Sunday, October 11, 2009

Tamasha la Vitabu, Minneapolis, 2009

Jana, tarehe 10 Oktoba, nilishiriki tamasha la vitabu mjini Minneapolis. Tamasha hili hufanyika kila mwaka mara moja. Nimeshahudhuria mara kadhaa miaka iliyopita, lakini hali ni mpya kila mwaka. Kwa mfano, waandishi maarufu wanaoalikwa kama wageni rasmi huwa tofauti kila mwaka. Pia, pamoja na kuwa baadhi ya waandishi na wachapishaji na wauza vitabu huja mwaka hadi mwaka, wako pia wengi ambayo ni wapya. Hapo juu mbele kabisa ni mezani pangu. Baadhi ya vitabu vyangu vinaonekana.
Watu wanawahi, na milango ukumbi wa maonesho inapofunguliwa, saa nne asubuhi, ukumbi unafurika watu. Siku nzima hali ni hiyo hiyo; kuna msongamano wa watu wakiwa wanaangalia na kununua vitabu, wakiongea na waandishi na wachapishaji, na kadhalika.

Waandishi wa kila aina wanakuwepo, wake kwa waume, wazee kwa vijana. Siku hizi wengi wanachapisha vitabu vyao kwa kutumia fursa zitokanazo na maendeleo ya tekinolojia, bila kupitia kwa wachapishaji kama ilivyokuwa zamani. Kila mtu anaweza kutumia tekinolojia hiyo ya kujichapishia mwenyewe, ambayo inapatikana sehemu mbali mbali mtandaoni, ili mradi awe na kompyuta iliyounganishwa mtandaoni.

Wamarekani wanafurika kwenye tamasha la vitabu sawa sawa na sisi waTanzania tunavyofurika sokoni kununua vyakula. Pamoja na hali ya uchumi kuwa ya matatizo nyakati hizi, watu wananunua sana vitabu. Sijui ni lini waTanzania wataanza kupata mwamko wa kuviona vitabu kuwa ni muhimu kiasi hicho. Niliwahi kutoa kauli hiyo kwenye mahojiano na mwanablogu maarufu Muhiddin Issa Michuzi tarehe 4 Septemba, 2009.
Wamarekani wanaliona tamasha la vitabu--au duka la vitabu--kama sehemu muhimu ya kujiongezea elimu na kupanua mawazo. Mazungumzo na waandishi, wachapishaji na wauza vitabu yanaendelea siku nzima. Watu wanakuja kutoka miji ya karibu na mbali pia. Wanakuja kuangalia vitabu, kuvinunua, kuongea na waandishi na wachapishaji, kujenga mitandao ya ushirikiano katika shughuli za uchapishaji na uuzaji wa vitabu na kadhalika.



Katika tamasha la jana, nilipangiwa meza namba 19, kama inavyoonekana hapa juu. "Africonexion" ni kampuni yangu, ambayo niliisajili hapa Minnesota. Inshughulika na warsha, uandishi na uchapishaji wa vitabu, elimu kuhusu utalii, mahusiano baina tamaduni mbali mbali, na kadhalika. Siku za usoni nitaiingiza kampuni hii Tanzania.
Kama inavyoonekana hapa juu, tamasha hili ni kazi kubwa kwa waandishi, kukaa na kuongea na watu siku nzima. Ingawa inachosha, ni shughuli muhimu kwa namna mbali mbali.
Hapo juu niko na Bukola Oriola, dada Mnigeria ambaye mwaka huu nilimsaidia kuchapisha kitabu chake kwa kutumia tekinolojia niliyoelezea hapo juu kwa kupitia kampuni ya Lulu. Anaendelea kuandika.

Hapo juu niko na Profesa Mahmoud El Kati, Mmarekani mweusi, ambaye ni mtu maarufu katika miji jirani ya Minneapolis na St. Paul, akiwa ni mwalimu, mtafiti, mwandishi na mwanaharakati. Nimefahamiana naye kwa miaka kadhaa.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...