, waandishi maarufu wanaoalikwa kama wageni rasmi huwa tofauti kila mwaka. Pia, pamoja na kuwa baadhi ya waandishi na wachapishaji na wauza vitabu huja mwaka hadi mwaka, wako pia wengi ambayo ni wapya. Hapo juu mbele kabisa ni mezani pangu. Baadhi ya vitabu vyangu vinaonekana.
Watu wanawahi, na milango ukumbi wa maonesho inapofunguliwa, saa nne asubuhi, ukumbi unafurika watu. Siku nzima hali ni hiyo hiyo; kuna msongamano wa watu wakiwa wanaangalia na kununua vitabu, wakiongea na waandishi na wachapishaji, na kadhalika.

Waandishi wa kila aina wanakuwepo, wake kwa waume, wazee kwa vijana. Siku hizi wengi wanachapisha vitabu vyao kwa kutumia fursa zitokanazo na maendeleo ya tekinolojia, bila kupitia kwa wachapishaji kama ilivyokuwa zamani. Kila mtu anaweza kutumia tekinolojia hiyo ya kujichapishia mwenyewe, ambayo inapatikana sehemu mbali mbali mtandaoni, ili mradi awe na kompyuta iliyounganishwa mtandaoni.

Wamarekani wanafurika kwenye tamasha la vitabu sawa sawa na sisi waTanzania tunavyofurika sokoni kununua vyakula. Pamoja na hali ya uchumi kuwa ya matatizo nyakati hizi, watu wananunua sana vitabu. Sijui ni lini waTanzania wataanza kupata mwamko wa kuviona vitabu kuwa ni muhimu kiasi hicho. Niliwahi kutoa kauli hiyo kwenye mahojiano na mwanablogu maarufu Muhiddin Issa Michuzi tarehe 4 Septemba, 2009.
Wamarekani wanaliona tamasha la vitabu--au duka la vitabu--kama sehemu muhimu ya kujiongezea elimu na kupanua mawazo. Mazungumzo na waandishi, wachapishaji na wauza vitabu yanaendelea siku nzima. Watu wanakuja kutoka miji ya karibu na mbali pia. Wanakuja kuangalia vitabu, kuvinunua, kuongea na waandishi na wachapishaji, kujenga mitandao ya ushirikiano katika shughuli za uchapishaji na uuzaji wa vitabu na kadhalika.



Katika tamasha la jana, nilipangiwa meza namba 19, kama inavyoonekana hapa juu. "Africonexion" ni kampuni yangu, ambayo niliisajili hapa Minnesota. Inshughulika na warsha, uandishi na uchapishaji wa vitabu, elimu kuhusu utalii, mahusiano baina tamaduni mbali mbali, na kadhalika. Siku za usoni nitaiingiza kampuni hii Tanzania.
Kama inavyoonekana hapa juu, tamasha hili ni kazi kubwa kwa waandishi, kukaa na kuongea na watu siku nzima. Ingawa inachosha, ni shughuli muhimu kwa namna mbali mbali.
Hapo juu niko na Bukola Oriola, dada Mnigeria ambaye mwaka huu nilimsaidia kuchapisha kitabu chake kwa kutumia tekinolojia niliyoelezea hapo juu kwa kupitia kampuni ya Lulu. Anaendelea kuandika.

Hapo juu niko na Profesa Mahmoud El Kati, Mmarekani mweusi, ambaye ni mtu maarufu katika miji jirani ya Minneapolis na St. Paul, akiwa ni mwalimu, mtafiti, mwandishi na mwanaharakati. Nimefahamiana naye kwa miaka kadhaa.

Thursday, October 8, 2009

Uraia wa nchi Mbili

Makala hii imechapishwa katika KWANZA JAMII, Oktoba 6-12, 2009

Profesa Joseph L. Mbele

Tarehe 4 Septemba, 2009, nilipata fursa ya kukutana na ndugu Muhiddin Issa Michuzi, mwanablogu maarufu Tanzania. Pamoja na maongezi kuhusu masuala mbali mbali, alinifanyia mahojiano mafupi kwa ajili ya kuweka kwenye blogu yake. Suali moja aliloniuliza ni kuhusu msimamo wangu juu ya suala la uraia wa nchi mbili. Nilijibu kifupi, kutokana na uchache wa muda. Lakini suali hili limekuwa mawazoni mwangu kwa miaka kadhaa, tangu lilipoanza kuongelewa na waTanzania.

Nilimweleza Ndugu Michuzi kuwa binafsi sitaki uraia wa nchi nyingine. Nilililelewa katika misingi ya kujitambua kuwa mimi ni mTanzania tu. Isipokuwa, nilisema kuwa watoto wa siku zijazo, watakuwa waishi katika dunia tofauti na yetu, na itakuwa dunia ambayo itakuwa imefungamana sana na kuwa kama kjiji. Hata mipaka ya nchi huenda haitakuwepo, wala nchi hazitakuwepo. Kwa hivi suala la uraia nalo litakuwa na sura tofatuti.

Tukiacha suala la hisia binafsi, ni vema kuangalia upana wa suala la uraia wa nchi mbili. Jambo moja na msingi ni kuwa sheria na taratibu za nchi mbali mbali kuhusu uraia zinatofautiana. Hali kadhalika, sheria na taratibu kuhusu uraia wa nchi mbili zinatofautiana kutoka nchi hadi nchi. Ziko nchi zenye sheria ngumu kuliko ilivyo katika nchi zingine. Ziko nchi ambazo sheria zake ni nyepesi.

Marekani ni nchi moja yenye sheria ngumu kuhusu uraia wa nchi mbili. Watu wengi wanachukua uraia wa Marekani. Na nadhani waTanzania wengi nao wanataka kuchukua uraia wa Marekani. Lakini ukweli ni kuwa wanaochukua uraia wa Marekani wanakula kiapo ambacho ni kizito sana. Katika kiapo hiki, wanaukana kabisa utii na uaminifu kwa kiongozi au dola ya nchi walikotoka. Ndio kusema, Mtanzania anayechukua uraia wa Marekani, anaapa hatambui amri ya kiongozi wa Tanzania juu yake. Anaapa kuwa atabeba silaha kuitetea Marekani kwa mujibu wa sheria. Kiapo hiki kinanitisha, kwa jinsi Marekani ilivyo na historia ya kushambulia nchi zingine, hasa nchi maskini.

Katika mijadala kuhusu uraia wa nchi mbili, suala linajadiliwa kwa namna ya kuelezea faida tu. Sisikii maelezo kuhusu wajibu na majukumu yanayotokana uraia wa nchi mbili. Ukweli ni kuwa hakuna nchi inayotoa uraia kama njugu, bila masharti na bila kumtwisha mhusika majukumu. Marekani inamtegemea mtu anayechukua uraia wa nchi ile kuapa kuwa atashika silaha kuitetea Marekani kwa mujibu wa sheria. Huo ni mfano mmoja wa majukumu yanayoambatana na uraia wa nchi mbili.

Kama nilivyosema, nchi nyingine hazina masharti kama haya ya Marekani. Kuna nchi ambazo hazina kiapo kama hiki cha Marekani. Nikisikia Mtanzania amechukua uraia wa nchi hizo, sioni kipingamizi chochote.

Kitu kimoja ambacho naamini waTanzania wengi hawajui ni kuwa Marekani yenyewe haipendelei raia wake wachukue uraia wa nchi zingine. Inatambua kuwa uraia wa nchi mbili unaweza kuleta matatizo. Vile vile Marekani inawatahadharisha raia wake kuwa kuchukua uraia wa nchi nyingine kunaweza kuhatarisha uraia wao wa Marekani. Hii inaweza kuwa ni ajabu kwa wale wanaoamini kuwa Marekani ndio nchi yenye uhuru kuliko nchi zingine duniani.

Hata hivi, kuna aina ya uraia wa nchi mbili ambao Marekani inautambua bila kipingamizi. Mtoto anayezaliwa Marekani na ambaye wazazi wake si raia wa Marekani anahesabiwa kuwa raia wa Marekani na pia raia wa nchi ya wazazi wake. Huu uraia wa nchi mbili hauna mgogoro katika taratibu na sheria za Marekani. Kadhalika, sheria za Marekani zinamtambua mtoto wa waMarekani anayezaliwa nchi nyingine kuwa ni raia wa Marekani, pamoja na kuwa anaweza pia kuwa raia wa nchi ile alimozaliwa. Huu ni uraia wa nchi mbili ambao Marekani inautambua bila tatizo.

Kwa upande wa Tanzania, tunao pia watoto wanaozaliwa nchi za nje lakini wazazai wao ni waTanzania. Naona ni sahihi kuwatambua watoto hao kuwa raia wa nchi mbili. Vile vile, kuna mtoto ambaye mzazi wake mmoja ni Mtanzania na mzazi mwingine si mTanzania. Mtoto huyu naona anastahili kuhesabiwa kuwa raia wa nchi mbili.

Sababu moja wanayotoa Watanzania wanopigania uraia wa nchi mbili ni kuwa uraia wan chi mbili utawafungulia milango ya uwekezaji nchini Tanzania au itawaletea urahisi wa uwekezaji. Sina hakika kama hoja hii ina uzito, kwani watu wengi ambao si raia wa Tanzania wanawekeza Tanzania bila matatizo. Je, ni kweli kwamba uraia wa nchi mbili ndio utawafungulia njia waTanzania kuwekeza nchini? Ni kweli kuwa wanapokuwa hawana uraia wa nchi mbili wanakutana na vipingamizi katika uwekezaji nchini? Naona suala hili linahitaji ufafanuzi.

Katika mahojiano na Ndugu Michuzi, nilisema kuwa kwa jinsi dunia inavyokwenda, chini ya utawandazi, labda nchi zitatoweka, na itabaki dunia tu. Vizazi vijavyo, vinavyolelewa katika mazingira tofauti na yale niliyokulia mimi vitakuwa na hisia na msimamo tofauti na wangu kuhusu uraia. Katika dunia ya leo inayozidi kukumbwa na utandawazi, juhudi za nchi mbali mbali kuungana kiuchumi, kisiasa, na kadhalika, yawezekana mipaka ya nchi itatoweka. Suala la uraia litachukua sura mpya. Labda hapatakuwa na sababu ya uraia wa nchi yoyote, wala uraia wa nchi mbili. Labda watu watakuwa raia wa Afrika Mashariki, basi, au raia wa Afrika basi, badala ya kuwa raia wa Tanzania, Cameroon, au Sudan, kama ilivyo sasa. Malumbano ya uraia wa nchi mbili sherti yazingatie huu uyakinifu.

Sunday, October 4, 2009

Diwani--"KWANZA JAMII Limefika Roya!"

(Taarifa hii imechapishwa katika blogu ya Mjengwa tarehe 4 Oktoba, 2009. Nikiwa ni mwandishi mmojawapo wa KWANZA JAMII, nafurahi jinsi gazeti hili linavyojitahidi kuingia vijijini. Hata kijijini kwangu, Wilaya ya Mbinga, linafahamika)

Mchana huu Diwani wa Kata ya Roya Bw. Emmanuel Kigodi amempigia simu mwandishi wa KWANZA JAMII Victor Makinda kumjulisha kuwa nakala nne za KWANZA JAMII zimemfikia. Gazeti hilo limebeba habari kubwa ukurasa wa mbele yenye kuhusiana na ujambazi uliotokea kwenye kata hiyo hivi karibuni. Kwa mujibu wa Diwani Kigodi, gazeti hilo la KWANZA JAMII sasa limekuwa gumzo kijijini Roya na linazunguka kwa wanakijiji wenye hamu ya kusoma habari zake!

Thursday, September 17, 2009

Warsha: "Utamaduni, Utandawazi na Maendeleo," (Tanga, Agosti 29)


Tarehe 29 Agosti niliendesha warsha Tanga, Tanzania, mada ikiwa ni "Utamaduni, Utandawazi na Maendeleo". Warsha hii ilifanyika katika kituo kiitwacho Meeting Point Tanga na ilidumu kuanzia saa nne asubuhi hadi saa kumi na moja jioni. Hapo juu anaonekana Mama Ruth Nesje, mkurugenzi wa kituo, akinitambulisha kwa washiriki wa warsha.

Niliamua kufanya warsha hii kutokana na uzoefu wangu wa kuelezea masuala haya ya utamaduni kwenye vyuo, taasisi, makampuni, makanisa, jumuia mbali mbali na watu binafsi huko Marekani. Warsha hii ilikuwa na mvuto mkubwa kwa washiriki na iliamuliwa kuwa zifanyike warsha hizi siku zijazo. Kitu kimoja kilicholeta msisimko na mjadala mkubwa ni makala yangu "Maendeleo ni Nini?"

Ninapangia kuandika zaidi kuhusu warsha hii, na nyingine ambayo niliendesha Dar es Salaam tarehe 5 Septemba, ila nimeona niweke hii taarifa fupi hapa, kwa sasa. Kama kianzio, nimeweka picha chache zilizopigwa siku hiyo.




(Photos by Vesla Eriksen)

Thursday, September 10, 2009

Nimeonana na Mheshimiwa Michuzi


Tarehe 4 Septemba, 2009 ilikuwa siku maalum kwangu, kwani nilipata bahati ya kuonana na gwiji wa blogu, Mheshimiwa Michuzi ofisini kwake pale Mtaa wa Samora, Dar es Salaam. Hii ilikuwa ni mara yangu ya kwanza kuonana na gwiji huyo.

Tuliongelea mambo mengi yahusuyo blogu na mawasiliano ya kisasa kwa ujumla. Kwa mfano, alikumbushia mkutano wa wanablogu unaopangwa kufanyika Dar es Salaam mwezi Desemba mwaka huu. Nilimwona Michuzi kuwa mtu mwenye hamu ya kuona maendeleo. Hasiti kutoa ushauri wa kuwasaidia wengine. Alisema kuwa anapitia blogu nyingi, na hapo akaniambia kuwa picha iliyopo kwenye blogu yangu si nzuri. Hapo hapo aliniambia nisimame na akanipiga picha nikaiweke kwenye blogu.

Michuzi anaheshimu taaluma yake na anapenda kuona wanablogu wanasukuma mbele gurudumu la mawasiliano hayo kwa kila mmoja kutafuta kipengele maalum na kukiendeleza, iwe ni taaluma, burudani, na kadhalika. Michuzi alisema, kwa mfano, si kila mmoja anaiweza shughuli ya mwanahabari. Tuliongelea mengi, na pia tulifanya mahojiano haya hapa.

Friday, August 21, 2009

Simlaumu JK kwa kuzunguka duniani

(Makala hii imechapishwa katika KWANZA JAMII, Agosti 18-24, 2009)

Profesa Joseph L. Mbele

Katika makala zangu za hivi karibuni, nimegusia suala la kuiga mambo, kama vile mashindano ya urembo na suala la vyama vya siasa. Inaonekana suala hili litahitaji kushughulikiwa tena na tena. Katika makala yangu moja, niliongelea safari za JK nchi za nje, na baadhi ya watu walilalamika kuwa JK anasafiri mno. Walikumbushia kuwa viongozi wa nchi zingine za jirani, kama vile Kenya, hawasafiri hivyo, lakini nchi zao zinapiga hatua kutuzidi. Hitimisho likawa kwamba JK awaige viongozi hao; atumie muda mwingi nchini badala ya nje.

Wazo kuwa JK afanye kama wanavyofanya viongozi wa nchi zingine linahitaji tafakari. Napenda kuliongelea wazo hilo, kwa kutumia mfano huo wa Kenya na Tanzania. Je, kiongozi wa Tanzania anaweza kuiendeleza Tanzania kwa kuiga anayofanya kiongozi wa Kenya? Tanzania inaweza kuendelea kwa kuiiga Kenya?

Tanzania ni nchi yenye upekee. Kenya nayo ina upekee wake. Hizi nchi mbili zinatofautiana, kama zinavyotofautiana na Uganda, Rwanda, Congo, au Burundi. Tanzania ina historia yake, jadi yake, mtazamo wake, na malengo yake. Mahusiano ya jamii ndani ya Tanzania ni ya kiTanzania. Na Kenya ni hivyo hivyo. Kenya ina historia yake, jadi yake, na malengo yake. Mfumo wake wa uchumi na kijamii ni tofauti na wetu.

Mahusiano ya Kenya na nchi za jirani au nchi za mbali ni tofauti na mahusiano ya Tanzania na nchi za jirani yake au za mbali. Kenya inapakana na Somalia, Sudan na Uganda. Somalia kuna matatizo yanayoitishia Kenya pia. Masuala ya kiusalama yanayoihusu Kenya si sawa kabisa na yale yanayoihusu Tanzania. Tanzania ina utulivu kwa kiasi kikubwa, na hakuna mpaka wenye matatizo kwa wakati huu. Kiongozi wa Tanzania hakabiliani na hali halisi anayokabiliana nayo kiongozi wa Kenya.

Wakenya ni watu tofauti, na Watanzania ni watu tofauti. Sasa je, anayofanya kiongozi wa Kenya, au anayotakiwa kufanya kiongozi wa Kenya, yanaweza kutumika katika Tanzania? Au anayofanya kiongozi wa Tanzania, anayotakiwa kufanya kiongozi wa Tanzania, yanaweza kuwa sawa na yale ya Kenya. Kiongozi wa Tanzania anaweza kweli kuiongoza Tanzania kama vile ingekuwa Kenya? Au je, kiongozi wa Kenya anaweza kuiongoza Kenya kama vile ingekuwa Tanzania?

Mtu anayezunguka duniani ataona kuwa Wakenya wametapakaa duniani kuliko Watanzania. Mahali kama Marekani, kwa mfano, kama kuna chuo chenye waAfrika labda watatu au wawili, uwezekano ni mkubwa kuwa Mkenya yupo, na Mnigeria. Wakenya wanaoishi nje wanajituma katika masuala kama biashara na jumuia za kuleta maendeleo nchini kwao. Wanafanya mikutano, ambayo inahudhuriwa na viongozi kutoka Kenya, kwa madhumuni hayo. Nimewahi kuhudhuria hapa Minnesota.
Wakenya huku Marekani wanayo magazeti na vyombo vingine vya habari ambavyo wanavitumia kuitangaza nchi yao. Kenya imefanikiwa sana kujitangaza.

Serikali ya Kenya inashirikiana na hao waKenya waishio nje. Ilishaweka kitengo katika wizara yake ya Mambo ya Nchi za Nje cha kushughulikia masuala ya Wakenya hao. Kenya inajua kuwa waKenya hao wana mchango mkubwa katika uchumi wa Kenya. Hela ambazo waKenya walioko nje wanaingiza katika uchumi wa nchi yao ni zaidi ya mara nne kufananisha na zile wanazoingiza waTanzania walioko nje katika uchumi wao. Kwa kiasi kikubwa hii ni kwa sababu waKenya walioko nje ya nchi yao ni wengi zaidi kuliko waTanzania walioko nje ya nchi yao.

Mbele ya yote hayo, Rais wa Kenya ana sababu gani ya kuzunguka duniani kuitangaza nchi yake? Watu wake wanafanya hii kazi vizuri kabisa. Watanzania tunalalamika kuwa Wakenya wamefanikiwa hata kuutangazia ulimwengu kuwa Mlima Kilimanjaro uko kwao. Ni wazi kuwa, hata rais wa Kenya akikaa nchini muda wote, watu wake wako makini, walioko nchini na nje.

Sasa sisi Watanzania tukoje, hadi tudiriki kusema kuwa JK abaki nyumbani kama anavyofanya rais wa Kenya? Watanzania huku ughaibuni hatuwafikii waKenya katika masuala ya maendeleo ya nchi. Jambo hili nililitaja katika makala yangu kuhusu safari za JK nchi za nje. Watanzania tunakutana kwenye sherehe au misiba. Siku hizi, waTanzania walioko Ulaya, hasa Uingereza, wanajibidisha katika kufungua matawi ya CCM, badala ya kufanya shughuli za maendeleo na kuitangaza nchi kama wanavyofanya waKenya. Tunaanzisha matawi ya CCM badala ya kuanzisha angalau magazeti ya kuitangaza nchi.

Kwa upande mwingine, tofauti na ilivyo Kenya, Watanzania walioko nyumbani na wale walioko nje hawana mshikamano. Mtanzania wa nyumbani akisikia kuhusu Mtanzania anayeishi nje anamkejeli kuwa ni mlowezi au msaliti. Anaisema kuwa huyu aliyeko nje arudi nyumbani kujenga Taifa. Hata serikali yetu haijawa na mkakati wa kuwatambua hao waTanzania walioko nje na kuwashirikisha kikamilifu katika ujenzi wa Taifa. Serikali haijawa na kitengo cha kushughulikia masuala ya waTanzania walioko nje. Ni wakati huu tu ndio tunasikia taarifa kuwa utaratibu wa aina hii utaanzishwa.

Kwa kifupi, Watanzania bado tuna njia ndefu. Simlaumu JK kwa kuzunguka duniani akijaribu kuitangaza nchi yetu. Wajibu wa kiongozi wa Tanzania ni kutathmini hali halisi ya nchi yake na kuamua nini kinachohitajika. Wiki chache zilizopita, uongozi wa Chuo Kikuu cha Dodoma katika kuongelea masuala fulani ya hapo Chuoni, ulisema kuwa unaona matunda ya ziara za JK nchi za nje. Nilitegemea wale ambao wamekuwa wakipinga sana ziara hizo wangetoa kauli. Labda bado wanatafakari. Papo hapo, kabla ya Chuo Kikuu cha Dodoma kutoa kauli hiyo, Mheshimiwa Charles Stith, aliyekuwa Balozi wa Marekani hapa Tanzania, naye alisema kuwa ziara za JK nchi za nje zina manufaa. Nilitegemea wapinzani wa ziara hizo wangejitokeza kuinga kauli hiyo, lakini hawajajitokeza. Kama wanaamini kuwa JK abaki nyumbani, kwa nini wasijitokeze na hoja yao wakati huu? Naamini kuwa kadiri siku zinavyopita, ukweli utaendelea kujitokeza, kuwa kiongozi wa Tanzania anapaswa kufanya yale yanayotokana na tathmini ya hali hali
si na mahitaji ya Tanzania.

Thursday, August 13, 2009

Tunahitaji Vyama vya Siasa?

(Makala hii imechapishwa katika KWANZA JAMII, Agosti 11-17, 2009)


Profesa Joseph L. Mbele

Jamii yetu, kama jamii zingine, inatafuta namna ya kujenga na kuimarisha demokrasia. Katika harakati hii, uamuzi ulifikiwa kwamba tuwe na vyama vya siasa, badala ya chama kimoja. Vyama vya siasa vinapiganiwa karibu kila mahali kwa imani kuwa ni njia muhimu ya kujenga demokrasia. Kama kuna nchi isiyo na vyama vya siasa, utawala wa nchi hiyo unahesabiwa kuwa si wa kidemokrasia.

Kwa maana hii, kuuliza kama tunahitaji vyama vya siasa inaonekana ni upuuzi. Lakini mimi sioni kama ni suali la kipuuzi.

Demokrasia ni nini? Ni aina ya utawala ambamo umma umeshika hatamu. Demokrasia ni utawala unaowakilisha na kuendeleza matakwa na maslahi ya umma. Hii ndio maana ya demokrasia. Dhana ya vyama haiko kwenye tafsiri hii, kwani sio msingi au uhai wa demokrasia. Ni namna gani demokrasia inaweza kujengwa? Ili demokrasia iwepo, ni lazima kuwe na vyama? Haya ndio masuali ya kujiuliza.

Huko Ulaya, katika historia yao na mazingira yao, waliamua kuwa mfumo wa vyama vya siasa ndio wanaouhitaji kwa kujengea na kuwezesha demokrasia. Huo ulikuwa uamuzi wao, kufuatana na hali halisi ya kwao.

Lakini je, Watanzania tulikaa lini tukatathmini historia na mazingira yetu, hadi kufikia uamuzi kuwa ili tuwe na demokrasia, tunahitaji mfumo wa vyama? Tumefanya hiyo tathmini au tumeiga tu? Je, kinachofaa au kuhitajika Ulaya ni lazima kiwe hiki hiki hapa kwetu? Hili ni suali muhimu.

Je, hatukuwa na historia na jadi yetu ambayo tungeweza kuitumia katika kujenga demokrasia yetu? Je, kwa nini tumeshindwa hata kuwazia hilo? Mataifa yanayotutawala kiuchumi nayo yanatushinikiza tuwe na vyama vya siasa. Je. huu si ukoloni mambo leo, ambao watu kama Frantz Fanon waliuelezea?

Vyama vya siasa tumevipata, na huenda vikaongezeka. Je, vimetusaidia au vimetuletea matatizo? Ni wazi kuwa katika nchi yetu, vyama vya siasa vimeleta mfarakano, ambao unazidi kuota mizizi. Kampeni za uchaguzi zinaendelea kuwa na sura ya magomvi. Kadiri siku zinavyopita, amani inazidi kuharibika. Hayo yote yako wazi, lakini wazo la kuhoji umuhimu wa vyama vya siasa halisikiki.

Mtu anaweza kusema kuwa tunaweza kuendesha siasa ya vyama vingi kwa amani na utulivu. Lakini hoja hii haitavunja hoja yangu ya msingi kuwa tumeiga mambo kikasuku.

Tunataka demokrasia. Hilo ni wazi. Ingekuwa bora iwapo tungetafuta mfumo tofauti wa kujenga na kuendeleza hiyo demokrasia, mfumo unaotufaa kwa mujibu wa historia, jadi na mazingira yetu. Mfumo huu ungekuwa ni wetu, usio na chembe ya kushinikizwa kutoka nje, kama ilivyo sasa.

Kuna tatizo gani, kwa mfano, kuwa na mfumo ambao ungetumia busara za wazee kama ilivyokuwa katika jadi zetu? Ingewezekana kila kijiji, tarafa, au wilaya kuwachagua wazee wenye busara na kukubalika, wakawa ndio wawakilishi kwenye ngazi hizo na kiTaifa pia. Kwa busara zao, hao wangewasilisha maoni na mahitaji ya jamii zao, kuanzia watoto hadi wazee, wanawake kwa wanaume.

Katika maisha ya kila siku ya jamii yetu, wazee wanashika wadhifa huo. Mbunge ambaye tunamchagua kwa mtindo huu wa vyama vya siasa anaweza kupotea muda mrefu, asionekane hadi wakati wa uchaguzi ujao, lakini masuala ya jamii anayopaswa kuiwakilisha yanatatuliwa na wanavijiiji wenyewe kwa njia zao za asili. Kuna wabunge ambao ni kama watalii kwenye majimbo yao ya uwakilishi, lakini maisha ya wanavijiji kwenye majimbo hayo yanaendelea kwa msingi wa utaratibu ambao si wa vyama, ikiwemo jadi ya kuwatumia wazee.

Miaka ya karibuni, tumeona kitu cha aina hiyo kikifanyika katika kutafuta ufumbuzi wa masuala ya bara la Afrika. Wazee kama Askofu Desmond Tutu, Jimmy Carter, na Kofi Annan, wamepekwa kushughulikia masuala kama yale ya Zimbabwe. Katika migogoro ya Somalia, mara kwa mara wazee wamekuwa ndio watafutaji wa suluhisho. Miezi kadhaa iliyopita, wazee hao walikusanyika Kenya, wakafanya mazungumzo ya muda mrefu kutafuta ufumbuzi wa matatizo ya nchi yao. Hapa Tanzania, tuliona jinsi Rais Ali Hassan Mwinyi alivyokuwa na utaratibu wa kuongea na wazee wa Dar es Salaam, kuhusu masuala muhimu ya kiTaifa. Binafsi, naona Mzee Mwinyi alikuwa na upeo mzuri ambao ungepaswa kuimarishwa. Mifano hii yote inaendana na hoja ninayojaribu kujenga hapa, kuhusu umuhimu wa waAfrika kutafuta mifumo inayofaa kwa demokrasia katika mazingira yetu.

Utawala wa nchi si lazima uwe kwa mfumo chama cha siasa au vyama vya siasa. Nchi inaweza kutawaliwa bila chama au vyama. Kuwepo au kutokuwepo kwa demokrasia ni suala ambalo si lazima lihusishwe na vyama. Unaweza kuwa na demokrasia bila vyama, kama ilivyokuwa enzi za mababu na mabibi zetu, kabla ya kuja wazungu. Hapakuwa na vyama. Lakini, kama Mwalimu Nyerere alivyoandika, wazee walikuwa wanakaa chini ya mti na kujadiliana masuala hadi kukubaliana. Hii ilikuwa ni demokrasia, bila vyama.

Kinachohitajika ni sisi kufanya tafakari sisi wenyewe, si kudandia mambo ya Ulaya kama tunavyofanya. Uganda imeonyesha mfano, ina mfumo ambao inaona unafaa katika nchi ile, kufuatana na historia na mazingira yake. Mfumo wao unaweza kuwa na dosari, lakini angalau ni matokeo ya tathmini yao wenyewe. Wanaweza kuubadili wakaunda mwingine, kufuatana na hali halisi, bila kuiga kikasuku. Hizi ni fikra za watu huru. Kwa kutumia na kuthibitisha uhuru wa fikra na uamuzi, kila nchi katika bara letu, ingeweza kujitungia mfumo wa aina yake, kwa mujibu wa hali halisi ya nchi ile. Kwa mtindo huu, tungejenga demokrasia ya kweli, kudumisha amani na mshikamano, na kuleta maendeleo, sio fujo hizi tunazoziendekeza sasa kwa kisingizio cha ushindani wa kisiasa.

Tunahitaji demokrasia, yaani mfumo wa utawala ambao chimbuko lake na nguvu zake ni umma, mfumo ambao unasimamia na kuendeleza maslahi ya umma. Lakini je, ili hayo yawepo, tunahitaji vyama vya siasa? Hili ndilo suali linalohitaji jibu.

Saturday, August 8, 2009

Je, Tunaweza Tukawa na Mrembo wa Tanzania?

(Makala hii ilichapishwa katika KWANZA JAMII, Agosti 4, 2009)

Profesa Joseph L. Mbele

Kwa wiki kadhaa nimewazia kuandika makala kuhusu mashindano ya urembo. Katika Tanzania ya leo, mashindano hayo yameshamiri katika miji mikubwa na yanazidi kuenea.

Kwa upande moja nimekuwa sipendezwi na mashindano hayo. Nimekuwa nikijiuliza kama yana maana gani katika jamii yetu, kwani ni wazi kuwa mwenendo wake ni wa kuigwa kutoka nchi za magharibi. Ninayachukulia kama ishara nyingine ya ukoloni mambo leo.

Kwa upande mwingine, nimelazimika kukubali kuwa yamesaidia kwa namna mmoja au nyingine kuitangaza nchi yetu, wakati washiriki wanapoenda nje wakiwa na bendera ya nchi yetu. Vile vile, washindi wa mashindano hayo wameweza kufanya mambo ya maana katika jamii yetu. Wamekuwa watu maarufu nchini, wenye mvuto na uwezo wa kuhamasisha shughuli mbali mbali za manufaa kwa jamii. Wengine wameweza kujijengea msingi wa kujiendeleza kimaisha, kama vile kuwa wanamitindo katika nyanja za kimataifa. Hayo nimeyawazia na kuyazingatia. Ni mifano ya manufaa yatokanayo na mashindano hayo.

Lakini duku duku haziishi. Masuali hayaishi. Bado ukweli uko pale pale kuwa mashindano hayo yanayoshamiri siku hizi ni mambo ya kuiga. Si yetu. Vigezo vinavyotumiwa ni vya kuigwa; si vyetu. Tunashinikizwa tufuate vigezo vya Ulaya. Kwa mfano, wanawake wanaoshiriki mashindano hayo ni lazima wawe wembamba, au wembamba sana. Wanene hawakubaliki.

Hii ni ajabu katika nchi yetu na bara letu kwa ujumla, ambamo vigezo vya uzuri wa mwanamke ni tofauti. Katika mila na desturi za makabila yetu, kuna vigezo vya urembo, tofauti na hivi vya Ulaya. Kwa ujumla, unene ni uzuri, jambo la kujivunia. Katika makabila mengi, kulikuwa na mila ya kuwanenepesha wasichana kabla ya kuolewa.

Pamoja kushamiri kwa mashindano ya urembo, siamini kuwa katika mioyo ya waTanzania, dhana ya kuuenzi unene wa mwanamke imetoweka. Bado unene wa mwanamke ni jambo linalomfanya avutie. Kwa nini basi, tunajitumbukiza katika mashindano ya urembo ambayo vigezo vyake ni tofauti na hisia zetu? Naamini kuna baadhi ya waTanzania, kama vile vijana waliokulia Ulaya au Marekani, ambao wanalelewa katika mtazamo wa huko walikokulia hata kwenye suala la vigezo vya urembo. Lakini je, hisia za Mtanzania wa kawaida ni zipi?

Mashindano ya urembo ni jambo la kawaida katika jamii za binadamu. Hapa Afrika hali ni hiyo hiyo, tangu enzi za mababu na mabibi. Kwenye ngoma ilikuwa ni sehemu maalum ya mashindano hayo. Katika utungo wake maarufu uitwao “Wimbo wa Lawino,” mwandishi Okot p’Bitek wa Uganda alielezea vizuri jadi hii ya wasichana na wavulana kushindana kwenye ngoma katika kabila la Acholi.

Ili tuwe na upeo mpana wa kujitambua, tujiulize, je, kwa mila na desturi zetu, vigezo vya urembo wa mwanamke ni vipi? Vigezo vya Mmasai ni vipi? Vigezo vya Mnyakyusa, Mmakonde, au Mhaya ni vipi? Je, tunaweza tukawa na mrembo wa Tanzania? Naamini kuwa, ili tuwe na mrembo wa Tanzania, ingebidi sisi wenyewe tukae tukubaliane vigezo badala ya kuiga vigezo vya Ulaya.

Leo hii, mashindano haya ya urembo ambayo yanatumia vigezo vya Ulaya yanazidi kushamiri nchini mwetu. Mwishowe yatafika hata vijijini. Hata katika vyuo vikuu vya Tanzania, mashindano hayo yanayotumia vigezo vya Ulaya yanapamba moto. Nilitegemea kuwa vyuo vikuu ni sehemu ya kutafakari masuala na mambo ya jamii, mahala pa kufanya uchambuzi na kujua baya na jema. Haipendezi kuona kuwa chuo kikuu, badala ya kuwa mahali penye watu wa kuongoza njia, panakuwa ni mahali pa watu waliopotea njia.

Huko Ulaya na Marekani baadhi ya watu wameanza kutambua madhara yanayoendana na mashindano ya urembo. Watu wameanza kutambua kuwa shinikizo wanalowekewa wanawake kuwa wembamba linawafanya wajitese kwa mazoezi, wajinyime chakula au wale vyakula vya aina fulani tu na kwa mpangilio fulani maalum. Matokeo yake, angalau kwa baadhi ya wahusika, ni kujikosesha lishe bora, kudhuru afya, na kuugua maradhi mbali mbali. Kuna pia matatizo ya kisaikolojia miongoni mwa wasichana. Hawajisikii vizuri au wanajichukia kwa kuambiwa kuwa hawapendezi kutokana na umbo lao. Wasichana na wanawake wanene wengi wanaishi na masononeko na hata kujichukia kutokana na suala la unene.

Nafahamu kuwa unene wa aina fulani ni dalili ya afya mbaya, au ni hatari kwa afya. Hakuna ubishi kuwa unene wa aina hiyo ni jambo lisilohitajika. Tatizo la mashindano ya urembo ni kuwa hata unene wa kawaida tu hauruhusiwi. Hapo ndipo penye tatizo.

Tufikirie masuala haya ili tuweze kuinusuru jamii yetu. Huko Ulaya, baadhi ya wanawake wanene wamechoshwa na hali ilivyo, na wanarudisha hadhi ya unene katika urembo. Wanaendesha mashindano ya uzuri wa wanawake wanene, kupinga haya mashindano yanayotamba, ambayo yanasifu wembamba tu.

Labda tunahitaji kujielimisha upya, ili tuweze kuliona suala la urembo kwa upeo mpana zaidi. Mwandishi wetu maarufu, Shaaban Robert, aliwahi kutunga shairi ambamo tunawasikia wanawake wakisifia uzuri wao. Mwanamke mnene anasifia unene wake, na mwembamba anasifia wembamba wake. Na wote wanafanya hivyo kwa ufasaha na mantiki nzuri. Naamini kuwa Shaaban Robert alituelekeza katika njia nzuri.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...