Friday, October 16, 2009

Warsha Dar es Salaam: Utamaduni na Utandawazi


Tarehe 5 Septemba, mwaka huu, niliendesha warsha Dar es Salaam, kuhusu Utamaduni na Utandawazi. Warsha hii iliandaliwa na Tanzania Discount Club. Siku chache kabla, tarehe 29 Agosti, niliendesha warsha nyingine Tanga, kuhusu Utamaduni, Utandawazi na Maendeleo. Warsha hii, ambayo ilihudhuriwa na watu wa mataifa mbali mbali, nimeiongelea kidogo hapa na hapa.

Warsha hii ya Dar es Salaam ilinipa fursa ya kukutana na waTanzania kutoka sekta binafsi, taasisi mbali mbali na Ubalozi wa Marekani.
Warsha ilidumu kuanzia saa nne na nusu asubuhi hadi saa 11 jioni. Sehemu ya kwanza ilihusu masuala ya jumla: dhana ya utamaduni, kama nilivyoielezea katika kitabu changu Africans and Americans, na dhana ya utandawazi. Kwa mtazamo wangu, utandawazi ni jambo ambalo lilianza zamani kabisa, pale binadamu wa mwanzo walivyosambaa duniani wakitokea Afrika Mashariki. Hapo ndipo utandawazi ulipoanzia, na baada ya hapo, kumekuwa na aina na awamu mbali mbali za utandawazi, hadi kufikia zama zetu hizi, ambazo zimeshuhudia utandawazi wa ubepari ambao uliongelewa vizuri na Karl Marx na Frederick Engels katika Communist Manifesto. Leo hii, tekinolojia, na hasa tekinolojia ya mawasiliano, inawezesha aina nyingine za utandawazi, ambazo hata akina Karl Marx hawakuziwazia, kwani hazikuwepo. Utandawazi unajitokeza katika uchumi, siasa, utamaduni, na mambo mengine mengi.
Baada ya maelezo haya ya jumla niliingia kwenye suala la nafasi ya utamaduni katika utandawazi, nikielezea jinsi kuwepo kwa tamaduni mbali mbali duniani kunavyoathiri au kuathirirwa na utandawazi. Nilitoa mifano ya athari hizi. Kutokana na utafiti na uzoefu wangu, niliongelea kwa undani masuala yanayojitokeza katika mahusiano baina ya Wamarekani na Waafrika, kama nilivyoeleza katika kitabu changu.
Washiriki wote walifurahiwa na warsha hii na walitaka warsha za aina hii zifanyike siku za usoni, katika vyuo na taasisi mbali mbali.
Kwa upande wangu, nilifurahi kupata fursa ya kuongea na waTanzania wenzangu na kuwaeleza yale ambayo nimekuwa nawaeleza waMarekani kwa miaka kadhaa. Imenipa motisha ya kuendelea kufanya warsha za aina hii.
Jambo mmoja nililosisitiza ni kuwa ni muhimu warsha kama hii iwe ni sehemu ya elimu endelevu, ni muhimu tuendelee kuwasiliana. Baadhi ya washiriki walijipatia nakala za kitabu changu. Siku zijazo itawezekana kufanya warsha juu ya yaliyomo na yatokanayo na kitabu hiki, kama ambavyo inafanyika huku Marekani. Kitabu kinapatikana Dar es Salaam, simu namba 0717 413 073 au 0754 888 647

Kadiri dunia inavyoendelea na utandawazi, ni muhimu tujizatiti kwa kuelewa yanayotokea na kujiweka sawa ili kukabiliana na kuitumia hali inayojitokeza. Kwa wale ambao wamelala, utandawazi unaweza kuwa tishio na kipingamizi, lakini kwa walio makini utandawazi unaweza kuwa fursa ya kufanya mambo ya maana.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...